Saturday, December 2

SUMATRA, TABOA KUJADILI KANUNI ZA ADHABU


WAMILIKI wa vyombo vya usafiri hapa nchini wanatarajia kukutana na Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (Sumatra) kujadili kanuni za adhabu zinazotarajiwa kuanza Januari, mwakani.
Akizungumza Dar es Salaam jana, Mweka Hazina wa Chama Cha Wamiliki wa Mabasi ya Mikoani (Taboa), Issa Nkya, alisema mkutano huo unatarajiwa kufanyika leo na watajadili kupunguza adhabu hizo na kutenganisha makosa ya mmiliki na dereva.
Alisema kanuni hizo zimetungwa makusudi ili kuwakomoa wamiliki wa vyombo vya usafiri, hali inayoweza kusababisha wadau hao kushindwa kutoa huduma hiyo.
“Tunatarajia kufanya kikao na Serikali ambacho kitakuwa na jukumu la kupunguza adhabu na kutenganisha makosa kati ya mmiliki na dereva, jambo linaloweza kupunguza malalamiko,” alisema Nkya.
Alisema sheria hizo zimetungwa na Sumatra na zinaonyesha kuwa, mmiliki anatakiwa kulipa faini ya makosa 57 kwa siku ambayo ni kiasi kikubwa ikilinganishwa na gharama nyingine za usafirishaji, zikiwamo mafuta na kodi.
Alisema ikiwa Sumatra itaendelea na msimamo wake wa kutopunguza adhabu hizo, watalazimika kufanya mgomo hadi watakapohakikisha suala hilo linashughulikiwa.
“Hatuwezi kulipa zaidi ya shilingi milioni moja kwa siku kutokana na faini za barabarani, wakati magari yanahitaji mafuta na kulipiwa kodi, hivyo basi kama Sumatra inaendelea na msimamo wake, tutalazimika kuweka mabasi yetu nyumbani,” alisema.
Kutokana na hali hiyo, alisema katika marekebisho hayo, wameiomba Serikali kutenganisha makosa yatakayomhusu mmiliki na dereva, ili kila mmoja aweze kubeba jukumu lake
Alizitaja baadhi ya faini hizo ni pamoja na dereva na kondakta wakivaa sare chafu mmiliki anatakiwa kulipa faini ya Sh 200,000, kuzidisha abiria Sh 250,000, kushindwa kuweka sanduku la huduma ya kwanza Sh 250,000, kuzidisha saa tofauti na muda uliopangwa Sh 250,000.
Alizitaja nyingine kuwa kuzidisha mwendo kasi Sh 250,000, taa ya indiketa ikiharibika Sh 250,000, basi lisilokuwa na ndoo ya uchafu Sh 250,000, wakipiga muziki usio na maadili Sh 250,000, ukikosa ‘reflector’ Sh 100,000, kuweka leseni ya Sumatra sehemu isiyohusika Sh 100,000, dereva kutokuwa na leseni Sh 250,000.
“Kila mwaka mmiliki anatakiwa kuandika ripoti ambayo itawasilishwa Sumatra ili waweze kuangalia utendaji wao na asipofanya hivyo anatakiwa kulipa faini ya shilingi 100,000.
“Itafika kipindi tutashindwa kufanya kazi, kwa sababu faini zilizopo kwa siku ni zaidi ya shilingi milioni moja, hali ambayo inatukatisha tamaa,” alisema Nkya.

Rushwa na ufisadi si ajenda pekee ya upinzani


Hivi karibuni mwanasiasa mmoja amehamia CCM kwa madai kuwa eti ajenda ya rushwa ya chama alichotoka sasa inashughulikiwa kikamilifu kabisa na CCM.
Kamusi ya Kiswahili Sanifu, Tuki, Oxford, Toleo la 3 ukurasa 484 inaelezea neno rushwa kuwa ni fedha au kitu cha thamani kinachotolewa na kupewa mtu mwenye madaraka ya jambo fulani ili mtoaji apewe upendeleo. Yaani hongo, mrungura au kadhongo. Lakini neno linalovuma zaidi siku hizi ni ufisadi. Kamusi niliyoirejea hapo juu punde tu inaelezea neno hili kwa maana tatu. Kwanza ni tendo la kuleta maovu au uharibifu katika jamii, pili, upokeaji au utoaji wa hongo; na tatu, ni wizi wa mali ya umma au Serikali. Kenya walianza kulitumia neno ufisadi kwa nguvu zaidi katika kashfa ya Goldenberg iliyoikumba nchi hiyo takriban miongo miwili iliyopita.
Neno ufisadi linatokana na kitenzi fisidi, ambacho kinaelezwa na kamusi hiyo kuwa ni kufanya uharibifu au ubadhirifu, iba mali ya umma, tumia kwa njia mbaya, haribu, potoa na hujumu.
Kwa kifupi basi ufisadi unajumuisha rushwa ya juu kabisa, kwa kimombo, grand corruption.
Ibara ya 9(c) ya Katiba ya Tanzania inasema kuwa; mamlaka ya nchi na vyombo vyake vyote vitawajibika kuelekeza sera na shughuli zake zote katika lengo la kuhakikisha kwamba shughuli za Serikali zinatekelezwa kwa njia ambazo zitahakikisha kwamba utajiri wa taifa unaendelezwa, unahifadhiwa na unatumiwa kwa manufaa ya wananchi wote kwa jumla na pia kuzuia mtu kumnyonya mwingine.
Pili, mwanasiasa yule aliyehamia CCM yafaa amaizi kwamba hakuna chama cha siasa chenye ajenda moja tu duniani. Siku zote ajenda hubadilika kulingana na nyakati zilizopo. Mathalan sasa hivi ajenda kuu kabisa ya upinzani ni kudai Tume Huru ya Uchaguzi ili kupata demokrasia ya kweli nchini hususan katika chaguzi zote kuanzia udiwani, ubunge hadi urais.
Chaguzi zote za kweli duniani lazima zifanyike chini ya usimamizi wa Tume Huru za Uchaguzi. Sharti hili ni muhimu ili kuepuka upendeleo wa dhahiri au uliofichika kwa chama chochote kile kinachoshiriki uchaguzi husika.
Na hakika msingi wa sharti hili si utashi tu wa binadamu. Ni kutekeleza moja ya kanuni adhimu ya haki za msingi za binadamu ambayo inakataza mtu au mamlaka yoyote ile kuamua jambo ambalo mtu huyo au mamlaka hayo wana masilahi nalo.
Na mahakama zote Tanzania na duniani zinazingatia kanuni hii.
Ripoti ya Tume ya Jaji Nyalali ya mwaka 1991 ilisisitiza (katika ibara ya 591) kuwa muundo wa Tume ya Uchaguzi ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania sharti ubadilike ili kukidhi haja ya demokrasia ya vyama vingi. Ili kuhakikisha kuwa Tume ya Uchaguzi inakuwa huru, katika ibara ya 592 Ripoti hiyo ilisema kuwa, “Mwenyekiti na wajumbe wa Tume ya Uchaguzi sharti wachaguliwe na Bunge au Baraza la wawakilishi. Wakurugenzi wa uchaguzi ambao watakuwa ni Makatibu wa Tume ya Uchaguzi nao sharti wachaguliwe na Bunge au Baraza la Wawakilishi baada ya kupendekezwa na Tume Ajiri zinazohusika.”
Ni dhahiri mapendekezo hayo ya Tume ya Jaji Nyalali yalizingatia kuwa uchaguzi wa vyama vingi sharti uendeshwe kwa viwango vinavyokubalika kisheria na kiutaratibu duniani kote. Kwa mfano Tamko la Dunia kuhusu Haki za Binadamu la mwaka 1948 linasisitiza kufanyika kwa uchaguzi wa kweli ulio huru na haki. (Ibara ya 21(3).
Sharti hili lilisisitizwa baadaye na Sheria ya Kimataifa kuhusu Haki za Kisiasa na Kiraia ya 1966 (Ibara ya 25(b). Na msemo maarufu labda katika medani ya utoji haki duniani unasema, “Haitoshi kwamba haki imetendeka; sharti ionekane kuwa imetendeka.”
Katika mazingira ya Katiba na sheria za uchaguzi hapa nchini haki haiwezi kutendeka wala kuonekana imetendeka kwa sababu zifuatazo.
Kwa mujibu wa ibara ya 74(1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Tume ya Uchaguzi ina wajumbe wafuatao wanaoteuliwa na Rais; Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na wajumbe wengine wanaotajwa na sheria iliyotungwa na Bunge.
Pia, Mtendaji Mkuu wa Tume ya Uchaguzi ambaye ndiye Mkurugenzi wa Uchaguzi naye huteuliwa na Rais kufanya kazi kwa mujibu wa masharti ya Sheria ya Uchaguzi ya mwaka 1985 (pamoja na mabadiliko yake). Ndiyo kusema, kimsingi Sheria ya Uchaguzi ya mwaka 1985 ilikuwa kwa ajili ya chaguzi za chama kimoja tu.
Mbali na Mkurugenzi wa uchaguzi, wasimamizi wa uchaguzi ni wakurugenzi wa majiji, Manispaa, Miji na wakurugenzi watendaji wa wilaya na watendaji wengine wote huteuliwa na Rais na hakika wote ni waajiriwa wa Serikali ya chama tawala.
Rais anaweza kumuondoa katika madaraka mjumbe yeyote wa Tume akipenda kufanya hivyo kwa mujibu wa Ibara ya 74(5) ya Katiba. Hakika basi, Rais ndiye mteuzi mkuu, mdhibiti na mnadhimu wa wajumbe, watendaji wakuu na hata wafanyakazi wote wa Tume ya Uchaguzi.
Hoja ya kuwa na Tume Huru ya Uchaguzi pia ilijadiliwa na Kamati ya Kuratibu Maoni Kuhusu Katiba 1999 iliyoongozwa na Jaji Rufaa Mstaafu Robert Kissanga. Moja ya mapendekezo yaliyotolewa na Kamati hiyo yalidai kwamba, “Muundo wa Tume ya Uchaguzi hauzingatii uwakilishi wa vyama vya siasa na kwamba wajumbe wa Tume huteuliwa na Rais ambaye pia anaweza kuwa ni kiongozi wa chama cha siasa kinachotawala. Kwa sababu hiyo, wajumbe wa Tume katika utendaji wa kazi zao, ama watakuwa na upendeleo kwa Chama husika au watakuwa wanalipa fadhila kwake. Wanaotoa hoja hii wanapendekeza kwamba kuwe na chombo kitakachochuja majina ya wajumbe wa Tume kabla Rais hajawateua.” Wengi wanakumbuka kabisa kuwa Rais wa wakati huo Benjamin Mkapa hakupendezwa na mapendekezo ya Ripoti ya Kamati hiyo mpaka akaonyesha hisia zake hizo waziwazi dhidi ya Mwenyekiti wake Jaji Robert Kissanga.
Serikali ilipinga mapendekezo hayo kwa kudai kwamba, “... ili Tume ya Uchaguzi iweze kutekeleza majukumu yake bila woga wala upendeleo, inapaswa kuwa ya kitaalamu au yenye wajumbe wenye hadhi, wanaokubalika na ambao uteuzi wao hautazingatia mwelekeo wa siasa wa chama chochote. Muundo wa sasa wa Tume unazingatia sifa hizo na serikali inaona muundo huo uendelee.” Kisha serikali ilipigilia msumari kwa kudai, “Kwa upande wa wateuzi wa Tume ya Uchaguzi serikali inaona kwamba Rais ambaye ana dhamana kubwa kikatiba ya kuwateua hata majaji, aendelee kuwateua wajumbe wa Tume.” Waingereza husema, “ He who pays the piper chooses the tune.” Yaani, “Amlipaye mpiga nzumari huchagua mwimbo.” Na kisheria tunarejea pale pale kwamba, “Haitoshi kuwa haki imetendeka, sharti ionekane kuwa imetendeka.”
Na sasa, chombo shehena, jaliza nanga! Maana watendaji ambao ndio wasimamizi wa uchaguzi kama tulivyoona hapo juu wana hofu ya kutumbuliwa pale watakapotangaza kuwa wagombea wa upinzani wameshinda kuanzia udiwani hadi urais. CCM wanataka kushinda nafasi zote, kwa vyovyote vile! Kama alivyosema Mzee Ngombale Mwiru, mwanasiasa nguli nchini aliyehama CCM mwaka 2015 kuwa,“Wapinzani hawawezi kuingia Ikulu bila ya kuwepo Tume Huru ya Uchaguzi.”
‘Ushindi wa kishindo’ wa CCM katika uchaguzi wa madiwani uliofanyika tarehe 25 Novemba 2017 ambapo upinzani unadaiwa kupata kiti kimoja tu cha udiwani kati ya viti arubaini na tatu, kwa kurejea msemo wa Waingereza ni “too good to be true.” Ni mbinu ya kuwakatisha tamaa wapinzani kuwa hawapendwi. Ni ithibati kamili ya kauli ya Mzee Ngombale Mwiru iliyorejewa punde.
Jumanne 28 Novemba 2006, Mwakilishi Mkazi wa Mpango wa Maendeleo wa Umoja wa Mataifa (UNDP) Tanzania, Oscar Fernandez Taranco “... alizitaka nchi za Kiafrika kuzingatia kanuni za demokrasia, utawala bora na kulinda haki za binadamu wakati wa chaguzi...” Akasisitiza kuwa, “Nia ni kuwa na mfumo wa uchaguzi ambao hautashawishi malalamiko kutoka kwa wale wanaoshindwa baada ya matokeo ya uchaguzi kutangazwa.”
Kupatikana kwa Tume Huru ya Uchaguzi ndiyo ajenda kuu kwa upinzani ili kupata demokrasia ya kweli Tanzania na kuepusha vurugu na uvunjifu wa amani ambao umetokea katika nchi nyingine Afrika na duniani kwa jumla.

Messi anatakiwa kumshukuru Ronaldo kwa mafanikio yake


 Lionel Messi hajawahi kuwa rafiki wa Cristiano Ronaldo, na hilo ni jambo la kawaida. Wachezaji wawili wanaoshinda kila msimu kuwani tuzo binafasi.
Wachezaji wanaocheza katika timu zenye upinzani wa jadi katika La Liga, wakitoka katika mataifa tofauti. Pia mjadala wa nani ni bora kati yao hajawahi kufikia mwisho.
 “Hatuna mahusiano yoyote,” Messi alisema wakati akipokea tuzo ya Kiatu cha Dhahabu ya kuwa mfungaji aliyefunga mabao mengi zaidi Ulaya.
“Urafiki unajengwa kwa kutumia muda mwingi pamoja na kujua vizuri kila moja. Tumekuwa tukionana wape kwenye sherehe za kupokea tuzo tu. Kila kitu kipo safi, lakini maisha yetu hayaingilia mara kwa mara.”
Messi yuko sahihi, lakini hiyo haiwezi kumzui kufaidika na mafanikio yanayotegenezwa na Ronaldo katika masoko yaliyochangia kwa Messi kusaini mkataba mpya wa miaka mitatu utakaomalizika akiwa na miaka 34. Hiyo ni moja ya njia nyingi ambazo Ronaldo anamsaidia moja kwa moja au kwa njia nyingine kwa Messi kuingiza fedha nyingi.
Kwanza, Ronaldo uwepo wa Real Madrid umelazimisha Barcelona kuwabakiza nyota wake, ndani na nje ya uwanja kwa ajili ya masuala la masoko.
Ushindani wa miamba hiyo ya La Liga umekwenda mbali kwani umechangia hata kuongezeka kwa pato lao kwa mujibu wa orodha ya Forbes.
Kwa sasa Barcelona imeizidi Real Madrid katika misimamo yote kwa mwaka 2017, Lakini Forbes imeikadilia utaji wa Barcelona kufikia dola 3.64 bilioni na Real Madrid utajili wake ni dola 3.58 bilioni.
Kama watapoteza Messi hakuna ubishi kwamba thamani ya Barcelona itashuka kwa sababu klabu hiyo itapoteza pointi kutokana na kukosekana kwa mabao ya nyota huyo.
Kuondoka kwa nyota wa Brazil, Neymar kwenda Paris Saint-Germain mwanzoni mwa msimu huu kulichangia Messi kupewa mkataba mpya unaokadilia kufikia dola 830 milioni.
Pia, Ronaldo kuongeza mkataba kulichangia kupandisha thamani ya Messi. Mshambuliaji huyo Mreno alisaini mkataba mpya 2016 utakaodumu hadi Juni 2021, utakaomlipa Ronaldo hadi akiwa na miaka 36, mshahara wa dola 475,000 kwa wiki.
Forbes imekadilia gharama ya mishahara na bonasi za Real Madrid kwa mwaka zinafikia dola 50-60 milioni. Akijumla fedha zake za matangazo ya biashara Ronaldo anapokea dola 93 milioni kwa mwaka 2017 hali inayomfanya kuwa mwanamichezo anayelipwa zaidi kwa mwaka huu.
Messi yupo katika orodha hiyo akiwa watatu akipokea dola80 milioni, akiwa nyuma ya Ronaldo na LeBron James. Lakini kuongeza kwake mkataba hadi 2021 utamfanya kuingiza dola 59.6 milioni, kwa mujibu wa gazeti la Hispania la El Mundo, nyota huyo atapokea mshahara wa dola 667,000 kwa wiki.

Pole Carzola sasa ni bora urudi Llanera


Hivi unadhani Santiago Carzola anajisikiaje pale mtoto wake India Ursula akimuuliza baba mbona huendi kazini? Katikati mwa msimu jibu rahisi la Carzola kwa mwanae lilikuwa "mwanangu nitarudi kazini mwezi wa kumi"
Mwaka mzima umepita na Carzola bado hajarudi kazini. Swali gumu zaidi kwa mwanae ni "baba mbona kwenye picha ya pamoja ya Arsenal ya msimu hu haupo? Carzola itabidi amwambie nitarudi kazini mwakani?
Mwaka 1993 dunia ilipata pigo baada ya moja wa washambuliaji hatari kwa wakati huo Marco Van Basten alipomua na kukaa nje kwa miaka miwili kabla ya kutangaza kustaafu soka akiwa na miaka 28 tu.
Van Basten alitikisa dunia akiwa na Ajax na baadaye AC Milan akkiwa amefunga mabao 300, lakini majeruhi yalimlazimisha kuacha soka 1995.
Michael Owen aliteseka na majeruhi maisha yake yote ya soka. Alipofika mwaka 2013 aliona bora awe Dk Leakey wa England ili acheze mpira wa mdomoni kwenye vituo vya Tv baada ya mateso ya misuli kwa kipindi kirefu.
Mwaka 2007 Dr Richard Steadman alimweleza Ji Sung Park kuwa opereshen yake ya goti itamweka benchi mwaka mmoja, haikuwa taarifa nzuri.
Huyu Dk maarufu aliwahi kuwatibu akina Ronaldo, Ruud van Nistelrooy, Michael Owen na Alan Shearer na kuwaeleza wazi kuwa matatizo yao ya misuli yatahitimisha soka lao.
Carzola naye tangu Oktoba mwaka jana hayupo uwanjani. Dr wake ndugu Roman Cugat huenda ndiye mwenye majibu sahihi kwa mtoto wa Carzola ambaye anamuuliza baba kwanini huendi kazini.
Jibu la Cugat kwa mtoto wa Carzola ni moja tu. Amweke wazi kama Steadman alivyofanya kwa akina Delima. Amweleze ukweli kuwa baba hawezi kurudi uwanjani mapema hivyo atarudi Lugo de Llanera in Oviedo (nyumbani kwao).
Michael Owen aliumia mnamo Aprili 12, 2002 akiwa na Liverpool kule Leeds. Mwaka 2007 alikaa nje ya uwanja takriban siku 315. Achana na 2012 ambapo alikaa nje kwa siku 129.
Maisha haya ya Owen kushindwa kuishi kwa amani ndiyo yanamrudisha Carzola Llanera. Wakazi wa Asturias walizoea kumuona Carzola akikatiza misitu ya akina Vidic, Terry na Cahil. Wamemisi kumuona Carzola akimpa Furaha Wenger.
Dr wake Roman Cugat ameshauri Carzola aachane na soka. Huu ni uamuzi mgumu sana kwake. Tokea mwezi wa 10 mwaka jana ilisemekana Carzola atatumia siku 346 akiwa benchi.
Lakini kutokuwepo kwa Carzola kwenge picha ya pamoja ya Arsenal msimu huu basi huenda asiwepo mpaka mwakani. Ana umri wa miaka 32 kwa sasa, unategemea nini?  Ingawa Carzola Bado anaamini kuwa pilipili ni tamu kuliko sukari, ana Imani na misuli yake ila nadhani vyema arudi llanera
Kiasi cha pesa alichokitumia kwenye upasuaji nadhani ni vyema arudi Cimavilla na fukwe za Abba Kaya kule Gijon akapunge upepo na mke wake Ursula. Aliyoyafanya ni makubwa. Asijikute Fransesco Totti.
Carzola amewekeza sehemu nyingi mno. Mwaka 2014 aliwekeza kwenye kampuni ya ardhi na makazi yenye ofisi zake Liverpool na Man United ijulikanayo kama Capital Centric Investments LLP.
Ambapo yeye na Luis Suarez, Mikel Arteta na Jose Henrique waliwekeza zaidi ya Euro milioni 50 na wanategemea kupata faida ya sio chini ya Euro 250 milioni kwa mwaka. Nadhani huu ni wakati wa yeye kusimamia mambo yake mengine ya kibiashara pamoja.

Uchaguzi wa marudio watia hofu wasomi kuelekea 2020


 Wasomi na wanasiasa wameeleza hofu yao kuhusu mustakabali wa uchaguzi wa Serikali za Mitaa 2019 na Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020 endapo kasoro zilizojitokeza kwenye uchaguzi mdogo wa madiwani hazitafanyiwa kazi.
Hofu hiyo imejitokeza katika uchambuzi wa wasomi waliozungumza na Mwananchi kwa nyakati tofauti kuhusu matokeo na malalamiko yaliyojitokeza katika uchaguzi huo uliofanyika Jumapili iliyopita na CCM kushinda kwa asilimia 97.
Miongoni mwa malalamiko yaliyojitokeza ni mawakala wa baadhi ya vyama vya upinzani kukamatwa na polisi na wengine kutimuliwa huku wengine na viongozi wao wakishambuliwa na kujeruhiwa.
Hata hivyo wakati upande mmoja wa upinzani ukilia kwa hujuma na kuambulia kata moja, upande mwingine wa chama tawala unachelea kwa ‘ushindi wa kishindo’ wa kata 42 kati ya 43, unaotajwa kuwa salamu za mwaka 2020.
Vurugu zilizotokea
Katika baadhi ya maeneo kulikofanyika uchaguzi huo, hali haikuwa tulivu bali yaliripotiwa matukio ya watu kupigwa, kukatwa mapanga, magari kuvunjwa vioo, wagombea kuzuiwa kutembelea vituo, wanachama kupigana, madai yaliyosababisha Chadema kujitoa katika kata tano za mkoa wa Arusha.
Hata hivyo, licha ya kujitoa katika kata za Ngabobo, Leguruki, Makiba, Maroroni na Mbureni, matokeo yalitangazwa na CCM kuibuka kidedea.
Matukio ya mawakala kuondolewa yaliripotiwa katika kata kadhaa, zikiwamo za Saranga (Dar es Salaam), Makiba (Arumeru) na Nyabubinza (Maswa).
Alipotafutwa kuzungumzia madai hayo jana, Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Kailima Ramadhan simu iliita bila kupokewa badala yake alituma ujumbe mfupi kuuliza anapigiwa na nani.
Alipotajiwa anayeuliza na swali kuhusu malalamiko yaliyotokea kuhusu uchaguzi huo likiwamo suala la mawakala kutolewa kwenye vyumba vya kupigia kura na wengine kukamatwa, hakujibu hadi gazeti linakwenda mtamboni.
Hata hivyo, Kailima alikaririwa na gazeti moja Novemba 27 akisema uchaguzi umekwenda vizuri kwa asilimia 100.
“Vituo vyote kufikia saa 10.30 jioni hali ilikuwa nzuri na kura zilikuwa zinahesabiwa. Kumekuwapo na kasoro ndogo, kwa mfano kule Mwanza kuna vijana wa Chadema walikuwa wakiwazuia watu kwenda kupiga kura Nyakato. Dar es Salaam kila kitu kimekwenda vizuri, Lushoto kulikuwa na mawakala walitaka waruhusiwe bila kuwa na kiapo cha uwakala, lakini wakazuiwa,” alisema Kailima.
Maoni ya wachambuzi
Katika uchambuzi wake, Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dk James Jesse alisema, “hii haiashirii jambo jema, kama uchaguzi mdogo umeleta shida namna hii, itakuwaje katika uchaguzi mkubwa wa mwaka 2020, hali itakuwa mbaya zaidi,” alisema Dk Jesse.
Alisema swali la kujiuliza ni kwa nini kunakuwa na matukio kama hayo kila wakati wa uchaguzi ilihali nchi ni ya kidemokrasia.
Alisema kibaya zaidi waliokuwa wakikamatwa ni wa upinzani zaidi, huku baadhi yao wakipigwa pia, “suala hili haliashirii mwanga mwema huko twendako. Uchaguzi ni suala la kisheria na kikatiba, kwanini linagubikwa na mambo yasiyofuata misingi hiyo, hakuna maana kukubali vyama vingi huku wagombea wa upande mmoja wakikamatwa,” alisema.
Msomi huyo alisema lazima kuwepo na malalamiko ya uonevu, wajibu wa Serikali ni kuhakikisha inasimamia uwanda mpana wa usawa wa kisiasa badala ya hali ilivyo sasa,” alisema Dk Jesse.
Alisema matukio hayo yakiachwa yaendelee yanaweza kutishia amani kwa sababu yanajenga chuki miongoni mwa wananchi.
“Pamoja na ushindi uliopatikana, sisiti kusema wazi kuna maeneo hawakushinda kihalali na hapakuonyesha hali ya kidemokrasia hata kidogo,” aliongeza Dk Jesse.
Kuhusu kauli ya mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Amos Makalla kuomba msamaha kwa sababu ya mkoa wake kukosa kata moja ya Ibhigi, msomi huyo alisema hilo linahitaji majibu kutoka kwake, lakini linaibua maswali.
“Inawezekana walipewa masharti lazima washinde, inawezekana walishindwa kwa uzembe, hawakusimamisha mgombea anayekubalika, hawakufanya kampeni, hawakuiba kura, hawakufanya fitina vya kutosha. Hizi zote ni hisia na mawazo kutokana na kauli ile, hivyo bado ana nafasi ya kufafanua sababu ya kuomba msamaha, kwa sababu kwenye uchaguzi wa kidemokrasia kuna matokeo mawili kushindwa na kushinda, hivyo kama kilichotokea ni demokrasia kwanini aombe msamaha,” alihoji Dk Jesse.
Maoni ya Dk Jesse hayaachani sana na ya Profesa George Shumbusho, mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Mzumbe, aliyesema, “nachelea kusema kila kitu moja kwa moja kwa sababu sioni mwanga huko tuendako, kauli ya Makalla nayo inaleta maswali mengi je, aliambiwa lazima ashinde?
“Kama hivyo ndivyo basi itakuwa bahati mbaya sana kwa demokrasia ya nchi, hata hivyo hakupaswa kusema hadharani ili kuepusha maswali kama haya, hata kama lilikuwa ni agizo,” alisema.
Hata hivyo, Profesa Shumbusho alisema ni ngumu kutoa tathmini ya uchaguzi kama hujafanya tafiti, lakini kupitia vyombo vya habari, matukio kadhaa ambayo hayaashirii hali nzuri ya kidemokrasia yaliripotiwa.
“Ninachofahamu kwenye uchaguzi huru na wa haki na wa kidemokrasia, matokeo ni mawili kushinda na kushindwa, inashangaza kusikia wanaoshindwa wanapaswa kuomba msamaha, why (kwanini),’’ alisema Profesa na kuhoji.
Alisema kama kusingekuwa na kamatakamata ya wapinzani na mawakala wao ilikuwa rahisi kusema CCM imeshinda kwa mafanikio.
Alipoulizwa ushauri gani anatoa kwa wapinzani, alisema kama uchaguzi ungekuwa huru wananchi wangemchagua wanayemtaka, hivyo kungekuwa na nafasi ya kuwaambia wapinzani wafanye nini, lakini kwa hali ilivyokuwa hakuna cha kuwaambia.
Kuhusu namna ya kuondokana na hali hiyo, Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dk Omari Mbura alisema kuna haja ya kuziangalia dosari zilizojitokeza kwa kina.
Alisema pia wananchi na watawala wanapaswa kutambua katika uchaguzi kuna kushindwa na kushinda na wasipende kutamani kushinda wakati wote.
“Sidhani kama kuna aliyeonewa kwa sababu polisi wanafanya kazi kwa mujibu wa sheria na wanafuata sheria, si rahisi kuacha kuwakamata watu wanaofanya fujo kwa sababu ni upinzani au chama tawala. “Wanachotakiwa kuzingatia ni kufanya kazi bila kupata maelekezo ya mtu au kwa ushabiki wa vyama,” alisema Dk Mbura.

Hali mbaya ya Ukimwi kwa wenye umri wa miaka 15-24

Mkurugenzi Mkuu wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu
Mkurugenzi Mkuu wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), Dk Albina Chuwa 
Dar es Salaam. Hali ni mbaya kwa vijana kuanzia miaka 15-24 kutokana na kuwa kwenye kundi lenye asilimia kubwa ya maambukizi mapya ya virusi vyaUkimwi nchini.
Pamoja na kwamba hali ni mbaya katika kundi hilo, lakini Tanzania kwa ujumla maambukizi yameshuka kwa asilimia 0.4 na kufikia asilimia 4.7 kutoka asilimia 5.1 ya utafiti uliofanyika 2011/2012.
Matokeo hayo yanatokana na utafiti wa viashiria na matokeo ya Ukimwi Tanzania (THIS) ya mwaka 2016/2017 uliofanywa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu ambao umeonyesha kuwa jumla ya Watanzania 1.4 milioni (sawa na asilimia 2.9) wanaishi na virusi vya Ukimwi.
Utafiti huo uliofanyika katika mikoa yote ya Tanzania Bara na Visiwani na kuhusisha kaya 14,811 zinaonyesha kuwa vijana walio kwenye umri huo (15-24) wengi wao wakiwa wasichana wanapata maambukizi mapya.
Takwimu hizo zimeonyesha kuwa kiwango cha maambukizi ya VVU kwa watu wenye umri wa miaka 15-19 ni asilimia 0.7 ambapo asilimia 1.0 ni watoto wa kike na asilimia 0.4 ni watoto wa kiume.
Kwa vijana wenye umri wa miaka 20-24 kiwango hicho kimeongezeka na kuwa asilimia 2.2 wasichana wakiwa ni asilimia 3.4 na wanaume ni asilimia 0.9.
Kiwango kimezidi kuongezeka na kufikia asilimia 4 kwa watu wenye umri wa miaka 25-29 wanawake wakiwa asilimia 5.6 na wanaume ni asilimia 2.3.
Akielezea sehemu ya utafiti huo Mkurugenzi Mkuu wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), Dk Albina Chuwa alisema ukubwa wa maambukizi ni wastani wa asilimia 4.7 wanawake wakiwa asilimia 6.5 na wanaume asilimia 3.5
Alisema ripoti hiyo inaonyesha maambukizi ya VVU kwa vijana wenye umri kati ya miaka 15-24 ni asilimia 1.4, wasichana wakiwa ni asilimia 2.1 huku wavulana wakiwa asilimia 0.6.
Maambukizi ya VVU kwa watu wazima wenye miaka 15 hadi 64 yako juu kwa wanawake kwa asilimia 6.5 ikilinganishwa na asilimia 3.5 ya wanaume.
Kiwango cha maambukizi kwa watoto walio chini ya miaka 15 ni asilimia 0.4
Takwimu hizo zinaonyesha Mkoa wa Njombe unaongoza kwa kuwa na asilimia 11.4 ya maambukizi ya Ukimwi ukifuatiwa na Iringa yenye asilimia 11.3 huku Lindi ikiwa ni mkoa wenye maambukizi machache zaidi kwa asilimia 0.3.
Kwa upande wa Dar es Salaam, Dk Chuwa alisema kiwango cha maambukizi ya Ukimwi katika ripoti hiyo mpya ni asilimia 4.7.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo kasi ya maambukizi ni kubwa zaidi kwa wanaoishi mijini kwa asilimia 6 ikilinganisha na asilimia 4.2 ya watu wanaoishi vijijini.
Kufuatia hali hiyo Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan amewaasa wanajamii kubadili mienendo wa maisha yao na kutambua kuwa Ukimwi ni tishio hivyo ni muhimu kuchukua tahadhari kujiepusha na ugonjwa huo.
Akizungumza wakati wa kilele cha maadhimisho ya Siku ya Ukimwi duniani ambayo kitaifa yalifanyika katika Uwanja wa Mnazi Mmoja jana, Samia aliwataka wasichana kutokubali kurubuniwa kwa sababu ya njaa ya siku moja.
Mama Samia alisema, “naomba wasichana wabadilike Ukimwi ukikutesa hautakutesa peke yako bali Taifa zima, takwimu hizi zinaonyesha hali si nzuri kwa kundi hili ambalo ndilo nguvu kazi ya Taifa, mjitahidi muwe na mienendo inayoeleweka.”
Samia aliwageukia pia wanaume waharibifu na kuwasihi kuzingatia maadili na kuwaacha watoto wa kike wasome na kuja kulisaidia Taifa baadaye.
“Tunaona maambukizi kwa vijana hasa wa kike yanaongezeka, tunaweza kujiuliza wanapata wapi jibu ni kwamba wanapata kwa wanaume. Kuna wanaume watu wazima kabisa ambao wamezunguka huko na hatimaye wanatua kwa watoto na kuwapelekea maradhi yao, huo ni uuaji,” alisema.
Kwa vijana wenye umri kati ya miaka 15-19, maambukizi yapo chini kwa asilimia 0.7 na yako juu kwa wanawake wenye miaka 45-49 kwa asilimia 12.0.
Upande wa wanaume maambukizi hayo ni makubwa kwa wenye umri kati ya miaka 40 hadi 44 kwa asilimia 8.4 ikilinganishwa na miaka 55 hadi 59.
Takwimu hizo zilimsukuma Waziri wa Sera, Bunge, Kazi, Vijana na Walemavu, Jenista Mhagama kumuagiza Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Kudhibiti Ukimwi (Tacaids), Dk Leonard Maboko kuanzisha kampeni maalumu kwa ajili ya wanaume kuwahamasisha kupima na kuanza kutumia dawa za kufubaza makali ya Ukimwi.
Naye Naibu Waziri wa Afya, Dk Faustine Ndugulile alisema Serikali inaendelea kuchukua hatua mbalimbali kukabiliana na janga hilo ikiwa ni pamoja na kutoa dawa kwa watu wote waliopimwa na kugundulika wana VVU.
Alisema wizara kwa kushirikiana na wadau inaendelea kutoa elimu kuhusu matumizi sahihi na endelevu ya kondomu na kuzisambaza bila malipo kupitia vituo vya huduma za afya.
Alisema, “katika kuendelea kudhibiti maambukizi kwa makundi maalumu, wizara inafanya majaribio ya namna ya kutumia ARV kujikinga na VVU kwa walio katika hatari zaidi ya kuambukizwa, ingawa hii sio mbadala wa njia nyingine za kujikinga.”
“Mafanikio katika mapambano dhidi ya Ukimwi yanaakisi mafanikio ya nchi katika kutekeleza lengo namba tatu la maendeleo endelevu hivyo tutahakikisha tunaendelea kutekeleza maendeleo hayo ili ifikapo 2020 malengo ya 909090 Tatu yanafikiwa na kuchangia malengo ya kutokomeza Ukimwi duniani ifikapo 2030,” alisema Dk Ndugulile.

Mtaka asema taarifa za kukamatwa ni uzushi


Dar es Salaam. Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Athony Mtaka amekanusha taarifa zinazoenea kwenye mitandao ya kijamii kuwa amekamatwa na Takukuru.
Taarifa hizo zinaeleza kuwa Mtaka amekamatwa na Takukuru kwa kugawa fedha za UVCCM kwenye uchaguzi.
Kutokana na taarifa hizo Mtaka amesema, “Kuna taarifa zinasambazwa kwamba nimekamatwa na Takukuru nikigawa fedha za UVCCM ni uzushi na uongo wa kupuuzwa.”

MBUNGE WA ARUMERU MASHARIKI MHESHIMIWA JOSHUA NASSARI AVAMIWA

Mbunge wa Arumeru Mashariki, Joshua Nassari akiwa na Mbunge wa Arusha mjini, Godbless Lema wameenda kwenye kituo cha polisi Usa River kutoa taarifa ya tukio la uvamizi uliofanyika nyumbani Nassari usiku wa kuamkia leo Jumamosi.
Tukio hilo limetokea Kijiji cha Nkwanekori wilayani  Arumeru mkoa wa Arusha.
Katika ukurasa wake wa Twitter Nassari ameandika, “Nimevamiwa nyumbani kwangu maeneo ya USA RIVER usiku huu na watu wenye silaha, na kufyatua risasi ambazo zimeua mbwa waliokuwepo nje ya nyumba. Nimefanikiwa kukimbia na mke wangu na kuripoti kituo cha Polisi. Nimekuwa nikitishiwa kuuawa kila siku, sina amani ndani ya nchi yangu.”
Baadhi ya majirani na viongozi wa Chadema wamefika nyumbani kwake kumjulia hali na baadaye kumsindikiza kituo cha polisi Usa River.
Mmoja wa majirani ambaye hakupenda kutajwa jina lake amesema alisikia milio ya risasi zaidi ya 12 na baadaye kimya kutawala.

Katambi apata mrithi

Dar es Salaam. Kamati ya Utendaji ya Baraza la Vijana wa Chadema (Bavicha) limemchagua  Patrick Ole Sosopi kuwa Mwenyekiti wa baraza hilo kuchukua nafasi ya Patrobasi Katambi aliyehamia Chama cha Mapinduzi.
Kamati hiyo pia leo Desemba 2  imetangaza kuziba nafasi ya nafasi ya Makamu Mwenyekiti kwa kumteua John Pambalu, nafasi iliyoachwa wazi na   Sosopi. Viongozi hao wameteuliwa kuongoza baraza hilo kwa muda wa mwaka mmoja.
Akizungumza na waandishi wa habari Katibu Mkuu wa Bavicha, Julius Mwita amesema uamuzi huo ulifanyika jana kufuatia kikao cha dharura cha kamati hiyo ya utendaji.
Amesema  baraza hilo ni mojawapo ya taasisi imara na  itaendeleza mapambano."Tunawahimiza vijana wa Chadema na vijana wote wa Tanzania wasimame kidete kwenye kazi ya kuijengea na kuipigania demokrasia ya nchi yetu katika misingi ya utawala bora na haki za binadamu,"
Kwa upande wake Ole Sosopi amesema katika uongozi wake atahakikisha baraza hilo linarudi kwenye misingi imara na kuongoza mapambano ya kudai demokrasia.
Amesema akiwa mwenyekiti hatavumilia kuendelea kuona uonevu wanaofanyiwa wanachama wa Chadema.
"Bavicha inaenda kuwa taasisi bora na imara zaidi baada ya kuondoka Katambi. Tunakwenda kupambania Demokrasia a, tutawashawishi vijana kuwa wamoja kulitetea taifa bila kujali maslahi ya vyama," amesema Ole Sosopi

Kenya ina majeraha, nani ataiponya?


Novemba 28, katika Jiji la Nairobi, Kenya taswira mbili zilitawala; Upande mmoja ulikuwa umejaa machafuko, milio ya bunduki, mabomu ya machozi, damu, majonzi na maombolezo. Pia, uharibifu wa mali ulikuwa mwingi mno.
Kwa upande mwingine, shangwe na vigelegele vilitawala huku wageni waalikwa na maelfu ya wafuasi wa Jubilee wakisherehekea hafla ya kuapishwa kwa Rais Uhuru Kenyatta katika Uwanja wa Kasarani, Nairobi.
Jua lilipotua siku hiyo watu watatu walikuwa wameuawa miongoni mwao mtoto wa miaka saba katika makabiliano kati ya polisi na wafuasi wa Muungano wa Nasa wanaokataa ushindi wa Kenyatta.
Muungano wa Nasa walikuwa wanajitayarisha kumkaribisha kiongozi wao, Raila Odinga kuwaongoza kwenye mkutano wa hadhara wa kuomboleza watu zaidi ya 57 waliopoteza maisha yao mikononi mwa polisi katika visa mbalimbali vya kisiasa kati ya Agosti 8 na Novemba 26.
Agosti 8 ndiyo tarehe ulipofanyika uchaguzi ambao ulikumbwa na kasoro nyingi na baadaye kubatilishwa na Mahakama ya Juu ya Kenya, wakati Novemba 26 ndipo ulifanyika uchaguzi wa marudio wa Rais na Uhuru kuibuka mshindi baada ya Odinga kuususia.
Baadhi ya watu waliuawa wakati Uhuru akiapishwa. Miongoni mwa waliouawa kwa kupigwa risasi ni mtoto Geoffrey Mutinda.
Wafuasi wengine upinzani wanadaiwa kuuawa katika kati ya polisi na wafuasi wa Nasa waliokuwa wanamlaki Raila aliporejea kutoka ziara ya siku 10 ughaibuni.
Wengine waliuawa katika mitaa ya mabanda na kuleta msisimko mkubwa wa vuguvugu la upinzani kuzidisha wito wao wa kutaka kuanza kile wanachokiita ukombozi wa tatu wa Kenya. Wafuasi na viongozi wa Nasa wanasema hawahisi kuwa ni Wakenya kwa jinsi wanavyohangaishwa na polisi na Serikali ya Jubilee.
Wanasema kuwa Katiba inakubali Wakenya wote kukutana mahala popote bora tu wamemwarifu mkuu wa polisi katika eneo wanapokutana, lakini licha ya Nasa kufuata sheria kwa kuwaarifu polisi kuhusu mikutano yao, hakuna siku wamekubaliwa kukutana.
Wiki jana, Raila aliongoza mchango wa kusaidia familia ya waliofiwa. Kiongozi huyo alipotoa machozi alipokumbuka maisha ya waliopotea kwa sababu ya siasa. Polisi wameendelea kuwa kizingiti kikubwa kwa juhudi za kuwaleta Wakenya pamoja na kudumisha amani na utangamano.
Popote wanapotumwa lazima wamwage damu. Mbaya zaidi ni kwamba hata watoto wameathiriwa kwa kuwa polisi hawachagui mtu mzima wala mtoto wanaporusha risasi. Visa hivi ni sawa na kunajisi Katiba.
Wengi wanasema polisi waliouwa na kujeruhi sharti wachukuliwe hatua za kisheria. Hatuwezi kuendelea kuishi na hofu katika nchi yetu ilhali tulipata uhuru 1963.
Baadhi ya Wakenya wamechoshwa na virumai za kila mara na wengine wao wanashangaa kwa nini walipigania huru kumfukuza mkoloni mweupe ilhali bado kuna watu weusi ambao ni wakatili kupita kisasi. Viongozi hawajali maisha—kile wanachokienzi ni uongozi. Lakini swali ni je, kukitokea vita vya kukata na shoka, viongozi hao watawaongoza nani? Wahenga walisema, vita havina macho na asiyeziba ufa atajenga ukuta.
Serikali ikiendelea kupuuza vifo hivi na hasara ya kila siku zinazosababishwa na malumbano, siku moja, na haitakuwa mbali, nchi inaweza kukumbwa na visa ambavyo vitakuwa vigumu kuvikomesha.
Kila mtu akijipiga kifua bila kujali matokeo ya matendo yake mwishowe itakuwa kulia na kusaga meno.
Wafuasi na viongozi wa Nasa wanasema hawahisi kuwa ni Wakenya kwa jinsi wanavyohangaishwa na polisi na Serikali ya Jubilee. Wanadai kuwa Katiba inakubali Wakenya wa tabaka zote kukutana mahala popote.
Kama ilivyofanyika kwa mikutano mingine ya hapo awali ya Nasa, Raila na viongozi wakuu wa upinzani walitimuliwa walipofika uwanja wa Jacaranda, Nairobi kuongoza maombolezo. Lakini, kwanza kiongozi huyo alitangaza uamuzi wa utata kuwa ataapishwa Desemba 12. Lakini je, ataapishwaje ilhali Katiba ina utaratibu wa jinsi Rais anafaa kuapishwa?
Wiki jana, kiongozi mwenza wa Nasa, Musalia Mudavadi alipohutubia wanahabari aligusia suala hilo la kuapishwa kwa Raila lakini muda mfupi baadaye, Raila alisema hakubaliani na matamshi hayo kwa sababu ni kinyume cha sheria.
Baadaye Raila na viongozi hao waliwakwepa maafisa wa polisi waliokuwa wanawafuata na kufika katika mtaa wa Mabanda wa Kibra ambako hali iliyojitokeza ni kwamba Kenya bado inaumia na suluhu ya tiba inahitajika haraka iwezekanavyo.
Rais wa Uganda, Yoweri Museveni aliongeza mafuta kwenye moto aliposema watu hawali siasa. Museveni angenyamaza na kuwaacha Wakenya watafute suluhisho la matatizo yao. Kiongozi huyo wa Uganda hana haki ya kuwashauri Wakenya ambao hawajasahau kwamba alishindwa kuipatia Kenya mradi wa ujenzi wa bomba la mafuta kutoka Kenya hadi Uganda badala yake ukaenda Tanzania. Wanaona sasa anawapaka mafuta kwa mgongo wa chupa.
Museveni alikuwa anahutubia halaiki ya watu waliosafirishwa na Jubilee kutoka maeneo yaliyompigia kura Uhuru, kwenye uwanja Kasarani, Nairobi.
Yeye mwenyewe hula, huota na hulala akifikiria siasa. Tafadhali Museveni atuache na shida zetu kwa sababu wewe si mfano mzuri wa kuigwa na wengine.
Ulimwengu wote unajua kuwa amemhangaisha kiongozi wa upinzani Uganda, Dk Kizza Besigye kwa miaka mingi, lakini hiyo si stori yetu leo.
Siasa mbaya, maisha mabaya. Kenya huenda ikaendelea kuzama zaidi kwenye hili, lakini kusema ukweli, ushauri huu wa Museveni ni potofu kwa sababu twamjua; amekuwa akila siasa tangu 1986 alipochukua hatamu za uongozi baada ya kumtimua Milton Obote. Nitatofautiana na kiongozi huo wa Uganda kwa sababu Wakenya hawawezi kutambua ushauri wake.
Rais Uhuru aliapa kuwa atahakikisha Wakenya wote wanatimiza ndoto zao. Pia, aliahidi kuwa atafanya kila aliwezalo kuhakikisha kuwa amewaleta Wakenya wote pamoja. Watu watatu walifariki dunia kwenye visa vya polisi kukabiliana na wafuasi wa Nasa waliokuwa wamefika katika uwanja wa Jacaranda yapata kilomita 12 mashariki mwa jiji la Nairobi.
Si ajabu wafuasi wa Nasa waliona cha mtema kuni. Nasa ilikaidi amri ya polisi kwamba mkutano wao wa maombolezo uahirishwe hadi siku nyingine kwa sababu Rais Uhuru alikuwa anaapishwa.
Tayari, kitumbua kimeingia mchanga kwa sababu upinzani na serikali ya Jubilee hawapatani kwa lolote lile wanalogusia. Kila mmoja anataka kuonekana ana ujasiri kuliko mwenzake, lakini ameshika mpini Raila ameshika makali.
Bado upinzani umeapa kuwa kamwe hawatamtambua Rais Uhuru kama kiongozi wao. Wanasisitiza wataweka shinikizo hadi uchaguzi mwingine ufanywe ndani ya siku 90. Raila amesisitiza kuwa yeye haogopi lolote na ataapishwa Desemba 12.
Siku hii ni sikukuu kwa Kenya kwa sababu ni siku ambayo nchi inaadhimisha siku ya kujinyakulia madaraka kutoka kwa mikono ya wabeberu.
Raila amechagua siku hii kuashiria ukombozi wa Kenya ambao umekuwa pambio kwa Nasa tangu Agosti 8 ambapo ushindi wa Uhuru ulipingwa na majaji kuamua kwamba uchaguzi haukufanyika kwa njia inayofaa.
Hii itakuwa vigumu mno kwa sababu Rais Uhuru ameshakula kiapo cha muhula wa pili na wa mwisho. Je, Nasa itatetea vipi lengo lao la kutaka uchaguzi mwingine ufanywe? Rais Uhuru alipokuwa akiapishwa, Nasa ilikuwa inapanga jinsi ya kuvuruga utawala wake. Hii haitakuwa rahisi kwa Nasa na Wakenya zaidi watakufa kabla siku zao kufika.
Je, Wakenya wasio na hatia watauawa hadi lini? Mbona damu imwagwe usiku na mchana ilhali Katiba ya Kenya inawapa wananchi uhuru kuandamana ilimradi tu wawajulishe polisi wanapotaka kuwa na mkutano.
Wafuasi wa Nasa ndio sasa wanamwamuria Raila kutekeleza wanachotaka. Hii inadhihirika wakati Raila aliposema hataki kuapishwa na baadaye kutangazwa kuwa ataapishwa kuwa rais wa Kenya kulingana na matokeo ya kura ya Agosti 8 ambayo hata hivyo Kenyatta ndiye alitangazwa mshindi.
Wafuasi wa Raila wana kiu cha kufika nchi mpya yenye maziwa na asali. Kiongozi wao Raila amewaahidi watafika nchi hiyo inagawa kuna matatizo mengi safarini. Ni matumaini yao kwamba watafika nchi hiyo kwa vyovyote vile.
Uhuru anasema atakuwa Rais wa Wakenya wote bila kujali misingi ya kabila wala chama. Lakini, vitendo vilivyoonekana hata kabla sherehe ya kuapishwa kwake kumalizika ni tofauti kabisa.
Mazungumzo ya kubuniwa kwa nyadhifa zaidi za kisiasa, yamepingwa mara kwa mara na upinzani lakini baadhi ya makanisa yanasema lazima kuwe na hali kama hii ili nchi isonge mbele. Muungano huo wa upinzani unasema hauwezi kukubali kugawana mamlaka kwa sababu ni washindi wa kura “iliyoibwa na Jubilee.”
Rais anawasihi viongozi wa Nasa waungane na kufanya kazi lakini wito wake ni kama mhubiri kuhubiria watu waliookoka. Ni kazi bure.

Katika kuhama vyama lipo eneo la kukupa tabasamu


Julai 29, 2005, Rais wa Tatu wa Tanzania, Benjamin Mkapa alihutubia kwa mara ya mwisho Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akiwa Rais, ikiwa ni hotuba ya kuaga na kulivunja Bunge la Nane, baada ya kuliongoza taifa kwa miaka 10, tangu mwaka 1995-2005.
Katikati ya hotuba yake, Mkapa alisimulia kisa kimoja cha wazazi wa makamo na mtoto wao ambaye alishakuwa kijana mkubwa wa kiume, lakini akawa haeleweki anataka kufanya kazi ya aina gani, kwa hiyo ikabidi wamjaribu kwa mtihani ambao wao waliamini ungewapa majibu.
Mtihani gani ambao wazazi walimpa mtoto wao? Mkapa alisimulia: “Wazazi walichukua vitu vitatu, noti ya Sh10,000, Biblia na chupa ya pombe aina ya whisky, wakaviweka mlangoni ili kijana wao akifungua mlango tu avione. Baada ya hapo wazazi wakajificha waone itakuwaje.”
Wakiwa wamejificha, baba wa yule kijana alimwambia mkewe: “Kijana wetu akichukua fedha, atakuwa mfanyabiashara, akichukua Biblia bila shaka atakuwa padri na Mungu apishie mbali akichukua chupa ya whisky atakuwa mlevi.”
Kweli, haukupita muda mrefu, kijana akawa amerudi nyumbani kutoka matembezini. Akafungua mlango na kukuta vile vitu vitatu. Wazazi wakawa wanachungulia kupitia tundu la ufunguo. Wakawa na shauku kubwa kuona kijana wao atachagua nini.
Wazazi wakiendelea kuchungulia, walimshuhudia kijana wao akichukua noti ya Sh10,000. Akaiangalia vizuri halafu akaielekeza kwenye mwanga kujiridhisha kama ni halali, kisha akaitia mfukoni. Wakadhani angeishia hapo ili kukamilisha tafsiri ya kuwa mfanyabiashara.
Mshangao ukafuata baada ya kuweka noti mfukoni, hakuishia hapo, yule kijana alichukua na Biblia, akaifungua na kutazama kurasa kadhaa, halafu nayo akaitia mfukoni. Wazazi wakapigwa na butwaa kwa uchaguzi ule wa mtoto wao lakini hawakuchanganyikiwa.
Wazazi walitaka kuuona mwisho wa kijana wao, wakaendelea kuchungulia kwa umakini mkubwa. Wakamuona anashika na ile chupa ya whisky na kuifungua, akaonja ili kujiridhisha ubora wake, kisha nayo akaitia mfukoni. Akaenda chumbani kwake na vitu vyote vitatu.
Mkapa alisimulia kuwa kwa kitendo cha yule kijana kuchukua vitu vyote vitatu, wazazi wake walibaki wameduwaa. Kisha baba wa yule kijana alijipiga kofi kwenye paji la uso na kumwambia mkewe: “Sasa nimejua, mtoto wetu bila shaka atakuwa mwanasiasa.”
Tafsiri ya kisa hicho mpaka hitimisho lake ni kuwa mwanasiasa ama huwa haeleweki anataka nini, kwani anabeba kila sifa au anaweza kutosha maeneo yote, mfanyabiashara yeye, vilevile mtumishi wa Mungu lakini wakati huohuo akawa mlevi.
Hata hivyo, Rais Mkapa alionya kuwa hiyo si sifa ambayo angependa wanasiasa wakashifiwe nayo. Kwani naye ni mwanasiasa. Kwamba haitakiwi siasa zimpe sifa mbaya mwenye kushughulika nayo. Hata hivyo, visa vya wanasiasa mara nyingi huvunja mbavu na kukupa tabasamu.
Mifano yenye tabasamu
Kuelekea Uchaguzi Mkuu 2015, aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani katika Awamu ya Nne, Lawrence Masha alihama CCM na kujiunga na Chadema. Masha alihama katika wimbi la waliomfuata Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa aliyehamia Chadema.
Lowassa ambaye ni kada wa muda mrefu wa CCM, sababu ya kuhama kwake inatambulika kuwa ilikuwa kusaka nafasi ya kugombea urais, baada ya kutoswa kwenye chama chake, huku akiwa amejipanga kwa maandalizi makubwa na uwekezaji wa kiwango cha juu kupita yeyote yule.
Matarajio ya Lowassa kushinda yalikuwa makubwa hata baada ya kuhama CCM, ndiyo ikawa sababu kukawa na wimbi la wanaCCM ambao waliamua kujiunga na Chadema, mmoja wapo akiwa ni Masha ambaye alipoteza ubunge tangu 2010.
Tabasamu na Masha; hivi karibuni alirejea CCM baada ya kudumu na uanachama wa Chadema kwa miaka miwili. Sababu za kuhama alieleza kuwa hakuna mipango ya kuchukua dola. Hiyo sababu aliyotoa si tatizo, kwani kila mwanasiasa huwa na kipimo chake cha kubaki au kuhama chama.
Mfano wa tabasamu ni kwamba Aprili 4, mwaka huu, Chadema waliwasilisha bungeni kwa upendeleo majina mawili kwa ajili ya nafasi mbili za ubunge wa Afrika Mashariki. Majina hayo moja ni la Masha na lingine la Mbunge wa zamani wa Nyamagana, Ezekia Wenje.
Kutokana na nafasi za Chadema kuwa mbili na majina kuwasilishwa mawili, ilibidi zipigwe kura za Ndiyo au Hapana. CCM kikiwa ndicho chama chenye idadi kubwa ya wabunge, kiliwakataa Masha na Wenje kwa kuwapigia kura nyingi za Hapana, hivyo kukosa ubunge.
Kanuni zilikuwa wazi kwamba katika wabunge tisa wa Tanzania, lazima Chadema kiwe na viti viwili, CUF kimoja, CCM sita, na kwa sababu wagombea wawili wa Chadema walikuwa wamekataliwa, ilibidi chama hicho kipendekeze majina mengine ya kupigiwa kura.
Katika kukwepa usumbufu wa mwanzo, Chadema mara ya pili kiliwasilisha majina sita ya Masha, Wenje, Salum Mwalimu, Profesa Abdallah Safari, Josephine Lemoyan na Pamela Maasay. Uchaguzi wa pili ulifanyika Mei 10, mwaka huu, Josephine na Pamela wakachaguliwa.
Kimsingi, Masha alikataliwa na CCM kuwa mbunge wa Afrika Mashariki, wakati Chadema walijaribu kumpendelea aipate nafasi hiyo, ila ameamua kujiunga na chama ambacho kilimkataa na kumnyima fursa ya kuitumikia nchi, ameachana na chama kilichompendelea.
Hilo ndilo eneo la kukufanya uduwae kuhusu wanasiasa. Hata hivyo, unaweza kuweka maneno yangu kichwani kuwa mwanachama ambaye hana kinachomzuia kuhama, kwa maana ya cheo au masilahi mengine ambayo huyakusudia, kumzuia kuondoka huwa kazi ngumu mno.
Mfano wa pili; Masha alipohamia Chadema mwaka 2015 alikutana na misukosuko ya polisi mara mbili. Agosti 2015 alitupwa mahabusu kituo cha Oysterbay, Dar es Salaam, akidaiwa kuwatolea lugha mbaya polisi, alipokwenda kuwawekea dhamana vijana wa Chadema waliokamatwa.
Tukio la pili ni Oktoba 20, 2015 alipokamatwa Mpanda, Rukwa, akituhumiwa kufanya kampeni kwenye kambi za wakimbizi. Masha akatupwa rumande. Utetezi wa Masha ni kuwa alikuwa akionewa kwa sababu amehamia upinzani. Alilaumu kwamba Serikali inatumia vibaya nguvu zake za dola dhidi ya wapinzani.
Hata hivyo, Masha baada ya kuhama, hivi karibuni alipokuwa anahutubia mkutano wa kampeni za udiwani, Mbweni, Dar es Salaam, alimtaka Waziri wa Mambo ya Ndani, Mwigulu Nchemba kuwalinda wanachama wa CCM, kwani alipokuwa waziri pia yeye aliwalinda CCM.
Ni Masha huyohuyo aliyelalamika mwaka 2015 kuwa CCM inatumia vibaya polisi ndiyo maana wapinzani wanakamatwa kiholela. Akiwa CCM anaona sawa kutamba CCM walindwe na polisi kwani naye aliwalinda alipokuwa waziri.
Tuisogelee mifano zaidi
Mbunge wa zamani wa Kigoma Kusini (NCCR-Mageuzi), David Kafulila ambaye baada ya kushindwa ubunge 2015, alihamia Chadema Desemba mwaka jana, hivi karibuni amehamia CCM. Kabla ya kuwa NCCR-Mageuzi Kafulila alikuwa Chadema.
Aliposhindwa ubunge mwaka 2015, alifungua kesi mahakamani kudai aliibiwa kura na CCM. Tafsiri baada ya kuhamia CCM ni kuwa sasa anaungana na wale ambao alilalamika na kuwashtaki mahakamani kwa kumpora ubunge wake.
Kuelekea Uchaguzi Mkuu 2015, Kafulila alisema kuwa asingejiunga na ACT-Wazalendo kwa sababu maudhui ya chama hicho ni kugawa kura za upinzani kwa kutumiwa na CCM, maneno ambayo yalibeba tafsiri ya kumponda Kiongozi wa ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe.
Miaka miwili baada ya Kafulila kutoa maneno hayo, amekuwa mwanachama wa CCM, huku Zitto na chama chake ambacho kiliitwa tawi la CCM, kikiwa kimewasha taa ya mapambano kisiasa, kikichuana vilivyo na CCM kwenye kampeni za uchaguzi mdogo wa udiwani.
Mabadiliko hayo ya rangi ya wanasiasa yasikuchanganye, bali yakujengee tabasamu. Kwamba Kafulila alimdhihaki Mbunge wa zamani wa Kasulu Mjini (NCCR-Mageuzi), Moses Machali, aliyegombea ubunge kwa tiketi ya ACT-Wazalendo mwaka 2015, kisha kuhamia CCM mwaka jana, mwaka huu ameungana naye CCM.
Mfano wa Rais Mkapa kuhusu wazazi wa makamo na kijana wao ukupe tabasamu zaidi na kukuondolea maswali ya mvurugiko wa wanasiasa kulamba matapishi yao, bali shusha pumzi kuwa Katibu Mkuu wa zamani wa Chadema, Dk Willibrod Slaa ameteuliwa balozi na Rais John Magufuli.
Dk Slaa ataapishwa na Rais Magufuli ambaye miaka iliyopita alimbebea bango kwa kukosa uadilifu wa mali za umma kwa kuuza kiholela nyumba za Serikali.
Ni sawa tu aliyekuwa Mbunge wa Singida Kaskazini (CCM), Lazaro Nyalandu ambaye alipokuwa Waziri wa Maliasili na Utalii, alishambuliwa kweli na wabunge wa Chadema kwa ufisadi sekta ya utalii na ugawaji wa vitalu vya uwindaji lakini leo Nyalandu ni Chadema, na ni kamanda wao. Tabasamu.