Wednesday, March 14

Kuna umuhimu kufuatilia tatizo la elimu Zanzibar

Makamu wa Pili wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi
Makamu wa Pili wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi akizungumza na wanafunzi wa Shule ya Sekondari Fujoni, Mkoa wa Kaskazini baada ya wanafunzi hao kutembelea Baraza la Wawakilishi mjini Unguja hivi karibuni wakati baraza hilo lilipokuwa likiendelea na vikao. Picha ya Maktaba 

Mara nyingi jamii inapojadili hali ya elimu Zanzibar kila mtu au kikundi huwa na lake linalotafautiana na la mwenzake.
Huyu humlaumu yule na yule humkosoa mwingine. Kwa ufupi unachosikia ni masikitiko na lawama.
Ukitafakari utaona ari ya kusomesha na kuwajibika kwa walimu wengi imeshuka na walimu nao kuwa na malalamiko mengi ya maslahi na mazingira ya kazi.
Maadili ya hii taaluma yameshuka. Wapo walimu, kama Rais Ali Mohamed Shein alivyoeleza, wamezigeuza shule vituo vya ujasiriamali vya kuuzia bagia, mbatata za urojo, chapati na maandazi.
Walimu wachache wasiojali maadili yao ya kazi hushughulika zaidi kuuza biashara walizotoka nazo majumbani kwao badala ya kukamata chaki kusomesha.
Taarifa zinaonyesha hata walimu wanaoishi karibu na shule walizopangiwa wamekuwa wakipokea mishahara wakati hawaendi kusomesha.
Mwishowe unabaki kujiuliza kama hali ndiyo hivi nini kifanyike ili masikitiko yaondoke na jamii iridhike na kiwango cha elimu.
Miongoni mwa yanayosikika ni uhaba wa walimu na miongoni mwa waliopo hawana sifa za taaluma hii, madarasa yamefurika (mengine yanao wanafunzi 70 au zaidi) na mazingira ya shule nyingi sio rafiki.
Pia, upo uhaba mkubwa wa vifaa vya kufundishia, kama vile vya maabara, nidhamu kupungua, wazazi kutofuatilia mahudhurio na maendeleo ya watoto wao na ushirikiano wao mdogo na walimu.
Vilevile hatuwezi kusahau uduni wa maslahi ya walimu na mengi wanayoahidiwa lakini hayatekelezwi.
Ni muhimu yote yaliyoelezwa, kujadiliwa hadharani na si pembeni na kutolewa maoni ya nini kifanyike.
Kwa bahati nzuri yote, ya kufurahisha na ya kusikitisha, yaliwekwa wazi hivi karibuni katika mkutano mkuu wa sita wa walimu uliofanyika Zanzibar.
Hali ya elimu si nzuri na ni haki ya kila mzalendo mkweli kuilalamikia, lakini lawama pekee hazitoshi. Kila mtu ajiulize anatoa mchango gani kusaidia kuondoka hapa tulipo.
Kazi ya kulaumu ni rahisi na nyepesi, bali ile ya kuondoa tatizo lililopo ndiyo mbinde.
Matokeo ya mtihani ya karibuni ya kitaifa sio ya kuridhisha, ijapokuwa wapo wanaokingia kifua na kusema sio mbaya sana.
Ni vizuri walimu kujitathmini na kukosoana na kurekebishana. Mwenendo wa baadhi yao kuchukua mishahara wakati hawaendi kusomesha au kutumia muda mwingi nje ya shule kwa shughuli binafsi au kujihusisha na bishara badala ya kusomesha ni wizi wa mchana.
Walimu kama hawa wanapaswa sio tu kufukuzwa kazi bali kushtakiwa kwa kupata fedha kwa kutumia hadaa.
Mtindo wa walimu kwenda shule na vikapu vya maandazi na visheti badala ya vitabu lazima ukomeshwe. Shule ni vituo vya elimu na si biashara.
Serikali nayo itimize wajibu wake na sio kila siku kutoa ahadi zisizotekelezwa juu ya madai halali ya walimu kama ya nyongeza za mihashara, posho za usafiri na likizo ambazo zimeainishwa kisheria, lakini hawazipati.
Si haki kumlaumu mwalimu kwa kutotimiza wajibu wakati Serikali inashindwa au haitaki kuwawekea mazingira yatakayopelekea kuona kazi yao inaheshimiwa na kuthaminiwa.
Kwa muda mrefu walimu wamesema wanashangazwa kuona wafanyakazi wa sekta nyingine za Serikali wanapata nyongeza za mishahara, posho na marupurupu bila ya bughudha, lakini kwao wao inakuwa nongwa.
Huu ni unyonge ambao hakuna anayeweza kuuvumilia na lazima uondolewe.
Lililonisikitisha ni kumsikia Rais wa Zanzibar akishangaa kuambiwa agizo lake la mwaka jana kwa Hazina ya Zanzibar na Wizara ya Elimu kuwalipa walimu malimbikizo yao ya malipo ya miaka mitatu halijatekelezwa.
Huu ni uzembe usiokubalika kwa sababu wahusika wameshindwa hata kutoa taarifa kwa nini hili halikutimizwa na ilikuwaje hata malimbikizo ya watumishi wengi wa Serikali au wajumbe wa Baraza la Wawakilishi hayawekwi kiporo kama tunavyoona kwa walimu.
Serkali inapaswa kuhakikisha inaweka mfumo mzuri wa ukaguzi wa shule zetu.
Nilishangaa siku moja kumsikia mwalimu mmoja anasema wanajitayarisha kuwapokea wakaguzi wa shule yao.
Ukaguzi sahihi huwa wa kushtukiza ili ionekane hali halisi ya shule. Pakiwepo taarifa ya awali lini ukaguzi utafanyika ni sawa na kumwambia mwizi weka nyumba yako sawa tunakuja kesho kukupekua.
Tatizo la madawati na msongamano katika madarasa ni la zaidi ya miaka 30 sasa na kila siku tunasikia juhudi zinafanyika kulimaliza.
Hii ni dosari na haihitaji tena ahadi, kinachotakiwa ni vitendo vya marekebisho.
Tusisahau kuwa aliyezoea kuandika akiwa amekaa kwenye sakafu hupata shida kufanya mtihani akikaa juu ya kiti na meza.
Hali hii inachangia watoto kupata maradhi ya mgongo kuokana na kujipinda wanapoandika wakiwa wamekaa chini.
Vilevile msongamano wa wanafunzi unampa taabu mwalimu kusomesha. Katika mfumo unaokubalika, darasa halitarajiwi kuwa na kuzidi wanafunzi 40. Fikiri hali inakuwaje kama darasa lina wanafunzi 100?
Hatua ya Serikali ya kutangaza elimu bure ni nzuri na inasaidia wanyonge, lakini gharama zake ni kubwa.
Hii inajidhihirisha wazi katika matokeo ya mtihani ambapo watoto wa shule binafsi zinazotoza ada hufanya vizuri zaidi kuliko wenzao wa shule za serikali.
Labda baada ya kuliona hili ndiyo mawaziri, viongozi wengi wa Serikali na makampuni na wafanya biashara wanawapeleka watoto wao kusoma shule binafsi nchini na nje.
Wanaobaki katika shule za Serikali ni watoto wa pangu pakavu na kauka nikuvae. Nitafurahi kupewa orodha ya viongozi wa serikali na zaidi wa Wizara ya Elimu ambao watoto wao wanasoma katika shule za serikali. Tuache kudanganyana.
Rais Shein alitoa takwimu kuonyesha bajeti ya Wizara ya Elimu Zanzibar imekuwa ikiongezeka kila mwaka. Hivi ndivyo inavyohitajika kufanyika kama kweli tunataka maendeleo.
Lakini suala ni kiwango gani cha fedha za bajeti zinazoidhinishwa na Baraza la Wawakilishi hutolewa kwa Wizara ya Elimu?

Wapandishwa kizimbani kwa kusafirisha magunia 400 ya mkaa


Dar es Salaam. Nahodha wa meli ya MV Kops, Buruhani Haji (25) na wenzake watano wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kujibu mashtaka mawili  likiwamo la kusafirisha magunia 400 ya mkaa ndani ya boti.
Washtakiwa wengine ni Juma Mcha (24), Ally Salum(22), Salum Zuberi (25), Mahazi Kombo (22) na Omari Ahmad(23), wote ni mabaharia na wakazi wa Zanzibar.
Wakili wa Serikali, Mosii  Kaima amedai leo Machi 14, 2018 mbele hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama hiyo, Thomas Simba  kuwa washtakiwa kwa pamoja wanadaiwa kutenda kosa hilo Machi 2, 2018 kati ya ufukwe wa Bahari ya Hindi jijini Dar es Salaam  na Unguja.
Kaima amedai katika shtaka la kwanza, washtakiwa wanadaiwa kusafirisha magunia 400 ya mkaa yenye thamani ya Sh30 mil, mali ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Washtakiwa wanadaiwa kusafirisha mkaa huyo kwa kutumia boti ya MV Kops yenye usajili wa namba  Z.931, bila kuwa na kibali cha usafirishaji kinachotolewa na mamlaka husika, huku wakijua kuwa kufanya hivyo ni kinyume cha sheria.
Wakili Kaima alidai kuwa katika shtaka la pili, washtakiwa walikutwa na mazao ya misitu katika boti hiyo, bila kuwa na leseni  inayotolewa na Mkurugenzi wa mamlaka ya misitu nchini.
Washtakiwa hawakutakiwa kusema chochote mahakamani hapo kutokana kesi inayowakabili kuwa ya uhujumu uchumi.
Hakimu Simba aliahirisha kesi hiyo, hadi Machi 19, itakapotajwa na washtakiwa wamerudishwa rumande.

Viongozi wawili mtandao wa wanafunzi wahojiwa


Dar es Salaam. Mpaka kufikia leo Machi 14, 2018 saa 7:45 mchana viongozi wawili wa Mtandao wa Wanafunzi Tanzania (TSNP) walikuwa wamekwisha hojiwa na Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI).
Akizungumza na MCL Digital, ofisa habari wa mtandao huo Helleh Sisya ambaye naye pia miongoni mwa watakaohojiwa, amesema hadi muda huo waliohojiwa ni mkaguzi wa haki za binadamu , Alphonce Lusako na katibu wa mtandao huo, Malekela Brigthon.
Viongozi wengine ambao hawajahojiwa hadi muda huu ni Sisya na mkurugenzi wa Idara ya sheria, Paul Kisabo.

Karume: Kuheshimu haki zawengine chanzo cha amani

Rais mstaafu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar,
Rais mstaafu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Amani Abeid Karume 

“Kuheshimu haki za wengine ni amani.” Ndivyo anavyosema Rais mstaafu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Amani Abeid Karume wakati akihutubia mkutano amani katika mji wa Belfast nchini Ireland hivi karibuni.
Karume ni rais wa sita wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, ni mtoto wa rais wa kwanza visiwani humo, Abeid Amani Karume.
Karume ambaye ana historia ya kumaliza mgogoro wa kisiasa Zanzibar na kufanya mabadiliko ya kikatiba na kuanzisha Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK), alizungumzia umuhimu wa amani kwa kumnukuu Rais wa zamani wa Mexico, Benito Juarez aliyewahi kusema palipo na heshima pana amani. Na kuwa kuheshimu haki za wengine maana yake ni amani.
Suluhu ya kisiasa ya Zanzibar kati ya vyama vya CUF na CCM wakati wa utawala wake pengine ndiyo iliyowafanya waandaaji wa mkutano wa amani kutoka Taasisi ya Amani Duniani (GBF), kumwalika Karume kuhutubia mkutano huo unaofanyika Belfast.
Karume anabebwa na mwafaka wa tatu baada ya kufanya mazungumzo na aliyekuwa mgombea urais kwa tiketi ya CUF na Katibu Mkuu wa chama hicho, Maalim Seif Shariff Hamad na kuunda SUK. Hapo ni baada ya mwafaka wa kwanza wa 1996 uliosimamiwa na aliyekuwa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola, Chifu Emeka Anyaoku na mwafaka wa pili uliokuwa kati ya Katibu Mkuu wa CCM kwa wakati huo, Philip Mangula na Maalim Seif.
Mbali na kunukuu kauli ya Benito, kwamba penye heshima ndipo ilipo amani, Karume pia amewaambia washiriki wa mkutano huo wa Belfast kwamba kiongozi mwenye maadili lazima awe mpole, anayeweza kujieleza vizuri, anayeongozwa kwa haki na usawa, kuwajibika kwa kasi inayotakiwa, kukiri makosa na kuheshimu haki za kila raia.
Hotuba ya Karume kwa washiriki wa mkutano huo ililenga umuhimu wa uadilifu na ubunifu wa viongozi kwa amani barani Afrika ambapo GPF tangu kuanzishwa kwake imejikita katika kuinua ubunifu na msingi bora kuendeleza ujenzi wa amani duniani.
Karume aliwaeleza washiriki wa mkutano huo kwamba hivi karibuni alikuwa Kampala nchini Uganda ambako alikutana na Rais Yoweri Museveni na mazungumzo yao yalijielekeza kwenye hoja mbili za kujenga amani na maisha bora kwa wananchi.
Akizungumzia hoja ya msingi ya uongozi wenye misingi ya uadilifu na ubunifu, Karume anasema hoja zote mbili ni muhimu katika kuendeleza amani na kuboresha maisha ya watu.
“Kwa ushahidi, si mimi tu ninayethamini uongozi wa uadilifu na ubunifu ikiwamo umuhimu wa kuijenga amani, mahudhurio yenu kwenye mkutano huu yanaonyesha namna mnavyothamini ujenzi wa amani. Tumekutana wote hapa kubadilishana mawazo ambayo ni muhimu sana yanayohusu maadili ya uongozi katika kujenga amani endelevu miongoni mwetu, hasa katika uongozi wenye uadilifu na ubunifu,” anasema Karume.
Karume aliweka historia ambapo uhasama wa CCM na CUF uliwekwa
pembeni Novemba 3, 2010 alipoapishwa rasmi kushika uongozi wa nchi kwa awamu ya kwanza Dk Ali Mohamed Shein. Sare za CCM, CUF na vyama vingine zilivaliwa bila kujali itikadi. Mfuasi wa CCM alivaa sare ya CUF na wa CUF alivaa ya CCM au NCCR-Mageuzi.
Historia hiyo ya uvumilivu wa kisiasa ilijitokeza pia kwenye hotuba ya Karume kwa kusema kiongozi mwenye maadili anatawala maeneo yote katika jamii kama ilivyokuwa kwa kiongozi wa kisiasa na wa kijeshi wa Roma ya kale, Julius Caesar.
Caesar au Gaius Julius Caesar anakumbukwa hasa kwa mafanikio mbalimbali yanayoonekana kuathiri dunia hadi leo. Baadhi ya mafanikio hayo ikiwamo kuheshimika na jina lake kuwa neno kwa ajili ya cheo cha watawala wa Kiroma waliomfuata. Kutokana na badiliko hilo la jina “Caesar” kuwa cheo, lugha mbalimbali zilipokea cheo hicho kama vile Kijerumani (“Kaiser”), Kirusi (“Tsar”) na Kiswahili (“Kaisari” - kutokana na neno la Kijerumani).
Pia, aliunda kalenda ambayo imekuwa msingi wa kalenda ya kimataifa leo (Kalenda ya Juliasi). Kwa heshima yake, mwezi wa saba unaitwa Julai.
Karume anasema historia ya Caesar ambayo inaendelea kugonga vichwa vya habari, kutawala mijadala ya wasomi na maeneo mbalimbali ina muhimu wake hata katika dunia ya sasa ambayo imeendelea kuwa na siasa zinazoyumba, misuguano ya kimaadili, migogoro ya uongozi wa kisiasa, rushwa na uroho wa madaraka.
Anasema kama inavyofahamika siasa ni moja ya shughuli muhimu za kibinadamu inayoongozwa na kanuni, sheria na usawa katika kuvumiliana. Karume anaendelea kusema siasa inahitaji uwajibikaji wa hali ya juu kutoka kwa wananchi, vyama vya siasa, wabunge, watendaji wa Serikali, mahakama, vyombo vya habari, jumuiya za wafanyabiashara, taasisi zisizokuwa za kiserikali, taasisi za dini na taasisi za elimu.
Karume ambaye wakati akigombea urais wa Zanzibar kwa mara ya kwanza alitambulishwa kama ‘mtoto wa simba’ kwa maana baba yake alikuwa na msimamo mkali katika uongozi wake na yeye (Karume) alitabiriwa kuwa vivyo hivyo, anasema uaminifu ni heshima katika siasa na vyombo vya umma ni muhimu kwa amani, maendeleo kwa jamii, hasa katika kuinua demokrasia.
Anasema kupitia uaminifu, viongozi wanatakiwa wawe imara katika utekelezaji wa majukumu yao ya kimaadili katika kukabiliana na changamoto za kisiasa na jamii iliyogawanyika kwa kuweka taratibu za kuaminia na zenye maadili, ikijumuisha uaminifu, ukweli na haki.
Karume anasema viongozi wa kisiasa wanatakiwa kuwa mfano kwa wanaowaongoza, wananchi wao waone uaminifu wao, ukweli na ujasiri huku akisema Afrika ina bahati ya kuwa na viongozi wengi ambao wameonyesha viwango vikubwa vya uongozi wa uadilifu na ubunifu kama vile Samora Machel (marehemu) wa Msumbiji, Kenneth Kaunda wa Zambia, Nelson Mandela (marehemu) wa Afrika Kusini na hakumsahau baba yake Abeid Amani Karume (marehemu) kwamba katika uongozi wake alibadili Zanzibar kiuchumi na kijamii.
Mwasisi huyo wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, baada ya Mapinduzi ya Zanzibar ya Januari 12, 1964 kwa kuondoa utawala wa kisultani wa Waarabu, Abeid Amani Karume alishika uongozi wa visiwa hivyo vya Unguja na Pemba na kuamuru mwingiliano wa kijamii kwa kuruhusu ndoa kati ya Waafrika na raia wa kigeni. Pia, ujenzi wa majumba ya Michenzani na mambo mengine ya kiuchumi kama ujenzi wa Hoteli ya Kitalii ya Bwawani na uanzishwaji wa kituo cha kwanza Televisheni ya rangi kwa Afrika.
Anasema Afrika ni bara lililo kwenye mabadiliko lina utajiri wa asili na rasilimali watu, lakini bado linaendelea kuogelea kwenye dimbwi la umaskini, njaa, kipato kisichowiana na usalama mdogo kama vile vita vya wenyewe kwa wenyewe, ugaidi na vurugu zinatokana na migogoro kadhaa.
Karume anasema kwa sasa uongozi wenye maadili ndiyo unaohitajika zaidi kuliko huko nyuma, hasa changamoto za kisiasa, kiuchumi na maendeleo ya kijamii. Mbali na kuzungumzia mkutano wa ‘kuendeleza amani, usalama na maendeleo endelevu kwa Afrika Mashariki’ uliofanyika Zanzibar 2015 ambao ulisisitiza umuhimu wa uaminifu na heshima kwa kila mmoja, pia alizungumzia uzoefu wake kuhusu Zanzibar ilivyogawanyika kutokana na migogoro ya kisiasa na kwamba ni namna gani uongozi wa uaminifu na ubunifu ulivyoleta amani Zanzibar.
Anasema uzoefu wake alipokuwa Rais wa Zanzibar mgawanyiko wa kisiasa uliwanya wabuni utamaduni wa maelewano kupitia ushirikishwaji wa pamoja kwa njia ya kidemokrasia, ilikuwa ni suluhisho pekee la kisiasa katika visiwani hivyo.
Karume anasema kama kiongozi, alitumia haki na uwakilishi wa wananchi wote kupitia vyombo vyao vya uwakilishi ikiwamo chama chake cha siasa, ilikuwa ni wakati wa kuwa mbunifu, mwenye msimamo, kufikiria malengo ya muda mrefu na kuweka pembeni hisia zake za kisiasa.
“Nina hakika hiyo ilikuwa ni uamuzi sahihi wa kisiasa kwa maslahi ya wananchi.” Anasema Karume huku akimnukuu mshindi wa tuzo ya amani duniani, Askofu Desmond Tutu wa Afrika Kusini alisema; “Tunataka watu ambao wapo kwa masilahi ya watu na si kwa masilahi binafsi.”

Yanayotajwa Ni maandamano ya kimwili ama ni ya kiroho

Mkuu wa Mwanza, John Mongella (katikati),
Mkuu wa Mwanza, John Mongella (katikati), akiongoza maandamano ya kupinga uwindaji haramu wa tembo na faru yaliyofanyika jijini Mwanza hivi karibuni, maandamano hayo hayakuwa ya kisiasa. Picha ya Maktaba 

Wahaya wana msemo wao usemao “Kyakutinisa kitakulye”, ni sawa na kitendawili. Jibu lake ni “mwilima”. Tasfiri yake inaondoa utamu wake. Kwa kujaribu; “Kinatisha lakini hakina madhara” na jibu lake ni “ giza”. Enzi zile kule vijijini hatukuwa na umeme, hivyo giza lilikuwa tishio kweli, lakini halikuwa na madhara.
Tumesikia kuna maandamano yanakuja mwezi wa nne. Mitandao ya kijamii inaandika kila siku juu ya maandamano haya na vyombo vya habari vimeanza kudakia baada ya viongozi kuyazungumzia.
Je, maandamano haya ni sawa na “Kyakutinisa Kitakulye”? Na tunaweza kujibu bila kusita kwamba ni “giza lisilo na madhara”? Tumesikia jeshi la polisi likisema kwamba atakayefanya maandamano atakipata cha moto. Na Rais John Magufuli akiwa Chato amesema kwa ukali kwamba atakayefanya maandamano atasimulia! Rais wa nchi ambaye ndiye amiri jeshi mkuu na mlinzi wa amani akitamka hivyo ni hatari sana.
Hata Waziri wa Mambo ya Ndani, Mwigulu Nchemba ameweka msisitizo kuwa hata wakiandamana nyumbani kwao kuzunguka kitanda watachukuliwa hatua.
Bahati mbaya kabisa, hatujasikia anayeuliza chanzo cha maandamano haya. Hakuna anayejadili namna ya kutafuta majibu ya maswali magumu yanayozunguka maandamano haya.
Hatujasikia mwenye kupendekeza njia za kuzigusa roho za wale wanaotaka kuandamana. Tunasikia mipango ya kuishughulikia miili ya watakaoandamana. Hatuwezi kujadiliana, hatuwezi kuzungumza, hatuwezi kubungua bongo na kuzama kwenye tafakuri, bali kupigana? Tunafikiri tutapata jawabu chanya kwa kupigana na pengine kupoteza maisha?
Hili ni swali langu kwa pande zote, wale wanaoandaa maandamano na wale wanaojiandaa kuyazuia. Haya ni maandamano ya kimwili au ni ya kiroho? Yawezekana pia wale wanaoandaa hawajatafakari juu ya hili. Ni muhimu kabisa kujua ni kitu gani kinalengwa hapa.
Maana kama ni maandamano ya kiroho, hakuna haja kubwa ya kuingia barabarani. Mtu anaweza kuyafanya akiwa nyumbani kwake. Maandamano ya kiroho ni hatari zaidi ya yale ya kimwili. Ni rahisi kupambana na maandamano ya kimwili kuliko ya kiroho. Ingawa kupambana na maandamano ya kimwili kunasababisha kupoteza maisha, maumivu na wakati mwingine ulemavu, ni mapambano ambayo mara nyingi yanaiacha roho salama.
Ninajua kabisa kwamba Rais Magufuli ana washauri wake, hivyo sina haja ya kusema ninamshauri; inawezekana wanamshauri na si lazima yeye kufuata kila unachoshauriwa, iwe ni ushauri mzuri, mbaya kwa nia mbaya au kwa bahati mbaya. Lakini hali inapoelekea kubaya hatuwezi kukaa pembeni na kuangalia yanayotokea kana kwamba tunaishi nchi ya jirani; sote tuna wajibu, vinginevyo historia itatuhukumu wakati ukifika na tuna la kusema mbele za Mungu; kwa vile mimi ni Mtanzania na nina uchungu na taifa langu, nashindwa kujizuia kutoa ushauri wa bure kwa Serikali inayoongozwa na CCM: Kabla ya kupambana kwa silaha na kuumizana, jiulize kwanza, maandamano haya ni “Kyakutinisa kitakulye” au ni ya kweli? Je, chanzo chake nini? Je, kuna la kujadili? Na swali kubwa kabisa ni: Haya yatakuwa ya kimwili au ya kiroho?
Kama ni maandamano ya kimwili inawezekana kuyazuia kwa njia zozote zile ikiwemo kutumia silaha za moto. Lakini kama ni ya kiroho kuna kazi, ni muhimu kutafuta njia nyingine ya kuzituliza roho.
Historia inatuonyesha kwamba kupambana na mwili hakujaleta mafanikio popote duniani. Tuna mfano wa Soweto na mifano mingine mingi ambapo maandamano yalizimwa kwa nguvu za silaha za moto, lakini hakukuwa na mafanikio. Mwili ni mapambo tu kwenye uhai wa mwanadamu. Mwili unakufa na kuzikwa; Kwa nini kupoteza muda na nguvu kushughulikia kitu kinachopita na kukiacha kile cha kudumu kama vile roho?
Mtu anayefikiri vizuri hawezi kumpiga binadamu mwenzake kwa nia yoyote ile; ukimpiga unaumiza mwili wake na roho yake inabaki salama, ukimpiga risasi akafa, unakufa mwili, roho yake inabaki salama. Hadi leo hii tuna roho za watu waliokufa, wako kaburini lakini roho zao ziko salama na zinaishi miongoni mwetu.
Roho ya Baba wa Taifa bado tunaishi nayo; roho ya Mkwawa bado tunaishi nayo, roho za mashujaa wote waliokufa wakitetea heshima na maisha ya Watanzania bado tunaishi nazo; wao walikufa ili sisi tuweze kuishi kwa uhuru na salama.
Sitaki kuamini kwamba Watanzania tumesahau historia. Hakuna popote duniani ambao risasi iliweza kupambana na wananchi. Watawala wote walioshughulika kuitesa miili ya wapinzani wao na wakati mwingine kuwaua, mwisho wao ulikuwa mbaya. Sitopenda kuingilia hili kwa undani, maana linaeleweka vizuri labda mtu kujifanya anaanzisha historia yake.
Hoja yake
Hoja yangu katika makala hii, ni kutaka tujiulize juu ya maandamano haya, ni ya kimwili au ni kiroho? Hili ni muhimu sana. Kama maandamano haya ni ya kiroho, kuna kazi ya ziada ya kufanya. Tanzania ni yetu sote – ni muhimu kabisa kutafuta chanzo na mzizi wa maandamano haya. Kuyazima kwa nguvu ni kufunika kitu kitakachochipuka kesho.
Viongozi wote waliofanikiwa kuongoza vizuri na kukumbukwa milele yote, ni wale waliofanikiwa kuzikamata na kuzifunga roho za wananchi wao, wale waliofanikiwa kutafuta majibu ya matatizo yanayogusa roho za watu wao. Mfano mzuri ni wa Mahatma Gandhi. Huyu hakuwa na Serikali, hakuwa na jeshi, hakuwa na polisi; lakini kwa vile alifanikiwa kuzishika na kuzifunga roho za Wahindi, alifanikiwa kutafuta majibu ya maswali yaliyokuwa yakigusa roho za Wahindi, walimsikiliza na kumfuata na kuungana kupambana na mkoloni bila kumwaga damu.
Hawakushika silaha kupambana, walifanya maandamano, waliendesha migomo na kususia bidhaa za Wazungu kama vile nguo na chumvi. Wafuasi wa Mahatma Gandhi, walipigwa na kuumizwa na polisi wa wakoloni, lakini walisonga mbele. Walifungwa na kuwekwa gerezani, lakini walisonga mbele. Yeye Mahatma Gandhi, alikuwa akifungwa usiku na mchana, lakini alisonga mbele kutetea haki na kuleta uhuru wa watu wa India.
Daima aliwaambia wafuasi wake, kwamba polisi wa wakoloni watapiga miili yao, lakini hawatazigusa roho zao. Filamu inayoonyesha maisha ya Mahatma Gandhi, inaonyesha vizuri kitu ninachojitahidi kuelezea kwenye makala hii. Nina imani viongozi walishaiona filamu hii. Kama ndio wanaisikia, basi waitafute waiangalie na kuona kama kuna la kujifunza.
Mfano mwingine ni wa Yesu wa Nazareti. Huyu hakuwa na mali, hakuwa na nyumba, hakuwa na Serikali, hakuwa na majeshi; lakini kwa vile alifanikiwa kuishika mioyo ya wafuasi wake na kuifunga, alitoa majibu ya maswali yaliyozigusa roho zao, walimfuata kila alipokuwa akienda na kuwa tayari kupoteza maisha yao kwa kufanya kazi yake.
Ukiondoa ujambazi ulioingizwa kanisani na Mfalme Constantine, watu waliingia kwenye imani ya Ukristo kwa mvuto; si risasi wala upanga, bali kwa kuvutwa; kwa mtindo wa kuzishika roho na kuzifunga, ni mfumo wa kutoa majibu ya maswali yanayogusa roho za watu. Bahati mbaya viongozi wa kanisa waliofuata baadaye hadi leo hii, wengi walishindwa kutengeneza mfumo mzuri wa kulifanya kanisa liwavutie waumini. Dini ya Ukristo ilienezwa kwa upanga na kumwaga damu kinyume kabisa na mafundisho ya Yesu.
Ingawa mfano wa magaidi si mzuri kuutumia katika makala hii, lakini kwa vile ni kitu kinachotokea kila wakati na sasa hivi nchi zote zimekuwa na mifumo ya kujikinga na magaidi, si vibaya kuutaja hapa. Nina imani wale wanaowaandaa magaidi si kwamba wanawafunga na kuwatesa ili kuwashawishi kukubali kujilipua, kinachofanyika ni kushika roho zao na kuzifunga.
Ni mfumo wa kuishughulikia roho zaidi ya mwili. Siungi mkono ugaidi, lakini huu ni mfano wa kuonyesha mafanikio ya kushughulikia roho badala ya mwili. Hata hivyo, dunia nzima imekataa kukaa chini na magaidi hawa kuongea na hao na kusikiliza matatizo yao. Kufikia hatua ya kujilipua, si kitu cha kudharau, wakisikilizwa mtu atashangaa kugundua kwamba hata hawa watu wazuri wanaopigana kwa njia hiyo kutetea uhai wao na uhai wa vizazi vijavyo.
Hata hivyo, ni muhimu nikaliweka jambo hili sawa hapa, ili nisieleweke vibaya. Ni haki kabisa kila mtu kutetea uhai wake, uhai wa ndugu zake na vizazi vyake, lakini ni dhambi ya mauti isiyokubalika, kutetea uhai kwa kuondoa uhai wa mwingine. Kutetea uhai, ni kuulinda uhai wa kila mtu na viumbe vyote.
Hivyo, kwa kiongozi anayetaka kuiongoza Tanzania, afahamu kwamba kuwapiga watu, kuwakamata na kuwafunga au kuwaua si msaada wa kumsaidia kuwaongoza vizuri. Njia hii imetumiwa na wengi na wameshindwa.
Makaburu wa Afrika Kusini walimkamata Mandela na kumfunga na kumtesa miaka 27, lakini kwa vile hawakufanikiwa kuigusa roho yake, wafuasi wake waliendeleza mapambano hadi alipofunguliwa. Makaburu walifikiri kumfunga Mandela ni kumaliza tatizo, kumbe ilikuwa imepandwa roho na inakua kwa kasi ya kutisha. Ingawa vyote vinategemeana, mwili na roho, lakini ukweli unabaki pale pale kwamba roho ina nguvu lakini mwili ni dhaifu. Basi sisi kama taifa tujishughulishe kutafuta dawa ya kutufanya tuwe na roho yenye nguvu.

ZFDA yateketeza nyama kutoka Afrika Kusini

Mkuu wa Jiko la kuteketezea bidhaa mbovu,
Mkuu wa Jiko la kuteketezea bidhaa mbovu, Khamis Khamis Mkanga akiingiza nyama katika jiko hilo lililopo Kivunge Mkoa wa Kaskazini Unguja kwa ajili ya kuteketezwa baada ya kuingizwa nchini kinyume na sheria zikitokea nchini Afrika ya Kusini. Picha na Abdallah Omar    
Zanzibar. Mamlaka ya Chakula na Dawa Zanzibar (ZFDA), imeteketeza  kilo 48 za nyama kutoka Afrika Kusini baada ya Serikali kusitisha uingizaji nyama kutoka nchini humo kutokana na mlipuko wa bakteria wa listeria.
Ilibainika kuwa nyama hizo ziliingizwa nchini kinyume cha sheria.
Nyama hizo ni mali ya kampuni ya Qamar ya Vingunguti jijini Dar es Salaam, ilikamatwa Uwanja wa wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Karume mwishoni mwa wiki iliyopita.
Akizungumza leo Machi 14 wakati wa zoezi hilo, mkuu wa kitengo cha uchambuzi wa hatari zinazotokana na chakula wa ZFDA, Aisha Suleiman amesema kilichosababisha kuteketezwa kwa nyama hiyo ni katazo lililotolewa na ZFDA baada ya kutokea mlipuko wa ugonjwa wa listeriosis.
Amesema ZFDA ndiyo yenye majukumu ya kuhakikisha wananchi wanapata chakula salama.
Aisha amesema uamuzi ya katazo hilo umetokana na uwapo wa maradhi ya Listeriosis nchini Afrika Kusini, hivyo ofisi yao imepiga marufuku uingizwaji nyama, maziwa na samaki kutoka nchi hiyo.
 Bakteria wa listeria, wanaosababisha maradhi ya listeriosis, wamesababisha vifo vya watu zaidi ya 180 Afrika Kusini.
Amesema katazo hilo si kwa Zanzibar pekee bali na Tanzania bara na nchi nyingine kutokana na utaratibu wa biashara kimataifa.
“Hili katazo siyo sisi tu, ni utaratibu wa kimataifa kwamba kutokana na maradhi ya listeriosis bidhaa za nyama, samaki, maziwa ni marufuku kuingizwa nchini sasa hii kampuni ya Qamar LTD ya Dar es Salaam wao waliamua kuingiza nyama hiyo, tumeikamata na kuiangamiza.” amesema Aisha.

Kampuni yashusha bei ya mbolea ya kupandia


Dar es Salaam.Katika kuunga mkono jitihada za Serikali kuhakikisha wakulima wanapata mbolea kwa wakati na gharama nafuu, kampuni ya uzalishaji na usambazaji wa mbolea ya Yara imeshusha bei ya mbolea ya kupandia.
Mbolea hiyo ya chumvi chumvi inayofahamika kama Yara Mila Otesha imepungua bei kwa asilimia 50.
Ofisa masoko wa kampuni hiyo, Linda Byaba amesema leo Machi 14, 2018 kuwa uamuzi wa kupunguza bei umekuja ili kuwasaidia wakulima waweze kupata mbolea kwa gharama nafuu.
Amesema mbolea hiyo ina virutubisho muhimu vinavyosaidia mazao kuzalishwa kwa wingi.
Amesema virutubisho vilivyo ndani ya mbolea hiyo ni lishe linganifu kwa mmea na husaidia katika kuchochea uotaji wa mizizi.
“Mbolea hii inasaidia sana kuufanya mmea kuwa imara,” amesema.

Wafuasi Chadema waliokamatwa msibani kupandishwa kizimbani


Mwanza. Wafuasi zaidi ya 10  wa Chadema waliokamatwa wakiwa nyumbani kwa mwanachama mwenzao kuhani msiba wanatarajiwa kupandishwa kizimbani muda mfupi ujao.
Watu hao, leo Machi 14, 2018 tayari wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Mwanza na kuwekwa katika mahabusu mahakamani hapo kusubiri kukamilika kwa taratibu za kimahakama ili wasomewe mashtaka dhidi yao.
Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Ahmed Msangi watu hao walikamatwa eneo la Mabatini Machi 13, 20018  baada ya kutokea kutoelewana kati yao na askari polisi.
Amesema askari hao walikuwa wakifuatilia nyendo za wafuasi hao  tangu walipokuwa wakikusanyika kutoka sehemu mbalimbali za Jiji la Mwanza kwenda nyumbani kwa wanachama mwenzao kwa kile kinachodaiwa ni kuhani msiba.
Katika tukio hilo, polisi walilazimika kutumia mabomu ya kutoa machozi kutawanya kundi la watu zaidi ya 500 waliokuwa kwenye eneo hilo.

Maadili ya uchaguzi na migogoro katika uchaguzi


“Migogoro ya uchaguzi ni asili ya chaguzi. Changamoto katika uchaguzi, mwenendo au matokeo yake, haipaswi kuonekana kama udhaifu wa mfumo wa uchaguzi, bali ni uthibitisho wa nguvu na uwazi wa mfumo wa kisiasa.
“Kwa hiyo kuongezeka kwa aina na idadi ya migogoro inayohusiana na uchaguzi hutokea kwa kiasi kikubwa kutokana na ongezeko la umma kuelewa mchakato wa kurekebisha mambo.”
Haya ni maneno ya Mwanasheria kutoka Ofisi ya Taasisi za Kidemokrasia na Haki za Binadamu (ODIHR) ya nchini Poland, Denis Petit aliyoyaandika kwenye andiko lake “Kutatua migogoro ya uchaguzi.”
Maneno haya ya Denis Petit yanathibitisha historia ya kuanzishwa kwa Maadili ya Uchaguzi katika uchaguzi hapa nchini ambayo moja ya malengo yake ilikuwa ni kutatua migogoro inayojitokeza katika chaguzi.
Migogoro ya uchaguzi ni hali ya kutoelewana na malalamiko yanayoibuka kabla, wakati na baada ya uchaguzi baina ya mgombea wa chama kimoja na mgombea wa chama kingine au baina ya chama kimoja na chama kingine.
Msingi wa migogoro ya uchaguzi ni ukiukwaji wa taratibu za uchaguzi na ufanyaji wa vitendo vilivyokatazwa katika uchaguzi kwa makubaliano baina ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Serikali, vyama vya siasa na wagombea.
Historia ya Maadili ya Uchaguzi ilianza kutokana na changamoto zilizojitokeza katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 1995 kati ya wagombea wa vyama tofauti na kati ya chama na chama kingine.
Hali hiyo iliifanya Tume ya Taifa ya Uchaguzi kuandaa mapendekezo ya Mwongozo wa Maadili ya Uchaguzi ya mwaka 2000 ili kuweka msingi wa mazingira sawa ya ushindani.
Lengo mahususi la kuandaa maadili hayo ni kuhakikisha chaguzi zinafanyika katika mazingira ya usawa, haki na amani, hivyo kusaidia katika kujenga demokrasia imara katika chaguzi.
Mapendekezo hayo yalijadiliwa na wawakilishi wa vyama vya siasa na Serikali Julai 31, 2000 na hatimaye Tume, vyama vya siasa na Serikali walitia saini Maadili ya Uchaguzi ya mwaka 2000.
Hata hivyo, maadili haya hayakuwa na nguvu ya kisheria kwa kuwa yalitumika kama mwongozo tu wa mambo yanayoruhusiwa na yanayokatazwa kufanywa wakati wa uchaguzi ambao uliandaliwa baada ya Tume, Serikali, vyama vya siasa na wagombea kukubaliana na kusaini maadili hayo.
Maadili haya yamekuwa yakifanyiwa mabadiliko na kuboreshwa kila ifikapo Uchaguzi Mkuu kutokana na changamoto mpya zinazojitokeza uchaguzi mbalimbali.
Katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010, marekebisho ya Sheria ya Taifa ya Uchaguzi Sura ya 343 yalifanyika na Kifungu cha 124 A kiliundwa kuyapa nguvu ya kisheria Maadili ya Uchaguzi.
Kifungu hicho kiliipa Tume jukumu la kuandaa Kanuni za Maadili ya Uchaguzi na kuzichapisha kwenye Gazeti la Serikali, baada ya kushauriana na vyama vyote vya siasa na Serikali.
Kanuni hizo zilielekeza kuandaliwa maadili ya vyama vya siasa na Tume wakati wa kampeni na wakati wa uchaguzi na mbinu za utekelezaji wa kanuni hizo.
Pamoja na kuilazimisha Tume na Serikali kutekeleza kifungu hicho, kila chama cha siasa na mgombea hushurutishwa kukubali kufuata maadili hayo wakati wa kuwasilisha fomu ya uteuzi wa mgombea katika uchaguzi.
Katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015, vyama vya siasa, Tume ya Taifa ya Uchaguzi na Serikali, walikubaliana Maadili ya Uchaguzi wa rais, wabunge na madiwani ya mwaka 2015 kwa kutoa tamko kwamba:
“Sisi vyama vya siasa, Tume ya Taifa ya Uchaguzi na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa pamoja, tumekubaliana kuwa na uchaguzi huru, wa haki, uwazi na wa kuamika.
“Na kwamba amani, ustawi wa nchi, usalama wa raia, uhuru wa vyama vya siasa na utii wa sheria, kanuni na taratibu za uchaguzi ndio msingi wa uchaguzi ulio huru, haki na wenye kuzingatia ushiriki wa makundi yote ya jamii katika uchaguzi.
“Tunajipa na tunakubaliana kuwajibika kuyatekeleza maadili haya yanayotokana na kifungu cha 124A cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi ya mwaka 1985 (Sura ya 343).
“Tutafanya jitihada za wazi kuhakikisha maadili haya yanajulikana na kuheshimiwa na wagombea na wanachama wote wa vyama vya siasa”
Makubaliano haya yalikubaliwa na kuahidi kutekelezwa na Katibu Mkuu Dk Florens Turuka kwa niaba ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume Jaji Damian Lubuva Julai, 27 2015.
Wengine waliokubali maadili hayo na kuahidi kuyatekeleza ni viongozi wa vyama vyote 22 vya siasa vilivyokuwa na usajili wa kudumu, kupitia makatibu wakuu au Naibu wake, wenyeviti au makamu wao.
Maadili hayo ambayo tutayachambua katika makala zinazofuata, hutumika katika Uchaguzi Mkuu na katika chaguzi ndogo zinazofuata baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka husika.
Kila chama cha siasa na mgombea huwajibika kusaini maadili hayo wakati wa uchaguzi na chama ambacho hakitasaini kitazuiliwa kushiriki kampeni za uchaguzi na mgombea atakayekataa kusaini ataondolewa kushiriki katika uchaguzi.

Serikali yapewa somo uhaba walimu wa hesabu


Dar es Salaam. Wadau wa hisabati nchini wameipatia Serikali mbinu zitakazosaidia kupambana na uhaba wa walimu ili kuinua kiwango cha ufaulu wa somo hilo kinachoendelea kushuka licha ya umuhimu  wake.
Wakizungumza leo Machi 14, 2018 wakati wa maadhimisho ya Siku ya Hisabati Duniani, wadau hao wamesema ufaulu mdogo wa somo hilo imekuwa kilio ambacho bado hakijapata suluhisho la dhati.
Mwenyekiti wa Chama cha Hisabati nchini (Mat/Chahita), Dk Said Sima amesema takwimu za ufaulu katika miaka kumi iliyopita katika mitihani ya hisabati kitaifa ni asilimia 17.63 kwa shule za sekondari na asilimia ya 31.86 kwa shule za msingi.
Amesema utafiti uliofanywa  kwa baadhi ya shule zilizoshikilia nafasi za mwisho kitaifa kwenye mitihani hiyo jijini Dar es Salaam, uhaba wa walimu ni kati ya sababu za ufaulu mdogo.
Amesema ipo dawa ya kupambana na uhaba wa walimu wa masomo ya hisabati kwa Serikali kuajiri walimu waliohitimu vyuo mapema wanapomaliza badala ya kusubiri muda mrefu.
"Hii ya kusubiri muda mrefu inawafanya walimu kwenda kuajiriwa kwenye sekta nyingine na inapokuwa hivyo inakuwa vigumu kuwapata tena,"amesema.
Alitaja mbinu nyingine kuwa ni kuajiri wahitimu wa shahada za sayansi kwa kuwapa mafunzo maalumu ya ualimu na baadae kusomea kabisa taaluma hiyo.
Ameshauri kuwapo kwa mpango maalumu kwa vyuo vya ualimu na vyuo vikuu kusaidia kufundisha kwa kutumia wanafunzi waliopo vyuoni hasa nyakati za likizo na mwisho wa wiki.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dk Leonard Akwilapo amesema wapo tayari kupokea ushauri wa wadau hao kwa kuwa ni ukweli usiopingika kwamba kiwango cha ufaulu wa hisabati kinaanguka.
Amesema  kuhusu suala la walimu, Serikali inaendelea kupambana nalo kwa kuwaajiri na kutilia mkazo wa ufundishaji wa masomo hayo ili kuongeza ufaulu na kuendelea kuzalisha walimu wa kutosha.
Awali, Ofisa Viwango Mwandamizi wa Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Hamis Sudi amesema hakuna taaluma yoyote anayoweza kusomea mtu bila kuhusisha hesabu.
"Hesabu ni maisha, kila kitu kinafanywa kwa kutumia hisabati," amesema.

KAKAKUONA: Hoja ya Bashe ina mashiko, isipuuzwe



Mbunge wa Nzega Mjini (CCM), Hussein Bashe
Mbunge wa Nzega Mjini (CCM), Hussein Bashe 

Mbunge wa Nzega Mjini (CCM), Hussein Bashe, ametangaza nia ya kuwasilisha hoja binafsi ya kuundwa kwa kamati teule ya Bunge kuchunguza matukio aliyosema yanayotishia usalama na umoja wa taifa letu.
Nionavyo mimi, japo suala lake limepata upinzani kiasi, tena kutoka kwa baadhi ya wabunge wa chama chake, ametumia njia sahihi ya kuisimamia Serikali kupitia ibara ya 63(2) ya Katiba.
Matukio hayo ni pamoja na kusinyaa kwa demokrasia na haki za binadamu, kupotea, kutekwa na kuuawa kwa raia katika chaguzi mbalimbali na matukio ya uhalifu katika medani za siasa.
Hoja nyingine ni kupigwa risasi na kuumizwa na kikundi ambacho kinaitwa “Wasiojulikana”, mauaji ya viongozi wa kisiasa na ukandamizaji wa uhuru wa raia kutoa maoni yao.
Si hivyo tu, Bashe anakusudia kulishawishi Bunge likubali kujadili na hatimaye kuundwa kwa kamati teule, kuchunguza matumizi mabaya ya sheria na ukandamizaji wa demokrasia ndani ya nchi.
Pia, haki za kikatiba na kisheria za vyama vya siasa kutoheshimiwa na tuhuma dhidi ya vyombo vya usalama na matumizi ya silaha za moto kwa raia kunakofanywa na vyombo vyenye mamlaka.
Ipo mifano mingi katika hoja za Bashe, ikiwamo kushambuliwa kwa risasi zaidi ya 30 kwa Mbunge wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu Septemba 7, 2017 katika eneo la makazi yake mjini Dodoma.
Kwenye suala la utekaji, hakuna ubishi hadi leo, wapo Watanzania wenzetu Ben Saanane na mwandishi wa habari, Azory Gwanda, ambao walichukuliwa na watu wasiojulikana na haijulikani wapo wapi.
Ipo mifano pia ya mauaji ya viongozi wa kisiasa si wa upinzani tu bali hata wa chama tawala tena wilayani Kibiti waliuawa zaidi ya viongozi 10 wa CCM, swali kuu likiwa ni nani wanaofanya haya?
Hoja hii ya Bashe si mpya kwani ndani ya Bunge kulishaibuliwa hoja za aina hii wabunge wakitaka chombo hicho kisimamishe shughuli zake zilizopangwa kwa siku husika ili lijadili kuongezeka kwa kitisho cha usalama.
Wapo wabunge waliokwenda mbali na kupendekeza hadi kuvialika vyombo vya kimataifa vya uchunguzi ikiwapo Scotland Yard, ili kuchunguza matukio ambayo pengine Serikali inanyooshewa kidole.
Kwa hiyo, nilitarajia leo hii wabunge wote wangemuunga mkono Bashe kwa sababu hoja yake imebeba maslahi ya umma.
Tutazame dhamira ya Bashe ya sasa, pasipo kutizama kauli zake zilizopita ambazo huenda alizitoa katika medani za kisiasa, huenda amekaa chini na kutafakari na kuona mahali alipokosea, sasa anarudi katika msitari sahihi.
Ni ukweli ulio dhahiri kuwa hofu imetawala kwa baadhi ya Watanzania kutokana na mwenendo wa matukio aliyoyataja Bashe, ambayo mengine yamesababisha damu za Watanzania kumwagika.
Kwanza inabidi tumpongeze mbunge huyo kwa ujasiri wake huu ambao hakika naamini, ni wabunge wachache wa CCM wangethubutu kulifanya hili. Hata kama haitaungwa mkono, lakini ujumbe utakuwa umefika.
Anachokifanya Bashe, ni kutumia chombo sahihi ili Watanzania wapate majibu sahihi ya hoja zake nane ambazo, kwa Mtanzania yeyote mwenye akili timamu, atajua ndizo zinazolitafuna taifa kwa sasa.
Wabunge na wananchi wanaomkosoa Bashe leo wanaweza kujiona wako salama sana, lakini wanaweza kukumbuka shuka wakati kumekucha. Bashe amewasilisha kile kilicho katika mioyo ya Watanzania. Hakuna ubishi kwamba umoja na mshikamano wetu umetikiswa na unaendelea kutikiswa na matukio aliyoyaorodhesha Bashe, ninaamini hoja yake itasaidia kuisafisha Serikali yetu inayonyooshewa kidole.
Kwa mtazamo wangu, huu ni wakati ambapo Serikali ingempa ushirikiano mkubwa Bashe ili kupitia Bunge, wale wanaoinyooshea kidole wakose cha kusema pale itakapobainika haina mkono wake.
Ndio maana nasema, tumuunge mkono Bashe, hoja yake ina mashiko.

Anayedaiwa kuua askari mwenzake apandishwa kizimbani

Dar es Salaam. Mwanajeshi MT 109795 Private Ramadhan Mlaku (28) amefikishwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu akikabiliwa na shitaka la mauaji ya askari mwenzie, MT 79512 SGT Saimon Munyama.
Mshtakiwa huyo alifikishwa mahakamani hapo leo Jumatano Machi 14, 2018 saa tano asubuhi na gari la kubebea wagonjwa.
Alishushwa katika gari hilo akiwa juu ya kitanda cha wagonjwa na kupelekwa chumba cha mawakili wa Serikali ambapo alisomewa shtaka linalomkabili.
Akisomewa shtaka mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba wakili wa Serikali, Mosii Kaima amesema mtuhumiwa huyo anadaiwa kufanya kosa hilo Oktoba 30, 2017.
Imedai kuwa mshtakiwa ambaye ni mwanajeshi wa kambi ya Jeshi Makongo siku hiyo akiwa Makao Mkuu ya JWTZ Upanga, Dar es Salaam alimuua askari mwenzie MT 79512 SGT Munyama.
Baada ya kusomewa shtaka hilo, mshtakiwa huyo hakuruhusiwa kuongea chochote kwa sababu Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu haina mamlaka ya kuisikiliza kesi hiyo.
Pia kosa hilo hakuna dhamana kwa mujibu wa sheria.
Upande wa mashtaka ulidai kuwa upelelezi bado haujakamilika na Hakimu Simba aliutaka upande wa mashtaka kujitahidi kukamilisha upelelezi wa kesi hiyo mapema.
Kesi imeahirishwa hadi Machi 28, 2018 kwa ajili ya kutajwa ili kuangalia kama upelelezi utakuwa umekamilika ama la.
Baada ya kusomewa shtaka hilo mshtakiwa huyo alipandishwa tena katika gari la wagonjwa na kurudishwa mahabusu.

Wakili wa viongozi mtandao wa wanafunzi afunguka


Dar es Salaam. Wakili wa viongozi wa  Mtandao wa Wanafunzi Tanzania (TSNP), Reginald Martine amesema wateja wake wameitwa kuhojiwa na mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI) ili kutoa ushahidi wa tukio la ‘kutekwa’ kwa mwenyekiti wao, Abdul Nondo.
Akizungumza na MCL Digital leo Machi 14, 2018, Martine amesema tayari viongozi wawili kati ya wanne wa mtandao huo wameshatoa ushahidi wao, kwamba hakuna vitisho vyovyote walivyopewa na polisi.
Amesema kuwa polisi wamemhakikishia kuwa hawatawashikilia viongozi hao na mara watakapomaliza kutoa ushahidi wataruhusiwa kuondoka.
“Utaratibu wa wakili mtu anapokuwa anatuhumiwa lazima uwe na mteja wako wakati anapohojiwa lakini kama mteja anatoa ushahidi wakili siyo lazima awepo hivyo wanaendelea kutoa ushahidi muda,” amesema.
Amesema walishauriana na  mmoja wa makamishna kuwa yeye asiwepo na viongozi hao wakati wanatoa ushahidi wao.
Waliofika kuhojiwa na  DCI ni mkaguzi wa haki za binadamu, Alphonce Lusako; katibu wa mtandao huo, Malekela Brigthon; ofisa habari Hellen Sisya na mkurugenzi wa Idara ya sheria, Paul Kisabo.
Waliokwisha hojiwa mpaka kufikia leo saa 7 mchana ni Lusako na Brigthon.

Zilivyoibuka mahakama za majukwaa ya kisiasa na mitandaoni


‘Mahakama ya Kangaroo’ ni msamiati wenye maana ya mabaraza ya uamuzi au mikutano yenye kutoa hukumu kwenye mashauri mbalimbali pasipo kuheshimu misingi ya sheria na haki. Kwamba watu wanakaa kikao na kutoa hukumu kwa mtu au watu bila kutimiza viwango vya kisheria katika utoaji haki.
Msamiati huo pia hubeba tafsiri ya uwepo wa mahakama halali kisheria yenye mamlaka kwenye nchi, lakini hakimu au jaji kwa makusudi anaamua kuendesha kesi nje ya sheria na maadili ya mahakama. Pia, huonekana kupitia hukumu zenye kukandamiza haki kwa makusudi.
Kauli kali zenye kuhukumu kabla ya kufika mahakamani ambazo hutamkwa na watawala au amri za kisiasa zenye kutolewa na viongozi wa nchi ni miongoni mwa masuala yenye kuelezwa kama Mahakama ya Kangaroo. Matamshi yenye kumtia mtu hatiani kwanza kisha vyombo vya sheria ndiyo vianze kuchukua hatua, ni kipimo chenye kuthibitisha hali hiyo.
Mfano wa Mahakama ya Kangaroo ni kama Baraza la Mapinduzi ya watu wa Cambodia, lililoketi Agosti 19, 1979 na kumhukumu kifungo cha maisha jela aliyekuwa Waziri Mkuu wa nchi hiyo, Pol Pot na ndugu yake, Leng San. Umoja wa Mataifa ulikataa hukumu hiyo kwa sababu baraza husika halikutimiza vigezo vya kimahakama, yaani hakukuwa na mchakato kabla ya hukumu.
Katika mahakama za kawaida ukweli wa pande mbili unasikilizwa kwa uhuru usio na vipengele. Ushahidi unatolewa na shahidi anavumiliwa wakati akieleza kile alichonacho kuhusiana na shauri husika. Mawakili wanaachiwa uga mpana wa kuhoji ili kurahisisha haki ionekane inatendeka. Mwisho jaji au hakimu anahukumu baada ya vipimo vya kisheria.
Mchakato wa mahakama umewekwa kwenye nchi ili kulinda haki za watu dhidi ya haki za kisheria. Kwamba mtu hata aonekane mkosefu kiasi gani kwenye macho ya wengine, hususan watawala, ahukumiwi kwa matakwa ya watu, bali anapimwa dhidi ya haki za kisheria. Huo ndiyo utaratibu wa nchi kama ulivyowekewa mwongozo na Katiba ya nchi.
Kwa kurejea tafsiri ya Mahakama ya Kangaroo ni kuwa maoni yoyote yenye kuhukumu watu wengine ni kosa, maana ni uthibitisho wa uwepo mahakama hiyo. Na kwa vile kwenye mitandao ya kijamii kumekuwa na maoni mengi yenye kuhukumu wengine, ni wazi kuwa mitandaoni kuna mahakimu na majaji wengi siku hizi.
Viongozi wengi wa kisiasa wamekuwa wakitoa amri na matamshi yenye kuhukumu. Huo ni uthibitisho kwamba mahakama hii inapatikana sana kwenye majukwaa ya kisiasa. Inapaswa kufahamika kwamba Mahakama ya Kangaroo ni kielelezo cha nchi kuwa na watu wasioheshimu haki za kisheria ambazo zimewekwa mahsusi ili kulinda haki za watu.
Kadhalika ni kipimo kuwa watu wengi hupenda watendewe haki lakini wao wenyewe hawaheshimu haki za wengine. Vilevile viongozi ni wepesi kusisitiza kuchukuliwa kwa hatua za kisheria, lakini katika nafasi zao hawaziheshimu. Mahakama za Kangaroo hazipaswi kuwepo. Kila mtu ni vizuri akajisikia kutendewa haki mbele ya sheria za nchi.
Nondo na Mahakama ya Kangaroo
Mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Abdul Nondo ambaye ni mwenyekiti wa Mtandao wa Haki za Wanafunzi Tanzania (TSNP), alidaiwa kutoweka usiku wa Machi 6, mwaka huu, kabla ya kupatikana jioni Machi 7. Inaelezwa kuwa Nondo alipokuwa kwenye mazingira aliyohisi ni yenye hatari, alituma ujumbe kwa rafiki yake.
Nondo anadaiwa kutuma ujumbe “Nipo katikati ya hatari”. Baada ya hapo hakupatikana tena. Jioni ya Machi 7, Nondo alipatikana au alijikuta yupo Mufindi, Iringa. Mtu aliyetoa taarifa za Nondo kupatikana Mufindi, alidai alimkuta akiwa haelewi alipo, ndipo alimsaidia pesa ya kukodi taksi aende Kituo cha Polisi Wilaya ya Mufindi kuripoti apate msaada zaidi.
Habari za awali ni kwamba Nondo alikuwa Dar es Salaam. Ujumbe kwamba alikuwa kwenye hatari, aliutuma akiwa Dar es Salaam. Siku iliyofuata ndipo alijikuta Mufindi. Taarifa za kupotea Nondo zilisababisha mwamko mkubwa wa kuhoji hasa kwenye mitandao ya kijamii. Nondo alipatwa na madhila hayo kipindi akiwa ameahidi kuongoza wanafunzi kuandamana kushinikiza Waziri wa Mambo ya Ndani, Mwigulu Nchemba ajiuzulu.
Nondo alisema, wangeandamana kwa sababu ya kuwapo kwa matukio mengi ya uvunjifu wa haki za binadamu. Watu wengi wakikutwa wameuawa nchini na kukosekana majibu ya kina kuhusiana na vifo hivyo. Zaidi ni tukio la kuuawa kwa mwanafunzi wa Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT), Akwilina Akwilini.
Akwilina aliuawa kwa kupigwa risasi akiwa kwenye daladala Februari 16, mwaka huu, wakati polisi wakizuia maandamano ya viongozi na wafuasi wa Chadema, waliokuwa wanakwenda ofisi za msimamizi wa uchaguzi jimbo la Kinondoni, kushinikiza mawakala wao wapewa hati za viapo na barua za utambulisho.
Akwilina hakuwa katika sehemu ya maandamano. Vilevile kuna wengine walikuwa kwenye maandamano na walipigwa risasi, lakini wakawekwa mahabusu bila kutibiwa wala kupewa dhamana. Kwa matukio hayo, Nondo aliona ni wakati mwafaka Mwigulu kung’oka Wizara ya Mambo ya Ndani.
Sasa basi, baada ya Nondo kuwa amepatikana na kwenda Kituo cha Polisi Mufindi, taarifa ya awali kabisa ya Kamanda wa Polisi Iringa, Juma Bwire ilieleza watamshughulikia kama taarifa alizotoa zilikuwa za uongo. Kwa hisia za Kamanda Bwire ni kwamba huenda Nondo alitoa taarifa za kutekwa ili kuhamasisha wanafunzi wenzake kufanya vitendo vya uvunjifu wa amani.
Izingatiwe kuwa Nondo ndiye mlalamikaji. Aliripoti polisi ili kueleza yaliyomsibu kuanzia kutekwa Dar es Salaam mpaka kujikuta Mufindi. Polisi wanaopaswa kushughulikia tukio hilo, kabla hata ya kufanya uchunguzi, wanaanza kutoa vitisho.
Ukiisoma kauli ya Kamanda Bwire, unaona kuwa polisi wanamtuhumu Nondo kwa nafasi ya kwanza kwamba ‘alijiteka’ kwa nia ovu, halafu wanazichukua tuhuma zake za kutekwa kwa nafasi ya pili.
Mpaka hapo inatia shaka ikiwa kweli Nondo alitekwa, kama utafanyika uchunguzi makini, wakati wachunguzi wenyewe wanamtuhumu anayetakiwa kusaidiwa kiuchunguzi.
Mkuu wa Mkoa wa Dar wa Salaam, Paul Makonda, yeye ameagiza polisi Iringa wakishamalizana na Nondo, wampeleke Dar es Salaam wamshughulikie kwa sababu hawezi kuuchafua ‘mkoa wake’ halafu aachwe. Hakuna namna nyingine ya kuitafsiri kauli hiyo zaidi ya kuusema ukweli kwamba Nondo ameshahukumiwa kuwa hakutekwa.
Katika mitandao ya kijamii hali ndiyo mbaya kabisa. Watoa maoni wengi wanamtuhumu Nondo kuwa alisafiri kwa basi mwenyewe kwenda Mufindi, kwa hiyo alitangaza kuwa ametekwa ili kusababisha taharuki kwa nchi, vilevile kujitafutia umaarufu kwa njia za kihalifu. Tayari Nondo ameshahukumiwa mitandaoni.
Haki batili
Viongozi na watumia mitandao ya kijamii wanatakiwa kuheshimu haki za kisheria. Waache kujigeuza Mahakama za Kangaroo. Hukumu kwa watenda makosa haitolewi mitandaoni wala kwenye majukwaa ya viongozi wa kisiasa. Misimamo ya kisiasa isiwe sababu ya kuwazodoa au kuwapuuza wenye kustahili haki.
Inatakiwa kwanza Nondo asikilizwe. Alichokisema kifanyiwe uchunguzi. Ikiwa maelezo yake yatakosa nguvu ya kiupelelezi, ndipo tuhuma zihame, kutoka kutuhumu kutekwa hadi yeye kutuhumiwa kujipoteza kwa nia ovu. Siyo kumshambulia na kuanza kutoa ahadi za kumshughulikia.
Tafakari iwapo Nondo kweli alitekwa. Maumivu aliyonayo kutokana na tukio hilo. Wakati akitegemea polisi na viongozi wa nchi wamsikilize, wamtendee haki na ikibidi waliomfanyia uhalifu wakamatwe, anajikuta akituhumiwa kutaka kusababisha taharuki kwa nchi kwa kutangaza alitekwa wakati haikuwa hivyo.
Wengine wanasema si kweli kwamba Nondo alitekwa, maana asingeachiwa nafasi ya kutuma ujumbe wa simu kwa rafiki yake. Wanasema kama alitekwa mbona hakuguswa hata kidogo? Watu hao wanajipa uchambuzi wa watu kutekwa. Utafikiri ipo kanuni kwamba kila mwenye kutekwa lazima anyang’anywe simu na apigwe mpaka aumizwe.
Aliyesema Nondo anauchafua mkoa wa Dar es Salaam kwa kutangaza alitekwa, maswali kwake ni je, anayechafua ni anayeteka au anayetekwa? Kwa nini watu wawe wakali kwa aliyetangaza kutekwa kuliko kusaidia kuwapata watekaji? Je, imesahaulika kuwa mwanamuziki Ibrahim Mshana ‘Roma Mkatoliki’ alitekwa wapi?
Roma akiwa na wenzake watatu, walitekwa Oysterbay, Dar es Salaam kwenye studio ya muziki ya Tongwe Records na walishikiliwa kwa siku tatu kabla kuachiwa na kujikuta wapo Ununio, Dar. Kada wa Chadema, Ben Saanane, alitoweka Dar es Salaam tangu Novemba 2016 na mpaka leo hajaonekana.
Wapo watu walituhumu kuwa Ben alijipoteza mwenyewe kutafuta umaarufu. Miaka inapita, hali ni kimya, Ben haonekani. Hata Roma na wenzake pamoja na kutokeza wakiwa wamejeruhiwa, bado walisemwa walijiumiza makusudi ili kuhalalisha kwamba walitekwa. Leo Nondo anaulizwa eti mbona hakuumia hata kidogo. Mahakama za Kangaroo ni hatari sana.