Friday, August 11

Wapangaji wagoma kulipa kodi ya nyumba wakihofia bomoabomo


Dar es Salaam. “Sijalala siku ya tatu leo tangu nione jirani yangu nyumba yake ikiwekewa alama ya X, najiuliza nitapona kweli?”
Ndivyo anavyosema Anselimi Nere (82) mkazi wa Kimara Stop Over ambaye wapangaji wake wamegoma kumlipa kodi ya nyumba ya mwezi Agosti wakihofia bomoabomoa.
Uwekaji wa X katika majengo yaliyo kando ya Barabara ya Morogoro kuanzia Kimara hadi Kiluvya ni mpango kuipanua unaofanywa na Serikali chini ya Wakala Barabara (Tanroads).
Nere ambaye nyumba yake bado haijawekewa alama ya X, amekuwa akiishi maisha ya hofu yeye na wapangaji wake tangu alipoona jengo la jirani yake Revy Kapinga likiwekewa alama ya X.
“Kila siku nimekuwa na kazi ya kuamka asubuhi na kukagua nyumba yangu, hata nikiwa nje nikiona vijana wamebeba mabegi mgongoni moyo wangu unashtuka paa! Nafikiri wanakuja,” alisema.
Nere ambaye anaishi peke yake huku akisumbuliwa na maradhi ya pumu, alisema wapangaji wake ambao ndiyo tegemeo lake wamegoma kabisa kulipa kodi.
“Niliwafuata wakaniambia ‘wewe mzee ina maana huoni kinachoendelea, tutakulipaje kodi wakati muda wowote nyumba yako inavunjwa’,” alisema akimnukuu mmoja wa wapangaji wake.
“Wamegoma, nina wapangaji wanne wananilipa Sh40,000 kwa mwezi nikiwaomba wananicheka inaumiza sana,” alisema.

Hali halisi ya mzee
Mwandishi wetu alifika nyumbani kwa mzee huyo ambaye amewahi kuwa mhasibu mkuu wa taasisi moja ya Serikali kuanzia mwaka 1967 hadi 1995 kwa sasa ni mstaafu.
Baada ya kujitambulisha kwake, mzee huyo alifurahi na kusema alitamani kuonana na waandishi wa gazeti la Mwananchi ambao wamekuwa wakiandika habari za bomoabomoa ili atoe dukuduku lake.
“Nimefurahi, yaani hapa nilikuwa najiuliza ni vipi nitawapata ili nitoe dukuduku langu ni kama Mungu amewaleta,” alisema na kuongeza: “Leo nitalala, nimekuwa na amani moyoni maana ni kama nilikuwa na sumu ikiniumiza sasa nimepata pa kuitolea,” alisema.
Nere alitumia nafasi hiyo kumwomba Rais John Magufuli awaonee huruma wananchi wake hasa wazee.
“Hata nikipata nafasi ya kuonana na Magufuli leo, nitamlilia awe na huruma hata kidogo na wazee, wanaoumia na hili zoezi wengi ni sisi wazee na wajane,” alisema.
“Wazee hawataki kukaripiwa tunahitaji maneno yenye faraja, kwa nini anakosa hata huruma, anapotufukuza hapa anataka twende wapi?” alihoji.
Mzee huyo pia alisema anaishi peke yake kwani waliachana na mkewe miaka mingi iliyopita.
Alisema nyumba yake ndiyo kila, kitu kwani alikuwa na shamba la ekari saba eneo la Kwembe na lenyewe lilichukuliwa na Serikali bila kulipwa fidia.

Wapangaji na majirani
Wapangaji kwenye nyumba ya mzee huyo walikiri kutolipa kodi ya nyumba wakihofia bomoabomoa.
“Tutalipaje kodi ya nyumba wakati muda wowote wanakuja kuweka X kama wameweka alama ya X kwa wananchi wengine ambao ni majirani wa babu unafikiri na yeye atapona?” alisema Hamida Ally.
Hamida alisema ni kweli mzee huyo anaishi maisha magumu na tangu operesheni ya bomoabomoa kuanza kwani amekuwa hana amani.
“Kuna siku aliamka asubuhi akakuta kuna hiki kibanda cha Mpesa kimeandikwa maneno mekundu mzee alihamaki kwa kweli mpaka alipokuja kujiridhisha kuwa siyo,” alisema Sabrina Hassan mpangaji mwingine wa mzee huyo.
“Si wote ambao wamegoma ni wachache, lakini wengine tumemlipa, ila kiukweli hata sisi tunalala mguu ndani mguu nje mtu unajiuliza ukilipa kodi leo kesho wakaja kuvunja utafanyaje? alisema.

CHANGAMOTO ZA WASANII WA NYIMBO ZA INJILI ZAWEKEWA MIKAKATI YA KUTATULIWA



Waziri wa Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Mhe. Dkt. Harrison Mwakyembe akizungumza na Wasanii wa Nyimbo za Injili (hawapo pichani) wakati wa mkutano na wasanii hao kujadili changamoto zinazowakabili na namna ya kutatua changamoto hizo leo Jijini Dar es Salaam. 
Katibu Mtendaji Chama cha Hakimiliki Tanzania (COSOTA) Bibi. Doreen Sinare akifafanua jambo wakati wa mkutano na wasanii wa nyimbo za Injili kujadili changamoto zinazowakabili na namna ya kutatua changamoto hizo leo Jijini Dar es Salaam. 
Rais wa Chama cha Muziki wa Injili Tanzania (CHAMWITA) Bw. Addo Novemba akiwasilisha changamoto zinazokabili muziki wa injili hapa nchini wakati wa mkutano na wasanii wa nyimbo za Injili kujadili changamoto zinazowakabili na namna ya kutatua changamoto hizo leo Jijini Dar es Salaam. 
Mwanamuziki wa Nyimbo za Injili Bi. Christina Shusho akichangia hoja wakati wa mkutano na wasanii wa nyimbo za Injili kujadili changamoto zinazowakabili na namna ya kutatua changamoto hizo leo Jijini Dar es Salaam. 
Waimbaji wa nyimbo za Injili wakitumbuiza wakati wa mkutano na wasanii wa nyimbo za Injili kujadili changamoto zinazowakabili na namna ya kutatua changamoto hizo leo Jijini Dar es Salaam.

Waziri wa Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Mhe. Dkt. Harrison Mwakyembe (waliokaa katikati) katika picha ya pamoja na viongozi kutoka serikalini pamoja na viongozi wa chama cha Muziki wa Injili Tanzania baada ya mkutano na wasanii hao kujadili changamoto zinazowakabili na namna ya kutatua changamoto hizo leo Jijini Dar es Salaam.

Picha na: Genofeva Matemu – WHUSM

…………………………….

CHANGAMOTO ZA WASANII WA NYIMBO ZA INJILI ZAWEKEWA MIKAKATI YA KUTATULIWA

Na: Genofeva Matemu – WHUSM

Tarehe: 10/08/2017

Waziri Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Harrison Mwakyembe amekutana na wasanii wa nyimbo za Injili leo Jijini Dar es Salaam kusikiliza changamoto zinazoikabili tasnia ya muziki wa nyimbo za injili na kuweka mikakati ya kuzitatua changamoto hizo hadi kufikia mwishoni mwa mwaka huu.

Akizungumza wakati wa mkutano na wanamuziki wa nyimbo za Injili Mhe. Mwakyembe amesema kuwa serikali ina wajibu wa kufuatilia changamoto za tasnia ya muziki ukiwemo muziki wa injili na kuzitatua ili kuweza kukuza kazi za wasanii kwa maslahi ya mtu mmoja mmoja na taifa.

“Muziki ni tasnia ambayo imewabeba vijana wengi hapa nchini, serikali ina wajibu wa kutetea, kulinda na kuhakikisha maslahi ya kazi za sanaa ikiwemo muziki wa injili inaheshimiwa na kulindwa” Amesema Mhe. Mwakyembe

Kwa upande wake Katibu Mtendaji Chama cha Hakimiliki Tanzania (COSOTA) Bibi. Doreen Sinare amewataka Wasanii wa Muziki wa Injili kutoshawishiwa kutoa malipo yoyote katika vyombo vya habari ili nyimbo zao ziweze kuchezwa kwenye vyombo hivyo bali vyombo vya habari ndio vinapaswa viwalipa wasanii wakati wanapotumia nyimbo zoa.

Aidha Bibi. Doreen amewaomba waimbaji hao wa nyimbo za injili kutembelea ofisi za Bodi ya Filamu, Cosota na Basata ili waweze kupata ushauri wa namna ya kuandika mikataba bora na inayofaa wakati wa kutengeneza na kuandaa albamu za nyimbo za injili.

Naye Rais wa Chama cha Muziki wa Injili Tanzania (CHAMWITA) Bw. Addo Novemba amewataka Viongozi wa nyimbo za Injili Tanzania kuhakikisha kuwa wanafanya kazi bega kwa bega na serikali na kwa bidii katika kukuza, kuendeleza, na kulinda maslahi ya wanamuziki wa Injili.

Aidha Bw. Novemba ameiomba serikali kuhusisha wanamuziki wa nyimbo za injili katika matukio mbalimbali ya serikali na ya nchi kwani wasanii wa nyimbo za injili wamekua wakiimba nyimbo zinazojenga taifa na kuendeleza amani, upendo na ushirikiano wa nchi yetu.

WAZIRI MKUU AWAONYA WATU WANAOCHUKUA DAWA KATIKA HOSPITALI ZA SERIKALI NA KUZIPELEKA KATIKA MADUKA YAO.


Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akiwahutubia Wananchi wa Wilaya ya Sikonge Mjini leo Agosti.10.2017 katika viwanja vya Tasaf Waziri Mkuu yupo Mkoani Tabora kwa ziara ya Kikazi 


Na Tiganya Vincent-RS-Tabora

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa amewaonya wamiliki wa maduka ya madawa ya binadamu na watumishi wa sekta ya afya wanaochukua dawa ambazo zinapaswa kupelekwa katika Hospitali za Serikali ili kuwahudumia wananchi na kuziweka katika maduka yao.

Mhe. Majaliwa alitoa kauli hiyo jana Wilayani Sikonge katika mkutano wa hadhara na wananchi katika Kiwanja cha TASAF.

Alisema kuwa vitendo hivyo ndivyo vimekuwa vikisababisha upungufu wa dawa katika Zahanati, Vituo vya Afya na Hospitali mbalimbali za Serikali na kufanya baadhi ya wananchi kuendelea kuteseka na maradhi kwa sababu ya kushindwa gharama za ununuzi wa dawa katika maduka ya watu binafsi.

Waziri Mkuu Mhe. Majaliwa aliwaonya watumishi wa afya na wamiliki hao wenye tabia hizo kuacha mara moja endapo watabainika kuendesha vitendo hivyo watachukuliwa hatua kali.

Alisema kuwa Serikali inatumia fedha nyingi kwa ajili kununua dawa ili zinasaidia kutoa huduma ya matibabu kwa wananchi wake lakini kuna baadhi ya watumishi wa afya wasio waadirifu ambapo wamekuwa wakitorosha dawa na kuwauzia wamiliki wa maduka ya dawa na ksuababisha upungufu katika vituo vya Serikali.

Waziri Mkuu kuwa Serikali haiwezi kuwavilimia watumishi wa afya wasio waaminifu wanaochukua dawa na kuzipeleka katika maduka binafsi huku wakisababisha upungufu katika baadhi ya hospitali za umma.

Alisema kuwa hospitali ni lazima ziwe na dawa za kutosha ili kuepusha usumbufu kwa wananchi.

Katika hatua nyingine Waziri Mkuu ameikabidhi Kamati ya Ulinzi na Usalama Mkoa wa Tabora orodha ya watu wenye tabia ya kuwarubuni wakulima wa tumbaku na kununua katika mfumo ambao si rasmi na kisheria (soko huria) na kuwanyonya ili wahojiwe.

Alisema kuwa watu hao kwa muda mrefu ndio wamekuwa wakiwanyonya wakulima kununua tumbaku zao kwa vishanda na kuwa fedha ambazo zinazidi kuwakandamiza.

“Nina majina ya watu ambao wamekuwa wakipita kwa wakulima na kununua tumbakuza wakulima kwa njia ya vishada ….huku wakiwanyonya kwa kuwapa fedha kidogo nawataka waache mara moja.” Alisisitiza Mhe. Waziri Mkuu.

Aliongeza “leo siwataji majina yao lakini nakuachia Mkuu wa Mkoa ili wewe na Kamati yako ya Ulinzi na Usalama muwaite na kuwahoji na kisha ziwaonye wasiendelee na biashara hiyo, kama wanataka kuendelea na uuzaji wa tumbaku wahakikishe wanayopeleka sokoni ni ile waliolima wenyewe na sio ya kununua kwa wakulima”

Aidha Waziri Mkuu alitoa onyo kwa watumishi wa umma ambao wamekuwa na tabia ya kugonja wakulima walime tumbaku na wakisha kuvuna na kukausha wao wanakwenda kununua kwa ajili ya kuipeleka katika makampuni ya tumbaku.

Alisema mtumishi hakatazwi kulima kulima tumbaku bali atakiwi kununua tumbaku kutoka kwa mkulima.

Waziri Mkuu huyo aliwaagiza viongozi wa Mkoa wa Tabora kukamata watu wote wanajihusisha na ulanguzi wa tumbaku ya wakulima na kuongeza kuwa watakamatwa wakiwa na tumbaku ya ulanguzi ichukuliwe pamoja na chombo cha usafiri kinachotumika kusafirishia.

Alisema kuwa tumbaku yote inauzwa kupitia vyama vya msingi na kila mtu atauza tumbaku kwa kiwango alicholima.

KATIBU MTENDAJI BODI YA FILAMU AFUNGA SEMINA YA MAMENEJA WA USAMBAZAJI WA KAZI ZA FILAMU KUTOKA MIKOA 25 YA TANZANIA



Katibu Mtendaji Bodi ya Filamu Bibi. Joyce Fissoo (katikati) akizungumza na mameneja wa usambazaji wa kazi za filamu (hawapo pichani) kabla ya kufunga semina elekezi kwa mameneja hao leo Jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Mkurugenzi Mkuu wa Barazani Entertainment Bw. John Kalage na kulia ni Mkuu wa Kitengo cha uenezi Bw. Singo Mtambalike 

Katibu Mtendaji Bodi ya Filamu Bibi. Joyce Fissoo (kushoto) akipata maelezo kutoka kwa Mkurugenzi Mkuu wa Barazani Entertainment Bw. John Kalage (Kulia) alipotembelea ofisi hizo leo Jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kufunga semina ya mameneja wa usambazaji wa kazi za filamu kutoka mikoa 25 ya Tanzania. 
Katibu Mtendaji Bodi ya Filamu Bibi. Joyce Fissoo (kushoto) akiteta jambo na viongozi wa Barazani Entertainment kabla ya kufunga semina ya mameneja wa usambazaji wa kazi za filamu kutoka mikoa 25 ya Tanzania leo Jijini Dar es Salaam. Kulia ni mkuu wa Mawasiliano kutoka Barazani Entertainment Bw. Jacob Steven na katikati ni Mkurugenzi Mkuu wa Barazani Entertainment Bw. John Kalage 
Katibu Mtendaji Bodi ya Filamu Bibi. Joyce Fissoo (katikati) katika picha ya pamoja na viongozi wa Barazani Entertainment na mameneja wa usambazaji kazi za filamu baada ya kufunga semina elekezi kwa mameneja hao leo Jijini Dar es Salaam. 

Picha na: Genofeva Matemu – WHUSM

NAIBU MEYA WA MANISPAA YA DODOMA JUMANNE NGEDE ATETEA NAFASI YAKE



Na Ramadhani Juma-Ofisi ya Mkurugenzi

NAIBU Meya wa Manispaa ya Dodoma aliyemaliza muda wake Jumanne Ngede amefanikiwa kutetea nafasi yake katika uchaguzi uliofanyika jana katika ukumbi wa Manispaa ya Dodoma ambapo wajumbe 56 walishiriki uchaguzi huo.

Katika uchaguzi huo Ngede ambaye ni Diwani wa Kata ya Chamwino kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) alishinda nafasi hiyo kwa kupata kura 47 dhidi ya mpinzani wake kutoka Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Samwel Mziba ambaye ni Diwani wa Kata ya Hazina aliyepata kura 9.

Mkurugenzi wa Manispaa ya Dodoma ambaye ni Msimamizi wa uchaguzi wa jimbo la Dodoma Mjini Godwin Kunambi alimtangaza rasmi Ngede kuwa Naibu Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma.

Baada ya kufanikiwa kutetea nafasi yake, Ngede aliwashukuru wajumbe kwa kumchagua kwa kura nyingi jambo linaonesha kuwa wana imani kubwa na utendaji wake na kwamba ataendelea kufanya kazi kwa uadilifu mkubwa na kwa kushirikiana na Madiwani wote.

Kwa upande wake, mgombea aliyeshindwa Samweli Mziba aliwashukuru wajumbe na kumpongeza mshindi huku akidai uchaguzi umepita na sasa ni kuchapa kazi tu.
 Mgombea aliyeshinda nafasi ya Naibu Meya wa Manispaa ya Dodoma Jumannne Ngede (CCM) akitoa neno kwa wajumbe mara baada ya kushinda nafasi hiyo kufuatia uchaguzi uliofanyika jana katika ukumbi wa Manispaa hiyo.
   Mgombea aliyeshindwa nafasi ya Naibu Meya wa Manispaa ya Dodoma Samwel Mziba  (CHADEMA) akitoa neno kwa wajumbe mara baada ya matokeo kutangazwa kufuatia uchaguzi uliofanyika jana katika ukumbi wa Manispaa hiyo.

DAWASCO WATOA ELIMU KWA WANANCHI JUU YA MFUMO MPYA WA UTOAJI NA UPATIKANAJI WA TAARIFA MUHIMU.


MENEJA Uhusiano wa DAWASCO, Bi. Everlasting Lyaro, amewataka wananchi wa Dar es Salaam na Pwani kupakua mfumo huu kwani ni rahisi kuutumia na hauna gharama zozote. Anasema ni mfumo ambao utamrahisishia mteja kupata taarifa muhimu zinazohusu huduma ya maji zikiwamo ankara ya mwezi, taarifa za lini mteja alifungiwa huduma ya maji, muda ambao alifanya malipo, lini mita yake ya maji ilisomwa na taarifa nyingine nyingi.
“Nawasihi wateja wetu na wananchi wote kupakua mfumo huu mpya katika simu zenu za mkononi ili kuweza kufurahia huduma zetu, hakuna gharama zozote ambazo utatozwa. Kupitia mfumo huu utaweza kupata taarifa zote muhimu za huduma ya majisafi zikiwemo taarifa za mivujo ya maji na ankara za maji za kila mwezi,”amefafanua Bi. Lyaro.
Amesema kwa sasa Wateja hawana haja ya kutumia muda mrefu katika ufuatiliaji wa kuunganishwa huduma ya maji, bali kilichorahisishwa ni mteja kuweka taarifa zake sahihi kwenye mfumo huo na DAWASCO.
Meneja Uhusiano wa DAWASCO, Bi Everlasting Lyaro akitoa elimu juu ya matumizi ya mfumo wa DAWASCO kwa kwa njia ya simu kwa watumiaji wa vyombo vya Moto hususani Bajaj na Pikipiki katika maeneo mbalimbali ya Jiji la Dar es salaam. Mfumo huo umezinduliwa rasmi ili kutoa nafasi kwa wananchi kupata na kutoa taarifa sahihi za DAWASCO.
Mmoja ya waendesha bodaboda akimuuliza swali Meneja Uhusiano wa DAWASCO, Bi. Everlasting Lyaro juu ya matumizi ya mfumo mpya wa DAWSCO katika utoaji na upatikanaji wa taarifa.
Mwendesha bajaji akihojiwana ITV juu ya matumizi ya mfumo mpya wa DAWASCO katika utoaji na upatikanaji wa taarifa.

RAIS DKT. MAGUFULI AKUTANA NA KATIBU MKUU WA JUMUIYA YA MADOLA MHE PATRICIA SCOTLAND IKULU JIJINI DAR ES SALAAM JIONI HII


 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akimlaki Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola Mhe Patricia Scotland Ikulu jijini Dar es salaam jioni ya leo Agosti 10, 2017
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akisalimiana na Balozi wa Tanzania nchini Uingereza Dkt. Asha-Rose Migiro aliyeongozana na Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola Mhe Patricia Scotland Ikulu jijini Dar es salaam jioni ya leo Agosti 10, 2017
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiwa katika mazungumzo  na Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola Mhe Patricia Scotland Ikulu jijini Dar es salaam jioni ya leo Agosti 10, 2017 akiwa ameongozana na Balozi wa Tanzania nchini Uingereza Dkt. Asha-Rose Migiro 
 
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiagana na  Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola Mhe Patricia Scotland Ikulu jijini Dar es salaam jioni ya leo Agosti 10, 2017 akiwa kaongozana na  Balozi wa Tanzania nchini Uingereza Dkt. Asha-Rose Migiro.

Picha na Ikulu

Waziri Mkuu amweka kikaangoni mweka hazina Sikonge



Tabora. Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amempa siku 15 Mweka Hazina wa Wilaya ya Sikonge, Evans Shemdoe ajieleze ni kwa nini ameshindwa kufikisha asilimia 80 ya makusanyo ya ndani.
Waziri mkuu ametoa agizo hilo leo Alhamisi wakati akizungumza na watumishi na watendaji wa wilaya hiyo, mjini Sikonge.
“Nataka maelezo yakayoniridhisha ni kwa nini hamkufikisha asilimia 80 ya makusanyo ya halmashauri ambacho ni kiwango cha chini. Nzega TC wamefikisha asilimia 112, Kaliua wana asilimia 91, Nzega DC wana asilimia 80, ni kwa nini wewe umeshindwa kufikisha kiwango hicho?Alihoji Waziri Mkuu.
“Ninataka nipate maelezo pia ni ipi mipango yenu ya kukusanya mapato kwa maeneo mliyoshindwa kufanya vizuri na pia mmejipangaje kwa mwaka ujao wa fedha. Niyapate maelezo hayo ifikapo tarehe 25 Agosti,” amesema.
Alipopewa nafasi ya kujieleza, Shemdoe alisema wamefikisha asilimia 76.7 na wameshindwa kufikia lengo kwa sababu ya upungufu wa mvua katika msimu uliopita, hali ambayo ilichangia kushuka kwa mavuno ya zao la tumbaku miongoni mwa wakulima.
Hata hivyo, Majaliwa aliwataka watumishi wa wilaya hiyo, washirikiane na watendaji na madiwani ili kuongeza mapato ya wilaya hiyo badala ya kuwaachia watendaji wa kata peke yao.







DKT TIZEBA ATEUA WAJUMBE WA BODI ZA WAKURUGENZI WA BODI ZA MAZAO CHINI YA WIZARA YA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI


Wajasiriamali, wadau wa biashara wakutana UDSM

Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam

Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Profesa Rwekaza Mukandala  
Dar es Salaam. Wajasiriamali, watalaamu na wadau wa biashara wamekutana kwa ajili ya kujadili namna ya kuwazesha wafanyabiashara wa kati, wakubwa na wadogo ili kukuza biashara zao zitakazosaidia kuongeza pato la Taifa.
Wajasiriamali na wadau wamekutana leo Alhamisi katika mkutano wa 17 wa wajasiriamali uliondaliwa na Shule Kuu ya Biashara ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDBS).
Akifungua mkutano huo, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Profesa Rwekaza Mukandala alisema mkutano huo ni muhimu kwa wajasiriamali na ni miongoni mwa juhudi zinazofanywa na katika kuwasidia wafanyabiashara wa kubwa, wa kati na wadogo ili kuijenga Tanzania ya viwanda.
"Lengo na mkutano huu wa 17 ni kuwasidia wafanyabiashara na wajasiriamali mbinu za kufanikiwa katika shughuli zao. Kuna vikwazo vingi wanakutana navyo ikiwamo mtaji mdogo  na mazingira yasiyo rafiki kwao,"alisema Profesa Mukandala.
Alisema mkutano ni wa siku mbili  na baada ya majadiliano washiriki watatoka na maazimio na yatakayokuwa chachu ya kukuza biashara zao kwa wafanyabiashara na wajasiriamali na yatasambazwa kwao kupitia njia mbalimbali ikiwamo vyombo vya habari.
Mkuu wa shule hiyo, Dk Ulingeta Mbamba alisema zaidi ya mada 50 zitwasilishwa kutoka kwa washiriki mbalimbali wa ndani ya nchi na nchi za  nje nane  zikiwamo za Afrika Mashariki.
Mbali na hilo, Dk Mbamba alisema shule hiyo itaendelea  kutoa elimu kwa wajasiriamali wa dogo, wakubwa na wakati sanjari na kuwatafutia mbinu za kutafuta masoko na namna ya kutunza fedha zao.
Mkuu wa Taasisi  Kuendeleza Sekta za Fedha (FSDT), Peter Kingu alisema mkutano huo utasaidia pia kubadilishana kuhusu ujasiriamali  miongoni wa washiriki kwa kuwa baadhi ya wamefanya tafiti mbalimbali .

Utaratibu wa kuingiza, kutoa hela nchini wawekwa


Dar es Salaam. Wizara ya Fedha na Mipango imeandaa kanuni za taarifa za usafirishaji na uingizaji wa fedha taslimu kutoka na kwenda nje ya nchi ambapo wasafirishaji wa fedha taslimu na wasafiri wote wanaotoka au kuingia nchini, watatakiwa kutoa taarifa za fedha taslimu wanazosafirisha ikiwa fedha hizo zinalingana au zinazidi kiasi cha dola za Marekani  10,000.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa warsha ya siku mbili ya maandalizi ya utekelezaji wa kanuni hizo, Kamishna na Mtendaji Mkuu wa Kitengo cha Kudhibiti Fedha Haramu (FIU),  Onesmo Makombe alisema utekelezaji wa kanuni hizo, pamoja na mambo mengine utaiwezesha nchi kuwa na takwimu za usafirishaji fedha taslimu.
“Takwimu hizo zitakazosaidia pamoja na mambo mengine kubaini vitendo vya kihalifu, kupunguza utoroshaji wa mitaji na kuhakikisha kuwa tunapunguza kama siyo kumaliza kabisa usafirishaji wa fedha zitokanazo na uhalifu na fedha kwa ajili ya kufadhili ugaidi,” alisema Makombe
Vilevile kanuni hizo zimeweka adhabu zitakazochukuliwa dhidi ya wale watakabainika kutaka kupita na fedha zinazolingana au zinazozidi kiwango kilichowekwa bila kutoa  taarifa au watakaotoa taarifa za uongo.
Alizitaja adhabu hizo kuwa ni pamoja na kukamatwa kwa fedha taslimu walizonazo na kuchukuliwa hatua nyingine za kisheria kama vile kufunguliwa mashtaka.
“Wahalifu pamoja na mambo mengine, wanapenda kusafiri na fedha taslimu kwani wanaogopa kutumia benki kutuma fedha kutokana na umakini unaoongezeka katika benki na udhaifu unaoweza kuwepo mipakani,”  alisema Makombe.
Kamishna huyo amewaasa washiriki wa warsha hiyo kutekeleza jukumu hilo  kwa uadilifu na uaminifu mkubwa  ili kuziba mianya yote ambayo wahalifu wanaweza kuitumia kutimiza kusudi lao ovu na kuhatarisha usalama wa nchi.

Rais Magufuli awafurahisha wafanyakazi Tanesco


Dar es Salaam. Chama cha Wafanyakazi wa Shirika la Umeme Tanesco (Tuico) wamepongeza Rais John Magufuli kwa uamuzi wake wa kutekeleza mradi wa umeme wa maji Rufiji.
Akizungumza leo Alhamisi,Mwenyekiti wa Tuico Tanesco, Athuman Hassan amesema mradi huo wa megawati 2000 utakuwa na manufaa kwa uchumi wa viwanda.
"Wafanyakazi tunamuunga mkono, tutamsaidia kwa kufanya kazi kwa weledi ili kuhakikisha tatizo la umeme Tanzania linakuwa historia,"amesema.
Amesema kukamilika kwa mradi huo wa Stieglers Gorge utamaliza tatizo la umeme na mwingine kuuzwa nje ya nchi.
Kuhusu vishoka, amesema watakuwa wakali kwa watu wanaojitambulisha kuwa ni wafanyakazi wa Tanesco wakati siyo.
"Tunaomba wananchi kutupa ushirikiano ili kuwatia nguvuni vishoka wanaowatapeli wateja wetu,"amesema.

Polisi waua 13 Kibiti, wakamata silaha nzito




Dar es Salaam. Jeshi la Polisi Jeshi la Polisi limedai kuwaua watu 13 wanaotuhumiwa kufanya mauaji wilayani Kibiti mkoani Pwani na limekamata bunduki nane, magazini mbili, risasi 158, mabomu manne, pikipiki mbili, vitenge na begi.
Taarifa ya Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP), Simon Sirro iliyotolewa jana imeeleza kuwa Agosti 4, katika eneo la Gari Bovu, Kijiji cha Chamiwaleni wilayani hapo polisi walimkamata Abdallah Mbindimbi Abajani akiwa ana majeraha maeneo mbalimbali ya mwili wake akionekana kuwa alikuwa anaendelea kujitibu mwenyewe kwa kificho.
Alisema alipohojiwa kuhusiana na tuhuma zinazomkabili, alikubali na alionyesha dhamira ya kwenda kuonyesha ngome yao.
Alisema juzi katika mapori ya Kijiji cha Rungungu, mtuhumiwa huyo aliwaonyesha polisi ngome ya watuhumiwa wenzake aliokuwa anashirikiana nao kufanya uhalifu.
“Baada ya kukaribia eneo la tukio ulitokea upinzani mkali wa majibizano ya risasi jambo lililosababisha hata Abdallah Mbindimbi Abajani kujeruhiwa kwa risasi sehemu mbalimbali za mwili wake.”
Alisema kutokana na majibizano hayo, polisi waliwajeruhi wahalifu 12 ambao baadaye walifariki dunia, (akiwamo Abdallah) kwa nyakati tofauti wakipelekwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kutokana na kuvuja damu nyingi zilizosababishwa na majereha ya risasi.
“Miili ya marehemu imehifadhiwa kwenye chumba cha kuhifadhia maiti Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.”
Aliwataja watuhumiwa saba kati ya 13 waliopoteza maisha kuwa ni Hassani Ali Njame, Abdallah, Saidi Abdallah Kilindo, Abdulshakuru Mohamed Ubuguyu, Issa Mohamed Mseketu, Rajabu Thomas na Mohamed Ally Kadude Upolo.
“Miili 6 (sita) iliyobaki haikuweza kutambulika mara moja hivyo utambuzi utaendelea huko ilikohifadhiwa hospitalini.”
“Taarifa za utambuzi wa vielelezo vilivyopatikana eneo la tukio na utambuzi wa baadhi ya miili ya watuhumiwa waliofariki zinaonyesha kuwa walishiriki matukio ya uhalifu maeneo mbalimbali kama ifuatavyo:
“Kuua OC CID na watumishi wawili wa Idara ya Maliasili katika tukio la Jaribu Mpakani, Wilaya Kibiti. Kuua askari polisi wanane katika tukio la Mkengeni wilayani Kibiti.”
Alisema matukio mengine ni kuua trafiki wawili katika eneo la Bungu “B” wilayani Kibiti, kumuua diwani wa zamani CCM katika tukio la Kibwibwi wilayani Kibiti na kuua ofisa mtendaji, mwenyekiti wa mtaa na mkulima katika tukio la Kijiji cha Mangwi wilayani Kibiti.

‘Ka-ta’ yaingiza Sh41 bilioni


Dar es Salaam. Agizo la neno moja ambalo Rais John Magufuli aliligawa na kutoa mawili la (kata), akiagiza Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) kuwakatia huduma wadaiwa sugu, limeingiza Sh41 bilioni ndani ya miezi mitano.
Machi 6, wakati Rais Magufuli akiweka jiwe la msingi kwenye kituo kipya cha Tanesco mkoani Mtwara, alilitaka shirika hilo kuwakatia huduma wadaiwa sugu zikiwamo taasisi, mashirika ya umma na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) iliyokuwa inadaiwa Sh21 bilioni.
“Tanesco pasitokee taasisi au wizara, hata Ikulu isipolipa umeme we kata tu. Natumia maneno mawili ka-ta, hatuwezi kujiendesha kwa hasara wakati kuna watu wanakwepa kulipia gharama,” aliagiza Magufuli.
Kufuatia agizo hilo, Shirika la Umeme Zanzibar (Zeco) na Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) waliokuwa miongoni mwa wadaiwa sugu walianza kulipa.
Akizungumza Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa Viwanda na Biashara (Tuico) tawi la Tanesco, Hassan Athuman alisema awali kiwango kilichokuwa kikidaiwa ni Sh275 bilioni.
Athuman alitoa mchanganuo wa malipo hayo kuwa ni Zeco imelipa Sh18 bilioni, taasisi za Serikali Sh18 bilioni na watu binafsi Sh5 bilioni.
“Wafanyakazi wa Tanesco tumeamua kumpongeza na kumuunga mkono Rais Magufuli kwa jitihada zake za kuhakikisha wadaiwa sugu wanalipa,” alisema Athuman.
Alifafanua kuwa wanamuahidi Rais Magufuli hawatamuangusha.
Katibu wa Tuico tawi la Tanesco, Mwandu Chandarua alisema licha ya madeni, wafanyakazi wamefurahishwa na Serikali kuahidi kutekeleza mradi wa umeme wa maji wa Stieglers Gorge wilayani Rufiji. Awali, Serikali ilisema mradi huo utakaotoa megawati 2,000 utajengwa kwa fedha za ndani.
“Tuna uhakika mradi huu na mingine inayotekelezwa, ikikamilika tutakuwa na umeme unaotutosha na mwingine tunaweza kuuza nje ya nchi,” alisema.
Kuhusu vishoka, Chandarua aliwataka wananchi kuhakikisha wanawasiliana na ofisi kama wanahitaji msaada, badala ya kutafuta watu mitaani.