Saturday, May 5

Mawaziri, hakuna sherehe, nendeni mkawajibike! by zittokabwe

Juhudi za kurejesha misingi ya uwajibikaji katika utumishi wa umma zimeanza kuzaa matunda Baada ya Rais kutekeleza shinikizo la Bunge la kuwafukuza kazi baadhi ya Mawaziri ambao Wizara zao zimetuhumiwa kwa ubadhirifu wa fedha za umma, rushwa na utendaji mbovu. Mawaziri 6 wamefukuzwa kazi baada ya kugoma kujiuzulu wao wenyewe, manaibu Waziri 2 wamefukuzwa pia.

Ndugu George Mkuchika alitakiwa kujiuzulu, akajiuzulu lakini Rais amemrudisha kwenye Baraza kama Waziri wa Utawala Bora. Yeye nampongeza kwani hakuwa na makuu ya kuanza kujitetea kama wengine. Atakuwa ametoa funzo kwa wenzake.

Kwa kawaida wateule hufanya sherehe kwa kuteuliwa kwao. Nitawashangaa watakaofanya sherehe safari hii kwani hakuna cha kufurahia. Nitawashangaa Watakaokwenda kuapa na Maua kwa furaha kwani furaha itakuwa ya muda mfupi tu. Mkutano wa Bunge wa Bajeti ni mwezi ujao tu na Wateule wote watakuwa kikaangoni. Too short honeymoon.

Hakuna cha kusherehekea kwa sababu nchi in a changamoto nyingi sana. Changamoto ya kuzalisha umeme wa kutosha na kuusambaza kwa wananchi wengi, changamoto ya kukuza uchumi wa vijijini na kukuza uzalishaji viwandani ili kutengeneza ajira kwa vijana, changamoto ya kuongeza mapato ya Utalii kutoka katika hifadhi zetu na kuvutia watalii zaidi katika nchi yetu.

Nimewapigia simu wateule wengi na kuwaambia, siwapi pongezi Bali nawatakia kazi njema. Nawatakia uwajibikaji mwema. Uwajibikaji ndio msingi wa kupambana na rushwa, uvivu na uzembe.

Kwa Waziri wa Fedha, ambaye mimi ni Waziri Kivuli wake (Kama Kiongozi wa Upinzani Bungeni hataniwajibisha pia), namwambia uteuzi wake ni changamoto kubwa sana katika maisha yake.

Hivi sasa eneo lenye Bajeti kubwa kuliko zote nchini ni huduma kwa Deni la Taifa (services to national debt). Lazima kuangalia upya Deni la Taifa. Hivi sasa Deni la Taifa ukijumlisha na Dhamana za Serikali (government guarantees) limefikia tshs 22trn mpaka Desemba 2011. Nimewahi kutaka ukaguzi Maalumu katika 'account' ya Deni la Taifa. Linarejea wigo huu. Tunalipa takribani 1.9trn tshs kwa mwaka kuhudumia Deni la Taifa. Zaidi ya Bajeti ya miumbombinu, Afya, Maji, Umeme nk.

Mfumuko wa Bei, misamaha ya kodi na kodi zinazozuia watanzania kujiajiri ni changamoto kubwa sana Wizara ya Fedha lazima ihangaike nayo.

Usimamizi wa Mashirika ya Umma kupitia Ofisi ya Msajili wa Hazina na hasa usimamizi wa Hisa za Serikali katika kampuni binafsi ni masuala yanayohitaji masuluhisho sasa na sio baadaye.

Kwa Mwalimu wangu Dkt. Mwakyembe, utakumbukwa kwa Jambo moja tu. RELI. 'make our Railway system work'. Hutakuwa na 'legacy' nyingine isipokuwa Reli maaana Bandari bila Reli ni sawa na Bure.

Tunatumia zaidi ya tshs 300bn kwa mwaka kukarabati barabara wakati tunahitaji tshs 200bn kukarabati Reli iweze kusafirisha mzigo kwenda Bandarini na kukupa Bandarini.

Ndio maana nasema hakuna Jambo la kusherehekea maana wajibu mliopewa na Rais ni mtihani mkubwa kwenu katika kukitumikia Taifa letu. Msipowajibika, mtakumbwa na fagio la chuma!

Mkisha kula kiapo, kimbieni kazini. Nothing to celebrate. Hit the ground running.

ZZK

Dar-es-Salaam

Jumamosi, Mei 5 2012