Tuesday, July 25

PROFESA LIPUMBA AWATIMUA WABUNGE NANE WA VITI MAALUM NA MADIWANI WAWILI WA CUF


Baraza Kuu la Uongozi la Taifa la Chama cha Wananchi, CUF linaloongozwa na Profesa Ibrahim Lipumba limewavua uanachama wabunge nane wa chama hicho kwa madai ya utovu wa nidhamu, yakiwemo kukisaliti chama hicho.
Mwenyekiti huyo wa CUF, anayetambuliwa na Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa, amesema, baraza pia limewavua uanachama madiwani wawili wa viti maalumu mkoani Dar es Salaam kwa makosa kama hayo. 
 Profesa Lipumba ametangaza uamuzi huo leo wakati wa mkutano na wanahabari uliofanyika makao makuu ya CUF, Buguruni, Dar es Salaam. Amesema wabunge hao nane ni kati ya 10 walioitwa hivi karibuni na Kamati ya Maadili na Nidhamu kwa mahojiano wakitakiwa kujibu tuhuma zinazowakabili za kukihujumu chama hicho kwa maelezo kuwa walitaka kushirikiana na CHADEMA kumwondoa yeye madarakani

KUKAMATA VIONGOZI WA KISIASA NA VIONGOZI WA DINI SI KOSA“ IGP SIMON SIRRO


Mkuu wa jeshi la Polisi Nchini Simon Sirro amesema kukamata viongozi wa kisiasa na dini si kosa bali ni sehemu ya majukumu ya Jeshi la polisi kukamata kama amevunja sheria. Hii hapa video yenye Kazi yetu Ruvuma TV ni kuhabarisha umma, hivyo tumekusogezea matukio sita yaliyotokea mkoani Ruvuma kuanzia Jul 17 – Jul 23, 2017. 

TIMU YA TANZANIA YASHIRIKI MASHINDANO YA ROBOTI NCHINI MAREKANI


Tarehe 16-18 Julai, 2017 Tanzania iliwakilishwa na Timu ya wanafunzi saba katika Mashindano ya Ubunifu yajulikayao kama First Global Robotic Challenge yaliyofanyika jijini Washington D.C

Timu hiyo iliongozwa na wakufunzi wawili, Bi. Mkufu Shaban Tindi na Bi. Carolyne Eryarisiima.

Tarehe 19 Julai, 2017 Timu hiyo ilitembelea Ofisi za Ubalozi wa Tanzaniani Washington, DC nchini Marekani kwa ajili ya kusalimia na kujitambulisha.

YONO KUPIGA MNADA JENGO LA ABLA COMPLEX LA MIKOCHENI JIJINI DAR ES SALAAM AGOSTI 12, 2017


 Kampuni ya udalali ya Yono Auction Mart inatarajia kupiga mnada jengo la Abla Complex lenye urefu wa ghorofa saba lililopo Mikocheni Dar es Salaam kutokana na mmiliki wake kushindwa kulipa mkopo anaodaiwa na KCB Bank Limited.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni hiyo Bi. Scholastica Kevela, Yono wataendesha Mnada huo August 12, 2017 hapo hapo mjengoni, na amekaribisha yeyote mwenye nia ya kununua jengo afike kwenye mnada huo kuanzia saa nne na nusu asubuhi (From 10.30 am).
 
 

TANZANIA NA MSUMBIJI ZAPANIA KUENDELEA KUDUMISHA MAHUSIANO


Mkuu wa mkoa wa Mtwara HALIMA DENDEGO Kwa kushirikana na mkuu wa mkoa wa RUVUMA DKT BILINITH MAHENGE wamesema watahakikisha wanaboresha mahusiano mema kati ya TANZANIA na pamoja na MAJIMBO YA NIASSA,na CABO DELGADO nchini MSUMBIJI hususani katika kuboresha miundombinu ili kuweza kutoa fursa wa wananchi katika pande hizo mbili hayo yamesemwa wakati wa kuitimisha mkutano wa ujirani mwema katika ya majimbo hayo kutoka MSUMBIJI na mikoa ya ruvvuma na mtwara. 

Msigwa ammiminia sifa Wakili Fatma Karume



Wakili Fatma Karume

Wakili Fatma Karume 
Dar es Salaam. Mbunge wa Iringa Mjini (Chadema) Mchungaji Peter Msigwa, amesema Wakili Fatma Karume ni miongoni mwa watoto wa viongozi wanaojitambua.
Msigwa ameandika katika ukurasa wake wa instagram leo na kusema, Fatma anajitambua na ndiyo maana hatembelei jina la baba yake.
Fatma ambaye ni miongoni mwa washirika wa kampuni ya uwakili ya IMMA, ni mtoto wa Rais Mstaafu wa Zanzibar, Amani Abeid Karume.
“Anajiamini, ni mshindani mzuri, ni mfano mzuri kwa wanawake hapa nchini,” amesema Msigwa.
Kwa sasa Fatma ndiye anamtetea Mbunge wa Chadema, Tundu Lissu katika kesi yake ya uchochezi.

Graca Machel amjia juu daktari aliyeandika kitabu cha Mandela

Mjane wa aliyekuwa Rais wa Afrika Kusini,

Mjane wa aliyekuwa Rais wa Afrika Kusini, Nelson Mandela, Graca Machel 
Nelson. Mjane wa aliyekuwa Rais wa Afrika Kusini, Nelson Mandela, Graca Machel, amesema atamshitaki daktari wa Mandela, kutokana na taarifa alizochapisha kwenye kitabu kuhusu siku za mwisho za Mandela.
Daktari huyo, Vejay Ramlakan aliongoza kikosi kilichomhudumia Mandela hadi kifo chake Desemba mwaka 2013.
Radio ya taifa nchini Msumbiji ilitangaza taarifa iliyotolewa na Machel ikilaani kitabu hicho vikali.
Machel amesema kuwa kitabu hicho kinakiuka heshima ya Mandela.
Kitabu hicho kimeandika taarifa kuhusu siku za mwisho kabla ya kifo cha Mandela, kimetaja kutokuwepo kwa maelewano kati ya madaktari na familia ya Mandela.
Machel anasema kuwa kitabu hicho kilikiuka siri iliyo kati ya daktari na mgonjwa.

Ruto awashutumu Nasa kwa kuchochea ghasia



Makamu wa Rais, William Ruto

Makamu wa Rais, William Ruto 
Nairobi, Kenya. Makamu wa Rais, William Ruto amewashutumu viongozi wa upinzani kwa kutoa madai ya uongo dhidi ya wanajeshi ili kuchochea wafuasi wao wazue fujo baada ya uchaguzi.
Ruto alidai jana Jumatatu kwamba muungano wa upinzani, Nasa, umetambua kuwa utashindwa uchaguzi ujao wa urais hivyo viongozi wake wanatafuta njia ya kupinga matokeo kwa kutumia ghasia baada ya uchaguzi.
“Inafahamika wazi kuwa upinzani umetambua utashindwa ndiyo maana unapanga kuanzisha ghasia kwa vile sasa mahakama imethibitisha uchaguzi utakuwa Agosti 8,” alisema.
Makamu wa Rais alisema hayo alipokuwa katika mikutano ya kampeni maeneo ya Kuresoi, Rongai, Likuyani na Amagoro katika Kaunti za Nakuru, Kakamega na Busia.
“Sasa wanatoa madai dhidi ya wanajeshi wetu na polisi kwa sababu njama yao ya awali ilifeli na wanataka kusababisha fujo siku ya uchaguzi,” akadai.
Viongozi wa Nasa wakiongozwa na mgombea urais Raila Odinga walidai wanajeshi wanatumiwa katika njama ya kuiba kura za urais.
Matamshi hayo ndiyo Ruto alisema ni ya uchochezi na yanatokana na kuwa upinzani hautaki pawepo usalama katika vituo vya kupigia kura.

Mugabe afanya kufuru sherehe ya shemeji yake



Rais wa Zimbabwe, Robert Mugabe

Rais wa Zimbabwe, Robert Mugabe 
Harare, Zimbabwe. Rais wa Zimbabwe, Robert Mugabe amemzawadia shemeji yake, Junior Gambochuma zawadi ya Dola 60,000 (Sh 133.2milioni) katika sherehe ya siku yake ya kuzaliwa.
Pia watoto wake (Gambochuma) wamempa dola 10,000 kama zawadi. Gazeti la Serikali la nchi hiyo, The Herald limeeleza.
Katika sherehe iliyofanyika shambani kwa Rais huyo mwenye umri wa miaka 93, Mugabe amesema anampa zawadi hiyo shemeji yake kwa kuwa amekuwa mlezi wa kiroho wa watoto wake.
Gambochuma, ni dada mkubwa wa mke wa Mugabe, Grace.
Mugabe alisema Gambochuma ambaye ni mchungaji ni mtu muhimu katika familia hiyo kwa kuwa amekuwa akiwalea watoto wake kwa kuwafundisha dini.

Mtoto aliyezaliwa na VVU aishi bila ya virusi kwa miaka minane


Afrika Kusini. Wanasayansi Afrika Kusini wamebaini kwamba mtoto aliyeambukizwa virusi vya Ukimwi, ameishi kwa miaka minane na nusu bila viini hivyo.
Mtoto huyo alipewa dawa za majaribio ya kukabiliana na virusi hivyo alipozaliwa lakini hajapewa dawa zozote za kukabiliana na  virusi hivyo tangu afikishe mwaka mmoja.
Hii ni mara ya kwanza kwa mtu mwenye VVU kuishi bila virusi hivyo barani Afrika.
Wanasayansi waliogundua kuhusu afya ya mtoto huyo mwenye miaka 9 na nusu kwa sasa, wanamuangalia na kumfuatilia kwa karibu zaidi.
Wanasema kuwa matukio kama hayo ni machache na kwamba familia ya mtoto huyo ina furaha.
Watafiti wanaamini kupotea huko kwa vurusi sio kwa sababu ya matibabu lakini mtoto huyo ana jeni ama kinga zisizokuwa za kawaida ambazo zimemlinda dhidi ya virusi vya Ukimwi.

TRA yaidai Acacia 'bajeti ya miaka 13'


Dar es Salaam. Mamlaka ya Mapato (TRA) imeitaka Kampuni ya Acacia kulipa zaidi ya Sh424 trilioni kutokana na ukwepaji kodi ilioufanya kuanzia mwaka 2000. Kwa kutumia bajeti ya sasa, fedha hizo ni sawa na bajeti ya Tanzania ya miaka 13.
Deni hilo, ambalo ni sawa na dola 190 bilioni za Kimarekani limetokana na hesabu zilizopigwa kwa kutumia taarifa iliyotolewa na kamati mbili zilizoundwa na Rais John Magufuli kuchunguza usafirishaji wa mchanga wa madini unaofanywa na kampuni hiyo kutoka migodi ya Bulyanhulu na Buzwagi.
Taarifa iliyotolewa jana na kampuni hiyo imekataa kulipa deni hilo kwa maelezo kwamba haijapewa ripoti ya kamati zote mbili.
“Hatuyakubali makadirio haya. Kampuni itaangaalia haki na namna zote zilizopo kuhusu suala hili,” inasema taarifa hiyo.
Kwa mujibu wa Acacia, deni hilo limeelekezwa kwa kampuni zake tanzu ambazo ni Bulyanhulu Gold Mine (BGML) inayoendesha mgodi wa Bulyanhulu, na Pangea Minerals (PML) inayosimamia mgodi wa Buzwagi.
Taarifa hiyo iliyopokelewa jana kutoka TRA inadai kodi hiyo ni kuanzia mwaka 2000 mpaka 2017 kwa BMGL na kati ya mwaka 2007 hadi 2017 kwa PML. Katika deni hilo, kodi ambayo haikulipwa ni dola40 bilioni za Kimarekani (zaidi ya Sh88 trilioni) pamoja na dola 150 bilioni (zaidi ya Sh330 trilioni) ambazo ni  faini na riba.
Bajeti ya mwaka 2017/18 ya Serikali ya Tanzania ni Sh31.7 trilioni na hivyo fedha hizo zinaweza kugharimia bajeti ya miaka 13 na miezi mitatu bila kutegemea misaada ya wahisani.
Endapo kila Mtanzania atapewa mgao kutoka kwenye fedha hizo, kati ya wananchi milioni 56 (kwa mujibu wa Benki ya Dunia) kila mmoja angepata zaidi ya Sh7.57 milioni. Fedha hizo pia ni zaidi ya mara nane ya deni la taifa ambalo ni takribani Sh51 trilioni ka sasa.
Mkurugenzi wa Elimu ya Mlipakodi wa TRA, Richard Kayombo hakuwa tayari kuzungumzia suala hilo.
“Kwa sasa siwezi kutoa maoni yoyote kwa sababu mawasiliano hufanyika kati yetu na mteja. Hata hivyo, sina waraka wowote ninaoweza kuutumia,” alisema Kayombo.
Sakata la Acacia lilianza wakati Rais John Magufuli alipozuia usafirishaji wa mchanga nje mwaka jana na baadaye Machi mwaka huu.
Makontena 277 yaliyokuwa bandarini kusubiri kupelekwa nje kwa ajili ya kuyeyushwa, yalizuiwa na baadaye Rais kuunda kamati kwa ajili ya kuchunguza kiwango cha madini kilichokuwa kwenye mchanga huo.
Siku chache baadaye, Rais aliunda kamati nyingine iliyopewa jukumu la kuangalia athari za kiuchumi ambazo nchi ilipata kutokana na kusafirisha mchanga huo nje.
Acacia inasafirisha mchanga huo nje kwa ajili ya kuuyeyusha kupata mabaki ya madini ya dhahabu na shaba ambayo yalishindikana katika hatua ya awali ya uchenjuaji ambayo hufanyika mgodini.
Acacia inadai kuwa kiwango cha dhahabu kilichomo kwenye mchanga huo ni takriban asilimia 0.3, lakini kamati iliyoundwa na Magufuli ilisema kuwa kiwango cha dhahabu ni mara kumi ya kile kilichotangazwa na wawekezaji hao kutoka Canada.
Matokeo hayo yalimfanya Rais Magufuli kutengua uteuzi wa Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo, kumsimamisha kazi mkurugenzi mkuu wa Wakala wa Ukaguzi wa Madini (TMAA) pamoja na kamishna wa madini.
Pia aliagiza wafanyakazi wa TMAA kutoendelea kufanya kazi kwenye migodi hiyo hadi hapo utakapotolewa uamuzi mwingine.
Rais pia alimuagiza Waziri wa Sheria na Katiba, Profesa Palamagamba Kabudi kuunda jopo la wanasheria kwa ajili ya kuangalia mabadiliko ya sheria ya madini na kuwasilisha bungeni mapendekezo ya mabadiliko hayo.
Tayari mabadiliko hayo yameshapitishwa na Bunge, ambayo yanaipa mamlaka Serikali kufanya mazungumzo upya na kampuni za uwekezaji kwenye madini na pia kuongeza mrabaha kutoka asilimia nne hadi sita.
Kamati ya pili iliibuka na matokeo yaliyoonyesha kuwa Tanzania imepoteza zaidi ya Sh108 trilioni kwa kusafirisha mchanga huo kwa miaka 20.
Kamati hiyo pia ilidai kuwa Acacia haijasajiliwa nchini na haina leseni ya kufanya biashara nchini na hivyo shughuli zake ni kinyume cha sheria.
Kamati hiyo pia ilinyooshea vidole wanasiasa na watumishi wa umma walioshiriki kuingia mikataba na kampuni za uwekezaji kwenye madini na pia walioshughulikia mabadiliko ya sheria ya madini ambayo yalilenga kuipunja nchi.
Hata hivyo, Acacia imekataa kuzikubali ripoti za kamati zote mbili ikisema haikushirikishwa na kwamba kamati hizo hazikuwa huru.
Acacia imekuwa ikisisitiza kuwa uchunguzi huo haukufanywa na kamati huru na hivyo kutaka iundwe kamati huru kufanya uchunguzi huo.
Pia imekuwa ikijitetea kuwa imekuwa ikitoa taarifa sahihi kuhusu kiwango cha madini kilichomo kwenye mchanga huo kuwa ni sahihi na kwamba kama matokeo ya uchunguzi wa kamati ya kwanza yangekuwa sahihi, Tanzania ingekuwa mzalishaji mkubwa wa dhahabu duniani.
Kuhusu matokeo ya kamati ya pili, Acacia imesema pia inaipinga kwa kuwa ilifanya tathmini yake kwa kuzingatia matokeo ya kamati ya kwanza, ambayo haikubaliani nayo.
Pamoja na hayo, mwenyekiti mtendaji wa Barrick Gold, ambayo ni kampuni mama ya Acacia, Profesa John Thornton (pichani) alikuja nchini kwa ndege ya kukodi kutoka Canada kwa ajili ya kuzungumza na Rais Magufuli.
Baada ya mazungumzo hayo, Rais aliwaambia waandishi wa habari kuwa Acacia imekubali kuwa ilifanya makosa na kwamba imeahidi kulipa fedha ambazo zitabainika kuwa hazikulipwa.
Alisema Serikali na kampuni hiyo zimekubaliana kuunda timu ya kufanya mazungumzo ya kutafuta muafaka wa suala hilo.
Hata hivyo, Acacia imesema haitashiriki kwenye mazungumzo hayo na badala yake Barrick ndiyo itahusika isipokuwa makubaliano yoyote yatakayofikiwa ni lazima yaridhiwe na kampuni hiyo.
Acacia pia imeshatoa notisi mahakamani kuonyesha nia yake ya kufungua kesi kupinga maamuzi hayo ya Serikali.