Saturday, August 8

Dk Magufuli, Lowassa pambano la karne


Dk John Magufuli (Kushoto) na Edward Lowassa (kulia) 

Dar es Salaam. Wakati zikiwa zimesalia siku 14 kabla ya kuanza kwa kampeni za urais, ubunge na udiwani, macho na masikio ya wengi yanaelekezwa kwa wagombea wawili kutoka vyama vikuu vya siasa, Dk John Magufuli wa CCM na Edward Lowassa wa Chadema, ambao uchambuzi wa gazeti hili unaonyesha wana mengi yanayoshabihiana.
Wawili hao ni kati ya makada saba waliosimamishwa na vyama saba kuwania urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na ambao inaelekea kuwa ndiyo watakaochuana vikali, hasa kutokana na ukweli kuwa Dk Magufuli anatoka chama tawala na Lowassa, ambaye alikuwa Waziri Mkuu, anaungwa mkono na vyama vinne vya Chadema, NCCR-Mageuzi, CUF na NLD vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).
Wengine wanaowania urais ni Mchungaji Christopher Mtikila wa DP, Chifu Lutayosa Chemba (ADC), Macmillan Limo (TLP), Hashimu Rungwe (Chauma), Fahami Dovutwa (UPDP) na mgombea wa ACT Wazalendo ambaye bado hajateuliwa.
Pamoja na kwamba katika siasa lolote linaweza kutokea, wagombea hao watano hawatazamiwi kuweka ushindani mkubwa zaidi ya ule wa Dk Magufuli na Lowassa.
Dk Magufuli hakutarajiwa kupita kwenye mbio za urais ndani ya CCM, ambako Lowassa na vigogo wengine walikuwa wakipewa nafasi kubwa, lakini ushindi wake umemfanya awe mgombea wa chama chenye mtandao mkubwa nchini na hivyo mwanzoni kupewa nafasi kubwa ya kushinda.
Hata hivyo, uamuzi wa Lowassa kujivua uanachama wa chama kilichomlea na kilichompa umaarufu mkubwa, umebadili upepo na sasa vita ya kuingia Ikulu Oktoba 25 inaonekana kuwa ya watu hao wawili.
Gazeti la Mwananchi linaangalia sifa ambazo wawili hao wanashabihiana pamoja na tofauti zao, kwa kuzingatia maelezo ya wachambuzi wa masuala ya kisiasa.
Wote wamesomea ualimu
Moja ya mambo ambayo wawili hao wanashabihiana ni kusomea ualimu, ingawa wa fani tofauti. Dk Magufuli, ambaye atakuwa akitimiza miaka 56 siku nne baada ya Uchaguzi Mkuu, ni mwalimu aliyejikita kwenye masomo ya kemia na hesabu.
Alipata diploma ya ualimu mwaka 1982 kwenye Chuo cha Elimu Mkwawa, kabla ya kujiunga Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ambako alipata shahada yake ya kwanza, ya umahiri na ya uzamiri akijikita kwenye somo la kemia.
Lowassa, ambaye Agosti 26 atakuwa akitimiza miaka 62, alisomea shahada ya ualimu Chuo Kikuu cha Dar es Salaam mwaka 1977, lakini shahada yake ya uzamili ilijikita kwenye masomo ya maendeleo ya jamii.
Dk Magufuli alitumia taaluma yake kufundisha kemia na hesabu kwenye Shule ya Sekondari ya Sengerema, lakini Lowassa hakufundisha.
Wote ni makini
Pengine ni kutokana na maadili ya ualimu, wawili hao wamedhihirisha kuwa ni watu makini katika utendaji wao, jambo ambalo limekuwa likiwafanya watu wanaofanya kazi chini yao kuwa na wasiwasi kila wanapowapeleka taarifa.
Dk Magufuli na Lowassa hutumia muda mwingi kujiridhisha na taarifa wanazopelekewa kabla ya kufanya uamuzi ambao wakati mwingine huonekana kama wamekurupuka.
Mhandisi mmoja ambaye amewahi kufungiwa leseni na Magufuli aliiambia Mwananchi kuwa kosa moja kubwa alilofanya ni kumwandikia Dk Magufuli taarifa ndefu, lakini iliyojaa mambo yasiyo sahihi.
Anasema kuwa aya hiyo ilikuwa ukurasa wa 20, lakini ndani ya muda mfupi Magufuli aliibaini na kibarua chake kiliota nyasi.
Hali ni kama hiyo kwa Lowassa, ambaye akiwa Waziri Mkuu aliwahi kumtimua mkandarasi wa Wilaya Temeke kwa kushindwa kukagua ujenzi wa maghorofa ikiwemo la Chang’ombe Village lililoporomoka na kusababisha maafa ya mtu mmoja na wengine kadhaa kujeruhiwa mwaka 2006.
Uchapakazi
Mbali na umakini, wawili hao wamedhihirisha kuwa ni wachapakazi hodari katika wizara na taasisi walizopitia kiasi cha kujijengea jina kubwa kwa wananchi.
Utendaji wa Dk Magufuli hauna shaka na ameshaeleza bayana kuwa hapendi wazembe na wasiowajibika sanjari, kama Lowassa ambaye hata siku ya kwanza alipoingia ofisini mwaka 2005 aliwataka wafanyakazi wa Ofisi ya Waziri Mkuu kuacha kufanya kazi kwa mazoea.
Wakati Dk Magufuli alipohamishiwa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, wengi walidhani kuwa amemaliza kisiasa, lakini mbunge huyo wa Chato alifanya kazi kubwa ya kutambua fursa za kiuchumi zilizoko hasa kwenye uvuvi na akafanikiwa kuonyesha ni kiasi gani Serikali ilikuwa ikipoteza fedha.
Wakati huo, Tanzania iliingia makubaliano na Afrika Kusini na nchi nyingine za ukanda huu kufanya doria kwa pamoja kwenye pwani ya Afrika Mashariki na juhudi hizo zilifanikiwa kunasa meli ya Tawaliq 1 iliyokuwa na samaki wenye thamani ya Sh20 bilioni.
Uchapakazi wake umedhihirika hasa kwenye ujenzi wa barabara, akiwa amefanikiwa kuunganisha takriban mikoa yote ya Tanzania katikja kipindi alichokaa Wizara ya Ujenzi.
Lowassa anaonekana zaidi katika kusimamia utekelezaji wa mradi wa maji ya Ziwa Victoria katika shughuli za maendeleo baada ya mpambano mkali dhidi ya Misri, ambayo ilikuwa na ukiritimba wa maji hayo kabla ya nchi tano kuungana na kusaini makubaliano ya matumizi ya maji hayo.
Lowassa pia anajinadi na mafanikio ya ujenzi wa shule za kata, ambazo kwa kiasi kikubwa zimefanikisha watoto wengi kupata elimu kwa gharama nafuu, ujenzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma ambao aliufanya kwa kukutanisha mifuko ya hifadhi ya jamii na kuiamuru ichangia gharama za ujenzi.
Jambo lingine walilonalo Dk Magufuli na Lowassa ni misimamo. Dk Magufuli ni kiongozi mwenye misimamo isiyotia shaka na siku zote husimamia anachokiamini, sanjari na Lowassa, ni mwenye misimo yake na itakumbukwa alipokuwa Waziri wa Maji na baadaye Waziri Mkuu alionyesha misimamo.
Dk Magufuli alitofautiana hata na Waziri Mkuu Mizengo Pinda wakati aliposimamia uendeshaji wa kivuko cha Kigamboni, na suala la kiwango cha mizigo inayobebwa na malori.
Moja ya kauli zilizonukuliwa sana ni ile ya “asiyekuwa na nauli ya kulipia kivuko, apige mbizi”, ambayo ilitafsiriwa kuwa ya kutojali wananchi, lakini faida zake ndio zinamfanya aonekane kuwa msimamo wake ulilenga kunufaisha wananchi.
Hali kadhalika Lowassa anajulikana kwa kusimamia uamuzi kama wa kubomoa maghorofa yaliyojengwa kinyume na sheria Masaki jijini Dar es Salaam. Msimamo wake pia kwenye suala la mkataba wa City Water iliyokuwa ikihusika na ugavi wa maji jijini Dar es Salaam ndio uliosababisha uvunjwe.
Ufuatiliaji
Lowassa na Dk Magufuli pia wanajulikana kwa kuwa wafuatiliaji wazuri kwa watu walio chini yao au wanaofanya kazi chini ya mamlaka zao. Dk Magufuli, ambaye anajulikana kwa kukariri tarehe, kiwango cha miradi, urefu wa barabara na kiwango cha fedha zilizotengwa kwenye miradi, hutumia talanta hiyo kufuatilia miradi mbalimbali na hasa muda wa kumalizika, hali inayomfanya kila mara atishia kuvunja mikataba na wakandarasi au kuivunja kabisa.
Hilo pia limekuwa likifanywa na Lowassa, ambaye akiwa Waziri Mkuu alikuwa akihakikisha wakuu wa wilaya na mikoa wako sehemu zao za kazi na yeyote ambaye alitaka kutoka alitakiwa awe na kibali, kwa mujibu wa baadhi ya watu waliofanya kazi naye.
Udhaifu
Mbali na sifa hizo nzuri, wanasiasa hao wanashabihiana katika udhaifu, hasa uamuzi wa papo kwa papo ambao pia husababishwa na kiu yao ya kutaka kuona kazi inafanyika.
Wote wawili hufanya uamuzi wa papo kwa pamo ambao wakati mwingine huwa na athari za kisheria. Uamuzi kama huo huwa na kadhia kwa wafanyakazi na makandarasi wanaopewa zabuni mbalimbali na Serikali.
Hawaachi mfumo wa utendaji
Udhaifu mwingine wa wawili hao ni hali ya kujituma wao bila ya kutengeneza mfumo ambao unaendeleza ufanisi na badala yake wanapoondoka, hali hubakia kama ilivyokuwa awali.
Hivi ndivyo ilivyokuwa kwa Dk Magufuli kwenye wizara alizopitia kama ya uvuvi na hali kadhalika kwa Lowassa.
Pia wanatofautiana
Tofauti kubwa kati ya Dk Magufuli na Lowassa ni mgombea huyo wa CCM kutokulia ndani ya chama na badala yake amekuwa kwenye nafasi za utendaji zaidi na uwaziri. Dk Magufuli amekuwa mwanachama wa CCM na mbunge, nafasi ambayo humuingiza kwenye kikao cha Halmashauri Kuu pekee.
Lakini Lowassa ameshika nafasi mbalimbali kwenye chama kuanzia katibu wa mkoa hadi mjumbe wa vyombo vya juu vya CCM.
Kauli za wachambuzi
Baadhi ya wachambuzi na wasomi kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, (Udsm) wamesema kwa nyakati tofauti kwamba wagombea hao wanaonekana kuwa na tofauti kubwa zinazoweza kufanikisha ushindi katika uchaguzi huo.
Mohammed Bakari, ambaye ni mhadhiri wa Idara ya Sayansi ya Siasa wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, alisema wagombea hao wanafanana katika kigezo cha utendaji kazi lakini kiuamuzi na uzoefu wanatofautiana.
“Dk Magufuli ana uamuzi wa kukurupuka ila Lowassa ametulia,” alisema. “Kuhusu uzoefu pia Lowassa ni mzoefu kiuongozi kuliko Dk Magufuli.”
Alisema suala la uadilifu siyo rahisi kupata kiongozi mwadilifu kwa wagombea hao na bila kuzitaja kashfa hizo, alisema wote wana kashfa. Aliongeza kwamba, Lowassa ni mgombea anayeweza kuleta mabadiliko kwa Taifa hili, lakini Dk Maghufuli hawezi kutokana na mfumo uliopo kwenye chama chake.
Mkuu wa Idara ya Sayansi ya Siasa wa Udsm, Dk Alexander Makulilo pia anaona sifa hizo zinazolingana.
Alisema wagombea hao wanafanana kwa utendaji mzuri wa kazi na uamuzi wa papo kwa hapo. Aidha, alisema Magufuli ni kiongozi anayeweza kuleta siasa mpya zisizokuwa na makundi.
Alisema Lowassa ni mgombea anayekabiliwa na changamoto ya Richmond iliyomfanya ajiuzulu uwaziri mkuu, wakati Dk Magufuli hana kashfa kubwa iliyowahi kujadiliwa bungeni.
“Lakini hali hiyo haiwezi kuwa changamoto kubwa kutokana na mwamko mkubwa wa kundi linalohitaji mabadiliko ya uongozi serikalini. Uchaguzi huu ninaufananisha na Zambia wakati chama cha UNIP kilipoondolewa madarakani kwa kuwa makundi ya kijamii yalikuwa yameamua kiondoke madarakani,” alisema.
Kuhusu mfumo kuibeba CCM, Dk Makulilo alisema ni sehemu ya changamoto kubwa inayoweza kufanikisha ndoto za Lowassa kuingia madarakani.

Gesi kuanza kusafirshwa Dar baada ya siku 14


Mtwara. Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Nchini (TPDC), James Mataragio amesema kuwa gesi asilia itaanza kusafirishwa kwa njia ya bomba kutoka Mtwara kuelekea Dar es Salaam, baada ya siku wiki mbili kuanzia sasa.
Mataragio ametoa kauli hiyo jana baada ya kutembelea kiwanda cha kuchakata gesi kilichopo kijiji cha Madimba Wilaya ya Mtwara mkoani hapa na kujionea sehemu kubwa ya mradi huo, ukiwa umekamilika kwa asilimia 100.
Hivi karibuni Waziri wa Nishati na Madini, George Simbachawene alisema umeme wa gesi utaanza kutumika mwezi ujao baada ya ujenzi wa bomba la kupitisha gesi hiyo kukamilika.
Mataragio alisema kuwa kutokana na kiwanda hicho cha kuchakata gesi asilia kukamilika kwa asilimia kubwa, Watanzania wategemee kuanzia mwezi ujao wataanza kutumia umeme unaotokana na Nishati hiyo ya Gesi Asilia.
“ Sisi kama TPDC kabla gesi haijaanza kusafirishwa tunajiridhisha kwanza kwa kufanya majaribio ya mitambo kwa sababu inakuwa bado haijaanza kufanya kazi, tunaangalia uwezo wake ili tuweze kujiridhisha ndiyo tuisafirishe kuelekea Dar es Salaam.” Alisema Mataragio.
Kadhalika Mkurugezi huyo alisema kuwa wananchi wa mkoani hapa watanuifaka na gesi hiyo kutokana na ujenzi wa kiwanda cha Saruji cha Dangote pamoja na shughuli mbalimbali zitakazowaongezea kipato kutokana na rasilimali hiyo.
Alisema kuwa wananchi hao watanufaika na kiwanda hicho cha kuchakata gesi asilia kwa kupata maji safi na salama, pamoja na kuwajengea kituo cha Afya ili kiweze kuwasaidia kupitia mradi huo.
Hata hivyo Mataragio alisema kuwa hadi sasa kuna visima ambavyo vimepatikana katika eneo la Mnazi Bay pamoja na Msimbati, na utafiti bado unaendelea kutafuta visima vingine.

NEC: Marufuku kutoa kadi ya kupigia kura

Mwenyekiti wa NEC, Jaji mstaafu Damian Lubuva 

Dar es Salaam. Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), imeonya kwamba mtu yoyote haruhusiwi kutoa kadi yake ya kupigakura au taarifa za kadi hiyo kwa ndugu, jamaa au mwajiri wake.
NEC imetoa onyo hilo wakati tayari kukiwa na tetesi kuwa baadhi ya wafanyakazi wa umma wakiwamo polisi, wanajeshi na askari magereza, wametakiwa kukabidhi kadi zao kwa viongozi wao wa ngazi za juu.
Wakati hayo yakisemwa, Naibu Katibu Mkuu wa Chadema Bara, John Mnyika jana aliitisha mkutano wa vyombo vya habari akidai kuna tetesi serikali imeviagiza vyombo vya usalama, kupeleka namba za vitambulisho vya askari wote kwa wakuu wa vitengo jambo ambalo ni kunyume na utaratibu
Mkurugenzi wa Uchaguzi wa NEC, Kailima Kombwey alitoa angalizo juu ya hilo na kusema kuwa kwa mujibu wa Sheria ya Uchaguzi ambayo inazungumzia Daftari la Kudumu la Wapigakura, hairuhusiwi na haitakiwi kwa mtu asiyehusika na kadi ya mpigakura kuimiliki kadi hiyo.
Kombwey alisema hakuna sheria yoyote inayomlazimisha mtumishi wa umma kutoa kadi yake ya kupigiakura kwa mwajiri wake.
Akizungumzia suala hilo, Msemaji wa JWTZ, Kanali Ngemela Lubinga alisema taarifa hizo ni za uongo na hazina ukweli wowote kuwa wanajeshi wameombwa nambari za vitambulisho.
Msemaji wa Polisi, Advera Bulimba alipopigiwa simu kuhusu madai hayo, alisema hana hizo taarifa.
Ofisa Mawasiliano wa Magereza, Deodatus Kazinja alisema hizo ni tetesi na wala hazina ukweli wowote.
*Imeandikwa na Hussein Issa na Florid Mapunda, Suzan Mwillo

‘Lipumba angetaka ningemwachia urais’

Profesa Ibrahimu Lipumba 
Dar es Salaam. Mgombea urais kupitia tiketi ya Chama cha Alliance for Democratic Change (ADC) Chifu Lutalosa Yemba, amemkaribisha aliyekuwa Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba kujiunga na chama hicho.
Chama hicho juzi kilifanya mkutano wa kuwatambulisha wagombea wake wa nafasi ya urais, Yemba anayewania urais wa muungano na mgombea mwenza wake Said Miraj Abdullah, pia alitambulishwa Hamad Rashid Mohamed, anayewania urasi wa Zanzibar.
Yemba kwenye mkutano huo alisema anaufahamu uwezo wa Lipumba katika siasa, ujasiri na uvumilivu wake, hivyo hatakuwa na kinyongo kufanya naye kazi ya kusukuma mbele gurudumu la siasa za upinzani.
Alisema hakujiunga na chama hicho kwa ajili ya kuwa rais, amejiunga kwa ajili ya kutengeneza dola ya uongozi itakayoondoa dhiki na mateso wanayopata Watanzania, hivyo kutokana na uzowefu alionao katika siasa anaamini watafanikisha hilo kwa ufanisi.
“Walinifukuza mwezi wa sita , mwezi wa nane Lipumba amejing’atua kwenye uongozi, watafahamu sasa kuwa kwenye chama kile kuna udhalimu, namkaribisha Lipumba na ninampongeza kwa uvumilivu wake, ingawa ninaumia kuona kiongozi shupavu aliyekuwa na uwezo wa kuhakikisha wananchi wanaamini katika vyama vingine vya upinzani kukatishwa tamaa na watu wachache wenye uroho wa madaraka, ”alisema Yemba.
Alisema kuwa anaingia katika kinyang’anyiro cha kuwania urais akipambana na chama kimoja tu, CCM, hivyo vilivyobaki hakuna wa kumtisha kwa sababu wenyewe kwa wenyewe wameanza kuvurugana.
“Sisi ADC kama bahari, tunachukua maovu yao tunameza, baadaye tunayatema, wakati ukifika wa kufanya hivyo tutafanya kwa sasa , nawaomba Watanzania mpime kwa makini na kuchagua kiongozi anayefaa.
“Mchagueni asiyekuwa mwizi, fisadi, mnyang’anyi asiye na kashfa na hakuna unapoweza kumpata kiongozi wa namna hiyo zaidi ya ADC, pimeni sikilizeni sera zetu, ilani yetu mtuunge mkono. ”alisema Yemba.
Jana, Yemba alichukua fomu za kuwania urais wa chama hicho, Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec), huku akiwasisitiza Watanzania kukipa nafasi chama hicho ili kuifanyia nchi mabadiliko ya haki na kuondokana na ukandamizaji.
Kabla ya kufikia uamuzi wa kuchukua fomu Nec, Yemba alinukuliwa akisema kama Lipumba angejitokeza jana, angemwachia nafasi ya kuwania urais wa Jamhuri ya Muungano. Hata hivyo kuna taarifa Lipumba alisafiri juzi usiku kwenda nje ya nchi.
Said Miraj Abdulla
Kwa upande wa mgombea mwenza wa chama hicho Said Miraj Abdulla, alisema kuwa anamualika Maalim Seif awaeleze Watanzania anataka nini katika siasa, kwa nini anavuruga utaratibu wa kuwapo kwa upinzani wa kweli.
Alieleza kuwa pamoja na kuunga mkono kilichofanywa na Lipumba kutokana na udhalimu unaofanywa na wanasiasa wachache wanaokatisha tamaa wengine, lakini hafurahi kumuona au kusikia anakaa nje ya ulingo wa siasa.
“Nani asiyejua mchango wa Lipumba katika siasa za upinzani wa nchi, arudi kwenye siasa aje kuendeleza safari aliyoianza mwaka 1995, kukaa kwake nje ya siasa kunapunguza nguvu ya Watanzania kufikia kilele cha mafanikio ya kupata rais atakayejali shida zao, kuwasikiliza, kuwanufaisha na rasilimali zinazopatikana nchini mwao, ”alisema Abdulla.
Hamad Rashid Mohamed
Kwa upande wa mgombea urais wa Zanzibar, Hamad Rashid Mohamed, aliwataka wananchi kuwa makini wanaposhabikia vyama na kuviepuka visivyoheshimu Katiba.
Alisema alipokuwa kwenye Bunge la Katiba alisema hakuna upawa wala Ukawa, matokeo yake ndiyo hayo watu wanalumbana, Wazanzibar wanahitaji mabadiliko wamekaa kwenye umasikini usiowahusu kwa sababu hakuna ajira.
Alieleza kuwa kwa wakazi wa Zanzibar wanaohitaji ajira, akijenga viwanda vitano tu hakutakuwa na kijana atakayekosa kazi na huo ndiyo mkakati wake katika miaka mitano ya uongozi.
“Watanzania shabikieni vyama huku mkiwapima wagombea wana nia gani na nyinyi, maslahi yao binafsi au kuwasaidia, maana “Tumbili akimaliza miti anakuja mwilini” kuweni makini, ”alisema.

Maalim Seif ‘amchana’ Profesa Lipumba

Katibu Mkuu wa CUF na Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar, Maalim Seif Sharrif Hamad 

Dar es Salaam. Katibu Mkuu wa CUF na Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar, Maalim Seif Sharrif Hamad amesema ameshangazwa na sababu zilizotolewa na Profesa Ibrahim Lipumba aliyejivua uenyekiti wa chama hicho, kuwa amechukizwa na kitendo cha kukaribishwa kwa makada wa CCM ndani ya Ukawa.
Akizungumza na wanachama wa CUF makao makuu ya chama hicho Buguruni, Dar es Salaam juzi usiku, Maalim Seif alimtakia kila la kheri profesa huyo mtaalamu wa masuala ya uchumi na kusisitiza kuwa chama hicho kitaendeleza malengo ya kuanzishwa kwake, ikiwa ni pamoja na kushika dola.
Profesa Lipumba, mmoja wa waasisi wanne wa Ukawa-Umoja wa Katiba ya Wananchi unaoundwa na vyama vinne vya Chadema, CUF, NCCR-Mageuzi alichukua uamuzi huo juzi na kwamba amejitahidi kuvumilia ujio wa makada wa CCM ndani ya Ukawa, lakini ameshindwa.
Wengine walioongoza harakati za kuasisi Ukawa ni Freeman Mbowe, ambaye ni mwenyekiti wa Chadema, James Mbatia wa NCCR-Mageuzi na Emmanuel Makaidi wa NLD.
Profesa Lipumba, mmoja wa wenyeviti wanne wa Ukawa na mwenyekiti wa wenyeviti hao, aliyeeleza sababu za kumkaribisha Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa kwenye umoja huo takribani siku 10 zilizopita, amejivua wadhifa huo kutokana na vyama hivyo kukubali kupokea watu walioshiriki kukataa Rasimu ya Katiba iliyopendekezwa na wananchi, kitu ambacho kilikuwa msingi wa kuundwa kwa Ukawa.
“CUF kipo imara na katika mikono salama kabisa. Mimi na viongozi wenzangu tuliobaki tutahakikisha chama hiki kinafikia malengo ya kuundwa kwake, hakuna jingine isipokuwa kukamata hatamu ya dola,” alisema Maalim Seif na kushangiliwa na kundi kubwa la wanachama wa chama hicho waliofika makao makuu ya chama hicho usiku kujua hatma ya uongozi na viongozi wao.
Mbali na kumshukuru, alisema Profesa Lipumba ndiye mwasisi wa Ukawa na alikuwa mwenyekiti wa wenyeviti wa Ukawa, kusisitiza kuwa alikaa na wenzake (wenyeviti wenza wa Ukawa) na kukubaliana kumkaribisha Lowassa ndani ya Ukawa.
“Na yeye ndiye aliyeanza kumsafisha mzee Lowassa. Nasema kwamba Ukawa ipo na imeimarika. Kwa kumuingiza Lowassa na nguvu za pamoja za vyama vinavyounda Ukawa ikiungwa mkono na wananchi wote wa Tanzania, Magufuli (John) hataiona Ikulu ya Kigamboni,” alisema.
Wakati akitangaza kujivua uenyekiti, Profesa Lipumba alipoulizwa sababu za kugeuka wakati yeye alikuwa ni miongoni mwa wenyeviti wa Ukawa waliomkaribisha Lowassa, alikiri akisema kuwa suala la rushwa na ufisadi ni mfumo ambao lazima uondolewe lakini kwa sasa “dhamira yangu na nafsi yangu vinanisuta.”
Katika maelezo yake ya juzi usiku, Maalim Seif alisema ana uhakika Ukawa itachukua dola kwa maelezo kuwa haitarudi nyuma na si dhamira yake kurudi nyuma.
“Lowassa ana msamiati wake kuwa kushindwa kwake mwiko, lengo letu ni moja tu, vyovyote itakavyokuwa tushike hatamu ya dola,” alisisitiza Maalim Seif.
Kikao cha Dharura
Wakati hali ya sintofahamu ikiwakumba makada wa chama hicho, uongozi wa CUF umeitisha kikao cha dharura cha Kamati ya Utendaji ya Taifa na Baraza Kuu la Uongozi ili kutafuta mwanachama atakayekaimu nafasi iliyoachwa wazi na Profesa Lipumba kitakachofanyika kesho.
Tamko hilo limetolewa na Kaimu Mkurugenzi wa Habari, Uenezi na Mawasiliano ya Umma, Ismail Jussa Ladhu, na kuwahahakikishia wanachama, wapenzi wa CUF na wananchi wa Tanzania kwamba chama hicho hakitayumba.
Alisema katika historia yake, CUF imepita katika dhoruba na misukosuko mingi, lakini mara zote imeonyesha uwezo mkubwa wa kuhimili na kukabiliana na athari zake.

Wamiminika Ofisi za Chadema ‘kumlaki’ Dk Slaa

Katibu Mkuu, Dk Willbrod Slaa 

Dar es Salaam. Baadhi ya wanachama na mashabiki wa Chadema jana walifika katika ofisi za Makao Makuu ya chama hicho, Kinondoni Dar es Salaam kumsubiri Katibu Mkuu, Dk Willbrod Slaa baada ya kuenea uvumi kuwa angeingia ofisini.

Hata hivyo, wanachama hao waliokuwa na shauku ya kumwona kiongozi huyo, hawakufanikiwa baada ya kuambiwa kuwa Dk Slaa asingefika katika ofisi hizo kinyume na taarifa zilizokuwa zimezagaa kuhusu kurejea kwake.
Kwa muda mrefu Dk Slaa hakuonekana kwenye matukio muhimu ya Chadema na yale ya Ukawa, kama wakati wa kumkaribisha Edward Lowassa ndani ya chama hicho, wakati Lowassa alipochukua kadi na alipochukua fomu ya kuwania urais.
Kadhalika kiongozi huyo hakuonekana katika Baraza Kuu la Chadema, mkutano wa Kamati Kuu na Mkutano Mkuu uliompitisha kwa kauli moja kuwa Lowassa aipeperushe bendera ya urais chini ya mwamvuli wa Ukawa.
Akihutubia Baraza Kuu la chama hicho wiki iliyopita, Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe alisema kuwa chama kiliridhia Dk Slaa apumzike wakati mchakato wa kuelekea Uchaguzi Mkuu ukiendelea baada ya Katibu Mkuu huyo kutofautiana katika uamuzi wa kumkaribisha Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa.
Baraza Kuu lilipiga kura ya wazi na kushauri kuwa endapo atafikiria kubadili uamuzi wake, anaweza kuendelea na harakati za chama hicho kuelekea Ikulu chini ya muungano wa Ukawa.
Mwandishi wetu aliyefika katika ofisi za Chadema zilizopo katika Mtaa wa Ufipa, Wilaya ya Kinondoni, alishuhudia idadi kubwa ya wanachama wakiwa wamekusanyika katika vikundi wakijadili masuala mbalimbali huku wakimsubiri Dk Slaa.
“Nimesikia taarifa kuwa kuna watu hapa wanamsubiri Dk Slaa nikaja kushuhudia, watu wanaongea mambo mengi kama vile Ukawa imevunjika wakati kila kitu kinakwenda sawa hapa,” alisema Ali Mundu mmoja wa wananchama hao.
Alisema kutokana na taarifa nyingi zilizosambaa mitaani kuhusu kuwepo kwa sintofahamu miongoni mwa viongozi wa Ukawa, kila mtu amekuwa akisema kitu anachojua hivyo ili kupata taarifa sahihi ni vyema wana-Ukawa wanafika kujionea kinachoendelea.