Tuesday, April 3

Tani 24.5 za bidhaa zilizoisha muda wa matumizi zateketezwa

Wafanyakazi wa Wakala wa Chakula, Dawa, na
Wafanyakazi wa Wakala wa Chakula, Dawa, na Vipodozi Zanzibar (ZFDA) wakishusha maboksi ya bidhaa ambazo hazifai kwa matumizi ya binadamu eneo la Kibele Mkoa wa Kusini Unguja. Picha na Haji Mtumwa.  
Zanzibar. Jumla ya tani 24.5 za bidhaa mbalimbali zilizobainika hazifai kwa matumizi ya binadamu zimeteketezwa kwa moto na Wakala wa Chakula, Dawa na Vipodozi Zanzibar (ZFDA).
Bidhaa hizo ziliteketezwa jana eneo la Kibele Wilaya Kusini Unguja na kusimamiwa na wadau mbalimbali wakiwamo, maofisa wa mazingira, askari polisi na watendaji wa ZFDA.
Msimamizi wa shughuli hiyo kutoka ZFDA, Aisha Suleiman alizitaja bidhaa hizo zilizoteketezwa kuwa ni mchele, dawa za kuulia wadudu, sabuni, mafuta na mipodozi.
Awali, ZFDA walifanya msako maalumu katika maeneo ya bandarini, kwenye maghala na maduka ndipo na kukuta bidhaa hizo hatari kwa matumizi.
“Hii ni kawaida yetu kwa kila kipindi kufanya msako maeneo ya biashara hasa kwa waingizaji na wauzaji mbalimbali, lengo ni kuona afya ya watumiaji zinakuwa salama muda wote kupitia chakula au vipodozi wanavyotumia,” alisema Suleiman.
Alifafanua kuwa pamoja na hatua hiyo, uingizwaji wa bidhaa zisizofaa kwa matumizi ya binadamu umepunguwa kwa asilimia kubwa ukilinganisha na miaka ya nyuma.
“Mwaka 2007 tulikuwa tunaweza kukamata na kuteketeza kwa moto zaidi ya tani 100 za bidhaa ambazo hazifai kwa matumizi ila sasa kiwango kimepungua sana. Tunashukuru baadhi ya wafanyabishara kuwa waelewa na kulinda afya za watumiaji,” alisema Suleiman.
Alifafanua kuwa hali hiyo inatokana na elimu inayotolewa na ZFDA kwa wafanyabiashara.
Pia, aliwataka wananchi kutoa ushirikiano kwa ZFDA ikiwamo kutoa taarifa za bidhaa watakazozibaini zimepitwa na wakati ili kulinda afya zao.
Mkaguzi wa Dawa na Vipodozi Zanzibar, Mohamed Hassan Mohamed alisema miongoni mwa vipodozi vilivyoteketezwa ni vile vilivyoisha muda wake wa matumizi ambavyo haviruhusiwi kuingizwa Zanzibar au kuuzwa.
Aliwataka wananchi kujenga mazoea ya kuzichunguza vyema bidhaa wanazonunua ili kujua muda wa kutengenezwa na muda wa mwisho wa matumizi.
Pia, aliwataka wafanyabiashara kuwa karibu na ZFDA ili kujua biashara inayofaa kuingizwa na isiyofaa kwa lengo la kuepuka hasara inayoweza kuepukika.

No comments:

Post a Comment