Saturday, August 8

Gesi kuanza kusafirshwa Dar baada ya siku 14


Mtwara. Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Nchini (TPDC), James Mataragio amesema kuwa gesi asilia itaanza kusafirishwa kwa njia ya bomba kutoka Mtwara kuelekea Dar es Salaam, baada ya siku wiki mbili kuanzia sasa.
Mataragio ametoa kauli hiyo jana baada ya kutembelea kiwanda cha kuchakata gesi kilichopo kijiji cha Madimba Wilaya ya Mtwara mkoani hapa na kujionea sehemu kubwa ya mradi huo, ukiwa umekamilika kwa asilimia 100.
Hivi karibuni Waziri wa Nishati na Madini, George Simbachawene alisema umeme wa gesi utaanza kutumika mwezi ujao baada ya ujenzi wa bomba la kupitisha gesi hiyo kukamilika.
Mataragio alisema kuwa kutokana na kiwanda hicho cha kuchakata gesi asilia kukamilika kwa asilimia kubwa, Watanzania wategemee kuanzia mwezi ujao wataanza kutumia umeme unaotokana na Nishati hiyo ya Gesi Asilia.
“ Sisi kama TPDC kabla gesi haijaanza kusafirishwa tunajiridhisha kwanza kwa kufanya majaribio ya mitambo kwa sababu inakuwa bado haijaanza kufanya kazi, tunaangalia uwezo wake ili tuweze kujiridhisha ndiyo tuisafirishe kuelekea Dar es Salaam.” Alisema Mataragio.
Kadhalika Mkurugezi huyo alisema kuwa wananchi wa mkoani hapa watanuifaka na gesi hiyo kutokana na ujenzi wa kiwanda cha Saruji cha Dangote pamoja na shughuli mbalimbali zitakazowaongezea kipato kutokana na rasilimali hiyo.
Alisema kuwa wananchi hao watanufaika na kiwanda hicho cha kuchakata gesi asilia kwa kupata maji safi na salama, pamoja na kuwajengea kituo cha Afya ili kiweze kuwasaidia kupitia mradi huo.
Hata hivyo Mataragio alisema kuwa hadi sasa kuna visima ambavyo vimepatikana katika eneo la Mnazi Bay pamoja na Msimbati, na utafiti bado unaendelea kutafuta visima vingine.

No comments:

Post a Comment