Friday, April 6

Wabunge, wasomi waeleza athari msimamo wa upinzani


Baadhi ya wabunge na wasomi wamesema msimamo wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni wa kutosoma hotuba za bajeti utawanyima wananchi haki.
Kiongozi wa kambi hiyo, Freeman Mbowe akizungumza na waandishi wa habari juzi mjini Dodoma alisema hawatawasilisha hotuba za bajeti za upinzani hadi watumishi wa sekretarieti yao ambao mikataba yao hutolewa na Bunge watakaporejeshwa.
Mbunge wa Mvomero (CCM), Sadiq Murad alisema uamuzi huo utaifanya hata Serikali kushindwa kujitafakari katika mipango yake.
Murad ambaye ni mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Viwanda, alisema jana kuwa maoni ya upinzani ni muhimu hivyo watafakari upya uamuzi huo.
Lakini Mbunge wa Kavuu (CCM), Dk Pudenciana Kikwembe alisema hakuna shida kwa wapinzani kusoma au kutosoma bajeti mbadala kwa kuwa ni watu wa hapana tu.
Alisema demokrasia inawaruhusu kuchangia bajeti kwa hotuba au hata kunyamaza.
Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine, Dk Charles Kitima alisema tangu utawala wa awamu ya tatu, Tanzania ilizoea kupata mawazo mbadala yanayotolewa na upinzani.
“Ieleweke kuwa mawazo mbadala yanajenga Taifa imara lenye kuwajibika,” alisema Dk Kitima.
Dk Kitima aliungwa mkono na Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dk Richard Mbunda aliyesema, “Hii ni hasara kwa wananchi. Mambo yaliyokuwa yakiibuliwa na upinzani sasa hayatafanyika, Serikali haitajua wapi inakosea.”
Alisema Serikali inaweza kuandaa bajeti inayopendelea eneo moja lakini upinzani katika hotuba zao watasema haina uwiano sawa hivyo irekebishwe na Serikali ikalifanyia kazi.
“Wakati mwingine, mambo muhimu na makubwa yalikuwa yanaibuliwa katika hotuba hizo na mawaziri walikuwa makini kufuatilia kujua upinzani wanasema nini juu ya wizara zao, sasa hilo halitakuwapo na bajeti zitakuwa zinapita tu,” alisema.
Mkazi wa Tabata jijini Dar es Salaam, Atway Selemani alisema si sahihi kwa upinzani kuchukua uamuzi huo kwa kuwa bajeti za wizara vivuli hutoa sura na udhaifu wa bajeti za Serikali.
Mkazi mwingine wa eneo hilo, Harrison Sogo alisema uamuzi huo una athari za moja kwa moja kwa wananchi ambao wamekuwa wakitegemea hotuba hizo kupata taarifa juu ya hali ya kiuchumi.
Imeandikwa na Habel Chidawali (Dodoma), Ibrahim Yamola na Kelvin Matandiko (Dar).

Tanesco yatoa kauli tozo ya Luku


Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) limezungumzia tozo ya asilimia 1.1 wanayokatwa wateja baada ya kununua umeme kwa njia ya mitandao ya simu na kupitia kwa mawakala wa benki.
Utaratibu huo ulianza Aprili 2 baada ya mfumo wa malipo wa Tanesco kuunganishwa na ule wa Serikali (GePG) ambao utawalazimu wateja wa huduma hiyo kulipia gharama za miamala husika, tofauti na ilivyokuwa awali ambapo huduma hiyo ilikuwa ikitolewa bure.
Akizungumza jana, Mkurugenzi Mtendaji wa Tanesco, Dk Tito Mwinuka alisema kuwa bei ya umeme bado haijapanda iko palepale kama ilivyokuwa awali.
“Hizi taarifa za kupanda kwa gharama za umeme siyo za kweli, hatuwezi kufanya hivyo kwa sababu bei ilipitishwa na Ewura (Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji), hivyo hatuwezi kupandisha bila wao kuridhia,” alisema Dk Mwinuka.
Alisema tozo baada ya kununua umeme si kitu cha ajabu kwani watu wa mitandao hawawezi kumfanyia mtu huduma bila kuigharamia.
Meneja Masoko wa Tanesco, Mussa Chowo alisema utaratibu uliopo siyo mpya kwa kuwa kulikuwa na mkataba baina ya Serikali na mitandao ya simu kuwa na tozo kwa anayenunua kwa njia ya simu.
Alisema sehemu ambayo mteja atanunua umeme bila tozo ni ofisi za Tanesco, Benki ya NMB na CRDB, lakini kama watanunua kwa wakala wa benki watatozwa asilimia 1.1.
Alisema mteja akinunua umeme wa Sh5,000 atachajiwa Sh55 na atakayenunua umeme wa Sh10,000 atatozwa Sh110 na umeme wa Sh100,000 atatozwa Sh1,100.

Heche mbunge wa 16 kuwa nje kwa dhamana kortini


Kupandishwa kizimbani kwa mbunge wa Tarime Vijijini, John Heche katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, kusomewa mashtaka matatu na kuachiwa kwa dhamana kumefanya idadi ya wabunge waliokumbana na hali kama hiyo kufikia 16.
Kesi zinazowakabili wabunge waliopo nje kwa dhamana ambazo wachambuzi wa siasa waliozungumza na Mwananchi wamesema hazileti picha nzuri katika siasa ya Tanzania, huenda zikaongezeka kutokana na jana mbunge mwingine, Ester Bulaya (Bunda Mjini) kuhojiwa Kituo Kikuu cha Polisi jijini Dar es Salaam na kuachiwa kwa dhamana.
Heche aliyekamatwa mahakamani hapo Jumanne iliyopita pamoja na wafuasi 23 wa chama hicho wakati wa kesi inayowakabili viongozi saba wa Chadema akiwemo Mwenyekiti, Freeman Mbowe, jana alifikishwa katika mahakama hiyo na kuunganishwa katika kesi ya viongozi hao na kusomewa mashtaka matatu ikiwamo kuchochea chuki.
Wakili wa Serikali Mkuu, Faraja Nchimbi alidai Heche na wenzake hao saba kwa pamoja walitenda makosa hayo Februari 16, mwaka huu maeneo ya viwanja vya Buibui na Barabara ya Kawawa wilayani Kinondoni jijini Dar es Salaam.
Washtakiwa wengine katika kesi hiyo ya jinai namba 112 ya 2018 ambao wapo nje kwa dhamana ni Mbowe; Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa; manaibu katibu wakuu, John Mnyika (Bara) na Salum Mwalimu (Zanzibar).
Wengine ni Mbunge wa Tarime Mjini, Esther Matiko; Katibu mkuu wa chama hicho, Dk Vicent Mashinji na Mbunge wa Kawe, Halima Mdee.
Baada ya kusomewa mashtaka hayo, Heche alikana na Aprili 16 mwaka huu yeye na wenzake saba watasomewa maelezo ya awali mahakamani hapo.
Heche aliachiwa baada ya kukamilisha masharti ya dhamana ya kuwa na wadhamini wawili wenye barua za viongozi wa mtaa, vijiji au waajiri wao na nakala za vitambulisho.
Kama ilivyokuwa kwa viongozi saba wa chama hicho, wadhamini wa Heche nao walisaini ‘bondi’ ya Sh20 milioni huku mbunge huyo akitakiwa kuripoti polisi kila Alhamisi.
Mbali na wabunge Heche, Mbowe, Mchungaji Msigwa, Mdee, Matiko na Mnyika, wabunge wengine wenye kesi na wako nje kwa dhamana ni Peter Lijualikali (Kilombero), Susan Kiwanga (Mlimba), Saed Kubenea (Ubungo), Godbless Lema (Arusha Mjini).
Wengine ni Tundu Lissu (Singida Mashariki), Cecil Mwambe (Ndanda), Kunti Yusuph na Zubeda Sukuru (wote viti maalumu) na Frank Mwakajoka (Tunduma) na Paschal Haonga (Mbozi).
Hata hivyo, jeshi la polisi limekuwa likisema mara kwa mara kuwa linapowakamata watu na kuwafikisha mahakamani huwa haliangalii kama ni wanasiasa au watu maarufu ila huangalia wahalifu.
Wachambuzi wanena
Mwanasiasa mkongwe aliyewahi kuwa waziri katika Awamu ya Tatu chini ya Rais Benjamin Mkapa, Njelu Kasaka alisema, “hili ni jambo jipya ambalo huko nyuma halikuwepo. Taifa linapaswa kujiuliza kwa nini wabunge wengi wana kesi.”
Kasaka aliyekuwa miongoni mwa wabunge waliounda kundi la G55 lililoibuka na hoja ya Muungano wa Serikali tatu mwaka 1993 aliongeza kuwa, “nafikiri tufike wakati kama Taifa tuone jinsi ya kuyamaliza bila kufikishana mahakamani.”
Alitolea mfano mataifa ya Korea Kusini na Marekani ambayo yalikuwa yakitishiana kwa makombora.
“Waliona wataangamiza wengi, wamekaa chini na kuyamaliza. Jambo kama hili linaweza kufanywa na viongozi tulionao, wana uwezo wa kuyamaliza na tukawa na maelewano mazuri kama huko nyuma,” alisisitiza.
Profesa wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Benson Bana alipingana na Kisaka na kubainisha kuwa huenda ukawa mkakati wa wapinzani kuendelea kuandikwa na vyombo vya habari na kudai hauna afya kwa wapiga kura waliowachagua.
“Wananchi wamekuchagua ukawawakilishe lakini wewe unashinda mahakamani badala ya kushinda nao kutatua kero zinazowakabili unabaki kupambana na kesi. Hii inawajengea kutokuaminika tena,” alisema.
Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Dk Hellen Kijo-Bisimba aliunga mkono hoja ya Kasaka na kuongeza kuwa wapinzani hawapaswi kuonekana kama wakosaji bali wachukuliwe ni sehemu ya jamii yenye manufaa makubwa. “Hiki kinachotokea sasa kama kingetokea mwaka 1995 au 1996 wakati upinzani unaanza tungeelewa, lakini si sasa ambapo tumeshuhudia upinzani ukiibua hoja zenye manufaa kama Escrow au Epa. Bila upinzani madhubuti hatuwezi kuwa na Taifa imara,” alisema Dk Bisimba.
“Kama wanataka kuua upinzani na kubaki chama kimoja watambue wanazalisha upinzani ndani ya chama hicho kimoja kwani hata G55 ilianzishwa ndani ya chama kimoja, kwa hiyo upinzani waachwe wawe huru na waikosoe Serikali ndio moja ya wajibu wao.”

Serikali sasa yaziweka njiapanda kesi za siasa


Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) ameziweka njiapanda kesi mbili za kikatiba zilizofunguliwa na watetezi na wanaharakati wa haki za binadamu na demokrasia kwa kushirikiana na vyama vya siasa, baada ya kuziwekea pingamizi la awali, huku akiiomba Mahakama izitupilie mbali.
Kesi hizo namba nne na sita za mwaka huu, zilizofunguliwa Mahakama Kuu, Masjala Kuu, Dar es Salaam dhidi ya AG zinahusu namna ya uendeshaji wa shughuli za siasa nchini, yakiwamo maandamano na wasimamizi wa uchaguzi.
Katika kesi namba nne wadai Francis Garatwa, Baraka Mwago na Allan Mwakatumbula wanaowakilishwa na Wakili Jebra Kambole, wanapinga vifungu namba 43, 44. 45 na 46 vya Sheria ya Jeshi la Polisi na kifungu cha 11 cha Sheria ya Vyama vya Siasa.
Katika kesi namba sita, mdai Bob Chacha Wangwe anayewakilishwa na Wakili Fatma Karume, anapinga wakurugenzi wa halmashauri za wilaya na manispaa kuwa wasimamizi wa uchaguzi kwa niaba ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec).
Kesi hizo zilitajwa jana katika majopo mawili tofauti ya majaji, ambayo yote yanaongozwa na Jaji Kiongozi, Ferdinand Wambali na katika kesi zote mdaiwa (AG) kupitia Wakili wa Serikali Mkuu (PSA), Alesia Mbuya ameieleza Mahakama kuwa wamewasilisha mapingamizi ya awali.
Wakili Mbuya ambaye alikuwa akisaidiana na mawakili wa Serikali wakuu, Abubakar Murisha na Aida Kisumo, aliomba Mahakama hiyo ipange tarehe nyingine kwa ajili ya usikilizwaji wa mapingamizi hayo ya awali.
Jaji Wambali alikubaliana na maombi hayo na akaelekeza kuwa kama sheria na kanuni zinavyoelekeza, kesi hizo zitahamishwa kwa jaji mmoja kwa ajili ya kusikiliza na kutolea uamuzi mapingamizi hayo kabla ya kuendelea na usikilizwaji wa kesi za msingi (ikiwa mapingamizi hayo yatakataliwa).
Akitoa amri za Mahakama katika kesi namba nne, Jaji Wambali kwa niaba ya majaji wenzake, Rose Teemba na Rehema Sameji, aliamuru kesi hiyo itajwe Aprili 20, mwaka huu kwa ajili ya kupanga tarehe ya usikilizwaji wa mapingamizi hayo.
Katika kesi namba sita, Jaji Wambali aliamuru kesi hiyo itajwe Aprili 17, mwaka huu kwa ajili ya kupanga tarehe ya usikilizwaji wa mapingamizi hayo kwa jaji atakayepangwa.
Akizungumza nje ya Mahakama, Wakili Karume alitaja mapingamizi hayo yaliyowasilishwa na AG kuwa ni hati za viapo vinavyounga mkono kesi hizo zina upungufu wa kisheria, kesi hizo zimefunguliwa isivyo sahihi kisheria na pia hazina maana bali ni za kuudhi tu zenye kupoteza muda wa Mahakama.

Ujasiri wa mtoto Anthony wa Ngara waikomboa familia


Ujasiri wa mtoto Anthony Petro, sasa umezaa matunda na kuleta mabadiliko katika familia yake.
Anthony, mtoto wa miaka 10, mkazi wa Ngara alisimama kidete kumzuia baba yake Petro Magogwa asiuze nyumba yao, iliyokuwa mali pekee wanayoitegemea.
Katika habari hiyo, Anthony alimzuia baba yake asiuze nyumba na kutishia kumburuza polisi, akieleza kuwa anafanya hivyo ili familia yao, wakiwamo dada zake wasikose mahali pa kuishi.
Baada ya Mwananchi kuchapisha taarifa zinazoonyesha ujasiri wa mtoto huyo, wasamaria wema wamejitokeza kuisaidia familia hiyo na sasa watajengewa nyumba ya kisasa. Miongoni mwa waliojitokeza kumjengea nyumba ni mtangazaji wa Redio Clouds na mmiliki wa mitandao ya kijamii, Millard Ayo ambaye amejitolea kujenga nyumba nzima kwa gharama zake.
Pia, uongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Ngara, umeahidi kuihamisha familia hiyo kutoka Kitongoji cha Mukitano, baada ya kubaini kuwa inaishi katika mazingira hatarishi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo, Aidan Bahama alisema Millard Ayo ameahidi kujenga nyumba hiyo na halmashauri itanunua kiwanja.
“Kiwanja kimepatikana kwa Sh4 milioni na tunataka kuhakikisha wanajengewa nyumba bora mzee huyu na watoto wake waishi kiafya na kiusalama,” alisema.
Mfadhili mwingine aliyejitokeza ni mmiliki wa Shule ya Amani Humwe, (Mwanga, Kilimanjaro), Isihaka Msuya ambaye ameahidi kumsomesha Anthony katika shule zake na kugharimia mahitaji yake yote.
Bahama alisema dada zake Anthony nao wanatafutiwa shule nyingine hivyo wanaojitokeza kusaidia familia hiyo wawasilishe michango yao kupitia akaunti ya Benki ya CRDB ya halmashauri hiyo au ofisi ya ustawi katika eneo hilo.
“Anthony atapelekwa shule wiki ijayo kuwahi masomo maana anaelekea sehemu ya ugenini hivyo anahitaji msaada zaidi wa kitaaluma kwa kupewa muda wa ziada” alisema.
Akizungumza kwa simu, Msuya alisema ameguswa na maisha ya mtoto huyo baada ya kusoma taarifa zake. Aliahidi pia kumtafutia mwalimu wa ziada kumfundisha ili aweze kwenda sambamba na wenzake.
“Nawahakikishia Watanzania na wenye kuguswa na maisha ya mtoto huyo kwamba atakuwa mazingira salama yenye kujali afya yake na kumsaidia aweze kutimiza ndoto za maisha yake,” alisema Msuya.
Baba mzazi wa Anthony, Petro Magogwa aliwashukuru wasamaria wema waliojitokeza kumsaidia na watoto wake na kueleza kuwa wakipata elimu itakuwa urithi wa maisha yao.
Mbali ya wahisani hao, Bahama alisema misaada mingine imeendelea kumiminika ndani na nje ya wilaya hiyo. Alisema wafanyakazi wa sekta mbalimbali wamechanga kiasi cha Sh 2.1 milioni, kati ya hizo, Sh 1 milioni ni ahadi.
Michango mingine ya Anthony imekuwa ikitolewa na wananchi kupitia namba ya simu inayoendeshwa na Kampuni ya Mwananchi Communications Limited (MCL), ambayo imeahidi kutangaza kiasi kilichopatikana kwa ajili ya mtoto huyo hivi karibuni.

Bakwata yafanya mageuzi makubwa ya uendeshaji


Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (Bakwata), limefanya mageuzi makubwa katika mfumo wake wa uendeshaji ikiwamo upatikanaji wa masheikh wa kata, wilaya na mikoa.
Akitangaza mageuzi hayo katika mkutano na wanahabari jana, Mwenyekiti wa Halmashauri Kuu ya Bakwata, Sheikh Khamis Mataka alisema mkutano mkuu wa baraza hilo uliofanyika hivi karibuni mjini Dodoma uliazimia kufuta utaratibu wa uchaguzi wa masheikh sambamba na maimamu wa misikiti.
Sheikh Mataka, alisema sasa viongozi hao watakuwa wakiteuliwa na Baraza la Ulamaa ambalo litawateua masheikh wa mikoa na wilaya na masheikh wa kata watateuliwa na mabaraza ya masheikh ya mikoa, huku maimamu wa misikiti wakiteuliwa na baraza la masheikh la wilaya.
Sheikh Mataka alisema ili kukabiliana na hali yoyote inayoweza kusababisha mali za Bakwata Baraza la Wadhamini litahakiki mali zote, kuziwekea wakfu ili kuzilinda, “Changamoto za kimfumo huwezi kuziondoa ila kwa majibu ya kimfumo. Kwa hiyo, changamoto za ubadhirifu na ufisadi uliokuwa unafanywa katika mali za wakfu za Waislamu tumeona jibu lake ni kuwa na kipengele cha kikatiba kinachozuia kuuzwa kwa mali za wakfu,” alisema.
Kuhusu mapato alisema ndani ya Bakwata mlikuwa na pakacha lililokuwa linasababisha kupotea kwa mapato na kwamba sasa kutakuwa na mfumo wa ukusanyaji kuanzia ngazi za chini hadi taifa.
“Ili kuutekeleza mfumo huu, Bakwata itaweka wahasibu katika mikoa yote na wilaya zote 196. Kutokana na hali ya Baraza ndio kwanza linajijenga, tunatoa wito kwa Waislamu wenye taaluma za uhasibu wajitokeze kuja kujitolea.”

Mambo muhimu ambayo hautaambiwa na bosi wako


Tunapoajiriwa mwajiri anakuwa na matarajio fulani kutoka kwatu na sisi utnakuwa na matarijio kadhaa kutoka kwake.
Kwa kifupi mwajiri anafikiri namna bora zaidi ya kutumia uwezo na vipawa vyako kwa manufaa yake kubwa ikiwa ni kutengeneza faida huku wewe pengine lengo lako ni moja tu kupata ujira japo inaweza kuwa zaidi ya hapo.
Katika mahusiano haya mara nyingi ni vyema kupeana taarifa zitakazo tuwezesha kuimarisha mahusiano yetu katika ajira lakini pia kufanya maamuzi sahihi.
Kwa bahati mbaya mara nyingi mwajiri au bosi wako hawezi kukupa taarifa zote unazozihitaji kwa sababu mbali mbali ila moja kubwa ikiwa ni apate kukutumia vyema.
Kuna baadhi ya mambo napenda kukushirikisha ambayo pengine unayajua na unayaona ya kawaida lakini inawezekana hauyajui kabisa.
Lengo la kukushirikisha mambo haya si kwa lengo la kukufanya utofautiane na mwajiri wako lakini kwa lengo la kukufanya uelewe thamani yako lakini pia utambue kuwa kuna maisha nje ya ajira zetu lakini suala jingine la msingi ni uwe mnyenyekevu na kuishi vyema na watu wengine nje na ndani ya ajira yako Ukifa Mwajiri wako atatafuta mtu mwingine.
Inawezekana unapenda sana ajira yako na uko tayari kutumia muda wako mwingi hadi ule wa ziada ili kuhakikisha mambo yanaenda sawa ofisini kwako na taasisi inafikia malengo.
Hili si jambo baya ni jema na shauku ya kila mwajiri kuona wafanyakazi wote wanakuwa na mtazamo huu. Pamoja na hayo kumbuka kuwa kazi unayofanya ni sehemu fulani tu ya maisha na kuna maisha mengine zaidi ya ajira au kazi yako.
Jitahidi kazi isiwe sababu ya kukuletea maradhi au kukusababishia umauti.
Kwa sababu ukipoteza maisha pamoja na kwamba mwajiri wako atasema msibani ‘pengo lako halitazibika’
baada ya siku kadhaa atatangaza nafasi uliyoiacha kuliziba pengo na pengine atapatikana mtu bora zaidi yako.
Kuna mengi ya kujifunza hapa; kama hatuishi milele basi na ajira yenyewe siyo ya milele. Jifunze kuishi maisha ya kujipenda, tapata muda wa kuichunguza afya yako, jiepushe na mazingira hatarishi kwenye ajira yako na pia ishi na watu vizuri bila kujali nyadhfa wala elimu zao. Kwa kifupi ajira yako isiwe chanzo cha matatizo ya kiafya wala kijamii.
Mwajiri hawezi kukulipa zaidi ya kile unachozalisha
Lengo la mwajiri yoyote ni kuhakikisha anatumia ujuzi na maarifa yako katika kuiletea tija taasisi. Ujira unaopata ni sehemu ndogo ya kile kikubwa unachozalisha kama mtu mmoja au kwa ujumla na waajiriwa wengine. Wala sisisemi kwa kuajiriwa tunadhurumiwa, hapana, nachojaribu kukumbusha ni kuwa uwezo na ujuzi wako unathamani zaidi ya mshahara unaoupata na huu ni mfumo unaokubalika kwa sababu mwajiri naye analengo la kupata faida. Kama unahisi nakutania anza kutega kazini au fanya uzalishaji chini kiwango ulichowekewa na mwajiri wako. Utaachishwa kazi kwa kutokuwa mfanisi. Suala hili pia linatukumbusha kuwa tunauwezo wa kutumia uwezo na ujuzi wetu kuanzisha biashara au miradi binafsi na siyo tu kuacha vipawa, uwezo na ujuzi tulio nao kutumika na mwajiri pekee.
Mafanikio yako ni ya taasisi pia lakini makosa yako ni yako mwenyewe
Kuna vitu huendelea nyuma ya pazia ambavyo pengine hauvifahmu kwa sababu haujapata muda kusikia taarifa zinazozungumzwa juu yako. Ukiwekewa lengo na mwajiri na ukalifikia kwa namna moja ama nyigine umeisaidia kufikia mafanikio ya taasisi. Katika mazingira haya mkuu wako wa idara anaweza toa taarifa kwa wakuu wake kwamba idara yake inafanya vizuri sana kwa sababu tu ya jitihada zako. Katika mazingira hayo hayo endapo utafanya makossa waweza jikuta unasimama peke yako na lawama zikakuangukia ‘idara yetu haijafikia malengo kwa sababu John alisababisha hasara ya milioni 5’. Hapa mkuu wako anajitoa na kujiweka pembeni.
Hii inatupa somo kuwa kuna umuhimu wa kuhakikisha tunafanya shughuli zetu kwa umakini mkubwa na jitihada pia. Lakini tunajifunza kutofanya ofisi zetu kama ndiyo kila kitu kwa sababu kuna siku tutasimama wenyewe kuwajibika kwa kile ammbacho pengine tulikifanya kwa lengo zuri lakini mambo hayakwenda sawa.
Ukistafu Kazi Taasisi Haitakuwa na Muda na wewe
Kwa sababu taasisi nyingi zipo kibiashara kinachofanyika ni kuwatumia watu kama njia ya kufikia malengo ya kibiashara lakini pale wanapokuwa hawahitajiki tena wanakuwa mizigo na hasara kwa taasisi. Muda wako wa ajira utakapo koma uhusiano wako na mwajiri au taasisi nao unakoma pia. Kuna mengi ya kujifunza hapa pia. Moja, kuna ulazima wa kujipanga mapema kuyakabili maisha baada ya ajira lakini pili, kuishi na watu vizuri nje na ndani ya taasisi na kuhakikisha ajira yako haikupi kiburi cha kuwadharau na kuwanyanyasa wengine. Mtu unaye mtegemea atakuwa msada kwako kukukingia kifua utakapo anza kupata madhara ya matendo yako naye si wa kudumu hapo ni wa kuja na kuondoka-kuwa mpole.
Ni vyema kujifunza kutumia ajira hizi za muda kutengeneza heshima ya kudumu. Nyadhfa, vyeo na fursa mbali mbali katika ajira zetu zina ukomo hivyo si vyema vikawa vyanzo vya kujiharibia sifa njema. Mtu mmoja aliwahi kunambia ‘Fanya kazi vizuri, fuata taratibu, kuwa mfanisi lakini kumbuka ofisi hi siyo ya baba yako.
Mwisho, mzunguko wa maisha una sehemu nyingi sana; familia, imani, marafiki, ndugu, michezo, buradani na mambo kadha wa kadha. Kumbuka kuwa yote haya yana umuhimu wake na usisahau kuyatengea muda. Kazi na ajira ni muhimu sana lakini haiwezi kwenda peke yake-changa karata zako vizuri.

ACT –Wazalendo waibuka na mpya


Dar es Salaam. Kiongozi wa Chama cha ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe amewaomba wanachama wa chama hicho na wananchi kuchagia Sh33.29milioni ili kusaidia huduma za afya na elimu katika kata zinazoongozwa na madiwani wa chama hicho.
Mbunge huyo wa Kigoma Mjini ametoa kauli hiyo leo Ijumaa Aprili 6, 2018 na kubainisha kuwa mpaka sasa watu mbalimbali wameshachanga Sh43.06milioni kati ya Sh75.35milioni zinazohitajika.
Amesema chama kimebaini changamoto zinazowakabili wananchi katika kata hizo baada ya Februari 19 hadi Machi 13, 2018, yeye pamoja na viongozo wenzake kutembelea kata zinazoongozwa na madiwani wa chama hicho.
“Chama kilifanya tathmini ya mahitaji, ambayo ni mifuko 1,371 ya saruji pamoja na mabati 2,680. Tunatambua kuwa wajibu wa ujenzi huu ni wa Serikali, kwa kuwa ndiyo inayokusanya kodi,” amesema.
“Lakini sisi ACT Wazalendo, kupitia falsafa yetu ya ‘Siasa ni Maendeleo’, tumeona tunao wajibu wa kushiriki kwa vitendo katika mapambano dhidi ya maradhi, ujinga na umasikini hata kama hatuongozi Serikali.”
Amesema gharama za mahitaji yote ni Sh75.35, mpaka sasa kiasi kilichopatikana ni Sh 42.06milioni, “tunakukaribisha mfuasi, mwanachama, mwananchi wa kawaida pamoja na mdau wa maendeleo, ili kushiriki.”

Rufaa ya Wambura TFF yatupwa


Mwenyekiti wa kamati ya Rufaa ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Wakili  Ebenezer Stafford Mshana ametupilia mbali rufaa ya aliyekuwa makamu wa rais wa TFF, Michael Wambura.
Wakili Mshana amesoma hukumu ya rufaa hiyo leo Aprili 6 makao makuu ya TFF, Karume jijini Dar es Salaam na kutangaza kutupilia mbali rufaa hiyo.
Wambura alikata rufaa kwenye kamati hiyo kupinga uamuzi wa kamati ya maadili kumfungia maisha kujihusisha na masuala ya soka kwa makosa matatu.
Makosa hayo ni kupokea/kuchukuwa fedha zaTFF za malipo ambayo hayakuwa halali ikiwa ni kinyume na kifungu cha 73(1) cha kanuni za maadili za TFF Toleo la 2013
 Jingine ni kughushi barua ya kueleza alipwe malipo ya Kampuni ya Jekc System Limited huku akijua malipo hayo sio halali ikiwa ni kinyume na kifungu cha 73(7) cha Kanuni za maadili za TFF Toleo la 2013
 Kufanya vitendo vinavyoshusha hadhi ya Shirikisho ikiwa ni kinyume na Ibara ya 50(1) ya katiba ya TFF kama ilivyorekebishwa 2015.
Hata hivyo, Wakili Ebenezer alisema Wambura anaweza kupeleka malalamiko yake kwenye mahakama ya kimataifa ya usuluhishi wa michezo (CAS).
"Hapa nchini baada ya hukumu hii, Wambura hawezi kupinga mahali pengine popote labda aende CAS kwa kuwa kamati hii ndiyo yenye uamuzi wa mwisho," alisema.
Wambura alishtakiwa na Sekretarieti ya TFF baada ya Kamati ya Ukaguzi kukutana na kupitia mambo mbalimbali ya ukaguzi na suala hilo la Wambura kuonekana linatakiwa kufika kwenye Kamati ya Maadili iliyotangaza kumfungia maisha katikati ya Machi.
Kigogo huyo wa mpira alinga uamuzi wa kamati ya maadili na kukuta rufaa, huku rais wa TFF, Wallace Karia akimtaja Athuman Nyamlani kukaimu nafasi ya Wambura TFF siku kadhaa zilizopita.
Karia alikaririwa na Mwananchi hivi karibuni akibainisha kuwa uteuzi wa Nyamlani umefanyika kwa matakwa ya katiba ya Shirikisho lakini pia akasisitiza ni haki ya rufaa ya Wambura kusikilizwa.

JPM atengua uteuzi wa mkurugenzi Mpwapwa



Katibu Mkuu wa Tamisemi, Mussa Iyombe 
Katibu Mkuu wa Tamisemi, Mussa Iyombe  
Dodoma. Rais John Magufuli ametengua uteuzi wa mkurugenzi  wa halmashauri ya wilaya ya Mpwapwa,  Mohamed Maje kuanzia leo Ijumaa Aprili 6, 2018 kwa kilichoelezwa kushindwa kutimiza majukumu yake.
Taarifa iliyotolewa na Katibu Mkuu wa Tamisemi, Mussa Iyombe leo imesema Maje ameisababishia Serikali hasara ikiwemo kushindwa hata kukusanya mapato ya Serikali.
"Hata makusanyo ya mwaka huu hatujui anapeleka wapi, hadi leo amekusanya asilimia 24 tu katika halmashauri kongwe kama Mpwapwa," amesema.

Ndugai atoa neno matibabu ya Lissu


Dar es Salaam. Spika wa Bunge, Job Ndugai amesema utaratibu wa Bunge kugharamia matibabu ya Tundu Lissu unaendelea kufanyiwa kazi na ukikamilika utatolewa ufafanuzi.
Spika Ndugai ametoa kauli hiyo jana Alhamisi Aprili 5, 2018 wakati akihojiwa na Kituo cha Televisheni cha Azam ikiwa ni siku moja kupita tangu aliporejea nchini akitokea India kwa matibabu.
Lissu ambaye ni mbunge wa Singida Mashariki kwa tiketi ya Chadema alishambuliwa kwa risasi zaidi ya 30, Septemba 7, 2017 na kupelekwa Hospitali ya Rufaa ya Dodoma na siku hiyohiyo alihamishiwa Hospitali ya Nairobi ambako alilazwa hadi Januari 6 alipohamishiwa Ubelgiji katika Hospitali ya Chuo Kikuu cha Leuven, anakoendelea na matibabu.
Tangu wakati huo, familia yake na viongozi wa Chadema wamekuwa wakililalamikia Bunge kutogharamia matibabu ya mbunge huyo huku Lissu naye mara kadhaa akizungumzia jambo hilo.
Lakini katika mahojiano hayo aliyofanya na mtangazaji wa televisheni hiyo, Charles Hilary, Ndugai amesema, “Lile tukio (la kushambuliwa Lissu) limekuwa ni jipya, linataka watu wengi waweze kuangalia jinsi ya kufanya. Kwa kifupi kila anayekwenda kutibiwa nje anakuwa na barua ya Wizara ya Afya au kibali kutoka Muhimbili, ndivyo sisi Watanzania tunafanya.”
“Hiyo ni kwa mbunge na asiye mbunge, hata mwananchi wa kawaida utaratibu ndio huo. Sasa kwa mheshimiwa Lissu alivyotoka Dodoma kila mtu anafahamu alipewa rufaa Nairobi na ndio maana tunaona kwa wabunge wengine wote wanaotibiwa kwa utaratibu huu huwa hawachangiwi hata na Bunge lenyewe.”
Amefafanua zaidi kuwa, “lakini mheshimiwa Lissu pale pale tulichanga sisi wenyewe wabunge kama wabunge kwa sababu tulikuwa tunajua safari hii ina tatizo ndio maana ikabidi watu wachange kutoka mfukoni.”
Amesema ni sawa na mtu aliyekata rufaa yeye mwenyewe kwenda katika hospitali aliyochagua, “kwa maana ile hakuchagua yeye mheshimiwa Lissu lakini familia yake na chama chake na kadhalika, halijawahi kutokea jambo kama lile katika Bunge letu, lina upya wa aina yake.”
Amesema upya huo unahitaji ushirikiano mkubwa wa familia na Bunge kuweka utaratibu ambao hautakuwa kwa kwa Lissu pekee.
“Hata kesho na keshokutwa huo ndio utakuwa utaratibu utatumika siku zijazo, kwa hiyo bado linafanyiwa kazi siku ya siku litakuja kutolewa maelezo kama linawezekana au haliwezekani.”
Kuhusu wabunge kupewa ulinzi baada ya Lissu kushambuliwa, Spika Ndugai amesema Dodoma hali ya ulinzi ni kubwa.
“Dodoma ni salama na tumemwomba RPC wakati wa Bunge na wakati wote ulinzi uwepo na umeimarishwa na sidhani kama litatokea tena,” amesema.

Dk Abbas awapa ushauri wasomi


Dar es Salaam. Msemaji Mkuu wa Serikali, Dk Hassan Abbas  amewataka vijana, hasa wasomi wa fani mbalimbali kutumia elimu yao kwa maendeleo ya Taifa.
Amesema badala ya kutumia elimu hiyo kushinda mitandaoni kutukana Serikali, waitumie kwa manufaa ya wengi.
Akizungumza leo Ijumaa Aprili 6, 2018 wakati wa uzinduzi wa kitabu cha ‘Uchumi wa viwanda’ Dk Abbas amesema kitabu hicho kimeandikwa wakati ambao nchi inahitaji uelewa mpana wa masuala ya viwanda.
"Huyu ni mhandisi muda huu angekuwa mitandaoni akiitukana Serikali yake au akiunga mabomba, lakini ametumia akili aliyonayo kutunga kitabu. Kitabu hiki kimeandikwa katika lugha rahisi na kimejaribu kuainisha aina za viwanda na umuhimu wa kuwa navyo,” amesema Dk Abbas.
Mkurugenzi huyo wa Idara ya Habari Maelezo amesema katika kipindi cha miaka miwili na nusu ya uongozi wa Serikali ya Awamu ya Tano, nchi ina viwanda 3,306.
Mtunzi wa kitabu hicho, mhandisi  Yuda Kemincha amesema ametunga kitabu hicho kuainisha aina za viwanda na namna ya kuvianzisha na kuviendeleza.
Amesema hakuna kinachoweza kuwaokoa vijana zaidi ya kusoma, kutambua kitu kwa undani na kukifanyia kazi.
"Nimejaribu kuainisha aina za viwanda hususani kwa wenye mitaji midogo na jinsi ya kuviendeleza.
"Lengo langu ni kuona hakuna anayebaki nyuma katika uchumi wa viwanda bila kujali ana kipato kikubwa au kidogo kiasi gani, nimetumia lugha rahisi ambayo kila mmoja ataielewa" alisema Mhandisi Yuda.

Bashe afunguka

Mbunge wa Nzega Mjini (CCM), Hussein Bashe ameiomba Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi na Ofisi ya Waziri Mkuu kuanzisha chombo huru cha kuchunguza matukio mbalimbali nchini, yakiwemo ya mauaji.
Bashe ametoa kauli hiyo leo Ijumaa Aprili 6, 2018 wakati akichangia mjadala wa bajeti ya ofisi ya Waziri Mkuu bungeni mjini Dodoma.
“Yapo mambo yanaanza kutokea katika nchini yetu yanaashiria kuanza kuwepo kwa mgawanyiko. Mambo haya tukiendelea kuyatizama kwa macho, hayaleti taswira njema huko mbele na wala hayataweza kulifanya Taifa hili kuwa moja wala kupambana na adui mkubwa ambaye ni umasikini,”amesema.
“Yanatokea matukio ya kusikitisha katika nchi yetu, ambayo ukitazama huoni any consign ya deliberate effort ambayo itawajengea Watanzania imani kwamba hata mimi mdogo nikikumbwa na dhahama yupo anayenilinda.”
Huku akitolea mfano tukio la kijana Allan Mapunda, aliyefariki dunia hivi karibuni mkoani Mbeya ikidaiwa sababu ni kipigo, Bashe amesema, “Naiomba Serikali kwa heshima kabisa, matukio ya namna hii yakiendelea kujengeka katika nchi yetu na  kuanzisha utamaduni ya kutowajibika yanaharibu amani.”
“Kijana huyu amekufa, ripoti ya daktari mkuu wa Hospitali ya Rufaa Mbeya inasema amefariki kwa majeraha ya ndani ya mwili wake. Familia yake imesema waliompiga ni polisi, RPC wa Mbeya (kamanda wa polisi) amesema hawahusiki, matokeo yake Serikali imeenda kutoa rambirambi ya Sh200,000.”
Amesema ndio maana matukio ya aina hiyo yameendelea kuwepo na kushauri kuwepo kwa chombo huru  kwa ajili ya kufanya uchunguzi wa matukio ya aina hiyo.
“Hatuwezi kuacha hii,  utamaduni wa kutojali kuendelea  katika nchi yetu si nzuri na ni jambo la kusikitisha maana unaharibu taswira na hii ndio inatumika na watu wasiopenda nchi yetu kuendelea kuharibu heshima ya Taifa,”amesema.

Msukuma ataka la saba warudishwe kazini

Mbunge wa Geita Vijijni, (CCM) Joseph Msukuma ameitaka Serikali kuwarudisha kazini watumishi wa umma waliofukuzwa kwa kuwa wana elimu ya darasa la saba hadi watakapostaafu.
Msukuma ameyasema hayo leo alipokuwa akichangia hotuba ya bajeti ya ofisi ya Waziri Mkuu kwa mwaka wa fedha 2018/19.
“Wabunge wenzangu, tuwatake Serikali wawarudishe kazini hadi hapo watakapostaafu. Hapa bungeni wabunge kama 100 hivi ni darasa la saba, wengine wamefeli, wengine wana vyeti feki,” amesema.
Amesema iwapo hawatawarejesha watumishi hao basi wawafukuze hata wabunge ambao wana elimu hiyo au wabunge hao warejeshwe kuwa wa viti maalum.
Kadhalika Msukuma ameitaka Serikali kuunda tume ya kuchunguza operesheni uvuvi haramu ili kubaini ukiukwaji wa haki za uvuvi unaofanywa kutokana na operesheni hiyo.
Amesema katika operesheni hiyo kuna mtu alitozwa Sh2milioni lakini risiti yake ikaandikwa ni ya mwaka 2015.
“Serikali iunde tume ichunguze hili jambo, operesheni uvuvi haramu? Kuna mvuvi anatozwa Sh2 milioni lakini anaandikiwa risiti ya 2015,” amesema.
Amesema kuna wakurugenzi wamewatumia watumishi katika operesheni hiyo ambao hukusanya fedha na ndiyo maana anaiomba Serikali kuunda tume.

Shoo ya Werrason Dar yasogezwa mbele


Dar es Salaam. Shoo ya mwanamuziki wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), Werrason Ngiama iliyokuwa ifanyike leo Ijumaa Aprili 6, 2018 kwenye ukumbi wa Escape One imeahirishwa kutokana na mwanamuziki huyo kuchelewa kufika nchini.
Kuchelewa huko kumetokana na hati za kusafiria za Werrason na wanamuziki wake nchini DRC kuchelewa, hivyo kukwamisha taratibu nyingine za kusafiri.
Taarifa za kuahirishwa kwa shoo hiyo zimetolewa leo na Katibu Mkuu wa Chama cha Muziki wa Dansi Tanzania (Chamudata), Hassan Msumari.
“Kundi  hili litaingia nchini Tanzania kesho Jumamosi na wote waliokata tiketi za onyesho la Escape One wazitunze kwa ajili ya kuzitumia tarehe itakayotangazwa la kundi zima la Wenge Mason Mere linaingia Jumamosi,” amesema Msumari.
Werrason ni miongoni mwa vijana waliojiunga pamoja mwanzoni mwa miaka ya 1980 na kuanzisha bendi ya Wenge Musica BCBG wakishirikiana na JB Mpiana, Didier Masela na Alan Makaba.

'Makaburi' ya magari ya Volkswagen nchini Marekani


Kampuni ya kuunda magari ya Volkswagen kutoka Ujerumani ililazimika kununua tena maelfu ya magari ambayo ilikuwa imewauzia wateja baada ya kugunduliwa kuwa na kasoro kwenye injini za dizeli, hatua iliyochangia kutolewa kwa gesi chafu.
Kampuni hiyo ina maeneo 37 ya kuegeshea magari kama hayo, ambayo kawaida hufahamika kama 'makaburi' ya magari.

Haki za Wanawake: Aina mbalimbali za unyanyasaji wa kingono kazini

Shirika la Uingereza linalofuatilia usawa katika jamii, Tume ya Usawa na Haki za Kibinadamulimetoa wito wa"hatua za dharura kuchukuliwa'' ili kuwalinda wahasiriwa na visa vya unyanyasaji wa kingono kazini.
Hapa wanawake sita vijana wanasimulia mifano sita ya jinsi wanawake husumbuliwa kazini.
Maelezo na Emma Russell.
Ushuhuda huu umetolewa na Tume ya Usawa na Haki za Kibinadamu na Wakfu wa Wanawake Vijana.
Unyanyasaji wa kigono kazini

"Kisa kibaya zaidi -mteja akija kazini anajipendekeza -iliniacha nikiwa na uoga sana.

Tangu hapo nimekuwa makini sana na nguo ninazozivaa,sketi zinazopanda juu ninapoketina mikufu ya kuning'inia, na kadhalika''
Jinsi ya kujikingaHaki miliki ya pichaAFP

''Nilikuwa na miaka 17. Ilibidi nijifungie chooni kutokana na matamshi ya mzaha yaliyobadilika kuwa tishio, wahudumu wenye umri mkubwa walikuwa wakisema mzaha kwamba nani angenivunja ubikira wangu kwa sababu nilikuwa nimpenda kwenda kanisani."

Mpiga picha

''Nilikuwa nikifanya kazi kwenye tamasha moja ya upigaji wa picha na mwanamume mmoja akanishika kutoka nyuma Kwa hivi sasa najiepusha kuvalia sketi fupi. Tunastahili kuweka wazi kwamba unyanyasaji wowote unaweza kumfuta mtu kazi''

Alinisukuma ukutani

''Nilifanya kazi kwenye kilabu na mteja mmoja alinisukuma kwenye ukuta na akajaribu kuweka mikono yake kwenye suruali yangu ya ndani -kwenye kilabu kilichojaa watu, sehemu ambayo kila mtu angeweza kuniona''

Kulia kila usiku

''Kitu kibaya zaidi nilisalia pekee yangu na sikuwa na mtu wa kumtegemea bali nilipatwa na mshtuko kila mara kwa wiki nzima, kulia wakati ninapolala, kupata msongo wa mawazo kuhusu vitu vidogo na kunisababishia kupata matamanio ya kula kila mara."

Msongo wa mawazo

''Nilimfahamisha mkubwa wangu afisini kuhusu unyanyasaji lakini viongozi wa kampuni hiyo walikuwa wanaume walidhani naongeza chumvi. Wanawake wengine watano waliacha kazi kutokana na unyanyasaji wa kingono uliosababishwa na mwanamume mmoja kwa kipindi cha mwaka mmoja.''

Ushuhuda huu umetolewa na kamati ya pamoja ya Tume ya Usawa na Haki za Kibinadamu na Wakfu wa Wanawake Vijana.