Monday, December 4

UTARATIBU UNAOSTAHILI KUFUATWA KABLA YA KUFUTIWA UMILIKI WA ARDHI.

Image result for HATI MILIKI
NA  BASHIR  YAKUB -

Yafaa  kujua  utaratibu unaotakiwa  kufuatwa  kabla  ya kufutiwa  hati miliki  ya  ardhi (nyumba/kiwanja).  Unapojua utaratibu  huu  ndipo  unapojua kama  ulionewa  au  hapana. Na kuonewa ni  pamoja na  kukiuka utaratibu.  Na  kukiuka  taratibu yoyote  ya  kisheria kunabatilisha  mchakato wa  kufutwa  kwa  hati yako na  kutakiwa  kurudishiwa  eneo  lako  au  fidia.

Makala  yaliyopita  tulieleza mambo  ambayo  ukifanya  unahesabika  kukiuka  masharti  ya  umiliki wa  ardhi   na ni hapo  unapoweza   kufutiwa  umiliki. Leo  tuangalie  utaratibu  wa  kufuta umiliki  ikiwa imethibitika  kuwa   tayari  umekiuka  masharti  hayo. Sheria  namba 4 ya 1999 , Sheria  Ya  ardhi  imeeleza  utaratibu  wa  kufuta  umiliki  wa  ardhi.

 UTARATIBU.

1.Ni  lazima  uwe umekiuka  masharti  au  moja  ya  masharti uliyopewa  wakati unakabidhiwa  ardhi/hati kwa  mujibu  wa  kifungu  cha 48 ( 1) cha  Sheria  ya  ardhi. Usikubali  kufutiwa  umiliki  ikiwa  hujakiuka  sharti/masharti ya umiliki uliyopewa,  labda   iwe  vinginevyo.

2.   Baada  ya  kuwa  umekiuka  masharti  yafaa  upewe  taarifa  maalum( notice) kwa  mujibu  wa  kifungu 48(2). Ni  taarifa inayoeleza  masharti  ya  umiliki  uliyokiuka  na  onyo  la  kufutiwa  umiliki.  Taarifa  hiyo  ni  ya  siku  90(miezi  mitatu).  Taarifa  hiyo utapewa wewe  mmiliki  na  kila  mwenye  maslahi  katika  ardhi  hiyo  mf, mpangaji, mrehani nk.

3.   Baada  ya  siku 90  kuisha na  pengine  hujajirekebisha  au  kufanya  kile  ulichoambiwa  kufanya  basi  kamishna  wa  ardhi  atatakiwa  kupeleka  pendekezo  kwa  rais  ili  kufutiwa umiliki. Ni  rais  tu  mwenye  mamlaka  ya  kufuta  umiliki  wa  ardhi. 

Zingatia, barua  au  nyaraka  nyingine yoyote  ambayo inasema  umefutiwa  umiliki  lakini  aliyefuta  sio  rais  wa  nchi,  sio  halali.

4.  Ikiwa rais  atakubali  kukufutia  umiliki  wa  ardhi basi  inatakiwa kufutwa  huko  kutangazwe  katika  gazeti  maalum  la  serikali/taarifa ya  serikali(GN)  na  katika  gazeti  la  kawaida(newspaper)  ambalo  linafika  eneo  ardhi  yako  ilipo.  Hii  ni  kwa  mujibu  wa  kifungu  cha 49(1).  Ili  utaratibu  uhesabike  umefuatwa  ni  lazima  matangazo  haya  yatolewe  la  sivyo  kufutiwa  huko  kunabatilika.

5.  Rais  atakapofuta  umiliki  wa  ardhi basi  ardhi  hiyo  itahama  kutoka  kwa  mmiliki  wa  awali  kwenda  serikalini  au  vinginevyo itakavyoamriwa kwa  mujibu  wa  kifungu cha 49(2).  

6. Ikiwa  kuna  maendelezo  yoyote  ya  kudumu  ambayo  ulifanya  kwenye  hiyo  ardhi  basi   ni  lazima  ulipwe  fidia  ya  maendelezo  hayo  kwa  mujibu  wa  kifungu  cha  49(3). 

Isipokuwa maendelezo  hayo  yawe  yalikuwa  ni sehemu  ya  masharti  ya  umiliki  wa  ardhi  hiyo.  Yasiwe  nje  ya  yale  uliyokuwa  umepewa kwenye umiliki.

7. Ikiwa   ardhi  hiyo  ilikuwa  inadaiwa  kodi au tozo  za ardhi basi  kodi  na  tozo  hizo  zinaondolewa  na  deni  hilo  linakufa, mpaka  isemwe  vinginevyo.  Hii  ni  kwa  mujibu  wa  kifungu cha 49(2)(e)..

NAMNA  YA  KUDAI  HAKI  YAKO  IKIWA  TARATIBU  ZIMEKIUKWA.

Kwanza, waweza  kupeleka  malalamiko  yako  kwa  kamishna  wa  ardhi    na  baadae  kwa  rais. Utaandika  barua  ikieleza kile  ambacho  unahisi  kuonewa au  taratibu  kukiukwa.

Pili, ni  kupeleka  malalamiko  yako  mahakamani. Hapo  sio barua  bali utapeleka  nyaraka  maalum  za  kufungulia  shauri(Plaint/Application). Humo  pia  utaeleza  pahala  unapohisi  kuonewa au  taratibu  kukiukwa pia.
Pia  unaqweza  kuchukua  hatua  hizi  kwa  pmoja na  kwas  wakati moja.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI   KILA   JUMANNE.  0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com

IDARA KUU YA MAENDELEO YA JAMII YAENDESHA MAFUNZO YA MFUMO WA UDHIBITI WA VIASHIRIA HATARISHI MAHALA PA KAZI

Kaimu Katibu Mkuu wa Idara Kuu ya Maendeleo ya jamii, Jinsia Wazee na Watoto Bw. Maercel Katemba akifungua Mafunzo ya Mfumo wa Udhibiti wa Viashiria Hatarishi Mahala pa Kazi kwa watumishi wa Idara Kuu Maendeleo ya Jamii yanayofanyika katika katika Ukumbi wa VETA mkoani Dodoma, tarehe 4 Desemba, 2017.
Mkurugenzi wa Kitengo cha Ukaguzi wa Ndani Bibi Mchome akitoa neno la utangulizi kwa washiriki wa Mafunzo ya Mfumo wa Udhibiti wa Viashiria Hatarishi Mahala pa kazi yanayoendelea ukumbi wa VETA mkoani Dodoma.
Mwezeshaji wa Mafunzo ya Mfumo wa Udhibiti wa Viashiria Hatarishi Bw. Dickson Rusage akielezea mwitikio chanya uliooneshwa na Wizara/ Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto katika kutekeleza Mfumo huo miongoni mwa Wizara zilizoanza utekelezaji wake.
Mtoa mada Bw. Moris Jackson akiwasilisha mada ya lengo, faida na Kanuni za Usimamizi wa Viashiria vya Vihatarishi mahala pa kazi katika semina ya wakururugenzi na watumishi wa Wiraza ya Afya na Mendeleo ya Jamii, inayofanyika, mjini Dodoma.
Mtoa Mada Bw. Godfrey Magese akiwasilisha mada kuhusu visababishi vya Viashiria vya Vihatarishi mahala pa kazi katika semina ya wakururugenzi na watumishi wa Wiraza ya Afya na Mendeleo ya Jamii, inayofanyika, mjini Dodoma.
Baadhi ya washiriki wa mafunzo ya Mfumo wa udhibiti wa viashiria hatarishi kutoka Idara kuu ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee, na Watoto wakifuatilia kwa makini mafunzo mfumo huo ili kuzuia ipasavyo vihatarishi mahala pa kazi. Picha na Kitengo cha Mawasiliano WAMJW.

Na Kitengo cha Mawasiliano WAMJW

Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto (Idara kuu ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto) imeendesha mafunzo kuhusu Mfumo wa Udhibiti wa Viashiria Hatarishi Mahala pa Kazi yanayofanyika Ukumbi wa VETA mkoani Dodoma.

Mafunzo haya ya siku nne yanajumuisha wakuu wa Idara, wakuu wa vitengo, wakurugenzi wasaidi na wasimamizi wa udhibiti wa vihatarishi katika sehemu ya kazi.

Akifungua mafunzo hayo Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Afya na Maendeleo ya Jamii- Idara kuu ya Maendeleo ya Jamii Bw. Marcel Katemba amesema kuwa suala la udhibiti wa viashiria hatarishi linatokana na matakwa ya Sheria ya Fedha za Umma ya mwaka 2001 (2010) na Waraka wa Hazina namba 12 wa 2012/2013 unaoitaka kila Taasisi ya Umma kuzingatia uandaaji na utekelezaji wa Mfumo wa Menejimenti ya Viashiria vya Vihatarishi mahala pa kazi.

“Mafunzo haya ni nyenzo ya utumishi wa umma katika kudhibiti wa mifumo ya ndani ya Taasisi na hivyo kuleta ufanisi katika shughuli na utendaji wa kazi za kila siku na kuwezesha upatikanaji wa taarifa za kiutendaji na za fedha zenye  kuaminika” alisema Bw. Katemba.

Kaimu Katibu Mkuu Bw. Marcel Katemba amewakumbusha washiriki kuwa, mafunzo hayo ni mwendelezo wa yale yaliyofanyika mwezi Julai, 2016, hivyo ni jukumu la pamoja kati ya  Menejimenti na watumishi wote wa Idara kuu ya Mendeleo ya Jamii kwa ujumla wao kusimamia kikamilifu Viashiria Hatarishi katika Idara na Vitengo husika.

Ameongeza kuwa muendelezo huo utawaongezea uwezo watendaji, kuwa na uelewa wa pamoja wa kutosha kuhusu viashiria vilivyo katika maeneo ya kazi.

Akitoa  mada katika mafunzo hayo, Mratibu Bw. Dickson Rusage amesema kuwa Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto ni miongoni mwa Wizara  tano (5) kati ya Wizara 21 za Serikali ambazo  zimeweza kuanzisha mfumo wa udhibiti wa viashiria hatarishi mahala pa kazi na kuutekeleza.

Ameongeza kuwa  Idara kuu ya Mendeleo ya Jamii imepiga hatua zaidi kwa kuwatumia wataalam wake wa ndani katika kutoa mafunzo ya uelewa na kusimamia udhibiti wa vihatarishi.

Bw. Rusage amebainisha kuwa changamoto zilizopo katika kuendesha mfumo huo ni pamoja na ukosefu wa rasilimali fedha, mfumo kutopewa kipaumbele, kutokuwepo dhamira ya dhati katika matumizi ya mfumo, kutozingatia mfumo katika kufikia malengo ya Wizara, Idara, na Taasisi husika.

Kwa upande wake Mwezeshaji katika  Mafunzo hayo Bw. Moris Jackson amesema  kuwa manufaa ya mfumo wa udhibiti wa viashiria mahala pa kazi ni kuwa Wizara inayokuwa na mfumo huu, wabia wa maendeleo wataiamini Taasisi kwamba rasilimali zinazotolewa zitakuwa salama maana viashiria vinafahamika na vimewekewa mifumo ya ufuatiliaji na udhibiti kwa manufaa mapema.   

Mada zitakazowasilishwa katika mafunzo hayo ni pamoja na Maana na makundi, Faida na Kanuni za Usimamizi wa Viashiria vya Vihatarishi, Matakwa ya kisheria kuhusu Usimamizi wa Vihatarishi nchini, Muundo na maeneo muhimu ya kimwongozo, Mgawanyo wa majukumu katika Usimamizi wa Vihatarishi na nyaraka mbalimbali zitakazotumika wakati wa kuandaa na kusimamia Vihatarishi.

Mategemeo ya mafunzo hayo ya mahala pa kazi yanalenga washiriki kuweza kubaini vihatarishi ambavyo viliwekwa mwaka jana na sasa havitakiwi kuwepo tena, kubaini vihatarishi vipya ambavyo ama vilisahaulika au vitaibuliwa sasa kutokana na shughuli na kazi za Idara na Vitengo hasa baada ya mwaka kuisha na kupata maoni na ushirikiano wa kutosha ili kwa pamoja kufikia malengo yaliyokusudiwa katika kudhibiti viahatarisi kazini.

KABURI LAFUKULIWA MOSHI KUONDOA UTATA WA MWILI WA MTU ALIYEZIKWA BAADA YA KUOKOTWA MTONI

 UTATA umeighubika familia ya Jackson Makundi ambayo kijana wake aliyetambulika kwa jina la Humphrey Makundi,Mwanafunzi wa shule ya Sekondari ya Scolastica iliyopo mji mdogo wa Himo kupotea katika mazingira tatanishi.
 Utata wa kupotea kwa mwanafunzi huyo unatiliwa shaka zaidi na familia hiyo baada ya kufukuliwa kwa kaburi ulimozikwa mwili uliookotwa mto Ghona mita 300 ,jirani na shule hiyo ukidaiwa kushabihiana na wa mwanafunzi huyo.
  Humphrey Makundi, mwanafunzi wa kidato cha pili katika shule ya sekondari ya Scolastica anatajwa kupotea tangu Novemba 7 mwaka huu akiwa shuleni hapo huku wanafunzi wenzake wakiendelea na mitihani ya kidato cha Pili ya upimaji ya kitaifa .

 Familia ya kijana huyo yenye makazi yake mkoani Dodoma ikalazimika kutumia mitandao ya kijamii kutoa taarifa za kupotea kwake ikidai mazingira ya kutoweka kwake ni ya kutatanisha na baadae kuwasilisha taarifa katika kituo cha Polisi cha Himo .

Kutokana na kuwepo kwa taarifa za kuokotwa kwa mwili huo ,familia iliwasilisha maombi katika mahakama ya Hakimu Mkazi, Moshi na mahakama ikaamuru kufukuliwa kwa Kaburi hilo zoezi lililoanza majira ya saa 8:30 mchana na kudumu kwa zaidi ya saa moja.
Jeshi la Polisi liliongoza zoezi hilo katika makaburi ya Karanga huku likishuhudiwa na ndugu wa mtoto aliyepotea ambapo baada ya mwili kutolewa kaburini hali ya simanzi ilionekana katika nyuso za baadhi ya ndugu wa Mwanafunzi huyo akiwemo baba mzazi wa kijana huyo.
Kamanda wa Polisi mkoa wa Kilimanjaro,Kamishna Msaidizi wa Polisi ,Hamis Issa akathibitisha uwepo wa tukio hilo huku akieleza kuwa tayari jeshi la Polisi linawashikilia wati 11 akiwemo mmiliki wa shule hiyo Edward Shayo huku likifanya uchunguzi wa kina kuhusu matukio hayo mawili.
Mwili uliofukuliwa katika makaburi ya Karanga upande wa marehemu wasiokuwa na ndugu ulipelekewa katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya KCMC kwa uchunguzi zaidi chini ya uangalizi wa jeshi la Polisi wakishirikiana na madaktari kutoka  KCMC.
Jeshi la Polisi likiwa limezungushia utepe eneo ambalo kuna kaburi ulimozikwa mwili ambao familia ya Mwanafunzi wa shule ya sekondari ya Scolastica iliyopo mji mdogo wa Himo aliyepotea ,Humphrey Makundi ulitilia shaka.
Kaburi ulimozikwa mwili wa mtu aliyezikwa na Manispaa ya Moshi baada ya kuokotwa Mto Ghona jirani na ilipo shule ya Sekondari .
Askari Polisi wakishirikiana na ndugu wa Mwanafunzi aliyepotea Humphrey Makundi wakifukua Kaburi ulimozikwa mwili wa mtu aliyeokotwa Mto Ghona katika wilaya ya Moshi.
Kaburi likifukuliwa.
Baba mzazi wa Mwanafunzi wa shule ya Sekondari ya Scolastica aliyepotea,Jackson Makundi (Katkati) akijadili jambo na wanandugu wakati zoezi la kufukua kaburi likiendelea.
Baba mzazi wa Mwanafunzi Humphrey ,Jackson Makundi (Mwenye suti nyeupe) akitizama mwili (haupo pichani) baada ya kaburi kufukuliwa.
Baba mzazi wa Mwanafunzi Humphrey ,Jackson Makundi (Mwenye suti nyeupe) akionekana akiwa amekaa chini baada ya kutizama mwili uliofukuliwa katika kaburi .
Askari Polisi na Wanandugu wa kijana aliyepotea wakijaribu kusaidia kumnyanyua mzazi wa Mwanafunzi huyo kutoka katika eneo lilipo kaburi lililofukuliwa .
Baba mzazi wa Mwanafunzi Humphrey ,Jackson Makundi (Mwenye suti nyeupe) akisindikizwa kutoka katika eneo la Makaburi ya Karanga katika manispaa ya Moshi.
Mwili uliofukuliwa katika makaburi hayo ukiwekwa katika gari la Polisi kwa ajili ya kwenda kuhifadhiwa katika Hosptali ya Rufaa ya KCMC.
Gari la Polisi likiwa na mwili uliofukuliwa katika Makaburi ya Karanga.

RAIS DKT MAGUFULI AKUTANA NA MWAKILISHI MKAZI WA BENKI YA DUNIA, AENDESHA BARAZA LA MAWAZIRI IKULU JIJINI DAR ES SALAAM LEO


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Joseph Magufuli akiwa na Mkurugenzi Mkazi wa Benki ya dunia nchini Bi. Bella Bird aliyekutana na kufanya naye mazungumzo Ikulu jijini Dar es salaam leo Novemba 4, 2017
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Joseph Magufuli akizungumza na  Mkurugenzi Mkazi wa Benki ya dunia nchini Bi. Bella Bird leo Ikulu jijini Dar es salaam leo Novemba 4, 2017
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Joseph Magufuli akimsindikiza Mkurugenzi Mkazi wa Benki ya dunia nchini Bi. Bella Bird aliyekutana na kufanya naye mazungumzo Ikulu jijini Dar es salaam leo Novemba 4, 2017.
w4, w5 na w6:  Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Joseph Magufuli akiendesha kikao cha Baraza la Mawari  Ikulu jijini Dar es salaam leo Novemba 4, 2017.

PICHA NA IKULU

RC: Mwanafunzi aliyeuawa alitaka kuwa rubani


Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Anna Mghwira amesema Humphrey Makundi, mwanafunzi aliyeuawa na kuzikwa katika mazingira ya kutatanisha, alitamani siku moja kuwa rubani, lakini ameondoshwa duniani kutokana na roho ya ukatili.
“Huu ni ukatili dhidi ya watoto na ni pengo kwa Taifa. Ni pengo kwa mkoa na pengo kwa Jimbo la Vunjo kutokana na mtoto huyu kuwa na ndoto kubwa kwa Taifa hili,” alisema Mghwira juzi katika ibada ya mazishi ya mtoto huyo aliyekuwa mwanafunzi wa Sekondari ya Scholastica ya mjini Himo.
“Nimepata taarifa kuwa alikuwa na ndoto ya kuwa rubani, haki itendeke na uvumilivu unahitajika zaidi hasa kipindi hiki kigumu cha kumpoteza Humphrey.”
Mwili wa mwanafunzi huyo aliyetoweka shuleni uliokotwa Mto Ghona, Novemba 10 na kuzikwa Novemba 12 na Halmashauri ya Manispaa ya Moshi, lakini ulifukuliwa kwa amri ya mahakama kwa ajili ya vipimo vya vinasaba (DNA).
Pia, mkuu huyo wa mkoa alieleza kusikitishwa na kutokuwapo mwanafunzi hata mmoja kutoka shule hiyo au mwalimu katika kuaga mwili wa Humphrey.
Alisema baadhi ya wananchi mkoani Kilimanjaro wamejawa na roho za kikatili, udhalimu na rushwa, mambo ambayo yanatakiwa kukomeshwa haraka.
Mkuu huyo wa mkoa alisema licha ya kwamba hakuna mtu aliyekamatwa, lakini ofisi yake imepata malalamiko mengi kuhusu vitendo vya rushwa vinavyoendelea mahakamani.
Mghwira aliyeongozana na kamanda wa polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Hamis Issah katiba ibada hiyo alisema Humphrey amepumzika, hivyo ni vyema wakaiachia mahakama ili haki itendeke.
Katika mahubiri kwenye ibada hiyo, mchungaji Samwel Mshana wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) alikemea vitendo vya kishirikina.
Mchungaji huyo aliiomba familia na jamii kutolipiza kisasi, badala yake wawasamehe wote na kushirikiana kupiga vita vitendo vya ukatili na ushirikina.
Alisema Mkoa wa Kilimanjaro ni miongoni mwa ile ambayo inasifika kwa amani, lakini katika miezi ya karibuni vitendo vya kikatili vimeanza kuongezeka.
Katika salamu zake kwa wananchi, mbunge wa Vunjo, James Mbatia alisema damu inayomwagika itawalaani waliohusika na kuwataka watu kuacha kujihusisha na ukatili.
Alisema sababu inayosababisha kumwaga damu kwa walio wengi ni jeuri, kiburi na kujiona wana mali jambo linalosababisha haki ya wanyonge na damu yao kupotea.
“Haki ni haki hata kama itadhulumiwa lakini ipo siku moja itapatikana. Ninawaomba viongozi wa kiroho kuendelea kuhubiri amani na upatanisho,” alisema Mbatia.
Mbunge huyo alisema damu ya Mtanzania mmoja ikimwagika humrudia Mwenyezi Mungu.
Pia, alimuomba Rais John Magufuli kuliangalia suala la umwagaji damu linalotokea katika maeneo mbalimbali nchini ili sheria ichukue mkondo wake.
Hivi karibuni mmiliki wa Sekondari ya Scolastica iliyopo mji wa Himo, Edward Shayo (63); mlinzi Hamis Chacha (28) na makamu mkuu wa shule hiyo, Laban Nabiswa (37) walifikishwa mahakamani wakituhumiwa kuhusika na kifo cha Humphrey.
Washtakiwa hao walifikishwa mbele ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Moshi na kusomewa shtaka la kuua kwa kukusudia.
Akiwasomea shtaka hilo Novemba 27, Wakili wa Serikali, Kassin Nassir alidai walitenda kosa hilo Novemba 11. Washtakiwa hawakutakiwa kujibu chochote kwa kuwa mahakama hiyo haina uwezo wa kusikiliza kesi za mauaji.
Baada ya kusomewa shtaka hilo walipelekwa rumande na kesi dhidi yao itatajwa Desemba 8.

BASHE ATEMBELEA GEREZA LA WILAYA YA NZEGA,ABAINI MSONGAMANO MKUBWA WA WAFUNGWA,AJITOLEA KUWALIPIA FAINI WOTE WALIOFUNGWA KWA MAKOSA MADOGO

 Mbunge wa Nzega Mjini, Mhe. Hussein Bashe amepata wasaa wa kutembelea gereza la Wilaya ya Nzega, ambapo ameongea na Mkuu wa Magereza Bw. Anatory Kyuza  na baadae kujionea msongamano mkubwa wa wafungwa katika gereza hilo.

Aidha, Mhe. Bashe amewalipia wafungwa wote waliokuwa wamefungwa kifungo cha makosa madogo hasa yale ya kushindwa kulipa Faini za kuanzia shilingi elfu Hamsini (50,000) mpaka shilingi  Laki tatu(300,000)  ili kusaidia kupunguza msongamano wa wafungwa katika gereza hilo.

Pia, Mhe. Bashe* alitembelea  shamba la magereza ambapo alikubaliana pamoja na Mkuu wa Magereza kuweka nguvu kwenye kilimo cha Muhogo ambapo Serikali imetoa mbegu bora kwa ajili ya kilimo hicho wilayani Nzega.

Gereza la Nzega limejengwa mwaka 1923 na lina uwezo wa kuhifadhi wafungwa 50 tu lakini sasa linahudumia wafungwa na mahabusu takribani 200.

Kwa upande mwingine, Ili  kuboresha makazi ya askari wa Jeshi la Magereza wilayani Nzega Mhe. Bashe  ameamua kuchangia jumla ya  mifuko ya Saruji 100 na matofali 10,000.  
  Mbunge wa Nzega Mjini, Mhe. Hussein Bashe amepata wasaa wa kutembelea gereza la Wilaya ya Nzega ambapo ameongea na Mkuu wa Magereza Bw. Anatory Kyuza  na baadae kujionea msongamano mkubwa wa wafungwa katika gereza hilo.
Mhe. Bashe pia alipata wasaa wa kutembelea  shamba la magereza ambapo alikubaliana pamoja na Mkuu wa Magereza kuweka nguvu kwenye kilimo cha Muhogo ambapo Serikali imetoa mbegu bora kwa ajili ya kilimo hicho wilayani Nzega.

Ombi la familia ya aliyepandikizwa figo kushughulikiwa


Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu amesema ombi la familia ya mgonjwa wa kwanza kupandikizwa figo katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Prisca Mwingira (30), linaweza kushughulikiwa na halina kipingamizi.
Ndugu wa mgonjwa huyo aliyefanyiwa upasuaji wa upandikizaji wa figo Novemba 21, wameiomba Serikali kumhamisha kituo cha kazi Prisca ambaye ni mwalimu wa Shule ya Sekondari Mikese iliyopo Morogoro ili apate matibabu akiwa karibu.
Akizungumza na gazeti hili, Waziri Ummy alisema suala la mgonjwa huyo kuhitaji uhamisho na mengine kuhusu ajira, uwezekano wa kusaidiwa upo, hivyo ameshauri afuate utaratibu.
“Kuhusu ombi la ajira, ninamshauri afuate utaratibu wa uhamisho wa watumishi wa umma. Sababu yake ina uzito, sina shaka kuwa maombi yake yatakubaliwa,” alisema Ummy.
Alisema anashukuru kuona upandikizaji wa figo kwa mgonjwa huyo wa kwanza nchini umekuwa na mafanikio makubwa.
“Kilichopo sasa ni kuzidi kumuombea afya njema ili aweze kuendelea na majukumu yake ya kila siku, kwa mara nyingine nawapongeza madaktari wetu wa Muhimbili,” alisema Ummy.
Akizungumzia suala hilo, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mwasu Sware alisema suala la ufuatiliaji wa ajira ya Prisca lipo chini ya Wizara ya Tamisemi kwa kuwa kurugenzi zote zipo chini ya wizara hiyo.
Naibu Waziri Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) anayeshughulikia afya, miundombinu na uwekezaji, Josephat Kandege alisema suala la Prisca ni la kipekee hivyo anaweza kusaidiwa iwapo atakuwa na vielelezo.
“Kisheria na utaratibu uliopo tunahitaji awasilishe vielelezo ambavyo ni nyaraka ambazo zinatoka Muhimbili zilizotoa maelekezo kama hayo baada ya hapo kuna utaratibu kadhaa, ikiwemo kuandika barua. Tunamthamini mfanyakazi akiwa mzima na mgonjwa,” alisema Kandege.
Alisema wakati mwingine wanapata kigugumizi kwa Dar es Salaam kwa kuwa shule nyingi walimu wamejaa, hivyo hiyo ni changamoto kwa kuwa ni lazima kuwa na namna ya kuziba pengo la anakotoka.
“Tunaweza pia kumpatia uhamisho wa muda katika kipindi ambacho yupo kwenye matibabu aweze kuwa hapa. Nafahamu wagonjwa wengi waliopandikizwa figo si lazima ahudhurie kliniki kila wiki inafikia kipindi atamwona daktari kwa mwezi na miezi, linatakiwa liangaliwe kwa uzito wake,” alisema.
Desemba Mosi, Prisca aliruhusiwa kurudi nyumbani baada ya kuwa chini ya uangalizi wa jopo la madaktari bingwa wa figo kwa siku 10. Alipatiwa figo na mdogo wake Bartholomew Mwingira (27).
Baba mdogo wa vijana hao, Einhard Mwingira aliipongeza Serikali, uongozi wa hospitali na madaktari kwa kuleta matibabu hayo ya kibingwa na familia yake kuwa ya kwanza kuneemeka, huku akiomba binti yake apewe uhamisho.
“Ombi langu kubwa mtoto wangu anakaa Morogoro, kule anafundisha Shule ya Sekondari Mikese naiomba Serikali ahamishiwe Dar es Salaam ili iwe rahisi kuendelea na matibabu kwa ukaribu hapa Muhimbili, ikiwezekana wambadilishie kazi kwani vumbi la chaki sidhani kama litakuwa zuri kwake,” alisema Mwingira.

Mahakama rufaa yamfungua mwingine kitanzi


Miaka saba tangu Mahakama Kuu ilipomhukumu adhabu ya kunyongwa mkazi wa Mabibo Upogoroni wilayani Kinondoni, Dar es Salaam, Japhary Ismail kwa kosa la kumuua binamu yake, Mahakama ya Rufani imeibatilisha na kuamuru kesi irudi Mahakama Kuu isikilizwe upya.
Uamuzi huo ulitolewa na jopo la majaji watatu wa Mahakama ya Rufani, lililoongozwa na Jaji Bernard Luanda, Augustine Mwarija na Rehema Mkuye kufuatia rufaa aliyoikata mfungwa huyo kupinga hukumu aliyopewa na Jaji Augustine Shangwa wa Mahakama Kuu.
Mahakama ya Rufani imeamuru kesi hiyo irudishwe Mahakama Kuu isikilizwe upya baada ya kujiridhisha kuwa mwenendo wa kesi hiyo wakati wa usikilizwaji ni batili, kutokana na makosa yaliyofanywa na washauri wa Mahakama kwa kufanya majukumu wasiyostahili.
Kasoro hizo zilizoifanya hukumu kubatilishwa ni kitendo cha washauri hao kumfanyia udodosaji jukumu ambalo hufanywa na wakili wa upande pinzani katika kesi.
Kasoro hiyo iliibuliwa na Wakili aliyemwakilisha mrufani, Daniel Welwel, katika sababu yake ya nyongeza kati ya sababu za rufaa alizokuwa ameziwasilisha awali.
Mahakama ya Rufani katika hukumu yake iliyosomwa na naibu msajili wa mahakama hiyo, Amir Msumi ilisema ingawa sheria haiwapi washauri wa mahakama mwanya wa kumfanyia shahidi udodosaji, lakini katika kesi hiyo jaji aliwapa mwanya wa kufanya hivyo kwa mashahidi wa pande zote.
Japhary alikamatwa Aprili 23, 2004 na kushtakiwa kwa tuhuma za kumuua binamu yake, Joseph Shedula aliyekutwa amekufa chumbani walimokuwa wamepanga huko Mabibo Upogoroni, baada ya kurejea kutoka Korogwe Tanga.

Jinsi ghorofa 10 jengo la Tanesco zitakavyobomolewa


Wakati ukumbi wa mikutano na ofisi za mapokezi za Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), vikivunjwa Wakala wa Majengo (TBA) umeeleza namna jengo la ghorofa 10 litakavyobomolewa.
Meneja wa Kikosi cha Ujenzi wa TBA, Humphrey Killo alisema jana kuwa uvunjaji wa ofisi na ukumbi ulifanyika usiku wa kuamkia juzi ikiwa ni maandalizi ya kuvunja sehemu ya jengo la ghorofa 10 lililoko eneo la Ubungo jijini Dar es Salaam ambalo liko kwenye hifadhi ya Barabara ya Morogoro.
Ubomoaji huo unafanyika pia ili kupisha utekelezaji wa mradi wa barabara za juu eneo la Ubungo ikiwa ni utekelezaji wa agizo la Rais John Magufuli.
Novemba 15, Rais Magufuli aliagiza Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads) kuweka alama za X kwenye jengo hilo katika sehemu zilizo katika hifadhi za barabara.
Akizungumzia uvunjaji wa jengo hilo, Killo alisema kwa sasa wanafanya maandalizi yakiwemo ya vifaa kama vile mitambo na malori ya kubebea vifusi. “Maandalizi haya ni pamoja na kubomoa majengo madogo kama vile ofisi za walinzi na ukumbi wa mikutano na sehemu ya mapokezi,” alisema Killo aliyekuwa akisimamia mchakato huo.
Killo alisema maandalizi yanatarajiwa kukamilika kesho na utaratibu utakaofuata ni kubomoa jengo la ghorofa akisema kazi hiyo inaweza kufanyika kwa mwezi mmoja.
Alisema kabla ya kubomolewa ghorofa hilo, jengo lote litawekwa vyuma na kuzungushiwa nyavu maalumu ili kuzuia vumbi kusambaa katika maeneo mengine ya jirani.
“Nyavu hizi zitasaidia pia kuzuia vitu au vipande vidogovidogo vitakavyokuwa vikitoka wakati wa ubomoaji,” alisema Killo.
Alisema ubomoaji ni hatari hivyo timu ya wataalamu 10 wa fani mbalimbali wakiwamo wasanifu wa majengo watapelekwa kusimamia kazi hiyo itakapoanza.
“Wataalamu wengine watakuwa ni wa fani ya uhandisi wa majengo, wakadiriaji wa majenzi na mafundi sanifu. Pia, watakuwepo maofisa usalama kwa ajili ya kuimarisha ulinzi na usalama,” alisema Killo.
Alisema jengo hilo lina sehemu tatu; ya mbele, katikati na nyuma hivyo ubomoaji utahusisha sehemu ya mbele pekee.
Novemba 27, uongozi wa Tanesco ulitoa taarifa kwa umma ukisema utekelezaji wa agizo la Rais Magufuli umeanza kuhusu kubomolewa jengo.
Kaimu Meneja Uhusiano wa Tanesco, Leila Muhaji, Novemba 28 alisema wafanyakazi wa shirika hilo wamehamia ofisi zingine za shirika hilo zilizoko jijini Dar es Salaam.