Thursday, November 23

Kutoeleweka tozo bandarini maduka yafungwa Kariakoo


Wafanyabiashara wa Soko la Kimataifa la Kariakoo wamelalamikia gharama za uondoshaji mzigo bandarini kudumaza ufanisi wa shughuli zao.
Katibu wa Jumuiya ya Wafanyabiashara Kariakoo (JWK), Abdallah Mwinyi amesema soko hilo liko mbioni kupotea endapo jitihada za kulinusuru hazitafanyika.
Alisema hilo linatokana na changamoto wanazokutana nazo Bandari ya Dar es Salaam ambako kuna mlolongo mrefu wa kukamilisha taratibu za kuondosha mzigo unaoingizwa na kuwapo kwa makadirio makubwa ya tozo zinazotakiwa kulipwa jambo linalowakatisha tamaa.
“Mtu unaambiwa utoe Sh60 milioni kutoa kontena moja la bidhaa. Fikiria ukiwa na makontena saba utayatoa kwa kiasi gani na bei uliyoambiwa sasa haitakuwa sawa na utakapoingiza mgizo mwingine hapo baadaye,” alisema Mwinyi.
Mwinyi alisema mzigo wa aina moja unaoingizwa na watu wawili tofauti bandarini hapo hutozwa kiasi kisicholingana. Wapo wanaopata unafuu wakati wengine wanaumia.
Kuepuka ubaguzi huo wa tozo kwa mizigo inayoingi, alisema walipendekeza kuwapo kwa bei elekezi ya utoaji makontena kulingana na bidhaa kurahisisha tathmini lakini utaratibu huo ulitumika kwa muda mfupi kabla ya kuondolewa na mambo yakaendelea kuendeshwa kwa mazoea.
“Ilitolewa kwa sababu hakuna pesa iliyokuwa inaenda mfukoni kwa mtu bali serikalini na kukosekana kwa bei elekezi ni kuruhusu mianya ya rushwa,” alisema Mwinyi.
Kutokana na utaratibu huo usiotenda haki kwa walipakodi hao, alisema biashara imepungua kwa kiasi kikubwa sokoni hapo kwani wafanyabiashara wengi wmeshindwa kuendelea na shughuli zao hivyo kurudisha fremu walizopanga na kuwalazimu wamiliki kubadilisha matumizi ya nyumba zao kuendelea kujiingizia kipato cha kujikimu.
Hali hiyo, alisema inasababisha baadhi ya wafanyabiashara kutoka nchi jirani kuanza kulikimbia soko hilo kutokana na kupungukiwa bidhaa tofauti na ilivyokuwa zamani.
“Wateja waliokuwa wanakuja kutoka nje siku hizi wamepungua, wananunua bidhaa zao Kenya na Uganda ambako bei ni nafuu kuliko sisi,” alisema Mwinyi.
Alisema hali Kufa kwa soko hili hakutawaathiri wafanyabiashara peke yake lakini pia mapato ya Tanzania kwa sababu karibu robo tatu ya mapato yote kila mwezi yanatoka hapa,” alisema Mwinyi.
Alisema madhara ya kudhorota kwa mwenendo wa biashara katika soko hilo ambako kumesababisha maduka kadhaa kufungwa kutokana na uchumi wa wafanyabiashara wengi kuyumba yataenda mbali zaidi ya jamii hiyo.
“Zamani mtu alikuwa anaweza kutafuta fremu ya biashara hata mwaka mzima na asipate, kuna watu walikuwa na stoo mpaka sita lakini hivi sasa wamezirudisha na kubaki na moja. Wenye fremu moja wanahifadhi na mzigo humohumo dukani,” alisema Mwinyi.
Kudhihirisha mabadiliko yaliyopo, alisema kwa sasa mtu anayehitaji hata fremu 15 kwa ajili ya kufungua maduka 15 au stoo 30 anazipata bila hata kutumia dalali. “Nyumba zipo tu. Madalali wa vyumba hawana kazi sasa hivi. Wenye nyumba wenyewe ndio wanapangisha sasa,” alisema.
Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wafanyabiashara Tanzania (JWT), Johnson Minja alisema malalamiko ya wafanyabiashara wanaoingiza mzigo kupitia Bandara ya Dar es Salaam ni ya nchi nzima na kwamba juhudi za kuzishawishi mamlaka husika kuondoa kero hiyo ni endelevu.
“Wengi wanalalamika. Tunaendelea kupiga kelele ili uwepo mfumo wa wazi kwa wote utakaomruhusu mfanyabiashara kufahamu kiasi atakacholipa mzigo wake ukiwasili,” alisema.

Kwa nini utalii unahamia kwenye vivutio vya asili?


Kuna kila dalili kwamba, utalii duniani unahamia kwa kasi kwenye vivutio vya utamaduni na vile vya zamani vinavyofahamika pia kwa jina la malikale.
Utafiti uliofanywa na Umoja na Mataifa kupitia Shirika la Elimu, Sayansi na Utamaduni (Unesco) miaka 12 iliyopita ulionyesha utalii wa utamaduni unaohusisha vivutio vya asili ulikuwa umeanza kushika kasi duniani.
Katika utafiti huo, Unesco ilieleza utalii wa aina hiyo unaotokana na vivutio vya asili kuwa ndio unaoelekea kuteka soko la sekta hiyo duniani.
Shirika hilo katika utafiti wake liliainisha sababu mbili kubwa za watu kuanza kupenda utalii wa aina hiyo.
Mosi, lilitaja sababu ya watu wengi duniani kuanza kumiliki wanyama katika makazi yao - sababu ambayo imewafanya wengi wao kutopenda kusafiri kwenda kuangalia wanyama, ilhali wanapatikana mahali walipo.
Kutokana na sababu hiyo, watu wanaopenda kusafiri kwa shughuli za utalii kufuata vivutio vya wanyama duniani walikuwa wameanza kupungua, lakini wengi wanaokwenda kutalii hufuata zaidi vivutio vya asili.
Unaweza kushangaa mbona unawaona watalii wengi wanakuja nchini na kutembelea maeneo ya hifadhi za Taifa. Jibu ni jepesi, nalo ni ukweli kwamba hifadhi nyingi zinatofautiana katika mambo mbalimbali ambayo pia ni vivutio kwa upande wake. Mathalan, Hifadhi ya Ruaha ndiyo kubwa kuliko zote, lakini ina wanyama wengi aina ya tembo, jamii ya miti na maua ambavyo havipatikani katika sehemu nyingine nchini na duniani kwa ujumla.
Vivyo hivyo ndivyo ilivyo Rubondo, uwapo wake kama kisiwa ndani ya ziwa unaifanya iwe na upekee ikiwa na ndege na pia huwavutia watalii kuitembelea kwa upekee wa utalii wa uvuvi.
Kuna Ngorongoro yenye eneo la kreta inayovutia kwa umbile lake la mfano wa sahani na uwapo wa idadi kubwa ya wanyama wanaoishi ndani ya ‘sahani’ hiyo, lakini pia namna wanavyoishi kwa kukwepana kati ya walao nyama na wanaoliwa ni aina ya kivutio cha pekee.
Ndivyo pia ilivyo kwa Serengeti ambako ni makazi ya nyumbu wanaohama nyakati fulani za mwaka na kuhamia Maasai Mara nchini Kenya wakifuatana katika mtitiriko unavyovutia macho kuwaangalia. Hivyo ndivyo ilivyo katika vivutio vya wanyama.
Sababu ya pili ni ukweli kwamba, utalii wa wanyama umezoweleka na umekuwapo duniani kwa miaka nenda rudi, hiyo ikiwa na maana kuwa karne nyingi zilizopita vivutio vya wanyama vilitumika kuwafanya watu kusafiri kwenda kuwaangalia mahali walikokuwa.
Licha ya hilo, katika dunia ya sasa watu wanafuga wanyama mbalimbali katika makazi yao wakiwa na hifadhi ndogo walizojianzishia na hilo linawafanya wawatumie kama vivutio vya utalii kwao na hata watu wanaohitaji kwenda kuwaangalia.
Utalii wa malikale, utamaduni
Utalii wa malikale na utamaduni unaingia katika kundi moja, lile ambalo uasili wa vitu unawekwa pamoja katika misingi ya utalii. Ndani ya malikale kuna vitu vilivyotumiwa zamani kama mikuki, mishale na mawe; mabaki ya viumbe vya kale kama wanyama, binadamu, ndege na mimea.
Ndani ya utamaduni kuna ngoma, majengo, minara (inayoonyesha utamaduni wa maeneo husika), mavazi, mapishi, chakula, lugha, heshima na mazungumzo. Pia kuna mambo ya utamaduni yanayoingia katika kundi hilo kama malezi, misiba, harusi, jando na unyago.
Katika mataifa yaliyoendelea, utalii wa utamaduni na malikale unapigiwa chapuo kuliko ule wa wanyama. Wanafanya hivyo pengine kutokana na kutokuwa na hifadhi nyingi kubwa zenye vivutio vingine ndani yake vinavyovutia watalii.
Ndiyo maana miji mikubwa katika Brussels (Ubelgiji), Paris (Ufaransa), London (Uingereza), Dublin (Ireland), Washington na New York (Marekani) imekuwa ikitengeneza vivutio binafsi ili kuwavutia watalii, lakini pia ina malikale nyingi ambazo zimehifadhiwa kwa miaka mingi.
Hizo ni pamoja na minara ya kumbukumbu, majengo ya zamani, maeneo ya kumbukumbu za vita, viwanja vya michezo na mazoezi, kumbi za burudani, maktaba kubwa zenye vitabu na machapisho ya karne, maumbile ya kuchora, nyumba walizoishi watu walioacha rekodi mbalimbali, picha, michoro na nyaraka za zamani.
Kwa mujibu wa sensa ya mwaka 2017, Ubelgiji yenye wakazi 11,303,528 ikiwa na pato la Dola 508.598 bilioni za Marekani (zaidi ya Sh1117.6 trilioni) kwa mwaka huku pato la mwananchi wa kawaida likiwa ni Dola 44,881 (zaidi ya Sh98.7 milioni, inategemea nusu ya pato lake litokane na utalii wa vivutio vya asili.
Nchi hiyo ina vituo vingi vya asili kuanzia maktaba kubwa, makumbusho na majengo ya zamani yanayovutia mamilioni ya watu kutoka mabara yote duniani kuitembelea. Ubelgiji haina hifadhi kubwa, mbali na ile maarufu ya Public Aquarium iliyopo katikati ya Jiji la Brussels.
Licha ya hifadhi hiyo ambayo haizidi kilomita 1.5 za mraba nyingine ni T’struisvogelnest (Lier), Bouillon Wildlife Park (Bouillon), Le Parc a Gibier (La Roche-en-Ardenne), La grange aux papillons (Chimay), Olmense Zoo (Olmen), Sea life (Blankenberge), De Zonnegloed Sanctuary (Vleteren), Serpentarium (Blankenberge), Bellewaerde (Ieper (Ypres) na Aquarium et Musee de Zoologie iliyopo Liege.
Kwa pamoja, maeneo hayo madogo ya kuhifadhi wanyama na mimea yaliyotengenezwa yanaiingizia nchi hiyo pato lisilozidi Dola 17 milioni za Marekani (zaidi ya Sh37.4 bilioni) kwa mwaka.
Fursa kwa Tanzania
Nchi nyingi zilizoendelea zimefanikiwa kuutuza utalii wa malikale kuliko ule wa utamaduni. Utamaduni katika mataifa mengi hasa yaliyoendelea umekufa na nyingi ya nchi hizo zinaigana katika mambo mengi kama vile mavazi na chakula.
Ndiyo maana katika utalii wa vivutio vya asili bado nchi zinazoendelea ikiwamo Tanzania zinaweza kutumia fursa hiyo kuingiza mapato makubwa kuliko kutegemea hifadhi pekee.
Kwa Tanzania, utalii wa utamaduni uko zaidi katika maeneo ya vijijini ambako wananchi wengi wanaishi kiasili. Huko ndiko bado kuna ngoma za asili, vyakula na hata mavazi mfano mzuri ni Umasaini.
Pia, Tanzania ina malikale nyingi zilizotapakaa kila kona. Mifano ya malikale hizo ni magofu ya Bagamoyo; mabaki ya majengo ya biashara ya watumwa yaliyopo Kilwa Kisiwani, Kilwa Kivinje na Kilwa Masoko; eneo la historia ya binadamu wa kale la Oldupai; mahala yalipogunduliwa mabaki ya mjusi aliyeishi miaka 150 milioni Tendaguru mkoani Lindi; michoro ya mapangoni ya Amboni na Kondoa; makaburi ya Waarabu ya Bagamoyo na Kunduchi yaliyojengwa kati ya karne ya tisa hadi 11.
Maeneo mengine yanayoweza kuchangia katika uchumi wa nchi kupitia utalii iwapo yatatangazwa ipasavyo ni yale ya matambiko ya makabila mbalimbali yakiwamo mapango, mawe makubwa, miti na maporomoko ya maji.
Si hayo tu, kuna minara, makumbusho mbalimbali na maeneo ya kihistoria mathalan yaliyotumiwa na wapigania uhuru kufanyia harakati zao, makaburi na majengo waliyolala au kuishi wapigania uhuru wa nchi zao za kusini mwa Afrika.
Kwa ujumla yapo maeneo mengi ya kale yaliyobeba historia inayoweza kuchangia pato la Taifa kupitia utalii, lakini tatizo mengi hayafahamiki kwa wananchi na hayajaendelezwa kuwezesha utalii kufanyika.
Fursa kwa Tanzania inawezekana iwapo Serikali itayaendeleza maeneo hayo kwa kuyapa ‘uhai’ wa miundombinu yaweze kufikiwa, mkakati wa kuyatangaza na pia kuzijengea uwezo jamii zinazoishi jirani au maeneo husika namna zinavyoweza kutumia fursa kujikwamua kiuchumi.
Wadau, Serikali
Ofisa utalii wa kampuni ya All Safaris, Fidelis Olakamtwa anasema watalii wengi wanaowahudumia wanapenda kuangalia na kujifunza juu ya malikale na vivutio vya asili, lakini mara nyingi hupendelea vilivyopo Ngorongoro (NCAA) kwa kuwa tayari vimeendelezwa.
Anavitaja vivutio hivyo kuwa ninyayo za binadamu wa kale, eneo la mabaki ya binadamu wa kale na wanyama pamoja na mchanga unaohama kutoka sehemu moja hadi nyingine. “Huu ndio utalii unaowavutia, hata tunapojitangaza tunazingatia sana kutumia vivutio vya aina hiyo. Vingine ni kama Makumbusho ya Kalenga (Iringa), nyayo zile za zamadamu, pale Bagamoyo kuna vivutio vingi sana vya kihistoria na vya asili,” anasema.
Mhitimu wa stashahada ya malikale na utalii wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Ole Naikoli anaishauri Serikal kutangaza utalii kwa kuangalia zaidi vivutio vya asili na malikale zilizotapaa nchini.
“Tunaweza kuona havina maana kwetu, lakini vina mchango mkubwa sana katika pato endelevu kwenye uchumi wa nchi ikizingatiwa kwamba baada ya miaka michache ijayo ni watu wachache watakaokimbilia kushangaa wanyama hifadhini,” anasema.
Hivi karibuni naibu waziri wa Maliasi na Utalii, Japhet Hasunga akiwa mkoani Rukwa alisema Serikali imepanga kuendeleza utalii katika maeneo ya Kusini, lakini itajikita pia kuangalia namna ya kuviendeleza vivutio vya asili. Hasunga aliyasema hayo alipotembelea maporomoko ya Kalambo ambayo ni ya pili kwa kina kirefu barani Afrika ambayo yamekuwa hayatembelewi na watalii wengi kutokana na kutotangazwa ipasavyo.
Akizungumza hivi karibuni juu ya uendelezwaji wa eneo la Tendaguru lililopo mkoani Lindi mahala ambapo watafiti wa Ujerumani walifukua na kuondoka na mabaki ya mjusi wa kale maarufu dinosaria zaidi ya miaka 100 iliyopita, mkurugenzi wa utalii kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii, Deogratius Mdami alisema Serikali inafanyia kazi maeneo yote ambayo yanahitaji uendelezwaji kwa ajili ya kuja kuwa vivutio vya utalii.

Muswada mfuko mpya hifadhi ya jamii ulivyobeba mambo mazito


Serikali imewasilisha Mus-wada wa Sheria ya Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma 2017 ambao ukipitish-wa, wanachama wake wanaotaka kujitoa watakabiliwa na masharti makali huku ukiruhusu mtoto mle-mavu kuendelea kulipwa kwa mai-sha yake yote.
Pamoja na mapendekezo mengi yaliyomo, muswada huo umeweka masharti kwa kwa watumishi wanaostahili kulipwa kabla hawa-jatimiza umri wa kustaafu kwa mujibu wa sheria ambao ni miaka 55 kwa hiyari au 60 kwa lazima.Atakayetaka kujitoa, muswada unamtaka awe na “cheti cha dak-tari kwamba hawezi kuendele akutekeleza majukumu yake amba-cho mwajiri wake atakiridhia au ajira yake ikisitishwa kwa maslahi ya umma au muda wake wa uteuzi utakapokamilika.”Muswada unaongeza masharti kwamba, mwanachama yeyote atastahili mafao endapo atakuwa amechangia walau miaka 15 au jum-la ya miezi 180.Mfuko unawatambua watoto na mwenza wa kila mwanachama. Kwa uzito uliopo, unapendekeza kum-lipa mtoto mlemavu wa mwana-chama atakayepoteza maisha akiwa kazini kwa maisha yake yote yali-yobaki wakati ambao ni wazima, mpaka watakapotimiza miaka 21.Wakati mtoto ikipendekezwa apewe mafao hayo, mjane naye, kul-ingana na umri na watoto alioachi-wa, amezingatiwa. Kwa aliyeachwa na watoto wenye chini ya miaka 15 naye akiwa na zaidi au chini ya miaka 45, muswada unapendekeza alipwe mafao kwa maisha yake yote au mpaka atakapoolewa tena.Endapo mwanachama hakuacha mtoto wala mke, inapendekezwa: “Wazazi wake walipewe haki zote za mtoto wao.”
Kutekeleza mabadiliko hayo, muswada unapendekeza kuvunjwa kwa mifuko ya PPF, GEPF, LAPF na PSPF kasha kuanzisha Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) utakaorithi mali na madeni yote ya mifuko hiyo iliyopo sasa.
Itakapopitishwa, kutakuwa na kipindi cha mpito cha miezi sita kukamilisha hatua zote za kisheria zinazohitajika kabla utekelezaji wa majukumu ya mfuko huo mpya utakaokuwa na thamani ya Sh5 trilioni haujaanza.
Mabadiliko hayo yataiacha mifuko minne kutoka saba ya sasa ukiwamo Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), Mfuko wa Bima ya Afya ya Taifa (NHIF) na Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF). Wakati PSSSF ukiwahudumia watumishi wa umma, NSSF utakuwa kwa ajili ya sekta binafsi.
Kwenye makabidhiano yatakayofanywa, michango na wanachama wa NSSF ambao ni watumishi wa umma watahamishiwa PSSF wakati wale wa sekta binafsi kutoka huko watahamishiwa NSSF. Wafanyakazi wenye sifa wa mifuko itakayovunjwa wataajiriwa PSSSF itakayochukua madeni na mali za mifuko hiyo pia.
Utafiti wa ajira na kipato wa Ofisi ya Takwimu ya Taifa (NBS) mwaka 2015 unaonyesha kuna watumishi milioni 2.3 nchini ambao kati yao, milioni 1.6 wanatoka sekta binafsi na 700,000 ni wa umma.
Mfuko huo utatoa mafao manane ambayo ni la kustaafu, warithi, kujitoa, uzazi na kutokuwa na ajira. Mengine ni fao la ugonjwa, kifo na mzishi.
Sharti limewekwa kwamba: “Haitaruhusiwa kwa mwanachama kupewa mafao mawili kwa wakati mmoja.”
Wanachama
Muswada unapendekeza wanachama kuwa na uwezo wa kuchukua mkopo wa nyumba kwa dhaman ya michango yao waliyonayo kwenye mfuko huu mpya. Vilevile, wanaochangia kwa hiyari kwenye mifuko minne itakayofutwa watahamishiwa PSSSF.
Muswada unashauri, mafao ya mwanachama yanaweza yakatumika kulipa deni la serikali, mkopo wa nyumba au malezi na matunzo ya mtoto au mke aliyetelekezwa baada ya kujiridhisha kwa mamlaka husika.
Kukabiliana na ucheleweshaji wa malipo ya mafao kwa wastaafu, muswada unapendekeza itakapodhihirika kuwa ucheleweshaji huo haukuchangiwa na mtumishi husika basi mfuko umlipe mafao yake pamoja na riba ya asilimia tano ya thamani ya mafao yake kwa mwaka.
Suala la makosa yanayoweza kuhumiwa kifungo gerezani, muswada unapendekeza wategemezi wake; mke na watoto walipwe stahiki za mtumishi husika ili waweze kujikimu kwa muda ambao mwanachama huyo atakuwa anatumikia kifungo chake.
Kwa mwanachama atakayehukumiwa kifungo lakini hana wategemezi, pindi hukumu yake ikiisha, mfuko unawajibika kumlipa mafao yake yote anayostahili kwa muda aliochangia.
Ikitokea mfanyakazi wa umma amebadili mwajiri na kwenda sekta binafsi, uanachama wake utahamishiwa NSSF lakini michango yake itaendelea kubaki PSSSF na muda wa kustaafu utakapofika au sababu nyingine ya kulipwa mafao yake, ukokotozi wa pamoja utafanywa kati ya mifuko hiyo miwili.
Jambo jingine muhimu kwenye muswada huo ni madai yaliyotelekezwa. Inapendekezwa, mwanachama ambaye warithi wake hawatajitokeza kwa miaka mitatu mfululizo kufuatilia michango yake kutokana na kifo au sababunyingine yoyote, kiasi kilichopo kitahamishiwa kwenye akaunti maalumu ya serikali.
Na hali ikiendelea kuwa hivyo kwa miaka 10, akaunti ya mwanachama itafutwa na fedha zake kuhamishiwa serikalini.
Mali, madeni
Muswada unatambua watumishi wa mifuko inayotarajia kuunganishwa, mali za taasisi hizo, madeni pamoja na miradi mbalimbali. Muswada unapendekeza kwamba, mikataba yote iliyopo ambayo inaendele akutekelezwa kuhamishiwa PSSSF.
Uhamisho huo pia utahusisha mali na madeni yaliyopo bila kusahau miradi. Haya yote yanatakiw ayafanywe ndani ya miezi sita ambayo ni kipindi cha mpito kwa ajili ya makabidhiano.
Hesabu za fedha
Ndani ya miezi sita baada ya kukamilika kwa mwaka wa fedha, bodi ya wakurugenzi ya PSSSF italazimika kuandaa hesabu za fedha na ripoti yake kuiwasilisha kwa waziri mwenye dhamana ambaye atawajibika kupeleka nakala na kuisoma bungeni.
Bodi itatakiwa kutoa ripoti hizi kila mwaka ambazo zitajumuisha taarifa za mali na madeni, operesheni za mfuko, matumizi ya fedha za mfuko na taarifa nyingine yoyote ambayo waziri au mamlaka za juu zaidi zitahitaji.
Mkurugenzi wa Mamlaka ya Udhibiti wa Mifuko ya Jamii (SSRA), Irene Isaka anasema mapendekezo haya yamefanywa baada ya tathmini ya kina iliyozingatia mambo mengi yaliyoshauriwa na vyama vya wafanyakazi.
Kukamilisha mchakato huo, Isaka anasema tahadhari inachukuliwa kuhakikisha watumishi waliopo hawapotezi kazi zao. Kwa waliopo ngazi za ukurugenzi, alisema wanaweza kupangiwa majukumu mengine endapo itaonekana nafasi zao zimejaa kwenye mfumo huu mpya.
“Hii sekta bado inahitaji wafanyakazi wengi kukidhi mahitaji yaliyopo na yanayoongezeka kila siku. Hatma ya wafanyakazi waliopo kwenye mifuko inayounganishwa itafahamika baada ya muda mfupi,” anasema.
Kuhakikisha mambo yanaenda sawa, anasema Wizara ya Utumishi inashughulikia suala hilo hasa kwa kutambua kwamba baadhi ya mifuko ilikuwa na wafanyakazi wengi kuliko mahitaji ilhali mingine ilikuwa nao wachache hivyo, kama watakuwapo watakaopoteza nafasi zao, hawatokuwa wengi.
Licha ya mustakabali wa watumishi waliopo, anasema wizara hiyo pia inaandaa mfumo sahihi utakaowahudumia waajiriwa waliopo sekta binafsi pamoja na wale wa sekta ya umma.
Mkurugenzi mtendaji wa taasisi ya HakiPension, Christian Gaya anasema muungano huo utakuwa mzuri endapo wananchi wengi zaidi watakuwa na nafasi ya kujiunga na huduma za hifadhi ya jamii na mmafao kutolewa kwa wakati. “Kwa sasa mafao ya wafanyakazi yanacheleweshwa ilhali kuna mifuko mingi yenye ushindani. Sijui itakuwa kutakapokuwa na mifuko miwili pekee,” anatia shaka Gaya.

Usipange kushindwa kwenye biashara uiwazayo



Ally  Mbuyu
Ally  Mbuyu 
Hakuna mtu anapanga kushindwa kwenye mradi anaouanzisha bali kupuuza misingi ya biashara ndiko husababisha anguko. Mjasiriamali ambaye kila wakati anafuata misingi na taratibu za biashara kwa maslahi ya biashara yake huepuka changamoto hii.
Mjasiriamali anayezingatia kanuni hulifahamu vyema soko la biashara yake. Huepuka kuanzisha biashara ambayo bidhaa zake hazina soko.
Kabla ya kuanza biashara, mjasiriamali makini anatakiwa afanye utafiti na kujiridhisha kama kuna soko la kutosha baada ya kutambua bidhaa inayohitajika.
Mjasiriamali huyu pia huepuka gharama kubwa za maisha yake binafsi. Kufanikiwa katika hili huhakikisha ana wafanyakazi wanaohitajika kutoa huduma za msingi kulingana na ukubwa wa biashara na kuzingatia maeneo mengine kama hayo.
Mjasiriamali makini hutangaza bishara yake. Hutengeneza nembo makini na imara sokoni. Wanaoshindwa kwenye kipengele hiki hukosa wateja na kumaanisha mwisho wa biashara. Hawa huanguka kwa sababu huridhika kwa kuwa na biashara bila kufanya matangazo makini.
Mteja ni mfalme. Ukishindwa kumthamini utampoteza. Kinachomtofautisha mjasiriamali makini na anayebahatisha ni umakini katika kipengele hiki. Wajasiriamali wengi hawana huduma nzuri kwa wateja wao hivyo kwa muda mfupi tu huanza kukimbiwa na kwenda kwa washindani wao.
Wanakokimbilia ndiko aliko mjasiriamali anayejua wajibu wake kwa wanaomuweka mjini. Huyu hawezi kufunga virago na kuhama mji. Ataendelea kuwepo huku akiongeza idadi ya wateja.
Biashara ni tofauti na mmiliki wake. Hii inamaanisha haina uhusiano wowote na familia au rafiki zako. Inapotokea mjasiriamali akaruhusu marafiki au familia yake kufanya maamuzi katika biashara husababisha iyumbe hata kufa kabisa.
Kufanikisha jambo lolote unahitaji elimu kulihusu. Kama ilivyo kwenye maeneo mengine, huwezi kuwa daktari kwa mfano bila kuwa taaluma hiyo. Mjasiriamali makini huhakikisha ana elimu ya kutosha kuendesha biashara yake kwa kutambua kwamba kutofanya hivyo husababisha kudorora sokoni.
Kila baada ya muda Fulani, mjasiriamali makini anatakiwa kuhudhuria mafuzo ili kukumbushwa misingi ya uendeshaji biashara na mbinu mpya za kuliteka soko zilizopo. Bahati mbaya wajasiriamali wengi wana dhana kuwa biashara haihitaji elimu, ni kuuza na kupata hela ndiyo maana biashara nyingi zinakufa jambo ambalo halitokei kwa wachache waliotulia.
Kuepuka pupa ni sifa nyingine ya mafanikio. unaweza kuwa na mawazo mengi ya kufanya biashara ingawa unatakiwa kulizingatia moja au machache ambayo una uwezo nayo kwa misingi ya elimu, usimamizi, uzoefu, masoko na fedha.
Hairuhusiwi kuvamia biashara nyingi kwa wakati mmoja wakati huna uwezo nazo kwani husababisha kuanguka kibiashara. Jambo hili huepukwa kwa umakini na mjasiriamali makini.
Kukosea maamuzi katika kuanzisha na kuendesha biashara ni sababu kubwa ya kushindwa sokoni. Walio makini huwa makini kuchagua biashara ya kuanzisha, huzingatia ubora wa wafanyakazi na bidhaa husika.
Wengi ambao biashara zao hishia njiani ni wale wanaoshindwa kutimiza ahadi. Kutumia nguvu nyingi kutangaza biashara kwa ahadi za uongo ambazo huzitekelezeki ni kujinyonga kibiashara. Wateja watakuwa na matarajio ya kupata ulicho ahidi na ukishindwa kutimiza matarajio yao watakimbia. Mjasiriamali makini huahidi vitu anavyoweza kuvitekeleza kwa ufanisi.
Kama kuna kitu kinapaswa kuepukwa basi ni kufanya kila kitu mwenyewe. Kumiliki biashara na mipango ya kupata faida hakumaanishi ufanye kila kitu mwenyewe kwani unahitaji wataalamu wengine kukusaidia.

Mgombea Chadema afutiwa kesi, akamatwa na polisi

Mgombea udiwani wa Kata ya Mhandu (Chadema),
Mgombea udiwani wa Kata ya Mhandu (Chadema), jijini Mwanza, Godfrey Misana. 
Mwanza. Mgombea udiwani wa Kata ya Mhandu (Chadema), jijini Mwanza, Godfrey Misana, meneja wake wa kampeni, Charles Chinchibela na wenzao wawili, wamejikuta wakiishia mikononi mwa polisi muda mfupi baada ya kufutiwa kesi ya kujeruhi.
Mahakama ya Hakimu Mkazi Mwanza leo Alhamisi Novemba 23,2017 iliwafutia kesi washtakiwa na baadaye walikamatwa na polisi.
Mbali ya Misana na Chinchibela, wengine katika shauri hilo ni Dominick Izengo na Ibeneza Mathew.
Hata hivyo, Mathew hakuhudhuria mahakamani kutokana na taarifa zilizowasilishwa na mdhamini wake, William Victor kuwa anaumwa.
Mdhamini huyo ameshikiliwa na polisi kwa kushindwa kuhakikisha mshtakiwa anahudhuria mahakamani.
Awali, Hakimu Mkazi, Ainawe Moshi aliwaachia huru washtakiwa katika shauri namba 540/2017 la kumjeruhi meneja kampeni wa CCM katika kata hiyo, Thomas Warioba iliyokuwa ikiwakabili.
Hakimu ametoa uamuzi huo baada ya upande wa Jamhuri kupitia wakili Castus Ndamugoba kuwasilisha ombi la kuondoa shauri hilo mahakamani.

Wakili Ndamugoba amewasilisha ombi hilo akitumia kifungu cha 91(1) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai na Marejeo yake ya mwaka 2002 inayotoa fursa kwa upande wa Jamhuri kuondoa shauri mahakamani wakati wowote lakini hakizuii washtakiwa kukamatwa tena.
Washtakiwa walikuwa wakidaiwa kumshambulia Warioba katika tukio lililotokea Novemba 14,2017.  
Polisi waliowakamata washtakiwa wamekataa kusema lolote kwa maelezo kuwa wao si wasemaji.
Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Faustine Shilogile  hajapatikana kuzungumzia suala hilo baada ya waandishi wa Mwananchi waliofika ofisini kwake kuelezwa kuwa yuko kwenye kikao.

Katambi ataka tuhuma dhidi yake zithibitishwe

Aliyekuwa mwenyekiti wa Baraza la Vijana la
Aliyekuwa mwenyekiti wa Baraza la Vijana la Chadema (Bavicha), Patrobas Katambi 
Dar es Salaam. Aliyekuwa mwenyekiti wa Baraza la Vijana la Chadema (Bavicha), Patrobas Katambi amewataka viongozi wakuu wa Chadema kuthibitisha tuhuma za kununuliwa kwake na CCM la sivyo atatoa sababu za kina za uamuzi wa kuhama chama hicho.
Katambi Jumanne Novemba 21,2017 alitangaza kujiunga CCM katika mkutano wa Halmashauri Kuu ya CCM uliofanyika Ikulu, Dar es Salaam akidai upinzani hauna dhamira ya dhati ya kupambana na ufisadi.
Akizungumza na Mwananchi  leo Alhamisi Novemba 23,2017, Katambi amesema, “Inaniuma kuona nazushiwa uongo, natishwa kwa uamuzi wangu, nilikaa kimya kulinda staha za watu, nimetoa muda  wathibitishe wanachokisema.”
Amesema, “Unajua hekima na busara zangu zilinilazimisha kuondoka Chadema na kuhamia CCM bila kufafanua yaliyonitoa ili kuacha haiba yao waendelee kwa amani na mfumo wao wa siasa mpya, lakini wameshindwa sasa nitasema ukweli kama watashindwa kudhibitisha hadharani.” Katambi amesema hakukurupuka kufikia uamuzi wa kuondoka Chadema na wala hakuwashirikisha wazazi wake, kwa hiyo anayepaswa kulaumiwa au kutishwa ni yeye si wazazi au mke wake.


“Nimekuwa nikipokea vitisho vya kila aina, wazazi wangu na mke wangu, niseme tu kwamba mlinzi wa kwanza wa maisha yangu ni Mungu. Namwachia Mungu maisha yangu niliyoyatoa katika ukweli kwa faida ya Watanzania,” amesema.
Amesema kama watashindwa kutoka hadharani kukanusha taarifa hizo, ataitisha mkutano na waandishi wa habari na kusema ukweli wa kile kilichomfanya akaondoka Chadema.
Jana Jumatano Novemba 22,2017 Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe akizungumza naMwananchi alisema Katambi hakuondoka hivihivi bali kuna hila ilifanyika ambayo ilitumia saa 48 kukamilisha mchakato na kujiondoa.
"Badala ya nguvu na fedha kuzielekeza kujenga viwanda wao nguvu wamezielekeza kushawishi viongozi wetu, wamewashawishi wengi na Katambi ni miongoni ingawa wengine wamekataa."

Manispaa Ilala yajipanga kutoa huduma ya afya bure

Dar es Salaam. Ili kukabiliana na changamoto ya msongamano wa watu wanaojitokeza kupata huduma za bure za afya, Halmashauri ya Manispaa ya Ilala mwakani itatenga fedha kwa ajili ya kuziwezesha zahanati kutoa huduma za vipimo bure mara moja kwa mwezi.
Mganga Mkuu wa Manispaa ya Ilala, Victorina Ludovick amesema hayo leo Alhamisi Novemba 23,2017 kwenye mkutano wa baraza la madiwani alipojibu swali la diwani wa Kata ya Mzinga, Isack Job.
Diwani Job alitaka kufahamu mipango ya halmashauri katika kuboresha huduma za afya ili kupunguza idadi ya wanaojitokeza kwenye huduma za bure.
Job ametoa mfano wa upimaji wa afya bure uliofanyika miezi michache iliyopita katika viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam na unaoendelea sasa katika meli kutoka nchini China.
Dk Ludovick amesema katika utafiti waliofanya imebainika watu wengi wanafuata huduma za bure za afya kwa kuwa wanashindwa kwenda kufanya vipimo  hospitalini kutokana na gharama kubwa.
Akifungua kikao, Naibu Meya wa Manispaa ya Ilala, Omari Kumbilamoto amewaeleza wajumbe kuwa, meya Charles Kuyeko anaugua na amekwenda kupata huduma kwenye meli ya China.

Raila arejea Kenya baada ya mapumziko Zanzibar


Zanzibar/Nairobi. Kiongozi wa muungano wa upinzani wa Nasa nchini Kenya, Raila Odinga amerejea nyumbani baada ya kujichimbia kwa siku nne Zanzibar nchini Tanzania.
Mwanasiasa huyo ambaye amegoma kuutambua ushindi wa Rais Uhuru Kenyatta alikuwa visiwani Zanzibar kwa mapumziko baada ya kumaliza ziara ya siku 10 nchini Marekani.
Taarifa za kurejea nyumbani kiongozi huyo zimethibitishwa na msemaji wake, Dennis Onyango ambaye aliliambia gazeti la Nation kuwa Odinga amerejea Kenya.
Pia, mkurugenzi wa mawasiliano wa chama cha Orange Democratic Movement (ODM), Philip Etale amezungumzia kuwasili kwa Odinga mjini Nairobi.
Ingawa baadhi ya picha zimekuwa zikimuonyesha mwanasiasa huyo akiwa mapumzikoni katika hoteli moja Zanzibar lakini ziara yake imehusishwa na hali ya kisiasa nchini mwake.
Mapokezi ya Odinga mwishoni mwa wiki aliporejea Kenya baada ya kuwa nje ya nchi kwa siku 10 yalikumbwa na taharuki baada ya kutokea ghasia zilizohusisha wafuasi wake na polisi.

Museveni awapandisha vyeo maofisa 300 wa jeshi


Kampala, Uganda. Rais Yoweri Museveni wa Uganda amewapandisha vyeo maofisa 300 wa jeshi, akiwamo Mkuu wa Usalama Jeshini (CMI), Kanali Abel Kandiho aliyepandishwa kuwa Brigedia.
Pia, yumo Kamanda wa Kikosi Maalumu, Kanali Don Nabasa ambaye sasa anakuwa Brigedia.
Brigedia John Mateeka amepandishwa cheo kuwa Meja Jenerali akiwa miongoni mwa majenerali wapya watano waliopandishwa vyeo.
Wakati huohuo, polisi nchini Uganda wamelifunga gazeti la habari za udaku la The Red Pepper na kuwatia mbaroni baadhi ya wafanyikazi wake.
Wakurugenzi wakuu watano wa gazeti hilo wanashikiliwa na polisi pamoja na wahariri kadhaa.
Kukamatwa kwao kunatokana na taarifa iliyochapishwa na gazeti hilo inayodai Rais Museveni alikuwa akipanga njama za kupindua utawala wa Rwanda.
Madai hayo yamekanushwa na Serikali ya Uganda.

Mgombea Kata ya Saranga azuiwa kufanya kampeni


Dar es Salaam. Zikiwa zimebaki siku tatu kufanyika uchaguzi mdogo wa udiwani katika kata 43 nchini, mgombea wa Chadema wa Saranga amewekewa pingamizi la kufanya kampeni.
Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imepanga uchaguzi mdogo wa udiwani kufanyika Novemba 26,2017.
Mgombea huyo, Ephaimu Kinyafu wa Kata ya Saranga iliyopo Manispaa ya Ubungo mkoani Dar es Salaam amewekewa pingamizi na Chama cha Wananchi (CUF) la kutofanya kampeni kwa siku zilizobaki.
Kampeni za uchaguzi huo zitahitimishwa Novemba 25,2017.
Msimamizi msaidizi wa uchaguzi huo ambaye pia ni mtendaji wa Kata ya Saranga, Dandasi Kijo amesema leo Alhamisi Novemba 23,2017 kuwa mgombea huyo amewekewa pingamizi baada ya kukiuka masharti ya kampeni.
Kijo amesema kanuni aliyokiuka ni kutamka akiwa jukwaani kuwa CUF haijasimamisha mgombea katika kata hiyo.
Akizungumzia pingamizi hilo, Kinyafu amesema hajashirikishwa kwa lolote hivyo hatambui uamuzi huo wa Jumanne Novemba 21,2017.
Kinyafu ambaye amekata rufaa ngazi ya wilaya, amesema katika kikao kilichofikia uamuzi huo Chadema iliwakilishwa na mjumbe badala ya katibu wa wilaya.
Mgombea huyo amesema hajawahi kupewa barua ya malalamiko wala muda wa kujitetea. Amesema rufaa aliyokata ngazi ya wilaya inasikilizwa leo.

Rais Magufuli kubariki ufunguzi wa hospitali Mloganzila


Dar es Salaam. Rais John Magufuli anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika ufunguzi wa hospitali ya Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (Muhas).
Akizungumza na waandishi wa habari leo Alhamisi Novemba 23,2017 Kaimu Makamu Mkuu wa chuo hicho, Profesa Apolinary Kamuhabwa amesema hospitali hiyo itakayofunguliwa Jumamosi Novemba 25,2017 imepewa hadhi ya kuwa hospitali ya rufaa ya Taifa.
Amesema hilo linatokana na kutoa huduma za kitabibu zinazohitaji madaktari bingwa na madaktari bingwa wabobezi, huku ikiwa imesheheni vifaa vya kisasa.
Profesa Kamuhabwa amesema uwepo wa vifaa vya kisasa na madaktari wa kutosha utasaidia hospitali kupunguza kwa kiasi kikubwa wagonjwa kwenda nje ya nchi kupata tiba.
"Hospitali hii itasaidia kuongeza idadi ya madaktari bingwa kwa kuwa imewekewa mazingira rafiki kwa ajili ya kufanya uchunguzi na utafiti ili kuboresha huduma na matibabu," amesema.
Amesema ujenzi wa hospitali hiyo ni mwendelezo wa Kampasi ya Mloganzila ikiwa ni jitihada za Serikali katika kuboresha chuo hicho.
Naibu makamu mkuu wa chuo na mwangalizi wa huduma za hospitali, Profesa Said Abood amesema hospitali hiyo ina mfumo wa Tehama katika kutuma na kupokea sampuli hivyo kurahisisha kasi ya majibu na huduma.
Amesema huduma zote za hospitali zipo katika jengo moja, hivyo hakutakuwa na usumbufu wa mgonjwa kuzunguka kufuata utaratibu ili kupata matibabu.
"Tuna vifaa vya kisasa ambavyo ni vichache nchini au havipo kabisa, mfano kifaa cha kuvunja mawe kwenye figo bila upasuaji," amesema.

Chadema yatoa tamko mgombea kuzuiwa kufanya kampeni


Dar es Salaam. Chama cha Chadema kimesema kimetii agizo la kutoendelea na kampeni za uchaguzi mdogo wa udiwani katika Kata ya Saranga ili kumlinda mgombea wake, Eprahim Kinyafu kutoenguliwa katika kinyang’anyiro hicho.
Katibu wa Chadema Kanda ya Pwani, Casmir Mabina akizungumza na waandishi wa habari leo Alhamisi Novemba 23,2017 amesema kuna kila dalili za kumuondoa Kinyafu katika uchaguzi huo na kwamba, kumzuia kufanya kampeni ni njia mojawapo.
Akizungumza na Mwananchi leo Alhamisi Novemba 23,2017 msimamizi msaidizi wa uchaguzi ambaye ni ofisa mtendaji wa Kata ya Saranga, Dandasi Kijo amesema Kinyafu amewekewa pingamizi la kutoendelea na kampeni baada ya kukiuka masharti ya kampeni.
"Uwezo tunao wa kuendelea na kampeni kutokana makosa yaliyofanyika katika mchakato wa kutuzuia lakini tumeona si busara kufanya hivyo kutokana na viashiria vilivyopo vya kutaka kumuondoa kabisa Kinyafu katika uchaguzi huu,” amesema Mabina.
Amesema, "Tumeona ni vyema tukatii ili tusiingie katika mtego ambao utasababisha wakazi wa Saranga kukosa mwakilishi bora na makini katika kusimamia kero zao."
Mabina amedai mchakato wa kuzuia kampeni za Chadema umefanyika kimakosa na mamlaka husika zina taarifa, hivyo wao kuendelea na kampeni ni sawa na kuingia kujimaliza.
Kwa upande wake, Kinyafu amewataka wakazi wa Saranga  kujitokeza kwa wingi Novemba 26,2017 kupiga kura ili Chadema ishinde.
"Hata tusipopiga kampeni wana Saranga wanajua nini cha kufanya. Wasishtushwe na pingamizi za kuzuia Chadema kufanya kampeni kwa siku zilizobakia," amesema  Kinyafu.
Wakati huohuo, Chadema imesema imeandika barua Tume ya Taifa ya Uchaguzi  (NEC), wakiomba kubadilishwa msimamizi wa uchaguzi John Kayombo ikidai amekiuka utaratibu wa maadili ya utumishi wa umma.
Pia, imeandika barua kwa Manispaa  ya Ubungo wakiomba wabadilishiwe msimamizi msaidizi wa uchaguzi wa Halmashauri ya Ubungo.
Mabina amesema wamefikia uamuzi huo baada ya Kayombo kuonyesha wazi kuwa yupo upande wa CCM akimpigia kampeni kwa njia ya mitandao ya kijamii mgombea wa chama hicho.
"Hatuna imani na Kayombo kutokana na mwenendo wake si mzuri na amekuwa akichukua picha za kampeni ya mgombea wa CCM kisha kuzisambaza katika mitandao ya kijamii ikiwamo makundi ya WhatsApp," amesema Mabina.
Amesema, "Huyu, hatumtaki asimamie uchaguzi huu. Hii ngoma ipo uwanjani huyu refa hatufai atavuruga mchezo kutokana na tabia ya kufanya kampeni kimyakimya."
Kuhusu mtendaji wa Saranga, Kijo amesema hawataki asimamie uchaguzi kwa madai ameshindwa kutekeleza majukumu yake ikiwamo kutoa uamuzi wa kuzuia kampeni za Chadema kinyume cha utaratibu.
Mwanasheria wa chama hicho, kanda ya Pwani, Gaston Garubi amesema Kayombo hafai kusimamia uchaguzi kwa sababu ameonyesha wazi kuipendelea CCM huku akijua yeye ni mtumishi wa umma.

Canada yatoa Sh14 bilioni kwa mpango wa uzazi


Zaidi ya wanawake milioni moja wanatarajia kunufaika na mpango wa uzazi salama na afya ya mtoto, baada ya ubalozi wa Canada nchini kutoa Sh114.2 bilioni kwa ajili ya mpango huo.
Mpango huo utakaotekelezwa na mashirika matano ya Aga Khan Foundation Canada, Amref, Care Canada, World Vision na Plan Intenational, utawanufaisha wanawake katika mikoa ya Tabora, Mwanza, Simiyu, Rukwa na Kigoma.
Akizindua mpango huo juzi, balozi wa Canada nchini, Ian Myles akiwa ameambatana na waziri wa afya, Ummy Mwalimu alisema lengo la mpango huo ni kuboresha afya ya mama na mtoto katika mikoa hiyo yenye changamoto.
Balozi Myles alisema mchakato huo utakwenda sambamba na utoaji mafunzo kwa watumishi wa afya na kuongeza vifaatiba, ili kupata matokeo mazuri.
“Canada itaendelea kuwa mdau wa mpango wa uzazi salama na afya ya mtoto. Pia, tunasaidiana na Serikali katika jitihada za kupunguza kiwango cha vifo vinavyotokana na uzazi,” alisema Balozi Myles.
Naye Mwalimu aliushukuru Ubalozi wa Canada kwa kushiriki kikamilifu katika jitihada za kuhakikisha mpango wa uzazi salama na afya ya mtoto unazidi kuboreshwa.
Alitumia nafasi hiyo kuyaasa mashirika yanayotekeleza mpango huo kutumia fedha hizo kwa uangalifu, sanjari na kushirikiana na Serikali hasa katika ngazi ya mkoa na halmashauri.
Mkurugenzi wa miradi wa World Vision, Revocatus Kamala alisema katika fedha hizo shirika hilo limepata Sh20 bilioni kwa ajili ya kutekeleza mradi huo Kigoma.
“Tutajikita katika kuimarisha mfumo wa uzazi bora na afya ya mtoto katika wilaya zote za Kigoma kwa miaka minne. Pia, tutajenga wodi za akina mama na chumba cha upasuaji,” alisema Kamala.
Naye mkurugenzi mkazi wa Plan International Tanzania, Jorgen Haldorsen alisema shirika hilo linafurahishwa kufanya kazi na Serikali ya Canada katika kutekeleza mpango huo mkoa wa Rukwa.