Tuesday, April 3

Wapalestina waendelea kudai haki zao baada ya 16 kuuwawa

Wapalestina wakimbeba mwanadamanaji mwenzao aliyejeruhiwa kwa risasi karibu na Ukanda wa Gaza kwenye mpaka na Israeli, Machi 31, 2018.
Maelfu ya Wapalestina wamebakia katika mahema katika mpaka wa Gaza Jumatatu (April 2), wakiendelea kuandamana wakidai haki ya kurejea kwa wakimbizi na vizazi vyao katika eneo ambalo leo ni Israel hata baada ya waandamanaji 16 kuuwawa na majeshi ya Israeli.
Idadi hiyo iliyokusanyika Jumatatu ilikuwa ndogo ukilinganisha na ile iliyoandamana mwisho wa wiki, ambapo ilionekana kuwepo uvunjifu wa amani uliopita kiasi katika ukingo wa Gaza tangia vita vya Israeli na Hamas vilipozuka mwaka 2014. Hamas ni jeshi la kundi la Kiislam ambalo linalishikilia eneo la pwani lililozingirwa.
Waandamanaji wengi Jumatatu wamekaa katika eneo salama mbali na mpakani, wakichukua tahadhari juu ya kuwepo majeshi ya Israeli ambao wameendelea kukalia eneo lenye kizuizi upande wa pili wa mpaka huo.
Jeshi la Israeli limesema kuwa baadhi ya wale waliorushiwa risasi Ijumaa, siku ya kwanza ya maandamano hayo, walikuwa wamewatupia risasi wanajeshi wa Israeli, wametuma matairi yaliyokuwa yanawaka moto kuelekea kwa wanajeshi hao na pia kutupa mawe na mabomu yakutengeneza wenyewe kwenda upande wa pili wa mpaka huo.
Hamas imesema watano kati ya wale waliouwawa walikuwa ni wanachama wa kitengo cha wapiganaji wake. Israel inasema wanane kati ya watu 15 waliouwawa walikuwa ni wa kikundi cha Hamas, na wengine wawili wa kikundi kingine.
Hata hivyo Hamas imekanusha kuwa wapiganaji wake hawakurusha risasi dhidi ya majeshi ya Israeli na wala hawakutumia waandamanaji kama ngome yao.
Siku ya Jumatatu, idadi ya Wapalestina waliouwawa ilifikia watu 16, baada ya madaktari wa Kipalestina kusema kuwa mtu mwenye miaka 29 alikufa kutokana na majeraha yaliyotokana na kurushiwa risasi siku ya Ijumaa.

Teknolojia kuwakumbusha wagonjwa wa ukimwi kufuatilia matibabu

Hii ni moja ya dawa mbalimbali zinazotumiwa kupambana na ukimwi.
Wanasayansi 16 kutoka bara la Afrika wameshiriki katika shindano la kutafuta ufumbuzi kwa changamoto kubwa zaidi zinazoikumba jamii katika bara la Afrika. Shindano hilo limefanyika katika jiji la Kigali nchini Rwanda.
Kwa muda wa miaka mitatu sasa, timu hii imekuwa ikiunda programu ya simu kwa ajili ya wagonjwa wa ukimwi.
Joel Gasana, kiongozi wa timu hii, ni mwanafunzi wa matibabu katika chuo kikuu mjini Kigali.
Amesema kuwa progamu hiyo ya simu, itawasaidia wagonjwa wa ukimwi kufuatilia matibabu yao.
Mwanateknolojia Joel Gasana ambaye ameunda programu hiyo (app) anasema :“Nchini Rwanda, viwango vya maambukizi ya ukimwi vipo juu sana, asilimia 3.3 ya idadi ya watu wameambukizwa.
Utafiti uliopo unaonyesha kwamba asilimia 27 ya watu walioambukizwa, hawazingatii matibabu inavyohitajika. Hiyo ndio sababu iliyonifanya kuunda program hii ili kuhakikisha kwamba wagonjwa wote wanazingatia matibabu”
Gasana ameongeza kuwa: “Kongamano hili limeniinua sana. Programu yangu imekubaliwa na wizara ya afya na kituo cha biolojia cha Rwanda. Tutakutana na maafisa wiki ijayo ili kuanzisha ushirikiano.”
Timu hii imechaguliwa kushiriki katika mashindano ya tuzo la uvumbuzi la jukwaa la Einstein, mwaka huu nchini Rwanda.
Jukwaa lijalo la Einstein, linatajwa kuwa kubwa Zaidi, na litawaleta pamoja wanasayansi kadhaa kutoka barani Afrika watakaojadili uvumbuzi na jinsi ya kutatua changamoto zinazolikumba bara la Afrika.
Wakati akifungua sherehe hiyo Rais Paul Kagame alisema, “Kwa mda mrefu, bara la Afrika limekubali kuachwa nyuma lakini hali hii imeanza kubadilika jinsi tunavyoona katika jukwaa hili”
Naye Dr Rose Mutiso, ni mwana teknolojia kuhusu nshati safi amesema, “nadhani ni jambo la kufurahisha na kuchochea kuona kwamba jamii hii ipo, inakua pamoja na kwa ushikamano na tupo sehemu ya jamii ya wanasayansi wa kimataifa”
Joel ameiambia VOA kuwa anaifanyia majaribio kazi ya uvumbuzi wake.
Amesema: “Nakaribia kumaliza uvumbuzi wangu. Naomba mnitakie kila la heri”
Baada ya siku tatu za kongamano na madajiliano kati ya wanasayansi hawa, ni wakati sasa wa kumaliza mashindano haya kuhusu uzinduzi wakisayansi.
Conrad Tankou, kutoka nchini Cameroon, amezindua mradi ya kisasa wa kuwasaida wanawake wanaougua saratani ya uzazi.
Rachel Sibande kutoka Malawi naye ana uzinduzi wa kutengeneza nguvu za umeme kutoka kwa mahindi.
Conrad, kutoka Cameroon, ameibuka mshindi na kutunukiwa dola 25,000 na kusema:
“Ningependa kusema kwamba hii ni mara ya kwanza programu hii inafanya natambuliwa”
Jukwaa limekamilisha kongamano hilo wakati washirika wakiwa wenye furaha tele na ahadi ya ushirikiano wa kudumu ili kuendeleza sayansi na teknolojia kote barani Afrika.

China yaongeza ushuru dhidi ya bidhaa za Marekani

Baadhi ya bidhaa za Marekani zilizoko kwenye soko la China ambazo zitaathiriwa na ushuru ulioongezwa na China.
China imeongeza ushuru kwa asilimia 25 kwenye bidhaa tofauti kutoka Marekani ikiwemo nyama ya nguruwe, matunda na bidhaa nyingine, zikiwa na thamani ya dola za marekani billioni 3.
Hatua hiyo ya China ambayo imeanza kutekelezwa Jumatatu hii ilitangazwa Jumapili na Wizara ya Fedha ya China, kama jibu dhidi ya hatua ya Marekani kuweka ushuru kwenye chuma na aliminium kutoka China.
Wizara ya Biashara ya China imefahamisha pia kwamba haitotekeleza baadhi ya vipengele vya mkataba wa kimataifa wa biashara ambapo China ilikuwa imekubali kupunguza ushuru kwenye bidhaa 120 kutoka Marekani.
Bali China imesema itaongeza ushuru kwa asilimia 15 kwenye bidhaa hizo za Marekani. Wachambuzi wa masuala ya kiuchumi wanahofia vita hivyo vya kibiashara kati ya mataifa hayo mawili vitaathiri uchumi wa dunia siku za mbele.

RAIS DKT. MAGUFULI APOKEA NDEGE MPYA YA TATU AINA YA BOMBARDIER DASH 8 Q400


 Ndege mpya ya Shirika la ndege la ATCL aina ya Bombardier Q400 ikiwasili katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es salaam Aprili 2, 2018
 Ndege mpya ya Shirika la ndege la ATCL aina ya Bombardier Q400 ikiwasili katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere huku ikipewa heshma ya  kumwagiwa maji(water salute) mara baada ya kutua.
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiongea wakati wa uzinduzi wa ndege Ndege mpya ya Shirika la ndege la ATCL aina ya Bombardier Q400 mara baada ya kuwasili katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere.


 
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiwa na mkewe Mama Janeth Magufuli, viongozi mbalimbali wa dini na Serikali akikata utepe kuashiria uzinduzi wa ndege mpya ya Shirika la ndege la ATCL aina ya Bombardier Q400 mara baada ya kuwasili katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere.


 
 Marubani walioileta ndege mpya ya Shirika la ndege la ATCL aina ya Bombardier Q400 kutoka Canada (wawili waliosimama kulia) na marubani na wahudumu wa ATCL mara baada ya kuwasili kwa ndege hiyo katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere.
  Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiwa viongozi wa dini na wa ATCL wakiwa ndani ya ndege mpya ya Shirika la ndege la ATCL aina ya Bombardier Q400 mara baada ya kuwasili katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere.
   Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiwashukuru Balozi wa Tanzania nchini Canada Mhe. Jack Zoka, Katibu Mkuu Wizara ya Katiba na Sheria Profesa Sifuni Mchome na marubani walioileta ndege mpya ya Shirika la ndege la ATCL aina ya Bombardier Q400 mara baada ya kuwasili katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere.
  Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akipongezwa na Mwenyekiti wa Jumuiya ya wakala wa Safari (TASOTA) Bw. Mustapha Khatawa kwa kuwasili kwa ndege mpya ya Shirika la ndege la ATCL aina ya Bombardier Q400 mara baada ya kuwasili katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere.

Saanane yaanza kampeni utalii wa ndani


Mwanza. Serikali imepanga kutekeleza mikakati itakayofanikisha kuongeza idadi ya watalii wanaotembelea nchini kufikia milioni tatu ifikapo mwaka wa fedha wa 2020/21.
Mikakati hiyo inayotekelezwa kupitia Shirika la Hifadhi za Taifa (Tanapa), Bodi ya Utalii Tanzania (TTB) na wadau wengine wa sekta hiyo, inalenga kuongeza idadi ya watalii kutoka nchini Marekani kufikia 300,000 kwa mwaka kutoka 60,000 wa sasa.
Mpango wa kuongeza watalii kutoka nchini Marekani ifikapo 2020, unatekelezwa kwa kushirikiana na ubalozi wa Tanzania nchini humo.
Mafanikio tayari yameanza kuonekana baada ya idadi ya watalii wanaotembelea nchini kufikia zaidi ya milioni 1.3, huku Taifa likiingiza zaidi ya Dola 1.9 bilioni za Marekani kwa mwaka.
Hifadhi ya Taifa ya Kisiwa cha Saanane haipo nyuma katika utekelezaji wa mikakati hiyo baada ya kuzindua kampeni maalumu ya siku kumi ya kuanzia Aprili Mosi hadi 10, kwa kutoa mafunzo ya uhifadhi na utalii wa ndani kwa wanafunzi wa taasisi za elimu ya juu jijini Mwanza.
Mhifadhi Mkuu wa Kisiwa cha Saanane, Abel Mtui anasema kampeni hiyo imelenga kuwafikia zaidi ya wanafunzi 5,000 kutoka vyuo vya Mtakatifu Augustine (Saut) Mwanza, Chuo cha Mipango, Chuo cha Biashara (CBE), Chuo cha Tiba Bugando (CUHAS) na Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA).
Akizungumza ofisini kwake mwishoni mwa wiki iliyopita, Mtui amesema licha ya elimu kwa vitendo na kutembelea hifadhi, wanafunzi hao watapata fursa ya kubadilishana mawazo na uzoefu kuhusu masuala ya uhifadhi miongoni mwao na watumishi wa Tanapa.
Kisiwa cha Saanane ndiyo pekee kati ya hifadhi za Taifa 16 zilizopo nchini ipo katikati ya mji ukiwa na vivutio kadhaa, wakiwamo Simba jike na dume walioko kwenye banda maalumu, pundamilia wapole ambao wageni wanaweza kupiga nao picha kwa mtindo wa selfie, swala, nguchiro, tumbuli na aina mbalimbali za ndege wakiwamo tausi.
Pia, kuna mawe yaliyobebana na mengine kusimama yenyewe yenye urefu wa zaidi ya mita 20, maeneo ya kupumzikia na kupiga picha na mwamba mkubwa ambao mtu akiruka juu yake na kupigwa picha, huonekana kama anayepaa juu ya maji ya Ziwa Victoria.
Hifadhi zingine nchini ni Arusha, Gombe, Katavi, Mlima Kilimanjaro, Kitulo, Milima ya Mahale, Mikumi, Mkomazi, Ruaha, Kisiwa cha Rubondo, Saadani, Serengeti, Tarangire, Manyara na Milima ya Udzungwa.
“Uhifadhi ni ajenda endelevu inayotakiwa kuhusisha makundi yote ya kijamii; tumeanza na wanafunzi wa taasisi za elimu ya juu kabla ya kufikia makundi mengine wakiwamo wanafunzi wa shule za sekondari na msingi,” anasema Mtui.
Anasema kampeni hiyo itatumika kusajili mabalozi wa uhifadhi wa Kisiwa cha Saanane miongoni mwa wanafunzi, ambao watatumika kuhamasisha utalii wa ndani badala ya kutegemea watalii kutoka nje ya nchi.
Mmoja wa waandaaji wakampeni hiyo, mhadhiri wa Saut, Judith Wanga anasema elimu kwa umma ikitiliwa maanani siyo tu itarahisisha kazi ya ulinzi wa rasilimali za Taifa, bali itapunguza gharama zinazotumika kuhifadhi na kulinda rasilimali hizo kwa njia ya sheria na adhabu.
“Elimu shirikishi itawapa wananchi fursa ya kuelewa umuhimu na faida ya kuhifadhi; jamii iliyoelimika na inayoona fadia italinda na kuhifadhi rasilimali za Taifa. Tuanze kujenga uelewa huo kwa vijana ambao ndiyo Taifa la kesho,” anasema Judith.
Ofisa Masoko wa Bodi ya Utalii Tanzania (TTB) Kanda ya Ziwa, Rhoda Michael anaunga mkono hoja ya elimu kwa umma itakayohimiza uhifadhi na ulinzi shirikishi kwa jamii na hatimaye kuongeza pato la Taifa kupitia sekta ya utalii hasa utalii wa ndani.
Vivutio na watalii
Licha ya hifadhi na mbuga zenye wanyama wengi na misitu, Tanzania imejaaliwa vivutio kadhaa vya utalii vikiwamo maeneo ya kihistoria na ya kiakiolojia, fukwe zisizochafuliwa na wingi wa utamaduni wa makabila 158.
Mwambao wa bahari wenye urefu wa zaidi ya kilomita 804, visiwa vya Unguja, Pemba na Mafia, Ziwa Victoria ambalo ni pili duniani kwa ukubwa na chanzo cha mto Nile na Ziwa Tanganyika ambalo ni la pili kwa kina kirefu duniani na la kwanza barani Afrika, ambalo ni miongoni mwa vivutio vinavyoipa sifa Tanzania.
Mwaka jana, mtandao wa Kimataifa wa SafariBookings.com uliitangaza Tanzania kuwa kituo bora kwa utalii barani Afrika baada ya kuchambua maoni kutoka kwa zaidi ya watalii 2,500 waliotembelea nchi za Afrika, wengi waliitaja Tanzania kuwa bora kuliko nchi nyingine kwa kuwa na eneo kubwa lenye wanyamapori wengi na misitu inayovutia.
Baadhi ya watu mashuhuri duniani akiwamo mwanamuziki wa Marekani, Usher Raymond, mwanasoka David Beckham aliyewahi kuchezea timu ya Taifa ya Engalnd na timu za Manchester United na Real Madrid wametembelea vivutio vya utalii nchini katika miaka ya hivi karibuni.
Mcheza filamu maarufu wa Marekani, Will Smith, mchezaji wa zamani wa timu ya Liverpool ya Uingereza, Mamadou Sakho na Morgan Schneiderlin wa timu ya soka ya Everton, pia wametembelea nchini kwa nyakati tofauti.

Maeneo ya ardhi yenye migogoro kuchukuliwa

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Idara Maalumu, Zanzibar, Haji Omar Kheir 
Zanzibar. Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Idara Maalumu, Zanzibar, Haji Omar Kheir amesema Serikali ya itachukua maeneo yote ya ardhi yenye mgogoro au iliyouzwa kinyume na taratibu ili yawe ya kilimo.
Waziri Kheir ambaye pia ni mwenyekiti wa kamati ya Baraza la Mapinduzi iliyoundwa kushughulikia migogoro ya ardhi visiwani hapa alisema: “Maeneo yaliyotolewa kinyume na taratibu na kusababisha migogoro baina ya wanunuzi na wauzaji yatachukuliwa na kupewa wananchi ili wayatumie kwa shughuli za kiuchumi na kilimo.
“Haya maeneo mengine ya Serikali yalikuwa yanatumiwa na wananchi kwa ajili ya shughuli zao za maendeleo lakini ghafla yameuzwa kinyume na taratibu.”
Kheir alisema jambo kubwa linalochangia kuibuka migogoro ya ardhi ni kuwapo baadhi ya viongozi wasio waaminifu katika kutekeleza majukumu yao kwa kuwa wanaendeleza hujuma za kuuza maeneo hayo kinyume cha sheria.
Waziri wa Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji Zanzibar, Dk Sira Ubwa Mamboya ambaye pia ni mjumbe wa kamati hiyo alitaja baadhi ya maeneo yanayoongoza kwa uuzwaji wa maeneo kinyume na taratibu ni Bwejuu, Paje, Michamvi, Marumbi, Kidimni na Kiboje.
Baadhi ya viongozi wa maeneo hayo, waliahidi kushirikiana na Serikali kuhakikisha kila eneo ambalo limeuzwa kinyume na taratibu za kisheria linarudi mikononi mwa Serikali.

Lema: Ni Mungu tu


Siku chache zilizopita, winga wa Kitanzania, Michael Lema (18) anayecheza soka la kulipwa kwenye klabu ya SK Sturm Graz ya Austria alipata ajali ya gari wakati akitoka kwenye matembezi yake ya kawaida.
Lema alipata ajali hiyo wakati akirejea mjini Graz kutoka kwenye matembezi yake ya kawaida ya kuwatembelea jamaa na marafiki ambao wanaishi nje kidogo ya mji huo.
Spoti Mikiki imefanya mawasiliano na winga huyo ambaye amepandishwa kikosi cha kwanza cha timu hiyo mara baada ya kufanya vizuri akiwa na Kikosi B kwenye ligi ya vijana na kupewa mkataba wa miaka mitatu.
Mawasiliano hayo, yalilenga kufahamu hali yake kwa ujumla, chanzo cha ajili hiyo na walezi wake walipokeaje taarifa ya kupata kwake kwa ajili hiyo akiwa kwenye gari yake aina ya Volkswagen.
“Nilitoka mazoezini na kumaliza program zote za siku hiyo kwa maana ya mazoezi binafsi ambayo nayo nimekuwa nikifanya kila siku ili kuhakikisha na kuwa fiti mara dufu.
“Siku hiyo nilikuwa na ahadi ya kuwatembelea marafiki zangu ambao muda mrefu kidogo hatukuonana nje ya mji ninaoishi, nilikwenda salama kabisa na kukutana nao.
“Muda ulikuwa umesogea kidogo na giza lilikuwa limeingia baada ya maongezi marefu na kufurahi pamoja, nilianza safari ya kurejea nyumbani, sikuwa kabisa nimetumia kilevi cha aina yoyote,” anasema Lema.
Winga huyo ambaye alifunga mabao matatu kwenye michezo nane ya kikosi B kabla ya kusaini mkataba na kupandishwa, alisema ajali hiyo ilichangiwa na kuendesha kwake kwa mwendo kasi.
“Ninakiri nilikuwa spidi na kilichotokea kiukweli nilishindwa kudhibiti mwendo kasi ule na nikayumba kwa kugonga ukingo wa barabara na kupata mstuko ambao ulinifanya kupoteza fahamu na nilijitambua wakati nikiwa hospitali.
“Sikupata majeraha na unafuu wa huku ni kwamba kuna kamera mitaani ni rahisi kupata msaada kama kuna tatizo limetokea, ajali haina kinga cha kushukuru Mungu ni kwamba nimetoka nikiwa salama.
“Ilinichukua siku tatu ambazo niliwekwa chini ya usimamizi wa madaktari ambao walinifanyia vipimo vyote na kubaini sikuwa na tatizo lolote ambalo limesababishwa na ajali hiyo zaidi ya michubuko wa kawaida,” anasema chipukizi huyo.
Anaendelea: “Kosa nililofanya ni kuendesha gari kwa mwendo kasi, kwa kosa hilo nimeadhibiwa kutoendesha chombo chochote cha mwendo moto kwa maana ya kuanzia gari hadi pikipiki kwa miezi sita.”
Hata hivyo, Lema hakuonyesha kusikitika kuharibika vibaya kwa Volkswagen yake yenye thamani ya Sh94 millioni.
“Thamani ya uhai wangu ni kubwa kuliko gari ambayo haitamaniki tena,” alisema Lema.
Nyota huyo wa Tanzania, anasema atarejea kwenye program za timu yake baada ya wiki tatu ambazo amepewa za kuhakikisha anarejea kwenye hali yake ya kawaida.
“Mwanasaikolojia wa timu alikuja na tukaongea na dhani atakuwa alikuja kuona ni kwa namna gari ile ajali iliniathiri kisaikolojia ila sioni kama nimeathirika kwa namna yoyote.
“Pamoja na yote nimesikita kupata ajali hii kwa sababu imefanya kukaa nje ya uwanja kwa wiki tatu tena ambazo kama ningekuwa kwenye program za timu ina maana ningekuwa kwenye nafasi nzuri ya kupewa nafasi ya kucheza.
“Hakuna ubaya lakini kwa sababu kila kinachotokea huwa na sababu zake, naamnini nitarejea na kuendeleza mapambano ya kuwania nafasi kwenye kikosi cha kwanza,” anasema.
Lema hakusita kuishukuru Spoti Mikiki kwa kuwa karibu naye hata hivyo alitumia nafasi hiyo kuwaambia ndugu na jamaa na marafiki zake ambao wapo Tanzania kuwa anaendelea vizuri mara baada ya kupata matibabu ya michubuko aliyopata kwenye ajali hiyo.

Tani 24.5 za bidhaa zilizoisha muda wa matumizi zateketezwa

Wafanyakazi wa Wakala wa Chakula, Dawa, na
Wafanyakazi wa Wakala wa Chakula, Dawa, na Vipodozi Zanzibar (ZFDA) wakishusha maboksi ya bidhaa ambazo hazifai kwa matumizi ya binadamu eneo la Kibele Mkoa wa Kusini Unguja. Picha na Haji Mtumwa.  
Zanzibar. Jumla ya tani 24.5 za bidhaa mbalimbali zilizobainika hazifai kwa matumizi ya binadamu zimeteketezwa kwa moto na Wakala wa Chakula, Dawa na Vipodozi Zanzibar (ZFDA).
Bidhaa hizo ziliteketezwa jana eneo la Kibele Wilaya Kusini Unguja na kusimamiwa na wadau mbalimbali wakiwamo, maofisa wa mazingira, askari polisi na watendaji wa ZFDA.
Msimamizi wa shughuli hiyo kutoka ZFDA, Aisha Suleiman alizitaja bidhaa hizo zilizoteketezwa kuwa ni mchele, dawa za kuulia wadudu, sabuni, mafuta na mipodozi.
Awali, ZFDA walifanya msako maalumu katika maeneo ya bandarini, kwenye maghala na maduka ndipo na kukuta bidhaa hizo hatari kwa matumizi.
“Hii ni kawaida yetu kwa kila kipindi kufanya msako maeneo ya biashara hasa kwa waingizaji na wauzaji mbalimbali, lengo ni kuona afya ya watumiaji zinakuwa salama muda wote kupitia chakula au vipodozi wanavyotumia,” alisema Suleiman.
Alifafanua kuwa pamoja na hatua hiyo, uingizwaji wa bidhaa zisizofaa kwa matumizi ya binadamu umepunguwa kwa asilimia kubwa ukilinganisha na miaka ya nyuma.
“Mwaka 2007 tulikuwa tunaweza kukamata na kuteketeza kwa moto zaidi ya tani 100 za bidhaa ambazo hazifai kwa matumizi ila sasa kiwango kimepungua sana. Tunashukuru baadhi ya wafanyabishara kuwa waelewa na kulinda afya za watumiaji,” alisema Suleiman.
Alifafanua kuwa hali hiyo inatokana na elimu inayotolewa na ZFDA kwa wafanyabiashara.
Pia, aliwataka wananchi kutoa ushirikiano kwa ZFDA ikiwamo kutoa taarifa za bidhaa watakazozibaini zimepitwa na wakati ili kulinda afya zao.
Mkaguzi wa Dawa na Vipodozi Zanzibar, Mohamed Hassan Mohamed alisema miongoni mwa vipodozi vilivyoteketezwa ni vile vilivyoisha muda wake wa matumizi ambavyo haviruhusiwi kuingizwa Zanzibar au kuuzwa.
Aliwataka wananchi kujenga mazoea ya kuzichunguza vyema bidhaa wanazonunua ili kujua muda wa kutengenezwa na muda wa mwisho wa matumizi.
Pia, aliwataka wafanyabiashara kuwa karibu na ZFDA ili kujua biashara inayofaa kuingizwa na isiyofaa kwa lengo la kuepuka hasara inayoweza kuepukika.

Wakimbizi waliokufa ajalini kuzikwa nchini



Ngara. Miili ya wakimbizi wanane raia wa Burundi waliopata ajali ya gari wilayani hapa Mkoa wa Kagera, Machi 29 mwaka huu wakitokea kambi za Nduta Wilaya ya Kibondo, Kigoma itazikwa leo (Jumatatu) eneo la Lumasi.
Mkuu wa Wilaya ya Ngara, Michael Mtenjele alitoa taarifa hiyo jana kwa waandishi wa habari waliotaka kujua hatima ya miili ya marehemu hao iliyohifadhiwa Hospitali ya Nyamiaga.
Mtenjele alisema baada ya kufanyika taratibu za kimatibabu kwa majeruhi wa ajali hiyo, watendaji wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi (UNHCR) Tawi la Ngara na Kibondo, wameomba ardhi ya kuhifadhi miili hiyo eneo la Lumasi ya Benako wilayani hapa.
“UNHCR ndiyo wanaratibu shughuli za mazishi ya miili hiyo, Serikali tunawapa ushirikiano wa kile wanachohitaji kwa mujibu wa sheria wala hatujapata tamko lolote kutoka Serikali ya Burundi kuhusu vifo hivyo,” alisema Mtenjele.
Katika ajali hiyo kulikuwa na msafara wa magari manane yenye wakimbizi 515, gari mojawapo lilifeli mfumo wa breki na kuligonga lingine kwa nyuma na kusababisha vifo vya watu wanane na majeruhi 95.
Mganga wa Hospitali ya Murugwanza, Remmy Andrew alisema majeruhi 22 wameruhusiwa na kupelekekwa kituo cha mapokezi kambi ya muda ya wakimbizi ya Lumasi.
Alisema majeruhi wanne wamepewa rufaa ya kwenda Hospitali ya Bugando, Mwanza kwa kusafirishwa na UNHCR, hivyo kubakia majeruhi wanane wanaoendelea kupata matibabu.

Mikoa vinara kwa wanafunzi watoro hadharani



Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa 
Dar es Salaam. Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ameitaja mikoa ya Tabora, Geita, Mtwara na Shinyanga kuwa inaongoza kwa utoro wa wanafunzi wa sekondari.
Waziri mkuu pia ameitaja mikoa ya Rukwa, Geita, Tabora, Singida na Simiyu kuwa inaongoza kwa utoro wa wanafunzi wa shule za msingi.
Majaliwa ambaye pia ni mbunge wa Ruangwa ameitaja mikoa hiyo leo Jumatatu Aprili 2,2018 akizindua mbio za Mwenge wa Uhuru katika uwanja wa Magogo mkoani Geita.
Mbio za Mwenge zitakazohitimishwa Oktoba 14,2018 mkoani Tanga zinaongozwa na kauli mbiu “Elimu ni ufunguo wa maisha, wekeza sasa kwa maendeleo ya nchi yetu.”
Majaliwa amesema Mkoa wa Tabora unaongoza kwa asilimia 9.7 ya wanafunzi watoro wa sekondari ukifuatiwa na Geita (asilimia 8.1), Mtwara (asilimia 6.1) na Shinyanga (asilimia 6.3).
Kwa shule za msingi, Rukwa inaongoza kwa asilimia 3.2, ukifuata Geita (asilimia 3.1), Tabora (asilimia 2.9), Singida (asilimia 2) na Simiyu (asilimia 2).
“Kwa jumla utoro wa wanafunzi wa sekondari ni mkubwa kuliko shule za msingi. Naikumbusha mikoa yote niliyoitaja kuhamasisha wananchi wakiwamo wazazi na walezi kuhusu umuhimu wa elimu na mahudhurio endelevu shuleni kwa kutumia utaratibu wa sheria zilizowekwa,” amesema Majaliwa.

Tumbili aiba mtoto na kutoroka naye India

macau monkeyHaki miliki ya pichaGETTY IMAGES
Polisi nchini India wanamsaka tumbili mmoja ambaye aliiba mtoto na kutoroka naye katika jimbo la Orissa, mashariki mwa nchi hiyo.
Mwili wa mtoto huyo ulipatikana baadaye kwenye kisima.
Mamake mtoto huyo mvulana anasema alishuhudia kisa hicho kikitokea lakini hakuweza kumuokoa.
Jamaa wake aliupata mwili wa mvulana huyo kwenye kisima nyuma ya nyumba yao, siku moja baada ya mvulana huyo kuibwa na tumbili huyo.
Mnyama huyo alikuwa ameingia ndani ya nyumba ya familia hiyo na kumtwaa mtoto huyo.
Polisi wanasema kisa hicho ni cha kipekee sana, ingawa mara kwa mara tumbili hupatikana wakiharibu mali eneo hilo.
"Tunatumai kwamba tutafanikiwa kumkamata tumbili huyu katika kipindi cha wiki moja," afisa mmoja wa polisi kwa jina Pradhan ameambia BBC.
"Ingawa visa vya tumbili kuwashambulia binadamu au kuingia kwenye manyumba ya watu wakitafuta chakula ni vya kawaida, hiki ndicho kisa cha kwanza kwa tumbili kutoroka na mtoto," ameongeza.
Polisi wanashirikiana na watu wa jamii moja eneo hilo, ambao ni stadi wa kuwakamata tumbili.
Maafisa wa idara ya msitu wameambia BBC kwamba tumbili huyo aliingia kwenye nyumba ya familia hiyo Jumamosi asubuhi na kutoroka na mtoto huyo.
Daktari aliyeuchunguza mwili wa mvulana huyo anasema haukuwa na alama za majeraha.
"Inaonekana alifariki kutokana na kukosa hewa pengine kutokana na kuzama kwenye maji kisimani," amesema daktari huyo.
Wakazi wameambia wanahabari kwamba huenda tumbili huyo alimwangusha mtoto huyo akitoroka.

Mamba apatikana katika bwawa la kuogelea Florida, Marekani

An alligator is dragged from a Florida poolHaki miliki ya pichaSARASOTA COUNTY SHERIFF'S OFFICE
Polisi katika jimbo la Florida, Marekani wamesema mamba wa urefu wa futi 11 alipatikana kwenye bwawa la kuogelea la familia moja katika jumba hilo.
Polisi wamepakia picha za mamba huyo mtandaoni.
Wakazi wa Nokomis waliwapigia simu polisi na kuomba usaidizi baada ya kumgundua mnyama huyo.
Afisa wa polisi wa eneo la Sarasota alipakia mtandaoni picha ya afisa wa wanyama aliyeitwa kumnasa akiwa anamburuta mnyama huyo kutoka kwenye maji Jumamosi.
Polisi wanasema mamba huyo alifanikiwa kupita kwenye uzio uliokuwepo na kuingia kwenye bwawa hilo.
Mamba nchini Marekani kwa kawaida hukua hadi kuwa na futi kati ya 11 na 15 na wanaweza kuwa na uzani wa kilo 454.
Mamba wa Marekani hupatikana mashariki mwa Marekani katika majimbo ya Florida na Louisiana, kila jimbo likiwa na zaidi ya mamba milioni moja.
MambaHaki miliki ya pichaSARASOTA COUNTY SHERIFF'S OFFICE
Eneo la kusini mwa Florida ndilo pekee ambalo mamba wa Marekani na mamba wa kawaida huishi kwa pamoja.
Ingawa awali walikuwa wameorodheshwa kama wanyama walio hatarini chini ya sheria za mwaka 1973, idadi yao iliongezeka sana kwa haraka na kufikia mwaka 1987 wakaondolewa kutoka kwenye orodha hiyo.
Inakadiriwa kwamba kuna mamba milioni moja hivi Florida, na wengine milioni moja Louisiana.