Sunday, November 26

Wanawake bado wanatafuta tofauti ya mwanaume na ng’ombe


Kuna mambo yasiyofanana lakini huwezi kuyatofautisha’; unaweza kuisoma sentensi hiyo kadri utakavyo ili uilewe, lakini kuna mfano kwa ajili ya kukufunulia.
Ni hivi, ulishawahi kugundua kuwa hakuna tofauti kati ya mke wako kukwambia ‘Tunaondoka sasa hivi baba Ashura, namalizia kuvaa’ na wewe kumwambia ‘niko njiani mke wangu, nafika nyumbani sasa hivi’?.
Ni sentensi mbili tofauti kabisa, zisizofanana karibu kila kitu, kuanzia muundo hadi maana lakini linapokuja suala la mantiki huwezi kuzitofautisha kwa sababu ‘kuvaa kwa mwanamke’ ni mwaka mzima na ‘nakaribia nyumbani ya mwanaume’ ni sawa na miezi kumi na mbili kama sio siku 365.
Kingine kisichofanana lakini huwezi kutofautisha ni wale waliobahatika kuzaliwa katika familia zenye watu wenye kiwango cha juu cha elimu. Zile familia za kila unayemgusa alikuwa anafanya vizuri darasani, halafu kwa bahati mbaya ni wewe tu katika familia nzima ndiye uliyekuwa na ‘perfomance’ mbovu.
Kitu ambacho wote tunatakiwa tufahamu ni kwamba, unapokuwa mtoto wa hivi, familia nzima, hasa wazazi wako waliokuwa wanakulipia ada, walikuwa hawaoni tofauti kati yako na ng’ombe. Na hata kama wakiamua kuitafuta, hawatapata ya maana zaidi ya utofauti wa mapigo ya moyo— kwamba moyo wa ng’ombe hudunda mara 48 hadi 84 kwa dakika na wa kwako 60 hadi 100.
Sasa jicho ambalo wazazi humtazama mtoto ‘kilaza’ ndilo ambalo wake zetu hututazama katika nyakati za migongano.
Ni hivi; ulishawahi kupita kwenye mikwaruzano na mwenza wako. Mikwaruzano mizito kabisa yakupitisha kwenye mpaka wa ndoa na kutengana—halafu ghafla mwanamke akatamka; “Hutokuja kupata mwanamke atakayeweza kuishi na wewe.”
Ulishawahi kufikia hatua hiyo? Kama ndiyo, uliichukuliaje kauli ya mwenza wako. Ulidhani ni kwa sababu umri umekwenda au kwamba wanawake wanaotaka kuolewa wameisha duniani kwamba ukimuacha yeye utasota? Au labda uliichukulia kawaida tu?
Kama uliichukulia kawaida, ulikosea, ulitakiwa kuipa uzito kwa sababu ndani ya moyo wake, hakuwa anamaanisha vitu vyepesi namna kama vile ulivyovisikia. Alikuwa anazungumzia jinsi ambavyo wewe huna tofauti na ng’ombe.
Alikuwa anamaanisha kwamba, siku mtakayoachana, wanawake wote wanaokupenda sasa hivi na kudhani kuwa wewe ni binadamu, watapata nafasi ya kuishi na wewe, wataziona tabia zako na kugundua ukweli kuwa wewe ni sawa na ng’ombe dume kitabia, kwa hiyo hakuna atakayeweza kuvumilia kuishi na wewe.
Wanawake wanajua kuzungumza kwa mafumbo sana. Sikiliza mara mbili mbili kila wanachokwambia.

Wagombea Chadema wajitoa Arusha


Arusha. Wagombea udiwani wawili wa Chadema mkoani Arusha wametangaza kujitoa kwenye kinyang’anyiro cha uchaguzi mdogo unaofanyika leo Jumapili katika Kata ya Maroroni na Embuleni.
Wagombea hao ni Asanterabi Lazaro(Maroroni) na Dominick Mollel (Embuleni).
Wakizungumza na Mwananchi  wagombea wamesema  hawana sababu ya kuendelea na uchaguzi  uliotawaliwa na vurugu na hujuma.
Mbise amesema mawakala wake wamezuia kuingia vituoni na wengine kukamatwa.
Kwa upande wake mgombea wa Embuleni, Mollel alisema anajitoa kwani uchaguzi sio huru na haki.
"Tutaenda mahakamani kudai haki huu sio uchaguzi ni vita," amesema.

Mgombea Chadema asema mawakala wake wameondolewa

Wakala wa Chadema, Mashua Stephen akiwa chini
Wakala wa Chadema, Mashua Stephen akiwa chini ya ulinzi wa polisi baada kudaiwa kuingia kwenye kituo cha kupigia kura akitumia jina la mtu mwingine, pia akiwa na nyaraka za uwakala kupitia chama cha ACT Wazalendo. 
Dar es Salaam. Mgombea Udiwani wa Kata ya Saranga (Chadema), Ephraim Kinyafu amelalamikia hujuma dhidi ya mawakala wake kwa madai kwamba wameondolewa kwenye vituo vya kupigia kura.
Kinyafu akizungumza na waandishi leo Jumapili baada ya kupiga kura amesema mawakala walitakiwa kuapishwa Novemba 22 mpaka 24 lakini badala yake waliapishwa jana Jumamosi na kupewa fomu za kiapo leo leo Jumapili saa 2 asubuhi wakati wenzao wa CCM walipewa jana Jumamosi.
Amesema kuna hujuma inafanyika dhidi ya chama chake kwa kuwaondoa mawakala wenye sifa ili tu wasiwepo kwenye vituo vya kupigia kura.
“Kanuni zinaelekeza kwamba wakala anatakiwa kuwa fomu ya kiapo ya Tume ya Uchaguzi na barua ya chama. Sasa wameongeza sifa nyingine kwamba awe na kitambulisho cha mpiga kura au cha Taifa, baadhi ya mawakala wetu hawana hivyo vitambulisho, hawajaruhusiwa," amesema Kinyafu.
Mgombea huyo amesisitiza kwamba katika vituo 129 vya kupigia kura katika kata hiyo, hakuna mawakala wa Chadema, wameondolewa kwa kukosa vitambulisho.
Amesema maandalizi ya uchaguzi huo siyo mazuri na yametawaliwa na figisufigisu vinavyolenga kumkosesha ushindi.

Mbowe aagiza wagombea wa Chadema kujitoa kata tano Arumeru Mashariki


Arusha. Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe ameagiza wagombea wote wa udiwani wajitoe kwenye uchaguzi wa kata tano Arumeru Mashariki, mawakala na viongozi wote watoke vituoni.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Jumapili alisema tayari amewasiliana pia na Tume ya Uchaguzi kwa kuwa Arumeru sio uchaguzi ni vurugu watu wanatekwa kama Mbunge wa Babati Mjini, Paulina Gekul hadi sasa ametekwa na hajulikani alipo
Kutokana na hali hiyo Mbowe ametaka Tume ya Uchaguzi kuitisha uchaguzi mpya.

Grace na urais, heshima na utu wa Mugabe

Wafuasi wa chama cha Zanu-PF wakiwa na bango
Wafuasi wa chama cha Zanu-PF wakiwa na bango lililo na maandishi ya kumuunga mkono Grace Mugabe mjini Harare, Agosti 30, mwaka huu. Picha ya Maktaba 
Wiki nzima iliyopita kwenye vyombo vya habari na mitandao Zimbabwe na Zambia, kulikuwa na habari kwamba Rais wa Zimbabwe aliyejiuzulu, Robert Mugabe, alilia mbele ya picha ya mke wake wa kwanza, Sally Mugabe.
Maelezo ya habari hiyo ni kwamba Novemba 15, baada ya Mugabe kuwekwa kuzuizini na jeshi la nchi hiyo ndani ya makazi yake, alimwaga machozi kumkumbuka Sally na mtoto wao aliyeishi duniani miaka mitatu tu, Michael Nhamodzenyika.
Chanzo cha habari hiyo kilitajwa kuwa wanajeshi waliohifadhiwa majina ambao walimweka Mugabe kuzuizini, ikiwa ni mwanzo wa safari ya kumshinikiza aachie madaraka. Kwa mujibu wa wanajeshi hao, Mugabe alisema: “Sally angekuwapo pengine haya yasingetokea.”
Ni hapo pa kukumbuka na kuchambua maneno ya mwanasheria wa Kenya, Profesa Patrick Lumumba kuwa maisha ya Mugabe yana sehemu mbili, moja kama kiongozi makini, shupavu na mtu bora akiwa mume wa Sally, pili ni kiongozi wa hovyo na asiyevutia kabisa akiwa mume wa Grace.
Mwaka 2008, meneja wa zamani wa Shirika la Ndege la Zimbabwe, Kevin Nolan, alifanya mahojiano na gazeti la Daily Mail la Uingereza na kutoa picha ambazo alimpiga Mugabe mwaka 1961 kwenye Kanisa Katoliki la jijini Salisbury, sasa Harare, Zimbabwe, siku alipofunga ndoa na Sally.
Katika mahojiano hayo na Daily Mail, Nolan alisema kuwa alimfahamu Mugabe kama mtu bora, msomi, mwenye maono ya kulikomboa taifa lake bila kujali tofauti za rangi.
Alieleza: “Nadhani Sally alichangia ubora ambao nilimuona nao Mugabe. Baada ya mwanamke huyo kufa Mugabe alibadilika kabisa.” Unapochukua maneno ya Nolan, yale ya Profesa Lumumba na taarifa za wanajeshi kuwa Mugabe alimwaga machozi kumkumbuka Sally, unapata taswira jinsi ambavyo mwanamke huyo alikuwa bora, vilevile namna Grace alivyombadili Mugabe kutoka kiongozi wa mfano bora kuwa wa mfano usiofaa.
Sally ni nani?
Sally alifahamika kama Sarah Francesca Hayfron. Alitambulika zaidi kama Sally Hayfron na baada ya kufunga ndoa na Mugabe, jina lililovuma ni Sally Mugabe. Ni raia wa Ghana aliyegeuka mama wa ukombozi Zimbabwe.
Sally na Mugabe walikutana katika Chuo cha Mafunzo ya Ualimu cha Takoradi, Ghana, wakati huo ikiitwa Pwani ya Dhahabu (Gold Coast) ilipokuwa koloni la Uingereza.
Wote walikuwa walimu na hapo ndipo mapenzi yalichanua kati yao kisha kufuatiwa na ndoa ya Kikatoliki mwaka 1961.
Sally alizaliwa mwaka 1931, ikiwa ni miaka saba baada ya Mugabe aliyezaliwa Februari 21, 1924. Zipo taarifa zinabainisha kuwa walipokutana Mugabe hakuwa na mawazo ya siasa, ila Sally kutokana na mwamko wa kiukombozi uliokuwepo nchini kwake (Ghana), tayari alikuwa ameanza kuvutiwa na siasa.
Kwa vile Sally alikuwa akivutiwa na vuguvugu la mabadiliko lililokuwa limeshika kasi Ghana, alipojua Mugabe anatokea Zimbabwe, wakati huo ikiitwa Rhodesia ya Kusini, alimshawishi kuingia kwenye harakati ili aikomboe nchi yake.
Zipo ripoti nyingine zenye kueleza kuwa Mugabe alikuwa mkimya na mwenye aibu sana lakini nadhifu, kwamba Sally ndiye alianza kumpenda kwa sababu alimuona mwenye akili nyingi, zaidi alivutiwa na ufundishaji wake, hivyo kujisogeza kabla ya kuunganisha nyoyo na kusafiri pamoja kimapenzi.
Ni mapenzi hayo yaliyowafanya waingie pamoja kwenye harakati za ukombozi dhidi ya Waingereza. Mugabe akiongoza mapambano, Sally akawa mama wa harakati, akiwahudumia wapiganaji waliowalazimisha Waingereza kukabidhi uhuru kwa Wazimbabwe.
Ni kipindi hicho cha mapigano ya kudai uhuru ambayo huitwa Chimurenga ya Pili au Rhodesian Bush War, ndipo Sally alipewa hadhi ya kuitwa Amai (Mama), akiwa mama wa Chimurenga hadi Mama wa Taifa. Chimurenga ya Kwanza ilikuwa vita ya mwishoni mwa Karne ya 19.
Sally alikuwa kishawishi kizuri cha wanawake Zimbabwe kuamka na kudai uhuru. Mwaka 1963 Mugabe alikamatwa na Serikali ya Rhodesia, kipindi hicho mtoto wake, Michael Nhamodzenyika alikuwa mchanga. Mwaka 1964 alihukumiwa kifungo cha miezi 21 jela. Hata hivyo, miezi hiyo ilipokwisha Mugabe alipewa sharti la kutojihusisha na harakati za ukombozi ili aachiwe, alipogoma hakuachiwa. Mwaka 1966 akiwa gerezani alipata taarifa za mtoto wake kufariki dunia lakini hakuruhusiwa hata kwenda kumzika.
Sally alisimama imara nyakati za msiba wa mwanaye, mwaka 1970 alifiwa na baba yake mzazi, ikabidi aombe makazi Uingereza kabla ya mwaka 1975 kwenda Msumbiji kuungana na Mugabe baada ya kuwa ameachiwa na kuendeleza mipango ya kudai uhuru.
Kuanzia mwaka 1980, Zimbabwe ilipopata uhuru, alitambulika kama Mama wa Taifa, akiwa mke wa Waziri Mkuu na Mkuu wa Serikali (Mugabe) kisha mwaka 1987, Canaan Banana alipoondolewa nafasi ya Rais kisha Mugabe kuchukua vyeo vyote, Rais kama Mkuu wa Nchi, Amiri Jeshi Mkuu na Mkuu wa Serikali, Sally alitambulika kama First Lady.
Sifa kuu ya Sally wakati huo hakuwahi kujiingiza kwenye siasa. Alishughulika zaidi na masuala ya kijamii na kutoa misaada. Siku zote alimpa mumewe nafasi ya kufanya kazi. Hakuwa na kashfa. Alikuwa mwanamke wa heshima na maarufu mno.
Sally alifariki dunia mwaka 1992 baada ya ini lake kushindwa kufanya kazi baada ya kuugua muda mrefu. Inaelezwa kuwa kipindi akiumwa ndipo Mugabe alianza mapenzi na binti mdogo wakati huo, Grace, ambaye wakati Mugabe na Sally wakifunga ndoa mwaka 1961, alikuwa hajazaliwa.
Grace ndani ya Mugabe
Balozi ambaye alipata nafasi ya kuwa waziri kwenye Serikali ya Mugabe, Christopher Mutsvangwa, alipata kumweleza mwandishi wa mtandao wa Khuluma Africa kuwa Zimbabwe iliharibiwa na Grace kwa sababu alihonga vyeo vya uwaziri kwa vijana wasio na uwezo.
Mutsvangwa alitumia maneno “first boyfriends” kutambulisha mawaziri ambao alidai wengi wao walipata upendeleo kwa sababu za kuwa na uhusiano usiofaa na Grace ambaye ndiye alikuwa akiendesha Serikali baada ya kumzidi nguvu Mugabe.
Ipo kashfa kubwa iliyotikisa Zimbabwe, kwamba Grace alipata kuwa na uhusiano na aliyekuwa Gavana wa Benki Kuu, Gideon Gono. Kashfa hiyo ilivuma zaidi mwaka 2010 kuwa wawili hao walidumu kwa zaidi ya miaka mitano na waliutumia ukaribu wao kufuja rasilimali za umma.
Mtandao wa Zambian Observer ulipata kutaja wanaume wawili, Peter Pamire ambaye alifariki dunia kwa ajali tata ya gari, vilevile James Makamba aliyetoroka nchi, kwamba ni wanaume waliopata kuwa na uhusiano kijamii na Grace, likaongeza kwamba dada wa Mugabe, Sabina ndiye alibaini vitendo vya wifi yake na Gono.
Mifano hiyo mitatu ni kuonyesha jinsi Grace alivyougharimu utu na heshima ya Mugabe, kwani kukosa nidhamu ya ndoa na kujionyesha kuwa ni mwenye msuli mbele ya mume wake, ilikuwa sababu watu kumdharau kiongozi huyo na kuamini kuwa nchi iliongozwa na mkewe.
Hata namna Grace alivyoingia kwenye maisha ya Mugabe ilikuwa kwa kashfa kubwa. Kwani mwaka 1996, Grace akiwa Katibu Muhtasi wa Mugabe, vilevile akiwa mke wa rubani wa ndege za kijeshi Zimbabwe, Stanley Goreraza, alibainika kuzaa watoto wawili na Mugabe ambao ni Bona Nyepudzayi na Robert Peter Jr.
Kwamba katika watoto watatu aliokuwa nao Grace wakati huo ni Russell (mtoto wa kwanza wa Grace) peke yake ndiye alibainika kuwa baba yake ni Goreraza. Baada ya hapo Grace alifungua kesi mahakamani, akaomba talaka kisha akaolewa rasmi na Mugabe.
Kimsingi ndoa na Grace ilimvunjia heshima Mugabe kwa kumuoa mwanamke ambaye ni dhahiri alilazimisha talaka kwa mumewe aolewe na Rais, zaidi alizaa naye watoto wawili akiwa mke wa mtu. Goreraza baada ya kumpa talaka Grace alikwenda kusoma China kisha akafanywa ofisa Ubalozi wa Zimbabwe nchini China.
Grace ambaye amezidiwa umri wa miaka 41 na Mugabe, alizaliwa Afrika Kusini na wazazi wahamiaji. Aliungana na mama yake nchini Zimbabwe, akaolewa na Goreraza kabla ya kupata kazi ya ukatibu muhtasi Ikulu, Harare.
Baada ya ndoa na Mugabe, alijiingiza kwenye biashara ya madini lakini alianguka kila siku, hata hivyo alitia fora kwa kuishi maisha ya anasa mpaka akapewa jina la Grace Gucci. Alijilimbikizia mali na kusababisha Mugabe achekwe maana alionekana hana ubavu kwa mkewe.
Hali ikawa mbaya Grace alipotokeza na kukanusha madai hayo kisha akamwambia Mnangagwa: “Naweza kuwa Makamu wa Rais mzuri kuliko wewe, nipishe kwenye hiyo nafasi.” Kauli hiyo ya Grace ilichochea moto na kusababisha Novemba 6, Mugabe amfukuze kazi Mnangagwa na kuanza mchakato wa kumteua Grace.
Kitendo hicho ndicho kilibeba maudhui kuwa Grace alikuwa njiani kurithi urais, hivyo kuibua taharuki, jeshi likaingilia kati na kuidhibiti Serikali, chama (Zanu-PF) kikamuondoa Mugabe kwenye uongozi na Bunge likaanza mchakato wa kumvua madaraka, mwisho Novemba 21, alijiuzulu baada ya kuongoza nchi miaka 37.

Kuapishwa kwa Uhuru, Kenya ikiwa njiapanda

Mahasimu wa siasa za Kenya, Raila Odinga
Mahasimu wa siasa za Kenya, Raila Odinga (kushoto) akizungumza jambo mbele ya Rais Uhuru Kenyatta. Viongozi hao walikutana katika shughuli za kitaifa kabla ya uchaguzi . Piacha ya Maktaba 
Hakuna matumaini kwamba hali ya vuta nikuvute katika ulingo wa siasa hapa Kenya itafika tamati karibuni.
Kiongozi wa upinzani Raila Odinga na mshindani wake wake Rais Uhuru Kenyatta bado wanatunishiana msuli, kila mmoja akidhihirisha mzozo utaendelea.
Wanasiasa hao na wafuasi wa mirengo hii miwili pia wanaendelea na migogoro yao inayochochewa na ukabila, siasa mbaya na ukosefu wa njia mwafaka ya kusuluhisha mizozo ya kisiasa. Hali hii inaweza kusababisha kudorora kwa uchumi na miradi ya maendeleo.
Raila hangeweza kuhimili joto la kisiasa na akaamua kuzuru Zanzibar ambapo alifanya mikutano ya faragha na viongozi kutoka mataifa ya kanda ya Afrika Mashariki.
Raila bado yuko katika mchakato wa kujaribu kufanya mataifa mengine yaelewe mazingara ambayo yalimsukuma kutoshiriki uchaguzi wa marudio.
Mwanasiasa huyu anayeenziwa na wafuasi wake, alirejea nchini hivi majuzi kutoka ughaibuni alipofanya mikutano na viongozi kadhaa wa siasa kuhusu hali ya siasa nchini na hatua zinazofaa kuchukuliwa kurejesha hali ya kawaida. Haijulikani ikiwa ziara zake zitasaidia kutibu makovu ya siasa yanayotishia kupasua Kenya na kuleta maafa.
Kenya imeshikwa mateka na siasa duni za kumalizana na kufungia wengine nje wahisi baridi huku wengine wakiendelea “kula mapochopocho”. Ni kwa sababu hii ambayo baadhi ya viongozi wanapendekeza kuwe na nyadhifa zaidi kwenye upeo wa uongozi ili wale waliokosa kushinda kwenye uchaguzi, haswa wagombea wa urais, waweze kupata nafasi za kuongoza.
Kiini cha matatizo ya upinzani ni kura za hivi majuzi ambazo mrengo huu unaamini zilifanywa kinyume cha sheria. Lakini, Jubilee na wafuasi wake, hawataki kusikia hadithi hii kwa sababu wana uhakika uchaguzi ulikuwa haki na huru. Wanasema Raila hana budi kukubali uamuzi wa Mahakama ya Juu uliosema Uhuru alichaguliwa kulingana na sheria.
Ingawa Raila hakwenda mahakamani safari hii kupinga tena ushindi wa Uhuru, inaaminika na wengi kwamba waliofikisha kesi hizo mahakamani (Mwanasiasa Harun Mwau na mwanaharakati wa haki za kibinadamu Njonjo Mue) walikuwa wanawakilisha matakwa ya Nasa kortini.
Lakini Nasa imeapa kuwa haihusiki kwa njia yoyote na kesi hizo wakiongeza kwamba, matokeo ya kesi hizo hayawezi kuathiri mipango yao kuhusu hatua itakayochukua kuhakikisha “wanarejesha Kenya kwa demokrasia.”
Raila amekuwa akijikuta pabaya kila alipojaribu kukutana na wafuasi wake. Wiki jana alipokuwa anarejea kutoka ng’ambo, aliponea chupuchupu wakati gari lake lilipopigwa risasi mara kadhaa. Wanasiasa wa Nasa pamoja na wafuasi wao wanasisitiza kuwa, risasi hizo zilikuwa jaribio la kumuua kiongozi huyo.
Kwa bahati nzuri, gari la Raila haliwezi kupenywa na risasi. Nasa imetangaza kwamba inapanga kumwapisha Raila ikiwa Rais Uhuru ataapishwa Jumanne bila muafaka kuhusu hatma ya badaye ya nchi. Wabunge wa Nasa pia wamesema wataendelea kususia Bunge hadi suluhu ya kisiasa ipatikane.
Hata hivyo, wahenga wanasema, kelele za chura hazimzuii ng’ombe kunywa maji mtoni. Serikali ya Jubilee inaendelea na matayarisho ya kumwapisha Uhuru Novemba 28 jijini Nairobi. Waziri wa Mashauri, Fred Matiang’i ametangaza siku hiyo itakuwa mapumziko.
Nasa imesema siku hiyo wataandaa mkutano mkuu katika bustani ya Uhuru, Nairobi kuomboleza na waliofiwa kutokana na ghasia zilizotokea wakati polisi na wafuasi wa Raila walipokabiliana.
Viongozi wa upinzani wamesema hawawezi kumtambua Rais Uhuru na hiyo ndiyo sababu kuu ya wao wanapanga kumuapisha Raila kivyao eti kuongoza eneo fulani la Kenya ambalo upinzani umebuni.
Upinzani unasema Raila alishinda uchaguzi wa Agosti 8 uliobatilishwa na mahakama na ana haki ya kuapishwa. Unasema, Rais Uhuru ataongoza sehemu ya Kenya inayoitwa Central Republic of Kenya). Eneo hili la Wakikuyu na Kalenjin na Wenye asili ya Somalia. Kwa mawazo haya Je, Kenya yaelekea wapi? Siasa itatumaliza.
Hakuna siku Jubilee itaketi ikakubali kuona nchi ikigawanywa mara mbili ama tatu. Eneo la Pwani limekuwa likisema linataka kujitenga. Nawasihi wanasiasa wasiaje nchi itumbukie kwenye bahari ya utengano. Kenya ni moja na watu wake ni wamoja.
Viongozi waache ulafi na tamaa ya siasa na kujilimbikizia mali. Wakumbuke kwamba Kenya si yao. Rasilimali zinazopatikana katika nchi hii ni za kila Mkenya, bila kujali msingi wa kabila wala mrengo wa siasa. Kizungumkuti hiki italeta maafa zaidi kwa watu wasio na hatia. Bila shaka, polisi watakabiliana nao na baadhi yao watauawa.
Wiki tatu zilizopita, viongozi wa Nasa walizindua sare rasmi za mrengo wa wapiganiaji wa muungano huo. Sare hizo zina nembo ya ngumi kuashiria wameanza mapambano ya ukombozi wa tatu wa Kenya.
Nasa inasema Kenya inahitaji ukombozi ili Katiba izingatiwe na wale walionyanyaswa kwa miaka nenda miaka rudi, wapate kujisihi kama Wakenya.
Mwanasiasa Miguna Miguna amewaambia Wakenya wasichukulie siku hiyo ya kuapishwa kwa Uhuru kama ni siku muhimu.
“Siku hiyo ni siku ya kawaida. Mwanasiasa huyo mbishi ambaye pia amejitwika wadhifa wa jemedari wa National Resitance Movement (NRM) ya Nasa, anasema siku ya kuapishwa kwa Uhuru ni siku ya kawaida kama ile ambayo kidikteta wa Uganda, Idi Amin Dada aliapishwa.
Alifananisha siku hiyo kuu kwa Kenya kama ile siku aliyoapishwa aliyekuwa Rais wa Zimbabwe, Robert Mugabe.
“Kuapishwa si kitu,” akasema. “Kuapishwa kwa viongozi kama Uhuru na Naibu wake William Ruto, hakuwezi kuwapa haki ya kuongoza Kenya,” akaongeza.
Matamshi ya Miguna ni mazito na yaliyojaa machungu lakini yanaungwa mkono na wafuasi na viongozi wengi wa Nasa. Hii inamaanisha kwamba, Rais Uhuru atakuwa na wakati mgumu wa kuongoza katika muhula huu wa pili na wa mwisho wa utawala wake ulioanza 2013.
Itakuwa vigumu kwa Rais kuongoza ikiwa sehemu nyingi za nchi zinalalamika huku zikitaka kujiondoa kutoka ramani ya Kenya.
Licha ya matamshi kama hayo na hisia zisizoambatana na sera za utawala wake, Rais Uhuru ambaye ni kama mzazi kwa Wakenya wote, anafaa kujinyenyekea na kutafuta njia mbadala za kuleta uponyaji kwa wananchi wote ili kila mmoja katika nchi hii ajihisi kama ni Mkenya.
Wananchi wanasema ikiwa kweli ulimwengu wote unaamini uchaguzi wa Oktoba 26 ulikuwa huru na haki, viongozi wa ulimwengu wangetuma risala zao bila kushurutishwa wala kuombwa.
Wadadisi wa masuala ya siasa wanasema kwa kutuma nyaraka kwa mataifa ya ughaibuni, Serikali ya Jubilee iliwashinikiza viongozi wa nchi hizo kutuma salamu hizo kinyume na mapenzi yao.
Ingawa Serikali imekana madai hayo, gazeti moja maarufu la kila siku lilichapisha mawasiliano kati ya Mohamed, balozi wa Kenya Uingereza na waziri wa Nchi za Kigeni wa Uingereza, Boris Johnson.
Johnson alijkuta pabaya baada ya kumpongeza Uhuru hata kabla ya nchi nyingine kufanya hivyo.
Hatua ya Johnson sasa imemweka pabaya Balozi wa Uingereza, Nicholas Hailey ambaye alikuwa anasubiri kuona mwelekeo wa siasa nchini kabla ya kutuma pongezi hizo.
Gazeti la Telegraph la Uingereza lilifichua kuwa, pongezi za Johnson zimeitenga Uingereza kutoka kwa mataifa mengine ya magharibi kwa sababu nchi hizo zimesita kupongeza Uhuru kwa pupa, zikisubiri kuona jinsi mambo yatakavyoendelea siku chache zijazo.
Hii si mara ya kwanza kwa Johnson kutuma risala bila kutafakari athari zake. Katikati ya mgogoro uliokumba ushindi wa Uhuru wa Agosti 8, Johnson alikuwa na haraka ya kumpongeza Uhuru. Ushindi huo ulifutilia mbali na mahakama na kuacha Uingereza na aibu kubwa.
Yote yanayoendelea nchini yanaonyesha Kenya ingali njia panda.

Rais Magufuli awapa siku saba vigogo sita wakiwemo mawaziri wake wawili

Dar es Salaam. Rais John Magufuli ametoa siku saba kwa Mamlaka ya Mapato( TRA),  Mamlaka ya Bandari(TPA), Takukuru na Wizara ya Fedha kuhakikisha inatoa taarifa ni nani alihusika kuagiza magari 50 kupitia mgongo wa Ofisi ya Rais.
Rais Magufuli ametoa maagizo hayo leo Jumapili Novemba 26 baada ya kufanya ziara ya ghafla bandarini mara baada ya kutembelea meli ya Wachina iliyofanya matibabu kwa Watanzania kwa muda wa siku 5.
Magari hayo aina ya ambulance ambayo mpaka leo yapo bandarini, yaliagizwa mwaka 2015 kupitia majina ambayo hayatambuliki na Ofisi ya Rais.
Kabla ya kutoa maagizo hayo, Rais amewahoji IGP, Waziri wa Fedha, Kamishna Mkuu wa TRA na Mkurugenzi Mkuu wa Bandari ambao hata hivyo hawakuwa na mujibu kuhusu nani hasa mwagizaji wa magari hayo.
"Natoa onyo kwa mawaziri na wateule wale wote waliotangaza, sitaki mpaka nije kubaini uozo mimi mwenyewe ninataka mpigane kuhakikisha uozo wote unaondoka, safari nyingine nikigundua jambo lolote na wewe ni eneo lako hautapona," amesema.
Ameongeza,  "Ninatoa siku saba,  nataka aliyeagiza haya magari kwa mgongo wa Ofisi ya Rais atambulike ni nani na ninatoa maagizo hata kama ni mtu mkubwa kiasi gani atambulike nahitaji mujibu."
Wakati huohuo Rais Magufuli ametembea umbali wa zaidi ya mita 700 ili kukagua magari ya polisi ambayo yaliingizwa nchini mwaka 2015 lakini bado zaidi ya magari 50 yameendelea kubaki eneo la bandari.
Amemwagiza IGP kuhakikisha anayakagua magari hayo na kuyatoa bandarini ili yakafanye kazi ambayo ilikusudiwa.
  "Kwa nini magari yanakuja hapa yanakaa miaka 10, wakati sheria inasema ni siku 21? Amehoji Rais Magufuli.

Meya Ubungo akamatwa



Meya wa Manispaa ya Ubungo, Boniface Jacob
Meya wa Manispaa ya Ubungo, Boniface Jacob 
Dar es Salaam. Chama cha Demokrasia na Maendeleo(Chadema), kimedai kuwa Meya wa Manispaa ya Ubungo, Boniface Jacob amekamatwa na polisi wakati uchaguzi wa mdogo wa Kata ya Saranga ukiendelea.
Akizungumza leo Jumapili, msemaji wa chama hicho, Tumaini Makene amesema haijulikani meya huyo amepelekwa kituo gani na kwa kosa gani.
Amesema Jacob aliapishwa kuwa wakala katika majumuisho ya uchaguzi wa Kata ya  Saranga hivyo alikuwa anahusika katika uchaguzi unaoendelea katika kata hiyo.
Makene amesema uongozi wa chama hicho unafuatilia ili kujua sababu za kukamatwa kwake na wapi alipo.
"Sasa kama mtu tunayemtegemea kuwa wakala kwenye majumuisho ya kuhesabu kura unategemea nini, hizi ni rafu ambazo mamlaka husika zinatakiwa kufuatilia," amesema.

Njia mbili za kulea kuku bandani

Mfugaji Saria Munisi wa Bomang’ombe mkoani
Mfugaji Saria Munisi wa Bomang’ombe mkoani Kilimanjaro, akiwahudumia kuku anaowafuga katika mabanda maalumu (cages). Hii ni mojawapo ya njia mbili za kulea kuku wakiwa bandani. Picha na Clement Fumbuka 
Banda la kuku linaweza kulea kuku kwa namna nyingi. Leo tutangalia namna mfugaji anavyoweza kutumia banda kulea kuku kwa namna mbili.
Ukiondoa kanuni za ujenzi wa banda zinazoelekeza sehemu ya kujenga banda na vigezo vyake, ufugaji wa kuku kwa njia ya kisasa unafaa uzingatiwe katika matumizi ya banda.
Katika ufugaji wa kuku kwa njia ya kienyeji, kuku huenda bandani kulala wakati wa usiku, huku wakitumia muda mwingi kuzagaa nje wakitafuta chakula na maji wakati wa mchana.
Lakini ufugaji wa kuku kwa njia ya kisasa, kuku hukaa bandani muda wote wakipatiwa mahitaji yao yote bandani. Ni muhimu kuzingatia ujenzi wa banda na njia utakayotumia kulea kuku wako bandani. Faida ya ufugaji wa kuku kwa njia ya kisasa hutegemea matumizi ya banda lako.
Kulea kwenye sakafu
Njia ya kwanza katika matumizi ya banda kwa ufugaji wa kuku kwa njia ya kisasa ni kulelea kuku kwenye sakafu. Kuku kwa njia hii huishi kwenye sakafu iliyowekwa maranda au pumba ngumu ya mpunga. Kwa muda mrefu njia hii imezoeleka na inatumika mara kwa mara na ni teknolojia ya muda mrefu.
Ufanisi wake hutegemea vigezo bora vya banda kama vile nafasi ya kutosha ndani ya banda ili kuku waishi bila kubanana.
Vingine ni hewa safi na ya kutosha itakayofanya kuku wakue vizuri na kuzuia magonjwa au vifo vya mrundikano na kukosa hewa. Mwanga wa kutosha ili kuku wale na kunywa vizuri bila kuhitaji taa wakati wa mchana.
Pia, kuwapo kwa ukuta, milango, na madirisha imara ili kuzuia wizi na banda kutumika kwa muda mrefu bila kuharibika. Uelekeo sahihi wa madirisha ili kuwakinga dhidi ya mvua, jua na upepo.
Kuwe na sakafu imara iliyonyanyuliwa chini ili kuepuka kuku kuchimba mashimo ndani ya banda na hatimaye vimelea vya magonjwa kuathiri kuku mara kwa mara.
Njia ya mabanda maalumu
Njia ya pili ni ya mabanda maalumu maarufu kwa jina la ‘cages’. Kuku huwekwa kwenye banda wakiwa ndani ya waya uliotengenEzwa kwa vyuma. Waya huo unaweza kubebeshwa juu ya mwingine kitaalamu na kutengeneza mfano wa ghorofa kama makreti ya soda ndani ya banda.
Katika teknolojia hii, kuku huwa wasafi muda wote kutokana na kinyesi chao kudondoka moja kwa moja sakafuni bila kukikanyaga.
Pia, kuku hupewa chakula sehemu safi na kula chakula bila kumwaga. Mayai hutagwa na kujikusanya yenyewe sehemu moja. Njia ni bora zaidi katika kuepuka matatizo ya kuku kula mayai, kudonoana na kupatwa na magonjwa ya mara kwa mara.
Aidha, banda linaweza kulea kuku wengi mara nne hadi tano zaidi ya idadi ya kuku wanalelewa kwa njia ya kulelea kwenye sakafu.
Uzalishaji wa kuku kwa kutumia cages ni nafuu kwani mfugaji akifunga cages zake atazitumia kwa muda mrefu na gharama zake ni za kawaida kuliko kujenga banda.
Kwa mfano, mfugaji akijenga banda la kufugia kuku 100 kwa njia ya kufugia sakafuni, banda hilo hilo anaweza kufugia kuku wa mayai 450 kwa njia ya cages. Kufanya usafi kwenye banda la ‘cages’ ni rahisi kuliko kufanya usafi kwenye banda lililofugiwa kuku kwa njia ya sakafuni na kuwekwa maranda.
Mfugaji anaweza kutathmini kwa kulinganisha njia zote mbili ili kubaini tofauti zake katika gharama na faida kabla hajaamua kutumia njia mojawapo..
Ufugaji wa kuku ni biashara sawa na biashara nyingine zenye kuhitaji bidhaa iliyoboreshwa kuvutia wateja kutengeneza soko na hatimaye kuleta faida.
Katika ufugaji, ubunifu upo katika kutumia vizuri rasilimali kama chakula, maji, eneo, mtaji, utaalamu na nguvu kazi.
Matumizi mabaya au kutotumia ipasavyo rasilimali hizi ni kupoteza mapato katika biashara yako. Jambo lolote linahitaji mazingira fulani ili liende vizuri.
Ufugaji nao unahitaji kuandaliwa mazingira rafiki ili kupata mavuno mengi. Watu wengi huchukua mambo kwa historia kitu ambacho hakipaswi kuwa hivyo. Jambo zuri hutokea kutokana na usimamizi wenye kujali kila kipengele kinachohusiana na kuleta matokeo tarajiwa.
Mambo haya yaliyotajwa katika mwongozo huu wa ufugaji wa kuku ni mambo ya msingi kama tofali katika ujenzi wa nyumba.
Huwezi kujenga nyumba bila kuwa na matofali. Kadhalika huwezi kuzungumzia faida katika biashara ya ufugaji wa kuku bila kuzingatia matumizi bora ya rasilimali unazotumia kuendeshea biashara yako.
Banda la kuku ni sawa na shamba kwa mkulima. Mkulima hawezi kupanda mazao yake hewani lazima atahitaji shamba.
Kwa mfano huo mfugaji hawezi kufuga bila banda; lazima ajenge banda bora lenye vigezo kama ambavyo mkulima atatafuta shamba lenye rutuba nzuri ili kupata mavuno mengi.
Kuna aina nyingi za matumizi ya banda kulingana na mfumo aliojiandalia mfugaji. Banda linaweza kutumika kulingana na ubunifu wa mfugaji. Mabanda mengi hujengwa kulingana na mipango ya mfugaji.
Ramani ya banda na malighafi iliyotumika kujengea vina maana kubwa sana katika uzalishaji wa kuku. Mazingira ni kitu muhimu cha kutazamwa hasa mfugaji anapotaka kuchagua njia ya ufugaji wake.
Kwa kuwa faida ni kipaumbele cha mambo yote, kila kitu kifanyike kwa kulenga faida. Biashara yoyote inalenga kupata faida, ndiyo maana mfugaji anashauriwa kuwa na mazingira yenye kuleta faida katika biashara yake.
Mfugaji ahusishe wataalamu katika kubuni ramani ya mradi wake ili kuepuka gharama zinazoweza kuepukika.

Kuhama vyama na fikra sahihi za wanasiasa


Gwiji wa siasa za Canada na Waziri Mkuu kwa vipindi vingi zaidi nusu ya kwanza ya Karne ya 20, William King maarufu kama Mackenzie King, alipata kuandika kanuni kuhusu wanasiasa na vyama vyao, aliandika; “My political party is not my religion and it shouldn’t be yours either”, yaani chama changu cha siasa si dini yangu na hakipaswi kuwa dini yako pia.
Chini ya maneno hayo, aliweka mwongozo wenye sehemu tatu kwa wanasiasa kuhusu vyama vyao.
Mosi, alisema “chama changu cha siasa si mwokozi wangu”. Wakristo huamini uwepo wa mwokozi ambaye ni Yesu Kristo. King anataka wanasiasa wasivichukulie vyama vyao sawa na Yesu Kristo.
Pili, “chama changu cha siasa hakinipendi”. Hili ni darasa kuwa hakuna chama cha siasa chenye kumpenda mtu. Vyama huhitaji watu ili vijijenge kuwa vikubwa lakini pale inapobidi chama kinaweza kumjeruhi yeyote kwa ajili ya kutimiza malengo yake.
Tatu; Chama changu hakina uzima wa milele. Hakuna chama ambacho kinatoa uhakika wa uzima wa milele kwa mwanachama wake. Hivyo, kila mtu kwenye chama ni wa kupita tu, leo upo kesho haupo. Hayupo ambaye uhai wake duniani utarefushwa na chama chake.
Mwongozo huo wa King ukibebwa na kila mwanasiasa kama kanuni, utaokoa kundi kubwa la watu ambao kwao huwa waaminifu kwa vyama na kujenga chuki na watu wengine kwa kudhani kwamba pumzi zao za uhai zinafungamana na kadi zao za uanachama.
Kila mwanachama, hasa kijana ambaye ndiye yupo kwenye kundi lililo na idadi pana ya watu wenye deni kubwa la kuishi, hupaswa kufahamu kuwa kadi ya uanachama haitoi oksijeni, hivyo wanapoielekea siasa lolote linaweza kutokea kwenye vyama vyao, ama kutimuliwa au kuhama.
Katika vyama inaweza pia kutokea kukimbiwa na watu ambao inaaminika ndiyo uhai wa chama au kuwa na viongozi ambao hukubaliani na mitazamo, hivyo ukajikuta huna furaha. Ukifika hapo kumbuka mambo manne; chama cha siasa yo dini wala mwokozi, hakina uzima wa milele na hakimpendi mtu.
Hiyo ndiyo sababu kati mwaka 1975 mpaka 1980 kiliundwa chama cha Zanu Zimbabwe na baadaye Zanu-PF kutoka mwaka 1980 mpaka Novemba 2017, Robert Mugabe ndiye aliyeaminika kuwa ni uhai wa chama, lakini sasa Zanu-PF wanamuona Mugabe sawa na kifo cha chama na wamemtimua.
Siasa ni malisho mema
Mwanasiasa anapopata wazo au kushiriki wazo la kuasisi chama, moja kwa moja huamini kuwa chama hicho kwake kitakuwa malisho mema. Sawasawa na ambaye hujiunga na chama hai ni baada ya kuvutiwa na sera pamoja na falsafa zake kuwa ndani yake malisho mema yatapatikana.
Mjadala wa malisho mema upo katika makundi mawili; kwanza ni mvuto wa kiitikadi, kisera na kifalsafa kwamba chama kinaweza kujibu matatizo ya watu, hivyo mwanachama anakiasisi au anajiunga nacho ili kushiriki kuyaendea matarajio yake.
Pili ni fursa binafsi, kwamba mwanachama anajiunga na chama kwa sababu ameona mwanya wa uongozi, kwamba atapata fursa ya kugombea cheo anachokitaka au ataweza kukitumia chama kwa vyovyote vile kutimiza malengo yake binafsi. Hayo ni malisho mema katika sura ya masilahi binafsi.
Ufafanuzi wa makundi hayo mawili unakuleta kwenye ukweli huu, kwamba watu wanajiunga au wanaasisi vyama vya siasa kwa sababu mbili kuu, ama kuviendeleza vyama ili vifikie malengo mazuri yaliyomo kwenye maandishi au kutafuta fursa za kuongoza au kutimiza matarajio binafsi.
Mantiki ya hapo ni kuwa mtu anaweza kubaki kwenye chama, kuondoka na kuhamia kwingine kwa sababu za malisho mema. Mwanachama anabaki kwa imani kwamba ama chama chake ndicho chenye majibu ya watu au bado anaona fursa ndani yake, hivyo aondoke azipoteze?
Kumbe sasa anaweza kuwapo mtu anashambulia wenzake wenye kuhama vyama kwa sababu yeye yupo pazuri au imani yake ni kamili kwamba chama chake ndicho chenye majibu ya msingi juu ya matatizo ya watu na nchi kwa jumla. Na anayehama anakuwa anaona aendako ndiko pazuri.
Yule anayeachana na siasa labda awe mzee aliyeshiriki muda mrefu lakini kama umri wake bado unadai, huyo anakuwa amekata tamaa ya kuendelea, kwamba ama haoni chama chenye matarajio ya utumishi wa watu (kama anatafsiri siasa ni huduma) au hakuna chama chenye masilahi yake (kwa tafsiri ya siasa masilahi).
Wimbi la sasa
Hivi sasa kuna wimbi kubwa la wanachama na viongozi wa kisiasa kuhama vyama, wengi zaidi wakitoka upinzani kujiunga CCM. Ukishiba nadharia ya malisho mema kwenye siasa, hutawabeza, maana nao wanaangalia kilicho bora kwao.
Waliokuwa wanachama na viongozi wa ACT-Wazalendo waliohamia CCM ni Profesa Kitila Mkumbo, Samson Mwigamba, Albert Msando na Edna Sunga, wakati kutoka Chadema kwenda CCM ni Lawrence Masha, David Kafulila na Patrobas Katambi ambaye alikuwa mwenyekiti wa Baraza la Vijana Chadema (Bavicha).
Sawa tu na aliyekuwa Mbunge wa Singida Kaskazini (CCM), Lazaro Nyalandu ambaye alipata kuwa Waziri wa Maliasili na Utalii, aliyeamua kuhamia Chadema hivi karibuni na kujiuzulu ubunge, alitoa sababu zake kuhusu umuhimu wa nchi kuwa na Katiba Mpya ili kuimarisha utawala bora.
Tuchambue; Nyalandu ameona CCM, ambacho ni chama kilichomwezesha kupata ubunge, hakina malisho mema upande wa utawala bora, demokrasia na upatikanaji wa Katiba mpya, hivyo ameona ahame. Kama kuna sababu za ndani hizo ni zake binafsi.
Masha alisema amehama Chadema kwa sababu ameona upinzani hakuna mipango mahsusi ya kushika dola. Tafsiri yake ni kuwa yeye kwake malisho mema ni kushika dola, hivyo amerejea CCM ambacho kipo madarakani ili kuyaelekea matarajio yake kisiasa.
Kafulila alisema anajivua uanachama wa Chadema kwa kuwa wapinzani wamepoteza shabaha ya kukabiliana na ufisadi. Bila kusema kama atajiunga na CCM au la, alisema anaungana na Rais John Magufuli kwa sababu anapambana na ufisadi. Kumbe kwa Kafulila malisho mema ni kupigana vita dhidi ya ufisadi?
Profesa Kitila alisema sababu ya kwenda CCM ni baada ya kuona chama kimekuwa cha wanachama, vilevile kinamvutia kiitikadi na sera za kiuchumi. Ukifika hapo unajua kuwa tafsiri ya malisho mema kisiasa kwa Kitila ni chama kuwa na itikadi, vilevile sera bora za kiuchumi.
Kitila ni mmoja wa waasisi wa ACT-Wazalendo, hivyo kwa tafsiri hiyo unaweza kujiuliza je, chama hicho ambacho alishiriki kukijengea misingi hakina itikadi bora ambazo zingembakisha? Hakuna sera nzuri za kiuchumi? Au vyote vipo ila aliona giza kwa chama kushika dola hivi karibuni?
Katambi alisema amehama kwa sababu kijana ukiwa upinzani unatumiwa kama karai, kwamba umuhimu wake huonekana wakati wa ujenzi tu, baada ya ujenzi kukamilika karai hutelekezwa. Hapo ni sawa na kusema malisho mema ya Katambi ni kijana kuthaminiwa.
Msando na Mwigamba walijielekeza kulekule kwenye utawala bora na namna Rais Magufuli anavyopambana na ufisadi. Unaweza pia kutafsiri eneo hilo kuwa ndilo lenye kubeba mtazamo wa malisho mema kisiasa ambayo Msando na Mwigamba wanaamini.
Tutanue fikra
Rejea tafsiri ya malisho mema kisiasa kwamba yupo mwenye kutazama misingi ya chama kuelekea kuihudumia jamii, mwingine anatazama fursa ya kuongoza. Hapohapo elewa kuwa yupo anaweza kuhama chama kwa kuona chama kina misingi lakini hakina msuli wa kupambana kushika dola.
Ukisogea mbele ya hapo unapata jawabu kwamba yupo ambaye anakuwa na fursa nzuri kwenye chama alichopo lakini anaamua kwenda kubanana na watu wengine kwa sababu anaona kwamba chama anachohamia kina msuli wa kupambana na anaweza kupata fursa.
Rejea tena kwenye mwongozo wa Mackenzie King kuwa chama si dini, mwokozi wa maisha, hakimpendi mtu wala hakitoi uzima wa milele, kwa hiyo ukiona mtu anahama ujue anatafuta malisho mema. Hupaswi kumshambulia kuwa ni msaliti kwa sababu kila mmoja anatazama mambo kivyake.
Mbunge wa zamani jimbo la Kasulu Mjini (NCCR-Mageuzi), Moses Machali alipohamia CCM mwaka jana kutokea ACT-Wazalendo, Kafulila alisema Machali hakuwa mpinzani halisi, hivyo bora alivyojiunga CCM, kisha akasema safari ya ukombozi ni ngumu, kwamba wachache tu watafika mwisho.
Katika maelezo yake, Kafulila alijitabiria kuwa mmoja wa wanasiasa ambao wangefika mwisho katika kile alichokiita ni safari ya ukombozi. Hata alipohama NCCR-Mageuzi kujiunga na Chadema alisema chama hicho ndicho chenye uhakika wa kushika dola.
Hoja za Machali alipojiunga CCM ni sawa na alizotoa Kafulila, kwamba Rais Magufuli ndiye mpambanaji wa ufisadi. Ulinganisho huo usikufanye umuone Kafulila sawa na aliyemcheka mlevi kilabuni kisha naye akavuta kiti na kuagiza kinywaji, bali ukutanue kifikra.
Kwamba kwenye siasa kila mmoja huangalia matarajio anayoyapa kipaumbele. Ni vizuri kumheshimu mtu na uamuzi wake. Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere alisema CCM si mama yake, hivyo angeweza kuhama.
Hata hivyo hili si la kuacha kulisema, maana lina msisitizo wake, kwamba ni vigumu mno mtu kukiri kuwa amehama kwa sababu ya maslahi binafsi, yaani malisho mema ya tumbo lake, isipokuwa atasingizia hoja nyingine. Siri ni yake.

Sababu za Dk Shika kualikwa Kahama



Kahama. Mkurugenzi wa Chuo cha Tiba ya Binadamu Kahama, Yona Bakungile amesema alimualika Dk Louis Shika kwenye mahafali ya kwanza ya wanachuo wake kwa sababu ya ahadi zake za shaka za ununuzi wa nyumba, alizoshinda kwenye mnada zitasaidia kutangaza chuo hicho.
Novemba 9, Kampuni ya Udalali ya Yono kwa niaba ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), iliendesha mnada wa nyumba mbili za Lugumi zilizopo Mbweni JKT na moja ya Upanga jijini Dar es Salaam ambazo zote Dk Shika alifikia bei ya kuzinunua kwa Sh3.2 bilioni lakini alishindwa kulipa asilimia 25 ya mwanzo.
Akizungumza na Mwananchi mjini Kahama juzi, Bakungile alisema aliona atumie nafasi hiyo kumwita Dk Shika Kahama na hiyo ilikuwa mara yake ya kwanza kwenda wilayani humo.
Baada ya kuulizwa na Mwananchi kwanini alitumia gharama kubwa kumsafirisha kwa ndege Dk Shika huku akijua wazi kwamba Dar es Salaam alishinda mnada na hakuwa na fedha za kulipa, Bakungile alidai kushindwa kulipa kwa fedha za mnada ndilo jambo lililompa umaarufu.
“Najua wazi Dk Shika alishindwa kulipa Sh900 milioni kwenye mnada wa nyumba za Lugumi hivyo katika chuo changu ameahidi kutoa kila mwaka Dola 1 milioni za Marekani (sawa na Sh2.2 bilioni) ambazo akishindwa kuzilipa ataendelea kutangazwa kwamba ameshindwa kulipa hiyo itakuwa fursa ya chuo changu kuendelea kutangazwa,” alisema Bakungile.
Alhamisi iliyopita Dk Shika aliingia mjini Kahama akiwa mgeni mwalikwa wa chuo hicho na baada ya kupewa nafasi ya kuzungumza alitoa ahadi hiyo ya fedha akisema ataziwasilisha baada ya miamala ya kuhamisha fedha zake kutoka Urusi itakapokamilika.
Hata hivyo, baadhi ya watu walisema ‘bilionea’ huyo hapaswi kupewa heshima hiyo na badala yake anapaswa kufikishwa kwenye vyombo vya sheria kwa kuvuruga mnada.

Watatu wajeruhiwa ajali ya mwenyekiti wa CCM Hai


Hai. Gari la Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi CCM Wilaya ya Hai mkoani Kilimanjaro, Hussein Mriri limepata ajali katika eneo la Kijiji cha Kikavuchini na kusababisha majeruhi watatu.
Akizungumzia kutokea kwa ajali hiyo leo Jumapili, mwenyekiti wa kijiji cha Kikavu chini, Swaleh Msengesi amesema gari hilo lilikuwa limebeba watu hao waliokua katika mkesha wa kuhamasisha wapiga kura usiku wa kuamkia leo Jumapili.
Miongoni mwa waliojeruhiwa katika ajali hiyo ni Sakra Mtenga ambaye ni mjumbe wa Baraza Jumuiya ya Wazazi Wilaya ya Hai, Veronika Mmboga ambaye ni Diwani Vitu Maalum Same na Sophia Sharikiwa, ambaye ni Diwani Viti Maalumu Mwanga.
"Wote wamepelekwa katika hospitali ya Mkoa ya Mawenzi," amesema mwenyekiti huyo.