Friday, December 6

HISTORIA FUPI YA MAISHA YA NELSON MANDELA



Taarifa ya kifo cha Mzee Nelson Mandela imetangazwa na rais wa Afrika Kusini Jacob Zuma saa saba kasoro usiku wa kuamkia Dec 6 2013 ambapo amefariki akiwa na miaka 95.

Akiutangazia Umma wa wakazi wa Afrika ya kusini hapo jana Rais wa Nchi hiyo bwana Jacob Zuma alisema maneno yafuatayo:
 
"Our nation has lost its greatest son, yet what made Nelson Mandela great was precisely what made him human,"

"We saw in him what we seek in ourselves, and in him we saw so much of ourselves."

Bwana Nelson Mandela alikuwa akisumbuliwa mara  na maradhi mbali mbali ikiwemo figo na viungo vingine vya mwili kufikia hali ya kushindwa kufanya kazi, hali iliyomlazimu kupuma kwa kutumia mashine maalum,

Nelson Mandela atakumbukwa kwa Juhudi zake katika kuleta Ukombozi Barani Afrika na bado anabaki kama Alama ya Ushindi kwa Bara hilo huku Akiwaachia Simanzi kubwa Wakazi wa Nchi Hiyo ambao Mpaka sasa wanaonesha kutoamiani kilichotokea.

HISTORIA FUPI YA MANDELA.

Nelson Rolihlahla Mandela ni Rais wa kwanza Mwafrika wa Afrika Kusini ya kidemokrasia. Ni mtu aliyejijengea heshima kubwa duniani kutokana na jitihada zake kubwa zilizofanikisha uhuru wa nchi hiyo na nyinginezo katika Bara la Afrika.

Mzee Mandela anayefahamika pia kwa jina la Mzee Madiba amelazwa hospitalini mjini Pretoria, Afrika Kusini kwa zaidi ya mwezi sasa akiwa mahututi. Anasumbuliwa na ugonjwa wa mapafu.

Kutokana na umaarufu wa Rais huyo mstaafu wa Afrika Kusini mwenye umri wa miaka 95, JAMHURI tumeona vema kuchapisha historia fupi ya maisha yake kama ifuatavyo:

Nelson Mandela ni mwanasiasa mkongwe na mwanaharakati aliyepambana na sera za ubaguzi za makaburu wa Afrika Kusini na hatimaye kuwa Rais wa kwanza Mwafrika nchini humo. Ni mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel. Pia amepata kutunukiwa zaidi ya tuzo 250 katika miongo minne iliyopita.

Ni rais wa kwanza aliyechaguliwa kidemokrasia nchini Afrika Kusini. Alikuwa mwanasheria na mwanachama wa Chama cha African National Congress (ANC) aliyepinga utawala wa ubaguzi wa rangi Afrika Kusini.

Nelson Mandela alizaliwa Julai 18, 1918. Baba yake mzazi alifariki wakati Mandela akiwa na umri wa miaka tisa. Tangu kipindi hicho alilelewa na Jonintaba hadi alipoitoroka familia hiyo baada ya kutakiwa aoe mwanamke aliyepangiwa.

Mwaka 1943 Mandela alijiunga ANC. Aliiongoza Afrika ya Kusini dhidi ya ubaguzi wa rangi na kuibuka kiongozi shujaa duniani.

Alipoanza mapambano ya kupinga utawala wa ubaguzi wa rangi na kutafuta usawa kwa wote, ilitegemewa kuwa mke wake ndiye angekuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha mambo yanakwenda sawa.

Mandela alipata kuoa wake watatu katika historia ya maisha yake. Alimuoa mke wa mwisho siku alipokuwa akiadhimisha miaka 80 ya kuzaliwa kwake.

Madiba anatajwa kuwa katika kipindi chote cha historia yake amekuwa akiwaunga mkono watoto na upatikanaji wa elimu. Mfuko wa Nelson Mandela wa kusaidia watoto ni sehemu tu ya ushahidi wa mafanikio ya Mandela kuwasaidia watoto.

Mandela ni baba wa watoto sita. Watoto wanne aliwazaa na mke wake wa kwanza, Evelyn Mase na watoto wawili aliwazaa na mke wake wa pili, Winnie Madikizela.

Inaelezwa kuwa baadhi ya watoto wake hawakupata kwenda kumwona Madela alipokuwa gerezani.

Watoto wake wote wawili wa kike aliowazaa na mke wa kwanza walikuwa wakitumia jina la Makazawie.

Mtoto wake wa kwanza alifariki akiwa na umri wa miezi tisa na mtoto wa pili aliyejulikana kwa jina la Madiba Thembikile (Thembi) alifariki katika ajali ya gari mwaka 1969 akiwa na umri wa miaka 25. Mandela alikuwa gerezani na hakuruhusiwa kwenda kuhudhuria mazishi ya mwanaye.

Mtoto mwingine, Makgatho alifariki kwa ugonjwa wa Ukimwi mwaka 2005. Mandela amekuwa mstari wa mbele kupiga vita virus vya Ukimwi na Ukimwi akitumia namba 46664 ambayo ni namba yake alipokuwa gerezani kupiga kampeni.

Mandela na Evelyn walidumu katika ndoa yao kwa miaka 13 kabla haijavunjika mwaka 1957. Evelyn alikuwa muumini wa dhehebu la Mashahidi wa Yehova lililokuwa haliruhusu waumini wake kushiriki kwenye siasa, hivyo muda wote hakujihusisha na siasa. Alifariki mwaka 2004.

Mandela alimuoa Winnie Madikizela mwaka 1958, ingawa muda mwingi hawakuishi pamoja kwa sababu alikuwa kifungoni huku Winnie akijijengea umaarufu katika majukwaa ya siasa.

Kutokana na misuguano iliyoibuka ndani ya umaarufu wa kisiasa ya Mandela na Winnie walijikuta wakipeana talaka mwaka 1994. Mwaka 1998 Mandela alimuoa Graca Machel ambaye alikuwa mke wa kwanza wa Rais wa Msumbiji, Samora Machel.

Rais wa sasa wa Afrika Kusini, Jacob Zuma, ameendelea kutoa wito kwa wananchi wa nchi hiyo wamwombee heri wakati huu anapougua. Maombi yamekuwa yakifanywa makanisani kote nchini Afrika Kusini kumwombea Mandela apone maradhi yanayomsumbua.

Hata hivyo, Mandela ameshaandika wosia wake na kuelekeza kwamba kama atakufa azikwe kwenye milima iliyojitenga nyumbani kwa mababu zake huko Qunu, Afrika Kusini.

Mandela alikuwa Rais wa Afrika Kusini kuanzia mwaka 1994 hadi 1999. Alifungwa jela miaka 27 kuanzia mwaka 1962 hadi mwaka 1990. Anaelezwa kuwa alikumbwa na ugonjwa wa mapafu alipokuwa akifanyishwa kazi ngumu katika machimbo ya mawe akiwa gerezani.

Mpekuzi Tunaungana na Wananchi wa Afrika ya Kusini Wengine wote duniani wenye Mapenzi mema kwa kuomboleza Msiba huu Mzito wa kuondokewa na Kipenzi chetu mzee NELSON MANDELA

Mungu Ailaze mahala Pema Peponi Roho ya Marehemu, Amina 

RAIS KIKWETE ATANGAZA SIKU 3 ZA MAOMBOLEZO KITAIFA, BENDERA KUPEPEA NUSU MLINGOTI


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Rais wa Jamhuri Ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amemtumia Salamu za rambirambi Rais Jacob Zuma wa Afrika ya Kusini  na kupitia kwake, kwa mkewe Bi. Graca Machel, wanafamilia wote na wananchi wote wa Afrika ya Kusini kufuatia kifo cha Mzee Nelson Mandela kilichotokea  tarehe 5 Desemba, 2013 baada ya kuugua kwa muda mrefu.

Rais ameuelezea msiba huu kuwa ni msiba mkubwa kwetu sote.


"Afrika ya Kusini, Afrika na dunia kwa ujumla imepoteza mtu mashuhuri na shujaa mkubwa wa Karne ya 20 na 21.Tunaelewa  machungu waliyonayo wananchi wa Afrika ya Kusini kwa kupoteza kiongozi shupavu, jasiri, mwana mapinduzi , mvumilivu na mstahimilivu". Ameongeza Rais Kikwete.

Rais amemuelezea  Mzee Mandela kuwa ni  kielelezo cha aina yake kwa wanadamu kwa moyo wake wa kusamehe, huruma na upendo uliomuwezesha  kuwaunganisha wananchi wa Afrika ya Kusini kuwa  taifa moja baada ya kipindi kirefu cha mapambano dhidi ya ubaguzi wa rangi.


"Mandela  ni mfano bora kwa wanadamu wa  jinsi binadamu muungwana anavyopaswa kuwa . Ni wajibu wa wana Afrika Kusini, Afrika na dunia kwa jumla kuiga mfano wake hasa moyo wake wa uzalendo, kujitolea hata maisha yake kwa ajili yake na wananchi wenzake"
.Rais ameongeza kusema, "Tuzidi kumuombea kwa Mwenyezi Mungu ailaze roho ya Marehemu Mzee Mandela  mahali pema peponi".

Kufuatia kifo hicho Rais ametangaza siku 3 za maombolezo kuanzia leo tarehe 6 hadi 8 Disemba, 2013.

Aidha, Mheshimiwa Rais ameagiza  kuwa katika siku hizo 3 bendera zote zipepee  nusu mlingoti.

Mwisho.