Monday, January 9

Muziki wa Bongo 2011

HIVI wasanii wa kike walikuwa wapi 2011? Ndiyo swali ambalo mashabiki wengi wa muziki nchini wanajiuliza wanapofanya majumuisho ya mwaka 2011 katika siku ya leo Jumamosi tunapoufunga mwaka.
Ukiachilia wachache ambao waliibuka na kupotea, vidole wananyooshewa zaidi wakubwa wawili ambao ni Ray C na Lady Jaydee. Walikuwa kimya muda mrefu na walikuwa wakifanya mambo kimahesabu zaidi.
Ray C aliamua kujichimbia Nairobi, Kenya na kupiga dili zake huko kimya kimya na kudondosha Dar es Salaam baadhi ya singo zake ambazo hazikutamba kama enzi hizo.

Jaydee akakomaa na bendi yake ya Machozi ambayo ilipata shoo nyingi ndani na nje, lakini hakuwa mwepesi kuachia singo kwa fujo kama siku za nyuma, waliokuwa wakienda kwenye kumbi za starehe Bongo ndiyo walimfaidi, lakini upande wa pili alikuwa kibiashara zaidi alizindua miradi yake mingi na kila mara alikuwa bize kuiendesha.

Lakini kuna vichwa ambavyo viliburuza sana kwenye Bongofleva japokuwa wengi wao walikuwa wana nyimbo za kufurahisha na kujirusha zaidi, ambazo zilikuwa hazina ujumbe wowote.

Inawezekana wakati mwingine labda ulizisikia ukaamua kusogeza mbele DVD yako ili zisikuchefue. Lakini huko mitaani wenzio walizipenda na jamaa wakapata mwanya wa kutengeneza fedha ndani na nje ya nchi.

BONGOFLEVA
Wasanii wengine walikuwa wakiibuka na wimbo mmoja na kupotea baada ya wiki chache, wala shoo hawakuambulia. Ingawa baadhi walijitahidi kujitengenezea kashfa na kucheza dili na magazeti ya udaku kupandisha majina yao, lakini bado wakashindwa kuhimili vishindo kutokana na kutokuwa na kazi za maana.

Wasanii wafuatao angalao walijitahidi kuwa bize mwaka mzima wa 2011 na walitengeneza kiasi cha fedha kutokana shoo nyingi za ndani na nje ya nchi, hawakutoka masikioni mwa mashabiki.

20 Percent:
Hakuhitaji kubebwa na prodyuza, redio wala kujitengenezea kashfa ili aibuke. Muziki wake ulimbeba na kumpa tuzo tano kwa wakati mmoja, kitu ambacho hakuna msanii aliyempiku.
Alizurura sana mikoani kufanya shoo pengine kuliko msanii mwingine yeyote na nyimbo zake zilizotamba ni zile zile kama �Tamaa Mbaya�, �Ya Nini Malumbano� mpaka mwisho wa mwaka alipoachia �Pasu Kwa Pasu� ambayo ni jibu baada ya kuacha na prodyuza wake wa siku nyingi Man Walter kwa ugomvi.

Ally Kiba:
Huyu jamaa ameshanasa kwenye masikio ya mashabiki na aliishi kiujanjaujanja kwa kujitangaza zaidi nje ya nchi ambako alipiga shoo nyingi sana.
Alipiga shoo Afrika Mashariki na Ulaya na wimbo wa �Dushedede� ambao uko kwenye staili ya Bolingo ulimbeba kwa kiasi fulani kwa vile ulipendwa na wote.

AY:
Huyu jamaa ni mjanja sana, kama alivyofanya mwaka jana na mwaka huu alifanya hivyo hivyo tena alipiga hatua zaidi na kuwa msanii wa Bongo aliyefanya shoo na wasanii wengi zaidi wa nje achilia mbali Afrika Mashariki hakuna aliyeamini kama angeweza kuwanasa Lamya na Romeo wa Marekani.
Amejiimarisha pia Bongo kwa kufungua maduka mengi ya biashara za nguo na saluni na hata maisha anayoishi ni bora.

DULLY Sykes:
Alifuata nyayo za mastaa wa Uganda na Kenya kibiashara. Ndiye msanii wa Bongofleva aliyekuwa na dili ya kueleweka ya matangazo mengi ya kampuni ya simu za mikononi ya Tigo.
Kama kawaida yake hakuna na nyimbo za kuumiza kichwa, ujumbe wake ulikuwa ni mwepesi sana uliojaa masihara, lakini vijana walimpenda sana na kumsapoti kwa kucheza nyimbo zake na kuibuika kwenye shoo.

BANANA
Kwenye redio hakusikika sana lakini akiwa na B-Band yake alikuwa bize sana kwenye kumbi za Dar es Salaam karibu wiki nzima alikuwa bize kuliko msanii yoyote yule wa muziki wa kizazi kipya. Kilichombeba ni ubunifu wake na bendi yake ambayo imekuwa na vijana wanaovutia wengi.

LINAH na BARNABA
Ukiachilia mbali nyimbo walizofanya kwa kushirikiana hata kila mmoja kivyake walibamba sana mashabiki ndani na nje ya Bongo, ni kizazi kipya kilicholeta mageuzi masikio mwa wengi na hawakutaka makuu.

Shoo za Ulaya wamepiga sana, Linah aliosha jina zaidi baada ya kunasa tuzo mbili za Muziki za Kili, ile ya Mwimbaji Bora wa Kike na Msanii Bora anayeibukia. Usisahau 2011 ndiyo mwaka ambao Linah alinunua gari aina ya Vitz.

DIAMOND
Awali wapinzani wake walidai kwamba alikuwa akichonga dili na magazeti ya udaku ili kujipandisha chati pamoja na kupanua njia yake kibiashara, ingawa hakuna aliyeweza kuthibitisha hilo.

Msanii huyo kama alivyo Ally Kiba walitunisha sana akaunti zao 2011 na walicheza karata zao vizuri na kufunika hata wakongwe.

Skendo zake na wasanii mbalimbali wa kike zimechangia kumweka bize machoni na masikioni mwa mashabiki, lakini hata kazi alifanya nzuri na yenye ubunifu.

BOB JUNIOR
Aliibuka kama masihara, lakini mwisho wa siku akaingia kwenye chati ya wasanii wanaovuma Bongo, singo zake kama Oyoyo zimembeba na kumpa shoo nyingi ingawa zote ni ndani ya mipaka ya Tanzania ya Rais anayependa michezo na Burudani, Jakaya Mrisho Kikwette.

PROF JAY
Kama ipo ndiyo wimbo wake uliotamba miezi ya hivi karibuni, lakini huwezi kuamini ndiyo msanii wa Bongo aliyefanya shoo nyingi zaidi Afrika Mashariki na Ulaya.
Heshima yake kimuziki imeendelea kuwa palepale licha ya kwamba ni mwajiriwa kwenye kampuni moja kubwa ya jijini Dar es Salaam.

Ni msanii msomi na anayefanya kazi kwa hesabu sana na anayefaa kuigwa na chipukizi ambao wamekuwa wakikimbia shule na kung�ang�ania muziki.
Alipokanyaga Uganda, Kenya, Rwanda au Burundi mashabiki walichanganyikiwa.

ROMA MKATOLIKI
Aliibuka kimasihara, lakini amefanya shoo nyingi pengine kuliko alivyotarajia, katika kila shoo kubwa 2011 lazima ungemkuta. Pengine hata yeye hakutarajia kama mashabiki wangeikubali staili yake kiasi hicho.

MWANA FA
Ni Msanii msomi ambaye ukikutana naye ana kwa ana mtaani ukilinganisha na makali yake kwenye kipaza sauti ni vitu tofauti kabisa.
Yuko simpo sana. Alikanyaga Afrika Kusini mara kadhaa na humu ndani ya Bongo aliendelea kujitunzia heshima yake hususani kwa vijana.

BELLE 9
Singo yake ya Sumu ya Penzi imembeba sana na ni mbishi kwelikweli kwenye fani, hachuji. Ameshirikishwa kwenye singo za mastaa kadhaa Bongo na wimbo wake wa Nilipe Nisepe hauna maneno halisi ya kuelezea kwa jinsi ulivyopokelewa mitaani.

JOH MAKINI
Kwa wanaoijua Hip Hop ya Tanzania, wanamjua na hata ambao hawafuatilii aina hiyo ya muziki wanamkubali. Ameonyesha ukomavu sana bila kutetereka au kupotea kama walivyofanya wasanii wengine wa aina hiyo ya muziki.

Wapinzani wake kama Chid Benz, Fid Q, Afande Sele walikuwa wakiibuka na kupotea kipindi kirefu zaidi na walionekana kujishughulisha na dili zingine binafsi zaidi.

DOGO JANJA
Ni msanii mdogo aliyetamba sana mwaka huu wa 2011 ingawa hakua na muda mwingi wa kufanya shoo kutokana na kubanwa na shule, lakini ameonyesha kwamba Bongofleva si jina bali kipaji na ubunifu binafsi.

CPWAA
Yupo kama hayupo, lakini ametengeneza sana na kwenye orodha ya wasanii wa Tanzania waliopiga hela kwa shoo za ndani na nje yumo, hakuna shoo ya maana itapigwa sehemu umkose. Wimbo wake wa Action umembeba.

CHEGE NA TEMBA
Hawa jamaa nuksi na pengine bila wao sasa TMK Wanaume Family itapotea kwenye ramani ya muziki, wao wako juu kuliko kundi na hakuna anayezungumzia tena kundi.

Ukiacha wimbo wao wa Mikono Juu, wametoa nyimbo ambazo zimekubalika ndani na nje na wameshirikishwa na wasanii tofauti na hata ndege wamekwea sana kwenda kufanya shoo zisizo na idadi Ulaya. Je nini hatma ya wengine waliobaki kundini?

TIPTOP CONNECTIONS
Madee na Tundaman waliwaongoza wenzao wa Tip Top kufanya shoo nyingi za ndani tofauti na makundi mengine ambayo ambayo yalionekana kupooza na hayakuwa na jipya 2011 labda tusubirie 2012.


BENDI ZA DANSI
Upepo wa bendi za dansi bado ulibaki kwa Twanga Pepeta, FM Academia, Akudo Impact na Extra Bongo ambazo zilikuwa zikipokonyana mashabiki na kuacha bendi nyingine zikitumbuiza viti katika shoo zao nyingi za Dar es Salaam.


Lakini 2012 huenda ukawa mwaka wa Twanga na Extra endapo FM na Akudo wasipojipanga kwani katika siku za hivi karibuni wameonekana kuyumba na kutokuwa na jipya jukwaani.

MUZIKI WA TAARAB
Taarab ilizoa mashabiki kadhaa wa dansi mwaka 2011, jambo ambalo liliwalazimu watu wa bendi kuwa wanafanya shoo za pamoja na bendi za Taarab ili kujaza mashabiki.

Bendi za Taarab zilizotamba sana ni Jahazi, Five Stars na Mashauzi Classic.

Filamu Bongo 2011

WASANII wa filamu Bongo mwaka 2011 walifanya mambo makubwa na kupiga hatua katika tasnia ya filamu, huku wasanii wengine wakiibuka na kuwa gumzo.

RAY
Ray yeye kama ilivyo kawaida ndiye kioo cha tasnia ya filamu kwa mwaka huo. Aliweza kufanya mambo makubwa ikiwa ni pamoja na kusafiri kwenda kununua vifaa vyake vya kazi Ulaya.
Pia kwa kutumia kampuni yake aliibua wasanii wapya kama Otilia Joseph.

MONALISA
Yvonne Cherryl �Monalisa� alishiriki tuzo za Pan African zilizofanyika nchini Marekani kupitia filamu yake ya Binti Nusa iliyotengenezwa na kampuni yake.

Mwaka jana pia alipata nafasi ya kwenda kushiriki filamu nchini Ghana ikiwa ni sehemu mojawapo ya kutafuta soko la kimataifa. Jambo jingine kubwa kwa mwanadada huyo ni kuwa alisambaza filamu ya Binti Nusa yeye mwenyewe.

KANUMBA
Kanumba naye hakuwa nyuma kwani alitoa filamu nyingi zilizofanya vizuri, si hayo tu bali pia alitumia uwezo wake katika kumleta msanii nyota wa kimataifa kutoka nchini Nigeria, Ramsey Nouah, kushiriki katika filamu yake ya Devil Kingdom.

Filamu ilitikisa katika tasnia ya filamu Bongo. Pia ndiye msanii ambaye amekuwa balozi wa makampuni mbalimbali kwa mwaka jana. Alisafiri kwenda nchini Marekani katika shughuli za sanaa, pia alikwenda Ghana kwa ajili ya kurekodi filamu akishirikiana na nyota wa filamu Afrika kutoka nchi kama Nigeria, Ghana na Afrika Kusini.

WOLPER
Jacqueline Wolper ni moja kati ya wasanii ambao kwa mwaka uliopita alifanya vizuri katika mauzo hata kuweza kuwafunika baadhi ya wasanii wa kike katika tasnia ya filamu.
Wolper pia alitengeneza filamu zake akiwa kama mtayarishaji, amefanya vema katika tasnia hii ya filamu Bongo anastahili Pongezi.

JB
Jacob Stephen �JB� ndiye msanii anayeshikilia nafasi ya kwanza kwa mauzo Bongo kupitia filamu anazoshiriki na kutengeneza mwenyewe.
Filamu yake ya Senior Bachelor ilionyesha uwezo wake wa hali ya juu na kumfanya ashikilie nambari moja.
Filamu zake nyingine ni pamoja na Nipende Monalisa, DJ Ben na Regina.

PATCHO
Patcho Mwamba ni mwanamuziki, lakini tangu alipoingia katika tasnia ya filamu akiwa sambamba na swahiba yake Kanumba. Moja ya sifa ya Patcho pamoja na kuigiza vizuri ni bingwa wa viwalo Bongo, kwa hiyo kama unampatia nafasi ya kuigiza suala la pamba unasahau.

DOTNATA
Dotnata alifungua kampuni ya Tanganyika Entertainment kwa ajili ya kusambaza kazi zake. Alitengeneza filamu iliyojulikana kwa jina la Chupa Nyeusi akiwashirikisha wasanii kutoka Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo na Burundi.

MR. MTUNIS
Amefanya vizuri sokoni baada ya filamu yake ya Mrembo Kikojozi kuwa gumzo. Hata filamu zake nyingine za Clinic Love na Kisasi zilitamba.

NDAUKA
Rose Ndauka ni moja kati ya akina dada waliofanya vizuri katika tasnia ya filamu Bongo, ikiwa ni pamoja na kufungua kampuni yake ya Rose Ndauka Entertainment kwa ajili ya kazi zake na kufanikiwa kutengeneza filamu kama Bad Girl, The Diary, Reuben na Angel.
Alienda Rwanda kwa ajili ya kurekodi filamu ya Maisha Baada ya Vita Rwanda.
Alitangaza ndoa na meneja wake Mariki iikiwa sambamba na kubadili dini, sasa anaitwa Aisha.


RICHIE
Single Mtambalike �Richie� ni moja kati ya wasanii waliofanya vizuri katika mauzo ya filamu Bongo na aliwaingiza wanaye katika uigizaji kwenye filamu ya Uswahilini Kwetu.

TINO
Hisani Muya �Tino� msanii huyu anarudi kwa nguvu zote, baada ya filamu yake ya Cut Off kufanya vizuri na kufuatiwa na Zowa, sasa ameingiza sokoni filamu ya Loreen inayofanya vizuri sokoni.

Kumbuka kuwa filamu yake ya Shoga ilikuwa gumzo baada ya Bodi ya filamu kuizuia na hatimaye kuibadili jina na kuwa ni Shoga Yangu badala ya Shoga.


DR CHENI
Naye alifanya vema kupitia filamu yake ya One By One na kuwa gumzo akiendelea kuuza sokoni.

Funga mwaka kubwa kuliko zote ni lile wazo la magwiji wa tasnia hiyo, Vincent Kigosi �Ray The Greatest� na Steven Kanumba �Kanumba The Great� walipoamua kutengeneza filamu kwa pamoja na kuipa jina la Off Side,

Walipoenda kuizindua nchini Kongo, ilisababisha baadhi ya watu kupoteza maisha wakipigania kuwaona nyota hao ambao waliandamana na Irene Uwoya, Jenifer na Johari.

Ukija katika fani ya uchekeshaji kwa vichekesho vya filamu, waliofanya vizuri ni King Majuto, Kingwendu, Sharo Milinea, Pembe bin Kichwa na Erick.
Katika upande wa wachekeshaji wa televisheni, kijana Lucas Mhuvile �Joti�' hakuwa na mpinzani. Kila siku amekuwa akibuni na kuibuka na kitu kipya ambacho ni burudani kwa mtazamaji.

Joti ameufunga mwaka kwa kuwa na pointi nyingi pengine kuliko msanii mwingine yeyote.

Madudu zaidi yabainika uwanja wa ndege D'salaam

UWANJA wa ndege wa Mwalimu Julius Nyerere umekumbwa na kashfa nyingine, baada ya abiria, Mtanzania aliyekuwa tayari amegongewa muhuri wa uhamiaji kwenye hati yake ya kusafiria kwenda nje ya nchi, kutokomea kusikojulikana akiwa amewatapeli raia wa Poland, dhahabu na fedha vyenye thamani inayokadiriwa kufikia Sh80 milioni.

Tukio hilo limetokea huku kukiwa na kumbukumbu ya tukio la Desemba 2, mwaka jana pale abiria Zainabu Kaswaka alipokutwa na bastola kwenye ndege ya shirika la Emirates wakati akisafiri kwenda nchini Uingereza.

Wiki mbili baadaye, Desemba 17 mwaka jana, vyanzo vya habari za kiuchunguzi vimethibitisha kwamba raia wawili wa nchini Poland, Hery Jabloiw ambaye kitaaluma ni mhandisi na mwingine ambaye jina lake halikuweza kupatikana mara moja, walitapeliwa walipokuwa katika harakati za kusafiri kuelekea Warsaw kwa ndege ya saa 5:00 usiku ya Shirika la KLM.

Kwa mujibu wa vyanzo hivyo, raia hao wawili wa kigeni, walikuwa nchini ambako siku zote walikuwa na urafiki na raia huyo wa Tanzania (jina tunalihifadhi kwa sasa) ambaye aliwasaidia kununua madhini ya dhahabu kwa mapatano kwamba wangemlipa kiasi fulani cha fedha.

Siku safari walifika naye uwanjani hapo kwa ajili ya kwenda naye Warsaw, Poland ambako wangemlipa malipo ya mwisho kwa mujibu wa makubaliano yao.

Vyanzo hivyo viliongeza kwamba katika mazingira ya kutatanisha, kabla ya kufanyiwa ukaguzi na kuingia uwanjani, raia huyo wa Tanzania aliwaambia Wapoland hao kwamba, madini wasingeweza kusafiri nayo kama mzigo wa mkononi na badala yake aliwashauri ufanyike utaratibu wa kusafirishwa kama kifurushi katika ndege ya mizigo.

Kufuatia ushauri huo, Mtanzania huyo alikwenda kushughulikia suala hilo na baadaye kurejea na nyaraka bandia zilizothibitisha kwamba mzigo ulikabidhiwa kwenye ndege kwa ajili ya kusafirishwa.

Baada ya mchakato huo, tapeli huyo na raia hao wa kigeni walipita kwenye mashine za ukaguzi, kisha kwenda ofis za Idara ya Uhamiaji ambako waligongewa mihuri kwenye hati zao za kusafiria.

Taarifa hizo zinadai kuwa wakiwa tayari wamepita idara ya uhamiaji na kupata idhini ya kusafiri kwenda ng’ambo na baadaye kukaa katika chumba cha kusubiria ndege, ghafla Mtanzania huyo aliwaambia Wapoland hao kwamba kama wana fedha za Tanzania wampatie ili akazibadilishe kuwa dola za Marekani.

Katika mazingira ya kushangaza, Mtanzania huyo alitoka nje na fedha hizo Sh100,000, licha ya kwamba alishafanyiwa ukaguzi na kugongewa muhuri wa uhamiaji kwenye hati aya kusafiria.

Mwananchi lilibaini kwamba, raia huyo ambaye tayari alikuwa amelipwa ujira wa Sh1.7 milioni na Wapoland hao kama shukrani ya kuwasaidia katika utafutaji wa madini, alipotoka nje alipita sehemu zote za ukaguzi bila kuulizwa na akatokomea.

Vyanzo hivyo vilisema Wapoland hao walipanda ndege kwa matarajio kwamba rafiki yao angerejea, lakini haikuwa hivyo kwani ndege ilipokaribia kuruka, walitoa taarifa kwa vyombo vya usalama uwanjani hapo, hivyo wakaahirisha safari.

Walikaa usiku mzima uwanjani bila kumwona raia huyo, na hapo walibaini kwamba walikuwa wametapeliwa na hawakuwa na fedha za akiba kwani walimwambia Mtanzania huyo kwamba, kiasi kingine cha fedha za shukrani wangempatia baada ya kufika Warsaw.

"Wale Wapoland walikaa uwanjani pale hadi asubuhi wakawa hawana hata senti moja. Kuna askari mmoja aliwasaidia na kuwapa chai na chapati. Lakini, watu wanahoji iweje mtu aliyegongewa mhuri wa uhamiaji tayari kwa kusafiri, arejee tena nje na aruhusiwe?" kilohoji chanzo kimoja uwanjani hapo na kuongeza:,

"Kwa sababu, kiutaratibu mtu ukishagongewa mhuri wa uhamiaji maana yake tayari unatakiwa usafiri ng'ambo. Kama akipatwa na dharura, lazima aombe wahusika wakamsadie hawezi kutoka hivihivi, hili ni kosa lakini hapa inaonekana kuna mchezo."

Mkurugenzi
Alipoulizwa Mkurugenzi Mkuu wa Uwanja huo, Moses Mlaki alisema asingeweza kuongea suala hilo kwenye simu, na badala yake alitaka apewe maswali kwa maandishi.

Mkuu wa usalama wa uwanja huo, aliyejulikana kwa jina la Msangi alipoulizwa yeye alisema asingependa kuzungumzia suala hilo kwani eneo lake la kazi, linaishia kwenye ukaguzi wa mashine tu.

Baadhi ya vyanzo vyetu kinachochangia uhalifu ni baadhi ya vibanda vinavyotumiwa na askari kulinda uwanja huo kutokuwa na huduma za umeme na maji hali inayowafanya kufanyakazi katika mazingira magumu.

"Yaani hakuna maji, umeme wala nini, angalia tunalinda mitambo nyeti ya uwanja yenye thamani kubwa lakini maeneo yetu ya kazi hayana umeme wala maji. Tutafanyaje kazi katika hali hii?," kilihoji chanzo kimoja.

Tukio la awali
Madudu hayo ni mwendelezo wa matukio ya kutatanisha uwanjani hapo, kufuatia tukio la Desemba 2, 2011 pale abiria Zainabu Kaswaka, alipokutwa na bastola kwenye ndege ya shirika la Emirates.

Kamanda wa Viwanja vya Ndege nchini, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Ulrich Matei alithibitha taarifa hiyo akisema tukio hilo lilisababisha ndege hiyo iliyokuwa tayari imeanza kuruka, kutua tena kwa ajili ya kuitoa bastola hiyo na kuikabidhi kwa walinzi uwanjani hapo kabla ya kuendelea na safari.

Abiria huyo alikuwa na hati ya kusafiria namba AB00828, alipita na kukaguliwa katika mashine mbili za usalama (X-ray machines), lakini walinzi ambao wanatajwa kutoka Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) Kikosi cha Anga Ukonga (Air wing), hawakuweza kubaini kama moja ya mzigo wa abiria huyo ulikuwa na bastola ndani.

Hadi sasa tukio hilo halijahitimishwa kwani abiria huyo hajarejea nchini.