Monday, January 16

Kikwete, Pinda waongoza waombolezaji kwa Mtema


RAIS Jakaya Kikwete jana alikuwa miongoni mwa mamia ya watu wa kada mbalimbali waliokwenda Tabata, Chang’ombe, Dar es Salaam kuifariji familia ya marehemu Regia Mtema aliyefariki juzi katika ajali ya gari eneo la Ruvu, Pwani. Mbali na Rais Kikwete, wengine waliofika msibani hapo kutoa pole ni Spika wa Bunge, Anne Makinda; Waziri Mkuu, Mizengo Pinda na mkewe Tunu na Mwenyekiti wa Chadema na Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe.

Marehemu Mtema ambaye alikuwa Mbunge wa Viti Maalumu (Chadema), alifariki juzi wakati akitokea Dar es Salaam kuelekea mkoani Morogoro. Jana katika msiba huo, msemaji wa familia, Canutte Mtema alisema ibada ya kuuaga mwili wa marehemu itafanyika leo katika Kanisa Katoliki Parokia ya Segerea kuanzia saa 9:00 alasiri.

Alisema kesho, mwili wa marehemu Mtema utaagwa katika Viwanja vya Karimjee, Dar es Salaam kisha kusafirishwa kuelekea Ifakara, ambako atazikwa Jumatano. Mbali ya viongozi, viongozi mbalimbali wa vyama vya siasa wakiwemo wabunge walifika msibani hapo kuwapa mkono wa pole kwa wafiwa wakiwemo Baba wa marehemu, Estelatus Mtema na mama yake, Catherine Kilaule.

Rais Kikwete atoa neno Akitoa pole kwa wafiwa, Rais Kikwete alisema Marehemu Mtema amefariki akiwa bado kijana mdogo na aliitaka familia kuwa na uvumilivu kwani kila mtu ana siku na mkataba wake na Mungu. Marehemu Mtema amefariki akiwa na umri wa miaka 32. “Poleni sana, tupo pamoja katika msiba. Nasi tutaangalia eneo gani tutaweza kuwa pamoja,” alisema Rais Kikwete.

Spika na wabunge Kwa upande wake, Spika Makinda alisema Bunge limepoteza mbunge kijana ambaye alikuwa na hulka kipekee. Alisema marehemu alikuwa na uwezo mkubwa wa kujenga hoja licha ya ugeni wa kazi bungeni. Kutokana na msiba huo, Spika Makinda alisema Kamati ya Uongozi ya Bunge itakaa na kupanga taratibu za jinsi ya kushiriki msiba huo ikiwa ni pamoja na kuchagua wawakilishi wa Bunge watakaokwenda katika mazishi.

“Tunasikitika kuondokewa na mbunge kijana Regia, alikuwa mchapakazi hodari na alikuwa na marafiki wengi bila kujali itikadi za vyama na kikubwa zaidi, alikuwa anakubali kukosolewa,” alisema Spika.

Mbunge wa Ubungo, John Mnyika alisema chama na Bunge kwa ujumla vimepata pigo kubwa kwa kuondokewa na marehemu Mtema. Alisema kutokana na uzito wa msiba huo, wabunge wote wa Chadema watashiriki mazishi yake huko Ifakara. Mnyika alisema wabunge wa chama hicho wameshaanza kuwasili kwa ajili ya msiba huo.

Aliyejeruhiwa asimulia
Mmoja wa majeruhi saba, Rogers Abdallah alisema ingawa ameruhusiwa, bado ana maumivu makali kifuani na kitu kibaya zaidi hakupata kipimo cha X-Ray... “Nimeruhusiwa lakini sikufanyiwa X-Ray, nina maumivu kifuani na ninashukuru nimetoka mzima nafikiri mkanda niliokuwa nimefunga umenisaidia,” alisema. Kati ya majeruhi hao, sita wameruhusiwa kutoka hospitalini isipokuwa mama mdogo wa marehemu, Bernadeta Mtema ambaye bado yupo katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH).

Kilombero kwazizima
Wakazi wa Wilaya ya Kilombero humo wamezipokea kwa masikitiko na majonzi makubwa taarifa za kifo cha mbunge huyo. Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Haji Mponda, Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Kilombero, Francis Miti, Mbunge wa Jimbo la Kilombero Abdu Mteketa, Mwenyekiti wa Halmashauri Ramadhani Kiombile, Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Kilombero, Abdallah Kambangwa na viongozi mbalimbali walifika nyumbani kwa marehemu kwa maandalizi ya mazishi.

Wakati hali ikiwa hivyo nyumbani kwake, ofisini kwa mbunge huyo nako kulikuwa na shughuli mbalimbali za maandalizi ya mazishi na viongozi wa Chadema na wanachama wa chama hicho, walikusanyika ili kuunda kamati maalumu itakayoshughulikia mazishi hayo.

Akizungumzia msiba huo, Dk Mponda alisema: “Namfahamu vizuri marehemu ukizingatia sisi wabunge wa wilaya hizi mbili za Kilombero na Ulanga tupo karibu sana katika ushirikiano bila kujali itikadi zetu na marehemu alikuwa makini katika kutetea wananchi punde anaposikia matatizo,” alisema Dk Mponda.

Kwa upande wake, Mteketa alisema: “Unajua nilikuwa nashirikiana naye vizuri sana tofauti na baadhi ya wananchi walivyokuwa wanadhani kutokana na sisi kuwa vyama viwili tofauti na ndiye aliyekuwa akinipa changamoto zaidi ili niweze kutekeleza ahadi zangu kwa wakati kwa wananchi walionichagua.”

Naye Kiombile alisema msiba wa Regia ni pengo kubwa ndani ya wilaya ya Kilombero hasa ikizingatiwa kwamba alikuwa mbunge kijana kama alivyo yeye na mara kwa mara alikuwa akimpigia simu ili kumpa ushauri naye kupokea ushauri kutoka kwake. Kambangwa alisema mbunge huyo alikuwa mwanasiasa kijana aliyekuwa akijali zaidi maslahi ya wananchi aliokuwa akiwaongoza na hakufuata itikadi za chama chake pekee.

Rafiki wa karibu wa marehemu Regia, Amina Simbamkuti alisema amempoteza mtu wa karibu aliyeshirikiana naye katika kutatua kero mbalimbali za wananchi. Mbunge huyo alifariki dunia baada ya gari alilokuwa akiendesha kupinduka saa 5:30 asubuhi karibu na Shule ya Sekondari Ruvu.

Habari hii imeandikwa na Joseph Zablon na Shakila Nyerere Dar na Venance George, Morogo

Ahadi ya Rais Kikwete kuhusu umeme utata mtupu


AHADI iliyotolewa na Rais Jakaya Kikwete ya kupatikana kwa megawati 3,000 za umeme huenda isitekelezwe katika muda uliopangwa kutokana na kutofanyika kwa maandalizi ya kutosha.Akilihutubia Taifa kuukaribisha mwaka 2012, Rais Kikwete alisema tatizo la umeme nchini litakuwa historia katika muda wa miezi 18 ijayo kutokana na mpango wa Serikali wa kusafirisha gesi kutoka Mtwara hadi Dar es Salaam.

“Maombi yetu kwa Serikali ya China ya kupata mkopo wa kujenga bomba la kusafirisha gesi kutoka Mtwara na mtambo wa kuchakata gesi inayotoka Songosongo yamekubaliwa,” alisema Kikwete katika hotuba yake ya Desemba 31, mwaka jana na kuongeza:“Utekelezaji wake unatarajiwa kuchukua miezi 18 na gesi itakayoletwa inaweza kuzalisha mpaka Megawati 3,000 za umeme. Baada ya hapo kasi ya kuongeza umeme itakuwa kubwa zaidi na tatizo la upungufu wa umeme linaweza kuwa historia.

”Hata hivyo, imebainika kuwa hadi sasa Serikali ya Tanzania na China hazijasaini mkataba wa kifedha ili kupata mkopo wa Dola bilioni moja za Marekani (karibu Sh1.6 trilioni) ambazo zitatumika kugharamia ujenzi wa bomba hilo, hivyo kuzua wasiwasi iwapo ujenzi wa bomba hilo utakamilika katika muda uliopangwa.Makubaliano ya awali ya ujenzi wa bomba hilo yalisainiwa China Septemba 26, 2011 na Tanzania ikiwakilishwa na Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja.

Baadaye ilisainiwa mikataba mingine midogomidogo lakini, kikwazo hadi sasa ni mkataba wa fedha.Waziri wa Fedha na Uchumi, Mustafa Mkulo alisema hadi mwishoni mwa wiki jana, mkataba wa kifedha ulikuwa bado haujasainiwa lakini akasema taarifa alizonazo ni kwamba utasainiwa hivi karibuni.“Kweli bado hatujasaini mkataba huo ila niko informed (nina taarifa) kwamba majadiliano yako kwenye hatua nzuri na yakikamilika tutasaini,” alisema Mkulo.

Mkulo alisema majadiliano yanayoendelea yanawahusisha Makatibu Wakuu wa Wizara za Fedha na Uchumi, Nishati na Madini, maofisa wa Serikali ya China na wakala wa utekelezaji wa mradi huo kutoka nchi hizo mbili.“Ninachoweza kusema ni kwamba bado tuko kwenye ratiba, tunafahamu umuhimu wa kukamilika kwa hatua hii, lakini lazima tujiridhishe.”Mapema wiki iliyopita, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Dk Servacius Likwelile alisema bado kuna maeneo machache ya majadiliano baina ya wataalamu wa Tanzania na China na kwamba yakikamilika mkataba huo wa kifedha utasainiwa.

“Ahadi ya Rais itatekelezwa kama alivyosema, kuna sehemu chache tu bado wataalamu wetu wanajadiliana na wenzetu wa China, wakikamilisha basi nadhani tutaweza kusaini ili kuwezesha mradi huo kuanza,” alisema Dk Likwelile.Kwa upande wake, Ngeleja alisema wizara yake imejipanga kusimamia kikamilifu ujenzi wa bomba hilo, baada ya mkataba wa fedha kusainiwa.

Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini, January Makamba katika maoni yake alisema kuchelewa kusainiwa kwa mkataba wa kifedha kunaweza kuathiri kasi ya utekelezaji wa mradi wa bomba la gesi kutoka Mtwara.“Ni vigumu sana kuwa na uhakika wa kutekelezwa kwa mradi kabla ya kuwa na uhakika wa fedha, sina uhakika kama hilo limefanyika lakini kwa kuwa tunaanza vikao vya kazi zetu karibuni, nadhani tutapata taarifa,” alisema January.Vikwazo vingineWakati Serikali ikihaha kukamilisha mchakato wa kusainiwa kwa mkataba wa fedha, habari kutoka ndani ya Serikali na Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) zinasema kinahitajika kiasi kikubwa cha fedha kwa ajili ya kujenga vituo vya kusambaza umeme na njia mpya za kusambaza umeme huyo.

Mmoja wa wahandisi ndani ya Tanesco ambaye aliomba jina lake lihifadhiwe alisema ikiwa kiasi hicho cha megawati 3,000 za umeme kitafikishwa Dar es Salaam basi vinahitajika vituo 30 kwa ajili ya kusambaza umeme.“Ujenzi wa kituo kimoja (sub-station) gharama zake si chini ya Dola za Marekani milioni 15 (zaidi ya Sh23 bilioni) kwa hiyo piga hesabu kama tunahitaji vituo 30 basi zidisha utapata majibu ni kiasi gani cha fedha kinachohitajika,” alisema mhandisi huyo wa umeme.

Kwa kuzingatia hesabu hizo, Serikali inalazimika kutafuta zaidi ya Sh700 bilioni kwa ajili ya ujenzi wa vituo hivyo ambavyo hata hivyo, hadi sasa bado mpango wake haujawekwa wazi. Pia italazimika kutafuta kiasi kama hicho kwa ajili ya ujenzi wa njia mpya ya kusafirishia umeme huo.

Habari zaidi zilisema ili kupatikana kwa megawati 3,000 za umeme, kunahitaji pia njia mpya za kusafirishia nishati hiyo ya msongo wa kilovolt 400, tofauti na njia za sasa ambazo uwezo wake ni msongo wa kilovolt 220.“Kama tunataka kuongeza kiasi cha umeme katika njia zetu za sasa, lazima tuongeze uwezo maana njia zetu zinazidiwa ndiyo maana wakati mwingine umeme unakatika ovyo,” alisema mhandisi huyo.Hivi sasa Serikali inajenga njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa Kilovolt 400 kutoka Iringa kupitia Dodoma, Singida hadi Shinyanga, ujenzi ambao utaigharimu kiasi cha Dola za Marekani milioni 500 (karibu Sh800 bilioni) hadi utakapokamilika.

Hata hivyo, njia hiyo ni maandalizi ya umeme unaotarajiwa kuzalishwa kutoka miradi ya makaa ya mawe ya Ngaka mkoani Ruvuma na Mchuchuma Wilaya ya Ludewa mkoani Iringa na siyo kwa ajili ya usafirishaji wa umeme utakaozalishwa kutokana na gesi ya Mnazi Bay kutoka Mtwara.Gharama za UmemeIkiwa ahadi ya Rais Kikwete itashindwa kutekelezwa katika muda wa miezi 18 kama alivyoahidi, inaamanisha kwamba taifa litaendelea kutumia umeme wa gharama kubwa unaozalishwa kwa mafuta.

Tayari gharama hizo zimeanza kuwaelemea watumiaji baada ya Mamlaka ya Udhibiti wa Maji na Nishati (Ewura), kuiruhusu Tanesco kupandisha gharama za umeme kuanzia leo kwa asilimia 40.29.Upandishaji huo umezua kilio nchi nzima ambako watu wa kada tofauti wamesema utaongeza gharama za maisha na kuwaathiri wananchi wa kipato cha chini.

Kutumika kwa umeme wa mafuta kunatokana na kutokuwepo kwa maji ya kutosha katika mabwawa ya kuzalisha umeme. Hadi mwishoni mwa wiki iliyopita, uzalishaji ulikuwa ni asilimia 62.9 ya uwezo wa mabwawa hayo.Meneja Uhusiano wa Tanesco, Badra Masoud alisema hadi sasa umeme unaotokana na maji ni megawati 353 kati ya 561 zinazotakiwa na kwamba hali hiyo inatokana na uhaba wa maji.

Mwisho……