Friday, October 9

Estomih Mallah wa ACT Wazalendo afariki dunia


By Louis Kolumbia, Mwananchi Digital
Dar es Salaam. Mgombea ubunge wa ACT-Wazalendo katika jimbo la Arusha Mjini Estomih Mallah amefariki dunia usiku wa kuamkia leo huko KCMC, Moshi alikohamishiwa jana kwa matibabu zaidi.
Makamu Mwenyekiti wa ACT-Wazalendo, Shaaban Mambo amethibitisha kutokea kwa kifo hicho na kusema alipigiwa simu alfajiri leo na mtoto wa kiume wa marehemu kumweleza kuwa baba yao alikuwa amefariki dunia.
Taarifa za awali zinasema kuwa marehemu alianza kuugua Jumanne baada ya mkutano uliohutubiwa na mgombea urais wa chama hicho, Anna Mghwira uliofanyika eneo la Ngaramtoni.
Mambo aliiambia Mwananchi Digital kuwa marehemu alipelekwa hospitali ya Mtakatifu Thomas iliyopo jijini Arusha alikolazwa hadi jana alipohamishiwa KCMC kwa matibabu zaidi ambako mauti yamemkuta.
Mambo alisema chama chake kimeshaanza vikao kujadili taratibu za mazishi na kwamba taarifa zaidi zitatolewa baada ya kujadiliana na familia.
Alisema Mallah aliyehudumu pia kama Mwenyekiti wa Kamati ya Uchumi ameacha pengo kubwa kutokana na nafasi yake iliyomfanya awe katika utendaji wa shughuli za kila siku za chama hicho.
Mwaka 2010 aligombea na kushinda nafasi ya udiwani katika kata ya Kimandolu kupitia Chadema na baadaye kuchaguliwa Naibu Meya wa Halmashauri ya Jiji la Arusha katika uchaguzi uliozua mgogoro baina ya CCM na Chadema.
Mwaka 2011 Mallah na madiwani wengine watatu (John Bayo (Elerai), Reuben Ngowi (Themi) na Charles Mpanda (Kaloleni) walivuliwa uanachama wa Chadema katika kile kilichoonekana kushamiri kwa mgogoro wa kisiasa ndani ya chama hususani katika kuwania nafasi ya umeya wa halmashauri ya jiji hilo.
Baadaye alitua ACT-Wazalendo ambako alipitishwa na chama hicho kuwania ubunge wa Arusha Mjini katika uchaguzi wa Oktoba 25 mwaka huu akipambana na mbunge anayetetea kiti chake, Godbless Lema wa Chadema na Philemon Mollel wa CCM.

‘Obama siyo rais mweusi kamili Marekani’



Washington, Marekani. Mmoja ya watu wanajulikana kwa utajiri mkubwa wa vyombo vya habari duniani amesema kuwa Marekani haijapata rais anayewakilisha uhalisia wa kweli juu ya jamii ya watu weusi.
Tajiri huyo Rupert Murdoch aliandika ujumbe katika akaunti yake ya Twitter akisema kuwa Rais Barack Obama siyo ‘rais mweusi kamili’.
Tajiri huyo hakuishia hapo bali alikwenda mbali zaidi kumsifia mmoja wa wanaotaka kuwania nafasi ya urais katika uchaguzi ujao kupitia chama cha Republican.
Alimmwagia sifa mgombea Ben Carson akisema kuwa :”Ben na Candy Carson wazuri sana. Itakuwaje tukiwa na rais mweusi kamili atakayeangazia kikamilifu masuala ya rangi? Na mengine mengi”.
Alipendekeza pia watu wasome makala iliyo kwenye jarida la New York Magazine inayozungumzia “kutamanishwa kwa makundi ya wachache” na uongozi wa Rais Obama.
Murdoch mwenye umri wa miaka 84, ndiye mwanzilishi wa himaya ya mashirika ya habari ya News Corporation iliyokita mizizi maeneo mengi duniani.
Kampuni yake inamiliki Fox News Channel, The New York Post na The Wall Street Journal nchini Marekani na magazeti ya Times nchini Uingereza.
Hivyo ni baadhi tu ya vyombo vya habari anavyomiliki tajiri huyo mkubwa duniani.
Yeye ameorodheshwa kuwa miongoni mwa watu wenye ushawishi zaidi duniani.
Mgombea huyo wa urais mwenye umri wa miaka 63 ni mtaalamu wa upasuaji wa mfumo wa neva na mmoja wa wagombea 15 wanaopigania tiketi ya chama cha Republican kuwana urais wa Marekani 2016.
Siku chache zilizopita, aliandika kwenye Twitter: “Kotekote, wadadisi wa masuala ya kisiasa wanamtambua Ben Carson. Lakini umma unafahamu na kupendezwa na upole na unyenyekevu.”
Hata hivyo, Rais Obama, katika uongozi wake, amekuwa mwangalifu kuhusu masuala ya ubaguzi wa rangi na asili.
Carson aliibua utata mwezi uliopita baada ya kusema kuwa Mwislamu hafai kuwania urais Marekani kwa vile Uislamu unakinzana na katiba ya Marekani.

Mtikila azikwa Ludewa


Njombe. Mwili wa aliyekuwa Mwenyekiti wa DP, Mchungaji Christopher Mtikila umezikwa jana katika Kijiji na Kata ya Milo, Wilaya ya Ludewa mkoani Njombe.
Katika mazishi hayo yaliyoshuhudiwa na Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi, ndugu, jamaa na marafiki, waombolezaji walimzungumzia Mchungaji Mtikila wakisema Taifa limempoteza mtu aliyekuwa mstari wa mbele katika harakati za kutetea masilahi ya Taifa.
Jaji Mtungi alisema Mtikila atakumbukwa kwa mambo mengi aliyoyafanya katika Taifa, kwani ni mtu aliyekuwa anapambana kusimamia kitu anachokisimamia.
Alisema marehemu hakuwa mtu wa kupenda njia za mkato kupata kitu, ndiyo maana alikuwa tayari kufungua kesi kuona matokeo ya kitu anachokisimamia.
Alisema Mtikila alikuwa anatetea haki na pia alikuwa anatetea amani ya nchi, jambo linalopaswa kuigwa na kila Mtanzania.
Dada wa marehemu Veronica Mtikila, alisema familia ilikuwa inamtegemea kama alivyokuwa akitegemewa katika kupigania masilahi maskini na wanyonge.
“Kifo hiki kimetushtua sana, alitusaidia kama familia... lakini tunamwachia Mungu,” alisema Veronica.
Marafiki waliosoma pamoja na Mtikila wanaoishi katika Kijiji cha Milo, Noel Haule na Peter Msigwa walisema tangu akiwa shuleni, marehemu alifahamika kutokana na misimamo na harakati zake za kutetea wenzake.
Walisema hata alipokuwa mwanasiasa na mwanaharakati, hawakushangaa kutokana na misimamo yake tangu akiwa mdogo.
“Alikuwa na ushawishi mkubwa tangu akiwa mdogo, alikuwa anaweza kushawishi wengine na wakamwelewa, lakini zaidi alikuwa anapenda kutetea haki,” alisema Msigwa na kuongeza: “Taifa limepoteza mtu muhimu ambaye alikuwa anaikumbusha Serikali kurekebisha mambo pale ilipokuwa inakwenda kinyume.”
Mtikila alifariki dunia Oktoba 4, katika ajali ya gari iliyotokea katika Kijiji cha Msolwa, Chalinze mkoani Pwani alipokuwa akitokea Njombe kwenda Dar es Salaam.
MUNGU AMUWEKE MAHALA ANAPOSTAHILI. AMEN