Thursday, July 16

UCHAGUZI CCM: Mambo matano mazuri ya Magufuli akiwa rais

Dk John Magufuli akiwasalimia Wajumbe wa Mkutano Mkuu 
katika ukumbi mpya wa CCM mjini Dodoma kabla ya kuanza kupiga kura juzi usiku.
Chama cha Mapinduzi (CCM) kimempitisha Dk John Pombe Magufuli kuwa mgombea urais wa chama hicho kwa ajili ya uchaguzi mkuu wa Tanzania utakaofanyika Oktoba 25, mwaka huu.
Kwanza kabisa napenda kumpongeza sana Magufuli kwa hatua aliyofikia na kumtakia kila la heri. Naomba kukiri kwa uwazi kwamba katika uchaguzi unaohusisha vyama vya siasa ni lazima mshindi atapatikana na kwa Tanzania ni lazima mshindi huyo atoke kwenye chama cha siasa.
Tanzania ina vyama 22 vilivyosajiliwa na vinavyofanya kazi sasa, tutake tusitake ni lazima rais wa nchi atatoka katika chama kimojawapo, na kwa sababu CCM imeshapitisha mgombea wake na yeye ana fursa ya kushinda uchaguzi kama ambavyo fursa hiyo ilivyo kwenye vyama vingine. Natumia nafasi hii kufanya uchambuzi wa dhati juu ya taswira ya serikali ya Magufuli ikiwa atafanikiwa kushinda uchaguzi wa mwaka huu. Taswira ya namna hii pia nitaifanya kwa wagombea wengine wa vyama ambavyo vitaamua kuweka wagombea urais.
Katika kulifanya jukumu hili nitachambua masuala 10 ambayo nafikiri kwamba yanaweza kujenga utawala wa Magufuli, ikiwa atachaguliwa na Watanzania kuwa rais wa awamu ijayo.
Mambo matano kati ya hayo nayatazama kama taswira bora na mengine matano yanaweza kuwa taswira hasi. Katika uchambuzi wa leo nitaanza na mambo matano ambayo ni taswira bora.
Usimamizi bora
Taswira ya kwanza ambayo Magufuli anaweza kuirejesha bila wasiwasi ni usimamizi thabiti wa serikali na nidhamu ya utendaji ndani ya serikali. Naamini kuwa serikali ya Magufuli itakuwa ya kiusimamizi na yeye mwenyewe anaweza kulifanya jambo hilo bila kusita. Katika nyadhifa nyingi alizopitia hadi sasa ameijenga taswira hii kila alikopita na bado inambeba hata ikitokea anachaguliwa kuwa rais wa awamu ya tano.
Tukumbuke kuwa moja ya mambo ambayo yameanguka kabisa nchini hivi ni utendaji ndani ya serikali. Tunafahamu kuwa wafanyakazi ndani ya serikali ukiachilia mbali matatizo waliyonayo kwa maana ya vipato, hata mambo madogo ambayo wangeweza kuyasimamia ndani ya dakika au saa chache huchukua wiki kadhaa na hata miezi kadhaa. Utaratibu wa utoaji huduma umekwama sana na nadhani kama akiwa na uwezo huo atafanikiwa kutatua changamoto kubwa na ya siku nyingi. Ikiwa utendaji wa serikali unaimarika na huduma zinatolewa kwa wakati, tutaweza kujenga taifa linalokwenda mbele bila kujali chama gani kiko madarakani.
Msimamo imara
Taswira bora ya pili ya serikali ya Magufuli inaweza kuwa ni misimamo katika masuala ya msingi na kutoyumba sana. Magufuli muda wote ambao amekuwa kiongozi ameonyesha jambo hilo. Kila mara amekuwa na misimamo hata kama siyo sahihi. Kwa tafsiri nyingine hii huwa ni njia bora ya uongozi wa nchi japokuwa misimamo ya serikali au kiongozi mkuu wa serikali huwa haipaswi kuwa juu ya haki na matakwa ya wananchi.
Moja ya mambo ambayo serikali iliyopita ilikosa, ni pamoja na kukosa misimamo na kuwa na “double standard”. Mfano mdogo tu ni kwenye mchakato wa katiba mpya ambapo Rais anayeondoka alisimamia uanzishwaji bora wa mchakato huo, akaunga mkono katika hatua zote na rasimu zote, lakini akaja kuwageuka wajumbe wa tume hiyo na rasimu yao ya pili alipolihutubia Bunge Maalumu la Katiba. Naamini Magufuli si mtu wa kugeuka na kuna masuala mengi anaweza kuyasimamia kwa dhati na kila mmoja wetu akakubali kuwa, naam! Hapa kuna kiongozi anasimamia masuala haya.
Uwezo wa kusimamia miradi
Taswira ya tatu ya serikali inayoweza kuundwa na Magufuli ikiwa atachaguliwa kuwa rais ni uwezo wa kusimamia miradi ya maendeleo. Magufuli ni mtu wa namna hiyo na ametuonyesha katika sekta ya ujenzi na hasa katika eneo la barabara. Moja ya masuala ambayo nayaona kama mafanikio makubwa ya serikali ya Kikwete ni ujenzi wa barabara, ukiniuliza, nitakwambia jambo hili ndilo Kikwete anapaswa kujivunia atakaporudi nyumbani kwake pale ‘Msoga’. Lakini aliyeleta mapinduzi hayo kiusimamizi ni Magufuli.
Mwalimu Nyerere aliwahi kusema kuwa “ikitolewa tenda ya ujenzi wa barabara nchini Tanzania na India halafu nchi zote zikakabidhi tenda hizo kwa watoto wa marais wa nchi, kule India walau barabara ya ‘kudanganyishia’ itajengwa lakini hapa Tanzania unaweza usione hata kokoto” (tafsiri yangu). Dhana hiyo ina maana kwamba huku kwetu wizi na kujijazia manoti ndivyo vitu vinavyoshamiri na kwa tafsiri ya Mwalimu “ilipasa Magufuli awe anaongoza kwa kuchukua noti za barabara na kuzijaza tumboni kwake”,  jambo ambalo limekuwa nadra kutokea na kama liliwahi kuwepo ndiyo tutajua sasa wakati watu wataanza kutoa taarifa zake kwa sababu anataka kwenda Ikulu. Kwa uwezo huu wa kiusimamizi namuona Magufuli akisimamia miradi ya serikali kwa ustadi mkubwa hata kama siyo “waziri wa miradi” katika serikali atakayoiunda.
Mawaziri imara
Taswira ya nne nayoiona katika serikali ya Magufuli ikitokea anashinda urais wa Tanzania ni uundaji wa Baraza la Mawaziri na nyadhifa za kiutendaji zilizojaa watu wenye uwezo kuliko marafiki. Serikali zetu kadhaa zilizopita ikiwamo hii inayoondoka zimekuwa na sifa ya kubeba marafiki kufa au kupona. Siyo siri kwa JK amelalamikiwa mno na mara kadhaa serikali yake ilionekana kama “imejaa washkaji” watu wanaolindana na kuoneana haya kwa heshima za urafiki kuliko kuangalia maslahi ya nchi.
Magufuli anaweza kuwa dawa ya serikali za ushkaji kwani tangu kwenye mchakato wa kupata wagombea ndani ya CCM hakuonekana kama “kitisho” na hakuwa na makundi nyuma yake, penyeza yake ya kimya kimya hadi anakuwa mgombea urais wa CCM imemsaidia kuanza kujenga marafiki wasio na masharti ya kutaka kubebwa naye. Marais wengi huunda mitandao na mitandao hiyo huwapa fedha mapema na huwasaidia kila jambo, wanapofika madarakani huwa na deni la kuilipa mitandao hiyo, malipo yenyewe ni miradi ya serikali, tenda mbalimbali na vyeo lukuki. Naamini Magufuli hatakuwa na tatizo hilo na itamsaidia kutengeneza serikali isiyo na “washkaji kibao.”
CCM yenye nguvu
Taswira ya tano inayoweza kujitokeza ni uwezekano wa kurejesha nguvu ya CCM ambayo inasambaratika, na naamini hili linaweza kujitokeza sana hasa kwenye kipindi cha kwanza cha uongozi wake. Siamini kama ataweza kurekebisha taswira ya CCM kwa miaka mitano mingine (ikiwa atapata vipindi vyote viwili) kwa sababu hatujaona utendaji halisi wa serikali ijayo, ikiwa CCM ndiyo itashinda. Wananchi wengi hawaiamini tena CCM na jambo hilo linaweza kuipeleka ikaangushwa katika uchaguzi wa mwaka huu, lakini ikitokea CCM inavuka kizingiti na inapona kuangushwa halafu Magufuli anakuwa rais, anaweza kujizatiti na akatumia miaka mitano kufanya mambo makubwa yatakayowafanya wananchi warudishe imani kwa chama hicho. Ila akifanya vibaya sana atazidi kuididimiza. Kwa mtazamo wangu wa msisitizo ni kwamba naona akifanikiwa kwenye eneo hili, japokuwa naweka msisitizo wa pili kuwa ni lazima tusubiri kujua ikiwa atashinda kipindi chake cha kwanza kitakuwaje kiuongozi.

UCHAGUZI CCM: Mambo matano ‘mabaya’ Magufuli akiwa rais

Dk John Magufuli akiwasalimia Wajumbe wa Mkutano Mkuu 
katika ukumbi mpya wa CCM mjini Dodoma kabla ya kuanza kupiga kura juzi usiku.

Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimempitisha Dk John Pombe Magufuli kuwa mgombea urais wa chama hicho kwa ajili ya uchaguzi mkuu wa Tanzania utakaofanyika Oktoba 25, mwaka huu. Tanzania ina vyama 22 vilivyosajiliwa na vinavyofanya kazi sasa, tutake tusitake ni lazima rais wa nchi atatoka katika chama kimojawapo, na kwa sababu CCM imeshapitisha mgombea wake na yeye ana fursa ya kushinda uchaguzi kama ambavyo fursa hiyo ilivyo kwenye vyama vingine. Natumia nafasi hii kufanya uchambuzi wa dhati juu ya taswira ya serikali ya Magufuli ikiwa atafanikiwa kushinda uchaguzi wa mwaka huu. Taswira ya namna hii pia nitaifanya kwa wagombea wengine wa vyama ambavyo vitaamua kuweka wagombea urais..
Uamuzi wa haraka
Moja ya taswira mbaya zinazoweza kujitokeza na kuikumba serikali ya Dk John Magufuli (ikiwa atashinda uchaguzi) ni maamuzi ya haraka na yasiyo na tija ya uhakika. Katika utendaji mzuri wa Magufuli serikalini, madoa makubwa aliyopata ni kwa nyakati kadhaa kusimamia mambo ambayo baadaye yalilalamikiwa sana. Niliwahi kutoa mfano namna ambavyo amewahi kulalamikiwa juu ya maamuzi yake ya kubomoa nyumba za wananchi bila kuwapa muda wa kutosha kuhama. Kibinadamu hayo ni matendo ya ukatili na yanatokana na ufanyaji maamuzi wa haraka katika jambo linalohitaji muda. Sijui kama Magufuli ataachana na tabia hiyo ya “haraka haraka” ili pia kuifanya serikali yake ijiendeshe kistratejia na kimipango kuliko haraka na nguvu. Ikiwa atasonga mbele na tabia hiyo na serikali yake ikaenda kwa kasi hiyo ya “pupa” kuna uwezekano kuwa kila mambo kumi atakayoyasimamia basi mawili hadi matatu yakawa yanafanywa bila kuwa na tija kwa taifa.
Kuyumba kichumi
Mtihani wa pili ambao unaweza kujenga taswira mbovu ya utawala au serikali itakayoundwa na Magufuli (ikiwa atachaguliwa kuwa Rais wa Tanzania) ni usimamizi wa masuala ya kiuchumi. Eneo hili naliona kama muhimu sana kwa sababu kama nilivyoeleza hapo juu, Magufuli amekuwa waziri bora katika serikali inayomaliza muda wake na amekuwa akitumwa na kufanya kila jambo haraka kwa wakati na kwa maamuzi yenye misimamo. Sielewi uwanda wake katika masuala ya kiuchumi na misimamo yake kwenye eneo hilo, hapa sina maana kuwa Rais wetu lazima awe mchumi, la hasha! Benjamin Mkapa hakuwa mchumi lakini alikuwa na uwezo mpana wa kusimamia uchumi, Jakaya Kikwete ni mchumi lakini amefanya vibaya kwenye eneo hilo kuliko Mkapa. Magufuli amejionyesha mara zote kama mtendaji kuliko “mfikiriaji na mpanga mambo”. Uchumi wa nchi uliopo kama Tanzania unahitaji akili ya ziada kuweza kuufufua tena, nchi haina viwanda, inanunua kila kitu kutoka nje. JK anaiacha ikiwa hoi sana kwenye eneo hilo. Ikiwa Magufuli ataingia na mtindo wa kusimamia utendaji zaidi kuliko kufikiri na kubuni vyanzo vipya vya uchumi, serikali yake itabeba taswira ya kushindwa kusimamia uchumi.
Serikali ya mtu mmoja
Taswira nyingine ya tatu ambayo si salama na ambayo inaweza kujitokeza kwenye serikali itakayoundwa na Magufuli ni serikali ya “One Man Show” (serikali ya mtu mmoja). Watu waliozoea kuwa watendaji wa juu kama Magufuli huwa na kasumba ya kutaka kila jambo liende kama wanavyotaka kila wakati na wakiona haliendi huingilia haraka na kutaka walifanye wao wenyewe, hili ni jambo la kisaikolojia zaidi. Kilema cha serikali za namna hii huwa ni kumjenga mtu mmoja zaidi kuliko wengine si kwa makusudi, bali kwa sababu watendaji wake wanashindwa kwenda na uwezo wa rais wao. Madhara ya hali hii ni kujenga serikali inayokosa vionjo pale ambapo rais anapokuwa hayupo, kunakuwa na hofu ya dhahiri kuwa ni nani anaweza kusimamia masuala mbalimbali kama awezavyo rais na huyo mtu hayupo. Taswira hii itavunjwa tu iwapo mkuu wa nchi ataamua kuwaachia watendaji wafanye maamuzi magumu wao wenyewe, wajifunze kukosea na kukosolewa.
Haki za binadamu
Jambo la nne ambalo linaweza kuwa “taswira dhaifu ya serikali ya Magufuli” (ikiwa atashinda) ni uwezo wa kusimamia masuala ya haki za binadamu na haki za msingi za raia. Hili linaweza kuunganishwa na ile kanuni yake ya ‘kufanya maamuzi kwa mbio na haraka sana kila mara’. Maamuzi ya haraka na yasiyotoa mwanya wa kutosha wa kuzingatia masuala mengine muhimu ya haki za kiraia huwa hayana tija na huumiza dhana ya usimamizi wa haki hizo na yasipokomeshwa huwaumiza raia. Mmoja wa wajumbe wa mkutano mkuu wa CCM ambaye nimeongea naye na hakumpigia kura Magufuli katika mkutano mkuu huo amenieleza kuwa hakufanya hivyo kwa sababu nyumba yake ya urithi iliwahi kubomolewa bila kupewa muda wa kutosha kwa sababu ilikuwa karibu na barabara. Dhana ya usimamizi wa sheria lazima iendane na dhana ya kusimamia haki za raia, watu wa namna hii wanaweza kuwa wengi na ni kielelezo cha wazi kwamba Magufuli atawajibika kurekebisha sana taratibu za ufanyaji maamuzi katika serikali yake ili aweze kulinda haki za raia. Serikali yake inaweza kuepukana na taswira hii mbovu kwa kuchukua muda na kutafakari kwa kina juu ya mustakabali wa wananchi kila jambo fulani linapotokea
Mwenyekiti wa CCM
Taswira ya tano mbaya inayoweza kujitokeza katika uongozi “serikali” ya Magufuli ikiwa atachaguliwa kuwa Rais wa Tanzania ni uwezo wa kukiongoza Chama Cha Mapinduzi. Mtu yeyote hawezi kuwa na shaka na uwezo wa Magufuli katika utendaji wake muda wote serikalini, lakini kunaweza kuwa na shaka kubwa katika uwezo wa kukiongoza chama chake. Mahasimu wake kisiasa tayari wameanza kuwa na hofu na uwezo wa CCM miaka ya mbele chini ya Magufuli, namna ambavyo anaweza kupambana na changamoto za kuongoza chama chenye watu wengi wenye maslahi tofauti tofauti sana.
Ukweli uliopo ni kwamba muda wote ambao Magufuli amekuwa serikalini hakuwahi kuwa kiongozi mkubwa wa moja kwa moja ndani ya CCM. Jambo hili linatafsiriwa kama linaweza kumsababishia makosa ya kiutendaji kwa sababu ya “kutaka kujinasibisha kama yuko karibu na wanachama wa CCM” kumbe akawa anaingizwa kwenye makosa.
Mfano mzuri ni wakati anashukuru wajumbe wa mkutano mkuu wa CCM na kabla hajataja jina la mgombea mwenza, mara kadhaa alisikika akisema “CCM kwanza, chama chetu kwanza….” Na kisha baadaye ndiyo anasema “Tanzania kwanza”. Wafuatiliaji wa mambo wanaweza kuanza kuhoji, gia hii ya Magufuli ndiyo kutaka kuwaonyesha wanachama kuwa yeye anaifahamu CCM vizuri sana? Kwa chama kikongwe kama CCM unatarajia kiongozi akitanguliza maslahi, kwanza aseme “Tanzania kwanza” chama baadaye. Kusimama hadharani na kusema “Chama Kwanza, Chama Chetu kwanza…” inaleta mtazamo kwamba anaweza kujikuta anafanya makosa ya kiutendaji katika serikali yake kwa lengo tu la kutaka “kuwaridhisha wana CCM”.  Ni bora Magufuli akajiamini, akajiona ni mwana CCM imara na asijione kama vile “kapewa hisani” kuwa mgombea wa chama hicho. Kujiamini kutamfanya akitazame na kukihukumu chama chake bila woga kila mara na pia aitazame nchi yake kama kipaumbele cha kwanza kabla ya chama, kama Rais wa nchi.
Hitimisho
Magufuli ni mtu mahiri ndani ya chungu kibovu. Ule ule mkakati wa kuiokoa CCM mwaka 2005 kwa “kumleta Jakaya” ndiyo unatumika mwaka 2015 tena, kwamba CCM inajitahidi na inajaribu kutaka kuendelea kuishi kwa kutumia mgongo wa kukubalika kwa mgombea wake, kwamba Watanzania wakaipigie kura kwa kumuamini zaidi Magufuli kuliko kutazama makosa ya kihistoria ya chama hicho tangu miaka 50 iliyopita. Kwa Watanzania waliokata tamaa na uongozi unaomaliza muda wake, aina ya watu kama Magufuli wanaweza kuwa kimbilio kubwa sana kwa maana ya upigaji kura, lakini hatujui baada ya kura hizo nini kitatokea, maana Magufuli anakwenda kuzungukwa na wana CCM, na watendaji lukuki serikalini ambao kwao “kuiba fedha za umma na kufanya utendaji mbovu ni amri ya kila siku”. Mambo haya yanaweza kuanza kuwa kikwazo kikubwa kwake hadi pale atakapoamua kuchukua hatua thabiti sana.Mimi binafsi napenda kumtakia kila la heri kiongozi huyu, katika safari aliyoianza.