Sunday, October 29

Cuba yakana kuwashambulia kwa sauti wafanyakazi wa ubalozi wa Marekani

A car with tourists drives past the US Embassy in HavanaHaki miliki ya pichaREUTERS
Image captionCuba yakana kuwashambulia kwa sauti wafanyakazi wa ubalozi wa Marekani
Cuba inasema kuwa hakujakuwa na mashambulizi ya kutumia sauti dhidi ya wafanyakazi wa ubalozi wa Marekani kwenye mji wake mkuu Havana, ikisema kuwa madai hayo ni kisiasa yenye lengo la kuharibu uhusiano kati ya nchi hizo mbili.
Waziri wa mashauri ya nchi za kigeni wa Cuba Bruno Rodriguez alipinga madai hayo ya kuwepo mashambulizi ya sauti akiyataja kuwa kuwa uwongo.
Marekani inasema kuwa karibu wafanyakazi wake 20 katika ubalozi wake walikumbwa na matatizo ya kiafya na kuwapunguza wafanyakazi wake kutokana na kisa hicho.
Ripot zinasena kwa hatua hiyo ilichukuliwa kutokana na mashambulizi ya sauti lakini hata hivo hakuna kile kimethibitishwa.
Cuban Foreign Affairs Minister Bruno Rodriguez speaking during a news conference at the Foreign Affairs Ministry in Havana on 3 OctoberHaki miliki ya pichaAFP
Image captionBw Rodriguez alitaja madai hayo kuwa uongo
Marekani haijailaumu Cuba kwa mashambulizi hayo, na serikali ya Cuba imekana mara kwa mara kuwalenga wafanyakazi wa ubalozi. wa Marekania mjini Cuba.
Marekani iliwatimua wanadiplomasia watano wa Cuba, ikisema kuwa Cuba ilishindwa kuwalinda wafanyakazi wake.
Serikali ya Marekani pia ilifuta shughuli za utoaji visa katika ubalozi wake mjini Havanna
Akizungumza mjini Washington wakati wa mkutana na raia wa Cuba wanaoishi nchini Marekani, Bw. Rodriguez alisema kuwa madai hayo yamesababisha kuharibika kwa uhusiano kati ya serikali hizo mbili.

AMANI HUJENGWA KWA MARIDHIANO


HIVI karibuni Waziri Mkuu mstaafu, Jaji Joseph Warioba, aliwataka viongozi wa kisiasa kujenga utamaduni wa kukutana mara wanapogundua kuna matukio yanayoashiria uvunjifu wa amani.
Jaji Warioba ambaye alikuwa Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, alisema waasisi wa taifa hili walijenga misingi ya umoja ambao hivi sasa unaelekea kutoweka.
Ushauri huo una mashiko kwa jamii.
Jaji Warioba amesema kuna viashiria vya kutoweka kwa amani na viongozi wa kiserikali na kisiasa wanapaswa kuiga mfano unaofanywa na viongozi wa dini, ambao hukutana mara kwa mara kujadili masuala mbalimbali yakiwamo ya kitaifa.
Jaji Warioba anasema: “Nchi haiwezi kuendeshwa kwa huyu kuongea hiki, huyu naye anamjibu kupitia vyombo vya habari, hapana, hawa watu wakae wazungumze.”
Bila shaka Jaji Warioba amezungumza hayo akiamini kuwa majibizano yenye mtazamo huo aliouzungumza hayawezi kujenga mshikamano, bali ni chanzo cha watu kuibua migogoro hali inayoweza kuhatarisha amani ya taifa.
Linapozungumzwa suala la amani, linajumuisha utulivu na masikilizano miongoni mwa jamii, wakiwamo viongozi wa kisiasa.
Kwa muktadha huo, ili kujenga ushirikiano na amani, ni muhimu viongozi wetu wa kisiasa kujenga utaratibu wa kukutana mara kwa mara na kutazama mwelekeo wa taifa kwa nia ya kujenga umoja wetu ulioasisiwa na Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Nyerere.
Wote tunafahamu kuwa amani ni kitu kinachojengwa kwa nguvu kubwa ya pamoja, lakini ikivunjika ni vigumu kuirejesha.
Kwa msingi huo, sisi kama taifa ni muhimu kuutazama ushauri wa Jaji Warioba kwa jicho pana badala ya kutumia nguvu kubwa kujibishana.
Ifahamike kuwa ustawi wa taifa haujengwi kwa misuguano au malumbano yasiyo na tija, bali hujengwa kwa kukaa pamoja kujadiliana kwa hoja hatimaye kukubaliana.
Jaji Warioba ametoa ushauri, ni vema uzae matunda. Naamini watu wazima akiwamo mzee Warioba wakitoa ushauri maana yake wameona jambo.

BASHE ATOA VITAMBULISHO VYA MATIBABU BURE KWA WAZEE NZEGA


MBUNGE wa Nzega Mjini, Hussein Bashe, ametoa vitambulisho vya matibabu bure kwa wazee 3,284 wa jimbo lake huku akisema amefanya hivyo kwa kuwa wazee hao wamelitumikia Taifa kwa muda mrefu na sasa ni vyema vijana wakawahudumia.
Utoaji wa vitambulisho hivyo ni utekelezaji wa Sera ya Taifa Matibabu ya Bure kwa wazee, ambapo baada ya kupata vitambulisho hivyo, itakuwa rahisi kwao kwenda hospitali na kupatiwa matibabu bila malipo.
Katika uzinduzi wa zoezi hilo, Bashe ametoa vitambulisho 540 na vingine vitaendelea kutolewa katika ofisi ya Mbunge iliyopo Nzega Mjini.
Akizungumza na wazee waliojitokeza kupokea vitambulisho hivyo, Bashe alisema: “Wazee hawa wameitumikia nchi hii kwa muda mrefu, ni jukumu letu sasa kama vijana na Taifa kuhakikisha nasi tunawalipa sehemu ya nguvu kubwa walizotumia kuifikisha Tanzania hapa ilipo leo kwa kuwapatia matibabu bora na kuwaondolea gharama za matibabu ili kuleta unafuu wa maisha.
“Nilichokifanya ni kugharamia fedha zote za vitambulisho ili kuhakikisha kila mzee ndani ya Jimbo la Nzega Mjini anapata kitambulisho cha matibabu ya bure.”
Mkuu wa Wilaya ya Nzega, Godfrey Ngupula,​ ambaye alikuwa mgeni rasmi kwenye zoezi hilo, alimpongeza Bashe kwa kusimamia  shughuli za maendeleo na kuwatumikia wananchi kwa moyo wake wote.

SIRI NZITO MAITI ZINAZOOKOTWA BAHARINI


WAKATI hali ya sintofahamu imetanda kutokana na mwenendo wa maiti kuokotwa mara kwa mara katika fukwe za Bahari ya Hindi, zikiwa zimefugwa ndani ya mifuko ya sandarusi (viroba) au ya plastiki,
wazoefu wa masuala ya bahari, hususani wavuvi, wamesema ni jambo la kawaida kwao, hasa msimu wa pepo za kusi.
Lakini licha ya kuwa matukio hayo ni jambo la kawaida kwao, kwa sasa nao wameingiwa hofu kubwa ndani ya msimu wa pepo hizo kwa mwaka huu, baada ya kuona maiti nyingi zikiwa zimefungwa katika sandarusi, mtindo waliodai ni mpya machoni mwao.
Uchunguzi uliofanywa na MTANZANIA Jumapili kwa kuwafikia wavuvi, madalali wa samaki na wafanyabiashara wadogo wadogo kwa nyakati tofauti katika fukwe tano za Bahari ya Hindi zilizopo Dar es Salaam, umebaini kuwa licha ya mshangao na hofu kubwa ya kuwapo matukio hayo, lakini wengi wao hawapendi kutoa taarifa katika vyombo vya dola pindi wanapoziona maiti zikielea baharini.
Baadhi waliliambia MTANZANIA Jumapili kuwa hawapendi kutoa taarifa katika vyombo vya dola kwa sababu ya kukwepa usumbufu.
Kuhusu uzoefu wao wa masuala ya baharini, walisema kuwa msimu wa pepo za kusi zinazoanza Juni na kumalizika Oktoba, umekuwa ni kawaida kwao kuona maiti nyingi baharini za watu wa jinsia tofauti.
Lakini walisema hali hiyo imekuwa tofauti katika msimu wa mwaka huu, baada ya kuona maiti nyingi baharini zikiwa zimefungwa ndani ya sandarusi na kufungwa kamba miguuni kiunoni na mikononi.
Pia walisema wamekuta maiti nyingine zikiwa zimefungwa mifuko myeusi iliyoziba uso hadi shingoni, huku miguu na mikono nayo ikiwa mefungwa ama kamba au nyaya.
Simulizi ya wavuvi hao inatoa picha tata yenye maswali mengi kuhusu mwenendo wa matukio hayo. Ni nani anayeua watu kwa mtindo huo? Wanauawa kwa sababu gani? Maiti hizo zinatoka wapi?
Zipo hisia kutoka kwa baadhi ya wavuvi, kwamba miili hiyo huenda imesukumwa na mawimbi ya bahari kutoka kusini mwa Tanzania, ambako pia kuna mataifa yanayotumia Bahari ya Hindi kama Msumbiji, Visiwa vya Comoro, Mayotte, Afrika Kusini, na Madagascar.

UCHUNGUZI
Wavuvi waliofanya mahojiano na MTANZANIA Jumapili katika Ufukwe wa Mbweni, walidai kwamba maiti zilizofungwa hazijawahi kuonekana katika maeneo ya ufukwe huo.
Kwa mujibu wa maelezo ya baadhi ya wavuvi hao, waliziona maiti zilizowekwa katika sandarusi kwa nyakati tofauti katika sehemu mbalimbali za katikati ya bahari.
Embes Haji Alli ambaye ni mmoja wa wavuvi katika eneo hilo, alisema Agosti, mwaka huu, akiwa katika eneo la kina kirefu cha bahari upande wa Unguja akifanya shughuli zake za uvuvi, aliona mzigo ukielea na alipousogelea kwa udadisi zaidi, akabaini ni maiti ambayo tayari ilikuwa imeharibika.
“Ilikuwa usiku wakati navua  samaki huko mkondoni (kina kirefu cha bahari) upande wa Unguja, niliona kitu kinaelea ikabidi niwe makini kukifuatilia, nilipokisogelea nikamulika vizuri kwa tochi kubwa, nikabaini ni maiti na tayari ilikuwa imeharibika na macho yalikuwa yamenyofoka.
“Baada ya kubaini hivyo, niliachana nayo kisha nikaendelea na shughuli zangu, lakini siku chache baadaye nilipata taarifa kwamba wavuvi wengine kwa upande wa Zanzibar walidai kuona maiti tano zikiwa katika mtindo ule ule wa kuwekwa katika sandarusi,” alisema.
Naye Abas Juma ambaye pia ni mvuvi katika ufukwe huo, alisema kati ya Julai na Septemba, mwaka huu, aliziona maiti tatu baharini, mbili kati ya hizo zilikuwa zimetiwa ndani ya sandarusi na moja ikiwa imefungwa kwa mfuko wa plastiki kichwani.
Juma alisema siku chache baadaye alipata taarifa kuwa wavuvi wenzake mkoani Tanga nao waliona maiti mbili zikiwa katika mtindo huo huo aliouona.
Pamoja na simulizi ndefu ya wavuvi hao, mwandishi aliwahoji kutaka kujua hatua walizochukua baada ya kuziona maiti hizo.
Juma alisema kuwa kwa kawaida huwa wanatakiwa kutoa taarifa polisi, lakini wavuvi wengi wamejenga tabia ya kutoripoti kwa kukwepa usumbufu, hivyo hata yeye hakuripoti sehemu yoyote zaidi ya kuwasimulia wenzake.
“Huku baharini tunakutana na maiti nyingi, lakini wengi wetu tumekuwa wazito kutoa taarifa kwa sababu unapotoa taarifa ya kuonekana maiti unajikuta katika wakati mgumu wa kutoa maelezo mara kwa mara polisi kana kwamba wewe ni mhalifu, hali hii unajikuta unapoteza muda wako polisi badala ya kwenda kutafuta riziki,” alisema Juma.
Katika Ufukwe wa Ununio, dalali mkuu wa samaki wa Soko la Ununio, Rashid Athuman, alieleza kuwa ana uzoefu wa miaka 15 katika shughuli hiyo na kwa muda wote huo hajawahi kusikia au kuona maiti imeingizwa katika mifuko ya sandarusi kama inavyotokea mwaka huu.
Alisema wakati wa pepo za kusi, maiti moja au mbili huonekana baharini, lakini si kama za sasa.
Alidai kuwa baadhi ya wavuvi katika ufukwe huo, waliwahi kumdokeza kwamba wakiwa katika shughuli zao waliona maiti zikiwa zimefungwa katika mifuko ya sandarusi.
“Hapa wavuvi wanashangazwa na hata sisi tunashangazwa, unajua nyakati kama hizi miaka ya nyuma tulikuwa tunapata habari ya kuonekana maiti huko baharini, labda watoto au watu wazima, lakini mazingira ambayo maiti hizo zinakutwa si ya kufungwa katika viroba au mawe kama inavyoripotiwa sasa.
“Nakumbuka mara ya mwisho nyakati kama hizi katika pwani hii, ulionekana mguu wa mtu akiwa amevaa viatu aina ya chachacha, tulitoa taarifa kwa mamlaka husika kisha tukauzika huo mguu, lakini tangu tukio hilo hakujawahi kuwapo taarifa za kuonekana maiti baharini zaidi ya hizo zinazotajwa sasa za watu kufungwa katika viroba,” alisema Athuman.
Naye Sesye Mwafongo, ambaye ni mvuvi katika ufukwe huo, alisema kawaida huwa anakwenda kuvua samaki baharini umbali wa kilomita 20 kutoka nchi kavu na kuna siku moja alidai kukutana na wavuvi wenzake baharini wakamwambia wameona mfuko wa sandarusi uliokuwa na maiti.
Hata hivyo, alisema hakuweza kuiona maiti hiyo kwa sababu alishindwa kusonga mbele zaidi kutokana na upepo mkali uliovuma kwa siku tatu mfululizo.
Mvuvi mwingine katika ufukwe huo, Mohamed Makuchele, alisema ndani ya miezi mitatu iliyopita amekutana na maiti tano baharini zikiwa zimewekwa katika mifuko ya sandarusi.
Pasipo kukumbuka tarehe, Makuchele alisema Septemba, mwaka huu aliona maiti tatu zilizofungwa katika mifuko ya sandarusi, zikiekea katika eneo la kina kirefu cha bahari upande wa Bagamoyo.
Pia alisema ndani ya mwezi huo huo, alikutana na maiti nyingine mbili zikiwa zimefungwa kwa mtindo huo huo katika eneo la kina kirefu cha bahari kwa upande wa Unguja Shamba.
Makuchele mwenye uzoefu na uvuvi baharini kwa zaidi ya miaka 25, alisema shughuli zake ni za kuhama hama kutokana na eneo wanakopatikana samaki wengi, ndiyo maana hakuweza kutoa taarifa sehemu yoyote.
Akielezea uzoefu katika mambo ya baharini, alisema ni kawaida nyakati za pepo za kusi kukuta maiti zikielea baharini na hali hiyo inatokana na ama wavuvi au wasafiri kutumia vyombo duni ambavyo ni rahisi kuzama kama kukiwa na upepo baharini.
Pia alisema maiti alizoziona zikiwa zimefungwa katika sandarusi ni suala geni kwake.
“Miaka ya nyuma kidogo tulikuwa tunavua samaki huko  karibu na Visiwa vya Comoro na ulikuwa msimu wa pepo hizi za kusi, kweli tuliwahi kukutana na maiti kama 10 hivi za watu waliofungwa mikono na miguu, nyingine zimefungiwa mawe kifuani na hilo lilikuwa ni jambo geni machoni mwetu, lakini hizi maiti za sasa za kuwekwa ndani ya mifuko ya sandarusi kama mizigo kwa kweli nastaajabu na sijawahi kuona tangu nimeanza kazi yangu hii,” alisema Makuchele.
Pamoja na Makuchele kudai kukutana na maiti zilizofungwa katika mifuko ya sandarusi kwa nyakati tofauti, lakini naye hajaripoti sehemu yoyote kwa sababu ya kukwepa usumbufu.
Bekuli Haule ambaye pia ni mvuvi katika eneo hilo, alisema kwa mambo aliyoyaona baharini katika kipindi hiki, hawezi kumsimulia mtu yeyote.
Alipoulizwa kama mambo hayo ndiyo maiti zilizowekwa katika mifuko ya sandarusi, alisema atakufa na siri yake moyoni.
Katika Ufukwe wa Kunduchi, Ali Mohamed ambaye ni nahodha wa boti ya uvuvi inayobeba wavuvi 12 hadi 15, alisema Septemba, mwaka huu akielekea katika eneo la uvuvi la kina kirefu cha bahari, kilomita chache kutoka Kisiwa cha Mbudya, alikuta maiti tatu zilizofungwa katika mifuko ya sandarusi zikielea.
Alisema wakati anarejea kutoka katika shughuli zake za uvuvi, alikuta miili miwili, kati ya hiyo, ikiwa imesogea karibu na kisiwa hicho ndipo akachukua jukumu la kutoa taarifa katika Ofisi za Idara ya Hifadhi za Bahari na maeneo tengefu zilizopo kisiwani Mbudya.
“Wakati tunaenda tuliona maiti tatu, moja imewekwa katika mfuko wa sandarusi na mbili zikiwa zimefunikwa kwa mfuko wa plastiki kichwani.
“Wakati tunarudi hatukuona maiti moja, ila tuliziona mbili, ile iliyowekwa katika sandarusi na moja iliyokuwa imevishwa mfuko wa sandarusi kichwani, lakini mfuko ulikuwa tayari umepasuka labda kwa sababu ya maiti kuvimba.
“Niliamua kufika pale kisiwani Mbudya na kuutaarifu uongozi wa Idara ya Hifadhi za Bahari na Maeneo Tengefu kisha sisi tukaendelea na kazi zetu,” alisema Mohamed.
Nahodha wa boti katika ufukwe huo, Idrisa Abdallah, alisema kati ya Agosti na Septemba, mwaka huu, ameona mifuko sita ya sandarusi iliyofungawa mizigo na minne kati ya hiyo ilikuwa na maiti.
Abdallah alisema mifuko hiyo ilikuwa imetawanyika katika maeneo mbalimbali ya karibu na visiwa vya Mbudya na Bongoyo.
Alisema baada ya kuona maiti hizo, alitoa taarifa kwa uongozi wa Idara ya Hifadhi za Bahari na Maeneo Tengefu na hajui kilichoendelea baada ya hapo.
“Sio simulizi tu kaka, kwa macho yangu nimeona maiti nne zimefungwa kwenye mifuko ya sandarusi, niliiona mifuko sita usiku wakati nakwenda kuvua, nikajaribu kudadisi nikaona maiti moja wakati tunarudi alfajiri nikaiona tena mifuko ile, ikabidi niidadisi zaidi, nikakuta maiti nyingine tatu na mifuko miwili ikiwa imefungwa kama kifurushi, sasa sikujua kuna nini ndani yake,” alisema Abdallah.
Naye Mjumbe wa Soko la Samaki la Kunduchi, Bakari Poka, alisema pamoja na kwamba maiti zinazokutwa katika mazingira ya kuwekwa katika mifuko ya sandarusi au kufungwa mifuko ya plastiki kichwani, bado haijaonekana katika ufukwe huo, lakini wavuvi wamedai kuona maiti nyingi za aina hiyo katikati ya bahari.
Katika Ufukwe wa Kawe, wavuvi waliokuwapo eneo hilo, walikataa kutoa ushirikiano kwa kile walichokieleza kwamba kuna kamanda wao anayehusika na kuzungumzia jambo lolote kwa niaba yao.
Walipoulizwa mahali alipo kamanda wao huyo, walisema yuko baharini anaendelea na uvuvi na walipoombwa mawasiliano yake ya simu, waligoma huku wakimweleza mwandishi kuwa analazimisha upelelezi.
Baada ya mahojiano hayo kuonekana kuibua hasira miongoni mwao, mwandishi aliachana nao na akaenda kuwahoji baadhi ya wafanyabiashara waliopo eneo hilo.
Justine Khalifani, anayefanya biashara ya chips na peremende katika ufukwe huo, alisema Septemba, mwaka huu ilionekana maiti ikiwa imenasa kwenye mawe ya pembezoni mwa bahari.
Khalifani alisema maiti hiyo ilionekana saa tisa mchana ikiwa imevishwa mfuko wa plastiki kichwani na kufungwa shingoni, huku miguu na mikono nayo ikiwa imefungwa.
Alisema polisi walifika eneo hilo mara moja na kuichukua.
Katika Ufukwe wa Coco, mwandishi alizungumza na wafanyabiashara ambao baadhi walidai kuona maiti tatu na wengine tano.
Mmoja wa wafanyabiashara katika eneo hilo, Hassan Haruna, alisema kati ya Agosti na Septemba, mwaka huu ziliokotwa maiti tatu kwa nyakati tofauti katika ufukwe huo.
Haruna alisema miili yote ilikutwa imewekwa katika mifuko ya sandarusi na imefungwa miguu, kiuno na mikono.
Naye Mathius Tumesana, maarufu kwa jina la Baharia, alisema mwili wa kwanza ulionekana eneo hilo karibu na sehemu wanakouza mihogo.
Alisema baada ya kuonekana, walitoa taarifa kwa Jeshi la Polisi na askari walifika kuuchukua mwili huo.
“Mimi nilipiga mbizi kwenda kuuchukua mwili, nilipewa glovu na askari nikaenda kuuchukua, maiti hiyo ilikuwa haijaharibika sana, ila tayari macho yalikuwa yamenyofoka na ilikuwa imefungwa kwa pamoja miguu na mikono kwa nyuma kisha wakamwingiza katika mfuko mkubwa wa sandarusi,” alisema.
Tumesana alisema baada ya wiki tatu, ilionekana miili mingine miwili katika eneo hilo hilo, ikiwa imefungwa katika mifuko ya sandarusi na mwishoni mwa Septemba, mwaka huu ulionekana mwili mwingine ukiwa umefungwa kwa mtindo huo huo.
Mwenyekiti wa Kikundi cha Wafanyabiashara wa Ufukwe wa Coco, Abdallah Hassani, alisema matukio hayo ameyasikia, lakini hajaziona maiti hizo kwa sababu hakuwapo katika eneo lake la biashara kwa muda mrefu.

Safari ya Mbudya
Uchunguzi wa gazeti hili ulikwenda mbali zaidi kwa kutembelea Kisiwa cha Mbudya kunakodaiwa kuonekana maiti kadhaa.
Nahodha wa boti ndogo, Hassan Ramadhan, anayesafirisha watalii kwenda Mbudya na Bongoyo, alisema katika ufukwe huo kuelekea eneo la White Sand, zilionekana maiti mbili zilizofungwa katika mifuko ya sandarusi.
“Ukiacha tukio hilo, siku moja jioni nilikuwa nafuata watalii katika Kisiwa cha Bongoyo nikitokea Mbudya, hapo katikati niliona maiti nne zikielea, huku zikiwa zimevishwa mifuko ya sandarusi miguuni na kufungwa kwa kamba.
“Nilipata hofu sana na ilikuwa inasukumwa na mawimbi kuelelea Ufukwe wa Kawe.
Kutoka Mbundya hadi Bongoyo ni takribani kilomita nne, hapo kuna uwazi mkubwa kutoka eneo lenye kina kirefu cha bahari na ukidadisi vizuri simulizi za wavuvi, miili mingi inaonekana katika eneo hilo kwa nyuma, ambako kuna mkondo mkubwa wa bahari na mawimbi yana nguvu sana,” alisema Ramadhani.
Mwandishi wa habari hii alipanda boti na kuelekea Mbudya ambako alifanikiwa kumhoji Ofisa Utalii na Uwekezaji wa Idara ya Hifadhi za Bahari na Maeneo Tengefu, Hussein Ngenje, aliyesema hana cha kuongea kuhusu suala hilo.
Alipoulizwa kama ana taarifa yoyote alijibu: “No coment.” Kisha alimtaka mwandishi akamuulize Mwenyekiti wa Mbudya, Khamis Azizi.
Alipoulizwa Azizi kama ana taarifa zozote juu ya kuonekana kwa maiti iliyofungwa katika sandarusi, alisema hawezi kuongelea jambo hilo hadi apewe ruhusa maalumu kutoka mamlaka za juu.
Alipoulizwa mamlaka za juu ni zipi, alisema ni Wizara ya Mifugo na Uvuvi kupitia Idara ya Hifadhi za Bahari na Maeneo Tengefu.
Alipofuatwa Meneja wa Idara ya Hifadhi za Bahari na Maeneo Tengefu zilizopo Upanga, Dar es Salaam, Dk. Milali Machumu, alikiri kupata taarifa mara mbili kuhusu maiti hizo na alizifikisha kwa Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam kwa utaratibu wa kuziopoa.
Alipoulizwa idadi ya maiti zilizookotwa, alisema hafahamu kwa sababu jambo la msingi kwake alitoa taarifa kwa Jeshi la Polisi kwa hatua za uopoaji.
“Sina ufafanuzi zaidi kwa kuwa lengo letu la msingi ni utalii, nadhani naomba nikomee hapo, ila taarifa nilipewa na mimi nikazifikisha katika ngazi husika ya usalama wa raia,” alisema Dk. Machumu.
Septemba 26, mwaka huu, Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa, alitoa taarifa ya matukio ya kuonekana maiti zilizowekwa katika mifuko ya sandarusi na kutupwa baharini.
Alisema kutokana na matukio hayo, jeshi hilo kwa kushirikiana na askari wa majini, wanaendelea na uchunguzi dhidi ya matukio ya mauaji yanayoendelea kutokea katika baadhi ya maeneo na kisha miili kutupwa.
Pia alisema matukio hayo yanaonekana kudhamiriwa na watu wanaoyafanya kwa sababu miili yote inakutwa imefungwa kamba.
“Jeshi la Polisi tunaendelea na ufuatiliaji tukishirikiana na askari wa majini, kwa sababu matukio haya yanatokea huko, kama kanda tunaendelea na uchunguzi wa hali ya juu na hawa wauaji wanakuwa wanadhamiria kabisa kufanya hivyo. Ni vifo vya shaka kwa kweli, yote inakutwa imefungwa, hii inamaanisha huyo mtu anadhamiria,” alisema Mambosasa.
Alisema miili mingine iliyookotwa katika Ufukwe wa Msasani haikujulikana ni kina nani na hakukuwa na mtu aliyekwenda kuripoti kupotelewa na ndugu yake, hivyo waliikabidhi Manispaa ya Kinondoni kuizika.

Upinzani Kenya sasa watishia kumuapisha Odinga kama rais

Raila Odinga
Baadhi wa viongozi wa muungano wa upinzani, NASA, walisema Jumamosi kwamba iwapo rais Uhuru Kenyatta atalishwa kiapo kwa muhula wa pili baada ya uchaguzi wa marudio uliozua utata, basi watamwapisha kiongozi wao, Raila Odinga kama rais.
Wakizungumza katika eneo la Mavoko kaunti ya Machakos, wanasiasa hao, wakingozwa na wakili wa muungano huo na seneta wa kaunti ya Siaya, James Orengo, walisema kuwa watafanya uchaguzi mwingine chini ya kipindi cha siku 90.
Aliyekuwa seneta wa Machakos, Johnston Muthama, alisema muungano huo uko tayari kumuapisha kiongozi wao.
" Wakimuapisha Uhuru, nasi tutamuapisha Raila," Muthama aliuambia umati wa watu uliokusanyika mjini Mavoko.
"Uchaguzi huru na wa haki ni lazima ufanyike ndani ya siku tisini," Orengo alisema.
Haya yalijiri huku tume ya uchaguzi na mipaka, IEBC, ikiendelea kujumulisha kura katika kituo cha kitaifa cha Bomas of Kenya.
Odinga alikiambia kituo cha televisheni cha CNN katika mahojiano ya moja kwa moja Ijumaa kwamba ni Wakenya milioni 3.5 tu ambao walitokea kupiga kura siku ya Alhamisi.
Hata hivyo, naibu wa rais na mgombea mwenza wa Uhuru Kenyatta, William Ruto, alikanusha vikali matamshi hayo ya Raila katika mahojiano na kituo hicho hicho siku ya Jumamosi.
"Raila anasema uongo. Ukweli wa mambo ni kwamba wapiga kura milioni 7.5 walijitokeza kwa zoezi hilo," Ruto alisema.
Kufikia Jumapili asubuhi, IEBC haikuwa imetoa idadi rasmi ya watu wote waliopiga kura.

PITIA VICHWA VYA HABARI KATIKA MAGAZETI YA LEO OKTOBA 29,2017

Mvua kubwa kuendelea kunyesha Tanzania - TMA


Mvua kubwa zanyesha Dar es Salaam, Mkoa wa Pwani
WAKATI mvua kubwa iliyonyesha jijini Dar es Salaam na mkoani Pwani, Tanzania tayari imesababisha maafa makubwa, Mamlaka ya Hali ya Hewa (TMA) inasema kuwa mvua kubwa nyingine zinatarajiwa kunyesha katika maeneo mbalimbali ya Kanda ya Ziwa na Magharibi.
Taarifa za TMA zimesema kuwa Mvua kubwa zinatarajiwa Jumamosi na Jumapili katika baadhi ya maeneo ya ukanda wa Ziwa Victoria na Magharibi ya nchi.
Taarifa ya Mamlaka hiyo iliyotolewa ilisema kuwa vipindi vya mvua kubwa inayozidi milimeta 50 ndani ya saa 24, vinatarajiwa katika baadhi ya maeneo ya ukanda wa Ziwa Victoria na Magharibi mwa nchi.
Ilisema kuwa baadhi ya maeneo ya mikoa ya Mara, Mwanza, Simiyu, Shinyanga, Geita, Kagera, Tabora, Katavi na Rukwa itakumbwa na mvua kubwa na kwamba hali hiyo inatokana na kuimarika kwa ukanda wa mvua katika maeneo hayo.
Kwa mujibu wa vyanzo vya habari nchini Tanzania watu watatu walipoteza maisha kutokana na mvua zinazoendelea jijini Dar es Salaam, huku nyumba 100 zikisombwa na maji na nyingine 700 kuendelea kuzingirwa na maji.
Aidha watu wengine wawili walipoteza maisha katika mvua zilizonyesha juzi mkoani Pwani, ambapo miili yao iliopolewa baada ya maji kupungua kwenye Mto Mpiji unaozigawanya mikoa ya Pwani na Dar es Salaam.