Monday, January 9

Muziki wa Bongo 2011

HIVI wasanii wa kike walikuwa wapi 2011? Ndiyo swali ambalo mashabiki wengi wa muziki nchini wanajiuliza wanapofanya majumuisho ya mwaka 2011 katika siku ya leo Jumamosi tunapoufunga mwaka.
Ukiachilia wachache ambao waliibuka na kupotea, vidole wananyooshewa zaidi wakubwa wawili ambao ni Ray C na Lady Jaydee. Walikuwa kimya muda mrefu na walikuwa wakifanya mambo kimahesabu zaidi.
Ray C aliamua kujichimbia Nairobi, Kenya na kupiga dili zake huko kimya kimya na kudondosha Dar es Salaam baadhi ya singo zake ambazo hazikutamba kama enzi hizo.

Jaydee akakomaa na bendi yake ya Machozi ambayo ilipata shoo nyingi ndani na nje, lakini hakuwa mwepesi kuachia singo kwa fujo kama siku za nyuma, waliokuwa wakienda kwenye kumbi za starehe Bongo ndiyo walimfaidi, lakini upande wa pili alikuwa kibiashara zaidi alizindua miradi yake mingi na kila mara alikuwa bize kuiendesha.

Lakini kuna vichwa ambavyo viliburuza sana kwenye Bongofleva japokuwa wengi wao walikuwa wana nyimbo za kufurahisha na kujirusha zaidi, ambazo zilikuwa hazina ujumbe wowote.

Inawezekana wakati mwingine labda ulizisikia ukaamua kusogeza mbele DVD yako ili zisikuchefue. Lakini huko mitaani wenzio walizipenda na jamaa wakapata mwanya wa kutengeneza fedha ndani na nje ya nchi.

BONGOFLEVA
Wasanii wengine walikuwa wakiibuka na wimbo mmoja na kupotea baada ya wiki chache, wala shoo hawakuambulia. Ingawa baadhi walijitahidi kujitengenezea kashfa na kucheza dili na magazeti ya udaku kupandisha majina yao, lakini bado wakashindwa kuhimili vishindo kutokana na kutokuwa na kazi za maana.

Wasanii wafuatao angalao walijitahidi kuwa bize mwaka mzima wa 2011 na walitengeneza kiasi cha fedha kutokana shoo nyingi za ndani na nje ya nchi, hawakutoka masikioni mwa mashabiki.

20 Percent:
Hakuhitaji kubebwa na prodyuza, redio wala kujitengenezea kashfa ili aibuke. Muziki wake ulimbeba na kumpa tuzo tano kwa wakati mmoja, kitu ambacho hakuna msanii aliyempiku.
Alizurura sana mikoani kufanya shoo pengine kuliko msanii mwingine yeyote na nyimbo zake zilizotamba ni zile zile kama �Tamaa Mbaya�, �Ya Nini Malumbano� mpaka mwisho wa mwaka alipoachia �Pasu Kwa Pasu� ambayo ni jibu baada ya kuacha na prodyuza wake wa siku nyingi Man Walter kwa ugomvi.

Ally Kiba:
Huyu jamaa ameshanasa kwenye masikio ya mashabiki na aliishi kiujanjaujanja kwa kujitangaza zaidi nje ya nchi ambako alipiga shoo nyingi sana.
Alipiga shoo Afrika Mashariki na Ulaya na wimbo wa �Dushedede� ambao uko kwenye staili ya Bolingo ulimbeba kwa kiasi fulani kwa vile ulipendwa na wote.

AY:
Huyu jamaa ni mjanja sana, kama alivyofanya mwaka jana na mwaka huu alifanya hivyo hivyo tena alipiga hatua zaidi na kuwa msanii wa Bongo aliyefanya shoo na wasanii wengi zaidi wa nje achilia mbali Afrika Mashariki hakuna aliyeamini kama angeweza kuwanasa Lamya na Romeo wa Marekani.
Amejiimarisha pia Bongo kwa kufungua maduka mengi ya biashara za nguo na saluni na hata maisha anayoishi ni bora.

DULLY Sykes:
Alifuata nyayo za mastaa wa Uganda na Kenya kibiashara. Ndiye msanii wa Bongofleva aliyekuwa na dili ya kueleweka ya matangazo mengi ya kampuni ya simu za mikononi ya Tigo.
Kama kawaida yake hakuna na nyimbo za kuumiza kichwa, ujumbe wake ulikuwa ni mwepesi sana uliojaa masihara, lakini vijana walimpenda sana na kumsapoti kwa kucheza nyimbo zake na kuibuika kwenye shoo.

BANANA
Kwenye redio hakusikika sana lakini akiwa na B-Band yake alikuwa bize sana kwenye kumbi za Dar es Salaam karibu wiki nzima alikuwa bize kuliko msanii yoyote yule wa muziki wa kizazi kipya. Kilichombeba ni ubunifu wake na bendi yake ambayo imekuwa na vijana wanaovutia wengi.

LINAH na BARNABA
Ukiachilia mbali nyimbo walizofanya kwa kushirikiana hata kila mmoja kivyake walibamba sana mashabiki ndani na nje ya Bongo, ni kizazi kipya kilicholeta mageuzi masikio mwa wengi na hawakutaka makuu.

Shoo za Ulaya wamepiga sana, Linah aliosha jina zaidi baada ya kunasa tuzo mbili za Muziki za Kili, ile ya Mwimbaji Bora wa Kike na Msanii Bora anayeibukia. Usisahau 2011 ndiyo mwaka ambao Linah alinunua gari aina ya Vitz.

DIAMOND
Awali wapinzani wake walidai kwamba alikuwa akichonga dili na magazeti ya udaku ili kujipandisha chati pamoja na kupanua njia yake kibiashara, ingawa hakuna aliyeweza kuthibitisha hilo.

Msanii huyo kama alivyo Ally Kiba walitunisha sana akaunti zao 2011 na walicheza karata zao vizuri na kufunika hata wakongwe.

Skendo zake na wasanii mbalimbali wa kike zimechangia kumweka bize machoni na masikioni mwa mashabiki, lakini hata kazi alifanya nzuri na yenye ubunifu.

BOB JUNIOR
Aliibuka kama masihara, lakini mwisho wa siku akaingia kwenye chati ya wasanii wanaovuma Bongo, singo zake kama Oyoyo zimembeba na kumpa shoo nyingi ingawa zote ni ndani ya mipaka ya Tanzania ya Rais anayependa michezo na Burudani, Jakaya Mrisho Kikwette.

PROF JAY
Kama ipo ndiyo wimbo wake uliotamba miezi ya hivi karibuni, lakini huwezi kuamini ndiyo msanii wa Bongo aliyefanya shoo nyingi zaidi Afrika Mashariki na Ulaya.
Heshima yake kimuziki imeendelea kuwa palepale licha ya kwamba ni mwajiriwa kwenye kampuni moja kubwa ya jijini Dar es Salaam.

Ni msanii msomi na anayefanya kazi kwa hesabu sana na anayefaa kuigwa na chipukizi ambao wamekuwa wakikimbia shule na kung�ang�ania muziki.
Alipokanyaga Uganda, Kenya, Rwanda au Burundi mashabiki walichanganyikiwa.

ROMA MKATOLIKI
Aliibuka kimasihara, lakini amefanya shoo nyingi pengine kuliko alivyotarajia, katika kila shoo kubwa 2011 lazima ungemkuta. Pengine hata yeye hakutarajia kama mashabiki wangeikubali staili yake kiasi hicho.

MWANA FA
Ni Msanii msomi ambaye ukikutana naye ana kwa ana mtaani ukilinganisha na makali yake kwenye kipaza sauti ni vitu tofauti kabisa.
Yuko simpo sana. Alikanyaga Afrika Kusini mara kadhaa na humu ndani ya Bongo aliendelea kujitunzia heshima yake hususani kwa vijana.

BELLE 9
Singo yake ya Sumu ya Penzi imembeba sana na ni mbishi kwelikweli kwenye fani, hachuji. Ameshirikishwa kwenye singo za mastaa kadhaa Bongo na wimbo wake wa Nilipe Nisepe hauna maneno halisi ya kuelezea kwa jinsi ulivyopokelewa mitaani.

JOH MAKINI
Kwa wanaoijua Hip Hop ya Tanzania, wanamjua na hata ambao hawafuatilii aina hiyo ya muziki wanamkubali. Ameonyesha ukomavu sana bila kutetereka au kupotea kama walivyofanya wasanii wengine wa aina hiyo ya muziki.

Wapinzani wake kama Chid Benz, Fid Q, Afande Sele walikuwa wakiibuka na kupotea kipindi kirefu zaidi na walionekana kujishughulisha na dili zingine binafsi zaidi.

DOGO JANJA
Ni msanii mdogo aliyetamba sana mwaka huu wa 2011 ingawa hakua na muda mwingi wa kufanya shoo kutokana na kubanwa na shule, lakini ameonyesha kwamba Bongofleva si jina bali kipaji na ubunifu binafsi.

CPWAA
Yupo kama hayupo, lakini ametengeneza sana na kwenye orodha ya wasanii wa Tanzania waliopiga hela kwa shoo za ndani na nje yumo, hakuna shoo ya maana itapigwa sehemu umkose. Wimbo wake wa Action umembeba.

CHEGE NA TEMBA
Hawa jamaa nuksi na pengine bila wao sasa TMK Wanaume Family itapotea kwenye ramani ya muziki, wao wako juu kuliko kundi na hakuna anayezungumzia tena kundi.

Ukiacha wimbo wao wa Mikono Juu, wametoa nyimbo ambazo zimekubalika ndani na nje na wameshirikishwa na wasanii tofauti na hata ndege wamekwea sana kwenda kufanya shoo zisizo na idadi Ulaya. Je nini hatma ya wengine waliobaki kundini?

TIPTOP CONNECTIONS
Madee na Tundaman waliwaongoza wenzao wa Tip Top kufanya shoo nyingi za ndani tofauti na makundi mengine ambayo ambayo yalionekana kupooza na hayakuwa na jipya 2011 labda tusubirie 2012.


BENDI ZA DANSI
Upepo wa bendi za dansi bado ulibaki kwa Twanga Pepeta, FM Academia, Akudo Impact na Extra Bongo ambazo zilikuwa zikipokonyana mashabiki na kuacha bendi nyingine zikitumbuiza viti katika shoo zao nyingi za Dar es Salaam.


Lakini 2012 huenda ukawa mwaka wa Twanga na Extra endapo FM na Akudo wasipojipanga kwani katika siku za hivi karibuni wameonekana kuyumba na kutokuwa na jipya jukwaani.

MUZIKI WA TAARAB
Taarab ilizoa mashabiki kadhaa wa dansi mwaka 2011, jambo ambalo liliwalazimu watu wa bendi kuwa wanafanya shoo za pamoja na bendi za Taarab ili kujaza mashabiki.

Bendi za Taarab zilizotamba sana ni Jahazi, Five Stars na Mashauzi Classic.

No comments:

Post a Comment