Sunday, June 18

Mtanzania atupwa jela Uingereza kwa kutupia picha za marehemu Facebook

Westminster. Mwanaume mmoja anayedaiwa kuwa ni Mtanzania amehukumiwa kifungo cha miezi mitatu jela nchini Uingereza kwa kosa la kurusha katika ukurasa wake wa Facebook, picha za mtu aliyefariki dunia kutokana na moto uliounguza jengo la ghorofa la Mnara wa Grenfell lililopo nchini humo.
Pia, mtu huyo ametakiwa kulipa faini ya Sh579,880 kwa mwathirika wa tukio hilo.
 Mtanzania huyo, Omega Mwaikambo (43) alituma video na picha za mwili wa marehemu uliokuwa kwenye begi  na baadaye picha nyingine tano zikionyesha uso wa  marehemu huyo.
Gazeti la mtandaoni la The Telegraph limeandika kuwa Mwaikambo amekiri makosa ya kutuma mara mbili picha zisizopendeza kwa umma katika mitandao ya kijamii mbele ya Mahakama ya Hakimu Mkazi ya Westminster jana.
Mwaikambo ambaye anaishi hatua chache kutoka lilipo jengo la Grenfell akifanya shughuli za upishi, alishuhudia jinsi jengo hilo lilivyoungua moto usiku na alikuwa ni miongoni mwa wapishi waliowapikia chai wafanyakazi wa zimamoto walipokuwa wakizima moto huo.

“Lakini juzi Jumatano asubuhi alipoangalia miili hiyo nje ya nyumba yake alichukua picha kwa kutumia simu yake aina ya iPad na kuzipakia kwenye mtandao wake wa Facebook,” liliandika gazeti hilo.
Mwendesha Mashtaka wa Polisi, Tom Little amesema; “Anaishi karibu zaidi na mnara wa Grenfell, kama ambavyo mahakama inajua janga hilo lilitokea Juni 14.”
Akitoa hukumu, Jaji wa mahakama hiyo, Tanweer Ikram amesema; “Dunia nzima imeshtushwa na yaliyotokea hapa kutokana na janga la moto, ni hali ya kutisha isiyostahimilika, wafu ni lazima waheshimiwe.”
Ameongeza; “Ulichokifanya kupakia hizo picha kwenye Facebook ni dhahiri kuwa hujaonyesha heshima kwa waathirika wa tukio hilo, kuonyesha uso wake  hadharani ni kosa kubwa na halielezeki.”
Mpaka sasa watu zaidi ya 17 wanadaiwa kufariki dunia kutokana na moto uliounguza jengo hilo refu na maarufu Magharibi mwa Uingereza.


Mtoto wa Kitanzania anabeba mizigo minne mikubwa




Dar es Salaam. Wakati Siku ya Mtoto wa Afrika ikiadhimishwa, ubakaji, ulawiti, mimba na ndoa za utotoni vimetajwa kuwa ni mizigo mikubwa anayoibeba mtoto wa Kitanzania.
Takwimu zinaonyesha kuwapo kwa ongezeko kubwa la matukio hayo na hivyo kumuweka mtoto njiapanda katika kupata haki zake za msingi.
Mbali na matukio hayo, bado watoto wengi wanakabiliwa na ukatili mwingine kama vipigo na kutumikishwa katika shughuli za kiuchumi na kijamii na hivyo kukosa fursa ya kupata elimu.
Kwa mujibu wa Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), mmoja kati ya watoto watatu wa kike, na mmoja wa kiume kati ya watoto saba hapa nchini wameshafanyiwa ukatili kama kunajisiwa, kulawiti na kuchezewa maungo yao.
Takwimu za Dawati la Jinsia la Jeshi la Polisi zilizotolewa mwaka jana zinaonyesha kuwa watoto 2,571 wa kike na kiume walibakwa na kulawitiwa hapa nchini, idadi inayoweza kuwa kubwa zaidi, kutokana na matukio mengi kutoripotiwa.
Utafiti wa Kidemokrafia wa Afya Tanzania (2015-2016) unaonyesha kuwapo kwa ongezeko la mimba za utotoni kutoka asilimia 23 mwaka 2010 hadi 27 mwaka jana.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti baadhi ya wadau, wakiwamo wanaharakati wa masuala ya jinsia na haki za binadamu, walisema hali ya watoto wengi si shwari na kwamba ubakaji, ulawiti, mimba na ndoa za utotoni ni janga linalohitaji nguvu kubwa kupambana nalo.
Meneja wa Idara ya Ujenzi wa Nguvu ya Pamoja wa TGNP, Grace Kisetu alisema ukatili wa kingono kwa watoto ni mkubwa na kwamba, unaathiri makuzi ya mtoto na kumfanya ashindwe kutimiza ndoto zake kimaisha.
“Tatizo hili linapaswa kuchukuliwa kwa uzito mkubwa kwa sababu watoto ni nusu ya Watanzania wote na hawa ndio Taifa la kesho, hivyo lazima walindwe na kuandaliwa vizuri,” alisema.
Kisetu alisema licha ya ukatili huo, utafiti wa TGNP walioufanya hivi karibuni ulibaini kuwa asilimia 72 ya watoto wa kike na asilimia 71 ya watoto wa kiume wanapigwa.
Mimba za utotoni
Pamoja na ukatili huo wa kingono, watoto pia wanakabiliwa na tatizo la mimba za utotoni. Mwenyekiti wa Mtandao wa Kutokomeza Ndoa za Utotoni Tanzania unaojumuisha zaidi ya mashirika 30 nchini, Valery Msoka alisema kuna ongezeko kubwa la mimba za utotoni hasa maeneo ya vijijini ikilinganishwa na mijini.
Msoka alisema katika utafiti uliofanywa na shirika hilo, asilimia 27 ya wasichana wenye umri kati ya miaka 15 hadi 19, wamepata ujauzito (2015-2016).
“Kiwango hiki ni kikubwa ikilinganishwa na ripoti ya mwaka 2010 na takwimu zinaonyesha kuwa asilimia 23 ya watoto walipata mimba,” alisema.
Ukatili unaofanywa na ndugu
Zipo simulizi nyingi za watoto waliofanyiwa ukatili, na tafiti mbalimbali zinaonyesha kuwa watoto wengi wanafanyiwa ukatili huo na watu wa karibu.
Mzazi (jina linahifadhiwa) alisimulia kuwa familia yao imeingia kwenye mtikisiko mkubwa baada ya mtoto wake kulawitiwa na mjomba wake aliyekuwa akimlea, katika eneo la Kimara jijini Dar es Salaam.
“Mwanangu yupo darasa la tatu na alikuwa anaishi na mjomba wake. Likizo hii ya mwezi wa sita amerudi cha ajabu amebadilika tabia na akawa anataka kufanya ngono na mdogo wake wa kiume,” alisema.
Alisema walipomuuliza kwa kina, akasema huwa kila siku anafanywa hivyo na mjomba wake.
“Tulipompeleka hospitali (walisema) mtoto alishaharibiwa siku nyingi. Tulimpeleka kwa mjomba wake kwa sababu ya urahisi wa elimu,” alisema.
“Tupo kwenye wakati mgumu na tunaendelea na taratibu za kumshtaki, japo ni kaka yangu.”
Pia hivi karibuni gazeti hili liliripoti habari ya mtoto wa kike mwenye umri wa miaka 12, aliyejifungua mtoto wa kiume baada ya kubakwa na binamu yake.
Mtaalamu wa saikolojia
Mtaalamu wa masuala ya saikolojia wa taasisi wa Mlee ya jijini Dar es Salaam, Dk Frank John alisema watoto wanapofanyika ukatili kila siku wanaharibiwa akili, na upo uwezekano mkubwa kwao kuwafanyia wengine.
“Mtoto aliyebakwa asiposaidiwa kisaikolojia, atabaki na maumivu makali ndani ya moyo wake, na akikua anaweza kuwa na kisasi,” alisema.
Alisema mtoto anapobakwa huwa anahisi upweke na kuanza kujitenga na wenzake.
“Mtoto huyu ataanza kuwa anazubaa, muoga na wakati mwingine kushuka kielimu. Kwa ujumla watoto wanaofanyiwa ukatili wa kijinsia lazima wapewe matibabu kwa umakini zaidi,” alisema.
Imeandikwa na Tumaini Msowoya, Bakari Kiango, Colnely Joseph na Henerietha Katula.   

Southmpton. Je ni fedha kiasi gani zinaweza kukushawishi kukubali kuambukizwa kikohozi ili kusaidia uvumbuzi wa kisayansi?
Watafiti wa Chuo Kikuu cha Southampton wamesema watampa pauni 3,526 (sawa na Sh10.3 milioni)  mtu yeyote atakayejitokeza ili kukubali changamoto hiyo.
Lengo lao kubwa ni ili kutengeza chanjo bora ili kuwalinda watoto na watu wazima ambao wapo hatarini kuambukizwa ugonjwa huo.
Ili kusaidia ni sharti mtu awe na umri wa kati ya miaka 18-45, awe na afya bora, awe tayari kutengwa kwa siku 17 na kuimba.
Kikohozi ni ugonjwa unaoweza kuambukizwa kwa haraka na huenezwa kupitia hewa ya kikohozi kutoka kwa mtu ambaye ameambukizwa.
Kundi hilo la watafiti wa Chuo Kikuu cha Southampton linataka kuwaambukiza watu walio na afya nzuri kwa kuwawekea puani viini vinavyosababisha maambukizi hayo na kuwachunguza.
 Baadhi ya watu waliojitolea watakuwa wagonjwa, lakini wanasayansi wanawataka wale ambao hawatakuwa na dalili zozote licha ya kuwekewa viini hivyo katika pua zao.
Hatu hii inalenga kujua wale wenye kinga ya asili ya ugonjwa huo.
 Vilevile, wapo wanaobeba ugonjwa huo kwa siri na huwaambukiza watu wengine, lakini huwa hawaambukizwi.

Rais wa Visiwa vya Vanuatu afariki dunia



Vanuatu. Rais wa visiwa vya Vanuatu, Baldwin Lonsdale amefariki dunia kwa kile kinachodaiwa kuwa ni mshtuko wa moyo leo.
Lonsdale ambaye pia ni Kasisi wa Anglikana amekuwa kiongozi wa kisiwa hicho cha Pacific kwa miaka miwili tangu Septemba 2014.
Gazeti la Daily Post nchini Vanuatu limesema kuwa Lonsdale alifariki ghafla kwenye mji mkuu wa Port Vila usiku wa kuamkia leo.
Akiwa rais, Lonsdale aliongoza ujenzi mpya wa maeneo ya kisiwa hicho kufuatia uharibifu uliosababishwa na kimbunga cha Pam kilichosababisha watu 75,000 kukosa makazi mwezi Machi mwaka 2015.
Oktoba mwaka huohuo aliapa kupambana na ufisadi nchini humo baada ya sakata lililomhusisha makamu wake la matumizi mabaya ya rasilimali za umma.

NEWS ALERT: MWANAMICHEZO ALHAJ SHAABAN MINTANGA HAJULIKANI ALIPO, NDUGU WANAMTAFUTA



MWANAMICHEZO ALHAJ SHAABAN MINTANGA HAJULIKANI ALIPO, AMEPOTEA, SIKU YA TATU LEO TANGU AONDOKE NYUMBANI HAJARUDI. 

KWA YEYOTE ATAKAEMUONA AU KUPATA TAARIFA ANITAFUTE KWA SIMU ZIFUATAZO.... 067528439107166633260719168547

ASANTENI -

FAMILIA YA MZEE KIBINDA, KAWE DSM...

Mabodi aitaka CCM iendelee kufanya sera za ushindani wa maendeleo


Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Abdulla Juma Saadalla ‘Mabodi’ amesema CCM itaendelea kufanya ushindani wa sera za maendeleo zitakazowanufaisha wananchi wa makundi yote mijini na vijijini.
Kauli hiyo ameitoa leo (Jumamosi) wakati akifungua mafunzo ya Wanawake na Uongozi kwa wanachama na viongozi wa Umoja wa Wanawake (UWT), Mkoa wa Mjini huko Amani Zanzibar.
 Dk Mabodi amesema wananchi wa Zanzibar kwa sasa wanachohitaji ni siasa za ushindani wa kisera katika kukuza kipato cha mwananchi mmoja mmoja hadi taifa kwa ujumla.
Amesema taifa lolote linalotamani kuendelea kiuchumi ni lazima wananchi wake wakubali kwa vitendo dhana ya siasa za ustaarabu katika kudumisha amani na utulivu wa nchi ili kufanya kazi za kujiongezea kipato na kukuza uchumi wa nchi.