Monday, November 27

Jica yasema iko tayari kuboresha makao makuu Dodoma




Dar es Salaam. Shirika la Kimataifa la Maendeleo la Japan (Jica) limesema liko tayari kushirikiana na Serikali kujenga miundombinu ya kisasa ya usafiri, nishati ya umeme, maji na usafi wa mazingira katika makao makuu ya nchi, Dodoma.
Ahadi hiyo imetolewa na Makamu wa Rais wa shirika hilo, Hiroshi Kato alipokutana kwa mazungumzo na Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango, jijini Dar es Salaam.
Kato katika taarifa iliyotolewa na wizara leo Jumatatu Novemba 27,2017 amesema mradi mwingine wanaotaka kuutekeleza katika Mji wa Dodoma ni udhibiti wa taka ngumu.
Amesema wanachosubiri ni Serikali kuainisha maeneo ya vipaumbele vilivyoko katika mpango mji wa Dodoma.
Kato amesema shirika hilo litaendelea kusaidia eneo la kilimo na hasa cha mpunga ili kuongeza thamani ya zao hilo na kuwakomboa wakulima.
Waziri Mpango amelishukuru shirika hilo kwa kuonyesha nia ya kusaidia ujenzi wa mji wa Dodoma.
Amesema mradi huo utasaidia kwa kiasi kikubwa kuupanga mji wa Dodoma mapema ili kuondoa changamoto za msongamano wa huduma za jamii kwenye eneo moja kama ilivyo jijini Dar es Salaam.
“Pamoja na umuhimu wa miundombinu ya maji, umeme, usafiri wa mjini, lakini pia tunataka tujenge mapema njia za juu ili kudhibiti msongamano wa magari,” amesema Dk Mpango.
Amesema mradi mwingine wa kipaumbele katika mji huo ni ujenzi wa uwanja wa ndege wa kimataifa katika eneo la Msalato, takriban kilomita 20 kutoka katikati ya mji huo ili kurahisisha usafiri kwa njia ya anga.

Hospitali za rufaa za mikoa zahamishiwa Wizara ya Afya


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tamisemi, Selemani Jafo amekabidhi hospitali za rufaa za mikoa kwa Wizara ya Afya.
Hatua hiyo ni utekelezaji wa pendekezo la Rais John Magufuli aliyetaka waziri wa Tamisemi na wa Waziri ya Afya wakae kujadili namna ya kuzifanya hospitali za mikoa kuwa chini ya Wizara ya Afya badala ya kusimamiwa na Tamisemi kama ilivyo sasa.
Jumamosi Novemba 25,2017 alipozindua Hospitali ya Taaluma na Tiba ya Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (Muhas), kampasi ya Mloganzila, Rais Magufuli alisema kufanya hivyo kutaondoa mkanganyiko na kupanga watumishi holela kwenye hospitali, jukumu ambalo wamepewa watu wasio na utaalamu wa masuala ya afya.
Rais Magufuli alisema Tamisemi watabaki wanasimamia hospitali za wilaya na nyingine ndogo.
Waziri Jafo amesema leo Jumatatu Novemba 27,2017 kuwa tayari wameshafanya mazungumzo.
"Kuanzia leo hospitali zote za rufaa zitakuwa chini ya Wizara ya Afya na kwetu sisi (Tamisemi) tutabaki na hospitali za wilaya, vituo vya afya na zahanati pekee," amesema.
Kuhusu madaraka ya waganga wakuu wa mikoa amesema wataendelea kuwa chini ya Tamisemi lakini waganga wafawidhi wa hospitali watapelekwa Wizara ya Afya.
Amewataka waganga hao kufanya kazi waliyokubaliana na Tamisemi ya kusimamia ujenzi wa vituo vya afya 172 nchi nzima.
Akizungumza mgongano wa madaraka kwa waganga wa mikoa, Naibu Katibu Mkuu Tamisemi (Afya), Dk Zainabu Chaula amesema hakutakuwa na shida kwa kuwa kila kitu kimewekwa sawa.
Dk Chaula amesema hata kabla ya kupelekwa huko, hospitali za mikoa zilikuwa zikipeleka taarifa moja kwa moja wizarani.

Mbunge Lijualikali atafutwa na polisi



Mbunge wa Mlimba (Chadema), Susan Kiwanga.
Mbunge wa Mlimba (Chadema), Susan Kiwanga. 
Polisi mkoani Morogoro inawashikilia watu 41 akiwemo mbunge wa Mlimba (Chadema), Susan Kiwanga.
Pia inawashikilia madiwani wawili, huku mbunge wa Kilombero (Chadema), Peter Lijualikali akitafutwa na jeshi hilo wakidaiwa kufanya fujo na kuchoma moto ofisi ya mtendaji baada ya kutangazwa matokeo ya uchaguzi mdogo wa udiwani katika Kata ya Sofi wilayani Malinyi.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Urlich Matei katika taarifa leo Jumatatu Novemba 27,2017 amesema tukio hilo lilitokea jana Jumapili Novemba 26,2017 saa tano usiku ambako walikwenda kwa ajili ya uchaguzi mdogo wa udiwani.
Kamanda Matei amesema wabunge hao na madiwani wawili wa Chadema kutoka Ifakara walionekana kuhamasisha baadhi ya wafuasi wao kufanya vurugu.
Amesema watuhumiwa wanadaiwa kuchoma majengo ya umma ambayo ni ofisi shule ya msingi Sofi, nyumba ya walimu wa shule hiyo na ofisi ya mtendaji kata.
Kamanda Matei amesema fujo na uharibu huo ulitokea baada ya msimamizi wa uchaguzi kutangaza matokeo kuwa mgombea wa CCM ndiye alishinda kwa kupata kura 2,099.
Mgombea wa chama alipata kura 1,684 jambo lililopingwa na wafuasi wa chama hicho na kuanza  vurugu.
Amesema baada ya kuchoma majengo hayo kwa kutumia petroli, walidhamiria pia kwenda katika zahanati lakini askari waliwakamata.
Kamanda Matei amesema polisi inaendelea kuwatafuta watu wengine waliohusika na vurugu hizo, akiwemo mbunge Lijualikali.
Amesema watuhumiwa 41 wamepelekwa wilayani Ulanga kwa ajili ya kufikishwa mahakamani kujibu tuhuma zinazowakabili.
Mbunge Lijualikali akizungumza na MCL Digital kwa simu kuhusu vurugu hizo amesema wakati matokeo yakitangazwa alikuwa Ifakara.
Amesema taarifa za kutafutwa na polisi ndiyo kwanza anazisikia kutoka kwa mwandishi wa habari waMCL Digital.
 “Baada ya kumalizika kampeni Jumamosi nilirejea Ifakara kwa hiyo sijui chochote kuhusu hizo vurugu na nashangazwa kuhusishwa na tuhuma hizo, lakini kama kweli natafutwa nitakwenda kujisalimisha polisi,” amesema Lijualikali.

Ubomoaji jengo la Tanesco waanza


Uongozi wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) umesema umeanza utekelezaji wa agizo la Rais John Magufuli la kubomoa jengo lake lililo ndani ya hifadhi ya barabara eneo la Ubungo jijini Dar es Salaam.
Kazi hiyo iliyoanza leo Jumatatu Novemba 27,2017 ni utekelezaji wa agizo la Rais Magufuli aliyeagiza majengo ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji na ghorofa la Tanesco kuwekwa alama ya X kwa ajili ya kubomolewa.
Novemba 15,2017 akitokea Chato alipokwenda kwa mapumziko baada ya ziara ya Uganda, Rais Magufuli aliagiza Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads) kuweka alama ya X katika majengo hayo sehemu zilizo katika hifadhi ya barabara.
Taarifa ya Tanesco kwa umma imesema kuanzia leo Jumatatu Novemba 27,2017 wameanza kubomoa ukuta wa mbele ya jengo.
Tanesco imesema baadhi ya watumishi wa shirika hilo wameanza kuhamishiwa katika ofisi nyingine za shirika zilizopo jijini Dar es Salaam ili kupisha shughuli za ubomoaji kufanyika kwa usalama.
Uongozi wa shirika hilo na Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) unaendelea kufanya utaratibu utakaowezesha ubomoaji wa jengo hilo la ghorofa kufanyika bila kuathiri huduma kwa wateja wa Tanesco.
“Katika kipindi hiki cha utekelezaji wa agizo la Rais. Tunapenda kuwahakikishia wateja  na Watanzania kwa jumla kuwa, huduma za umeme zitaendelea kupatikana kama kawaida ikiwemo huduma ya ununuzi wa Luku,” imesema taarifa hiyo.
Uongozi wa shirika hilo umesema utaendelea kutoa taarifa kwa kadri kazi hiyo itakavyokuwa ikiendelea.

Dart inalenga kuwa na mabasi 305


Dar es Salaam. Wakala wa Mabasi Yaendayo Haraka (Dart), unatarajia kuongeza mabasi katika mfumo wake kutoka 140 yaliyopo sasa hadi 305 pindi awamu ya kwanza ya mfumo huo itakapokamilika Juni 2018.
Taarifa iliyotolewa leo Jumatatu Novemba 27,2017 kwa vyombo vya habari imemkariri Mtendaji Mkuu wa Dart, Ronald Lwakatare akitoa kauli hiyo baada ya kupokea wageni sita kutoka Serikali ya Rwanda waliokuja nchini kwa ziara ya siku tano kujifunza namna wakala huo unavyotoa huduma.
Mhandisi Lwakatare amesema kuongeza mabasi kutaongeza idadi ya abiria kutoka 200,000 kwa siku hadi kati ya 400,000 na 500,000 kwa siku.
“Mbali na hilo pia tutaongeza njia za mlisho kutoka mbili zilizopo sasa hadi tisa zitakazokuwa zikienda Masaki, Sinza, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam  na maeneo mengine ambayo yapo jirani ili kupanua huduma ya usafiri katika maeneo yaliyomo ndani ya mfumo wa mabasi yaendayo haraka katika awamu ya kwanza ya mradi,” amesema Mhandisi Lwakatare.
Pia, amezungumzia athari iliyotokana na mvua iliyonyesha Oktoba 26, akisema mfumo wa mabasi uliathiriwa kwa kuwa mabasi 20 yaliharibika zaidi lakini yameshatengezwa na kuanza kutoa huduma.
Amesema Dart imejipanga kuhakikisha mitaro yote inayozunguka karakana ya Jangwani inasafishwa ili kuepuka eneo hilo kukumbwa tena na mafuriko.
Kuhusu wageni hao, Mhandisi Lwakatare amesema wamekuja kujifunza kuhusu mradi huo na hatua waliyoifikia Dart ikizingatiwa Jiji la Kigali lina mpango wa kuwa na mfumo kama huo.
Kiongozi wa ujumbe huo kutoka Mamlaka  ya Halmashauri ya Jiji la Kigali, Rwagatore Etienne amesema wameamua kuchagua kutembelea wakala huo kwa sababu ndiyo mradi uliofanikiwa barani Afrika na upo karibu na nchi ya Rwanda.
Katika msafara, Etienne ameambatana na  wataalamu washauri ambao ndio waliopewa kazi ya usanifu wa Jiji la Kigali ili liweze kuwa na mfumo wa mabasi yaendayo haraka.

Mugabe apewa sikukuu ya taifa Zimbabwe

Mugabe alikuwa ameongoza Zimbabwe tangu uhuru 1980Haki miliki ya pichaAFP
Image captionMugabe alikuwa ameongoza Zimbabwe tangu uhuru 1980
Serikali ya Zimbabwe imetangaza siku kuu mpya ya kukumbuka mchango wa Robert Mugabe ambaye aliondolewa madarakani wiki iliyopita.
Gazeti la serikali la Herald limesema sikukuu hiyo itakuwa ikiadhimishwa siku ya kuzaliwa kwa Bw Mugabe kila mwaka.
Uamuzi wa kusherehekea Siku ya Taifa ya Vijana ya Robert Gabriel Mugabe kila 21 Februari ulifanywa rasmi kupitia tangazo rasmi kwenye gazeti la serikali.
Tangazo hilo lilichapishwa Ijumaa - siku ambayo Rais Emmerson Mnangagwa aliapishwa kuwa rais, na kufikisha kikomo uongozi wa Mugabe wa miaka 37.
Serikali ya Bw Mugabe ilikuwa imeamua kutangaza siku ya kuzaliwa kwake kuwa sikukuu ya taifa mwezi Agosti, baada ya kampeni kutoka kwa mrengo wa vijana katika chama cha Zanu-PF.
Image captionRaia walimshangilia rais Mpya wa Zimbabwe Emmerson Mnangagwa siku ya kuapishwa kwake
Bw Mugabe aliondolewa mamlakani wiki iliyopita kutokana na shinikizo kutoka kwa wanajeshi waliokuwa wamechukua udhibiti wa serikali wiki iliyotangulia.
Alijiuzulu na Bw Mnangagwa, makamu wa rais aliyekuwa amefutwa kazi wiki iliyotangulia na kutorokea nje ya nchi, akarejea na kuchukua usukani na kuapishwa Ijumaa baada ya Bw Mugabe kushurutishwa kujiuzulu.

Ulinzi waimarishwa Nairobi Kenyatta akitarajiwa kuapishwa Jumanne

Wafuasi wa upinzani wamekuwa wakikabiliana na polisi mara kwa mara tangu AgostiHaki miliki ya pichaAFP/GETTY
Image captionWafuasi wa upinzani wamekuwa wakikabiliana na polisi mara kwa mara tangu Agosti
Ulinzi umeimarishwa katika jiji kuu la Kenya, Nairobi pamoja na miji mingine mikuu Rais Uhuru Kenyatta akitarajiwa kuapishwa kuongoza nchi hiyo kwa muhula mwingine hapo kesho.
Muungano wa upinzani umetangaza kwamba hautambui sherehe hiyo na haumtambui Bw Kenyatta kama rais aliyechaguliwa na wananchi.
Kiongozi mkuu wa upinzani Raila Odinga amepanga kuandaa mkutano mkubwa wa kuwakumbuka watu waliofariki wakati wa makabiliano kati ya wafuasi wa upinzani na polisi.
Bw Odinga na muungano wake wa National Super Alliance (Nasa) wamesisitiza kwamba mkutano huo utafanyika katika uwanja wa Jacarada, Nairobi, takriban kilomita kumi hivi kutoka uwanja wa Kasarani ambapo sherehe ya kuapishwa kwa Bw Kenyatta itakuwa inaendelea.
Polisi hata hivyo wamesisitiza kwamba hakutakuwa na mkutano mwingine Nairobi ila sherehe ya kumuapisha Bw Kenyatta.
Bw Odinga alisusia uchaguzi wa marudio uliofanyika 26 Oktoba baada ya kufutiliwa mbali kwa uchaguzi wa kwanza uliokuwa umefanyika tarehe 8 Agosti.
Mahakama ya Juu ilifutilia mbali uchaguzi huo wa kwanza kutokana na kesi iliyokuwa imewasilishwa na Bw Odinga.
Bw Kenyatta alipata asilimia 98 ya kura katika uchaguzi wa marudio, ushindi ambao uliidhinishwa na Mahakama ya Juu iliyofutilia mbali kesi mbili zilizokuwa zimewasilishwa na wanaharakati wawili na mbunge wa zamani kupinga uchaguzi huo.
Serikali imesema viongozi 20 wa mataifa mbalimbali wanatarajiwa kuhudhuria sherehe hiyo ya kuapishwa kwa Bw Kenyatta, akiwemo kiongozi wan chi jirani ya Tanzania Dkt John Magufuli.
Mwezi uliopita, ripoti ya Tume ya Taifa ya Haki za Binadamu ilisema watu 37 waliuawa tangu kutokea kwa uchaguzi wa tarehe 8 Agosti.
Tume hiyo iliwatuhumu polisi kwa kutumia nguvu kupita kiasi wakikabiliana na wafuasi wa upinzani.
Idara za usalama nchini Kenya zimekanusha tuhuma hizo.

Baiskeli zinavyosaidia wananchi kukabiliana na uhaba wa maji Mwanga


Kutokana na uhaba wa upati-kanaji wa majisafi na salama katika Wilaya ya Mwanga mkoani Kilimanjaro, wananchi wanalazimika kutumia usafiri wa baiskeli kwenda maeneo ya mbali kutafuta huduma hiyo. Asilimia kubwa ya wananchi wa vijiji vya Mwanga hata katika baadhi ya maeneo ya mjini hutu-mia baiskeli kama usafiri wa kubeba maji kutoka eneo moja kwenda lingine.
Katika maeneo yaliyoendeleana yenye maji ya kutosha ni nad-ra kuona mtu amebeba maji kwa baiskeli, lakini wilayani hapa ni jambo la kawaida kwa sasa.Jambo hili huchangiwa na uhaba wa maji katika baadhi ya maeneo, hivyo baiskeli kubakia kuwa ndio usafiri unaotegemewa kuwasaidia wananchi hasa wan-awake wilayani humo.
Kiwango cha maendeleo ya jamii yoyote kinategemea kuwe-po kwa maji ya kutosha yaliyo safi na salama. Maji ni mojawapo ya huduma muhimu katika kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Mwaka 2025. Licha ya malengo hayo kusema kila mwananchi anapaswa kutembea umbali wa mita 400 tu ndipo apate majisafi na salama, kwa Wilaya ya Mwanga jambo hilo bado ni kutendawili. Inaendelea uk 24
Ukosefu wa maji katika wilaya hii umekuwa ni tatizo sugu na linalowapa mateso wakazi wa wilaya hiyo.
Tatizo hili limekuwa likiwatesa zaidi akina mama na watoto ambao huwa wakiamka usiku wa manane kwenda kusaka maji kwenye maeneo yanakopatikana.
Licha ya kuwepo kwa miradi mbalimbali ya Serikali na ile iliyojengwa na taasisi mbalimbali za kiraia, bado tatizo hili limekuwa ni kitendawili kisichokuwa na majibu.
Namna baiskeli zinavyotumika
Sikushangaa kuona baiskeli zikitumika kubebea maji, bali nilishangaa kuwa katika nchi inayoelekea kuwa ya viwanda bado wapo watu wengi wanaohangaika kubeba maji kwa kutumia baiskeli kutokana na uhaba mkubwa wa huduma hiyo.
Juma Amini mkazi wa Kata ya Jipe, anasema kuwa usafiri wa baiskeli umekuwa msaada mkubwa kwao kupata maji kwa ajili ya matumizi ya nyumbani.
Amini anasema takribani kila nyumba ina baiskeli ya kubebea maji. Anatahadhalisha kuwa tatizo hilo si la kupuuzwa na Serikali kwakuwa linahatarisha maisha ya watoto na wanawake ambao mara nyingi wao ndio wanategemewa kusaka maji.
Watoto wa kike nao wanatumia usafiri huo kwa kubeba madumu matatu hadi manne ya maji hali ambayo inaweza kuhatarisha usalama wa afya zao.
Mkazi wa Kijiji cha Kivisini Kata ya Kivisini, Amina Ally anasema wanawake na watoto wanachangamoto nyingine ya kusubiri maji kwenye foleni kwa muda mrefu.
Anasema baada ya kuyapata huduma hiyo hutumia baiskeli au mkokoteni ili kubeba madumu mengi ya maji kwa wakati mmoja.
Amini anaeleza kuwa matumizi ya baiskeli yanawasaidia wananchi kuokoa muda na kupata maji mengi kwa wakati mmoja.
Anasema wanatoka nyumbani saa 11 alfajiri kwaajili ya kuwahi foleni ya maji.
“Kama unavyoona foleni ya maji haya ni ya mvua yanatiririka kutoka mlimani, wakati wakiangazi tunachota maji kijiji kingine hivyo mtu hawezi kuchota ndoo moja akarudi inambidi aje na baiskeli au mkokoteni,”anasema Amini.
Haruna Msofe, anasema bila kutumia usafiri wa baiskeli wanaume wengi hawawezi kubeba maji kichwani hasa wanapoyafuata maji maeneo ya mbali.
Msofe anasema, baiskeli na mikokoteni hutumika zaidi kipindi cha kiangazi wakati ambao uhaba wa maji huwa mkubwa zaidi.
Anaongeza kuwa wakati wa msimu wa kiangazi ndio matumizi ya baiskeli huongezeka mara dufu kwakuwa maji hupatikana mbali zaidi katika maeneo ambayo kuna kisima.
Kwa upande wake Hawa Amani anasema licha ya kuyafikia maji hayo, wanachota ndoo sita kila mtu kwa siku kutokana na uchache wa maji.
Hata hivyo, matumizi haya yanatumiwa na wahudumu wa Serikali kwakuwa alionekana mhudumu wa afya katika zahanati ya Kivisini akiwa katika foleni ya kuchota maji.
Mhudumu huyo ambaye alikataa kutaja jina lake, alipoulizwa alisema kuwa wanalazimika kutumia mikokoteni kubebea maji ya kufanyia usafi pamoja na shughuli nyingine katika zahanati hiyo.
“Nafanya kazi Zahanati ya Kivisini, nimelazimika kuja hapa kuchota maji kwaajili ya zahanati, natumia mkokoteni kila siku kuja kubebea maji ili yatoshe,” anasema mhudumu huyo.
Katika Kijiji cha Jipe, Kata ya Jipe ambako wanatumia maji ya ziwa, wakihitaji maji kwaajili ya kunywa wanayapata mbali kwa kuyanunua ni lazima waende na usafiri huo.
Wakati nikielekea Kijiji cha Jipe wananchi wamebeba ndoo za maji kwa kutumia baiskeli, mikokoteni na wengine vichwani.
Mwenyekiti wa Kijiji cha Jipe, Abdalah Hatibu anaeleza shida wanayoipata wananchi wa kijiji hicho ikiwa ni pamoja na hatari ya kukumbwa na magonjwa kutokana na matumizi ya maji ya Ziwa Jipe.
Hatibu anasema kutokana na ukosefu wa majisafi na salama katika eneo hilo, usafiri huo hutumika kufuata maji walau ya kupooza kiu tu.
Anasema: “Katika ziwa hilo, mifugo wanakunywa maji hapo, wavuvi nao wanafanya kila aina ya uchafu huko ziwani halafu hapo hapo tunachota maji tunakunywa na kupikia.”
Hatibu anasema kuwa wakitaka kupata maji mazuri ya kunywa wanalazimika kwenda kununua katika kijiji kingine kwa Sh500 kwa ndoo moja.
“Kwa mtu ambaye ana uwezo mdogo ndiye anaweza kwenda na baiskeli kununua maji hayo walau ya kunywa,” anasema Hatibu.
Watumia Punda
Katika Kijiji cha Pangaro, Kiverenge na mgagao Kata ya Mgagao wanawake wa kabila la Wamasai nao wanakabiliana na adha hii ya maji hivyo hutumia usafiri wa punda.
Pamoja na kwamba wao hutumia maji yaliyo kwenye malambo, lakini lazima usafiri wa punda uwepo.
Wanawake na watoto ndio wahusika wakuu na wanateseka zaidi wanalazimika kutumia maji ya lambo kwa matumizi ya nyumbani.
Agnes Moleli, anasema licha ya maji hayo kuwa mabaya lakini yamekuwa mkombozi kwao na usafiri wa punda unawasaidia kwakuwa bwawa hilo lipo mbali kidogo.
“Hatuna njia nyingine ya kupata majisafi na salama hivyo lazima tutumie haya, tunakuja hapa na punda halafu tunaingia nao kwenye bwawa tunajaza madumu ya maji kisha tunaondoka,” anasema Mollel.
Anasema kuwa kipo kijiji cha jirani ambacho kuna maji ya kisima lakini hata kwa usafiri huo ni mbali zaidi.
Akizungumza kijijini hapo, diwani wa Kata ya Mgagao, Longoviro Kipuyo anasema kuna kisima kimoja ambacho kipo Pangaro lakini kipo mbali na Kijiji cha Kiverenge.
Anaiomba Serikali kuwasaidia kutafuta mashine na mabomba kwaajili ya kusambaza maji katika vijiji hivyo, kwakuwa kipo kisima ambacho kimechimbwa, lakini hakitoi maji kutokanana ukosefu wa vifaa hivyo.
Kauli ya Mkuu wa Wilaya
Mkuu wa Wilaya ya Mwanga, Aron Mbogho anasema kuna mradi mkubwa wa maji unaoendelea kwa sasa, unaofadhiliwa na Serikali kwa asilimia 50.18 na asilimia 49.82 ni kutoka Benki ya Kiarabu kwa Maendeleo ya Afrika (Badea) na Shirika la Opec Fund For International Development (OFID).
Anasema, mradi huo utakapokamilika unatarajia kuwahudumia wananchi zaidi ya laki nne wa vijijini 24 vya tambarare wilaya za Same na Mwanga na vitano katika Wilaya ya Korogwe.

Kilio kingine chatumwa kwa Rais Magufuli


Kituo cha Kuendeleza Kilimo Ukanda wa Nyanda ya Juu Kusini mwa Tanzania (Sagcot), kimewasilisha kilio kwa Rais John Magufuli kikimuomba atoe msukumo kwa miundombinu katika ushoroba kinaousimamia.
Naibu ofisa mtendaji mkuu wa Sagcot, Jennifer Baarn alisema iwapo Rais atauangalia ushoroba huo utasaidia kufikia Tanzania ya viwanda.
Jennifer ambaye anamaliza muda wake katika nafasi hiyo alisema kuwa kitu pekee atakachokikumbuka kwa miaka sita aliyokaa Tanzania ni kufanya kazi na watu wanaopenda kujifunza na kuifikisha nchi juu kiuchumi.
“Namuomba Rais Magufuli kusaidia shughuli za Sagcot katika ushoroba wa Nyanda za Juu Kusini mwa Tanzania na hasa katika masuala ya miundombinu na shughuli za kongani. Vilevile asaidie watendaji wa Serikali ambao tunashirikiana nao katika kuinua kilimo nchini,” alisema Baarn.
“Nitakumbuka vitu viwili, kwanza kufanya kazi, tena kufanya kazi na watu wanaosoma kwa bidii ili kusaidia maendeleo ya nchi yao katika nyanja mbalimbali. Kingine nitakachokikumbuka ni Bagamoyo, naupenda mji ule mkongwe ambao ulikuwa kama nyumbani.”
Mbali ya mafanikio aliyoyapata kwa miaka sita aliyokuwa kwenye kituo hicho kinachofanya kazi kwa ubia kati ya sekta binafsi na ile ya umma, Baarn alisema zipo changamoto kadhaa za kiutendaji ambazo zikipatiwa ufumbuzi Tanzania itakuwa sehemu salama kwa chakula.
Alisema, hakuna uwiano katika utendaji wa kazi hasa zinazowagusa wakulima wadogo na mambo mengi wanayotwishwa kwa wakati mmoja hadi wanachanganyikiwa na kushindwa kufuata lipi kwa wakati gani.
Mkazi wa Tukuyu mkoani Mbeya, Mwasele Kalipingu alisema uzalishaji katika sekta ya kilimo unakwazwa na pembejeo ambazo huwa hawazipokei kwa wakati na wakati mwingine hazitoshelezi.
“Ukanda huu wa Nyanda za Juu Kusini pia una maeneo mengi ambayo kupitika nyakati za mvua hususan vijijini ni shinda,” alisema.

Yatima ajinyonga baada ya kufeli mitihani IMTU


Dar es Salaam. Mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Udaktari cha Imtu, Daniel Mabisi (28) anadaiwa kujinyonga kutokana na kufeli mitihani.
Mabisi ambaye ni mkazi wa mtaa wa Mgeninani, Kata ya Kijichi wilayani anadaiwa kukutwa amejinyonga jana saa saba mchana maeneo ya Mgeninani.
Taarifa zilizopatikana zinadai siku mbili kabla ya kujinyonga, mwanafunzi huyo alionekana mtaani hapo baada ya kutoka chuo alikokuwa akisoma.
Inaelezwa kuwa mwanafunzi huyo amefeli mara mbili mfululizo.
Akizungumza kwa simu kutoka Morogoro, baba mdogo wa marehemu, Joseph Lukuba alisema amepokea kwa mshtuko taarifa za mtoto wake.
“Nimepigiwa simu mchana huu nikaambiwa Daniel amejinyonga, nimeshtuka kwa sababu ni juzi tu tulimtumia nauli ili arudi nyumbani Mwanza baada ya kupata taarifa kuwa amefeli kwa mara nyingine,” alisema Lukuba.
Alisema uamuzi aliouchukua unasikitisha kwa kuwa kufeli, isingekuwa sababu ya kushindwa maisha hadi kufikia uamuzi wa kujinyonga.
“Kama familia tumehama na tuko mbali kikazi, tumemuomba jirani asimamie suala hili wakati taratibu za mazishi au kusafirisha mwili zikiendelea,” alisema.
Akizungumzia tukio hilo, mwenyekiti wa Mtaa wa Mgeninani, Khuruka Mwinyimvua alisema baada ya kupata taarifa hizo alifika eneo la tukio na kukuta mwili ukiwa umening’inia juu ya mwembe.
“Kijana huyo alionekana tangu juzi akizunguka mtaani hapa baada kurejea kutoka chuoni anakosoma, alionekana kama mtu asiyekuwa na furaha,” alisema Mwinyimvua na kuongeza: “Hadi sasa mwili umechukuliwa na polisi kwa taratibu nyingine.”
Naye kamanda wa polisi Mkoa wa Temeke, Emmanuel Lukula alithibitisha kupokea taarifa za kujinyonga kwa kijana huyo na kuwaagiza askari walio karibu na maeneo hayo kuchukua mwili huo.

Buzwagi waanza kuaga wananchi


Mgodi wa Acacia Buzwagi uliopo mjini Kahama umeanza maandalizi ya kufungwa kwa kuwaaga wananchi ambao waliguswa na miradi yake, huku ikiwapa elimu ya kufanya shughuli za kujitegemea bila uwapo wake.
Buzwagi ambao umedumu takriban kwa miaka 10, ulikuwa tegemeo kubwa kwa mapato ya halmashauri ya mji wa Kahama.
Meneja wa mgodi huo, Stewart Hamilton aliliambia gazeti hili mwishoni mwa wiki iliyopita kuwa ufungaji wa mgodi huo ni kawaida na hauna uhusiano na tatizo la uzuiaji usafirishaji makinikia nje ya nchi. Alisema wanafunga na kuondoka baada ya dhahabu kuisha, hivyo hawawezi kuendelea kuchimba kwa hasara.
Hata hivyo, Hamilton alisema maandalizi ya kufunga yameanza na ifikapo mwaka 2020 watakuwa hawapo, hivyo kutokana na wananchi wengi kwa miaka 10 kuishi kwa kutegemea uchumi kutoka ndani ya mgodi huo, watapitia kila mradi wakiwafundisha kuishi bila utegemezi wa mishahara.
Katika kuwajengea uwezo wananchi hao, alisema tayari wameweka maktaba katika mji wa Kagongwa kwenye halmashauri ya mji wa Kahama ambayo itakuwa na vitabu mbalimbali na machapisho yanayofundisha mbinu za ujasiriamali. “Katika maktaba hiyo ambayo tumeiweka kwa kushirikiana na Shirika la Read International, wananchi watapa fursa za kusoma bure vitabu hivyo,” alisema.
Wakati mgodi huo unafunguliwa ulikuwa na wafanyakazi 860, hali iliyosababisha kustawi kwa uchumi wa Kahama.
Naye mkurugenzi wa Read International, Magdalena George alisema kuna vitabu vinavyofundisha kilimo, ufugaji, ujasiriamali na shughuli mbalimbali za uchumi.
Akizungumzia hatua hiyo, kaimu mkurugenzi wa halmashauri ya mji wa Kahama, Mary Chima alisema ofisi yake itahakikisha inasimamia vizuri maktaba hiyo ili ilete matokeo mazuri kwa jamii.

PITIA VICHWA VYA HABARI KATIKA MAGAZETI YA LEO NOVEMBA 27,2017