Sunday, May 26

Jeshi lafanikiwa kudhibiti vurugu Mtwara

Shughuli za mauzo na manunuzi zilirejea rasmi jana mjini Mtwara,
baada ya huduma hizo kusimama kwa siku tatu kutokana na
vurugu zilizotokea kuanzia Alhamisi baada ya kusomwa
hotuba ya Wizara ya Nishati na Madini na wana-
Mtwara kubaini kuwa suala lao la gesi halijapewa umuhimu unaostahili.
Picha na Abdallah Bakari  

Mtwara. Mkuu wa vikosi vya aridhini wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Meja Jenerali SM Kijuu amewahakikishia ulinzi wafanyabiashara hao, baada ya kukutana na uongozi wa Chama cha Wafanyabiashara Sokoni (Wabisoco) jana asubuhi, kufuatia wafanyabishara hao kudai kuendelea kusitisha biashara zao kwa kuhofia usalama.

Katibu wa Wabisoco, Saidi Namata ameliambia Mwananchi Jumapili kuwa wafanyabiashara hao wamekubaliana kufungua biashara zao, baada ya makubaliano ya kulinda eneo hilo na askari wa JWTZ.

“Sisi wafanyabiashara tulikuwa tayari kuendelea kusitisha huduma kutokana na hali ya usalama kuwa mbaya, alipokuja kiongozi wa jeshi na kutuhakikishia kuwa dhamana ya ulinzi itakuwa chini yao tulikubaliana,” alisema Namata

Alisisitiza: “Kama ulinzi ungekuwa mikononi mwa polisi, katu tusingefungua. Polisi wenyewe ndiyo hawa wanaovunja maduka na kuiba, kwa kuwa dhamana hii imebebwa na wanajeshi hatuna shaka, tunaomba wafanyabiashara wengine wafungue biashara zao.”

Tangu juzi magari ya matangazo yamekuwa yakipita mjini Mtwara na kuwatangazia wananchi kuendelea na kazi zao kama kawaida kwa kuwa ulinzi umeimarika, huku askari wa JKT na JWTZ waliosheheni silaha wakizunguka mitaani.

Pinda awasili Mtwara

Wakati tukiewnda mitamboni Waziri Mkuu Mizengo Pinda amewasili Mtwara jana jioni na kukutana na viongozi wa mkoa.

Bungeni Dodoma

Suala la mgawanyo wa rasilimali za taifa jana liliendelea kutikisa Bunge, baada ya baadhi yao kueleza kuwa ni haki kwa maeneo yanakotoka rasilimali hizo kunufaika kwanza kabla ya maeneo mengine.

Wakati wabunge hao wakieleza hayo, wengine wamesisitiza kuwa kwa kuwa nchi ni moja Tanzania, rasilimali zote ni mali ya Watanzania wote.

Wabunge wanaotaka rasilimali zinufaishe kwanza maeneo zinakotoka. Wanasema pamoja na ukweli kwamba Tanzania ni moja, watu hao wana haki ya msingi kupata huduma hizo kwanza kuliko wengine.

Mbunge wa Msalala (CCM), Ezekiel Maige alisema anashangaa kwa nini fomula ya rasilimali kuyaendeleza maeneo iliyopatikana, inatumika kwenye Idara ya Wanyamapori na haitumiki katika sekta ya nishati na madini.

“Wananchi walichosema rasilimali tugawane mrabaha. Zinufaishe wao kwanza. Kwenye wanyamapori, tunafanya hivyo kwa nini kwenye madini tunasema taifa litagawanyika? Alihoji.

Maige alisema Tume ya Bomani ilishauri kuwa asilimia 40 ya mapato itumike kuendeleza maeneo ilikopatikana rasilimali hizo na asilimia 60 zikaendeleze maeneo mengine, lakini ushauri huo haufanyiwi kazi.

Mbunge wa Mpanda (Chadema) Said Arfi alitaka hekima kutamalaki katika suala la mgororo wa gesi Mtwara ili taifa iendelee kuwa na hali ya amani na utulivu

“Naishauri Serikali wawashirikishe wananchi katika mambo yanayohusu mustakabali wa maendeleo yao. Elimu ya kutosha ingalikuwapo na ushirikishwa ulio mpana, tusingalifika hapa. Kadiri tunavyochelewa kulitatua tatizo hili, ndivyo tunavyorudi nyuma katika maendeleo,” alisema.

Kwa upande wake Mbunge Mlalo (CCM), Hassan Ngwilizi, alisema anaunga mkono msimamo wa Rais Jakaya Kikwete kuwa rasilimali za taifa ni mali ya Watanzania wote, hivyo ni mwafaka kwa watu kudhani kuwa wanastahili kunufaika na rasimali kwa sababu zimetoka kwao.

“Wale wote wanaofikiri kuleta chokochoko, wajue nchi hii inavyo vyombo vya dola. Kinachowatokea au kuweza kuwatokea, wajilaumu wenyewe,” alisema Ngwilizi na kusisitiza;

Hamad Ali Hamad (CUF) alisema gesi iliyopatikana Mtwara isiwe laana bali ionekane kama baraka. “Serikali ikazungumze na watu wa Mtwara na hili naomba serikali msione tunafanya jambo baya. hakuna lisilozungumzika,” alisema.

Christopher Ole Sendeka wa Simanjiro (CCM) alisema: “Amani ya Tanzania ni tunu isiyoweza kuchezewa na mtu yeyote yule na kwa sababu yeyote ile .

“Natambua kuna haja ya baadhi ya mambo wanayodai kuangaliwa kwa makini, lakini nawashauri Wanamtwara waendelee kuleta madai yao na Serikali iwasikilize kwa sababu wao ni watu wazima, hawawezi kupiga kelele hivi hivi tu,” alisema.

Ole Sendeka alitaka Waziri asikubali kuendelea kudanganywa na watalaamu wake kwa kuwa watamharibia.

“Usikubali kuuziwa mbuzi kwenye gunia,” alisema Sendeka na kuendelea, “ mwaka jana ulidanganywa na watalaamu wako ukalidanganya Bunge kuhusu nguzo za Tanesco na misumari.”

“Mwaka 2010 Rais Kikwete aliahidi kuwapa mgodi wa Tanzanite One wachimbaji wadogo lakini leo tunaambiwa wakifunga, mgodi huo utakabidhiwa kwa Stamico. Sasa Rais Ni Muhongo au Dk Jakaya Kikwete?”

Kamati yaundwa

Bunge limeunda kamati maalumu kwa ajili ya kuchunguza vurugu zilizotokana na mradi wa kusafirisha gesi, kutoka mkoani Mtwara kwenda jijini Dar es Salaam.

Spika wa Bunge Anne Makinda, alisema kamati hiyo itakayoongozwa na Mbunge wa Muleba Kaskazini, Charles Mwijage, itakuwa na hadidu nne za rejea.

Wajumbe wake ni Mbunge wa Mpanda Mjini, (Chadema) Said Arfi , Mbunge wa Sikonge (CCM), Said Nkumba, Mbunge wa Wawi (CUF) Hamad Rashid Mohamed na Mbunge wa Tunduru Kaskazini (CCM) Ramo Makani na Rukia Kassim Ahmed (CCM).

Pia wamo Dk Dalaly Kafumu (CCM-Igunga), Cynthia Hilda Ngoye (Viti Maalumu-CCM), Muhamed Chombo (CCM), Agripina Buyogera NCCR- Mageuzi, Cecilia Paresso (Viti Maalumu-Chadema), Mariam Kisangi (Viti Maalumu- CCM), Seleman Jafo (Kisarawe CCM),

Hadidu za Rejea

Spika Makinda alisema kamati hiyo ambayo hata hivyo hakuipa muda maalumu, itakuwa na jukumu la kufuatilia mambo manne muhimu yanayochangia vurugu hizo.

“Kamati itakuwa na jukumu la kujua nini chanzo cha vurugu, kujua hatua zilizochukuliwa na Serikali, kukutana na wadau mbalimbali ili kupata maoni yao na kuangalia mambo yote yenye uhusiano na vurugu hizo,” alisema.

Imeandikwa na Abdallah Bakari, Elias Msuya , Mtwara na Kizitto Noya, Dodoma. - gazeti la mwananchi