Thursday, August 29

Dk Ndalichako: Siasa zisipewe nafasi kwenye mitihani yetu


Swali: Unazungumziaje alama za upimaji wa mwanafunzi (continuous assessment) zinazotoka shuleni na nafasi yake katika matokeo ya mwisho?

Jibu: Ni vigumu kujua uhalisia wa alama zinazoletwa kutoka shuleni, wengine wanasema Necta tufuatilie huko shuleni ili kujua uhalisia wake, tutafanya vipi hilo wakati wafanyakazi wote wa Necta ukijumlisha na walinzi tupo 297 na shule za sekondari pekee zipo 430?

Mwaka 2011 wale wanafunzi walioandika vitu visivyoeleweka kwenye mitihani ya mwisho, kwenye alama zao za maendeleo zilizoletwa walikuwa mpaka na 75. Wengine walishindwa kuandika chochote kwenye mtihani wa mwisho lakini kwenye alama zao za maendeleo walikuwa na alama nzuri tu.

Ukiwauliza walimu wengine wanasema hawakuwa na walimu, wanasema walikuwa wanatumia waliomaliza kidato cha sita na hawajui kujaza vizuri hizo alama.

Wengine walisema mitihani ya ndani watoto wanatazamiana majibu na sababu nyingi kama hizo.

Kwa sasa kuna kamati imepewa jukumu la kuangalia hizo alama za maendeleo, kwa hiyo hilo ni eneo ambalo lazima tuliangalie.

Pia nafikiri kwa sababu ya mazingira ya shule zetu, tufike mahali tuwe na uwazi zaidi.

Nafikiri tufike mahali kwenye cheti tuweke alama za mtihani wa Necta na zile zilizotoka shuleni.

Tuseme mathalan huyo mtoto amepata A, lakini kwenye mtihani wa Necta alipata alama hii na ile ya shuleni alipata hivi. Baada ya hapo tukifika kwenye soko la ajira mwajiri achague kama ataangalia alama za shule au za Necta.

Swali: Tangu uanze kuiongoza Necta mpaka sasa unajivunia nini?

Jibu: Nimekaa Necta tangu mwaka 2005, yapo mengi naweza kujivunia, kwanza wakati naingia kila kitu kilikuwa manual (hatukutumia mashine), lakini hivi sasa kila kitu kuhusu mtihani kuanzia usajili tunatumia kompyuta.

Hili limesaidia kupunguza makosa, hasa kwa upande wa watahiniwa wa kujitegemea kwa sababu zamani watu walikuwa wanafanya udanganyifu sana.

Sasa hivi haiwezekani kutumia namba ya mtu mwingine. Usahihishaji kwa darasa la saba sasa hivi pia tunatumia mfumo wa OMR, zamani tulikuwa tunatumia watu 480 kusahihisha mitihani kwa siku 30.

Baada ya kufanya tathimini ya mfumo huu kwa mwaka jana, tumebaini kuwa mashine haikufanya kosa hata moja, baadhi yaliyotokea yalisababishwa na watu na mashine iliwaumbua.

Kwa kidato cha nne na kuendelea, hatujaanza kutumia kompyuta lakini kuna mengi tumefanya, sasa hivi tumeweka mfumo kuweka alama, zikishaingizwa kwenye mfumo kutoka kwenye kituo cha usahihishaji hakuna mtu anayeweza kuzigusa na akigusa anaonekana.

Hata msahihishaji akishaziweka mara moja hawezi kuzigusa tena na akigusa anaonekana. Kwa hiyo kwa mfumo huu, huwezi kumwongezea mwanafunzi alama. Kwa hiyo alama za wanafunzi zinakuwa katika mazingira salama sana.

Databank (benki ya mitihani) tumeiimarisha, maswali ni mengi tofauti na zamani ulikuwa unakuta kwa somo husika kuna mitihani miwili tu.

Kwa sasa maswali ni mengi, ndiyo maana hata kuvuja kwa mitihani hakuna. Kwa mfano, somo kama hisabati kuna maswali kama milioni moja, hata ukimpa mwanafunzi hawezi kuyafanya yote na ajue kwenye mtihani ni lipi litatoka.

Sasa hivi kweli mitihani ni salama sana, lengo letu ni kupunguza mikono kwenye mitihani. Naamini zaidi mifumo kuliko mtu na kwenye mitihani tukileta kuaminiana tunaweza kuwa pabaya.

Swali: Nini ambacho bado unatamani kukifanya ndani ya Necta?

Jibu: Ninachotamani kwa sasa ni kufika mahali tuwe na mashine zinazochapisha mitihani, kuhesabu na kuweka zenyewe kwenye bahasha.

Kwa sasa tunatumia kama siku 40 kuweka mitihani ya shule za msingi kwenye bahasha tu, hii ni kwa sababu lazima watu wanaofanya hii kazi wawe ni wachache na wenye weledi mkubwa. Hawa watu wangetumia hizi siku kufikiri namna ya kuwa na mitihani bora zaidi ingesaidia.

Suala jingine ni kuwajengea uwezo wa wafanyakazi wetu, haswa wa kuandaa maswali. Nina bahati nimesoma nje ya nchi nikasoma kwa undani juu ya mitihani.

Nataka tuwe tunawepeleka watu nje kusomea zaidi juu ya kazi zao, utunzi wa mitihani na masuala mengine, wawe na taaluma nzuri mtu awe na shahada au shahada ya uzamili kwenye eneo la utungaji wa mitihani tu.

Natamani pia jamii ijue majukumu yetu sisi kama baraza, baraza ni kama daktari tu, ukija unapimwa na kuambiwa una vijidudu 10 vya malaria. Daktari akishakupa hayo majibu ni jukumu lako kuangalia kama unatumia neti au mazingira yako vipi na ufanye nini ili usipate tena malaria. Kwa sasa watu wanakuwa na mtizamo hasi sana.

Nimekaa miaka minane baraza, wakati naingia watoto walikuwa hawaandiki madudu lakini sasa hali ni ngumu, wanachora vitu vya ajabu wanaandika matusi, wengine wanaonyesha kabisa hawajui kitu walichokuwa wanafanya.Baada ya hali hiyo, watu wengine wanasema kwa nini mnapeleka mitihani shuleni na hakuna vifaa, wengine wanasema kwa nini mtihani mmoja wakati shule hazifanani, mimi nauliza kwa nini shule isiwe na vitabu.

Wanasema mitihani ilingane na mazingira, Watanzania wote tuko sawa, kama hakuna vifaa shuleni hiyi siyo kazi ya baraza, umma unabidi uelewe hilo. Kwa sasa kitu ambacho naona ni tishio kwa baraza na mitihani ni mitizamo watu. Wengi wanaukataa ukweli, muda wote anatumia nguvu nyingi kuukataa ukweli.

Suala ni la kweli kabisa lakini mtu anakataa mimi naona hiyo ni hatari sana, huwezi kutibu tatizo bila kujua na kuukubali ukweli, ili tuweze kuboresha elimu lazima tukubali ukweli na kukubali kurekebisha, hali ikiendelea ilivyo sasa huko mbele tutakuwa kwenye hali mbaya sana


Ponda asimamisha shughuli Morogoro

Sheikhe Ponda Issa Ponda akiwa chini ya ulinzi wa
askari magereza wakati akielekea katika mahakama ya
hakimu mkazi Morogoro kusikiliza kesi yake inayomkabili. 

Morogoro. Kiongozi wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu, Sheikh Ponda Issa Ponda jana alisababisha kusimama kwa shughuli za Serikali wilayani Morogoro baada ya ofisi kadhaa ikiwamo ya Mkuu wa Wilaya na baadhi ya mitaa kufungwa ili kupisha kusikilizwa kwa kesi inayomkabili katika Mahakama ya Mkoa wa Morogoro.

Tofauti na Agosti 19, mwaka huu wakati aliposafirishwa kwa helikopta, jana Sheikh Ponda alisafirishwa kwa barabara kutoka Dar es Salaam hadi Morogoro akiwa chini ya ulinzi.

Mbali ya Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Morogoro kufungwa, nyingine ni Hazina Ndogo, Madini, Posta, Vipimo, Ukaguzi na Maktaba ya Mkoa.

Sababu za kufungwa kwa ofisi hizo pamoja na Mtaa wa Stesheni na maeneo ya Posta ni kuwa jirani na Mahakama hiyo. Magari yalizuiwa kutembea katika njia na maeneo ya karibu na ofisi pamoja na Mahakama hiyo huku kukiwa na idadi kubwa ya askari polisi na magereza kwa muda wote wa takriban saa mbili.

Alifikishwa mahakamani hapo saa 4:10 asubuhi akiwa katika basi la Magereza ambalo lilisindikizwa na jingine dogo, huku magari mengine yakisimamishwa kupisha msafara huo. Mahakama hiyo ilifurika umati wa wafuasi wa kiongozi kiasi cha kuwalazimu polisi na wana usalama wengine kuweka utepe kuwazuia wengi wao kufika katika jengo lililokuwa likitumika kuendesha kesi hiyo.

Shughuli katika eneo hilo zilirejea katika hali yake ya kawaida saa 6:25 mchana baada kesi yake kuahirishwa na msafara wa Sheikh Ponda kurejea katika Gereza la Segerea, Dar es Salaam ambako yuko rumande.

Muda wote tangu kuwasili mpaka kusikilizwa kwa kesi hiyo, wafuasi hao walikuwa kimya hadi pale ilipoahirishwa na hasa baada ya Sheikh Ponda kuwapungia mkono alipokuwa akielekea kwenye basi ambako walisikika wakisema: “Takbriir na kuitikia Allahu Akbar – (Mungu Mkubwa).”

Kesi yenyewe

Katika kesi hiyo, Wakili wa Serikali, Benard Kongola alisema mbele ya Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mkoa wa Morogoro, Richard Kabate kuwa Sheikh Ponda alitenda makosa ya uchochezi Agosti 10, mwaka huu saa 11.45 jioni kwenye maeneo ya Kiwanja cha Ndege, Morogoro.

Alisema siku hiyo, Sheikh Ponda alialikwa kutoa maelezo machache kwenye Kongamano la Eid lililoandaliwa na Umoja wa Wahadhiri Mkoa wa Morogoro (Uwamo) na kwamba akiwa hapo alitamka maneno: “Ndugu Waislamu, msikubali uundwaji wa kamati za ulinzi na usalama za misikiti kwani kamati hizo zimeundwa na Baraza la Waislamu Tanzania (Bakwata), ambao ni vibaraka wa CCM na Serikali na kama watajitokeza kwenu watu hao na kujitambulisha kwamba wao ni kamati za ulinzi na usalama za misikiti, fungeni milango na madirisha ya misikiti yenu na muwapige sana,” huku akijua kutoa maneno hayo ni kosa kisheria.

Alisema kwa kufanya hivyo, Sheikh Ponda anayetetewa na mawakili watatu wanaoongozwa na Juma Nassoro, alivunja masharti ya Mahakama ya kifungo cha nje iliyotolewa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu ya Mei 9, mwaka huu iliyokuwa imetamka kuhubiri amani.

Katika shtaka la pili, Sheikh Ponda anadaiwa kuwashawishi wafuasi wake kutenda kosa la jinai kwa kuwaambia: Serikali ilipeleka jeshi Mtwara kushughulikia suala la vurugu iliyotokana na gesi kwa kuwaua, kuwabaka na kuwatesa wananchi kwa sababu asilimia 90 ya wakazi wake ni Waislamu, lakini haikufanya hivyo kwa wananchi wa Loliondo waliokataa Mwarabu asipatiwe kipande cha ardhi ya uwindaji baada ya kudai ni mali yao kwa sababu asilimia 90 ya wakazi wake ni Wakristo.” Shtaka la tatu ni kudaiwa kutamka maneno yaliyoumiza imani ya watu wengine kama yalivyo katika shtaka la pili.

Baada ya kusoma mashtaka hayo, Kongola alisema walikuwa na mashahidi 15 na vielelezo vitatu ambavyo ni DVD mbili na kibali kilichotolewa na Mkuu wa Polisi Wilaya ya Morogoro(OCD), Agosti Mosi, 2013 cha kongamano husika na hati ya hukumu iliyotolewa na Mahakama ya Kisutu, Mei 9, 2013.

Baada ya kusomewa, Sheikh Ponda alikana mashtaka yote matatu huku akikubali kuwemo kwenye kongamano hilo. Alikiri kukamatwa na polisi Agosti 11, Dar es Salaam.

Wakili wa utetezi, Nassor aliwasilisha ombi la dhamana kwa mteja akisema mashtaka hayo yote kisheria yana dhamana. Pia aliwasilisha ombi la kupatiwa hati yenye maelezo ya mlalamikaji ambaye ni Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwani alisema kuwa kutokana na upelelezi upande wa mashtaka kukamilika, wanahitaji maelezo hayo kwa ajili ya kuandaa utetezi.

Hata hivyo, Wakili Kongola aliiomba Mahakama kutompa dhamana mshtakiwa kutokana na cheti kilichotolewa na Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), kupinga dhamana ya mshtakiwa huyo kwa masilahi ya usalama wa nchi.

Akitoa mwongozo wa maombi yaliyowasilishwa na pande zote mbili, Hakimu Kabate aliahirisha kesi hiyo hadi Septemba 11, mwaka huu itakapotajwa tena na kwamba Septemba 17, mwaka huu Mahakama itatoa uamuzi endapo mshtakiwa atapewa dhamana au la wakati itakapoanza kusikilizwa.

MWIGULU NCHEMBA ATAKA MBOWE NA DR. SLAA WAKAMATWE KWA MAUAJI YA RAIA

MBUNGE wa Iramba Magharibi, Mwigulu Nchemba (CCM), amechafua hali ya hewa bungeni kwa kuitaka Serikali kuwachukuliwa hatua viongozi wa juu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA). Mbunge huyo alisema mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe pamoja na Katibu Mkuu wake, Dk. Wilbroad Slaa, wanapaswa kuchukuliwa hatua kwa madai ya kusababisha mauaji ya raia.

Mwigulu, ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Bara, alisema katika kipindi cha miaka miwili tangu nchi ilipotoka kwenye uchaguzi, viongozi hao wamekuwa wakihamasisha maandamano na kusababisha umwagaji wa damu za Watanzania.

“Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi cha miaka miwili tangu nchi yetu ilipomaliza Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010, Mbowe na Dk. Slaa wamekuwa wakitoa kauli za wazi na hata kusababisha mauaji ya watu bila hatia.

“Kutokana na hali hii, sijui Serikali inafanya nini katika kuwachukulia hatua, kwani viongozi hawa wamekuwa wakitafuta umaarufu wa kisiasa kwa kuchochea chuki na mauaji dhidi ya raia.

“Kwa hali hiyo, tangu kipindi hicho hadi leo hii wanasubiri nini badala ya kwenda kuwaweka jela, kwani huko ndiko wanatakiwa kuwa,” alisema.

Mwigulu, alisema kukosekana kwa maadili kwa baadhi ya viongozi wa siasa, ambao wamekuwa wakitumia majukwaa na kuhubiri umwagaji damu ni hatari kwa taifa.

Alisema viongozi hao wamekuwa wakitumia majukwaa hayo na kusababisha vifo vya wananchi, huku akitaja vurugu zilizotokea katika mikoa ya Morogoro, Iringa, Arusha na Singida.

Akijibu swali hilo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Utawala Bora), George Mkuchika, alisema Serikali inafanya kazi kwa mujibu wa sheria, ikiwa ni pamoja na kukusanya ushahidi na kwamba mahakama ndicho chombo chenye uamuzi wa mwisho dhidi ya adhabu kwa raia au kiongozi yeyote wa kisiasa.

Kauli hiyo ya Mwigulu ilionekana kuchafua hali ya hewa ndani ya Bunge, ambapo Mbunge wa Nyamagana, Ezekiel Wenje (Chadema), alisimama na kuomba mwongozo wa Spika, huku akimtaka Mwigulu kuthibitisha kauli yake, vinginevyo aombe radhi.

Wenje alisema hoja ya Mwigulu imekosa mashiko na ina lengo la kuwadhalilisha viongozi wa Chadema, huku akisahau kuwa baada ya uchaguzi wa Arumeru Mashariki, aliyekuwa Mwenyetiki wa Chadema tawi la Usa River, Omari Mbwambo, aliuawa na watu anaodaiwa kuwa ni wafuasi wa CCM.

Awali katika swali la msingi, Mbunge wa Same Mashariki, Anne Kilango (CCM), alitaka kujua Serikali inachukua hatua gani kwa wanasiasa wanaokiuka maadili na kusababisha uvunjifu wa amani.

“Wanataaluma kama vile madaktari, wahandisi, wahasibu na hata wakandarasi pindi wanapokiuka maadili ya kazi zao huchukuliwa hatua kwa kufutiwa leseni zao.

“Vile vile viongozi wa kisiasa wanayo maadili yanayowaongoza, kwanini pale wanapokiuka maadili ya kazi zao hawachukuliwi hatua kama ilivyo katika makundi hayo? (taaluma),” alisema Kilango.

LUKUVI: WABUNGE WENGI WAMO ORODHA YA DAWA ZA KULEVYA


Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi

Dodoma. Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi amesema baadhi ya majina ya wabunge yametajwa miongoni mwa watu wanaoshukiwa kujihusisha na biashara ya dawa za kulevya lakini Serikali haiwezi kuwataja hadharani kwa haraka.

Majibu hayo ya Waziri Lukuvi yamekuja baada ya wabunge kumbana na wengine wakizomea baada ya kueleza ugumu wa kutaja majina ya washukiwa pasi na ushahidi wa kutosha.

“Serikali haiwezi kutaja majina haraka kiasi hicho kwani inaogopa kukurupuka na kushindwa mahakamani, hivyo lazima tuwe makini sana na jambo hilo. Hatuwezi kukurupuka tu eti ni fulani wakati hatuna vithibitisho.

“Kumbukeni wengine mpo humu ndani ya Bunge na tukianza wengi mtakwisha maana katika orodha hiyo kubwa na ninyi mmo na orodha ni kubwa kweli ambayo wakati mwingine inatakiwa umakini wa hali ya juu,” alisema Lukuvi alipokuwa akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Karatu (Chadema), Mchungaji Israel Natse.

Katika swali lake ambalo lilisababisha kelele za kuzomea, Natse alitaka majina hayo yatajwe hadharani. Hata hivyo, hali ilitulia baada ya Spika wa Bunge, Anne Makinda kuingilia kati na kusema: “Hii tabia ya zomeazomea siitaki humu ndani, acheni tabia hiyo lazima mumsikilize mtu kwa kile anachokisema kwanza lakini mtindo huu si mzuri...”

Patashika hiyo ilitokana na swali la Mbunge wa Viti Maalumu (CCM), Catherine Magige aliyetaka kujua iwapo Serikali inaweza kuwaambia Watanzania ukubwa wa biashara hiyo nchini na kama haioni kama kuna tatizo katika ukaguzi wa abiria na mizigo katika viwanja vya ndege na juhudi za Serikali kumaliza tatizo hilo.

Akijibu swali hilo, Lukuvi alisema ukubwa wa biashara hiyo hapa nchini unadhihirishwa na idadi ya Watanzania 274 waliokamatwa kati ya mwaka 2008 hadi Julai mwaka huu kwa kosa la kujihusisha na dawa za kulevya katika nchi mbalimbali za nje.

Alisema Serikali inafahamu ukubwa wa tatizo la matumizi ya biashara hiyo haramu ya dawa za kulevya nchini na alitaja takwimu za ukamataji wa dawa hizo katika kipindi cha kuanzia mwaka 2000 hadi Machi, 2012.

Alisema pamoja na kukamatwa kwa Watanzania hao nje ya nchi, wageni 31 wanashikiliwa mahabusu katika Magereza ya Keko na Ukonga, Dar es Salaam ambao ni raia wa Iran, Pakistan, Senegal na Afrika Kusini.

Hata hivyo, katika swali lake la nyongeza, Magige alisema uteketezaji wa dawa zinazotajwa kukamatwa umekuwa wa siri kiasi cha kutiliwa shaka kuwa huenda zinachukuliwa na maofisa waliozikamata ndiyo maana hakuna uwazi.

Kuhusu hilo, Waziri Lukuvi alisema suala la uteketezaji wa dawa hizo hauko wazi kutokana na sheria zilizopo kutotoa nafasi ya kuteketezwa mapema kwa kuwa zinatumika kwa ajili ya ushahidi akisema wakati mwingine hukaa zaidi ya miaka 10.