Thursday, November 16

Profesa Kitila ajiunga CCM


Dar es Salaam. Chama cha Mapinduzi (CCM) kimemtangaza Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji na Umwagiliaji, Profesa Kitila Mkumbo amejiunga na chama hicho.
Uamuzi huo wa Profesa Mkumbo kujiunga na CCM ameufanya ikiwa ni siku 39 zimepita tangu alipotangaza kujivua uanachama wa ACT- Wazalendo Oktoba 9.
Taarifa ya CCM aliyoitoa mwenyekiti wa chama hicho Mkoa wa Singida, Martha Mlata imesema chama hicho Mkoa wa Singida wanamkaribisha kwa mikono miwili ili waendelee kuimarisha chama katika mkoa huo.
“Nina furaha kuwatangazia wanachama na wapenzi wa CCM Mkoa wa Singida na Tanzania kwa ujuma kuwa…Profesa Kitila Mkumbo amejiunga tena na chama chetu,” amesema Mlata na kuongeza:
“Ni fursa kubwa kwa mkoa kumpokea mwalimu baada ya kumpoteza mwanafunzi siku chache zilizopita.”
Akifafanua zaidi katika mazungumzo na Mwananchi baada ya kutoa taarifa hiyo, Mlata amesema “Profesa Mkumbo amejiunga wiki moja iliyopita na amelipita ada yote aliyokuwa akidaiwa katika kipindi chote na na mimi nilichokifanya ni kuwajulisha tu wanachama wetu kuwa mwana mpotevu karudi nyumbani.”
Alipoulizwa kama ni njia ya kwenda kugombea ubunge wa Singida Kaskazini amesema “hapana, pale kuna vijana wengi sana ambao wako tayari kuwatumikia wananchi, kwanza hawezi kuacha madaraka makubwa aliyopewa na mheshimiwa Rais, yeye ameamua tu kurudi nyumbani.”
Kuhusu kujiunga CCM huku akiwa mtumishi wa umma, Mlata ambaye ni mbunge wa viti maalum wa chama hicho amesema hilo halina tatizo kwani hata alipokuwa ‘uhamishoni’ bado alijipambanua ni mwanachama wa chama fulani kwa hiyo kurejea nyumbani si kosa.

Uchaguzi majimbo mawili wakaribia


Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC),
Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Jaji Mstaafu Semistocles  Kaijage 
Dar es Salaam. Kivumbi  kutimka tena katika uchaguzi mdogo wa ubunge utakaofanyika wakati wowote katika majimbo mawili ya Singida Kaskazini na Longido.
Jimbo la Singida Kaskazini liliachwa wazi baada ya Mbunge wake,  Lazaro Nyalandu  kutangaza kujiuzulu  wakati Longido likiachwa wazi  baada ya Mahakama Kuu kutengua  matokeo ya uchaguzi wa mbunge wake, Onesmo Ole Nangole.
Taarifa ya Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Jaji Mstaafu Semistocles  Kaijage imesema  mbali na majimbo hayo, zipo kata nyingine tano zilizo wazi zitakazopaswa kufanya uchaguzi huo mdogo.
Kaijage amesema tayari tume hiyo imepokea  taarifa kutoka kwa Spika wa Bunge, Job Ndugai juu ya  kuwepo kwa nafasi  wazi ya Ubunge katika Jimbo la Singida Kaskazini baada ya  Nyalandu kuvuliwa uanachama wa CCM  na hivyo kupoteza sifa ya kuwa Mbunge. 
Amesema kwa kuzingatia masharti ya Sheria ya Taifa ya Uchaguzi Sheria ya Uchaguzi ya Serikali za Mitaa, tume hiyo  itatoa ratiba ya uchaguzi wa kujaza nafasi wazi za Majimbo hayo na kata hizo baadaye.
“Aidha, kwa mujibu kifungu cha 113(1) cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi, Sura ya 343, Tume imepokea Hati ya Mahakama Kuu ya Tanzania ikithibitisha uamuzi wa Mahakama hiyo juu ya kutengua matokeo ya Uchaguzi wa Mbunge wa Jimbo la Longido ambalo, Onesmo Ole Nangole alikuwa ni Mbunge,” ameeleza Jaji Kaijage kwenye taarifa yake.
Katika hatua nyingine, tume hiyo imesema Waziri mwenye dhamana ya Serikali za Mitaa kwa kutumia mamlaka aliyopewa chini ya kifungu cha 13(1) cha Sheria ya Uchaguzi ya Serikali za Mitaa, ameitaarifu uwepo wa nafasi wazi za madiwani katika Kata tano zilizopo katika Halmashauri mbalimbali nchini.
Taarifa hiyo imezitaja kata zilizowazi kwamba ni  Keza mkoani Kagera, Kimandol (Arusha),  Kurui mkoani Pwani, Bukumbi ,mkoani (Tabora) na Kwagunda ,(Tanga).

Rais Mugabe azungumza na wajumbe wa Sadc


Harare, Zimbabwe. Rais Robert Mugabe wa Zimbabwe ambaye anazuiliwa nyumbani wake mjini Harare amekutana na ujumbe wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika( Sadc), Serikali ya Afrika Kusini imesema.
Hata hivyo, hakuna maelezo zaidi yaliyotolewa mbali ya kusisitizwa kuwa pande hizo zimekuwa na mazungumzo mjini Harare. “ Sadc imekuwa ikikutana na Rais Mugabe Ikulu,” alisema msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Afrika Kusini, Clayson Monyela alipozungumza na AFP.
Hayo yanajiri huku mawaziri wa mambo ya nje wa Sadc wanakutana nchini Botswana katika kikao cha dharura kilichoitishwa na  mwenyekiti wa jumuiya hiyo ambaye pia Rais wa Afrika Kusini, Jacob Zuma. Mugabe amekuwa akizuiliwa nyumbani wake tangu Jumatano na amekuwa akishinikizwa aachie madaraka kwa amani.

ACT wasema ujumbe wa Rais Magufuli kwa Mpango ni binfasi

Dar es Salaam. Chama cha ACT-Wazalendo kimemjia juu Waziri wa Fedha na Mipango na Uchumi, Dk Philip Mpango kuhusu na kauli yake kupigiwa simu na Rais John Magufuli ili afikishe ujumbe kwa wabunge  wa CCM, Nape Nnauye na Hussein Bashe.
Chama hicho kimesema hakukuwa na ulazima wowote kwa Dk Mpango kueleza suala hilo bungeni kwani ni jambo binafsi kati yake na Rais Magufuli.
Hivi karibuni wakati akijibu hoja za wabunge kuhusu Mpango wa Taifa wa Maendeleo kwa mwaka 2018\2019, Dk Mpango alisema Rais Magufuli amewataka wabunge hao ambao michango yao imekosoa uendeshaji wamepeleke majina ya wawekezaji wanaokwamishwa ili awape kazi
Dk Mpango alisema, “Naomba ninongo’neza na Bunge lako Tukufu. Mheshimiwa Rais Magufuli aliposikia huu mjadala alinipigia na aliniambia hivi,” alisema Dk Mpango
“Waziri waambie ndugu yako mheshimiwa Bashe kuwa nawataka sana wawekezaji hao wa Standard Gauge Railway.
Lakini leo Novemba 16 ACT kupitia kwa kaimu mwenyekiti wake, Yeremia Maganja kimeibuka na kusema “Dk Mpango ni yeye ni waziri  na haya  mambo binafsi kati yake na Rais Magufuli na hakulazimika kuyaweka bungeni. Maana yake Dk Mpango anataka kutuonyesha Rais Magufuli ni ofisa ugavi ambaye ana uwezo wa kuelekeza miradi badala ya Bunge.
“Ndiyo maana tunasema Dk Mpango amekuwa mpango kweli, wewe unaongea na Rais unakuja kuwaambia watu? Rais angetaka angeongea na Spika.

Spika Ndugai aigomea Serikali jina la shirika



Spika wa Bunge, Job Ndugai
Spika wa Bunge, Job Ndugai 
Dodoma. Spika wa Bunge, Job Ndugai leo Alhamisi amegomea Serikali na kulazimika kuahirisha Bunge kwa muda wa saa moja ili warudi na kukubaliana kubadili jina la Shirika la Wakala wa Meli wa Taifa (NASAC)
Spika Ndugai alitoa agizo la kuahirisha Bunge baada ya mvutano wa Serikali na Kamati ya Bunge ya Miundombinu ambao walipendekeza kubadilishwa kwa jina hilo.
Mapema wakati Serikali ikijibu maoni ya wabunge kuhusu muswada huo, Spika alionyesha dhahiri kutokukubaliana na wazo la Serikali na badala yake akasimama katika mawazo ya kamati na wabunge wengine kuwa jina hilo halifai.
Mara baada ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, George Masaju kumaliza yake, Spika alihoji ni kwa nini asikubaliane na mapendekezo ya wabunge katika kubadili jina la muswada lakini mwanasheria huyo akatupia mpira kwa waziri kuwa angekwenda na majibu.
Hata hivyo, katika majumuisho ya michango ya wabunge, Waziri Profesa Makame Mbarawa alitoa sababu za kutobadilisha jina akisema halikuwa na maana yoyote na wala lililopendekezwa halikuwa na madhara kwani waliosema kuwa jina hilo ndilo lililofilisi hawakujua kuwa kulikuwa na usaliti.
“Mheshimiwa Spika, jina halina shida yoyote kwani hata lile la awali siyo kwamba lilipeleka madhara bali kilichotokea ni namna ambavyo baadhi ya watu waliokuwa ndani ya chombo hicho walikuwa ni wasaliti,” amesema Mbarawa
Baada ya hoja za waziri huyo Bunge lilikaa kama kamati na kuanza kuangalia vifungu hivyo ndipo Spika akampa nafasi mwenyekiti wa kamati hiyo Profesa Norman Sigala ambaye akasema Serikali ilikuwa imewadanganya.
“Nakushukuru mheshimiwa Spika, Serikali hapa ni kama imetudanganya maana kusema itaangalia huko mbeleni ni sawa na kutudanganya sisi, tulichokubaliana kwenye kamati sicho kilichowasilishwa bungeni,” amesema Profesa Sigala.
Spika alimpa nafasi Waziri ambaye aliendelea kuweka msimamo kuwa jina hilo liendelee kama lilivyowasilishwa na Serikali ili kama kutakuwa na marekebisho mbeleni Serikali itafanya hivyo.
Kauli ya waziri ilimuinua Spika ambaye amesema jina hilo linapeleka picha mbaya kwani haiwezekani Serikali kuunda chombo kipya kizuri lakini ikatumia jina ambalo lina maudhui mabovu.
“Hapa ndipo tunatunga sheria yenyewe, sasa kama mnaona kubadili jina kunaweza kuathiri kisheria niambie lakini kama hakuna, sioni kwa nini tuendelee kuvutana sana, naahirisha shughuli za Bunge kwa saa moja nendeni katika ukumbi wangu hapo mkutane na mjadiliane ili mkirudi hapa mniletee jina,” amesema Spika na kuahirisha Bunge
Wabunge walilipuka kwa makofi na makelele ya kumshangilia Spika huku wanasheria wakikutana kwa haraka ambapo Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Waziri wa Katiba na Sheria, Profesa Palamagamba Kabudi waliwaongoza wajumbe wa kamati na serikali haraka kuingia ukumbini kwa ajili ya kutafuta jina hilo.

Aliyejisalimisha Takukuru afikishwa mahakamani


Dar es Salaam. Aliyekuwa mhasibu mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na  Kupambana na Rushwa (Takukuru), Godfrey Gugai na wenzake watatu amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.
Gugai na wenzake watatu wamefikishwa mahakamani hapo leo Alhamisi wakikabiliwa na mashtaka 43  ikiwemo utakatishaji fedha, kughushi, pamoja na kumiliki mali wasiyoweza kuielezea.
Hatua hiyo imekuja baada ya jana kujisalimisha Takukuru siku moja baada ya kutangazwa dau la Sh 10  milioni kwa atakayetoa taarifa alipo.

Watu 11 waliofariki ajali ya ndege Ngorongoro wapatikana


Ngorongoro. Miili 11 ya abiria na rubani wa Ndege ya Shirika la Coastal Aviation iliyoanguka eneo la Creta ya Empakai yapatikana.
Ndege hiyo iligonga mlima wa kingo za creta hiyo ilianguka saa saba mchana kutokana na matatizo ya hali ya hewa.
Ilikuwa inatoka Kilimanjaro kwenda Seronera  Serengeti ikiwa na abiria 11 na wote wamefariki.
Mkuu wa Wilaya ya Karatu, Theresia Mahongo amesema zoezi la kutafuta miili limekwenda vizuri.
"Miili yote imepatikana na tutaipeleka Karatu na baadaye Arusha," amesema.
Naibu Mhifadhi wa Ngorongoro, Dk Maurus Msuha amesema wamefanikiwa kuipata miili na kuitoa eneo la ajali kutokana na ushirikiano mkubwa na wenyeji.
"Tuliwaomba kulala hapa wenyeji jana kuilinda isiliwe na wanyama na hadi leo tumeikuta miili salama," amesema.
Mmoja wa mashuhuda wa ajali hiyo, Lunda Mollel amesema ndege hiyo kabla ya kuanguka ilikuwa inazunguka kutoka eneo la milima zaidi ya dakika 20 hadi baadaye kuanguka baada ya kugonga mlima.

Mawakili wa utetezi kesi ya bilionea Msuya waingiwa hofu bastola ya askari


Moshi. Mahakama Kuu imesimama kwa muda kesi ya mauaji ya bilionea Erasto Msuya baada ya shahidi wa 16, PF 1878 Willium Mziu, ambaye ni  mkaguzi wa polisi upelelezi makao makuu kuingia na bastola mahakamani hali ambayo ilileta hofu kwa mawakili  upande wa utetezi.
Hali hiyo iliyotokea leo Alhamisi imesababisha wakili upande wa utetezi, Hudson Ndusyepo kuiambia mahakama hiyo kuwa hawawezi kuendelea kusikiliza kesi hiyo kutokana na shahidi huyo kuonekana na silaha na kumwambia Jaji Salma Maghimbi kuwa hawapo salama.
Kwa upande wake wakili upande wa mashtaka, Abdallah Chavula ameiambia mahakama hiyo kuwa shahidi huyo anaruhusiwa kuingia na silaha mahakamani kutokana na kwamba yeye ni ofisa wa polisi.
Hata hivyo, muda kidogo Jaji Salma Maghimbi aliahirisha kusikilizwa kwa kesi hiyo muda wa nusu saa moja.
Kesi hiyo ya mauaji ya kukusudia inasikilizwa na Jaji Maghimbi ikiwa na washtakiwa saba ambao ni Sharifu Mohamed, Shaibu Jumanne, Musa Mangu, Jalila Zuberi, Karimu Kihundwa, Sadik Mohamed na Ally Musa.

Wabunge wapinga majukumu ya ‘Nasaco’ mpya

By Sharon Sauwa, Mwananchi ssauwa@mwananchi.co.tz
Dodoma. Wabunge wamepinga Shirika la Taifa la Wakala wa Meli (Nasac) kupewa majukumu ya kufanya biashara na udhibiti kwa sababu yanasababisha mgongano wa maslahi kwa yenyewe kuwa mdhibiti na wakati huo huo kufanya kazi ya uwakala wa meli.
Kuundwa kwa shirika hilo jipya kunakuja baada Serikali kubinafsisha Kampuni ya Wakala wa Meli (Nasaco) mwaka1998 ambayo ilidumu kwa miaka 25.
Kauli hiyo imekuja mara baada ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliani Profesa Makame Mbarawa kuwasilisha bungeni Muswada wa Sheria ya Wakala wa Meli wa Taifa ya Mwaka 2017 ambayo inaunda shirika hilo na kuainisha majukumu yake.
Akiwasilisha maoni ya Kamati ya Miundombinu leo Alhamisi, makamu mwenyekiti wa kamati hiyo, Moshi Kakoso amesema kamati imebaini kuwa Nasac inayopendekezwa itakuwa na jukumu la udhibiti na kufanya kazi za uwakala.
“Kamati inashauri kuwa ni vyema Serikali ikatenganisha masuala ya udhibiti na ufanyaji wa biashara ili kuweza kuondoa mgongano wa kimaslahi kwa mdhibiti kufanya kazi uwakala,” amesema.
Kakoso amesema pia sheria iliyokuwepo awali ilikuwa inaruhusu wakala wa meli kuwa pia wakala wa mizigo.
Hata hivyo, amesema sheria inayopendekezwa kifungu cha 38(2) (a) kinachohusu utoaji leseni kwa mawakala wa meli hakiruhusu mwenye meli kupewa leseni ya uondoshaji wa shehena.
“Kamati inaona kuwa hakuna sababu za msingi za kuzuia hii kwani ni ngumu sana katika dunia ya sasa kuepuka muungiliano huo. Jambo la msingi ni kuwa ni kuwa na udhibiti na ufuatiliaji wa karibu ili kuepuka ubadhilifu ambapo awali ulikuwa unajitokeza,” amesema.
Vifungu hivyo pia vilipingwa na Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni ambapo wamesema muswada huo unalipa shirika hilo mamlaka makubwa ya kuweza kuiua sekta ya usafirishaji wa majini kwa kuwa mdhibiti lakini wakati huo huo mtoa huduma za uwakala.
Msemaji wa kambi hiyo, Suzan Lyimo amesema kuna hoja ambazo zinaletwa kwa nguvu zote ili kupitisha muswada hatari ikiwa sababu za udanganyifu wa shehena iliyomo katika meli kuwa sio inayotakiwa kulipiwa ushuru.

Kampeni zamuibua meya mstaafu, apigia debe CCM

Meya mstaafu wa halmashauri ya manispaa ya
Meya mstaafu wa halmashauri ya manispaa ya Iringa, Amani Mwamwindi 
Iringa. Meya mstaafu wa halmashauri ya manispaa ya Iringa, Amani Mwamwindi amewaomba wakazi wa Kitwiru kumchagua Baraka Kimata kuwa diwani ili kuwaongezea nguvu ya kupinga kupitishwa mambo yasiyofaa ndani ya baraza la madiwani.
Halmashauri ya Manispaa ya Iringa inaongozwa na meya Alex Kimbe kutoka Chadema, huku CCM ikiwa na madiwani wanne kati ya 18 wa kuchaguliwa.
Akihutubia mkutano wa kumnadi mgombea wa CCM, Baraka Kimata, Mwamwindi alisema uongozi wa halmashauri hiyo umeshindwa kufanya kazi za kuwaletea maendeleo wananchi, badala yake umekuwa ukiendesha siasa za chuki na ubaguzi.
“Hali ilivyo ninyi wenyewe ni mashahidi, hakuna miradi ya maana ya maendeleo iliyoanzishwa na uongozi wa sasa, miradi yote ya barabara hata ujenzi wa stendi mpya ya mabasi ni ile tuliyoipanga sisi,” alisema Mwamwindi.
Naye diwani wa Mshindo, Ibrahim Ngwada alisema CCM inahitaji kuongeza nguvu ya diwani huyo ili washiriki kupambana na vitendo vinavyofanywa kwenye baraza la madiwani ambavyo havina masilahi kwa umma.
Alisema tangu baraza hilo lianze kazi limepitisha mambo kadhaa ambayo hayana masilahi kwa umma, badala yake ni kuleta hasara.
Kimata, ambaye alikuwa diwani wa kata hiyo kupitia Chadema aliyejiuzulu miezi miwili iliyopita, aliwataka wakazi wa kata hiyo kumchagua ili aweze kuwaletea maendeleo.

Mjadala wenye thamani bungeni wafunikwa na sinema ya Dk Shika


Hoja nzuri na zenye thamani kubwa zilichomoza bungeni wakati wa mjadala wa Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa mwaka 2017/18. Baadhi ya wabunge walisimama na kulinda thamani na heshima ya Bunge kama yalivyo matakwa ya Katiba.
Mambo muhimu yaliyochanua ni kupaa kwa Deni la Taifa, Mpango wa Maendeleo kutoakisi hali halisi ya nchi, wakulima kusahaulika, Serikali kujielekeza kwenye kukusanya kodi na kubana badala ya kutanua uzalishaji.
Jambo jingine ambalo lilijadiliwa ni madai ya upindishwaji wa takwimu za Serikali, kukiwa na mkanganyiko kutoka mwaka mmoja hadi mwingine, vilevile tarakimu kupishana.
Ni hoja ambazo zinapaswa kumpa sura mbili kila Mtanzania. Ya kwanza ni ndita; kwamba Serikali haitumii sayansi katika utawala ndiyo maana Wizara ya Fedha imewasilisha bungeni Mpango wenye kasoro nyingi. Ya pili ni tabasamu; kwamba wabunge wanatimiza wajibu wao wa kuisimamia Serikali.
Wakati wabunge wakipaza sauti kueleza athari na maumivu ya kiuchumi kwa nchi kupitia kasoro ndani ya Mpango mpya na kutotekelezwa ipasavyo kwa mipango iliyopita, nchi kwa sehemu kubwa ya watumia mitandao ya kijamii, ilijielekeza kujadili tukio la mnadani.
Alhamisi ya Novemba 9, kampuni ya udalali ya Yono ilifanya mnada wa nyumba tatu za mfanyabiashara Said Lugumi anayedaiwa malimbikizo ya kodi na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA). Nyumba hizo, mbili zipo Mbweni, Kinondoni na Upanga, Dar es Salaam.
Katika mnada huo, alijitokeza mtu aliyejitambulisha kwa majina ya Dk Louis Shika ambaye alishinda mnada wa kununua nyumba zote tatu kwa Sh3.2 bilioni. Moja Sh900 milioni, nyingine Sh1.1 bilioni na ya tatu Sh1.2 bilioni. Baada ya kushinda akapepewa na kushangiliwa.
Taarifa za ushindi wa Dk Shika zilipovuja tu, picha yake ilianza kusambaa kwenye mitandao ya kijamii, huku sifa kuu akipambwa kuwa si mtu mwenye wajihi wa kuogopesha au wa kitajiri, bali mwonekano wake ni wa kawaida tu, lakini amethibitisha ni bilionea kwa kununua majumba ya Lugumi.
Sheria ya minada nchini inaelekeza kwamba ukishinda kununua mali husika, unapaswa kulipa papohapo asilimia 25 ya bei uliyoshinda kununua, asilimia 75 inayosalia hulipwa ndani ya siku 14. Hivyo, kwa nyumba tatu ambazo Dk Shika alishinda kuzinunua kwa Sh3.2 bilioni, alipaswa kulipa mara moja Sh800 milioni ambazo ndiyo asilimia 25.
Zikafuatia taarifa kuwa Dk Shika hakuwa na Sh800 milioni za kulipa siku hiyo. Ikabainishwa kuwa mtu huyo ama alijituma au alitumwa kukwamisha mnada. Taarifa za polisi zilikwenda mbali zaidi na kueleza kuwa Dk Shika ni tapeli. Hizo ni tuhuma na sheria bila shaka itachukia mkondo wake.
Hoja ni kuona kuwa sinema ya mnadani, iliyochezwa na Dk Shika, ilipata mapokeo makubwa na kujadiliwa na watu wengi kwenye mitandao ya kijamii na vyombo vya habari kwa jumla, kuliko kilichojiri bungeni kulikokuwa na mjadala wenye hadhi kubwa kwa Taifa.
Kilichokuwapo bungeni
Siku Dk Shika alipocheza sinema yake mnadani, ndiyo ambayo Mbunge wa Kigoma Kaskazini (CCM), Peter Serukamba alibainisha mkanganyiko wa takwimu za Deni la Taifa. Mpango wa mwaka 2016-2017, ulieleza kuwa mpaka Oktoba 2015, deni lilikuwa dola 19 bilioni (Sh42.8 trilioni), ikiwa limeongezeka kutoka dola 18 bilioni (Sh40.5 trilioni) mwaka 2014.
Serukamba alibainisha kuwa taarifa ya Mpango uliopita, kulikuwa na maelezo kuwa Deni la Taifa lilifikia dola 18 bilioni (Sh40.5 trilioni), ikiwa ni ongezeko la asilimia 9.76 kutoka Oktoba 2015 ambako deni lilikuwa dola 16 bilioni (Sh.36 trilioni). Hapo kwa hakika kuna mkanganyiko wa haja.
Serukamba alibainisha pia kuwa Mpango mpya unasema Deni la Taifa limefikia dola 26 bilioni (Sh58.6 trilioni) hadi Juni mwaka huu, kutoka dola 22 bilioni (Sh49.6 trilioni) Juni 2016. Taarifa iliyopita inasema Oktoba 2016 deni lilikuwa Sh40.5 trilioni, mpya inaeleza Juni 2016 deni lilisoma Sh49.6 trilioni.
Mshangao ni kwamba taarifa zote zinaandikwa na Wizara ya Fedha. Hapo ndipo shaka inakuwepo kuhusu utendaji wa watu ambao wamekabidhiwa majukumu ya kiutendaji kuhusu nchi. Je, ni umakini mdogo? Kufanya bora liende au makusudi kupindisha takwimu?
Mchango wa Serukamba uligusa pia namna Mpango wa Maendeleo ulivyoiacha sekta binafsi na kilimo. Alieleza jinsi ambavyo Serikali inanadi nchi ya Viwanda wakati kwenye Mpango hakuna tamko la kuongeza tija kwenye kilimo, zaidi inazungumzwa kubana na kukusanya kodi bila kuweka mipango ya uzalishaji.
Alitoa mfano kwamba Bangladesh kiwanda kimoja kinatumia pamba robota 5,000,000, wakati Tanzania inahubiriwa kubadilika kuwa nchi ya viwanda kwa kutegemea mavuno ya pamba robota 240,000. Ni hapo Serukamba aliuliza: “Tunamdanganya nani hapa?”
Bashe na Nape
Mbunge wa Mtama (CCM), Nape Nnauye alizungumzia kasoro ya Serikali kutoishirikisha sekta binafsi katika miradi inayoweza kujiendesha kibiashara, badala ya kuendelea kukopa, kitu ambacho alionya kwamba kitakuja kusababisha athari kubwa kwa nchi.
Jambo la kwanza Nape alisema kuwa Serikali inakopa fedha nyingi kwa ajili ya miradi mikubwa ambayo ukamilikaji wake unachukua muda mrefu, wakati mikopo husika marejesho yake yanafanyika ndani ya muda mfupi. Kutokana na hali hiyo, alitahadharisha kwamba marejesho yataathiri miradi mingine.
Nape alisema kwa vile miradi itachelewa kukamilika, wakati wa marejesho ya mikopo, itabidi kuchukua fedha kwenye miradi ya huduma kama elimu, afya na kadhalika ili kuwalipa wadeni wa nchi. Katika hili Nape alisema anatilia shaka uzalendo wa wachumi ambao wanamshauri Rais.
Upande wa pili, Nape alionya kuwa nchi inapiga hatua kwenda kuwa isiyokopesheka ikiwa itakopa kwa ajili ya miradi miwili tu; wa kwanza ni ujenzi wa reli ya kisasa na wa ufuaji umeme wa Stiegler’s Gorge megawati 2,100.
Nape alisema taarifa za Mpango mpya zinaeleza Deni la Taifa limefikia dola 26 bilioni (Sh58.6 bilioni) sawa na asilimia 32 ya uhimilivu wa deni. Kwamba ili Tanzania ifikie kikomo cha kukopeshwa, deni lake linapaswa kufikia dola 45 bilioni (Sh101.4 trilioni).
Kutokana na hoja hiyo ya Nape, anasema endapo Serikali itaongeza mkopo kwa miradi miwili tu ya standard gauge na Stiegler’s Gorge, itafika kwenye kiwango chake cha mwisho cha kukopa.
Hoja ya Bashe iligusa kuporomoka kwa wastani wa ukuaji wa Pato la Ndani la Taifa (GDP) na Benki Kuu kutoripoti kiwango cha uingizaji na usafirishwaji wa bidhaa nje ya nchi, tangu Juni mwaka huu ikiwa ni mara ya kwanza katika historia ya nchi.
Bashe pia alizungumzia Mpango wa Maendeleo kukosa mkazo kwenye sekta ya kilimo kuwa Serikali inadhibiti mfumuko wa bei kwa kumkandamiza mkulima, vilevile alikosoa mipango ya viwanda kwamba haiendani na hali halisi.
Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe, alitaka wabunge wa CCM kuwa imara zaidi kwa kile alichoeleza kwamba nchi inakwenda vibaya na wao ndiyo wenye dhamana kubwa kama chama tawala.
Aliwapongeza Serukamba na Bashe kwa kuamua kuwa wakweli na kuzungumza hali halisi kuhusu mwenendo wa uchumi kwa nchi.
Ndugai aliwasema wabunge wa CCM kuwa hawatakiwi kuunga mkono tu kwa sababu CCM ndiyo kabisa haitaki mipango mibaya. Kimsingi Ndugai alichokimaanisha ni Bunge analoliongoza kuwa la hoja zenye mantiki kwa faida ya nchi na siyo kuwachekea mawaziri ikiwa wanapeleka bungeni hoja zenye kasoro nyingi.
Alichokizungumza Ndugai kuwaamsha wabunge kujadili Mpango wa Maendeleo kwa uwazi na bila woga, alikopita Serukamba na hoja zilizojengwa na Nape, Bashe na Mbowe, kwa pamoja ndiyo tafsiri ya Bunge la kisasa. Bunge lenye kuyatangulia maisha ya watu.
Kimsingi hoja za vikao vya Bunge kuanzia Alhamisi iliyopita mpaka Ijumaa, ndizo ambazo zilipaswa kung’ara na kutembea zaidi kwenye mitandao ya kijamii na kwenye vyombo vya habari kwa jumla. Kinyume chake Dk Shika na sinema yake ya mnadani akafunika mjadala bora mno kwa maslahi ya Watanzania.   

Msekwa asema kilichotokea kwa Mugabe ni kipya

Makamu mwenyekiti wa CCM mstaafu, Pius Msekwa.
Makamu mwenyekiti wa CCM mstaafu, Pius Msekwa. Picha na Maktaba 
Dar es Salaam. Sintofahamu iliyotokea Zimbabwe baada ya jeshi la nchi hiyo kutanda jijini Harare na kumuweka chini ya uangalizi Rais Robert Mugabe imeelezwa ni jambo jipya ambalo halijawahi kutokea.
Baada ya taarifa kusambaa kuwa jeshi linaidhibiti nchi hiyo baadhi ya wachambuzi wa masuala ya kisiasa hapa nchini mbali ya kueleza kuwa ni jipya, pia wameeleza kuwa ung’ang’anizi wa madaraka ni tatizo.
Akizungumza na Mwananchi jana kuhusu kilichotokea Zimbabwe, makamu mwenyekiti mstaafu wa CCM, Pius Msekwa alisema ni jambo jipya kuwahi kutokea katika kipindi hiki ambacho nchi nyingi za Afrika zinafuata mfumo wa demokrasia wa kuchagua viongozi kupitia vyama.
Msekwa, ambaye pia aliwahi kuwa Spika wa Bunge alisema anasita kuita mapinduzi kutokana na kilichotokea Zimbabwe kwa kuwa mapinduzi ya kijeshi huhusisha kuitoa Serikali iliyopo madarakani kisha jeshi kushika hatamu, jambo ambalo kwa nchi hiyo wanajeshi wametangaza kuwa hawako tayari kukamata madaraka.
“Katika kumbukumbu zangu sikumbuki kama hili jambo limewahi kutokea tangu miaka ya 60, kuna tofauti kubwa sana kuita haya ni mapinduzi ya kijeshi. Ni mapinduzi kwa sababu Serikali iliyokuwepo imetolewa lakini jeshi limesema halina nia ya kuchukua madaraka, ni jambo jipya sana kwangu ndiyo maana nasita kuita ni mapinduzi ya kijeshi,” alisema.
Hata hivyo, kada huyo wa chama tawala alisema kila jambo lina mwanzo wake pengine na hilo limekuja kwa makusudi ili watu wajifunze.
Msekwa alilipongeza jeshi hilo kwa kuhakikisha wanafanya mambo hayo kwa amani bila kumwaga damu.
Makamu mkuu wa Chuo Kikuu cha Ruaha (Rucu), Profesa Gaudence Mpangala alisema jambo lililofanyika nchini humo ni matokeo ya ung’ang’anizi wa madaraka, ingawa nyuma Mugabe alisukumwa na chama kilichokuwa kikitaka kiendeee kutawala milele. “Sasa tupo katika utawala wa kijamhuri unaotaka kuwe na uchaguzi huru, ukimuangalia Mugabe alishafika umri wa zaidi ya miaka 90 na bado alikuwa anang’ang’ania madaraka ndiyo maana amepata aibu,” alisema.
Profesa Mpangala alisema Mugabe angejiwekea heshima kubwa kama angekubali kung’atuka mapema na kuandaa vijana ambao wangemrithi na siyo mpaka kusubiri jeshi ‘limpindue’.
Alisema tukio hilo ni funzo kubwa kwa nchi mbalimbali kwa kuwa si kiongozi pekee anayeng’ang’ania madaraka anachokwa, lakini pia chama kiking’ang’ania nacho kinajiweka katika wakati mgumu.
“Ni lazima kuwe na mfumo wa kubadilishana madaraka, hiyo ndiyo demokrasia unayotaka na ni lazima Serikali iweke mazingira ya ushindani sawa kwa vyama vyote vya upinzani,” alisisitiza Profesa Mpangala.
Akizungumzia suala hilo, mratibu wa Mtandao wa Wapigania Haki za Binadamu, Onesmo Ole Ngurumwa alisema Rais Mugabe amejitengenezea mwenyewe mazingira hayo.
“Kilichotokea ni matokeo ya kutoheshimu demokrasia, alikuwa na muda wa kutoka kwa heshima na kuandaa watakaomrithi lakini ameshindwa hilo na matokeo yake akafanya chama ni mali ya familia,” alisema.
Ole Ngurumwa alipongeza hatua hiyo na kusema kuwa ilifika wakati wake na kuwa wananchi walishachoshwa na kiongozi huyo ambaye alianza kuongoza mara tu baada ya uhuru wa nchi hiyo kupatikana kutoka kwa wakoloni wa Uingereza.
Hata hivyo, Ole Ngurumwa alilipongeza jeshi hilo kwa kitendo chake cha kutomwaga damu na kusababisha maafa kwa wananchi.
“Wakati mwingine tunashuhudia damu ikimwagika bila sababu za msingi, tunashukuru jeshi la Zimbabwe limefuata njia bora ya demokrasia ambayo haimwagi damu na kuheshimu watu,” alisisitiza Ole Ngurumwa.

Mbunge asema majibu ya Serikali ni yale yale kila mwaka



Mbunge wa Songwe(CCM),  Philipo Mulugo
Mbunge wa Songwe(CCM),  Philipo Mulugo 
Dodoma. Mbunge wa Songwe(CCM),  Philipo Mulugo amekerwa na majibu ya Serikali na kusema yamekuwa ni yaleyale kila mwaka.
Mulugo alisimama na kuliambia Bunge kuwa hana mpango tena hata wa kuuliza swali la nyongeza kutokana na ukweli kuwa majibu ya Serikali kuhusu uvunaji wa mamba katika ziwa Rukwa yamekuwa hayaridhishi.
"Majibu ya Serikali ni yale yale kila mwaka na hata mwaka jana nilijibiwa hivyo kwa  hivyo bora kunyamaza tu," amesema Mulugo
Mwanzoni mwa mwaka jana mbunge huyo aliuliza swali kama hilo na katika swali la nyongeza aliangua kilio kwa kumbukizi kuwa mama yake mzazi aliuawa na mamba.
Akijibu swali la msingi Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga amesema uwindaji wa mamba hufanyika kwa kuzingatia takwimu kuhusu idadi ya mamba.
Hasunga amesema wizara imekuwa ikifanya utafiti wa wanyamapori na sensa hiyo inalenga kubaini idadi ambayo inawezesha upangaji wa kuvuna wanyama hao.

Viboko 12 vyamsubiri ‘bilionea’ nyumba za Lugumi

Dk Louis Shika akiwasili nyumbani kwake Tabata
Dk Louis Shika akiwasili nyumbani kwake Tabata Mawenzi jijini Dar es Salaam juzi baada ya polisi kumuachia kwa dhamana. Picha na Ericky Boniphace 
Busega. Siku moja baada ya Jeshi la Polisi kumwachia kwa dhamana, Dk Loius Shika ambaye alikuwa ameshikiliwa kwa siku sita kwa madai ya kuharibu mnada wa nyumba za Said Lugumi, familia ya daktari huyo imesema lazima achapwe viboko 12 kama anataka kusamehewa.
Akizungumza na Mwananchi nyumbani kwake katika kitongoji cha Misheni katika Kijiji cha Chamugasa juzi, kaka mkubwa wa Dk Shika, Pelanya Lunyalula alieleza kuwa mila na tamaduni za kabila la Wasukuma hazitoi msahama hivihivi hadi pale kikao cha baraza la ndugu kitakapoketi na kumpa adhabu ya viboko.
“Mpaga ibanza lya badugu (hadi kwenye kikao cha baraza la ndugu wa ukoo) wakiketi kumjadili na yeye akiwepo ndipo uamuzi hufanyika wa kumuonya kwa tabia za kudharau ukoo na huchapwa viboko zaidi ya 12 na kutakiwa kujirekebisha vingine atafutwa kabisa,” alisema.
Lunyalula alisema uamuzi huo hufanywa endapo mtu kama huyo ameamua kutengana na ndugu zake kama anavyodaiwa kufanya Dk Shika kwa madai misiba mingi imetokea na yeye kupatiwa taarifa lakini hakufika kuhani.
“Hii ni dhahiri kwamba ameona ndugu zake hawaendani na elimu yake kitendo ambacho kila mmoja alishakichukia, hivyo hata hilo suala lililomkuta huenda ni malipo ya matendo yake aliyoyafanya,” alisema Pelanya mwenye umri wa miaka 84.
Kauli hiyo iliungwa mkono na mpwa wa Dk Shika ambaye pia ni mwenyekiti wa Kitongoji cha Misheni, Emmanuel Komanya ambaye alitumia nafasi hiyo kuwaonya watu wengine wasiige tabia kama hiyo.
Ndugu hao ambao kwa pamoja walionekana kuwa na huzuni wakati wakizungumza na Mwananchi baada ya kupata taarifa za kushikiliwa kwake, walisema hawataweza kwenda kuonana naye.
“Kwanza familia yetu ni masikini hatuna uwezo wa kutafuta fedha za kwenda huko, lakini pia hata kama tungekuwa na uwezo tusingeweza kwenda (Dar es Salaam),” alisema.
Hata hivyo, Dk Shika mwenyewe alipozungumzia kuhusu familia yake hiyo alisema hawasiliani nayo kwa kuwa huenda wenzake hawana simu na hadhani kama atakwenda huko kwa kuwa wazazi wake wote wameshakufa hivyo hata akienda haitasaidia.
Juzi Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam lilifikia uamuzi wa kumwachia baada ya kutimiza masharti ya dhamana ya kujidhamini mwenyewe kutokana na kukosa mtu wa kumwekea dhamana.
Kamanda wa kanda hiyo, Lazaro Mambosasa alisema, “uchunguzi wa tuhuma dhidi yake unaendelea lakini mpaka sasa hakuna mtu yeyote aliyefika kutaka kumwekea dhamana, yaani anaishi kama mtu wa nyikani.”

Ajali ya boti yahofiwa kuua wawili


Kagera. Watu wawili wanasadikika kufa maji baada ya boti ya mizigo ya Mv Julias kuzama majini wakitoka kisiwa cha Goziba katika ziwa Viktoria mkoani Kagera kuelekea jijini Mwanza.
Diwani wa Kata ya Goziba, Masaba Nkunami amesema boti hiyo imezama usiku wa kuamkia leo Alhamisi muda mfupi baada ya kuanza safari zake kutoka kisiwani hapo.
Licha ya kutotaja idadi kamili ya watu waliokuwamo kwenye boti hiyo ya mizigo, Nkunami amesema kwa sasa wanaendelea na jitihada za kuwatafuta watu wawili wanaosadikika kuzama ziwani.
Amesema boti hiyo iliundwa kwa vyuma mfano wa meli ambayo hufanya shughuli za kusafirisha mizigo kati ya kisiwa cha Goziba na Mwanza.
“Jitihada za kutafuta watu hao zinaendelea hadi sasa watu wapo majini wakiwatafuta, hivyo taarifa zaidi zitatolewa baadaye,” amesema Nkunami.
Kwa upande wake Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kagera, Augustine Ollomi amekiri kuzama kwa boti hiyo lakini akasema “mpaka sasa hakuna taarifa za vifo.”

Spika awataka mawaziri kusikiliza maswali ya wabunge



Spika wa Bunge, Job Ndugai
Spika wa Bunge, Job Ndugai 
Dar es Salaam. Spika wa Bunge, Job Ndugai amewataka mawaziri waache kupiga stori bungeni na kusikiliza wabunge wanapouliza maswali.
Ndugai ametoa agizo hilo leo Alhamisi asubuhi wakati wa kipindi cha maswali na majibu bungeni.
“Kipindi cha maswali waheshimiwa mawaziri acheni kupiga stori… waheshimiwa mawaziri hamsikilizi,’’ amesema Ndugai
Kauli ya Ndugai imekuja baada ya Mbunge wa Viti Maalum, Mwantumu Dau Haji kuuliza swali la nyongeza kuhusu kilimo cha umwagiliaji alilolielekeza kwenye Ofisi ya Makamu wa Rais – Muungano na Mazingira.
Wakati akiruhusu naibu waziri kujibu swali hilo, Spika amesema kuwa swali hilo lilipaswa kujibiwa na wizara ya maji hivyo kumtaka naibu waziri wa wizara hiyo kujibu.
“Hilo swali lilitakiwa liende Wizara ya Maji, Naibu Waziri Maji, Mh Aweso (Jumaa),” Ndugai alimtaka Naibu Waziri wa Maji kujibu swali na kuongeza kuwa, “ndo shida mnakuwa mnaongea, hamsikilizi humu ndani, jibu swali.”
Baada ya hapo, Spika alimwambia Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais – Mazingira na Muungano, Kangi Lugola kujibu swali hilo. “Mh Kangi Lugola okoa jahazi’ alisema Ndugai ambaye alikuwa akiwasisitiza mawaziri kuwa makini kusikiliza. 
Pia, Spika amewataka baadhi ya mawaziri kujiandaa kutoa majibu mafupi katika maswali yanayohusu wizara zao, “Wizara ya Maliasili na Utalii, Wizara ya Afya, Wizara ya Maji kwa majibu yanayokuja na Ofisi ya Makamu wa Rais kwa majibu yanayokuja, ni marefu sana mawaziri wawe wanatoa majibu kwa ufupi,” amesema

Mwanafunzi aliyepelekwa ‘mochwari’ akidhaniwa kufa amaliza kidato cha nne


Tayari mwaka mmoja umepita tangu Isack Ernest (17), mwanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Lumo jijini Dar es Salaam alipopigwa na wananchi wenye hasira kali, kuzimia na kudhaniwa amefariki dunia akituhumiwa kuiba kupitia kundi la uhalifu la ‘Panya Road’ waliokuwa wanajiita ‘Taifa Jipya.’
Japo Oktoba 15 mwaka jana ilikuwa siku ya maumivu makali kwake na kunusurika kifo, tarehe hiyo hiyo mwaka huu ameungana na wanafunzi wenzake wa kidato cha nne, kusherehekea kumaliza masomo ya kidato cha nne
“Panya road azinduka akiwa mortuary”, ni kati ya vichwa vilivyobeba habari mbalimbali zilizomuhusu mwanafunzi huyo katika tukio lililotokea Mbagala, jijini Dar es Salaam ambako zaidi ya vijana 10 walitiwa mbaroni siku hiyo.
Isack anasema kupona kwake na kumaliza mitihani ya kidato cha nne ni kwa neema ya Mungu tu na si vinginevyo.
“Siamini kama leo hii namaliza shule, nilikata tamaa, kiukweli bila polisi kufika eneo la tukio siku ile na kuniokoa ningekufa,” anasema.
Ni kumbukumbu mbaya isiyofutika kichwani kwa Isack, hata hivyo ilishatokea.
“Kuna wakati nikikumbuka nashtuka, nimeathirika kisaikolojia, sipo sawa na zamani hata uwezo wangu darasani umepungua. Ninachoshukuru ni mzima tu,” anasema Isack.
Jana Jumatano, Isack alimalizia elimu yake ya sekondari kwa kufanya mtihani wa baolojia kwa vitendo.
Siku ya tukio
Aliyekuwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Temeke, Gilles Muroto wakati huo alisema baada ya polisi kupigiwa simu na raia wema kuwa kuna vijana watatu wamefariki dunia, walikwenda eneo la tukio na kuwakuta wakiwa na hali mbaya.
Alisema mmoja wao anayeitwa Kelvin Nyambocha (14) alifariki dunia baada ya kupigwa na kuchomwa moto na wananchi baada ya kuwapora huku wakiwa na silaha za jadi.
Alieleza kuwa Isack alipigwa kiasi ambacho walijua amefariki dunia na ndipo alipopelekwa chumba cha kuhifadhia maiti na kufanyiwa taratibu zote, ikiwa ni pamoja na kuvuliwa nguo na kuwekewa namba tayari kwa kuingizwa kwenye jokofu.
“Wakati amewekwa chini kwa ajili ya kuingizwa kwenye jokofu, alizinduka kwa kupumua na kuonekana bado yupo hai, hali iliyosababisha kupelekwa Chumba cha Uangalizi Maalumu (ICU),” alisema Muroto.
Simulizi ya Isack
Mwenyewe anasimulia kuwa siku ya tukio akiwa na wenzake waliamua kwenda kwenye tamasha la kuinua vipaji lililofanyika Zakhem, Mbagala jijini Dar es Salaam.
Hata hivyo, baba yake anasema siku hiyo mwanaye alimuaga kwamba anaenda kuangalia mpira hivyo, hakuwa na wasiwasi.
Walifika salama kwenye tamasha hilo lakini lilipoisha wakiwa njiani kurejea nyumbani ndipo, purukushani ilipoanza.
Isack anasema kati yao wengine walikuwa na miaka kati ya 13 hadi 16.
“Mimi nilikuwa nyuma, ndio nikasikia kelele za wezi kumbe wale walio mbele walianza kuwapora watu vitu,” anasema.
Anasema ghafla alishangaa mwenzake mmoja amekamatwa na kuwekwa kwenye tairi kisha kuwashwa moto.
“Ilibidi nikimbie kujiokoa. Huku nikikimbizwa kwa kuitwa mwizi, nilifanikiwa kufika eneo la Sabasaba nikitokea Zakhem Mbagala,” anasimulia.
Anasema watu waliokuwa mbele yake walifanikiwa kumkamata na kuanza kumpiga kwa nguvu huku wengine wakitaka achomwe moto mara moja.
Isack anasema huku akipigwa, alisikia wananchi hao wakibishana kwani walikuwepo waliotaka achomwe moto hapohapo na wengine, wakitaka apelekwe walikokuwa wakipigwa wengine.
“Walianza kubishana, wengine wanasema nichomwe moto hapo hapo, wengine wanataka nirudishwe waliokokuwa wenzangu…kwa kweli maisha yangu yakawa mikononi mwa Mungu, nilijitahidi kujitetea bila msaada,” anasema mwanafunzi huyo.
Mwanafunzi huyo anasema wakati akiendelea kupigwa, ghafla walitokezea polisi ambao waliwatawanya watu na wakati huo bado alisikia kila kinachoendelea.
“Ghafla nilisikia kishindo kikubwa na kuanzia hapo nilikuja kujiona hospitali ya Temeke. Tangu hapo sijui kilichoendelea ndio nasikia nilipelekwa chumba cha kuhifadhia maiti,” anasema.
Baba mzazi wa Isack, Ernest Chalo anasema anakumbuka siku hiyo alikuwa anafuatilia mchezo wa Ligi Kuu Bara kati ya Simba na Kagera Sugar, alipopigiwa simu na mtu asiyemfahamu akimpa taarifa kuwa mtoto wake amefariki dunia, hivyo anatakiwa kwenda chumba cha kuhifadhia maiti, ili amtambue mwanaye.
“Nilichanganyikiwa, sikujielewa yaani ilibidi nitoke mbio hadi Temeke, moja kwa moja nilielekea kwenye chumba cha kuhifadhia maiti nikaonyeshwa miili ya vijana waliokuwa wameuawa. Kwa sababu waliumizwa sana usoni sikuwatambua,”anasema.
Aliamua kuwakagua tumboni akiamini kwamba angemtambua mwanaye kwa upekee wa kitovu lakini hakufanikiwa, ndipo akatokea msamaria mwema akamwambia mtoto wake alizinduka.
“Kutokana na baridi kali ya chumba cha kuhifadhia maiti, mtoto wangu alipoingizwa mle ndani alipumua na hivyo akatolewa. Niliambiwa alivishwa nguo za mwenzake kwa sababu zake zilivuliwa,” amesema.
Anasema huenda kabla mwanaye hajapoteza fahamu aliitaja namba yake ya simu hivyo ikasaidia yeye apate taarifa.
Anasema alifanikiwa kumuona mwanaye akiwa hai japo alikuwa akivuja damu kwa kipigo huku hali yake ikiwa mbaya.
Taarifa zafika shuleni
Taarifa za kifo cha Isack ziliwafikia walimu wake shuleni.
Makamu mkuu wa shule hiyo Amosi Tinde anasema taarifa hizo ziliwashtua na kuwashangaza kwa sababu siku za masomo, Isack alihudhuria vipindi vyote na hatukuwahi hata kuhisi kwamba ni ‘panya road’.
“Tulishangaa kuambiwa Isack ameuawa akiwa miongoni mwa vijana ‘panya road’ na tukapigiwa simu mwili wake upo chumba cha kuhifadhia maiti, kiukweli hakuwa mwanafunzi mtoro na ni kijana mwenye nidhamu tu, hizi habari zilitushtua sana.” anasema.
Mwalimu huyo anasema baada ya kupokea ujumbe huo, iliwalazimu waanze kuandaa taarifa za mwanafunzi huyo shuleni.
Hata hivyo, baadaye tena wakaambiwa hajafariki dunia, isipokuwa alizimia tu.
Isack anasema hofu yake kubwa ilikuwa ni kupoteza masomo yake kutokana na kuhusishwa na ‘panya road.’
Lakini walimu wanasema, waliamua kumsaidia ili awe mwanafunzi mzuri na hatimaye kumaliza mitihani yake ya kidato cha nne,
“Uzuri wake leo hii anamaliza kidato cha nne, tunamuombea Mungu afaulu na ikitokea vinginevyo, anaweza kusoma hata ufundi,” anasema Tende.
Mwalimu Tinde anasema hatua ya kumaliza mitihani yake ni ujasiri mkubwa kwani, mwanafunzi mwingine angeweza kuacha shule kwa woga au aibu.
Maisha yake baada ya tukio
Awali haikuwa rahisi kwa Isack kurejea shuleni na kuendelea na masomo.
Baba yake anasema baada ya matibabu na kesi kuisha, ilimlazimu ampeleke Tanga kwa ndugu zake ili akakae kidogo kurejesha fahamu zake vizuri kabla ya kuendelea na masomo.
Walimu wake pia waliamini kwamba hataweza tena kuendelea na masomo.
Mwalimu Tende anasema ilibidi walimshauri baba yake walau amuhamishie shule nyingine kwa sababu waliamini atakuwa ameathirika kisaikolojia.
“Lakini baadaye tukaona amerudi na anaweza kumudu masomo hivyo kazi kubwa ikawa kumsaidia kisaikolojia,”anasema.
Mwalimu wake wa darasa, Janeth Swai anasema moja ya jukumu kubwa lililokuwa mbele yake mwaka huu ni kumsaidia mwanafunzi huyo, sio tu kwamba aachane na tabia zilizomsababishia matatizo ya kupigwa, bali kuwekeza nguvu kwenye masomo yake.
“Nilikuwa naongea naye kila mara, nikamfanya rafiki yangu na akaanza kunisimulia vitu vingi. Kwa hiyo niliweza kumsaidia sana,” anasema.
Mwalimu Swai anasema Isack alikuwa mtulivu zaidi na akaanza kuwakwepa rafiki zake hasa wa mitaani.
Mwalimu mwingine, Joyce Madenge anasema isingekuwa makundi mabaya ya rafiki zake, mwanafunzi huyo asingekutwa na janga lililomkuta.
Anasema bado kuna kazi kubwa ya kumsaidia Isack kisaikolojia na kuhakikisha hajiungi tena na makundi ya aina hiyo baada ya kumaliza masomo yake.
Baba yake anasema ameshamuandalia sehemu ya kujifunza ufundi wa magari baada tu ya kumaliza kidato cha nne wakati akisubiri majibu.
Kuhusu kujihusisha na ‘panya road’
Anasema siku ya tukio hakuwa anajua kama wenzake hao wangefanya uhalifu huo na kwamba, alishtukia tu wameanza kupora kisha kuanza kupigwa.
“Kwa hiyo nilishtuka tu wenzangu mbele yangu wanaanza kupora mara kelele za wezi. Ndio tukaanza kukimbizwa na kupigwa,” anasema.
Hata hivyo anasema baada ya kupata ahueni, aliwapeleka polisi kwa mwenzake mmoja ambaye nyumbani kwao alikutwa na bendera ya kundi la ‘panya road’ wanaojiita ‘Taifa Jipya’ iliyochorwa picha za maghorofa, silaha za jadi na askari akikimbizwa.
“Ninachoshukuru nimekuwa kijana mzuri, sina tena marafiki na ninamaliza shule. Kweli sikuwa mwizi,”anasema.
Majuto ni mjukuu
Isack anatamani tukio hilo lisingetokea lakini limeshatokea.
“Naumia nikikumbuka na niwaombe vijana wenzangu waache tabia hizi mbaya zinawaumiza sana wazazi. Baba yangu aliumia na akaingia gharama kubwa kunitunza,”anasema.
Isack anatamani kuwa mwalimu wa sekondari.
“Napenda kuwa mwalimu mzuri kama Swai, napenda nije niwasaidie wenzangu hata hivyo masomo ninayoyapenda ya Kiswahili, Kingereza na History yananisukuma kuwa mwalimu zaidi kuliko kazi nyingine,” anasema.
Anasema mitihani si migumu sana na kwamba maswali mengi walikuwa wamefundishwa.
“Kama nitafeli ni kwa sababu ya tatizo lililonitokea, lakini naomba Mungu nifaulu,” anaema.
Mwalimu Tinde anasema jambo zuri ni kuwa amemaliza kidato cha nne.