Tuesday, July 18

TAMKO LA NCCR MAGEUZI KUHUSU UFISADI WA IPTL KUPITIA AKAUNTI YA TEGETA ESCROW


TAMKO LA NCCR MAGEUZI KUHUSU UFISADI WA IPTL KUPITIA AKAUNTI YA TEGETA ESCROW
UTANGULIZI
Itakumbukwa na watanzania kuwa kwa takribani miezi miwili sasa watanzania wamekuwa wakishuhudia bunge la bajeti ambalo pamoja na mambo mengine, hoja ya ufisadi wa fedha za Umma zilizochotwa kifisadi kwenye akaunti ya Tegeta Escrow ilichukua sehemu kubwa ya mjadala wan chi hii. Kama chama tunachukua nafasi hii kumpongeza Mbunge wetu Mhe David Kafulila kwa ujasiri wake wa kutimiza wajibu wake wa kibunge kwa kiwango cha juu kabisa katika kuhakikisha Bunge  linakuwa na udhibiti wa fedha za serikali ambazo ni mali ya Umma.
Aidha, Chama kinachukua nafasi hii kuwapongeza wabunge wote wanaounda Kambi rasmi ya upinzani hususani wa CHADEMA na CUF pamoja na NCCR MAGEUZI kwa ushirikiano wao mkubwa katika kuhakikisha  wanaisimamia serikali katika mambo yote ya msingi likiwemo hili la ufisadi wa fedha za  akaunti ya Escrow. Wameonesha mfano mzuri ndani ya bunge na tunaomba wadau wote wa maendeleo tuungane katika vita hii kwani ni kwa maslahi ya Taifa letu masikini kabisa. Kwa nukta hii tunaomba viongozi wa dini, Asasi za kiraia(NGO), Wanazuoni  watanzania kwa ujumla tuungane pamoja kutaka uwajibikaji ili kudhibiti mzimu huu wa ufisadi wa IPTL/ESCROW ulioanza tangu awamu ya pili ya uongozi wan chi hii na sasa huenda ukaendelea kulitafuna taifa hadi awamu wa tano.
KWANINI ESCROW AKAUNTI ILIFUNGULIWA
Pamekuwa na upotoshaji wa maksudi kabisa kuhusu sababu za kufunguliwa akaunti hii. Upotoshaji huu umefanywa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali bungeni na watuhumiwa wenzake kwa maana ya Maswi na Muhongo kwa maana ya watuhumiwa ambao tayari wamesikika wakizungumzia suala hili. Watuhumiwa hawa wamesikika wakidai kuwa escrow ilifunguliwa kufuatia mgogoro baina ya wabia wa IPTL kwa maana ya Mechmar mwenye 70% na VIP mwenye 30%. Haya wanayapotosha  ili kuhalalisha hoja yao kuwa fedha hizo sio za serikali
NCCR MAGEUZI inapenda Umma wa Watanzania ufahamu kuwa akaunti hii ilifunguliwa na pande mbili; Tanesco na Serikali kwa upande mmoja na IPTL kwa upande wa pili. Na kwamba Akaunti hii ilifunguliwa kufuatia mgogoro wa malipo ya gharama za umeme ambapo Tanesco ililalamika kuwa inatozwa zaidi. Msingi wa Tanesco kulalamika kutozwa zaidi kulitokana na IPTL kudanganya kuhusu mtaji wa asilimia 30% (equity) ambapo ilidai iliwekeza dola 38millioni kumbe iliwekeza dola 50, sawa na Tsh 50,000/= wakati huo mwaka 1995-1998 ambapo exchange rate ya dola kwa Tsh ilikuwa 1; 1000.
Nikatika msingi huo, Mwaka Februari2014 Mahakama ya Usuluhishi wa migogoro ya kibiashara ICSID ilielekeza gharama ziangaliwe upya tangu TANESCO ilipoanza kununua umeme wa IPTL maka 2002 mpaka 2014 ili kuona ni kwa kiasi gani IPTL ilipata fedha isiyostahiki na kiasi gani ilikuwa stahiki ili kuweka msingi wa mgawo wa fedha za escrow. 
Hivyo  Akaunti ya Escrow ilifungulimwa mwaka 2006 ikiwa ni miaka miwili tangu 2004 ambapo TANESCO ilibaini kasoro hiyo ya udanganyifu uliofanywa na IPTL kwenye equity ya dola 38milioni wakaweka dola 50.
KWANINI FEDHA ZA ESCROW NI MALI YA UMMA
Fedha ya Escrow ni mali ya Umma kwa sababu zifuatazo;
1.Ziliwekwa kusubiri kumalizika mgogoro wa gharama ambazo IPTL ilikuwa anatoza TANESCO kifisadi. Mgogoro huo ambao msingi wake ulitokana na IPTL kudanganya kuhusu mtaji wa dola 38milioni kumbe ilikuwa dola50.Mpaka sasa hakuna mahala mgogoro huo umeamuliwa.
2.Ndio sababu Hukumu ya awali ya ICSID ilielekeza pande mbili zifanye hesababu upya ili kubaini ni kiasi gani IPTL ilizidisha na ni kiasi gani ilikuwa halali kwa kuangalia tangu mwaka 2002.  
3.Ndio sababu fedha hizo zilionekana kwenye vitabu vya shirika la Umma Tanesco
4.Ndio sababu Kamati ya PAC, Spika na Waziri Mkuu wote wamelekeza CAG achunguze akaunti hiyo kwani kisheria CAG hana mamlaka ya kuchunguza fedha za wafanyabiashara bali fedha za Umma. Na CAG anachunguza fedha za Umma kwenye makampuni ambayo umiliki wake sio chini ya asilimia 50
MASWI, MUHONGO, MRAMBA, WEREMA NA IPTL NDIO WALISHINIKIZA UFISADI HUU
May 30, 2014 Waziri wa Nishati na Madini Mhe Muhongo alidanganya Bunge kuwa uamuzi wa Serikali kumlipa IPTL/PAP ulikuwa uamuzi wa hukumu ya Mahakama ya Setemba 2013. Ukweli ni kwamba hukumu hiyo hakuna mahala ilielekeza PAP alipwe fedha hizo. Ukweli ni Kwamba uamuzi wa kifisadi wa kutoa fedha hizo ulifanywa na Wizara ya Nishati na Madini na Tanesco kwa upande mmoja na IPTL kwa upande wa pili na ukapewa Baraka na Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Hivyo Tunaomba Umma uelewe hivyo.
NYARAKA ZA PAP KUMILIKI ASILIMIA 70 ZA IPTL NI ZA KUGUSHI
Nyaraka za TRA zinaonesha kwamba SingaSinga ambaye ndiye mliki wa PAP alinunua hisa asilimia za 70 za IPTL kutoka kwa PIPERLINK kwa 480millioni, na kwamba PIPERLINK ilinunua Asilimia hiyo 70 kutoka kwa Merchmar kwa Tsh6millioni wakati kampuni hiyohiyo ilinunua asilimia 30 kutoka kwa VIP alinunua kwa 120billioni. Pia inaonesha kwamba kodi ililipwa disemba 6, 2013 wakati alipewa hela za escrow tangu Novemba 2013. Kwa tafsiri nyingine alilipwa fedha za Escrow kabla ya kuwa mmiliki halali wa IPTL.
Na zaidi Umma unapaswa kuelewa kuwa Kwa mujibu wa sheria ya kodi(Finance Act 2012), hisa zinapouzwa kutoka kampuni moja kwenda nyingine uhamishaji huo unathibitishwa na waziri wa wizara husika baada ya kodi kulipwa. Sasa muulizeni waziri wa Nishati na Madini ni lini uhamishaji huo wa hisa aliupitisha kama waziri? Na zaidi taarifa za TRA zinaonesha kuwa kodi ya mauzo ya hisa hizo asilimia 70 kutoka Mechmar kwenda PIPERLINK na Kutoka PIPERLINK kwenda PAP ilipwa tarehe moja yaani Disemba6, 2013.
Huu ni uthibitisho kuwa documents hizi zote ni za kughushi, na watanzania hawawezi kuchezewa akili kiasi hiki.

MKATABA WA WIZARA YA NISHATI NA IPTL KWENDA BOT NI UFISADI
Mkataba huu ulikuwa kifisadi kwasababu hauna msingi wowote wa kisheria wala kimkataba. Mkataba wa kuzitoa fedha hizi ni wa kifisadi mgogoro uliosababisha fedha hiyo iwekwe hapo haukuwa na haujamalizika. Ndio msingi wa hukumu ya mahakama ya ICSID uliotaka mahesabu kufanywa upya. Ikumbukwe kuwa kwa mujibu wa mkataba wa IPTL, pande mbili zilikubaliana kuwa maamuzi kuhusu mgogoro baina yao utamuliwa na mahakama ya ISCID na sio vinginevyo.
MMILIKI WA PAP ANA REKODI YA UFISADI AFRIKA SIO MWEKEZAJI
Kwa mujibu wa report ya wikleaks, Singasinga anaetajwa kuwa mmiliki wa kampuni ya PAP ametajwa katika orodha ya mafisadi waliohusika katika skendo ya ufisadi wa Goldenberg nchini Kenya jina lake likiwa no8 akishirikiana na mtoto wa Rais mstaafu wa Kenya, Gideon Moi. Huu ndio ufisadi mkubwa kupata kufanyika nchini Kenya, uliohusisha Majaji, Viongozi wakubwa kisiasa, familia ya rais na watendaji wakubwa serikalini. Kama CCM haitachukua hatua kali kuhusu ufisadi huu wa escrow ijiandae kufuata nyayo za chama cha KANU kwani kuna kufanana sana kwa skendo hii na ile ya Goldenberg.
KIFO CHA MGIMWA KICHUNGUZWE
Mhe Mbunge David Kafulila, alisisitiza ndani ya Bunge kuwa kama tungekuwa na Bunge makini hata kifo cha aliyekuwa waziri wa Fedha, Mhe Mgimwa kilipaswa kuchunguzwa. Chama kinapenda kusisitiza kauli hiyo kwakuwa Mzee Mgimwa aliugua na kufariki katika kipindi ambacho kulikuwa na shinikizo kubwa la kutoa fedha za escrow bank kuu. Hivyo Kama Chama tunapenda Umma uelewe kuwa huo ndio msingi wetu wa kutaka uchunguzi wa kifo hicho. Na familia ya Mhe Mgimwa tunaipa pole kutonesha madonda lakini tunafanya haya kwasababu ndugu yao alikuwa public figure, alikuwa kiongozi ndani ya nchi hivyo umma una maslahi na chochote kinachomuhusu mtu huyu.
HATMA YA USALAMA WA MBUNGE KAFULILA
Mhe Spika amegoma kuchukua hatua kuhusu mwongozo uliombwa na mbunge Mhe David Kafulila kuhusu kutishiwa maisha ndani na nje ya Bunge. Kama Chama Tunapenda kurejea na kusisitiza kuwa tuna hofu na uhai wa Mbunge wetu hasa kutokana na mazingira yanayozunguka ajenda hii anayoisimamia ikiwa inagusa vigogo na mafisadi wakubwa. Tunao uzoefu wa mazingira kama haya pale kijana Amina Chifupa alipozungumzia madawa ya kulevya, tunao uzoefu na kilichotokea kwa Dr Mvungi alipokuwa mhimili imara wa serikali tatu ndani ya Tume ya warioba, wote tunafahamu kilichowakuta. Kama chama kwakuwa Bunge la vyombo vya dola havioni umuhimu huo, tunamwachia  Mungu, lakini chochote kikitokea tunafahamu ushiriki wa serikali na vyombo vyake.
SPIKA MAKINDA ANADHALILISHA BUNGE
Kazi ya Bunge ni kusimamia Serikali. Ufisadi wa IPTL ulianza tangu awamu ya pili 1994. Ni aibu kwa Spika kukataa Bunge lisichukue jukumu lake la kuichunguza serikali. Wote mnafahamu CAG alivomsafisha Jailo au PCCB ilivosafisha Richmond. Ni katika Msingi huo, Kama chama tunashauri suala hili linalogusa vigogo wakubwa nchini, lichunguzwe na Bunge lenyewe kupitia Kamati teule au uchunguzwe ufanywe na Kampuni za Kimataifa za ukaguzi kama ilivofanyika kwenye fedha za EPA.
Mhe Mbunge alitoa ushahidi wa hukumu ya Septemba 2013 ikionesha dhahili kuwa hakuna mahala hukumu ile ilielekeza IPTL/PAP wapewe fedha hizo za Escrow. Na kuthibitisha kuwa waziri huyu alizungumza uongo bungeni kwa jambo nyeti kama hili, lakini Spika badala ya kutumia kanuni ya kusema uongo anaelekeza mbunge aende PCCB, Kambiwa na nani PCCB wanachunguza uvunjifu wa kanuni za bunge?
Aidha, Ni udhaifu wa Spika huyu ndio sababu haoni aibu kwa Bunge lake kuwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Nishati na Madini ambaye ni Makamu Mwenyekiti wa bodi ya Tanesco. Hii Kamati inawezaje kukosoa uchafu wa TANESCO katika mazingira hayo? Au ndio sababu taarifa ya Kamati hiyo haikuzungumza chochote kuhusu ufisadi wa escrow unaohusu TANESCO na wizara yake?
JAJI WEREMA AJIPIME KAMA ANASTAHILI KUENDELEA KUWA JAJI NA MWANASHERIA MKUU
Uamuzi wa Jaji Werema kutaka kupigana bungeni hata kuzuiwa na Mhe Sitta na Wasira na baadae nje ya Bunge kumtishia uhai Mhe Mbunge ni kielelezo kuwa amepungukiwa sifa za msingi kuweza kuendelea kuwa mwanasheria mkuu wa serikali. Ni aibu serikali ya Kikwete kuwa na Mwanasheria mkuu ambaye kazi yake kubwa ni kuelekeza na kushauri utawala wa sheria nchini harafu anageuka na kuwa mfano wa raia mwenye mapenzi ya kujichukulia sheria mkononi ndani ya bunge na kuahidi kukata kichwa mbunge anaemkosoa. Hii haijapata kutokea katika historia ya Tanzania.
MWISHO
Tunapenda kuhitimisha kwamba tunaitaka Serikali kuchukua hatua madhubuti kuhusu ufisadi huu, na kwamba haturidhishwi na hatua zinazochukuliwa, na kwamba tutafanya utaratibu wa kuwasiliana na vyama ndani ya UKAWA kuona namna bora zaidi ya kulisukuma suala hili ili watanzania waelewe namna nchi yao inavotafunwa. Tunaomba vyama vyote ndani na nje ya UKAWA vitambue ukweli huu kama ambavyo wameanza kutambua ili tusaidiane kuelimisha Umma kuhusu ufisadi huu na watanzania wafanye maamuzi ya nchi yao kwani wanayo haki ya kuhoji na kufaidi utajiri wa taifa lao kwani hawapo kwenye ardhi hii kama wakimbizi au tumbili kama inavyotambuliwa na Serikali ya CCM sasa. Wiki ijayo tutaanza ziara ziara Mkoani Kigoma wakati taratibu zingine zinaendelea kushughulikiwa. Wiki ijayo tutaanza ziara ziara Mkoani Kigoma wakati taratibu zingine zinaendelea kushughulikiwa.
Imesainiwa na;

…………………………….
NYAMBABE
KATIBU MKUU

KAULI YA TUNDU LISSU KUHUSU KAMATAKAMATA YA VIONGOZI WA UPINZANI




Tanzania yanyooshewa kidole Uchaguzi Kenya

Waziri wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika
Waziri wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki, 
Kikanda na Kimataifa, Dk Augustine Mahiga 
Dar es Salaam. Wakati Uchaguzi Mkuu wa Kenya ukikaribia, kampeni zikipamba moto na wanasiasa nchini kuonekana kuwa sehemu ya mchakato huo, muungano wa Nasa unadaiwa kuwa na mpango wa kuanzisha kituo cha kujumlisha matokeo nchini.
Hata hivyo, Serikali imekanusha madai hayo ikisisitiza kwamba haiwezi kuruhusu chama chochote kutoka Kenya kuja kuanzisha kituo cha kujumlisha matokeo kwa sababu kufanya hivyo ni kuingilia mambo ya nchi hiyo jirani.
Uchaguzi huo unatarajiwa kufanyika Agosti 8 na wagombea wanaochuana vikali ni Rais Uhuru Kenyatta anayetetea nafasi hiyo kupitia chama cha Jubilee na Raila Odinga anayewakilisha muungano wa Nasa.
Gazeti la Daily Nation la Kenya liliripoti jana kwamba, Juni mwaka huu, Nasa ilitangaza kwamba itaanzisha vituo vitatu maalumu kwa ajili ya kujumlisha kura zake katika nchi za Kenya, Ujerumani na Tanzania.
Gazeti hilo lilibainisha kwamba Serikali ya Tanzania iliridhia mpango huo wa Nasa na kwamba kituo hicho kitawekwa huko Kigamboni. Pia, limeeleza kwamba Odinga alikuja Tanzania Mei kwa ajili ya maandalizi.
Hata hivyo, Waziri wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa, Dk Augustine Mahiga alisema amesikia maneno hayo lakini hakuna chama cha siasa cha Kenya kilichoomba kuanzisha kituo cha kujumlishia matokeo yake na kwamba Serikali haiwezi kukubali.
Dk Mahiga alisema wameihakikishia Serikali ya Kenya kwamba maneno hayo ni ya uongo, hakuna kitu kama hicho na Serikali haiwezi kuruhusu kwa sababu itakuwa ni kuingilia mambo ya ndani ya Kenya.
Rais John Magufuli na Edward Lowassa waliogombea urais nchini katika uchaguzi wa mwaka 2015 nchini, kupitia CCM na Chadema, mtawalia, wanatajwa kuongeza nguvu ya ushawishi kwa wapigakura wa Kenya.
Lowassa na chama chake wametangaza kumuunga mkono Rais Kenyatta kwa imani kwamba ndiye mgombea bora kwenye uchaguzi huo.
Lakini pia vyama vikubwa vya siasa vimekuwa vikijinadi kwamba vikipewa dhamana, vitaiga mfano wa Rais Magufuli katika kupambana na ufisadi nchini humo na kuzingatia masilahi ya watu wa chini.
Odinga amekuwa rafiki mkubwa wa Rais Magufuli na alimuunga mkono katika wa uchaguzi wa 2015.
Desemba 6, 2012 kwenye kampeni za Uchaguzi Mkuu wa Kenya, Dk Magufuli akiwa Waziri wa Ujenzi, alikwenda Kenya na kumpigia debe Odinga na chama chake cha ODM.
Urafiki huo uliendelea hata baada ya Dk Magufuli kushinda urais kwani Aprili mwaka jana, Odinga alikuja nchini kumtembelea na wawili hao walikutana Chato, Geita wakati Rais akiwa mapumziko.
Juzi, Lowassa aliyekuwa Kenya kuhudhuria mazishi ya aliyekuwa waziri wa mambo ya ndani wa nchi hiyo, Joseph Nkaisery katika mahojiano na gazeti la Daily Nation, alisisitiza kwamba anamuunga mkono Kenyatta kwa sababu analinda uhuru wa demokrasia.
Hata hivyo, tofauti na Chadema, chama kingine cha upinzani nchini cha ACT-Wazalendo jana kilitangaza kuunga mkono muungano wa Nasa katika uchaguzi huo kikilekeza kuwa ni baada ya kupitia ilani za vyama vyote na kujiridhisha kwamba ndiyo upande pekee ambao wananchi wataupigia kura.
Katika barua iliyosainiwa na Kiongozi wa chama hicho, Zitto Kabwe, ACT Wazalendo imebainisha kwamba imekuwa ikifuatilia siasa za Kenya na inaamini kwamba Nasa inaweza kuwaletea Wakenya mabadiliko ya kweli.
“Tumefuatilia ahadi na ilani zote za uchaguzi. Tumefikia uamuzi kwamba Nasa ndiyo chama ambacho Wakenya watafikiria kukipigia kura ili kiwaletee mabadiliko ya kijamii na kiuchumi na Afrika Mashariki kwa ujumla,” alisema Zitto katika barua hiyo, “Tunajua kwamba uchaguzi wa Kenya ni kwa ajili ya Wakenya kuamua lakini tunatambua pia kwamba Kenya imara ni EAC (Jumuiya ya Afrika Mashariki) imara. Tunaamini Nasa italeta uongozi imara chini ya kiongozi wake, Raila Odinga.”

Magunia 428 ya bangi yakamatwa Arusha

Arusha. Shehena ya magunia 428 ya dawa za kulevya aina ya bangi imekamatwa katika kitongoji cha Longong, Kijiji cha Engalaoni wilayani Arumeru usiku wa kuamkia jana.
Akizungumza  leo Jumanne, Julai 18 wakati wa operesheni hiyo maalum ya kufanya ukaguzi wa nyumba kwa nyumba kwenye kitongoji hicho, Kamishina wa Intelijensia wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya nchini, Fredrick Kibute, amesema wamefanikiwa kukamata dawa hizo baada ya kupata taarifa kutoka kwa wananchi.
Amesema walituma kikosi kazi cha watu wachache kuchunguza uwepo wa taarifa hizo.
“Baada ya kujiridhisha na taarifa hizo, tulianza safari kutoka Dar es salaam na juzi usiku wa manane tulianza upekuzi na kukamata magunia hayo 428,"amesema Kamishna huyo.
Amesema walikamata magunia 428 ya bangi usiku huo na magunia sita ya mbegu za bangi ambazo zilikuwa zimefichwa ndani.
"Lilikuwa jambo la kushangaza usiku huo hatukukuta watu ndani ya nyumba ingawa zilikuwa wazi, baadhi ya nyumba zilikuwa zimefungwa, zilizofungwa tuliamua kuchukua uamuzi wa kuvunja na tulikuta kila nyumba ina bangi," amesema.
Kamishna Kibute amesema pia licha ya eneo hilo kuwa mbali limesababisha viongozi wengi kushindwa kufika maeneo hayo kwa ajili ya ukaguzi.
"Huku ni mbali hasa ukiangalia ni eneo wanaloishi watu wachache, kikubwa tunaomba ushirikiano zaidi kutoka kwa wananchi juu ya uwepo wa madawa hayo kwenye maeneo hayo," amesema.
Kamishna Kibute aliwataka wananchi wa wilaya ya Arumeru kuacha mara moja biashara ya kilimo cha bangi kwa kuwa serikali ya awamu ya tano si mchezo na kuwataka watambue kuwa hawapo salama na atahakikisha anakomesha kilimo haramu cha biashara ya dawa za kulevya.

Mbunge mwingine Chadema ahojiwa na Polisi

Dodoma.  Mbunge wa Viti Maalum (Chadema) Kunti Majala alishikiliwa na polisi kwa zaidi ya saa tatu akidaiwa kufanya kusanyiko lisilo halali katika kijiji cha Mapango, kata ya Chandama wilaya ya Chemba mkoani Dodoma jana jioni.
Akizungumza na Mwananchi leo Jumanne, Julai 18, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Lazaro Mambosasa amesema mbunge huyo aliitwa na polisi kuhojiwa baada ya kupokea malalamiko kuwa alikuwa akiitukana Serikali na kutumia lugha chafu katika shughuli zake za kisiasa kwenye jimbo hilo.
Pia amesema mbunge huyo alikuwa akifanya mkutano wa hadhara bila kuwa na kibali cha polisi.
Hata hivyo, Kunti amesema kuwa aliruhusiwa kufanya mkutano huo na Mkuu wa Polisi wa Wilaya ya Chemba kwa njia ya simu.
Hata hivyo jana alipomaliza kuhojiwa, polisi walitoa barua ya kukataza mikutano yake ya hadhara aliyokuwa aifanye jimboni humo kuanzia jana hadi Julai 20.

MUIGIZAJI NYOTA WA FILAMU ZA KIHINDI SANJAY DUTT ATUA NCHINI


 Mbunge wa Manonga / Igunga Seif Khamis Gulamali akimpokea na kumpa sapoti ya safari yake Muigizaji wa Filamu za Kihindi Sanjay Dutt kwenda Mapumzikoni Mbuga za Wanyama Ngorongoro Mkoani Arusha Mapema leo
 Mbunge wa Manonga / Igunga Seif Khamis Gulamali akimpokea na kumpa sapoti ya safari yake Muigizaji wa Filamu za Kihindi Sanjay Dutt kwenda Mapumzikoni Mbuga za Wanyama Ngorongoro Mkoani Arusha Mapem leo



Muingizaji wa Filamu za Kihindi Sanjay Dutt akipanda ndege tayari kwa kuruka  kwenda Mapumzikoni Mbuga za Wanyama Ngorongoro Mkoani Arusha Mapema leo

RC MAKONDA ATOA SIKU SABA KUHAKIKISHA WIZI WA VIFAA VYA MAGARI UNAKOMESHWA MARA MOJA


Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mheshimiwa Paul Makonda leo ametoa siku saba kwa Kaimu Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam DCP Lucas Mkondya kuhakikisha wizi wa vifaa vya Magari unakomeshwa mara moja.

Akitoa maagizo hayo, Mheshimiwa Makonda amesema wizi wa vifaa vya magari vikiwemo Vioo, Radio, Side mirrow, Power Window,Taa pamoja na Shoo ya mbele na nyuma ya Gari vimekuwa vikishamiri kila kukicha jambo linalowakera wananchi na kuwapa hofu ya kuweka magari yao kwenye maegesho kwa kuhofia kuibiwa kitendo ambacho amesema hakivumiliki.

“Sitaki kusikia watu wanaibiwa vifaa vya Magari yao,watu wanaibiwa Vioo, Power Window,Radio, Taa,Side Mirror na wakati mwingine wanavunja vioo vya gari na kuiba Pochi na Laptop, sasa haiwezekani wizi wa namna hii uendelee kwenye Mkoa  wangu, sasa Kaimu Kamanda Kanda Maalumu nakuagiza na ninakupa siku saba sitaki kusikia wizi wa vifaa vya magari ukiendelea, nataka ifikie hatua mtu aweze kuegesha Gari lake na kulikuta likiwa salama” Alisema Makonda.

“Mwananchi yoyote atakaeibiwa na akapeleka taarifa Polisi na hatua za kisheria zichukuliwe atoe taarifa kwangu bahati nzuri wananchi wana namba zangu, haiwezekani Mwananchi anajikusanya na kununua gari alafu anaibiwa watu wanaiba vifaa vyake, wizi wa namna hii nasema Mwisho ndio umefika leo," Alisisitiza Makonda.

Aidha Makonda ameagiza Maduka na Vijiwe vyote vinavyouza vifaa vya Magari kujisajili mara moja iliviweze kutambulika na Serikali.“Kinachoshangaza ni kwamba hawa wanaoiba wana vijiwe vyao ambapo wanauza hivyo vifaa, ukienda Kariakoo, Magomeni na pia Temeke (Keko) kuna vijiwe ambavyo ukienda kule unakuta kifaa kilichoibiwa kwenye Gari lako kipo mtaani kinauzwa” Aliongeza Makonda.

Akipokea Maagizo hayo, Kaimu Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam  DCP Lucas Mkondya amesema kuwa maagizo hayo yanaanza kutekelezwa leo ambapo msako utaanza leo kuhakikisha Genge la wezi wa vifaa vya magari vinasambaratishwa.

Aidha amewaagiza Makamanda wa polisi Temeke, Ilala na Kinondoni kuanza utekelezaji wa maagizo hayo kuanzia leo na kuwataka wote wanaouza vifaa vya wizi kujisalimisha mara moja kwa Jeshi la Polisi.

RC RUKWA AITAHADHARISHA MANISPAA YA SUMBAWANGA KUTUMIA VIZURI BILIONI 1.1 ZA UKARABATI KANTALAMBA


Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Kamishna Mstaafu Zelote Stephen amewataka wale wote wanaohusika na usimamizi wa fedha za ukarabati wa moja ya shule Kongwe nchini, kuhakikisha kuwa fedha hizo zinatumika kama zilivyokusudiwa.

Ameyasema hayo baada ya kuzungukia maeneo yote ya shule yanayoendelea kukarabatiwa wakati alipofanya ziara ya kushtukiza ili kujionea hatua waliyofikia katika ujenzi na kutathmini kama thamani ya pesa inakwenda sambamba na ujenzi unaoendelea katika shule hiyo.

Shule ya Sekondari ya Kantalamba ni miongoni mwa shule kongwe 20 nchini ambazo serikali kupitia Wizara ya Elimu imeweka mpango wa kukarabati shule hizo kwa lengo la kutunza hadhi na kuziboresha zaidi. Ambapo shule hiyo imepata mgawo wa shilingi 1,123,353,700/=
“Tafadhalini sana Mwalimu Mkuu, Mkurugenzi, Afisa Elimu na sisi wote tuhakikishe kwamba shule hii imebadilika kwa kuwa hizi pesa si kidogo, bilioni sio hela kidogo, zisichezewe, zifanye kazi iliyokususdiwa na kazi yenyewe ioneshe sura ya bilioni, isijekutokea tukapata kazi nyingine ya kusema kwamba hizi pesa kazi iliyofanyika ni ya hovyo hovyo,” Mh. Zelote Alisisitiza.


Baada ya kuona juhudi zinazoendelea katika ukatabati huo Mh. Zelote amesifu uongozi wa shule wa kuajiri mafundi vijana waliopo mtaani ili kuwa na matumizi mazuri ya fedha hizo tofauti na kuwatumia wakandarasi ambao wangesababisha fedha nyingine zipotee bila ya sababu, na kusisitiza kuwa vijana hao wasimamiwe kwa ukaribu sana na kupewa maelekezo ili wasilipue kazi inayoendelea.  

Pamoja na hayo Mh. Zelote alilisisitiza uwazi kwenye matumizi ya fedha za umma, na kuwataka wakaguzi kuwa makini na kukagua kila hatua ya ujenzi na kuona kuwa kila senti inayotumika inaendana na thamani ya ujenzi inayoonekana. Aidha alizitaka Halmashauri zote Mkoani Rukwa kutenga bajeti kwa kupitia mapato yake ya  ndani ili kuboresha miundombinu ya shule jambo ambalo linaweza kubadilisha muonekano wa shule nyingi mkoani humo.
“Ningependa kuona shule hii inakuwa ya mfano kwakuwa ipo katika makao makuu ya mkoa na pia alishauri kujenga uzio na kuendeleza utunzaji wa mazingira kwa kuweka sharia kali kwa wanafunzi ili waendelee kutunza mazingira ya shule,” Mh. Zelote aliongezea.  

Awali alipokuwa akisoma taarifa fupi ya ukarabati wa shule kongwe Sekondari ya Kantalamba mwalimu Mkuu wa Shule hiyo Martin Kasansa alitaja changamoto kadhaa zinazorudisha nyuma kasi ya ukarabati wa shule hiyo ikiwemo uchakavu mkubwa wa bwalo uliosababisha kuanza upya ujenzi, upatikanaji wa baadhi ya vifaa mkoani Rukwa kuwa mgumu na kulazimika kuagiza kutoka mkoa wa Mbeya na kutopatikana kwa maji kumechelewesha ujenzi unaoendelea.  

“Kazi ya ukarabati ilianza rasmi mwezi June 2017 na inasimamiwa na mwandisi kutoka Chuo cha Sayansi na teknolojia Mbeya na inategemewa kumalika ndani ya miezi mitatu, lakini upatikanaji wa maji umekuwa ni tatizo katika eneo letu, ” Martin Alisema.
Ukarabati unaoendelea katika shule hiyo unahusisha mabweni 6, vyumba vya madarasa 14, ofisi za walimu, vyoo, mfumo wa maji safi na maji taka, mfumo wa umeme, jiko, bwalo, maabara pamoja na jingo la kilimo. Ambapo mapaka sasa Shilingi 648,051,540.90/= imeshatumika na kufikia asilimia Zaidi ya 58.

Nae Katibu Tawala wa Mkoa wa Rukwa Bernard Makali aliutaka uongozi wa shule kuangalia maeneo muhimu na kuweaza kuyamalizia ili wanafunzi wasiachwe nyuma na muhula wa mwaka huu na kusisitiza kuwa upishi wa kutumia kuni si mzuri na kuahidi kushikiana nao kutafuta namna ya kupikia kwa kutumia gesi jambo ambalo litatunza mazingira.

JAFO ATOA AGIZO KWA MAAFISA WA ELIMU KUBORESHA MAZINGIRA YA SHULE




Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Tamisemi Selemani Jafo akizungumza na wananchi wa kijiji cha Maneromongo katika mkutano wa kuhamasisha maendeleo. 
Ujenzi wa madarasa na mabweni unaoendelea katika shule ya sekondari Maneromango 
Wananchi wa kata ya Maneromango wakiwa katika mkutano wa pamoja na Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Tamisemi Selemani Jafo.

Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Tamisemi Selemani Jafo akishuhudia upangaji wa mawe katika moja ya majengo yanayojengwa wilayani Kisarawe.

…………………………………………………………………….

NAIBU Waziri, Ofisi ya Rais, Tamisemi Selemani Jafo ameagiza maafisa elimu nchini kuboresha mazingira ya shule za msingi na sekondari katika halmashauri zao wanazoziongoza ili ziwe na mandhari ya kuvutia.

Jafo ametoa maagizo hayo alipokuwa akitembelea ujenzi wa madarasa, vyoo, na mabweni katika wilaya ya Kisarawe.

Katika ziara yake, Jafo amefurahishwa sana na ujenzi unavyo endelea wilayani humo kwa ulazaji wa matofali katika majengo yote kutokana na ujengaji wa aina hiyo unayafanya majengo kuwa na ubora mkubwa.

Naibu Waziri Jafo ametaka mazingira ya shule zote nchini yawe safi kwa kupanga mawe pembeni na barabara, kupanda majani, maua na miti ili shule ziwe kivutio kwa watoto.

Jafo alitembelea na kukagua ujenzi katika Shule ya msingi Kwala ambayo kuna ujenzi wa vyumba vya Madarasa matatu, matundu ya vyoo kumi na mbili pamoja na ujenzi wa ofisi ya walimu.

Pia alitembelea ujenzi wa mabweni mawili, vyoo matundu kumi na sita, madarasa matatu, na ujenzi maktaba katika shule ya sekondari Maneromango ambayo inatarajiwa kuchukua wanafunzi wa kidato cha tano.

PROF. MBARAWA: FIDIA ZITALIPWA KWA WANAOSTAHILI KISHERIA



Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (kulia), akipokea taarifa kutoka kwa Mkandarasi wa Kampuni ya CHICO (katikati), anayejenga barabara ya Mwigumbi-Maswa KM 50.3 inayojegwa kwa kiwango cha lami ambao ujenzi wake umefikia takribani asilimia 77. 
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa, akizungumza na wananchi wa Wilaya ya Mwigumbi, wakati alipokagua ujenzi wa barabara ya Mwigumbi-Maswa KM 50.3 inayojengwa kwa kiwango cha lami. 
Muonekano wa sehemu ya Barabara ya Mwigumbi-Maswa KM 50.3 inayojengwa kwa kiwango cha lami mkoani Shinyanga. 
Meneja wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), mkoa wa Mwanza Eng. Marwa Rubirya (kushoto), akitoa taarifa kwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (kulia), kuhusu maendeleo yaliyofikiwa ya ujenzi wa barabara ya Usagara-Kisesa KM 16.135 inayojengwa kwa kiwango cha lami mkoani humo 

Muonekano wa sehemu ya Barabara ya Usagara-Kisesa KM 16.135 inayojengwa kwa kiwango cha lami mkoani Mwanza.

…………………………………………………………………

Serikali imesema itawalipa fidia kwa mujibu wa sheria wananchi wote waliopisha ujenzi wa barabara katika maeneo mbalimbali ya nchi.

Amesema hayo Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa wakati akizungumza na wananchi wa Mwigumbi mkoani Shinyanga alipokagua ujenzi wa barabara ya Mwigumbi – Maswa yenye urefu wa KM 50.3 inayojengwa kwa kiwango cha lami na mkandarasi wa Kampuni ya CHICO na kuridhishwa na kasi ya ujenzi wake ambao unagharimu kiasi cha Shilingi Bilioni 61.

“Kila anayestahili kulipwa fidia atalipwa kama sheria inavyoelekeza na endapo akatokea yeyote mwenye malalamiko Serikali ipo itamsikiliza”, amesema Waziri Prof. Mbarawa.

Amewataka wananchi kutoa ushirikiano kwa Mkandarasi na Viongozi wa Wakala wa Barabara (TANROADS), wa mkoa ili kuhakikisha barabara hiyo inakamilika kwa wakati na spidi inayotakiwa.

Aidha, Waziri Prof. Mbarawa amewahimiza makandarasi wote nchini kutoa kipaumbele cha ajira kwa wakazi wa maeneo husika inapopita miradi ya maendeleo ya ujenzi wa miundombinu mbalimbali ili kuwapatia kipato na kuinua uchumi wao.

Naye, Kaimu Meneja wa TANROADS mkoa wa Shinyanga Eng. Batholomeo Ndirimbi, amesema mpaka sasa tayari fedha zimetengwa kwa ajili ya ulipaji fidia na watahakikisha kuwa fedha hizo zinalipwa kwa watu sahihi wanaostahili fidia hizo.

“Tutasimamia zoezi hili kwa umakini na kutoa fidia kwa wale wote wanaostahili kisheria”, amesema Eng. Ndirimbi.

Ameongeza kuwa ujenzi wa barabara hiyo umefikiwa asilimia 77 na unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwaka huu.

Katika hatua nyingine, Waziri Prof. Mbarawa amekagua mradi wa ujenzi wa barabara ya Usagara-Kisesa KM 16.1 inayojengwa kwa kiwango cha lami ambapo ujenzi wake umefikia asilimia 75 na daraja la Nyashishi lenye urefu wa mita 67.9 ambalo ujenzi wake umekamilika kwa asilimia 99.5 mkoani Mwanza.

Kwa upande wake, Meneja wa TANROADS Mkoa wa Mwanza Eng. Marwa Rubirya, amesema ujenzi wa barabara hiyo unaendelea vizuri na mkandarasi atamaliza kwa wakati uliopangwa na viwango walivyokubaliana katika mkataba.

BANK OF AFRICA YAKABIDHI GREDA KWA MTEJA WAKE


BANK OF AFRICA imekabidhi rasmi mtambo wa ujenzi (Greda jipya aina ya JCB) lenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 300 kwa kampuni ya Dezo Civil Contactors Limited, kwa ajili ya kutekeleza miradi mbalimbali ya ujenzi ikiwemo kandarasi ya ujenzi wa kuta kwenye Pwani ya Bahari ya Hindi. 

Makabidhiano ya mtambo huu ni sehemu ya mpango endelevu wa benki wa kununua na kukodisha mitambo (lease finance), ambayo inawawezesha wateja kujiongeza kiutendaji kwa kupata vifaa vya kisasa bila ya kulazimika kuwa na pesa taslimu za manunuzi ya vifaa hivyo. 

Makubaliano haya ya ukodishaji wa mitambo yanaakisi katika sekta mbalimbali ikiwemo ujenzi, usafirishaji, teknolojia ya habari na mawasiliano, utalii, madini, mafuta na gesi.

BANK OF AFRICA imebaini huu ni mpango ambao una tija kubwa kwa wajasiriamali wakubwa kwa wadogo, kwa ajili ya kufanikisha uendeshaji wa biashara zao ambao utaongeza uzalishaji na faida kubwa. Mteja kupitia mpango huu anapewa fursa pana ya kufanya chaguo lake bila kikwazo chochote na bila ya uhitaji wa amana ya awali au dhamana nyingine. Marejesho ni malipo ya ukodishaji ya kila mwezi na mteja ana uwezo wa kuchagua kua mmiliki wa mali husika pindi ifikapo mwisho wa mkataba wa ukodishaji. 

Benki humsaidia mteja kuhakiki chombo anachotaka kuingianacho mkataba kama kina ubora ili kuweza kuinua uchumi wake na uchumi wataifa kwa ujumla.
Naibu Mkurugenzi mtendaji wa BANK OF AFRICA TANZANIA Bw. Wasia Mushi akikabidhi mfano wa funguo kuashiria makabidhiano ya Greda kwa Mteja Bw. T Hitesh Vishram ambae ni Project Supervisor wa Kampuni ya Dezo Civil Contractors Limited, Katikati ni meneja wa masoko, Utafiti na maendeleo wa BANK OF AFRICA TANZANIA Bw. Muganyizi Bisheko.

BENKI YA NMB YASHINDA TUZO YA BENKI BORA YA MAENDELEO AFRIKA 2017


BENKI ya NMB PLC imeshinda tuzo mbili katika sherehe za utoaji wa tuzo wa benki bora duniani zilizofanyika Jijini London, Uingereza. NMB Imetajwa kwa mara ya kwanza kuwa ni Benki Bora ya Maendeleo Barani Afrika huku tuzo ya pili ikiwa ni Benki Bora Tanzania 2017 hii ni mara ya Tano Mfululizo.

Kila Mwaka, Jarida la Euromoney huandaa hafla ya kuyatambua zaidi ya Makundi 20 ya bidhaa za kitaasisi za kifedha zikiwemo benki kote duniani kwa kuagalia benki bora na ya kiwango cha juu kwa kila bara na benki bora katika nchi takribani 100 duniani kote. Tuzo hii huzitambua taasisi za kifedha duniani kote ambazo zimepata mafanikio ya hali ya juu katika maeneo yao, kwa kuonyesha ugunduzi na kupata mafanikio ya kifedha kila mwaka.

Jarida ya Euromoney liliandika kuwa,“NMB siyo benki iliyo hai bali ni benki inayofanya kazi. Maamuzi makubwa yanafanyika kwenye maeneo ya mtaji, biashara na watu yamekuwa yanafanyika. Katika maboresho hayo, bado benki imeweza kutoa gawio zuri kwa wanahisa kuliko taasisi yoyote ya fedha nchini.”

Mkurugenzi Mtendaji wa NMB, Ineke Bussemaker alisema kuwa ubunifu katika huduma, tekinolojia na uwekezaji katika fedha za kielektroniki kwa msaada wa mtandao mpana wa matawi na ATM imechangia kuiboresha benki na kuifanya taasisi bora ya kifedha nchini.

“Kutatua changamoto za jamii ya watu wasiotumia huduma za kibenki nchini inachukua uwekezaji, ubunifu na uwezo wa kuwaleta wadau katika malipo na huduma zingine za kifedha,” alisema bi Ineke

Bi Ineke alisema “kuwa ushindi wa tuzo mbili kwa mpigo za benki ya maendeleo Afrika na benki Bora Tanzania ni kielelezo tosha kuwa juhudi zetu zinaonekana situ Tanzania bali Afrika nzima.”

“Tunatoa shukrani zetu wa wateja, wafanyakazi na washika dau wote kwa kuwa sehemu ya mafanikio haya makubwa kwa benk, “ alisema Bi Ineke na kuongeza kuwa NMB itaendelea na ahadi yake ya kuwapa huduma bora wateja wake sasa na siku za mbeleni.

Akizungumza kwenye hafla, Mhariri wa jarida la euromoney Bwana Clive Horwood alisema “mchuano wa kupata tuzo mwaka huu ulikuwa wa ushindani sana katika taasisi zilizoshiriki na hivyo kufanya uamuzi kuwa mgumu sana Benki zilizoshinda na kujipatia tuzo zetu zimechukua hatua kubwa katika mipango yao ya kibenki. Mabenki huko miaka ya mbele yatakuwa yanaangalia nini unafanya na pia nini ambacho hukifanyi. Mwaka huu, benki zilizong’ara zimetafsiri kwa unaga ubaga ni wapi kwenye nguvu Zaidi na kuzingatia maeneo hayo.”

ESRF YAANDAA MKUTANO KUJADILI BIASHARA NA UWEKAZAJI KATI YA TANZANIA NA CHINA


WAZIRI wa Fedha na Mipango, Mhe Dkt. Philip Mpango ametaka kuwapo na uratibu wenye maslahi mapana katika biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na China. 
 Alisema hayo wakati akifungua mkutano wa 6 wa mwaka wa ESRF unaozungumzia biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na China. Alisema mahusiano yaliyopo kati ya Tanzania na China ambayo ni ya kihistoria yasitumike vibaya bali yanahitaji kuratibiwa kiuangalifu kwa maslahi ya pande zote mbili. 
 Aliwataka washiriki wa mkutano huo wa mwaka kujadili kwa makini namna ya kuratibu vizuri vitega uchumi na biashara kwa manufaa ya nchi zote mbili. 
Alielezea kufurahishwa kuwapo na mada mbalimbali zinaozungumzia biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na China na kusema mada hizo zitumike vyema kuweka misingi mizuri yenye manufaa kwa pande zote mbili. Aidha aliipongeza ESRF kwa kuona haja ya kuwapo kwa mazungumzo ya aina hiyo na kusema kupitia tafiti mbalimbali taifa hili litaenda mbele katika kujenga uchumi wa viwanda. 
Mkutano huo unaohusisha washiriki mbalimbali wa ngazi za juu wa biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na China umeitwa kama sehemu ya mchango wa ESRF katika ujenzi wa uchumi wa viwanda wa Tanzania. “Sisi serikalini tunaridhishwa na juhudi zinazofanywa na taasisi za kitafiti kama hii zenye lengo la kusaidia juhudi za serikali za kuhudumia watu wake na kuongeza ustawi” alisema Mpango.
Mkutano huo ambao unazungumzia mahusiano ya kibiashara na uwekezaji umeelezwa na Mh. Dk Mpango kuwa moja ya mikutano inayotoa fursa za kuangalia uwekezaji wenye tija unaozingatia maslahi mapana ya mataifa husika. 
Alisema Tanzania na China zina uhusiano mzuri wa kihistoria na hadi sasa na kwamba kinachostahili ni kuoanisha uhusiano huo na kuuweka katika hali bora zaidi za kunufaisha pande zote mbili. 
Baadhi ya miradi mikubwa ambayo Tanzania imesaidiwa na China ni pamoja na ujenzi wa Reli ya Tanzania na Zambia (TAZARA) na kiwanda cha Urafiki; kuanzishwa kwa shamba la mpunga la Mbarali; kiwanda cha sukari cha Mahonda na mgodi wa mawe wa Kiwira. 
Kwa sasa China ni moja ya taifa lililo na uwekezaji mkubwa nchini Tanzania pia ikifanya shughuli nyingi za ujenzi zenye gharama kubwa kama daraja la Kigamboni na barabara. 
Naye Mwenyekiti wa bodi ya ESRF, Philemon Luhanjo, akimkaribisha Mheshimiwa Waziri Mpango alisema kwamba alisema kwamba mkutano huo umeandaliwa kwa pamoja kati ya ESRF na Chuo kikuu cha Kilimo cha China. Alisema mkutano huo umewaleta pamoja wanazuoni wa Kichina na Kitanzania kuangalia mahusiano yaliyopo na kutengeneza mustakabli bora wa namna ya kushirikiana. 
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Tafiti za Kiuchumi na Kijamii (ESRF), Dk. Tausi Kida amesema kwamba mkutano huo ni sehemu ya juhudi za kusaidia serikali kwa njia ya utafiti ambapo majibu yanatumiwa kutengeneza sera au majibu ya changamoto mbalimbali. Mkutano huo ulifungwa na Waziri Mkuu mstaafu, Mh. Dkt. Salim Ahmed Salim.
Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe Dkt. Philip Mpango akisoma hotuba kwa niaba ya Makamu wa Rais Mh. Samia Suluhu Hassan (hayupo pichani) wakati akifungua mkutano wa 6 wa mwaka wa ESRF unaozungumzia biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na China uliofanyika jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Tafiti za Kiuchumi na Kijamii (ESRF), Dk. Tausi Kida akitoa neno la ukaribisho kwa washiriki wa mkutano wa 6 wa mwaka wa ESRF unaozungumzia biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na China uliofanyika jijini Dar es Salaam. Mwenyekiti wa bodi ya ESRF, Philemon Luhanjo akizungumza machache kabla ya kumkaribisha mgeni rasmi kufungua mkutano wa 6 wa mwaka wa ESRF unaozungumzia biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na China uliofanyika jijini Dar es Salaam.Mwakilishi wa Ubalozi wa China nchini Tanzania anayeshughulikia wa Masuala ya Uchumi na Biashara, Lin Zhiyong akizungumza kwa niaba ya balozi wa China wakati wa ufunguzi wa mkutano wa 6 wa mwaka wa ESRF unaozungumzia biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na China uliofanyika jijini Dar es Salaam.Katibu Mkuu Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Profesa Adolf Mkenda akiwasilisha mada inayohusu namna watanzania wanavyoweza kunufaika na fursa za kibiashara na uwekezaji China wakati wa mkutano wa 6 wa mwaka wa ESRF unaozungumzia biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na China uliofanyika jijini Dar es Salaam.Pichani juu na chini ni sehemu ya washiriki kutoka China na Tanzania waliohudhuria mkutano wa 6 wa mwaka wa ESRF unaozungumzia biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na China uliofanyika jijini Dar es Salaam. Mwenyekiti ya Taasisi ya Utafiti wa Maendeleo China (CIDRN), Prof. Dr. Li Xiaoyun akitoa neno la ukaribisho kwa washiriki wa mkutano wa 6 wa mwaka wa ESRF unaozungumzia biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na China uliofanyika jijini Dar es Salaam.Balozi wa Tanzania nchini China, Mh. Mbelwa Kairuki akizungumzia namna ambavyo watanzania wanaweza wakafaidika na fursa za biashara na uwekezaji nchini China wakati wa mkutano wa 6 wa mwaka wa ESRF unaozungumzia biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na China uliofanyika jijini Dar es Salaam.Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Anthony Mtaka akiwasilisha mada inayohusu mahusiano ya kibiashara ya uwekezaji kati ya Tanzania na China kwa mtazamo wa Serikali za Mitaa wakati wa mkutano wa 6 wa mwaka wa ESRF unaozungumzia biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na China uliofanyika jijini Dar es Salaam.Kutoka kushoto ni Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Utafiti wa Uchumi na Jamii (ESRF), Dk. Tausi Kida, Balozi wa Tanzania nchini China, Mh. Mbelwa Kairuki, Waziri Mkuu mstaafu, Dkt. Salim Ahmed Salim, Mwenyekiti wa bodi ya ESRF, Philemon Luhanjo, Mwenyekiti na Afisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni za Infotech Investment, Ali Mfuruki wakifuatilia mada mbalimbali zilizokuwa zikiwasilisha wakati wa mkutano wa 6 wa mwaka wa ESRF unaozungumzia biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na China uliofanyika jijini Dar es Salaam.Mkutano ukiendelea.Balozi wa Tanzania nchini China, Mh. Mbelwa Kairuki pamoja na Waziri Mkuu mstaafu, Dkt. Salim Ahmed Salim wakifuatilia mada mbalimbali zilizokua zikiwasilishwa katika mkutano wa 6 wa mwaka wa ESRF unaozungumzia biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na China uliofanyika jijini Dar es Salaam.Profesa Humphrey Moshi kutoka idara ya Uchumi katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam akiwasilisha mada inayohusu uhusiano wa China na Tanzania katika masuala ya uwekezaji na biashara wakati wa mkutano wa 6 wa mwaka wa ESRF unaozungumzia biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na China uliofanyika jijini Dar es Salaam.Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka Maalum ya Uwekezaji (EPZA), Kanali Mstaafu Joseph Simbakalia akichangia maoni wakati wa mkutano wa 6 wa mwaka wa ESRF unaozungumzia biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na China uliofanyika jijini Dar es Salaam.Mwanachama wa Chama cha Wanafunzi walisomea China (CAAT), Linas Kahisha akielezea uzoefu wake katika fursa za kibiashara nchini humo katika mkutano wa 6 wa mwaka wa ESRF unaozungumzia biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na China uliofanyika jijini Dar es Salaam.Pichani juu na chini ni washiriki kutoka Tanzania na Chini waliohudhuria mkutano wa 6 wa mwaka wa ESRF unaozungumzia biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na China uliofanyika jijini Dar es Salaam.[/caption]Mgeni rasmi Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe Dkt. Philip Mpango, Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Utafiti wa Uchumi na Jamii (ESRF), Dk. Tausi Kida na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Anthony Mtaka wakiwa katika picha ya pamoja na wanafunzi watafiiti kutoka nchini China.Mkuu wa Idara ya Utafiti na Machapisho wa ESRF, Prof. Fortunata Makene (kushoto) katika picha ya kumbukumbu na Mkuu wa Idara ya Maarifa na Ubunifu wa ESRF, Bi. Margareth Nzuki (kulia) mara baada ya ufunguzi rasmi wa mkutano wa 6 wa mwaka wa ESRF unaozungumzia biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na China 
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Utafiti wa Uchumi na Jamii (ESRF), Dk. Tausi Kida (katikati), Mkuu wa Idara ya Maarifa na Ubunifu wa ESRF, Bi. Margareth Nzuki na Mwenyekiti ya Taasisi ya Utafiti wa Maendeleo China (CIDRN), Prof. Dr. Li Xiaoyun katika picha ya kumbukumbu.Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Anthony Mtaka (katikati) katika picha ya pamoja na washiriki kutoka TPSF na ESRF na Mshereshaji wa mkutano huo Eng. George Mulamula (kushoto).Baadhi ya washiriki kutoka China wakichukua baadhi ya makabrasha yenye taarifa mbalimbali zilizoandaliwa na ESRF wakati wa mkutano wa 6 wa mwaka wa ESRF unaozungumzia biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na China uliofanyika jijini Dar es Salaam.Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe Dkt. Philip Mpango akisalimiana na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Utafiti wa Uchumi na Jamii (ESRF), Dk. Tausi Kida alipowasili katika ufunguzi wa mkutano wa 6 wa mwaka wa ESRF unaozungumzia biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na China uliofanyika jijini Dar es Salaam.Mgeni rasmi Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe Dkt. Philip Mpango (katikati) akiongozana na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Utafiti wa Uchumi na Jamii (ESRF), Dk. Tausi Kida (kushoto) na Mwenyekiti wa bodi ya ESRF, Philemon Luhanjo baada ya kuwasili katika mkutano wa 6 wa mwaka wa ESRF unaozungumzia biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na China uliofanyika jijini Dar es Salaam. 
Mgeni rasmi Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe Dkt. Philip Mpango katika picha ya kumbukumbu na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Utafiti wa Uchumi na Jamii (ESRF), Dk. Tausi Kida mara baada ya kufungua mkutano wa 6 wa mwaka wa ESRF unaozungumzia biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na China uliofanyika jijini Dar es Salaam.