Tuesday, October 3

ALIYEMTUSI RAIS MAGUFULI MTANDAONI AHUKUMIWA KWENDA JELA MIEZI 12 AU KULIPA FAINI YA MILIONI TANO


Na Karama Kenyunko, blogu ya jamii.
MHASIBU wa Shule ya Sekondari ya St Joseph Cathedral, Elizabeth Asenga leo amehukumiwa kulipa faini ya Sh Milioni tano au kwenda jela miezi 12 baada  ya kukutwa na hatia ya kutumia lugha ya matusi dhidi ya Rais Dk, John Magufuli.
 
Mhasibu huyo anadaiwa kumuita Rais Magufuli  kilaza kupitia mtandao wa WhatsApp.

Akisoma hukumu hiyo Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi amesema mshtakiwa amepatikana na hatia baada ya kuridhika na ushahidi uliowasilishwa mahakamani hapo na pande wa Jamuhuri kwa kuleta mashahidi saba na kumuona mshitakiwa  ana hatia.

"Upande wa mashtaka umeweza kuthibitisha pasipo kuacha shaka kuwa mshtakiwa umetenda kosa hivyo mahakama  inakutia hatiani kwa makosa uliyoshitakiwa nayo" 

Akimsomea adhabu yake amesema "utatakiwa kulipa  faini ya Sh Milion tano au kutumikia kifungo cha miezi 12 jela," alisema Hakimu Shaidi. 

Kabla ya kutolewa adhabu, mshitakiwa aliomba mahakama impunguzie adhabu kwa kuwa mama yake mzazi ni mzee anamtegemea na ana watoto wanaomtegemea.

Hata hivyo, mshtakiwa amelipa faini na amefanikiwa kukwepa kwenda jela

Katika kesi ya msingi, inadaiwa   Agosti 6, mwaka jana mshtakiwa huuo aliwasilisha maneno kinyume cha sheria kupitia mtandao wa WhatsApp katika group la wafanyakazi la STJ kwa nia ya kumtusi Rais.

Mshtakiwa alinukuliwa kuwa "Habari za asubuhi humu hakuna rais kilaza kama huyu wetu duniani angalia anavyompa Lissu umashuhuri,  fala yule picha yake ukiweka ofisini  nuksi tupu ukiamka asubuhi ukikutana na picha yake kwanza siku inakua ya mkosi mwanzo mwisho." 

MAKAMU WA RAIS SAMIA SULUHU HASSAN UZINDUZI WA MAKUMBUSHO MPYA YA OLDUVAI - NGORONGORO

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan akikata utepe kuashiria uzinduzi wa Makumbusho mapya ya mambo ya kale katika bonde la Olduvai ndani ya hifadhi ya Ngorongoro, wengine pichani  ni Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Profesa Jumanne Maghembe (kushoto) pamoja na Mkuu wa mkoa wa Arusha Mhe. Mrisho Gambo (kulia). ( Picha na Ofisi ya Makamu wa Rais)
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan akipiga makofi pamoja na Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Profesa Jumanne Maghembe (kushoto) pamoja na Mkuu wa mkoa wa Arusha Mhe. Mrisho Gambo (kulia) mara baada ya kukata utepe kuashiria uzinduzi wa Makumbusho mapya ya mambo ya kale katika bonde la Olduvai ndani ya hifadhi ya Ngorongoro. 
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan akipata maelezo mbali mbali kuhusu maisha ya binadamu na wanyama wa kale kutoka kwa Mhifadhi wa Mambo ya Kale kutoka Makumbusho ya Taifa Dkt. Agness Gidna mara baada ya kufungua Makumbusho mapya ya mambo ya kale katika bonde la Olduvai ndani ya hifadhi ya Ngorongoro. 
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan akiangalia historia kuhusu maisha ya binadamu na wanyama wa kale iliyopo kwenye Makumbusho ya Olduvai mara baada ya kufungua Makumbusho mapya ya mambo ya kale katika bonde la Olduvai ndani ya hifadhi ya Ngorongoro.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan akiangalia uzinduzi wa tovuti na mtanzao wa bure wa Hifadhi ya Ngorongoro mara baada ya kufungua Makumbusho mapya ya mambo ya kale katika bonde la Olduvai ndani ya hifadhi ya Ngorongoro.
:Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan akihutubia mara baada ya kufungua kufungua Makumbusho mapya ya mambo ya kale katika bonde la Olduvai ndani ya hifadhi ya Ngorongoro. (Picha na Ofisi ya Makamu wa Rais)

RAIS DKT MAGUFULI AFUNGUA MKUTANO MKUU WA 33 WA JUMUIYA YA TAWALA ZA MITAA TANZANIA (ALAT) JIJINI DAR ES SALAAM LEO

Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Mhe. Paul Makonda akiongea machache wakati wa kuanza kwa hafla ya ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa 33 wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT) katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere jijini Dar es salaam leo.
Mwenyekiti wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT) Bw. Gulma Hafeez Muccadam akisoma risala yao mbele ya Rais Dkt magufuli wakati wa kuanza kwa hafla ya ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa 33 wa katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere jijini Dar es salaam leo.
Naibu Waziri wa Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Mhe. Suleiman Jaffo mbele ya Rais Dkt magufuli wakati wa kuanza kwa hafla ya ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa 33 wa katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere jijini Dar es salaam leo.
Waziri Mkuu Mhe Kassim majaliwa akimkaribisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli kufungua wa Mkutano Mkuu wa 33 wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT) katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere jijini Dar es salaam leo.




Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli akifungua wa Mkutano Mkuu wa 33 wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT) katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere jijini Dar es salaam leo.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli na meza kuu wakipata picha ya kumbukumbu na wadau wa maendeleo na wafadhili wakuu wa Mkutano Mkuu wa 33 wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT) baada ya kuufungua katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere jijini Dar es salaam leo.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli akipeana mikono na Mkurugenzi Mtendaji wa benki ya NMB Bi. Ineke Bussemaker baada ya kufungua Mkutano Mkuu wa 33 wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT) katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere jijini Dar es salaam leo.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli akiagana na Makamu Mwenyekiti wa ALAT Bw. Stephen Mhapa baada ya kufungua Mkutano Mkuu wa 33 wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT) katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere jijini Dar es salaam leo.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli akiagana na Mstahiki Meya wa Dar es salaam Mhe. Isaya Mwita Baada ya kufungua Mkutano Mkuu wa 33 wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT) katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere jijini Dar es salaam leo.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli akifurahia ngoma ya Kigogo wakati akiwasili kufungua Mkutano Mkuu wa 33 wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT) katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere jijini Dar es salaam leo.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli akitembelea banda la benki ya NMB na mabanda mengine kabla ya kufungua wa Mkutano Mkuu wa 33 wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT) katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere jijini Dar es salaam leo. PICHA NA IKULU.

PICHA ZA UNYANYASAJI WA KINGONO ZATAKIWA KUTOLEWA TAARIFA ZIWEZE KUONDOLEWA -TCRA

Taasisi ya kutetea watoto ya C-SEMA kwa kushirikiana na Mamlaka ya Mawasiliano nchini wamefungua dirisha 'portal' kwa ajili ya picha zinazohusu matukio ya watoto,  zenye maudhui ya unyanyasaji wa kingono kwa watoto,  kuondolewa katika mitandao ya kijamii.

Akizungumza katika ufunguzi wa dirisha, Meneja Huduma wa Simu ya Mtoto , Thelma Dhase amesema kuwa picha za matukio za ukatili wa watoto hazitakiwi kuendelea kusambaa katika mitandao.

Amesema kuwa mfumo huo umeanza nchini lakini mradi huo unafanywa duniani nchi 18, ambapo kwa Afrika Tanzania ni ya Nne kuwa na mpango huo katika kutoa taarifa za picha za unyanyasaji wa kingono katika mitandao.

Dhase amesema kuwa mradi huo utasaidia kuongeza usalama wa watutmiaji wa mitandao kuhakikisha watoto waliothirika na picha za unyanyasaji wa kingono hawapitii unyanyasaji zaidi katika mitandao ya kijamii.

Kwa upande wa Kaimu Meneja wa Mawasiliano wa Mamlaka ya Mawasiliano nchini, Semu Mwakyanjala amesema picha za watoto zinaonesha ukatili au udhalilishaji wa watoto, hazitakiwi kusambazwa katika mitandao ya kijamii na mtu akipata picha hizo anatakiwa kutoa taarifa ziweze kutolewa katika mitandao.

Mwakyanjala amesema picha zinazodhalilisha watoto hazitakiwi kutokana na picha hizo zitaawathiri kisaikolojia wakishakuwa watu wazima.

Mradi wa kutolea taarifa za unyanyasaji wa kingono kwa watoto unaendeshwa na Internet Watch Foundation ambao unatekelezwa nchi 18 duniani.

.Kaimu Meneja wa Mawasiliano wa Mamlaka ya Mawasiliano nchini (TCRA), Semu Mwakyanjala akizungumza na waandishi wa habari katika ufunguzi wa watumiaji wa mitandao kutoa taarifa juu ya picha za unyanyasaji wa kingono kwa watoto iliyofanyika leo jijini Dar es Salaam.
Meneja wa huduma wa simu ya mtoto wa C-SEMA, Thelma Dhase akizungumza juu utoaji wa taarifa zinazohusiana na picha za unyanyasaji wa kingono kwa watoto kuweza kuondolewa katika kulinda watoto wengine leo jijini Dar es Salaam.
Sehemu ya waandushi wa wakiwa wadau katika ulinzi wa watoto katika kutoa taarifa za picha za unaynyasaji wa kingono kwa watoto leo jijini Dar es Salaam.
Kaimu Meneja wa Mawasiliano wa Mamlaka ya Mawasiliano nchini, Semu Mwakyanjala akiwa katika picha ya pamoja na Taasisi ya C-CEMA.

SEMINA KWA MAFUNDI UMEME WA MIKOA YA TANGA, ARUSHA, MANYARA NA KILIMANJARO KUHUSU KANUNI MPYA ZA EWURA ZA UFUNGAJI UMEME



STARS WAJICHIMBIA NJE YA MJI KUJIANDAA NA WAMALAWI JUMAMOSI UWANJA WA UHURU


TIMU ya Taifa Tanzania Taifa Stars wameingia kambini jana kwa ajili ya kujiandaa na mchezo wa kirafiki dhidi ya Malawi unaotarajiwa kufanyika siku ya Jumamosi kuanzia saa 10 alasiri katika dimba la Uhuru.
 
Stars inakutana na Malawi ikiwa ni mara ya pili kwa mwaka baada ya kuvaana nao June 25 mwaka huu katika michuano ya COSAFA yaliyofanyika nchini Afrika Kusini na kufanikiwa kupata wa ushindi wa goli 2-0. 

Timu hiyo chini ya Salum Mayanga inafanya mazoezi katika Uwanja wa Boko Veterani nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam na tayari Nahodha wa Taifa Stars, Mbwana Ally Samatta tayari ametua nchini kuungana na nyota wengine wa Tanzania katika mazoezi ya pamoja. 

Kocha Mayanga mapema wiki iliyoisha aliita kikosi kitakachounda Taifa Stars kwa ajili ya kuvaana na Malawi siku ya Jumamosi na akiwajumuisha nyota mbalimbali na akimrudisha Ibrahim Ajib baada ya kutokumuita kwa muda mrefu sambamba na golikipa Peter Manyika. 

Mayanga aliteuliwa Januari 4, mwaka huu ameita nyota watano wanacheza soka nje ya mipaka ya Tanzania akiwamo nahodha wa kikosi hicho, Mbwana Ally Samatta.

Kikosi hicho kina makipa Aishi Manula (Simba SC), Ramadhani Kabwili (Yanga) na Peter Manyika (Singida United).Mabekii ni Gardiel Michael (Yanga), Boniphace Maganga (Mbao FC), Abdi Banda (Baroka FC/Afrika Kusini), Kelvin Yondani (Yanga), Salim Mbonde (Simba SC), Erasto Nyoni (Simba SC) na Adeyum Ahmed (Kagera Sugar). 

Viungo ni Himid Mao ambaye pia ni Nahodha Msaidizi (Azam FC), Hamisi Abdallah (Sony Sugar/Kenya), Muzamil Yassin (Simba SC), Raphael Daud (Yanga), Simon Msuva (Difaa El Jadidah/Morocco), Shiza Kichuya (Simba SC), Abdul Hilal (Tusker/Kenya) na Morel Orgenes (FC Famalicao/Ureno). 

Washambuliaji ni Mbwana Samatta (KRC Genk/Ubelgiji), Ibrahim Hajib (Yanga) na Mbaraka Yussuph (Azam FC). 

Benchi la Ufundi la Mayanga linaundwa na yeye mwenyewe ambaye ni Kocha Mkuu, Fulgence Novatus (Kocha Msaidizi), Ame Ninje (Kocha Msaidizi), Patrick Mwangata (Kocha wa Makipa), Danny Msangi (Meneja), Dkt. Richard Yomba (Daktari wa timu), Dkt. Gilbert Kigadye (Daktari wa Viungo) na Ally Ruvu (Mtunza Vifaa). 

Shirkisho la mpira wa miguu nchini wamewataka watanzania kwa ujumla kujitokeza kwa wingi kuja kuishangilia timu ya Taifa kwa kujenga dhana ya mchezaji wa 12 uwanjani wakati wale 11 akiwamo Msuva, Ajib, Mbaraka wakileta faraja ya mabao.

Rais Uhuru amtuma Ruto kumwakilisha kwenye Tume ya Uchaguzi


Rais Uhuru Kenyatta amemtuma Makamu wa Rais William Ruto kuhudhuria kikao kilichoitishwa naTume ya Taifa ya Uchaguzi (IEBC) licha ya maelekezo yaliyotaka wagombea urais kufika wenyewe.
Mwishoni mwa wiki iliyopita, Mwenyekiti wa IEBC Wafula Chebukati alisema wagombea urais watapaswa kuhudhuria wao wenyewe badala ya kuwatuma wawakilishi wao.
Ruto amewasili kwenye jengo la Bomas of Kenya, Nairobi saa 10:15 alasiri akiwa pamoja nakiongozi wa wabunge wengi Seneta Kipchumba Murkomen (Elgeyo Marakwet) na Aden Duale (Garissa Mjini).
Waliwasili muda mfupi baada ya viongozi wa muungano wa upinzani wa Nasa wakiongozwa na Raila Odinga kumaliza kikao chao. Raila aliongozana na mgombea mwenza wake Kalonzo Musyoka, seneta wa Bungoma Moses Wetang'ula (Ford Kenya), Musalia Mudavadi (ANC) na wa Siaya, James Orengo.
Orengo amewaambia waandishi wa habari kwamba kikao hicho hakikuwa na matunda yoyote akasema kitakuwepo kikao kingine siku zijazo.
Orengo alisema IEBC imewapa maelezo ya nini wanachofanya na siyo wanachotarajia kufanya ili kurekebisha makossa yaliyojitokeza katika uchaguzi wa Agosti 8 uliosababisha matokeo ya urais kufutwa.
"Lazima ufanyike ukaguzi kuhakikisha usalama na kuaminika kwa teknlojia itakayotumika. There should be an audit to ensure security and integrity of the technology to be deployed. IEBC haiku wazi katika hili," alisema.
Mazungumzo kama haya yalivurugika Jumatano iliyopita baada ya wawakilishi wa Nasa kutoka nje wakidai Jubilee hawakuwa na nia njema. Orengo alisema hiyo ilitokana na mapendekezo ya marekebisho ya sheria.

Makocha walia upendeleo Mwanza


Huenda waamuzi wanaochezesha mechi kwenye Uwanja wa Nyamagana siyo wazalendo kutokana na lawama wanazopewa na makocha wa timu ngeni.
Jana,  Jumatatu, mechi kati ya Pamba FC ya jijini Mwanza na Biashara ya mkoani Mara ilimalizika kwa suluhu, lakini bado kocha wa Biashara alishusha mvua ya lawama kwa waamuzi wa mchezo huo.
Kocha msaidizi wa Biashara FC, Amani Josiah, alimtupia lawana mwamuzi wa mchezo huo huku akitolea mfano baadhi ya nafasi na makosa yaliyopuzwa wakati wa pambano.
“Mchezo umekuwa ni mgumu sana, vijana wangu wamejituma kadri wawezavyo lakini mwamuzi wa leo amewanyima ushindi ambao ulikuwa wa wazi kabisa. Kipenga cha mwamuzi huyu kimekolea sana kwa upande wetu. Hata mngewasikiliza mashabiki wa Pamba wenyewe walikuwa wanamshabikia mwamuzi badala ya mchezo,” alisema Josiah.
Hata hivyo alishukuru kwa kupata pointi muhimu ugenini na pia kufahamisha kwamba hiyo ndio historia ya mpira wa miguu na zaidi ya yote akaridhia matokeo.
Kocha wa Pamba, Mathias Wandiba alisema wapinzani wao walikuwa na ‘rafu’ nyingi na ndio maana mwamuzi akawa anajaribu kutenda haki.
Aidha matokeo hayo yalimsikitisha kocha huyo kwani hakutarajia kutoka sare ya 0-0 akiwa nyumbani ingawa mpira wa miguu hautabiriki hadi kipenga cha mwisho.
Awali kwenye mchezo wa Trans Camp na Toto Africans uliopigwa uwanjani hapo juma lililopita, kocha mkuu wa Trans Camp, Nevelin Kanza alimlaumu mwamuzi wa mchezo huo kwamba alikuwa na mapendeleo ya wazi. Shirikisho la mpira wa miguu nchini liliangalie hili.
“Kiukweli mwamuzi ametumaliza kabisa. Imetulazimu kunyamaza ili kuheshimu sheria za soka lakini amekuwa kikwazo,” alisema kocha Kanza.
Kwenye mchezo huo, Toto Africans walipata ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Trans Camp uwanjani Nyamagana.

Tahadhari yatolewa kwa Watanzania juu ya ugonjwa wa tauni

Wizara ya Afya imetoa tahadhari kuhusu kuwepo ugonjwa wa tauni katika nchi ya Madagascar ulioibuka Agosti.
Imeelezwa kuwa, kati ya wagonjwa 104 walioripotiwa, 20 wamefariki dunia.
Taarifa iliyotolewa leo Jumanne na Ofisa Habari wa wizara hiyo, Catherine Sungura imesema Shirika la Afya Duniani (WHO) limeeleza nchini Madagascar mikoa minane  imeripoti kuwepo wagonjwa ukiwemo mji mkuu wa nchi hiyo, Antananarivo.
Ugonjwa huo ulianza kuripotiwa Agosti 23 hadi Septemba 28.
“Wengi walioripotiwa wameonyesha kuwa na uhusiano kwa njia moja au nyingine na mgonjwa wa kwanza jambo linalothibitisha yapo maambukizi ya ugonjwa wa tauni kati ya binadamu na binadamu. Hivyo, kwa mujibu wa WHO, ipo hatari ya wastani (moderate risk) ya ugonjwa huo kusambaa katika nchi jirani na Madagascar,” imesema taarifa hiyo.
Wizara imesema tahadhari hiyo inatolewa kwa kuzingatia kwamba, Madagascar haiko mbali sana na Tanzania na inawezekana kukawa na mwingiliano kati ya wananchi wa nchi hizi mbili.
“Serikali inasisitiza kuwa mpaka sasa ugonjwa wa tauni haujaingia nchini. Kwa kuwa magonjwa hayaangalii mipaka, tunahitaji kuchukua tahadhari madhubuti ili kuzuia ugonjwa huu usiingie nchini. Hivyo, wananchi wanahimizwa kuzingatia kanuni za afya za kuzuia ugonjwa huu, pia wanatakiwa kuripoti haraka kwenye vituo vya huduma za afya waonapo dalili zozote za ugonjwa huu,” imesema wizara.
Sungura amesema hatua zilizochukuliwa baada ya kupata taarifa ya tahadhari ya WHO Septemba 29 ni kusambaza barua za tahadhari ya ugonjwa huo kwa makatibu tawala wa mikoa yote ya Tanzania Bara.
Makatibu tawala katika barua hizo wametakiwa kuchukua tahadhari ikiwa ni pamoja na kuimarisha ufuatiliaji wa ugonjwa katika viwanja vya ndege, mipakani na bandari ili kubaini wagonjwa waingiao nchini wakiwa na dalili za ugonjwa huo.
“Kupitia kwa waganga wakuu wa mikoa na wilaya, wizara inatoa maelekezo ya kuimarisha mfumo wa ufuatiliaji na utambuzi wa magonjwa katika vituo vya kutolea huduma,” amesema.
Pia, wizara itatoa elimu kwa jamii kuhusu ugonjwa huo.

Kuhusu tauni
Ugonjwa huu husababishwa na bakteria anayejulikana kitaalamu “Yersinia pestis” ambaye hupatikana katika baadhi ya wanyama wadogo kama vile panya, paka, mbwa na viroboto.
Taarifa hiyo imezitaja njia kuu tatu ambazo mtu anaweza kupata maambukizi kuwa ni kung’atwa na viroboto vyenye maambukizi ya bakteria hao kutoka kwa wanyama kama vile mbwa na paka ambao huweza kubeba viroboto.
“Kugusana bila kuwa na kinga mwili na majimaji yenye vimelea vya bakteria kutoka kwa mtu/mnyama aliyeathirika kwa njia ya kugusa sehemu zenye vimelea zilizochafuliwa na mgonjwa/mnyama na kisha mtu huyo kujigusa mdomoni au puani,” imesema taarifa hiyo.
Njia nyingine ni kugusana na majimaji yanayotoka kwa mgonjwa kwa njia ya kukohoa au kupiga chafya bila ya mgonjwa kufunika pua au mdomo.

Aliyemimina risasi kwenye tamasha ni mfuasi wa IS



Kundi la Islamic State (IS) limeripoti katika mtandao wake wa propaganda wa Amaq kwamba linahusika na shambulio jijini Las Vegas, Marekani lililogharimu maisha ya watu 59 na wengine 527 kujeruhiwa.
Hata hivyo makachero wa Marekani wametupilia mbali madai hayo na wanaendelea na uchunguzi kubaini lengo la shambulio hilo lililofanywa dhidi ya watu waliokuwa wakishiriki tamasha la muziki kwenye eneo la wazi.
Maofisa waandamizi wa serikali ya Marekani wamesema hakukuwa na kitu chochote chenye uhusiano kati ya mshambuliaji wa Las Vegas na kundi lolote la kigaidi. Vilevile shirika la upelelezi la FBI limethibitisha kwa upande wake kwamba hakuna ‘mpaka sasa’ uhusiano na kundi la kijihadi
Pamoja na FBI kukanusha, mtandao huo wa IS umesema mshambuliaji huyo ni mfuasi wao ambaye ‘abadili dini kuwa mwislamu miezi michache iliyopita’. Amaq limemtaja Paddock kuwa mpiganaji wake mpya aliyepewa jina la kivita la ‘Abu Abd el-Bir al-Amriki’.
Polisi wamethibitisha kwamba baada ya Paddock kutekeleza shambulizi hilo alijiua kabla ya polisi kumkaribia.
Polisi walipofanya ukaguzi wa kina nyumbani kwake karibu na Mesquite, Nevada walikuta bunduki 19, vilipuzi, maelfu ya risasi na vifaa vya kielektroniki.
Pia, katika chumba cha hoteli ya Mandalay Bay Resort and Casino ambamo Paddock alikuwa anaishi, polisi walikuta silaha 23, zikiwemo ‘handgun’ moja na ‘rifles’. Polisi walikuta ndani ya gari lake kilo kadhaa za ‘ammonium nitrate’ dawa inayotumika kutengenezea milipuko.

Mbunge ataka mahakama imzuie Raila kususia uchaguzi


Nairobi, Kenya. Mbunge wa Jimbo la Pokot Kusini David Pkosing amefungua kesi Mahakama Kuu akitaka itoa amri ya kumshinikiza mgombea urais kupitia muungano wa National Super Alliance (Nasa) Raila Odinga kushiriki uchaguzi wa marudioOktoba 26 bila kukosa.
Katika kesi hiyo Pkosing anamtaka Raila atekeleze uamuzi wa Mahakama ya Juu iliyoamuru uchaguzi wa marudio na kwamba vitisho vya kutaka kususia uchaguzi huo ikiwa masharti kadhaa hayajatimizwa ni ukiukwaji wa sheria.
Kupitia kwa wakili wake Kibe Mungai, mbunge huyo amesema ikiwa Raila na mgombea mwenza wake Kalonzo Musyoka watajitoa utatokea mgogoro wa kikatiba ambao unaweza kuitumbukiza nchi katika sintofahamu.
Mbunge huyo anataka mahakama itoe amri kwamba hatua ya Odinga, Musyoka au kiongozi yeyote wa Nasa kutoshiriki uchaguzi wa marudio ni kitendo cha uhaini na lazima wawajibike.
Katika hatua nyingine, Nasa wamemtaka Mkurugenzi Mkuu wa Mashtaka (DPP) katika muda was aa 72 kumfungulia mashtaka wakala wa chama cha Jubilee Davies Chirchir baada ya kumtuhumu kwa makossa kadhaa yanayohusiana na uchaguzi.
Kupitia kwa mwanasheria wake Anthony Oluoch, Nasa imemlalamikia kwa makossa manne Chirchir, ambaye alikuwa wakala mkuu wa Uhuru Kenyatta katika kituo cha kujumlishia matokeo ya Bomas of Kenya.
Vilevile, Muungano huo wa Nasa unataka wafanyakazi sita wa kampuni ya Safaricom wanaodaiwa kuwa waliingilia uchaguzi wa rais wa Agosti 8 washtakiwe.
Muungano huo umesema kwamba ikiwa DPP Keriako Tobiko atashindwa kuchukua hatua katika muda wa saa 72, wataandaa mashtaka kivyao dhidi ya Chirchir kwa kuzingatia kifungu cha 28 cha Sheria ya Ofisi ya DPP ambayo inaruhusu watu binafsi kuendesha mashtaka.
Alipoulizwa Chirchir kuhusu tuhuma anazorushiwa na Nasa alisema hakutenda kosa lolote kwani Tume ya Taifa ya Uchaguzi (IEBC) ilimpa haki ya uwakala kama mawakala wengine. “Ikiwa wanataka kumshtaki basi wafanye hivyo hata kwa mawakala wao,” amesema Chirchir.
Hii itakuwa mara ya pili Nasa wanampa DPP sharti la kuwafungulia mashtaka watu binafsi inaodai waliingilia uchaguzi wa Agosti 8 ambao ulifutwa na Mahakama ya Juu. Mara ya kwanza ilikuwa Septemba 22 Nasa walimpompa Tobiko saa 72 kuwashtaki maofisa wa IEBC iliodai walivuruga uchaguzi huo.

Wanaharakati wakataa msaada wa mke wa Mugabe



Mke wa Rais Mugabe, Grace Mugabe
Mke wa Rais Mugabe, Grace Mugabe 
Harare, Zimbabwe. Mke wa Rais Mugabe, Grace Mugabe ameshutumiwa na wataalamu wa afya na wanaharakati baada ya kudaiwa kutoa msaada wa nguo za ndani zilizotumika kwa wanachama wa Zanu-PF mjini Mutare.
Kwa mujibu wa gazeti la NewsDay, msaada huo ulikabidhiwa kwa wafuasi hao na mfanyabiashara mashuhuri na Mbunge wa Chikanga –Dangamvura, Esau Mupfumi aliyedai umetolewa na mke wa rais.
"Hivi karibuni nilikwenda Ikulu ambako nilikutana na Grace Mugabe na alinikabidhi nguo hizi ili niwapatieni. Ninazo hapa na nimeambiwa zenu haziko katika hali nzuri kwa hiyo tafadhali njooni mchukue leo. Kuna nguo za kulalia, ndala na nguo, njoni mchukue, hizi zinatoka kwa Grace Mugabe," gazeti lilimnukuu Mupfumi akisema.
Kadhalika ripoti ilimnukuu mnufaika mmoja wa chupi hizo ambaye hakutaka jina lake litajwe akimlaumu Grace kwa kuwapatia kama msaada badala ya kutengeneza ajira ili kumaliza tatizo la ukosefu wa kazi katika nchi hiyo ya kusini mwa Afrika.
"Haya ndiyo masuala yanayohitaji kuzungumziwa badala ya kutupatia nguo ya ndani. Hatuna kazi na kwa nini ametufanyia hivi?" alihoji mwanaharakati wa Zanu-PF.
Ripoti zilizotolewa na shirika la kazi la Zimbabwe Congress of Trade Unions ukosefu wa kazi nchini ni zaidi ya asilimia 85, ingawa shirika la takwimu la serikali linasema ukosefu wa kazi ni asilimia 11 tu.

Mwalimu Nyerere watafuta mgeni rasmi mwingine

Mkuu wa chuo cha MNMA, Profesa Shadrack
Mkuu wa chuo cha MNMA, Profesa Shadrack Mwalalila 
Dar es Salaam. Baada ya Rais John Magufuli kueleza hatahudhuria kongamano la kumbukizi ya Mwalimu Nyerere, uongozi wa Chuo Kikuu cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere (MNMA) unatafuta mgeni rasmi mwingine atakayelifungua.
Chuo hicho ambacho kimeandaa kongamano hilo kimekuwa kikitangaza kwenye vyombo vya habari na kwenye mitandao ya kijamii kwamba kongamano hilo litafunguliwa na Rais Magufuli Oktoba 11.
Hata hivyo, Oktoba Mosi, Ikulu ilitoa taarifa kwamba Rais Magufuli hatahudhuria kongamano hilo kwa sababu ana majukumu mengine kulingana na ratiba yake ya kazi.
Ikulu ilielekeza taasisi za umma na zisizo za umma zinazomualika Rais katika shughuli zao kutotangaza ushiriki wake hadi zipate uthibitisho kuwa atahudhuria.
Akizungumza leo Jumanne, Mkuu wa chuo cha MNMA, Profesa Shadrack Mwalalila amesema bado hawajapata mgeni rasmi atakayefungua kongamano hilo.
“Bado hatujapata mgeni rasmi lakini kesho  tunaweza kumpata na tutawatangazia,” amesema.
Kwa mujibu wa tangazo la chuo hicho, mada kuu ya kongamano hilo ni mtazamo wa Mwalimu Nyerere katika uchumi wa viwanda na maendeleo ya jamii.
Watoa mada ni Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere (MNF), Joseph Butiku ambaye atatoa mada kuhusu uongozi bora katika ustawi wa uchumi wa viwanda.
Mada nyingine itatolewa na Msajili wa Hazina, Dk Oswald Mashindano kuhusu fursa na changamoto katika ustawi wa uchumi wa viwanda.
Nyingine itatolewa na Samuel Kisori kuhusu uadilifu na utaifa katika ustawi wa uchumi wa viwanda.
Kongamano hilo litafanyika ikiwa ni maadhimisho ya Siku ya Mwalimu Nyerere ambayo kitaifa huadhimishwa Oktoba 14 ya kila mwaka.

Bodi ya mishahara yapewa vigezo 10 vya utendaji kazi

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais  Menejimenti ya

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais  Menejimenti ya umma na utawala bora Angela Kairuki akizungumza Leo jijinj Dar es Salaam, wakati wa uzinduzi wa bodi ya pili ya mishahara ya maslahi kwa utumishi wa umma. 
Dar es Salaam. Serikali imetoa vigezo 10 vya utendaji kwa bodi ya mishahara na masilahi katika utumishi wa umma (PSRB), inavyotakiwa kuvizingatia katika utekelezaji wa majukumu yake.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa bodi ya pili inayoundwa na watu saba, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Angellah Kairuki amesema katika kutekeleza majukumu yake, bodi hiyo ni muhimu kuvizingatia vigezo hivyo.
Kairuki amesema licha ya vigezo kuwa vingi, ni muhimu kuzingatia malipo ya mshahara na masilahi kwa watumishi wa umma yanapatikana na kuwa endelevu.
Vigezo vingine ni utumishi wa umma kuvutia na kubakiza taaluma zinazohitajika katika kuendesha shughuli zake; utendaji wenye tija unatambuliwa; uwazi, usawa na haki zinazingatiwa.
Pia, kuhakikisha malipo yanayostahili, yanayolipika na endelevu yanatolewa kwa ngazi zote katika utumishi wa umma ili kuvutia na kubakiza vipaji maalumu nchini.
Kairuki amesema vigezo vingine ni matakwa ya mlipa kodi na umma kwa jumla yanapewa kipaumbele dhidi ya masuala mengine wakati wa kubuni na kuendesha vyombo vya masilahi.
Vigezo vingine amesema ni kuepuka upendeleo katika kupanga masilahi kwenye utumishi wa umma na aina yoyote ya ushawishi wa kisiasa katika uamuzi unaohusu mishahara na masilahi.
“Uamuzi au ushauri kuhusu mishahara na masilahi uzingatie hali ya soko la ndani na kikanda, pia viwango vya malipo kisekta visitofautiane sana isipokuwa kwa kuruhusu tofauti kutegemeana na aina ya kazi na majukumu,” amesema Kairuki.
Amesema sekta ya utumishi wa umma ina changamoto nyingi mojawapo ikiwa ni kuboresha masilahi ya watumishi ili kuongeza tija katika utendaji kazi.
“Ni dhahiri Serikali haiwezi kufanya uamuzi sahihi bila ushauri wa kitaalamu unaotokana na utafiti kuhusu kuboresha masilahi ya watumishi wa umma na hiyo ndiyo kazi yenu,” amesema.
Wajumbe wa bodi hiyo ni Mwenyekiti Donald Ndagula, ambaye ni Kamishna wa Uhamiaji mstaafu na makamu wake ni Balozi Charles Mutalemwa ambaye ni katibu mkuu mstaafu.
Wajumbe wa bodi hiyo ni George Mlawa ambaye ni Katibu wa Bunge mstaafu; Gaudentia Kabaka, waziri mstaafu; Jaji mstaafu Regina Rweyemamu; Meja Jenerali mstaafu Zawadi Madawili na Kamishna Mwandamizi wa Polisi mstaafu Jamal Rwambow.