Saturday, December 2

Katambi apata mrithi

Dar es Salaam. Kamati ya Utendaji ya Baraza la Vijana wa Chadema (Bavicha) limemchagua  Patrick Ole Sosopi kuwa Mwenyekiti wa baraza hilo kuchukua nafasi ya Patrobasi Katambi aliyehamia Chama cha Mapinduzi.
Kamati hiyo pia leo Desemba 2  imetangaza kuziba nafasi ya nafasi ya Makamu Mwenyekiti kwa kumteua John Pambalu, nafasi iliyoachwa wazi na   Sosopi. Viongozi hao wameteuliwa kuongoza baraza hilo kwa muda wa mwaka mmoja.
Akizungumza na waandishi wa habari Katibu Mkuu wa Bavicha, Julius Mwita amesema uamuzi huo ulifanyika jana kufuatia kikao cha dharura cha kamati hiyo ya utendaji.
Amesema  baraza hilo ni mojawapo ya taasisi imara na  itaendeleza mapambano."Tunawahimiza vijana wa Chadema na vijana wote wa Tanzania wasimame kidete kwenye kazi ya kuijengea na kuipigania demokrasia ya nchi yetu katika misingi ya utawala bora na haki za binadamu,"
Kwa upande wake Ole Sosopi amesema katika uongozi wake atahakikisha baraza hilo linarudi kwenye misingi imara na kuongoza mapambano ya kudai demokrasia.
Amesema akiwa mwenyekiti hatavumilia kuendelea kuona uonevu wanaofanyiwa wanachama wa Chadema.
"Bavicha inaenda kuwa taasisi bora na imara zaidi baada ya kuondoka Katambi. Tunakwenda kupambania Demokrasia a, tutawashawishi vijana kuwa wamoja kulitetea taifa bila kujali maslahi ya vyama," amesema Ole Sosopi

No comments:

Post a Comment