Wednesday, September 6

Tom Thabane alaani mauaji ya mkuu wa jeshi Lesotho

Thabane amesema mauaji hayo yanarudisha nyuma juhudi za kutafuta amani nchini humo
Image captionThabane amesema mauaji hayo yanarudisha nyuma juhudi za kutafuta amani nchini humo
Waziri mkuu wa Lesotho ameelezea mauaji ya mkuu wa kikosi cha jeshi Khoantle Mots'omots'o yaliyofanywa na maafisa wa jeshi kama kitendo cha kurudisha nyuma juhudi za kutafuta amani nchini humo.
Tom Thabane amesema upelelezi unaendelea juu ya tukio hilo lililotokea katika mji mkuu Maseru siku ya Jumanne.
Mashuhuda wanasema, watu wawili waliovalia sare za jeshi waliingia katika ofisi ya Mots'omots'o na kisha kumfyatulia risasi kabla ya wao kuuawa na walinzi wa kiongozi huyo.
Lesotho ipo katika hali ya taharuki, ikiwa na hostoria ya mapinduzi ya kijeshi ya mara kwa mara.

Virusi vya Zika vinaweza kutibu saratani ya Ubongo

Brain tumourHaki miliki ya pichaGETTY IMAGES
Image captionVirusi vya Zika vinaweza kutibu saratani ya Ubongo
Virusi hatari vinavyoweza kusababisha madhara kwa ubongo wa watoto vinaweza kusaidia kwenye matibabu mapya kwa saratani ya ubongo kwa mtu mzima, kwa mujibu wa wanasayansi nchini Marekani.
Hadi sasa virusi vya Zika vinaonekana tu kuwa tisho la afya duniani.
Lakini utafiti wa hivi punde unaonyesha kuwa virusi hivi vinaweza kuvamia na kuua seli zinazosababisha saratani ya ubongo wa mtu mzima.
Majiribio yaliyofanyiwa panya yalionyesha kuwa virusi vya Zika vilikula seli za saratani ya ubongo.
a virus in the brainHaki miliki ya pichaGETTY IMAGES
Image captionVirusi vya Zika vinaweza kutibu saratani ya Ubongo
Binadamu bado hawajafanyiwa utafiti huo, lakini wataalamu wanaamini kuwa virusi hiyo vinaweza kuingizwa kwa ubongo wa binadamu wakati wa upasuaji ili kuangamiza seli za saratani ya ubongo.
Pia matibabu hayo ya kutumia Zika yameonekana kufaulu kwenye sampuli za binadamu katika mahabara.
Kuna aina tofauti ya saratani ya ubongo. Aina ya Glioblastomas ndiyo maarufu zaidi kwa watu wazima na moja ya saratai ngumu zaidi kutibiwa.
Aina hii ya saratani husambaa kwa haraka, ikimaanisha kuwa ni vigumu kubaini imeanzia wapi na kuishia wapi.
Baby with microcephalyHaki miliki ya pichaREUTERS
Image captionZika huathiri zaidi watoto wanaozaliwa
Lakini utafiti wa hivi punde kwa panya walio hai na kwa sampuli za binadamu unaonyesha kuwa matibabu ya kutumia Zika yanaweza kuua seli ambazo ni sugu kwa matibabu ya kipindi hiki.
Wanasayansi wa Uingereza katika chuo cha Cambridge nao wameanzisha utafiti sawa na huo.
Dr Catherine Pickworth, kutoka taasisi ya utafiti wa saratani nchini uingereza anasema kuwa virusi vya Zika vilivyofanyiwa mabadiliko vinaweza kushambulia seli za saratani ya ubongo kwenye mahabara.

Rais Kenyatta: Ni haki yangu kuikosoa mahakama

Rais Uhuru Kenyatta akifanya kampeni katika eneo la Kajiado nchini KenyaHaki miliki ya pichaFACEBOOK/IKULU YA RAIS
Image captionRais Uhuru Kenyatta akifanya kampeni katika eneo la Kajiado nchini Kenya
Rais Uhuru Kenyatta ametetea hatua yake ya kuikosoa mahakama ya juu na jaji mkuu David Maraga kwa kubatilisha matokeo ya uchaguzi wa urais akisema ni haki yake kufanya hivyo.
Akizungumza katika kampeni za chama cha Jubilee katika kaunti ya Kajiado siku ya Jumanne, rais Kenyatta amesisitiza madai yake kwamba mahakama hiyo ya juu ilipuuzilia mbali haki ya wananchi ili 'kumfurahisha' mtu mmoja aliyemtaja kuwa mpinzani wake Raila Odinga.
''Nina hasira kwasababu nilikosewa.Walibatilisha uchaguzi wangu kimakosa.lazima tuseme ukweli'', alisema wakati wa kampeni za chama chake katika eneo la Kiserean.
Alisema kwamba licha ya kuwa anaheshimu uamuzi wa mahakama hiyo anajua kwamba alishinda uchaguzi huo kwa zaidi ya kura milioni 1.4.
Licha ya uamuzi huo bwana Kenyatta amesema kuwa ana imani atashinda tena.
Akiandamana na naibu wa rais William Ruto pamoja na viongozi wa chama tawala cha Jubilee, rais alisema kuwa hakuna kilichobadilika kwa kuwa Wakenya waliompigia kura watampigia kura kwa mara nyengine.
''Tulishinda kwa haki. Tulishinda kwa zaidi ya kura milioni 1.4, lakini mahakama ikaamua kutunyima ushindi wetu.Tuko tayari kwa uchaguzi mpya'', alisema bwana Kenyatta.

Australia kuwalipa wahamiaji dola milioni 55 kama fidia

Wahamiaji hao wote walipelekwa katika kituo kilichopo Manus walipokuwa wakijaribu kuingia nchini humo.
Image captionWahamiaji hao wote walipelekwa katika kituo kilichopo Manus walipokuwa wakijaribu kuingia nchini humo.
Hakimu mmoja nchini Australia amepitisha malipo ya zaidi ya dola milioni hamsini na tano kama fidia kwa wahamiaji waliokuwa wanashikiliwa na wanaoshikiliwa mpaka hivi sasa nje ya kituo cha kushikilia watu kilichopo katika kisiwa cha Manus.
Zaidi ya watu elfu moja mia tatu waliokuwa wanaomba hifadhi na wakimbizi watapokea malipo hayo, kama sehemu ya makubaliano nje ya mahakama na serikali yaliyofanyika mwanzoni mwaka huu.
Wahamiaji hao wote walipelekwa katika kituo kilichopo Manus baada ya kujaribu kuingia nchini humo.
Wanasema walizuiwa kinyume cha sheria hivyo kupata matatizo ya kisaikolojia na kimwili.
Wengi wa wanaoshikiliwa wanatoka nchini Iran, Iraq na Afghanistan.
Kituo hicho kitafungwa mwezi ujao.

Watakaosimamia uchaguzi wa urais Kenya wateuliwa

Mwenyekiti wa IEBC Wafula Chebukati
Image captionMwenyekiti wa IEBC Wafula Chebukati
Tume ya uchaguzi nchini Kenya imetangaza kundi la watu sita ambalo litasimamia uchaguzi wa urais wa tarehe 17 mwezi Oktoba katika hatua inayoonekana kuwatenga maafisa wakuu wa tume hiyo.
Wale waliotengwa ni mkurugenzi mkuu wa tume hiyo Ezra Chiloba, naibu wake Betty Nyabuto, mkurugenzi wa usajili wa wapiga kura pamoja na mkuu wa operesheni za uchaguzi Immaculate Kasait, naibu wake Mwaura Kamwati , mkuu wa operesheni za tume hiyo na mkuu wa teknolojia James Muhati.
''Katika uwezo wangu mimi kama afisa mkuu wa uchaguzi wa urais, nimewachagua maafisa wafuatao kuhudumu katika kusimamia uchaguzi wa urais utanaofanyika tarehe 17 mwezi Oktoba 2017'', alisema mwenyekiti wa tume hiyo Wafula Chebukati.
Atakayesimamia mahala pake Ezra Chiloba ni Marjan Hussein Marjan ambaye alikuwa naibu wake na alisaidia kusimamia miundo mbinu katika tume hiyo.
Bwana Marjana ambaye sasa atakuwa mshirikishi katika uchaguzi huo aliongoza tume hiyo katika eneo la Bomas , ambacho ndicho kilichokuwa kituo kikuu cha kuhesabu kura cha tume hiyo kupokea fomu za matokeo za 34B kutoka katika maeneo bunge.
Wadhfa wake bi Nyabuto umechukuliwa na Dkt Sidney namulungu ambaye atakuwa kiongozi wa operesheni huku kazi ya bi Kasait na bwana kamwati ikichukuliwa na bi nancy kariuki ambaye ataongoza kitengo cha mipango
Katika mabadiliko hayo bwana Chebukati alimbadilisha bwana Muhati na Albert Gogo.

Kifo cha ugonjwa wa Malaria chawashangaza madaktari Italia

Vimelea vya Plasmodium Falciparum vinavyobebwa na mbu wanaosambaza malaria vinaweza kuuwa mtu katika kipindi cha saa 24.Haki miliki ya pichaSCIENCE PHOTO LIBRARY
Image captionVimelea vya Plasmodium Falciparum vinavyobebwa na mbu wanaosambaza malaria vinaweza kuuwa mtu katika kipindi cha saa 24.
Msichana mmoja wa miaka minne amefariki kutokana na malaria ya ubongo kaskazni mwa Italia, eneo ambalo halina ugonjwa huo katika kile ambacho madaktari wanasema ni kisa kisicho cha kawaida.
Sofia Zago alifariki mjini Brescia siku ya Jumapili usiku baada ya kupelekewa huko akiwa na vipimo vya juu vya joto mwilini siku ya Jumamosi.
Italy haina mbu wanaosambaza ugonjwa huo, ukiwa ndio mbaya miongoni mwa magonjwa yote ya malaria.
Lakini baada ya jua kali la mwezi Agosti huenda ugonjwa huo umewasili nchini Italia.
Sofia alikuwa katika likizo na wazazi wake katika eneo la Bibione eneo la kitalii lilipo mji wa Venice.
Ni mara ya kwanza katika kipindi cha miaka 30 kuweza kuona kisa cha ugonjwa wa malaria kilichotoka eneo la Trentino, alisema Dkt Claudio Paternoster ambaye ni mtaalam wa magonjwa ya usambazaji katika hospitali ya Santa Chiara.
Tangu miaka ya hamsini ,italia haijawahi kupata kisa cha malaria kwa kuwa maeneo wanayozaana hutibiwa.
Kuna uvumi kwamba Sofia huenda alipata malaria hiyo kutoka kwa watoto wawili waliotibiwa katika hospitali ya Trento mnamo tarehe 15 mwezi Agosti .
Waliupata ugonjwa huo barani Afrika na kupona.
Vimelea vya Plasmodium Falciparum vinavyobebwa na mbu wanaosambaza malaria vinaweza kuuwa mtu katika kipindi cha saa 24.
Takriban watu 438,000 walifariki 2015 katika mataifa 95 ya eneo la tropiki ambapo ugonjwa huo ni janga.

Odinga apinga tarehe mpya ya uchaguzi Kenya

Raila OdingaHaki miliki ya pichaAFP
Image captionRaila Odinga
Kiongozi wa upinzani nchini Kenya Raila Odinga ametangaza kuwa hayuko tayari kushiriki marudio ya uchaguzi mkuu wa urais nchini humo.
Bwana Odinga amesema kuwa anataka kuwepo mikakati ya kisheria na kikatiba inayohitajika, kabla ya yeye kukubali kushiriki uchaguzi huo.
Bwana Odinga pia anataka mabadiliko kufanyiwa Tume ya uchaguzi nchini humo, ambayo imelaumiwa na mahakama ya juu kwa wa kuendesha uchaguzi kwa njia ambayo haiukuwa nzuri ambayo ilisababisha kufutiliwa mbali matokeo.
Jana Jumatatu Tume ya Taifa ya uchaguzi nchini Kenya ilitangaza kwamba uchaguzi mpya wa urais nchini humo utafanyika tarehe 17 Oktoba.
Mwenyekiti wa tume hiyo Wafula Chebukati alisema uchaguzi huo utashirikisha wagombea wawili pekee wa urais, Rais Uhuru Kenyatta na waziri mkuu wa zamani Raila Odinga.
"Hakutakuwa na uteuzi mpya wa wagombea wa urais katika uchaguzi huo upya. Waliopinga matokeo ya uchaguzi kortini, Bw Raila Odinga na mgombea mwenza wake Stephen Kalonzo Musyoka na mshtakiwa wa tatu Rais Uhuru Kenyatta na mgombea mwenza wake William Samoei Ruto, watakuwa ndio wagombea pekee," taarifa ya bw Chebukati ilisema.
Katika kufutilia mbali matokeo ya uchaguzi uliofanyika tarehe 8 Agosti, Mahakama ya Juu iliiwekea lawama Tume ya Uchaguzi.

Suala la nguvu za kiume laibuka bungeni



Naibu Waziri wa Afya, Dk Hamisi Kigwangalla
Naibu Waziri wa Afya, Dk Hamisi Kigwangalla 
Dodoma. Swali la mbunge wa Konde (CUF), Khatib Said Haji kuhusu nguvu za kiume limewaibua wabunge wengine wakitaka kuuliza maswali ya nyongeza, ingawa Naibu Spika, Dk Tulia Ackson hakuwapa nafasi.
Mbunge huyo ametaka kujua kuhusu ongezeko la wanaume wanaopungukiwa nguvu za kiume, hivyo kuhoji iwapo Serikali inalijua tatizo hilo.
"Kama jibu ni ndiyo, je, Serikali inachukua hatua gani kukabiliana na tatizo hilo ambalo linaondoa amani ndani ya nyumba na kwa nini Tanzania imekuwa ya 10 duniani miongoni mwa nchi zilizopoteza furaha," alihoji Haji.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Afya, Dk Hamisi Kigwangalla amesema Serikali inalitambua tatizo hilo ijapokuwa hakuna jibu la moja kwa moja kwa kuwa tendo la ndoa ni siri ya wanandoa.
Dk Kigwangalla ametaja baadhi ya sababu za kupungua nguvu za kiume ni umri wa zaidi ya miaka 60, maradhi sugu, kifua kikuu, kisukari, kansa, ukimwi na wanaotumia dawa muda mrefu.
Kuhusu wauza dawa zinazoelezwa kuwa zinaongeza nguvu za kiume, Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu ameagiza waganga wakuu wa mikoa kuwakamata wote ambao wanafanya hivyo na hawana vibali kutoka mamlaka husika.

Kampeni ya upimaji afya bure yaanza Dar

Dar es Salaam. Kampeni ya siku tano ya upimaji wa afya bure imeanza leo kwenye viwanja vya Mnazi Mmoja jijini hapa.
Upimaji huo utakaohitimishwa Septemba 10 unaendeshwa na madaktari bingwa na wauguzi zaidi ya 200 kutoka hospitali za umma, Jeshi na za watu binafsi.
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda alisema jana Septemba 5 kuwa upimaji wa afya bure unalenga kuwapatia  wananchi fursa ya kujua hali zao na kuwa na utaratibu wa kupima mara kwa mara.
Amesema kutakuwepo vifaa tiba vya kisasa, magari ya kubeba wagonjwa, vyoo, sehemu za watoa huduma na za kupumzika wakati wa kusubiri huduma.

Wanachama watatu CUF wafa ajalini



Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani, Onesmo Lyanga

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani, Onesmo Lyanga 


Dar es Salaam. Watu watatu wamefariki dunia na wengine watatu kujeruhiwa baada ya gari aina ya Toyota Noah kugongana na lori eneo la Ubena Zomozi mkoani Pwani usiku wa kuamkia leo.
Naibu mkurugenzi wa ulinzi na usalama wa CUF, Masoud Mhina akizungumzia ajali hiyo, amesema waliokufa ni wanachama wa chama hicho mkoani Tanga.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani, Onesmo Lyanga amesema ajali hiyo ilitokea saa 8:30 usiku wa kuamkia leo Septemba 6 baada ya Toyota Noah lililokuwa likitokea Dodoma kuhama njia na kugongana na lori.
Lyanga amesema lori hilo lilikuwa likiendeshwa na Yassin Hamad mkazi wa Dar es Salaam.
Amesema waliokufa katika ajali hiyo ni Uledi Salumaa (32) ambaye alikuwa dereva wa Toyota Noah, Mary Komba (40) na mwingine aliyetambuliwa kwa jina moja la Isack, wote wakazi wa Muheza mkoani  Tanga.
Kamanda Lyanga amewataja majeruhi wa ajali hiyo kuwa ni Juma Nindi, Chausiku Hassan na Esther Masie ambao pia ni wakazi wa Muheza.
Amesema miili ya marehemu imehifadhiwa katika Hospitali ya Tumbi mjini Kibaha na majeruhi walipelekwa kwa matibabu katika Kituo cha Afya Chalinze.
Kamanda Lyanga ametoa wito kwa madereva kuacha kuendesha kwa mwendo wa kasi na hasa usiku kwa kuwa madhara yake huwa makubwa.
“Niwatake madereva wote wanaoendesha magari usiku, ukijihisi umechoka weka gari pembeni pumzika. Ukilazimisha utakuwa kama huyu ambaye alihama upande wake na kugongana na lori,” amesema.

Kitendawili cha uchaguzi wa Rais Kenya





Kilichotokea Kenya Septemba Mosi 2017 ni mshtuko wa zaidi ya mripuko wa bomu. Ni tukio la kihistoria ambalo litakuwa na nafasi katika vitabu vya sheria za kikatiba duniani.
Ijumaa iliyopita Mahakama ya Juu ya nchi hiyo ilibatilisha matokeo ya uchaguzi wa urais wa Agosti 8, mwaka huu yaliomtangaza Rais Uhuru Kenyatta (55) kuwa mshindi wa urais.
Majaji wanne wa jopo la watu saba likiongozwa na Jaji Mkuu David Maraga walisema uchaguzi huo haujaendeshwa kwa mujibu wa Katiba na sheria, hivyo Kenyatta hatakuwa rais halali.
Waliitaka Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka nchini Kenya(IEBC), iandae uchaguzi mpya ndani ya siku 60.
Imekuwa ni tabia kwa uchaguzi unaofanyika katika nchi mbalimbali za Afrika kwamba upinzani unapotangazwa umeshindwa hukataa kuyatambua matokeo na huenda mahakamani kuyabishia. Pia, huko mahakamani hushindwa. Hali hiyo husababisha wananchi kupoteza imani kwa taasisi za “kidemokrasia”, ikiwamo mahakama katika nchi zao.
Wananchi hujiuliza, ikiwa wizi wa waziwazi wa kura unafanywa na Tume za Uchaguzi na Mahakama zinafumbia macho, ina maana gani kwa wananchi kwenda kupiga kura?
Mara kadhaa matokeo ya uchaguzi katika Afrika yanakuwa tayari yameshajulikana hata kabla ya kutangazwa na hata kabla ya chaguzi zenyewe. Inakuwa tu ni suala la kumtangaza na kumtawaza mtawala ambaye tayari ameshapangwa na walio na nguvu katika nchi.
Kenya sasa imejaribu kuuvunja mduara huu wa kikaragosi usiokuwa na haya wala aibu. Majaji huko Nairobi, japokuwa walimuona Rais Kenyatta hana makosa katika mchakato wa uchaguzi huo, lakini waliiona Tume ya Uchaguzi ya nchi hiyo imekwenda kinyume na Katiba na sheria.
Swali linazuka, ilikuwaje kwamba makamishna wa tume hiyo wakaachilia kwa kujua au labda kwa dharau, uchafu uliofanyika katika zoezi zima la uchaguzi uliomfaidisha Kenyatta?
Yawezekana wafanyakazi wa IEBC kwa kujipendekeza kwa Kenyatta walifanya hayo walioyatenda bila ya yeye mwenye kuwaamrisha kufanya hivyo.
Mara nyingi tumeona kwamba kwenye nchi zenye taasisi dhaifu za Serikali maofisa, hata bila ya kushawishiwa na wanasiasa walioko madarakani, hujipendekeza kwa wanasiasa hao na kutenda mambo yaliyo kinyume na viapo vyao vya utumishi wa Serikali.
Isisahaulike pia katika mifumo ya tawala za kidikteta utumishi wa Serikali ulio huru ni nadra. Mtumishi wa Serikali hutakiwa kwa uwazi awe si tu mtiifu wa Serikali, lakini hata pia kada wa chama tawala.
Udanganyifu iliofanywa katika uchaguzi wa Kenya na kuanikwa wazi mahakamani haujaupiku ule uliofanywa mwaka jana katika nchi ya Afrika Magharibi ya Gabon. Agosti 2016, Rais Ali Bongo katika kuwania urais wa nchi hiyo kwa mara ya pili, alishinda kwa shida kwa kupata asilimia 49.8 ya kura dhidi ya mpinzani wake, Jean Ping, aliyepata asilimia 48.2.
Wakati wote ambapo kura zilikuwa zikihesabiwa Ping alikuwa anaongoza, akiwa na asilimia 59 ya kura, wakati Ali Bongo akiambulia asilimia 37. Hadi karibu ya mwisho pale kura za jimbo anakotokea Ali Bongo zilipohesabiwa.
Kwa mshangao mkubwa ilitangazwa Bongo amepata asilimia 99.93 ya kura katika jimbo hilo, na watu waliojitokeza kupiga kura katika jimbo hilo walifikia asilimia 95.46. Udanganyifu uliofanyika ulikuwa wazi kabisa. Ghasia na fujo zikazuka mitaani na damu ikamwagika.
Mahakama Kuu ya Gabon ilimtangaza Bongo kuwa mshindi, akatawazwa na anabaki anatawala hadi leo. Pia, huko Kenya mwaka 2013, licha ya kuwa na sababu zaidi za kimsingi, upinzani, ukiongozwa na mgombea yuleyule Raila Odinga (72), haujaweza kufua dafu katika jaribio la kuishawishi mahakama itengue ushindi wa Kenyatta.
Hata mwaka huu kiongozi huyo wa Muungano wa Nasa, Raila Odinga hajawa na tamaa kubwa kwamba mahakama ingempa haki. Hasa alipungukiwa na tamaa pale jumuiya mbili zisizokuwa za kiserikali ambazo zilitaka kuishtaki IEBC kwa kuendesha uchaguzi ovyo zilipotishiwa kupigwa marufuku. Mara hii mahakama ya Kenya imekwenda mbali zaidi kuliko vile mahakama za nchi nyingine za Afrika zilivyowahi kufanya – si tu kusema kulikuwapo dosari hizi na zile katika zoezi la uchaguzi, lakini kuwa na ujasiri wa kusema kwamba dosari hizo ni kubwa mno kufanya matokeo ya uchaguzi mzima kuwa batili na matokeo yake yasitambuliwe.
Kabla ya matokeo ya uchaguzi wa Kenya kutangazwa, waangalizi wa kigeni wa uchaguzi huo walikuwa tayari wanataja kwamba uchaguzi huo uliendeshwa kwa haki na namna iliyo sawa. Kati ya waangalizi hao walikuwapo Taasisi ya Jimmy Carter ya Marekani, Umoja wa Ulaya, Umoja wa Afrika (AU) na Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Swali linaloulizwa ni je, imekuwaje waangalizi hao wa kimataifa wakafikia uamuzi huo ambapo Mahakama ya Juu nchini Kenya imeona vingine?
Japokuwa uangalizi wa kutoka nje ni jambo zuri na la kukaribishwa, lakini jambo hilo lichukuliwe kwa tahadhari. Waangalizi hao wanakuwa wachache mno kuweza kusimamia kila kituo cha kupigia kura, si wajuzi waliobobea na siasa za undani za Afrika na hukaa siku chache kabla na baada ya uchaguzi, hivyo si rahisi kutoa makadirio ya kina.
Uchaguzi mtu hashindi tu katika siku ya kupiga kura, bali hushinda kwa kupitia zoezi zima, tangu uandikishaji wa wapiga kura, upigaji na kuhesabiwa na kusafirisha kura kutoka kwenye vituo pamoja na kutangazwa matokeo. Pia, yasidharauliwe masuala ya usalama wakati wa kampeni za uchaguzi na uhuru waliokuwa nao wagombea wakati wa kampeni zao. Kwa hivyo, inafaa tuwe waangalifu, tusiamini kila kitu kinachosemwa na waangalizi wa nje.
Swali jingine linaloulizwa ni kama IECB itaweza kuutayarisha uchaguzi mpya ndani ya siku 60 kama mahakama ilivyotaka. Mabishano yameshaanza kati ya Jubilee na Nasa.
Odinga na muungano wa Nasa hawana imani na IEBC na wanataka viongozi wa tume hiyo waliochangia katika uchakachuaji uliofanywa wafikishwe mahakamani.
Wangepanda uchaguzi mpya usimamiwe na chombo kingine na si IEBC, labda Umoja wa Mataifa. Kenyatta na Jubilee wanataka uchaguzi huo usimamiwe na IEBC ileile na tarehe ya uchaguzi itangazwe kwa haraka kama inavyowezekana. Wanasema wao wako tayari na mara hii watashinda zaidi kuliko hapo kabla.
Mashambulizi kwa mahakama
Jambo la kushtua ni kwamba Rais Kenyatta na makamu wake ambaye pia ni mgombea wake mwenza, William Ruto wameushambulia vikali uamuzi wa Mahakama Kuu ya Kenya na kuwavurumishia matusi majaji waliotoa uamuzi huo.
Kufanya hivyo inaonesha vipi wanasiasa hao wawili wasivyostahamili jambo lolote ambalo haliambatani na matakwa yao; ni harufu ya udikteta.
Wanasahau kwamba mahakama ni muhimili wa tatu huru katika demokrasia yeyote ile. Haitakiwi kutishwa na rais na makamu wake. Cha kushtusha zaidi ni kwamba Jubilee wamewasingizia majaji hao mambo ya uongo na kuitisha mahakama, hiyo kwamba itaona cha mtema kuni siku zijazo.
Ni Kenyatta huyohuyo aliyemshawishi Odinga baada ya uchaguzi uliopita wa Agosti 8 akalalamike mahakamani kama kaonewa na si kwenda barabarani.
Odinga amefanya hivyo, na sasa Kenyatta analalamika na kuwaita majaji “wakora.” Ni Kenyatta huyohuyo aliyeisifu mahakama hiyo mwaka 2013 pale ilipoamua na kuhakikisha kwamba yeye ni mshindi wa uchaguzi wa urais wa mwaka huo, naye Odinga akatoka patupu.
Leo Kenyatta anataka kuilazimisha mahakama ipigie magoti matakwa yake. Hii ni aibu ya hali ya juu na yaonesha kuna wanasiasa wanaopiga porojo tu pale wanapozungumzia juu ya uhuru wa mahakama na utawala wa sheria chini ya Serikali zao.
Kwa “kufunguka kisanduku cha uchawi huko Kenya”, sasa yamechomoza matumaini kwa Afrika. Bila ya kujali ikiwa Kenyatta atamshinda Odinga katika uchaguzi mpya - mara hiyo labda kwa njia safi- muhimu ni kwamba sheria katika Kenya si kitu kilichopotea kabisa.
Mahakama ya Kenya, kama alivyosema Odinga, imeinusuru hadhi ya Afrika na kwamba Afrika sasa haitakamata mkia linapokuja suala la haki. Kenya imeweka mfano mzuri kwa nchi nyingine za Afrika, tena bila mbwembwe.
Mwakani watawala wa muda mrefu katika Afrika, Paul Biya wa Cameroon na Robert Mugabe wa Zimbabwe, watataka wachaguliwe tena. Wao ni wazoefu na maarufu linapokuja suala la wizi wa kuchakachua katika uchaguzi na pia majeshi yao ni hodari katika kuwapiga mikong’oto wapinzani.
Kutokana na mambo yalivyochomoza huko Nairobi, wazee hao wawili sasa hawatakuwa tena na “mambo poa tu” katika chaguzi zijazo nchini mwao.

Acacia yaanza kukabidhi Buzwagi


Dar es Salaam. Baada ya Acacia kutangaza kupunguza operesheni zake Bulyanhulu, kampuni hiyo imeanza kuikabidhi Serikali baadhi ya mali zake kwenye Mgodi wa Buzwagi ambao unatarajiwa kufungwa miaka mitatu ijayo.
Katika utekelezaji wa makabidhiano hayo, jana kampuni hiyo iliikabidhi Serikali uwanja wa ndege uliopo katika mgodi huo. Huu ni mgodi wa pili kufungwa na kampuni hiyo baada ya ule wa Tulawaka ambao iliuuza kwa Shirika la Taifa la Madini (Stamico) mwaka 2013.
Jana, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga,  Zainab Telack alisema hiyo ni hatua ya awali katika mchakato wa mgodi huo kusitisha shughuli zake za uchimbaji madini kwa mujibu wa mkataba uliopo.
“Tumeanza na uwanja wa ndege baadaye tutakabidhiwa majengo na vitu vingine kama ulivyo utaratibu,” alisema Telack.
Alisema Desemba mwaka huu utakuwa mwisho wa shughuli za uchimbaji na baada ya hapo wataanza kusaga mawe yaliyochimbwa kwa miaka mitatu mfululizo mpaka 2020.
Juzi, kampuni hiyo ilitoa taarifa ikibainisha lengo lake la kupunguza operesheni zake kwenye Mgodi wa Bulyanhulu baada ya kuzuiwa kusafirisha mchanga wa dhahabu tangu Machi hivyo gharama za uendeshaji kuwa juu kuliko ilivyotarajia huku mapato yakishuka.
Kwa miezi sita ya kutosafirisha mchanga huo, Acacia imedai kuwa imepoteza zaidi ya Sh583 bilioni.
Katika utekelezaji wa mkakati wake wa kubana matumizi, kampuni hiyo inatarajia kupunguza wafanyakazi na kandarasi mbalimbali ilizonazo. Kwa sasa, ina wafanyakazi 1,200 na wakandarasi 800 kwenye Mgodi wa Bulyanhulu.
Taarifa hiyo pia ilibainisha kucheleweshwa kwa leseni za wakandarasi wa machimbo ya chini ya ardhi kwenye Mgodi wa Buzwagi jambo linaloongeza changamoto.
Ingawa mazungumzo baina ya Serikali na kampuni ya Barrick inayomiliki asilimia 64 ya hisa za Acacia bado yanaendelea, uamuzi wa kupunguza operesheni kwenye mgodi huo unatarajiwa kupunguza uzalishaji kwa karati 100,000 kutoka kati ya karati 850,000 hadi 900,000 zilizokadiriwa awali.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa Jumatatu, bei ya hisa zake kwenye Soko la London (LSE) ilishuka kwa asilimia sita mpaka Pauni 1.94 huku kwenye Soko la Dar es Salaam (DSE) ikishuka kutoka Sh5,940 mpaka Sh5,400 jana mchana. Tangu kutolewa kwa zuio hilo, bei ya hisa hizo imepungua kwa asilimia 65.
Taratibu za kupunguza operesheni zake kwenye Mgodi wa Bulyanhulu zitakamilika ndani ya miezi mitatu na kampuni hiyo inaamini itatengamaa kuanzia mwakani.