Saturday, January 12

UTATA KUHUSU MUONEKANO WA DARAJA LA MANZESE


Picha hii imekua ikisambaa kwenye mitandao ya kijamii wakidai kuwa huu ndiyo utakua muonekano wa daraja la Manzese. ....

Mdau wa tulonge amejaribu kufanya uchunguzi kugundua kuwa hii ni project ambayo ilipangwa kufanywa na wachina huko Thailand mwaka 2010.....

Mimi binafsi pia sijawahi sikia serikali ikisema kuwa huu ndiyo utakua muonekano wa daraja la Manzese na Morogoro road kwa ujumla.....

Kama kuna mdau anafahamu mengi kuhusu hili atujuze ili tusije tukawa tunadanganyana na kufarijiana.....





POLISI WATANO WATIWA MBARONI KWA UPOTEVU WA MILIONI 150 KATIKA TUKIO LA WIZI LILILOTOKEA KARIAKOO HIVI KARIBUI




Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam linashikilia askari Polisi watano kwa tuhuma za kuhusika na upotevu wa Sh milioni 150 zilizoporwa na watu wanaosadikiwa kuwa majambazi eneo la Kariakoo.

Sambamba na askari hao pia wamekamatwa watu wawili wanaodaiwa kuhusika na tukio hilo ambao ni Deogratias Kimaro (30), mkazi wa Kalakata na Kulwa Mwakabala (30) mkazi wa Kijiwesamli Ilala.

Akizungumza na waandishi wa habari jana Dar es Salaam, Kamanda wa Kanda hiyo, Suleiman Kova alisema askari hao wanashikiliwa kutokana na uchunguzi wa kina uliofanywa na jopo la upelelezi likiongozwa na Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai wa Kanda hiyo, Ahmed Msangi.

Alisema baada ya tukio hilo zilipatikana taarifa kwamba fedha hizo zilipotea baada ya mtuhumiwa Augustino Kayula au Frank Mwangiba, kukamatwa akiwa na bastola aina ya Browning bila fedha zilizoporwa wakati inasemekana ndiye aliyepora fedha hizo akiwa na wenzake.

“Askari hawa tunawashikilia na tayari mashitaka ya kijeshi yameanza huku uchunguzi ukiendelea na utakapokamilika, tutapeleka jalada kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa hatua za kisheria ili kuleta uwazi na uwajibikaji ndani ya jamii yetu”.

Alisema Jeshi hilo limekuwa likionesha uwajibikaji ambapo mwaka jana pekee askari 20 walichukuliwa hatua mbalimbali za kinidhamu.

Aidha, alisema majina ya askari hao yanahifadhiwa kwa sasa, kwa ajili ya usalama na wakati ukifika yatawekwa wazi huku polisi wakiendelea na upelelezi na gwaride la utambulisho.

Alisema baada ya tukio hilo kulikuwa na taarifa zenye kutuhumu askari hao juu ya upotevu wa fedha hizo na ndipo uchunguzi ulipoendelea ili kubaini ukweli.

“Baada ya uchunguzi wa kina na ushahidi uliokusanywa, umefanya askari hao washikiliwe na kuhojiwa … pamoja na uchunguzi askari kwanza watajibu mashitaka ya kijeshi,” alisema.

Katika tukio hilo la uporaji Desemba mwaka jana, inadaiwa Kayula na wenzake wakiwa wamepanda pikipiki mtindo wa ‘mshikaki’, walivamia duka la Kampuni ya Artan Limited na kupora Sh milioni 150, zilizokuwa zikitolewa dukani Kariakoo kwenda benki, ambapo watu watatu walipoteza maisha.

Waliopoteza maisha ni pamoja na mtuhumiwa Kayula, Sadiki Juma (38) na Ahmed Issa (55) waliopigwa risasi na majambazi katika eneo la tukio.

Katika hatua nyingine, Kova alikanusha taarifa kwamba alisema ameunda tume ya kuchunguza tukio la kiongozi wa Jumuiya ya Madaktari, Dk Stephen Ulimboka badala yake akasema ameunda Jopo la Upelelezi.

MCHAKATO WA KATIBA:Mtikila aibua mapya



MAKUNDI maalumu jana yaliendelea kutoa maoni yao kwenye mchakato wa Katiba Mpya, huku DP kikipendekeza Rais aapishwe baada ya siku 90 tangu kumalizika kwa Uchaguzi Mkuu.
Mbali na maoni hayo yaliyowasilishwa na Mwenyekiti wa chama hicho, Mchungaji Christopher Mtikila, makundi mengine; wakulima, wafugaji, wanahabari na Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) nayo yalijitokeza kutoa moyoni.
Mtikila alisema kipindi hicho cha siku 90 kitatoa fursa kwa watu wanaotaka kuwasilisha pingamizi dhidi ya ushindi wa Rais mteule kufanya hivyo, kabla ya kuapishwa.
Alisema pingamizi linaweza kufanyiwa kazi kwa kipindi hicho cha miezi mitatu ili kuhakikisha kuwa taifa linapata kiongozi halali mwenye ridhaa ya wananchi.
“Pia tunataka kinga ya Rais ikome pale anapomaliza muda wake wa uongozi, kama alifanya makosa yoyote ya jinai aweze kushtakiwa ili kujenga nidhamu ya uongozi katika ofisi ya umma. Utaratibu wa kumwondoa madarakani uimarishwe asisubiriwe hadi amalize muda wake wa uongozi.”
Alisema kuwa Katiba ya nchi inapaswa kuwa mali ya wananchi wenyewe ili watawala wasijihusishe katika kuwaundia wananchi Katiba kama ilivyo kwa mchakato unaoendelea sasa wa kupata Katiba Mpya.
“Kumekuwa na hoja ya kuwapo kwa Serikali ya Tanganyika, hilo ni jambo muhimu na watu kutoka Tanganyika ni lazima wawe na Serikali yao ndani ya mipaka ya ardhi yao kupitia Katiba Mpya,” alisisitiza Mchungaji Mtikila.
Aliongeza kuwa nafasi za wabunge wa viti maalumu bungeni ziondolewe ili viti hivyo vishindaniwe kidemokrasia. Alisema wanawake wanatakiwa waelimishwe na kupikwa ili wahimili ushindani katika medani za kisiasa. Alisema kuwa taifa linahitaji viongozi bora na siyo kustarehesha jinsia.
Jukwaa la Wahariri
Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) limependekeza Katiba ijayo kutambua uhuru wa vyombo vya habari, haki ya kupata habari na uhuru wa kutoa mawazo.
“Kwa Katiba hii na sheria nyingine yoyote isiyoendana na Katiba hii, milele haitaruhusiwa kudhibiti habari nchini Tanzania,” ilieleza taarifa hiyo.
TEF ilisema kuwa haitakiwi kuwe na vikwazo katika kuanzisha magazeti au vyombo vya habari binafsi, kwamba wahariri na wachapishaji wa magazeti na vyombo vingine vya habari hawatakiwi kudhibitiwa au kuingiliwa na Serikali.
“Chombo chochote cha habari chenye wajibu wa kusambaza taarifa kwa jamii ambacho kinachapisha taarifa kuhusu, au dhidi ya mtu yeyote kinawajibika kutoa fursa ya kuchapisha mawazo ya upande wa pili, ikiwa yapo, kutoka kwa mtu ambaye taarifa au chapisho linamhusu,” ilieleza taarifa hiyo.
Vilevile, wamependekeza kuwe na sheria ya Bunge ya kuanzisha Baraza la Habari la Taifa, ndani ya miezi sita tangu siku ya kuanza kutumika kwa Katiba Mpya, baraza ambalo litakuwa na wajumbe 15 kutoka katika taaluma mbalimbali.
“Wajibu wa Baraza la Habari la Taifa itakuwa ni kusimamia vyombo vya habari, kuweka viwango vya kitaaluma kwa vyombo vya habari, kufuatilia utekelezaji wa viwango vilivyowekwa, kukuza taaluma na weledi katika vyombo vya habari,” ilisema taarifa hiyo na kuongeza;
“Kusikiliza mashauri au malalamiko dhidi ya vyombo vya habari, gharama za uendeshaji wa baraza. Kwa mujibu wa Katiba hii, Baraza la Habari la Taifa ndicho kitakuwa chombo cha mwisho katika kusimamia tasnia ya habari nchini.”
Katika suala la haki ya kupata habari, TEF imesema kila mwananchi ana haki ya kupata taarifa zozote hata zile zilizopo mikononi mwa Serikali.
Katika suala la uhuru wa kutoa mawazo Jukwaa hilo limeeleza kwamba kila mtu ana uhuru wa mawazo unaohusisha uhuru wa kutafuta, kupokea au kutoa taarifa au mawazo.
Baraza hilo limesema kuwa uhuru huo hautahusisha propaganda kwa ajili ya vita, uchochezi wa kuanzisha vurugu, hotuba za chuki, utetezi wa chuki, ukabila, ubaguzi kwa watu wengine au kuchochea mapambano.
Mtandao wa Jinsia
Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) umetaka Katiba Mpya iwe na dira ya kitaifa inayosisitiza ustawi wa wananchi katika kujenga mazingira ya kuwezesha mihimili mitatu kufanya kazi zake.
Mwenyekiti wa TGNP, Mary Rusimbi alisema kuwa moja ya mambo muhimu ambayo Katiba kwa kupitia itikadi hiyo inapaswa kuyasimamia na kuyastawisha ni haki za wanawake.
“Mchango wa mwanamke ni lazima utambulike kikatiba. Wanawake wana mchango mkubwa katika suala zima la malezi na uzalishaji mali wa aina mbalimbali, hivyo rasilimali za nchi pamoja na bajeti ya nchi zinapaswa kuwanufaisha wanawake kama ilivyo kwa wanaume,” alisema Rusimbi.
Profesa Ruth Meena alisema ni wajibu wa Serikali kuhakikisha mwanamke hafi kwa matatizo ya uzazi kwa kuboresha huduma ya uzazi katika hospitali zote nchini.
“Pia tunataka kuwapo na uwajibikaji wa viongozi. Viongozi ambao hawatimizi wajibu wao wanapaswa kujiuzulu badala ya kusubiri hadi wamalize muda wao wa uongozi, uwe wa miaka mitano au zaidi. Katiba ya sasa haiwapi wananchi mamlaka ya kuwawajibisha viongozi wazembe,” alisema Prof Meena.
Kuhusu Viti Maalumu, Profesa Meena alisema vinapaswa kuboreshwa ili hata wanawake ambao hawana chama cha siasa waweze kuwa na fursa ya kuteuliwa au kuchaguliwa kushika nafasi za uongozi.
Alisema kuwa kwa mfumo wa sasa ni wanawake walio kwenye vyama tu ndiyo wenye haki ya kupata nafasi za viti maalumu.
Wakulima
Wakulima nchini wametaka Katiba Mpya iweke uwiano sawa katika ugawaji wa ardhi kati ya wakulima na wafugaji ili kuondoa migogoro ya mara kwa mara.
Mwenyekiti wa Chama cha Wakulima Taifa (Taso), Engelbert Moyo alisema hatua hiyo itasaidia kuondoa migogoro ya wakulima na wafugaji na kuimarisha uchumi wa nchi.
“Tunapozungumzia wakulima hata ufugaji unaingia hapo ndiyo maana tukaona kuna haja ya kupendekeza kuwe na maeneo maalumu ya kufanyia shughuli hizo. Katiba iwe chanzo cha kuondoa migogoro hiyo kwa kuweka uwiano sawa katika ugawaji ardhi,” alisema na kuongeza;
“Kama Katiba Mpya itasema hivyo kwamba kutakuwa na ugawaji sawa wa ardhi kwa wakulima na wafugaji itasaidia kuondoa migogoro ambayo inaibuka mara kwa mara kati ya wakulima na wafugaji kitu ambacho hakileti picha nzuri kwa taifa letu.”
Alisema zaidi ya asilimia 80 ya uchumi wa taifa unategemea kilimo, lakini bado maisha ya wakulima yapo chini kitu ambacho ni vyema Katiba Mpya ikaliona.
Wafugaji
Umoja wa Wafugaji, umependekeza Katiba Mpya ijayo ianzishe sheria mpya ya ardhi kwa jamii pamoja na kutambua na kulinda mila na tamaduni za jamii mbalimbali nchini.
“Katiba itambue miliki ya pamoja ya ardhi kwa wafugaji inayoratibiwa na taasisi za jadi kwa mujibu wa sheria za mila za jamii mbalimbali,” alisema William Olenasha.
Alisema kitendo cha hakimiliki ya ardhi kuwa mikononi mwa Rais ni kuwanyima haki wananchi hususan wafugaji.
Rehema Mkalata, mfugaji kutoka Morogoro alisema kwa muda mrefu jamii ya wafugaji imeonekana kuwa ni jamii ya watu duni ndiyo maana hata matatizo yao hayapewi kipaumbele.
Alisema kuwa ni matarajio yake kwamba Katiba Mpya itawatambua jamii ya wafugaji kuwa na thamani sawa na watu wengine.
Pia alisema kuwa Katiba Mpya inatakiwa kuzitambua dawa asilia kuwa zinafaa kwa ajili ya matumizi ya binadamu.

Imeandikwa na Fidelis Butahe, Aidan Mhando, Ibrahim Yamola na Matern Kayela.