Wednesday, July 19

Jaji Upendo Msuya afariki dunia



Dar es Salaam. Aliyekuwa Jaji wa Mahakama Kuu ambaye amejiuzulu  hivi karibuni, Upendo Msuya amefariki leo Julai 19 baada ya kuugua kwa muda mrefu ugonjwa wa kiharusi.
Akizungumza na Mwananchi kwa njia ya simu, mjomba wa marehemu, Niva Mbaga amesema kwamba marehemu amefariki akiwa Hospitali ya Kairuki alipokuwa amelazwa.
Amesema kwamba shughuli za mazishi zinafanyika nyumbani kwa marehemu Tegeta jijini Dar es Salaam.
“Amesumbuliwa kwa muda mrefu na ugonjwa wa kiharusi hivyo akawa anapelekwa hospitali na kurudi nyumbani zaidi ya miezi mitatu sasa na leo hii amefariki dunia’’ amesema Mbaga
Amesema marehemu ameacha watoto wanne.







Kenyatta: Hakuna kuahirisha uchaguzi Kenya

 


Nairobi. Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta amesema kwamba uchaguzi utafanyika mwezi ujao kama ulivyopangwa licha ya wapinzani kuweka vikwazo.
Akizungumza katika eneo la Ukunda, Kwale, Rais Kenyatta amesema ni lazima uchaguzi ufanyike Agosti 8 kama ulivyopangwa.
“Nimegundua upinzani hauko tayari kwa uchaguzi tangu mwaka jana walipoanza kushambulia Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC),” amesema.
Rais Kenyatta akiwa ameandamana na naibu wake William Ruto amesema.’Hatutaruhusu kuahirishwa kwa uchaguzi’.
“Tunatangaza kwamba Wakenya watachagua viongozi wawapendao Agosti 8 ili waendelee na shughuli zao za kila siku,” amesema.
Viongozi hao wa Jubilee wamedai Muungano wa National Super Alliance (Nasa) hauko tayari kwa uchaguzi bali unahitaji kunyakua mamlaka kupitia 'mlango wa nyuma’.
Upinzani wamedai mbele ya Mahakama Kuu kwamba, tume ya IEBC imeshindwa kuzingatia sheria inayoitaka kutangaza mbinu mbadala zitakazotumiwa endapo mitambo ya kielektroniki itakwama.

Profesa wa CCM ndiye meya Dodoma



Dodoma. Madiwani wa Manispaa ya Dodoma leo wamemchagua Diwani wa Kuteuliwa (CCM), Profesa Devis Mwamfupe kuwa meya wa manispaa hiyo baada ya kumgaragaza Diwani wa Kikombo (Chadema), Yona Kusaja kwa kura 50.
Msimamizi wa uchaguzi huo ambaye pia ni Mkurugenzi wa Manispaa ya Dodoma, Godwin Kunambi amemtangaza Mwamfupe kuwa meya baada ya kupata kura 50 huku Kusaja akiambulia kura nane kati ya kura 58 zilizopigwa katika uchaguzi huo ulioshuhudiwa na Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Christina Mdema na kamati yake ya ulinzi na usalama.
Uchaguzi huo umefanyika baada ya Jaffary Mwanyemba kuondolewa katika uongozi kwa tuhuma za ubadhirifu wa fedha za mradi wa maji katika kata ya Zuzu na matumizi mabaya ya madaraka.







Mtandao waitangaza Tanzania nchi bora kwa utalii Afrika




David Beckham
David Beckham 
Dar es Salaam. Wakati idadi ya watu maarufu kutoka nje ya nchi wanaokuja kutazama vivutio vya utalii nchini ikiongezeka, mtandao wa   kimataifa wa kibiashara umeitangaza Tanzania kuwa nchi ya kwanza Afrika inayowavutia zaidi watalii.
Mtandao huo, SafariBookings.com ulifanya uchambuzi kwa kuchukua maoni ya watalii zaidi ya 2,500 waliotembelea nchi za Afrika na idadi kubwa waliitaja Tanzania kuwa bora kuliko nchi nyingine.
Hii ni mara ya pili kwa mtandao huo wa Marekani  kuitaja Tanzania kama nchi ya kwanza inayowavutia zaidi watalii. Mara ya kwanza ilikuwa 2013.
Sifa kubwa iliyoipa hadhi ya juu Tanzania ni kuwa na eneo kubwa lenye wanyamapori na misitu. Nchi nyingine zilizoshika nafasi ya juu ni Zambia na Kenya.
 Wakati mtandao huo ukiitaja Tanzania kuwa eneo bora la utalii, watu maarufu kutoka mataifa makubwa duniani wameendelea kumiminika nchini wakitembelea  hifadhi za Taifa na vivutio vingine.
 Miongoni mwa watu maarufu waliotembelea vivutio hivyo ni pamoja na mwanamuziki wa Marekani, Usher Raymond na mcheza soka maarufu David Beckham aliyewahi kuchezea timu ya Taifa ya England na timu za Manchester United na Real Madrid.
Mara baada ya kutembelea vivutio hivyo, Usher aliweka picha za ‘matanuzi’ aliyopata akiwa Tanzania, katika mitandao yake ya kijamii ya Twitter na Instagram.
Usher alikuwa ameongozana na familia yake wakiwamo watoto wake wawili wa kiume katika Hifadhi ya Serengeti.
“Safari hii imekuwa ya maajabu, tumefurahi sana kuona uzuri wa mbuga hii nikiwa na familia yangu,” ameandika katika ukurasa wake wa Twitter.
Si hao tu, watu wengine maarufu waliofika ni mcheza filamu wa Marekani, Will Smith na familia yake na mchezaji wa zamani wa timu ya Liverpool, Mamadou Sakho.
Pia, mchezaji wa Everton Morgan Schneiderlin alitembelea vivutio hivyo hivi karibuni akiwa fungate.
Wiki hii, msanii maarufu wa filamu za Bolywood, India, Sanjay Dutt naye aliwasili kwa ajili ya kutembelea vivutio hivyo.
Shirika la Hifadhi za Taifa (Tanapa) limesema kazi kubwa inayofanywa na shirika hilo kutangaza vivutio vya utalii duniani ndiyo iliyozaa matunda hayo.
Msemaji wa Tanapa, Paschal Shelutete alisema lengo lao ni kufikia watalii milioni tatu ifikapo mwaka 2020. Alisisitiza kwamba Tanapa inatathmini namna ya kuwatumia watu mashuhuri wanaotembelea nchini kujitangaza zaidi kimataifa ili kufikia lengo hilo.
Alipoulizwa namna wanavyoitumia fursa ya watu hao mashuhuri kutembelea nchi, Mkurugenzi wa Masoko wa Bodi ya Utalii Tanzania (TTB), Phillip Chitaunga alisema,  “Hili ni jambo ambalo kwetu tunalichukulia kwa mapana yake kwa sasa.”
Akizungumzia vivutio vilivyopo nchini, mwandishi wa habari za usafiri na utalii wa Marekani, Tim Bewer alisema, “Tanzania ina Mbuga nyingi nzuri kama Serengeti na Ngorongoro, wanyama watano bora, simba wapandao miti, kikubwa ni ubora wa hifadhi hizo ambazo zimetumia robo tatu ya ardhi yake kuhifadhi wanyamapori.”
Pia, mtaalamu wa masuala ya safari na utalii na raia wa Uingereza, Phillip Biggs amekaririwa na jarida mtandao la Huffpost akisema, “Hakuna majadiliano, hakuna nchi ya Afrika, kusema ukweli, yenye wanyama wakubwa katika eneo kubwa kama Tanzania.”

Siri ya Mlima Mbeya kushika mkia matokeo kidato cha sita yaanikwa





Dar es Salaam. Siri ya Shule ya Sekondari ya Mlima Mbeya kushika mkia katika matokeo ya mtihani wa kidato cha sita imewekwa hadharani na mkuu wa shule hiyo iliyoko mkoani Mbeya, Atuganile Bwile akisema baadhi ya wanafunzi walikuwa na nidhamu mbovu.
Katika matokeo yaliyotangazwa na Baraza la Mitihani Tanzania (Necta), Jumamosi iliyopita mjini Zanzibar, Mlima Mbeya ni miongoni mwa shule 10 zilizofanya vibaya.
Orodha hiyo inajumuisha shule za Chasasa ya Pemba, Kiembesamaki (Unguja), Mwenyeheri Anuarite (Dar es Salaam), Ben Bella (Unguja), Meta na Mlima Mbeya (Mbeya), Njombe (Njombe), Al-Ihsan Girls (Unguja), St Vincent (Tabora) na Hagafilo (Njombe).
Bwile alisema baadhi wanafunzi walikuwa watoro na wengine walikuwa wakichagua mada za kusoma akitoa mfano wa baadhi waliokuwa wakisoma Kemia ambao walimueleza mwalimu wao husika kwamba mada anayofundisha ni ngumu hivyo hawataijibia mtihani. “Nimehamia shule hii nina miezi mitatu tu sasa, hawa wanafunzi walishindikana. Walikuwa wakiingia darasani wanavyotaka, huku wakiwa wamenyoa viduku. Nililazimika kuwabadilisha kitabia baadhi yao ndiyo maana tukaweza kupata hata daraja la kwanza mwanafunzi mmoja,” alisema.
Alisema daraja la pili wamefaulu wanafunzi  watano, la tatu 29, la nne 28 na sifuri ziko sita tofauti na matokeo ya mwaka jana ambayo hayakuwa na mwanafunzi aliyepata daraja la kwanza.
Bwile alisema kingine kilichosababisha matokeo mabaya ni kuwa walipokaribia kufanya mitihani, wanafunzi walifanya vurugu baada ya wenzao watatu kusimamishwa masomo kutokana na utovu wa nidhamu wakidai kwamba wenzao wameonewa ilhali uamuzi huo ulifikiwa na kikao cha walimu. Alisema vurugu hizo zilisababisha polisi kutumia mabomu ya machozi kuwatuliza.
Hata hivyo, ofisa mmoja wa idara ya elimu mkoani Mbeya alisema walimu wa shule hiyo wanafundisha chini ya kiwango.
Ofisa huyo ambaye hakutaka jina lake litajwe gazetini alisema alishaenda shuleni hapo zaidi ya mara mbili na kubaini kiwango cha ufundishaji kipo chini na kushauri yafanyike marekebisho, ushauri ambao alisema haukuzingatiwa.
“Wanafunzi kutokuwa na nidhamu kumesababishwa na walimu wenyewe kwa kufundisha chini ya kiwango,” alisema.

Manji apatiwa matibabu gerezani

Mfanyabiashara Yusufali Manji 
Dar es Salaam. Mfanyabiashara Yusufali Manji (41) bado anaumwa na anatibiwa katika Hospitali ya Magereza Keko.
Hayo yameelezwa leo na Wakili wa Serikali Mwandamizi, Nassoro Katuga, mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi wakati kesi yake na wenzake watatu ilipotajwa.
Katuga aliiambia mahakama kuwa upelelezi bado haujakamilika na akaomba kesi hiyo ipangiwe tarehe nyingine. Kesi hiyo imeahirishwa hadi Agosti 4, 2017.
Katika kesi hiyo, Manji na wenzake wanakabiliwa na mashtaka saba chini ya sheria ya uhujumu uchumi na usalama wa Taifa kwa kukutwa na vitambaa vinavyotengeneza sare za Jeshi la Wananchi wa Tanzania vyenye thamani ya zaidi ya Sh 200 milioni pamoja na mihuri.
Washtakiwa wengine katika kesi hiyo ni Deogratius Kisinda(28), Abdallah Sangey(46) na Thobias Fwere (43).
Awali, akiwasomea hati ya mashtaka inayowakabili washtakiwa hao, Wakili wa Serikali, Tulumanywa Majigo amedai kuwa Juni 30,2017 katika eneo la Chang’ombe ‘A’wilaya ya Temeke Dar es Salaam washtakiwa hao kwa pamoja wamekutwa na askari polisi wakiwa na mabunda 35 ya vitambaa vinavyotumika kushonea sare za Jeshi la Wananchi Tanzania zenye thamani ya Sh 192.5milioni na kwamba mali hiyo ilipatikana kinyume cha sheria.
Katika shtaka la pili, Wakili Majigo alidai kuwa Julai Mosi, 2017 huko Chang’ombe ‘A’ washtakiwa hao walikutwa na polisi wakiwa na mabunda manane ya vitambaa vinavyotumika kushonea sare za Jeshi la Wananchi Tanzania zenye thamani ya Sh44 milioni mali ambayo ilipatikana isivyo halali.
Katika shtaka la tatu, washtakiwa hao kwa pamoja wanadaiwa kuwa Juni 30, 2017 Chang’ombe ‘A’ walikutwa na muhuri wa Jeshi la Wananchi Tanzania wenye maandishi ‘Mkuu 121 kikosi cha JWTZ’ bila ya kuwa na uhalali kitendo ambacho kingehatarisha usalama wa nchi.
Wakili Majigo katika shitaka la nne, anadai kuwa Juni 30, 2017 kwenye eneo hilo la Chang’ombe ‘A’ Manji na wenzake hao watatu walikutwa wakiwa na muhuri wenye maandishi’ Kamanda Kikosi 834 KJ Makutupola Dodoma bila ya kuwa na uhalali kitendo ambacho kingehatarisha usalama wa nchi.
Shitaka la tano, Manji na wenzake hao wanadaiwa kuwa Juni 30, 2017 huko Chang’ombe ‘A’wamekutwa na muhuri wa Jeshi la Ulinzi la Tanzania wenye maandishi (Commanding Officer 835 KJ Mgambo P.0. Box 224 Korogwe) kitendo ambacho kingehatarisha usalama wa nchi.
Katika shtaka la sita, washtakiwa hao kwa pamoja wanadaiwa kuwa Julai Mosi, 2017 katika eneo hilo la Chang’ombe ‘A’ walikutwa na askari polisi wakiwa na namba za usajili SU 383 ambayo ilipatikana kwa njia isiyo halali.
Kwenye shtaka la saba washtakiwa hao wanadaiwa kuwa Julai Mosi, 2017 kwenye eneo hilo la Chang’ombe ‘A’ washtakiwa hao walikutwa na skari polisi wakiwa na namba za usajili wa gari SM 8573 ambayo ilipatikana kwa njia isiyo halali.
Baada ya kusomewa mashtaka hayo, washtakiwa hawakuruhusiwa kuongea chochote kwa sababu Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu haina mamlaka ya kuisikiliza kesi hiyo.
Manji na wenzake wanatetewa na mawakili Hudson Ndusyepo, Malimi Seni na Emmanuel Safari. 

Samia azindua ripoti ya tamthmini



Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan
Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan 
Dar es Salaam. Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan amezindua rasmi ripoti ya nchi ya kujitathmini yenyewe ambayo utekelezaji wake unaendelea.
Akizungumza kabla ya uzinduzi huo leo Julai 19, Mama Samia amesema Serikali imetekeleza mapendekezo 25 kati ya 92 yaliyotolewa kwenye ripoti hiyo na kusisitiza kwamba itatekeleza mapendekezo yote.
Amewataka wadau mbalimbali kuendelea kufadhili utekelezaji wa ripoti hiyo ambayo inalenga nyanja mbalimbali za uchumi na utawala bora.
"Serikali imeshatoa maelekezo kwa watendaji kuandaa ripoti za kila mwaka juu ya utekelezaji wa mapendekezo yaliyobainishwa kwenye ripoti. Tutaendelea kusimamia utekelezaji wake mpaka mwisho," amesema Mama Samia.
Makamu wa Rais amesema ripoti hiyo ina mchango mkubwa katika kufikia azma ya serikali ya kuwa nchi ya viwanda kwa sababu imebainisha pia mbinu za kuinua uchumi.
Ametaja baadhi ya mambo yaliyofanyiwa kazi kuwa ni kutatua migogoro ya ardhi, kuongeza uzalishaji na usambazaji wa umeme, kuboresha mfumo wa elimu, kusimamia suala la jinsia na kupiga vita rushwa.

Mghwira: Lowassa Kuhamia Chadema Ufisadi wa Kisiasa

Moto wa Uchaguzi Mkuu wa 2015 ulishazimika lakini kuna kila dalili kwamba majivu yake bado hayajapoa na moja ya dalili za kuwapo kwa hali ya uvuguvugu ni kauli ya hivi karibuni ya Anna Mghwira dhidi ya Edward Lowassa kwamba njia aliyotumia kugombea urais ilikuwa ni aina nyingine ya ufisadi.

Katika uchaguzi huo, Mghwira ambaye sasa ni Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, alikuwa mwanamke pekee aliyegombea urais na kwa mujibu wa matokeo yaliyotangazwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), alishika nafasi ya tatu nyuma ya Lowassa akipata kura 98,763 sawa na asilimia 0.65 ya kura zote.

Lowassa,  aliyekuwa Waziri Mkuu wa kwanza katika Serikali ya Awamu ya Nne, katika uchaguzi huo aliwania kiti hicho kupitia Chadema akiungwa mkono na vyama vilivyoungana chini ya Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa)na alipata kura 6,072,848 sawa na asilimia 39.97 ya kura zote. Dk John Magufuli aliibuka mshindi kwa kupata kura 8,882,935 sawa na asilimia 58.46.

Juni 3, Mghwira aliteuliwa na Rais Magufuli kuwa Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro wakati huo akiwa mwenyekiti wa ACT –Wazalendo na muda mfupi baadaye chama hicho kikamuondoa katika nafasi hiyo kutokana na uteuzi huo.

Katika mahojiano maalumu na gazeti hili wiki hii, Mghwira alisema njia aliyoitumia Lowassa kugombea urais ilikuwa ni aina nyingine ya ufisadi wa kisiasa kwa kuwa hakupitishwa na chombo chochote ndani ya chama chake.

Alidai kuwa hata katika kampeni, Ukawa haukuzungumzia ajenda ya ufisadi baada ya waziri mkuu huyo wa zamani kujiunga Chadema.

“Kwenye kampeni 2015 chama kikuu cha upinzani (Chadema) hakikuwa kinazungumzia tena ufisadi labda kwa hofu kwamba mshutumiwa mmojawapo wa ufisadi ndio alikuwa mgombea wao. Kwa bahati mbaya ni wao walioibua tuhuma hizo za ufisadi. Lakini kuondoka Dk Slaa (Wilbroad aliyekuwa katibu mkuu wa Chadema) nako kulileta tatizo ambalo watu hawakutaka kulifuatilia.

“Ni tatizo watu walitakiwa kuuliza alikuwa (Dk Slaa) na sababu ya msingi ya kuondoka? Ameondoka kwa nini? Anaenda wapi na anaenda kufanya nini. Ilikuwa ni ajabu kwamba kiongozi ambaye unataka uje kuwa mfano wa demokrasia, unaingia kugombea nafasi kubwa kama hiyo ya urais bila kuchaguliwa na chombo chochote cha chama,” alisema.

Mghwira aliendelea kujiuliza maswali kuhusu hatua hiyo ya Lowassa, “Umeingiaje? Inatokeaje?” Kisha alihitimisha, “Hiyo ni aina nyingine tena ya ufisadi wa kisiasa. Lowassa kama anataka kujisafisha vizuri kisiasa aangalie sana angeweza kufika mbali kama angetumia njia sahihi.”

Mghwira ambaye ni kiongozi wa kwanza wa upinzani kushika wadhifa wa ukuu wa mkoa tangu kurejea kwa mfumo wa vyama vingi vya siasa mwaka 1992, alisema, “Njia iliyotumiwa na Chadema si tu kwamba inarudisha nyuma siasa zetu lakini haikutoa picha nzuri ya uwepo wa demokrasia ndani ya upinzani. Hili lilikuwa doa kubwa kwa Mzee Lowassa.”

Uteuzi wa Lowassa kugombea urais kupitia Ukawa ulishuhudia Dk Slaa aliyetajwa sana wakati huo kuwa mgombea wa nafasi hiyo , akijiuzulu siasa na kwenda kuishi nje ya nchi.

Mbali na Dk Slaa, aliyekuwa mwenyekiti mwenza wa Ukawa, Profesa Ibrahim Lipumba naye aliamua kuikimbia CUF aliyokuwa mwenyekiti wake kabla ya kurejea baadaye na kutambuliwa na ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa jambo lililozua mgogoro mkubwa ndani ya chama hicho hadi sasa.

Alikerwa kuvuliwa uenyekiti

Katika mahojiano hayo yaliyofanyika nyumbani kwake Shanty Town mjini Moshi, Mghwira alikumbuka karaha aliyoipata baada ya furaha ya kuaminiwa na Rais na kupewa wadhifa huo.

Alisema kama si ubabaishaji wa kisiasa Tanzania, asingeondolewa kwenye uenyekiti wa ACT-Wazalendo.

“Changamoto niliyokutana nayo ACT-Wazalendo kama mwenyekiti ni kukosa wigo sahihi wa kisiasa kwa sababu kama tungekuwa tunafanya siasa sahihi, nisingeondolewa uenyekiti,” alisema.

Mghwira alisema, “Naapishwa tu kuwa RC (mkuu wa mkoa) kesho yake naondolewa tena tukiwa tumepanga kukutana kwenye kikao na mpaka leo hatujawahi kukutana.

“Nimesoma kwenye magazeti kuwa mrithi wa Mghwira kutembelea mikoa saba, yaani na mrithi ameshapatikana. Hizo si siasa, huo ni ubabaishaji. Ubabaishaji wa kisiasa Tanzania ni tatizo,” alisema.

Aliongeza, “Sisi kina mama tukisimama imara tunaweza kuondoa dhana hii ya siasa za ubabaishaji. Ni siasa za kipuuzi kabisa. Mmekubaliana mkutane muongee, hamuongei wenzako wanakaa pembeni. Umechaguliwa na mkutano mkuu unaondolewa na kamati ndogo. Watu 370 karibu 400 hivi walikuchagua, siku ya kuondolewa unaondolewa na watu watatu au wawili au mmoja. Hiyo si siasa ni dalili tosha kuwa hakuna siasa.”

Alisema mbaya zaidi ni kuwa watu wanaokuondoa hawakutumwa na mkutano mkuu, wala hawakukaimishwa na kamati kuu.

Hakuna upinzani nchini

Baada ya kujumuisha yote hayo na hasa alivyotimuliwa kwenye uongozi, mkuu huyo wa mkoa akawa na jibu moja kuhusu siasa za upinzani, “Hakuna siasa za upinzani, bali zilizopo ni za kurudishana nyuma maendeleo.

“Siasa ni kitu kizuri kwa maana ya ile mijadala, kubadilishana mawazo na kuzungumzia masuala ya itikadi, mipango ya kijamii... hakuna hiki kitu Tanzania.”

Badala yake alisema, “Tumeweka siasa kama ni uhasama kati ya chama tawala kilichoshinda kihalali na vyama hivi vingine. Kila siku watu wanatafuta makosa ya wenzao (Serikali) hata kama inafanya vizuri. Hiyo sio siasa.

“Vyama vya upinzani hapa hatuendeshi siasa. Awali, chama chochote kitakachoibuka na siasa inayoeleweka kinaweza kutawala nchi hii kwa miaka 100 ilimradi tu kitoke na siasa inayoeleweka.”

Mghwira alisema, “Vikitokea vyama vitatu vinaendesha siasa inayoeleweka tunakuwa mahali pazuri zaidi. Kwa maana kwamba wale wakiongea jambo lao, hata kama hawatawali, mtawala asikie na kuthamini.

“Sisi hapa Tanzania kuna aina ya siasa za kudidimizana. Kwa sisi wanawake wanaharakati tunaziita PhD (pool her down). Unavutwa tu chini hutakiwi kukua. Nchi haiwezi kwenda kwa staili hii.”

Alisisitiza, “Kuna watu wanafikiri kwamba ili kitu kiwe sahihi ni lazima wao wakifanye (upinzani) lakini kikifanywa na watu wengine hakiko sahihi. Hiyo ni kutokuwa mwanasiasa. Kuwa mwanasiasa si kugombana ni kuwa na uwezo wa kujenga hoja, kuitetea na kuisimamia. Mwenzako akija na hoja kubwa zaidi kubali.”

Changamoto za ugombea urais

Mghwira alisema wakati akigombea urais alikumbana na changamoto mbili, moja ikiwa ni ya nchi na nyingine ni ya yeye kutojiandaa kugombea.

“Changamoto zangu binafsi sizijali sana kwa sababu sikuwa nimejiandaa kugombea urais. Ingawa sikushinda urais, lakini nilishinda hatua ya kushiriki kwenye kampeni. Nilishinda ndiyo maana hata Rais Magufuli ameona na akaniteua kuwa RC. Kushinda kwenye kampeni ni kushiriki na kutoka ukiwa umewaachia watu kitu.

“Nafikiri nimeacha hicho kitu. Kila mtu ana ushindi wa viwango vyake. Yeye (Rais Magufuli) alishinda ushindi halisi wa kura na nafasi lakini hajanyima nafasi, amegawa,” alisema na kuongeza kuwa kinachobaki ni kushirikiana ili kuijenga nchi.

“Kuna watu wanasema nilishindwa, sikushindwa kwa sababu sikuenda kushinda, bali nilienda kushiriki. Uchaguzi unashiriki kwanza, ukishashiriki wananchi ndio wanaamua nani ni mshindi.

“Kura zikishahesabiwa na akapatikana mshindi, mnarudi kuijenga nchi. Kuna wapinzani wa Magufuli ndani ya chama chake, nao wamo kwenye Serikali na tuko nao pamoja. Hao ni wabaya zaidi kuliko mimi kwa sababu mimi namkubali kwa asilimia 100 wao wanamkubali sehemu kwa sababu wanatoka chama kimoja. Wanajua mambo yao ndani ya chama yalikuwaje,” alisema.

Alisema wanaotoka upinzani wanaweza kuwa na ufanisi mzuri na uhusiano mzuri zaidi wa kikazi na Rais kwa sababu hawana masilahi ya kisiasa.

“Sina masilahi ya kisiasa CCM ila ACT-Wazalendo. Kama nina masilahi ya kisiasa kwenye chama changu hicho hakimdhuru yeye wala hakiharibu kazi yangu huku kwa sababu mimi na yeye tunahusiana kikazi tu,” alisisitiza.

ACT-Wazalendo ni CCM B?

Alipoulizwa kuhusu dhana iliyoanza kujengeka kuwa huenda ACT-Wazalendo ni tawi la CCM na ndiyo maana Rais ameteua wanachama wake wawili kushika nyadhifa kubwa serikalini alisema hilo si kweli.

Alisema katika kuunda Serikali ya mseto, ukitaka kwenda vizuri huchukui sana wale watu mnaopingana mno kwa kuwa mtapingana tu kila siku.

“Lazima uchukue watu ambao mnaendana katika utendaji kazi. Hata ACT-Wazalendo sidhani ana maanisha atachukua kila mtu...”

Mbali na Mghwira, Rais Magufuli amemteua aliyekuwa mshauri wa chama hicho, Profesa Kitilla Mkumbo kuwa katibu mkuu wa Wizara ya Maji na Umwagiliaji.

Uteuzi ambao uliibua mijadala katika mitandao ya kijamii baadhi wakipongeza na wengine wakishutumu, huku baadhi ya wana-CCM wakinuna.

WAZIRI UMMY MWALIMU APONGEZA WASICHANA WALIOFAULU MTIHANI WA KIDATO CHA SITA (2017)


Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy A. Mwalimu (Mb), anatoa pongezi za dhati, kwa wanafunzi wote waliofaulu mtihani wa kidato cha Sita kwa mwaka 2017, ambapo kiwango cha ufaulu wa matokeo ya kitaifa kimepanda kwa asilimia 0.59 ikilinganishwa na mwaka 2016, huku watoto wa kike wakiongoza kwa ubora mwaka huu.

Waziri Ummy amempongeza Sophia Juma wa shule ya Sekondari Mazinde juu (Tanga) kwa kushika nafasi ya kwanza, sanjari na Agatha Julius Ninga wa shule ya Wasichana Tabora ambaye ameshika nafasi ya pili kitaifa.

Kadhalika, Waziri Ummy amewapongeza wanafunzi wote wa kike kwa jitihada walizoonesha na kuweza kufaulu mitihani yao kwa kiwango cha asilimia 97.21 ya waliofanya mtihani; ikilinganishwa na asilimia 95.34 ya wavulana waliofaulu. Waziri ameeleza kufarijika na juhudi ya wanafunzi wa kike, kufuatia ufaulu wa daraja la kwanza hadi la tatu kupanda kwa asilimia 94.07 katika madaraja haya ikilinganishwa na wavulana waliofaulu kwa asilimia 93.49. Juhudi hizi sio za kubezwa, na ni ishara thabiti kuwa mtoto wa kike akipewa nafasi hakika anaweza.

Wizara inatambua ushirikiano wa walimu, wazazi, na jamii ambao wamewezesha kufikiwa kwa ubora wa ufaulu wa watoto wa kike. Juhudi zenu zimesaidia utekelezaji wa azma ya Serikali ya Awamu ya Tano ya kutoa fursa sawa kwa watoto wa kike na wa kiume katika kupata haki ya elimu. Mhe.Ummy amewasa watoto wa kike wa shuleni mbalimbali nchini kutafakari matokeo ya mwaka huu ili kuwa chachu ya kujitambua na kujikinga na mimba shuleni. Kama wanafunzi wa kike watajitambua watasoma kwa ari kubwa kwa manufaa yao na Taifa kwa ujumla.

Niwatake watoto wote wa kike waelewe kuwa wamehitimu daraja moja, hata hivyo bado wanalojukumu la kujiendeleza zaidi katika taaluma mbalimbali kama njia ya kumwezesha mtoto wa kike na mwanamke kuchangia katika maendeleo ya taifa kwa umahiri mkubwa.

YANGA YAUNDA KAMATI MPYA YA MASHINDANO, MAGID "KABURU' APEWA UENYEKITI




Makamu Mwenyekiti wa Yanga  Clement Sanga Pamoja na uteuzi wa wa Mwenyekiti na Wajumbe wapya watakaounda  Kamti ya Mashindano ya Klabu hiyo kwa ajili ya msimu mpya wa 2017/18.

Makamu Mwenyekiti Clement Sanga amemrejesha Magid Suleiman ambaye atakuwa Mwenyekiti akisaidiwa na makamu Mustapha Urungu huku wakiteuliwa wajumbe wapya 10.

Sanga atafanya kikao cha kwanza na  kamati hiyo  siku ya jumamosi Saa 4 asubuhi, Makao Makuu ya klabu,jijini Dar es Salaam.

MEYA WA JIJI LA DAR AFANYA ZIARA KITUO CHA MABASI UBUNGO


 Mstahiki Meya wa Jiji la Dar es Salaam Isaya Mwita akizungumza na wafanyabiashara wa Stendi ya Mabasi Ubungo,wajumbe wa Kamati ya Fedha na uchumi ya Halmashauri ya Jiji alipofanya ziara ya kushtukiza katika kituo cha mabasi ubungo jana,kushoto ni Kaimu Mkurugenzi wa Jiji.
 Mstahiki Meya wa Jiji la Dar es Salaam Isaya Mwita akiwasikiliza Askari Polisi wa Ubungo alipofanya ziara ya kushtukiza jana katika kituo cha mabasi yaendoyo mikoani. katikati Mwenye Shati jeupe ni Diwani wa kata ya segerea ambaye pia ni mjumbe wa Kamati ya fedha na uchumi ya Halmashauri ya Jiji, Patrick Asenga.wa kwanza kushoto ni Meneja wa Kituo cha mabasi ubungo Iman Kasagara.
  Meneja wa Kituo cha mabasi Ubungo , Iman Kasagara akizungumza na waandishi wa habari leo mara baada ya Mstahiki Meya wa Jiji la Dar es Salaam Isaya Mwita na Kamati ya fedha na Uchumi walipofanya ziara ya kushtukiza katika kituo cha mabasi Ubungo.
 Mstahiki Meya wa Jiji la Dar es Salaam Isaya Mwita akizungumza na waandishi wa habari jana alipofanya ziara ya kushtukiza ya kutembelea kituo cha mabasi ubungo. 
 Mbunge wa Jimbo la Ubungo, ambaye pia ni Mjumbe wa Baraza la Madiwani la Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam akizungumza na waandishi wa habari jana kwenye ziara iliyofanywa na Mstahiki Meya wa Jiji la Dar es Salaam na Kamati ya fedha ya jiji.

CHUNGULIA FURSA BODA TO BODA


Kituo Kikuu cha Mabasi, Dodoma
Bw. Justin Kisoka, Mtumishi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ambaye amebobea katika masuala ya uchumi akitoa somo namna vijana wa Kitanzania watakavyoweza kuuza bidhaa zao ndani ya soko la Afrika Mashariki lenye nchi sita na idadi ya watu wanaofikia milioni 165. 
Mfanyabiashara akielezwa namna bidhaa zake ambazo amezibeba kichwani atakavyoweza kuziuza katika nchi za Afrika Mashariki na kupata faida kubwa.

Ujumbe wa kutaka vijana na Watanzania kwa ujumla wazinduke ili wanufaike na soko la Afrika Mashariki ulifikishwa kwa njia tofauti ikiwemo sanaa ya maigizo.

Baadhi ya watu waliojitokeza kupata mbinu za kufanya biashara ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki. Hapa ilikuwa Kituo Kikuu cha Mabasi mjini Dodoma.


Gandhi Hall , Mwanza 

Bw. Justin Kisoka akiwa kwenye bustani ya Gandhi Hall mjini Mwanza akitoa somo namna Wanamwanza watakavyoweza kuuza Sato, Sangara na bidhaa nyingine katika soko la Afrika Mashariki.

Wanamwanza acheni woga, vukeni mipaka ya Tanzania kuuza bidhaa zenu, ni baadhi ya maneno aliyokuwa anayatumia Mchumi huyo katika kuwashajihisha vijana wachangamke kuvuka mipaka ya Tanzania kuuza bidhaa zao.

Dada somo limemkolea anapata maelezo zaidi kutoka kwa wataalamu wa Wizara ili shughuli ya kuvuka mipaka ianze mara moja.


Viwanja vya Furahisha, Mwanza
Bw. Abel Maganya, Mtaalamu wa Masuala ya Afrika Mashariki kutoka Wizara ya Mambo ya Nje akitoa somo kwenye viwanja vya  furahisha. 

Serikali za Nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki zinatimiza majukumu yake kwa kuweka mazingira mazuri ikiwemo sheria, kanuni na miundombimu ili wanajumuiya mfanye biashara katika nchi unayopenda bila bugdha. Msijifungie ndani vukeni mipaka kupeleka bidhaa mbalimbali.

Baadhi ya Wananchi waliojitokeza katika viwanja vya furahisha.

Mzee anasema somo limengia barabara hivyo na  uzee wangu nawahimiza wajukuu zangu kufanya biashara ya kuvuka mipaka. Anafikisha ujumbe wake kwa kushiriki kusakata dance linalohimiza biashara za kuvuka boda.