Wednesday, November 15

Zuma awasihi wanajeshi Zimbabwe kutulia


Johannesburg, Afrika Kusini. Mwenyekiti wa Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (Sadc), Rais Jacob Zuma wa Afrika Kusini amelitaka Jeshi la Ulinzi Zimbabwe kuimarisha utulivu na kujizuia kufanya mambo yaliyo kinyume cha protokali ya umoja huo.
“Rais Jacob Zuma, kwa niaba ya Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (Sadc), ametoa wito wa utulivu na kujizuia na ameelezea matumaini yake kuwa kinachofanyika Zimbabwe hakitasababisha mabadiliko ya serikali kwani itakuwa kinyume cha msimamo wa Sadc na Umoja wa Afrika,” imesema taarifa yake.
Rais ameitaka serikali ya Zimbabwe na Jeshi la Ulinzi la Zimbabwe (ZDF) kutatua mgogoro wa kisiasa kidugu na pia amelitaka jeshi kuhakikisha kwamba amani na usalama wa nchi havitetereki.
Amesema Sadc itaendelea kufuatilia kwa karibu sana hali na iko tayari kusaidia inapobidi kutatua mgogoro wa kisiasa kwa kuzingatia protokali na taratibu zilizowekwa na Sadc.
Zuma ametoa kauli hiyo baada ya askari na vifaru kuonekana jana wakiranda katikati ya jiji la Harare na ilipofika usiku zikatolewa taarifa na picha zilizoonyesha wamezingira majengo kadhaa ya serikali yakiwemo ya Shirika la Utangazaji Zimbabwe (ZBC).
Mapema alfajiri leo msemaji wa jeshi, Meja Jenerali Sibusico Moyo alitoa taarifa kupitia ZBC akisema jeshi limechukua udhibiti likilenga “wahalifu” wanaomzunguka Rais Mugabe ambao walikuwa “wakifanya uhalifu uliosababisha mateso ya wananchi kijamii na kiuchumi ili kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria.”
Katika taarifa yake hiyo, Moyo alisema Mugabe na familia yake wako “salama na wenye afya njema na kwamba ulinzi wao ni wa uhakika.”
Akisisitiza kwamba hayo hayakuwa mapinduzi, Moyo alisema “mara watakapokamilisha kazi hali itarejea kuwa ya kawaida”.
“Tunawahimiza mtulie na dhibitini mienendo isiyo ya lazima. Hata hivyo, tunawahimiza wafanyakazi na wanaojihusisha na biashara muhimu katikati ya jiji kuendelea na shughuli kama kawaida,” alisema Zuma.

COP23: Viongozi wasema wakati wa kuyaokoa mazingira ni sasa

Rais wa Ujerumani Frank-Walter Steinmeier amesisitiza kuwa nchi zilizoendelea zina wajibu mkubwa wa kuyalinda mazingira ikilinganishwa na nchi zinazoendelea na nchi ndogo za visiwani.

UN-Klimakonferenz 2017 in Bonn | Espinosa & Macron Bainimarama & Merkel & Guterres (Reuters/W. Rattay)
Rais Steinmeier amesema nchi zinazoendelea na za visiwani zinachangia kwa kiasi kidogo mno katika uchafuzi wa mazingira yanayosababisha mabadiliko ya tabia nchi lakini ndizo zinazoathirika pakubwa na kuwa katika hatari ya kuangamia kutokana na athari za mabadiliko ya tabia nchi kama vimbunga, mafuriko, joto la kupita kiasi na kina cha maji ya bahari kuongezeka ilhali sauti zao hazijapewa nafasi kubwa ya kusikika ulimwenguni.
Steinmeier ameongeza kusema kuwa makubaliano ya kuyaokoa mazingira yaliyofikiwa mjini Paris, Ufaransa, mwaka 2015 yatakuwa tu ya ufanisi iwapo yatatekelezwa kikamilifu huku akiyasifu mazungumzo ambayo yamekuwa yakiendelea hapa Bonn kwa siku kumi zilizopita kama ya tija.
Viongozi kuongoza juhudi za kuyalinda mazingira
Rais huyo wa Ujerumani anawaongoza viongozi wengine takriban 30 wa nchi mbali mbali katika mkutano huo wa kimataifa wa mazingira hapa Bonn. Kansela wa Ujerumani Angela Merkel na Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron ambao wametwishwa jukumu la kuwa manahodha wa kuuongoza ulimwengu kufikia malengo ya kuyaokoa mazingira watahutubia pia leo katika mkutano huu wa COP23.
UN-Klimakonferenz 2017 in Bonn | Steinmeier & Macron (Reuters/W. Rattay)
Rais wa Ujerumani Frank- Walter Steinmeier na wa Ufaransa Emmanuel Macron
Wanaharakati wa kuyalinda mazingira wanamtaka Merkel kuwa katika mstari wa mbele kuchukua hatua madhubuti za kupunguza kiwango cha gesi chafu ya Carbon inayotoka viwandani ambayo ni mojawapo ya vichocheo vya kuongezeka kwa joto duniani.
Ujerumani bado inazalisha kwa wingi nishati ya makaa ya mawe ambayo inachangia asilimia 40 ya umeme nchini humu na inahofiwa huenda nchi hii ikashindwa kufikia malengo yake ya kupunguza kwa asilimia 40 gesi chafu ya Carbon ifikapo mwaka 2020.
Je Ujerumani itafikia malengo yake?
Makundi ya watetezi wa mazingira yamefanya maandamano nje ya ukumbi wa mkutano wa COP23 kupinga matumizi ya makaa ya mawe Ujerumani. Ni wakati mgumu kwa Merkel ambaye anajaribu kuunda serikali ya mseto na vyama vya kijani cha walinda mazingira na cha Free Democrats FDP ambapo mojawapo ya masuala makuu yanayozua utata ni la mazingira.
Kampuni za kuzalisha nishati zimeonya kuwa nishati ya makaa ya mawe inahitajika kuhakikisha kuwa kuna kiwango cha kutosha cha nishati ya kuendesha viwanda Ujerumani, taifa imara zaidi kiuchumi barani Ulaya.
Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amesema kuendelea kuwekeza katika nishati za makaa ya mawe, mafuta na gesi kutasababisha kuangamia kwa binadamu katika siku za usoni akizitaka nchi kutowekeza kifedha katika nishati hizo zenye madhara kwa mazingira.

Tillerson yuko Myanmar kuzungumza na viongozi wa nchi hiyo

Waziri wa mambo ya nje wa Marekani Rex Tillerson yuko Myanmar atakutana na Aung San Suu Kii na pia mkuu wa jeshi Min Aung Hlaing. Tilleson atarajiwa kusisitiza kurudi Myanmar wakimbizi wa Rohigya.

Pakistan Islamabad US-Außenminister Rex Tillerson | (Reuters/A. Qureshi)
Waziri huyo wa mambo ya nje wa Marekani yuko nchini Myanmar kukutana na mkuu huyo wa jeshi la Myanmar jenerali Min Aung Hlaing. Waziri huyo wa mambo ya nje wa Marekani Rex Tillerson atakutana pia na kiongozi wa Myanmar Aung San Suu Kyi  katika ziara yake hii ya kwanza nchini humo. Viongozi hao baadae wanatarajiwa kuwahutubia waandishi wa habari. Waziri Tillerson anatarajiwa kutoa mwito wa kumaliza matumizi ya nguvu katika jimbo la Rakhine. Majeshi ya Myanmar yanalaumiwa kwa kuitendea maovu jamii ya Waislamu walio wachache ya Rohingya.
Myanmar General Min Aung Hlaing (picture-alliance/AP Photo/Aung Shine Oo)
Mkuu wa jeshi la Myanmar Jenerali Min Aung Hlaing
 Jeshi la Myanmar limekanusha vikali madai ya kukiukwa haki za binadamu za jamii ya Waislamu wa Warohingya wakati wa operesheni zilizofanywa baada ya Warohingya wenye msimamo mkali kufanya mashambulio mnamo mwezi wa Agosti. Warohingya zaidi ya laki 6 wamekimbilia nchi jirani ya Bangladesh tangu kuzuka kwa mashambulio dhidi yao.
Umoja wa Mataifa umeyaita kuwa ni mauaji ya kimbari. Afisa mwandamizi wa wizara ya mambo ya nje ya Marekani amewaambia waandishi wa habari  kwamba Tillerson anasisitiza kurudi salama nchini Myanmar kwa wakimbizi wa Rohingya. Hata hivyo haijulikani kama Tillerson atatoa vitisho vya kuwekwa vikwazo vipya dhidi ya jeshi la Myanmar.
Hivi karibuni bunge pamoja na baraza la Seneti nchini Marekani lilipitisha sheria ya kuizuia nchi hiyo kutoa msaada wa kijeshi kwa Myanmar. Sheria hiyo pia ililenga kuwawekea vikwazo vya kifedha na kuwanyima viza maafisa wa kijeshi wa Myanmar. Kaimu mkurugenzi wa shirika la kutetea haki za binadamu la Human Rights Watch Phil Robertson amesema ni vizuri kuwachukulia hatua hizo maafisa wa jeshi la Myanmar.
Myanmar Rohingya-Konflikt Aung San Suu Kyi (picture-alliance/dpa/AP)
Kiongozi wa Myanmar Aung San Suu Kyi
Taarifa iliyotolewa mapema leo inasema maelfu ya Warohingya bado wanaendelea kukimbilia nchi jirani ya Bangladesh. San Suu Kyi mwanaharakati wa muda mrefu wa demokrasia aliingia madarakani baada ya uchaguzi wa kwanza wa wazi kufanyika mwezi Novemba mwaka 2015 nchini Myanmar, lakini pia kiongozi huyo anakabiliwa na lawama za kimataifa kwa kushindwa kuutatua mzozo wa wakimbizi unaoikabili jamii ya Waislamu walio wachache wa Rohingya. Kunyamaza kwake kumemuharibia sifa ya kuwa kiongozi bora katika nyanja za kimataifa. 

Mhasibu wa Takukuru aamua kwenda kujisalimisha mwenyewe


Dar es Salaam. Aliyekuwa Mhasibu mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na  Kupambana na Rushwa (Takukuru), Godfrey John Gugai amejisalimisha katika taasisi hiyo.
Akizungumza na Mwananchi leo Novemba 15,  Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, Kamishna Valentino Mlowola amesema Gugai amejisalimisha na hatua za kisheria zinaendelea.
"Ni kweli amejisalimisha na yupo chini ya vyombo vya ulinzi na usalama na hatua zaidi za kisheria zitafuata" amesema Kamishna Mlowola
Mtumishi huyo anatuhumiwa kujipatia mali kinyume cha Sheria za Utumishi wa umma huku Takukuru wakidai kwamba kama atadhibitisha uhalali wa umiliki wake ataachiwa na akishindwa atachukuliwa hatua.
Gugai amejisalimisha ikiwa ni siku moja imepita tangu Takukuru ilipotangaza zawadi ya Sh 10 milioni kwa mwananchi yoyote ambaye angefanikisha kumtia nguvuni mtumishi  huyo.
Hata hivyo, Kamishna Molowa ameshindwa kufafanua kama amejisalimisha mwenyewe au kuna mtu katoa taarifa.

Jengo la Tanesco Ubungo kubomolewa

Dar es Salaam. Rais John Magufuli amemwagiza Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads) kuweka alama ya X kwenye jengo la Shirika la Umeme (Tanesco) na sehemu ya jengo la Wizara ya Maji na Umwagiliaji ili kupisha ujenzi wa daraja la juu katika eneo la Ubungo (Ubungo Interchange).
Rais Magufuli ametoa agizo hilo leo Jumatano baada ya kuwasili jijini Dar es Salaam akitokea Chato alikokwenda baada ya kumaliza ziara ya siku tatu nchini Uganda.
Amewataka Tanroads kuwapa taarifa wahusika kuhusu kubomolewa kwa majengo yao ili wapate eneo la kutosha kwa ajili ya ujenzi wa mradi huo unaolenga kupunguza foleni katika jiji la Dar es Salaam.
“Sasa mimi nataka ikiwezekana leo au kesho muweke X jengo la Tanesco…muweke X sehemu ile ya mwanzo ya Wizara ya Maji,” amesema Rais Magufuli huku akishangiliwa na wananchi waliojitokeza katika eneo hilo.
Kiongozi huyo Serikali amesema kwamba Sheria ya Hifadhi ya Barabara ilianza tangu mwaka 1932, ikafanyiwa mabadiliko mwaka 1959, 1964 na 1967.
“Sheria ni msumeno, Serikali ikifanya kosa inasulubiwa, Rais akijenga kwenye Road Reserve (hifadhi ya barabara) anachukuliwa hatua hizo hizo,” amesema Rais Magufuli wakati wa ziara hiyo.
Wakati wa Serikali ya Awamu ya Nne, Rais Magufuli akiwa Waziri wa Ujenzi wakati huo aliagiza kubomolewa kwa jengo la Tanesco, hata hivyo, aliyekuwa waziri mkuu, Mizengo Pinda alizuia kubomolewa kwa jengo hilo na mengine yaliyokuwa kwenye hifadhi ya barabara.

Kampuni ya Kilimanjaro yadaiwa Sh 500 milioni



Dar es Salaam. Mamalaka ya Mapato Tanzania (TRA) imesitisha utoaji wa huduma za usafiri kwa kampuni ya mabasi ya Kilimanjaro Express Limited baada ya kushindwa kulipa kodi ya Sh500 milioni.
Akizungumza na Mwananchi leo Jumatano, Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa Mlipa Kodi wa TRA, Richard Kayombo amesema wamefikia uamuzi huo baada ya majadiliano ya muda mrefu na kampuni hiyo kutokuzaa matunda.
Kayombo amesema biashara ya mmiliki huyo kwa kipindi cha hivi karibuni haikuwa nzuri kwani mabasi yake 26 yalipungua hadi kufikia 12 lakini si kigezo cha kutokulipwa kwa kodi ya Serikali.
“Ni kweli Kilimanjaro Express inadaiwa Sh500 milioni jambo ambalo lilitufanya sisi kusimamisha shughuli tangu Jumatatu (ya Novemba 13) hadi hapo atakapolipa kodi anayodaiwa,” amesema Kayombo
Kwa upande wake, mmiliki wa kampuni hiyo, Roland Sawaya amesema wamezuia mabasi yake ambayo yalikuwa yameegeshwa katika ghala mjini Moshi mkoani Kilimanjaro huku akieleza kuwa ni kweli anadaiwa lakini amekuwa akilipa deni hilo kwa awamu.
Amesema hivi karubuni alilipa Sh50 milioni na mwezi huu walitaka kulipa Sh35 milioni lakini TRA walikataa na kuwataka kulipa kiasi chote kilichobaki cha Sh500 milioni huku akieleza kwamba mazungumzo yanayoendelea ana imani yatafikia mwafaka na kurejea kutoa huduma
Kilimanjaro ambayo imekuwa ikifanya safari zake kati ya Dar es Salaam, Moshi na Arusha kwa zaidi ya miaka 20 ni kampuni tanzu ya Kilimanjaro Cargo Truck.

Walimu wajikuta wamelala nje



Buchosa. Walimu saba wanaofundisha Shule ya Msingi Soswa wilayani Sengerema wamejikuta wamelala nje pamoja na familia zao huku wawili kati yao wakiwa wamenyolewa nywele kichwani na sehemu za siri.
Mwalimu wa Shule ya Msingi Soswa, Petro Lukas amesema tukio hilo limetokea usiku wa kuamukia leo Jumatano ambapo walimu hao walipokuwa wamelala ndani ya nyumba zao na walipotahamaki usiku walijikuta wamelala nje.
Amesema palipokucha walimu hao walizinduka na kutokuamini kilichotokea na walipoingia ndani ya nyumba zao walikuta damu zimetapakaa vyumbani na sebuleni pia vibuyu vikiwa vimevalishwa shanga nyeupe vikiwa kitandani na chini kitendo kiliwafanya kuhaha kuomba msaada kwa jamii inayowazuguka.
Mwalmu Lukas amesema kati ya walimu hao wawili wameathirika zaidi na tukio hilo na kwa kupata mshituko ambao ni Wape Kisumo aliyenyolewa nywele kichwani pmaoja na Daud Shule ambaye alinyolewa nywele sehemu za siri.
Kutokana na mshtuko huo Kisumo alipelekwa kituo cha afya cha Mwangika kwa matibabu na mwalimu Shule yeye anaendelea na matibabu ya tiba na hali zao zinaendelea vizuri.
Mganga Mkuu Halmashauri ya Buchosa, Dk Ernest Chacha amekiri kumpokea mwalimu Kisumo katika kituo cha afya Mwangika na kwa sasa anaendelea kupatiwa matibabu na baada ya uchunguzi wa kitaalamu kukamilika watatoa taarifa lakini alipofika kituoni alikuwa haongei ila baada ya kupatiwa huduma ya kwanza ameanza kuongea kidogo.
Akizungumzia mkasa huo mwalimu Shule amesema kuwa wao baada ya kupata chakula cha usiku walilala ndani nyumba zao na ilipofika usiku wa manane wakasikia mwalimu mwenzao Wape Kisumo akilia na kulalamika kichwa kinamuuma.
Amesema walipotahamaki walijikuta wakiwa nje watupu na kuona kuwa wamedhalilishwa na kitendo hicho hivyo wanaiomba Serikali iwasaidie kumaliza tatizo hilo.
Mmoja wa wananchi wa Kisiwa cha Soswa, Sumari Diplospa amesema kitendo hicho kinapaswa kukemewa kwa kuwa walimu hao wanasaidia kufundisha watoto wao.
Ofisa Mtendaji wa Kata ya Bulyaheke Musa Mwilomba amesema kuwa tukio hilo ni tatu kutokea  katika shule hiyo ambapo mwaka jana mwezi nne walimu walipondwa mawe nyumba zao wakiwa wamelala.
Pia Mei 5 mwaka huu nyumba za walimu zilipondwa tena mawe na usiku wa kuamkia leo wamejikuta wamelala nje na baadhi yao kunyolewa nywele sehemu za siri kitendo ambacho kinapaswa kukemewa.
Kwa upande wake Ofisa Elimu Msingi Halmashauri ya Buchosa, Magareth Kapolesya amesema amepata taarifa ya tukio hilo na kusikitishwa na kitendo hicho na wao kama wasimamizi wa elimu watalishughulikia na kupata ufumbuzi juu ya suala hilo kwa kuwa linawanyima raha walimu na kukosa morali ya kufundisha.

Zuma asema Mugabe yuko kizuizini Zimbabwe


Johannesburg, Afrika Kusini. Rais Robert Mugabe wa Zimbabwe amewekwa kizuizini na Jeshi la Ulinzi usiku wa kuamkia jana katika mji mkuu wa Harare, Rais wa Afrika Kusini, Jacob Zuma amethibitisha.
Zuma alisema jana kwamba alipigiwa simu na Mugabe mwenyewe. Taarifa kutoka ofisi ya Zuma ilisema: "Rais Zuma alizungumza na Rais Robert Mugabe mapema leo na amedokeza kwamba anazuiliwa nyumbani kwake lakini alisema yuko salama."
Kuanzia Jumanne wanajeshi walionekana wakivinjari na kupiga doria katikati ya Harare, baada ya kuteka kituo cha televisheni cha Shirika la Utangazaji la Zimbabwe (ZBC) kwa kile kilichoelezwa wanawalenga “wahalifu”.
Hatua hiyo ya jeshi inaweza kuwa ni mpango wa kumwondoa Mugabe na kumweka katika nafasi hiyo makamu wake aliyefukuzwa kazi wiki iliyopita Emmerson Mnangagwa, shirika la BBC limeripoti.
Ofisa mmoja wa jeshi, Meja Jenerali Sibusiso Moyo alionekana kwenye televisheni baada ya kukiteka kituo hicho akisema Mugabe na familia yake wako “salama na afya njema na ulinzi wao ni wa uhakika ".
Meja Jenerali Moyo alisema, “Sisi tunawatafuta wahalifu waliomzunguka yeye (Mugabe) ambao wanafanya uhalifu na kusababisha machungu ya kijamii na kiuchumi nchini.”
"Mara tutakapokuwa tumekamilisha operesheni hii, tunatarajia kwamba hali itarudi kuwa ya kawaida."
Kufukuzwa kazi kwa Mnangagwa wiki iliyopita kutengeneza njia kwa mke wa Rais Mugabe, Grace kuteuliwa katika nafasi hiyo hivyo kuwa na matumaini ya kuteuliwa kuwa mrithi wa kiti cha mumewe.
Milio mizito ya bunduki ilisikika kaskazini mwa mji wa Harare hadi jana alfajiri.

Muswada wa Fao la kujitoa kusomwa bungeni


Dodoma. Hatima ya Fao la Kujitoa ambalo limekuwa kilio cha muda mrefu cha wafanyakazi, sasa iko mikononi mwa Bunge wakati Serikali itakapowasilisha Muswada ya kuiunganisha Mifuko ya Hifadhi ya Jamii.
Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG),George Masaju ameliambia Bunge leo Novemba 15 kwamba  Muswada wa kuiunganisha Mifuko hiyo, utasomwa kwa mara ya kwanza katika mkutano wa Bunge unaomalizika kesho kutwa.
Kwa mujibu wa AG Masaju, suala la Fao la Kujitoa litafikiriwa katika Muswada huo wa Sheria, na kama suala hilo halitakuwamo kwenye Muswada huo, basi wabunge ndio watakaoamua.
Masaju ametoa  kauli hiyo wakati akijibu hoja ya Mbunge wa Temeke (CUF), Abdalah Mtolea, aliyehoji kwanini Serikali imewasilisha marekebisho mepesi ya sheria, wakati Fao la Kujitoa ni kilio kikubwa.
Mtolea aliibua suala hilo wakati akichangia Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria mbalimbali  namba 4 wa mwaka 2017, uliowasilishwa Bungeni na AG Masaju na kupitishwa na bunge hiyo jana.
Mbunge huyo amesema walitarajia Serikali ingeleta Muswada wa kuiunganisha Mifuko ya Hifadhi ya Jamii, kama ambavyo Rais John Pombe Magufuli, ameonyesha kukerwa na utitiri wa mifuko hiyo.
“Vitu vingi ambavyo tumetegemea Serikali ingevileta hapa hawajavileta wameleta vitu vyepesi vyepesi. Mheshimiwa Rais kila siku anapiga kelele kwamba ana kerwa na utitiri wa hii mifuko,” alisema.
“Amelisema hili (Rais) mara kadhaa na AG ndio watu wa kumsaidia Rais katika kuhakikisha wanaharakisha mchakato wa kupunguza hii mifuko ya hifadhi uwe mmoja au miwili,”
Amesema tangu Rais atoe kauli hiyo, ana taarifa kuwa Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii (SSRA), imefanya tafiti na kufanya maandalizi ya kuwasilishwa kwa Muswada huo.
“Tulitarajia muswada huo unaletwa leo hapa mambo hayo hayapo. Kila siku waheshimiwa wabunge hapa wanapiga kelele kuhusu fao la kujitoa,” amesema Mbunge huyo na kuongeza
“Wananchi wanapiga kelele wanalalamika kwanini wananyimwa fursa ya kujitoa kwenye mifuko ya Jamii hadi watimize miaka 55.  Wachukue fedha zao waende wakafanye shughuli nyingine”.
“Mtu ameshafanya kazi miaka yake 10 anaona kwamba kilichopo kwenye mifuko ya Jamii kinamtosha kufanya mtaji. Kinamtosha kutengeneza kiwanda chake unamzuia”
“Miaka 55 ni muda wa uzee ni muda wa kula mafao na muda wa kupumzika. Tunataka fedha sasa hivi ili tuweze kuwekeza ili wakifika miaka hiyo 55 wawe wameshakuwa matajiri”
Hata hivyo akijibu hoja hiyo, AG Masaju alisema alichowasilisha ni marekebisho ya sheria ya Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi na sio Muswada wa Marekebisho ya mifuko ya Hifadhi ya Jamii.
“Kwenye masuala makubwa ya kisera yanayoletwa na muswada mahsusi sio unaoletwa na AG kwa ajili ya marekebisho ya sheria ambazo zimeleta shida katika utekelezaji wake”.
“Nishauri hata hii hoja ya kwamba ingetegemewa ingekuja hapa muswada mahususi kwa ajili ya kuunganisha mifuko ya Hifadhi ya  Jamii, hii nayo isingeweza kuletwa kwenye muswada huu”
“Imekuwepo mifuko mingi wewe mwenyewe umesema kwamba ni ya utitiri, unaileta yote pamoja unaunganishwa upi na upi  na utakuja na skimu gani,” amesema na kuongeza;
“Naomba kushauri Bunge lako tukufu kuwa katika mkutano huu wa Bunge  wa Bunge linaloendelea sasa, muswada huu wa  mfuko wa Hifadhi utasomwa kwa mara ya kwanza kwenye bunge hili”
“Pamoja na mambo mengineyo utahusika pia na hiyo hoja ambayo ameisema ya Fao la kujitoa itakuwa considered (litafikiriwa ) wakati huo. Kama haitakuwamo mtaamua nyinyi wenyewe wabunge”.
 “Serikali inafanya kazi kwa makini sana na naomba kuwashukuru wabunge nyinyi kuweni imara, kuweni macho muisaidie Serikali na kuishauri lakini mutoe ushirikiano mzuri kwa Serikali.
“Hii ya sheria inayounganisha mifuko ya Hifadhi ya Jamii itasomwa kwa mara ya kwanza katika mkutano huu wa bunge lako linaloendelea,” amesisitiza Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
Suala la Fao la Kujitoa, limekuwa likiibuka karibu kila mkutano wa Bunge, huku baadhi ya vyama vya wafanyakazi navyo vikitishia kuchukua hatua za kisheria endapo Fao hilo la Kujitoa halitarejeshwa.
Juzi suala hilo liliibuka tena Bungeni, lakini Naibu Spika, Dk Tulia Ackson akasema kwa anavyofahamu kwa sasa na kwa msimamo wa sheria, Fao la Kujitoa lilishafutwa na sheria.

Madai yafanya mhadhiri azuie matokeo ya wanachuo

Chuo kikuu cha Mount Meru kilichopo Ngaramtoni mkoani Arusha kimeingia katika mgogoro na mhadhiri wa wake, Naiman Solomon baada ya kushindwa kumlipa stahiki zake na hivyo kuzuia matokeo ya wahitimu wa Stashahada  Ualimu na Uongozi.
Akizungumza na waandishi leo Jumatano, Solomon amesema licha ya kuzuia mitihani hiyo uongozi wa chuo hicho umegushi matokeo ya mitihani ya wahitimu jambo ambalo ni makosa kisheria.
"Kutokana na mgogoro huu nimemwandikia Waziri wa Elimu, Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, TCU na Necta, kuelezea mgogoro huo  wa kugushi  matokeo ya wanafunzi wa Stashahada ya Ualimu  na Uongozi ya Chuo Kikuu cha Mount Meru kutokana na ukiukwaji wa taratibu za kutolewa kwa matokeo chuoni hapo," amesema.
Akizungumzia hilo kaimu makamu mkuu wa chuo hicho, Utawala na Fedha, Twazihirwa Mzava amesema kuwa  uongozi wa chuo hicho ulilazimika kuwapatia matokeo wanachuo hao nje ya taratibu baada ya mhadhiri kutokuwasilisha matokeo ya mitihani hiyo kwa uongozi wa chuo kutokana na  kudai stahiki zake ambazo alikuwa hajalipwa.
Mzava amesema  mhadhiri  Solomon hakuwasilisha matokeo kwa sababu anadai stahiki zake kwa kipindi kirefu na hiyo inatokana na ukata unaokikabili chuo hicho.

Ridhiwani, Msigwa wavutana bungeni


Dodoma. Mbunge wa Chalinze (CCM), Ridhiwan Kikwete na Mbunge wa Iringa Mjini (Chadema), Peter Msigwa, leo Jumatano, wamerushiana maneno bungeni kila mmoja akionyesha ubabe wa kutunga sheria.
Hayo yalijitokeza wakati Bunge lilipoketi kama kamati chini ya mwenyekiti wa Bunge, Najma Murtaza Giga kupitia vifungu vya muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali wa 2017.
Muswada huo ambao ulichangiwa na wabunge wawili tu,mmoja wa CCM na mwingine kutoka kambi ya upinzani uliwasilishwa bungeni na Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), George Masaju.
Hali hiyo ilijitokeza baada ya Mbunge wa Viti Maalum (Chadema), Ruth Mollel kushikilia msimamo wa kuwepo usawa wa kijinsia katika muundo wa bodi ya mfuko wa fidiwa kwa wafanyakazi.
AG Masaju alipendekeza bodi hiyo na iwe na wajumbe tisa wakiwamo wawakilishi wawili wawili wanaowakilisha vyama vya waajiri vyenye wanachama wengi kwenye mfuko huo wa fidia.
Pia alipendekeza wajumbe wawili wawili wanaowakilisha vyama vya wafanyakazi vyenye wanachama wengi kwenye mfuko na wakili wa Serikali kuanzia ngazi ya mwandamizi atakayemwakilisha AG.
Wajumbe wengine ni mwakilishi wa wizara yenye dhamana ya Hifadhi ya Jamii, Mwakilishi wizara ya Fedha, mwakilishi wizara ya Tumishi wa Umma na mwakili wa Jumuiya ya watu wenye ulemavu.
Hata hivyo, Mollel aliwasilisha jedwali la marekebisho, akipendekeza muundo huo uzingatie jinsi ya kike badala ya kuliacha suala hilo katika utashi wa mtu mmoja ambaye atakuwa anateua.
Pamoja na AG Masaju kueleza madhara ya kuingiza kifungu cha aina hiyo katika sheria, bado mbunge huyo alisimama katika msimamo wake na kutoa hoja kuwa Bunge lijadili suala hilo.
Ndipo mwenyekiti alipomruhusu Ridhiwan kuchangia na aliposimama alisema yeye amesimama sio kuunga mkono hoja ya Mbunge huyo bali kutoa maoni yake kuhusiana na uandishi wa sheria.
“Sina hakika sana kama mama yangu (Ruth) ni mwanasheria. Katika uandishi wa sheria nchi hii hakuna sheria inayoandikwa kwa kuzingatia gender (jinsi). Hilo la kwanza tuelewane,”alisema.
“Unapoweka kipengele chochote kile kwamba iwe kipengele hiki kimzungumzie mtu huyu awe mwanamme ni tayari kuna mtu (mwanamke) umeshambagua,”alisisitiza na kuongeza;-.
“Unaposema kipengele hiki kiwe mwanammke maana yake kuna watu tayari umeshawatenga. Kinachotakiwa ni busara ya wale wanaoteua sio jambo la kuandika gender,”
Hata hivyo, Mchungaji Msigwa alipopewa fursa alisema itakuwa ni makosa makubwa kutoingiza kipengele hicho na kurudi nyuma kwenye historia ya jinsi mwanamke alivyofanywa kama “object”.
“Ni wakati sasa hivi wa wanawake kuamka ili kuhakikisha mnatetea haki zenu ili tufikie kiwango kile cha  50-50 hata tunapotunga sheria. Mfano mzuri ni ile sheria inayomlazimisha Rais kuteua wabunge”.
Mchungaji Msigwa alisema sheria hiyo inamlazimisha Rais kuteua angalu nusu ya wabunge wawe wanawake na kuna wakati Rais John Magufuli alighafulika na kuteua wabunge wengi wanaume.
Hali ndani ya ukumbi wa Bunge ilikuwa kama ifuatavyo:
Ridhiwan: Mwenyekiti Taarifa
Msigwa:Hatutoagi taarifa kwenye kuchangia
Ridhiwani: Leo ndio unapewa taarifa hapa leo. Wanataka kutuyumibisha bwana. Hatuwezi kuyumbishwa bwana sisi tunatengeneza sheria.
Msigwa: Hata mimi natengeneza sheria
Ridhiwani: Hakuna namna hiyo Msigwa bwana. Hatuwezi kutunga sheria ambazo ziko biased (zina pendelea)
Mwenyekiti wa Bunge: Waheshimiwa wabunge. Naomba mkae nyinyi nyote wawili Naomba mkae  wote wawili. Mheshimiwa AG Tuendelee.
Ridhiwan: Sie tumesoma sheria bwana
Mwenyekiti wa Bunge: Mheshimiwa Stella Manyanya (Naibu Waziri wa Elimu)
Stella Manyanya: Kwanza nataka kumuambia Bwana Msigwa . Si vyema kutumia vibaya kumtaja mheshimiwa Rais kwa mambo ambayo sio lazima sana. Kwa mfano kumwambia alimuondoa mbunge”
Naibu Waziri huyo alimtaka Mchungaji Msigwa asipitilize katika suala hilo akisema kama Mbunge alijiuzulu mwenyewe ni vyema akasema hivyo, kuliko kusema Rais ndiye aliyemuondoa.
AG Masaju alipopewa kuchangia mjadala huyo alianza kwa kusema,“namshukuru sana mheshimiwa Ridhiwan Kikwete ametusaidia kuweka suala hili vizuri. Ukirudi kwenye uandishi wa sheria”
“Tunayo sheria ya kwanza kabisa inayoitwa sheria ya tafsiri ya sheria. Yenyewe ndio msingi wa tafsiri ya sheria zote  na ndio muongozo wa kutafsiri sheria,”.
“Mbona kwenye sheria inasema HE (mwanamme) lakini wanawake wamo humo ndani. Tunao muongozo mahsusi unaotuongoza katika kuandika sheria,”alisisitiza Masaju.
Mollel alipopewa fursa ya kuhitimisha hoja yake, alisema amesikitishwa sana na jinsi hoja hiyo ilivyochukuliwa akisema yeye akiwepo serikalini waliweka utaratibu wa usawa kwa wote.
Mwenyekiti aliamua suala hilo liamuliwe kwa kura, ambapo baada ya kuwahoji wanaoafiki hoja ya Mbunge huyo waseme Ndioo na wasioafiki waseme Sioo, waliosenda Sioo wakashinda.
Muswada huo ulipitishwa na Bunge kuwa Sheria na sasa unasubiri sahihi ya Rais Magufuli ianze kutumika.

Wezi wachimba njia ya chini kwa chini na kuiba pesa kwenye benki India

A view inside the 25ft tunnel that the thieves dug
Image captionWezi walichimba njia hiyo kwa miezi kadha
Wezi katika mji wa Mumbai magharibi mwa India walitekeleza wizi kwenye benki moja inayomilikiwa na serikali baada ya kuchimba njia ya chini kwa chini ya urefu wa futi 25 (mita 8).
Walichimba njia hiyo kwa miezi kadha.
Polisi wameambia BBC kwamba pesa taslimu pamoja na vito vya thamani isiyojulikana viliibiwa.
Maafisa wanaamini kwamba wezi hao walikodisha chumba karibu na Benki ya Baroda kuwawezesha kuchimba njia hiyo.
Wanadaiwa kuendesha biashara ya kuuza mboga na matunda katika kiduka chao kuficha mipango yao.
Wezi hao walitoweka tangu Jumamosi usiku baada ya kutokea kwa wizi huo.
Polisi wanaamini wezi hao walikodisha duka karibu na benki hiyoHaki miliki ya pichaANUSHREE FADNAVIS
Image captionPolisi wanaamini wezi hao walikodisha duka karibu na benki hiyo
Haijabainika ni vipi wanaume hao walifanikiwa kuchimba njia hiyo kwa miezi kadha bila kugunduliwa.
Vyombo vya habari nchini India vimezungumza na wateja wa benki hiyo ambao vitu vyao vya thamani viliibiwa.
"Akiba yangu yote ilikuwa imewekwa kwenye sefu. Vito ambavyo tumemiliki kwa vizazi kadha, vimeibiwa," Dagdu Gavani, mmoja wa wateja aliambia Mumbai Mirror.
Wafanyakazi wa benki hiyo iliyo viungani mwa mji wa Mumbai waligundua wizi huo Jumatatu na kuwafahamisha polisi.
Polisi wameambia BBC kwamba sefu 30 kati ya 225 kwenye benki hiyo ziliporwa.
Washukiwa bado hawajatambuliwa.
Benki ya Baroda humilikiwa na serikaliHaki miliki ya pichaANUSHREE FADNAVIS
Image captionBenki ya Baroda humilikiwa na serikali

Mugabe azuiliwa na wanajeshi nyumbani kwake na wanajeshi Zimbabwe

Young women walk past an armoured personnel carrier in Harare, 15 NovemberHaki miliki ya pichaAFP
Image captionWanajeshi wanashika doria barabara za mji mkuu Harare
Jeshi nchini Zimbabwe linamzuilia Rais Robert Mugabe kwake nyumbani katika mji mkuu wa nchi hiyo Harare, Rais wa Afrika Kusini Jacob Zuma amesema.
Bw Mugabe alimwambia bw Zuma kwa njia ya simu kwamba yuko salama, kwa mujibu wa taarifa kutoka kwa afisi ya Zuma.
Wanajeshi wanashika doria katika barabara za Harare baada ya kuchukua udhibiti wa runinga ya taifa katika kile walichosema ni juhudi za kuwaandama "wahalifu".
Hatua hiyo huenda ikawa juhudi za kutaka kumuondoa madarakani Bw Mugabe na badala yake kumuingiza madarakani makamu wake wa rais Emmerson Mnangagwa, ambaye alimfuta kazi wiki iliyopita, waandishi wa BBC wanasema.
Kufutwa kwa Bw Mnangagwa wiki iliyopita kulikuwa kumemuweka mke wa Rais Mugabe, Grace, katika nafasi nzuri ya kumrithi.
Bw Mugabe, 93, ameongoza taifa hilo tangu lilipojipatia uhuru mwaka 1980 kutoka kwa Uingereza.
Wanajeshi nchini Zimbabwe walichukua udhibiti wa kituo cha taifa cha utangazaji usiku na milipuko mikubwa ilisikika pamoja na ufyatuaji wa risasi usiku kucha mjini Harare.
Jenerali mmoja wa jeshi alitokea kwenye runinga na kusisitiza kwamba hakujatekelezwa mapinduzi ya kijeshi.
Alisema Rais Robert Mugabe na familia yake "wako salama salimini."
Harare
Nini kimetokea?
Kuna taarifa kwamba wanajeshi wanatumia vifaru na magari ya kivita kufunga barabara karibu na majengo ya bunge mjini Harare na pia nje ya makao makuu ya chama tawala cha Zanu-PF.
Awali, milipuko pamoja na milio ya risasi vilisikika kaskazini mwa mji huo mkuu. Milio ya risasi ilisikika pia karibu na makao ya kibinafsi ya Rais Mugabe, 93.
Wanajeshi wanadaiwa kuingia katika makao makuu ya runinga ya taifa ZBC, na Meja Jenerali Sibusiso Moyo alisoma taarifa kwenye runinga ya taifa.
Alilihakikisha taifa kwamba Bw Mugabe na familia yake wako salama na kusisitiza kwamba usalama wao umehakikishwa.
Jeshi lilisema linawaandamana tu wale aliosema ni "wahalifu" wanaomzingira rais.
Alikanusha kwamba kumekuwepo na mapinduzi ya kijeshi.
Wanajeshi wakiwa na magari ya kivita viungani mwa Harare, Zimbabwe jana Novemba 14,2017Haki miliki ya pichaREUTERS
Image captionWanajeshi wakiwa na magari ya kivita viungani mwa Harare, Zimbabwe Jumanne
Jumatano asubuhi, akaunti ya Twitter ambao inajidai kuwa ya Zanu-PF ilisema kulikuwa kumetokea "ubadilishanaji wa mamlaka bila umwagikaji wa damu".
Zimbabwe Army Gen Constantino Chiwenga, commander of the Zimbabwe Defence Forces (R), and Valerio Sibanda, commander of the Zimbabwe National Army address a media conference held at Zimbabwean army headquarters in Harare on MondayHaki miliki ya pichaAFP
Image captionMaafisa wakuu katika jeshi wamekuwa wakilalamika kuhusu yaliyokuwa yakijiri nchini humo karibuni
Muda mfupi awali, akaunti hiyo ilikuwa imesema "familia ya rais" ilikuwa inazuiliwa, lakini tuhuma hizi hazikuthibitishwa.
Jumanne, maafisa wa Zanu-PF walimtuhumu mkuu wa majeshi Jen Constantino Chiwenga kwa "vitendo vya uhaini" kwa kukosoa hatua ya Rais Mugabe ya kumfuta kazi makamu wa rais Emmerson Mnangagwa wiki iliyopita.
Zanu-PF alisema msimamo wa Jen Chiwenga ulikuwa "na nia wazi ya kuvuruga amani ya taifa ... na unaashiria vitendo vya uhaini kwa upande wake na tamko lake lilikuwa na nia ya kuchochea maasi".
Jumatatu, Jenerali Chiwenga alitishia kwamba operesheni ya kuwaondoa wanaompinga rais katika chama tawala inafaa kusitishwa la sivyo jeshi lingeingilia kati.
Nini hakijatokea?
Hakujakuwa na tamko lolote kutoka kwa serikali kuhusu yanayojiri - jambo ambalo linaashiria kwamba huenda ni kweli Mugabe na watu wake hawana udhibiti tena wa serikali, wachanganuzi wanasema.
Na kwa sasa hakuna taarifa zozote kwamba kikosi cha Walinzi wa Rais, ambacho humtii Bw Mugabe, kimeingilia kati.
Iwapo walinzi wake wangeingilia kati, bila shaka kungekuwa na umwagikaji wa damu.
Haya ni mapinduzi ya kijeshi?
Ni hatua ambayo imetajwa kama "ya kubahatisha sana" na mwandishi wa BBC anayeangazia kusini mwa Afrika Andrew Harding.
Anasema ni muhimu kukumbuka kwamba Bw Mugabe sasa hatishiwi na nchi za magharibi ambazo amekuwa akiwaonya raia wake dhidi yake kwa miongo mingi, au na wanasiasa wa upinzani nchini Zimbabwe au hata na maasi ya raia kutokana na hali ngumu ya kiuchumi.
Robert Mugabe (R) na Grace Mugabe 9 Novemba 2017Haki miliki ya pichaAFP
Image captionMajaribio ya Bw Mugabe kumuweka mkewe katika nafasi ya kumrithi imewakera wengi katika Zanu-PF na katika jeshi
Na kwa mujibu wa Harding, mzozo wa sasa umetokana na mvutano wa ndani ya chama cha Zanu-PF. Atakayeibuka na ushindi anaweza kutarajia kwamba chama, baada ya kutakaswa, kitamfuata.
Kwenye hotuba yake kupitia runinga, Meja Jen Moyo alisema angependa ieleweke wazi kwamba "jeshi halijatwaa udhibtii wa serikali, Tunajaribu kutatua mzozo wa kisiasa, kijamii na kiuchumi katika taifa letu."
Amesema nchi hiyo itarejea katika hali ya kawaida hivi karibuni baada ya jeshi kutimiza alichosema ni "lengo" lake.
Nini kimechangia hatua ya sasa?
Robert Mugabe na Emmerson Mnangagwa during celebrations marking his birthday at the Great Zimbabwe monument in Masvingo on 27 February 2016Haki miliki ya pichaAFP
Image captionMakamu wa rais Mnangagwa na Robert Mugabe walipokuwa bado marafiki Februari 2016
Bw Mugabe anapoendelea kuzeeka na kupoteza udhibiti wa nchi yake, macho yote yamekuwa yakiangazia nani atamrithi.
Inaonekana kana kwamba hatua ya jeshi imechochewa na kufutwa kwa makamu wa rais Emmerson Mnangagwa wiki iliyopita.
Amekuwa ndiye mpinzani mkuu kwa Grace Mugabe, mume wa Rais Mugabe ambaye ni mdogo wake kwa miaka arobaini.
Bw Mnangagwa ni wa kizazi cha wazee ambao waliongozwa vita vya ukombozi nchini Zimbabwe miaka ya 1970 na kuchangia uhuru wa Zimbabwe kutoka kwa Uingereza mwaka 1980 ambapo Mugabe aliongoza akiwa waziri mkuu na baadaye kama rais.
Maj Gen Sibusiso Moyo speaking on ZBC, 15 November 2017
Image captionMeja Jenerali Sibusiso Moyo
Kundi hilo la wazee linapingwa na kizazi cha vijana wanaojiita "Generation 40" au "G40", kundi la wanasiasa wa Zimbabwe wanaomuunga mkono Grace Mugabe.
Hatua wazi ya Bw Mugabe ya kupendelea wanasiasa wa kizazi hiki inaonekana kuwa iliyowakera viongozi wa jeshi, wachanganuzi wanasema.