Saturday, August 1

Kada wa Vijana Chadema Dar auawa kwa risasi


Dar es Salaam. Mwenyekiti wa Vijana Chadema Tawi la Luis, Mbezi Luis, Dar es Salaam, Dennis Kasanga ameuawa kwa kupigwa risasi shingoni usiku wa kuamkia jana, huku taarifa zilizotolewa na polisi zikitofautiana na mashuhuda wa tukio hilo.
Kasanga, mkazi wa Mbezi Luis alipigwa risasi na watu wanaodaiwa kuwa majambazi waliovamia baa inayojulikana kwa jina la Mtauli iliyopo njiapanda ya Barabara ya Goba na Makabe saa saba usiku. Hata hivyo, polisi wamesema tukio hilo halihusiani na ujambazi na wala halikutokea muda huo.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kipolisi Kinondoni, Camillius Wambura alisema jana kuwa tukio hilo lilitokea saa 10 alfajiri kuamkia jana.
Alisema tukio hilo lilitokea Barabara ya Goba baada ya watu wanne waliokuwa wakisukuma gari bovu kuvamiwa na watu wengine wanne na kuibuka mzozo kati yao.
“Baada ya mzozo, ghafla mmoja aliibuka na kuanza kuwafyatulia risasi iliyowajeruhi watu wawili na kuua  mmoja aliyepigwa risasi shingoni,” alisema Kamanda Wambura.
Kamanda Wambura alisema tukio hilo halihusiani na ujambazi kama watu wanavyodai. “Siyo kila mtu anayefyatua risasi ni jambazi, subiri kwanza tunaendelea na uchunguzi wa tukio.”
Hata hivyo, mashuhuda wa tukio hilo walidai kuwa marehemu aliuawa kwa kupigwa risasi na majambazi, ambao pia waliwajeruhi watu wengine wawili akiwamo mlinzi wa baa hiyo.
Mbali na kujeruhi, watu waliokuwa na bastola, mapanga na marungu pia waliwapora simu na fedha wateja wachache waliokuwapo kwenye baa hiyo.
Kati ya waliojeruhiwa, mmoja ni mlinzi aliyepigwa rungu usoni na mwingine aitwaye Erasmo Basheja, mkazi wa eneo la Basondole aliyepigwa risasi begani.
Mhudumu mmoja wa baa hiyo aliyekataa kutaja jina lake, aliliambia gazeti hili jana kuwa watu kati ya sita au saba walifika kwenye baa hiyo saa saba usiku wakijifanya wateja waliotaka kuhudumiwa vinywaji.
Alisema wakati wakifika, baa ilishafungwa ila kulikuwa na wateja wachache nje na yeye muda huo alikuwa ndani. “Baa ilishafungwa zamani, ila kulikuwa na wateja wachache nje wakimalizia vinywaji,” alisema shuhuda huyo.
Alisema baada ya watu hao kuelezwa kuwa baa imeshafungwa, ghafla walibadilika na kuwataka watu waliokuwa hapo kulala chini na wakaanza kuwapekua mifukoni na kupora simu zao.
“Nilisikia mlio wa risasi na haraka haraka nilifunga mlango wa kuingia kaunta ya vinywaji kisha nikalala uvunguni kwenye chumba kinachotumia mlango mmoja na kaunta,” alisema shuhuda huyo.
Aliongeza: “Niliwasikia wale majambazi wakisema, ‘hawa wanawake wameshafunga geti.’ Nilikaa kimya nikiwa nimejilaza chini ya godoro.”
Alisema majambazi hao wanaijua fika baa hiyo, kwani baada ya kuwalaza watu chini walizunguka nyuma, ambako ndiko kwenye geti la kuingia kaunta na vyumba vya ndani.
Mlinzi wa baa hiyo, ambaye amejeruhiwa usoni kwa kupigwa na rungu aliiambia gazeti hili kuwa majambazi hao walifika kwenye baa hiyo saa saba usiku wakati tayari pameshafungwa.
Alisema alikuwa amekaa kaunta pamoja na marehemu na mtu mwingine ambaye hakumbuki jina lake, ndipo aliposikia mlio wa risasi na wakati akitaharuki, alivamiwa na mmoja wa watu hao na kupigwa rungu usoni huku akisema: “Usiniangalie usoni.”
“Nilidondoka chini na wakaanza kunisachi mifukoni huku wakinitaka kutoa simu na fedha, niliwajibu sina kitu na baada ya kunipiga niliamua kutoa simu na kuwapa,” alisema mlinzi huyo.
Alisema marehemu alipigwa risasi wakati akiondoka alipoketi na kwenda sehemu ambayo alisikia mlio wa risasi. “Alikuwa kaunta na baada ya mlio wa risasi alinyanyuka na kwenda sehemu ya nje ya baa huko ndiko alikopigwa risasi na kufariki dunia papo hapo,” alisema.
Kifo cha kiongozi huyo wa vijana Chadema pia kimethibitishwa na mjumbe wa Serikali ya Mtaa wa Luis, Finna Massawe.
Majirani wa eneo ilipo baa hiyo walidai kuwa baa hiyo imekuwa ikivamiwa na majambazi, mara kwa mara, na kwamba ingawa tukio la kuuawa mtu ni mara ya kwanza kutokea, lakini tayari uhalifu wa kuvamiwa baa hiyo ulishafanyika mara mbili.

CCM Zanzibar ‘wamteta’ Lowassa

Zanzibar: Chama cha Mapinduzi (CCM) visiwani hapa jana kilifanya mkutano na waandishi wa habari kwa ajili ya kutoa tamko la kurasa nane kuzungumzia msimamo wake dhidi ya uamuzi wa Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa kujivua uanachama, kikisema kuwa hakipo pamoja naye.
Lowassa, ambaye uamuzi wake wa kuhamia Chadema mapema wiki hii umeongeza ushindani katika mbio za urais, alijivua uanachama wa CCM akisema mchakato wa kumpata mgombea wa urais kwa tiketi ya chama hicho ulikiuka katiba na kanuni.
Uamuzi wa mbunge huyo wa Monduli kuhamia upinzani na kitendo cha CCM kuengua jina lake umefuatiwa na wabunge, madiwani na wanachama kadhaa kutangaza kujivua uanachama na kujiunga na vyama vya upinzani, hasa Chadema.
Uamuzi wa mbunge huyo wa Monduli kuhamia upinzani na kitendo cha CCM kuengua jina lake umefuatiwa na wabunge, madiwani na wanachama kadhaa kutangaza kujivua uanachama na kujiunga na vyama vya upinzani, hasa Chadema.
Lowassa hakuwahi kusema kuwa uamuzi wake unaungwa mkono na CCM Zanzibar.
Lakini jana, uongozi wa chama hicho mjini hapa uliitisha mkutano na waandishi wa habari kueleza kuwa hakimo katika wimbi hilo la kumfuata Lowassa kwenda upinzani.
Wakizungumza katika mkutano huo uliofanyika ofisi za makao makuu ya CCM mjini hapa na kurushwa moja kwa moja na kituo cha televisheni cha Shirika la Utangazaji Zanzibar pamoja na kituo cha TBC1 cha Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC), viongozi hao walitetea utaratibu uliotumika kuengua jina lake wakisema ulikuwa sahihi.
“Sisi kama wana-CCM na maelfu ya wanachama wengine hatukubaliani naye,” alisema katibu wa Mkoa wa Mjini, Mohammed Omar Nyawenga wakati akisoma tamko hilo katika mkutano huo uliohudhuriwa na viongozi mbalimbali wa chama cha Serikali, akiwamo Spika wa Baraza la Wawakilishi Pandu Ameir Kificho na mjumbe wa Kamati Kuu, Shamsi Vuai Nahodha.
“Wana-CCM waliomuunga mkono Lowassa hasa kutoka mikoa mitano ya Zanzibar walimuunga kwa kuamini kwamba yeye ni kiongozi ambaye amepitia katika uozefu mkubwa katika chama chake, lakini hawakumuunga mkono kwa sababu ya sura yake wala utajiri wake. Hapana.
“Bali ni kwa sababu ya siasa, sera na ilani za chama alichokiamini na kukipigania, yaani CCM hivyo kwa kuwa sasa ameamua kujitenga na CCM basi nasi tumeamua kujitenga naye na kamwe hatupo pamoja naye.”
Alisema maelfu ya wana-CCM wa Zanzibar walimuunga mkono kutokana na azma yake ya kuomba kuteuliwa na CCM kuwa mgombea wake wa kiti cha urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, lakini kutokana na kubadilika kwake wamemuachia mkono.
 Alisema CCM ni muumini wa haki za binaadamu, usawa, wa sheria hivyo kujiondoa Lowassa ni sawa na ilivyokuwa wakati wa kujiunga kwake .
“Ni suala la hiyari yake na wala hatuna ugomvi naye. Ila tunamkumbusha tu kwamba inawezekana kabisa umaarufu alionao sasa umejengwa kutokana na CCM, lakini haiwezekani kabisa kuwa maarufu wa CCM umejengwa na au umetokana na yeye. Ndio maana tunasema chama kwanza, mtu baadaye,” alisema katibu huyo.
 Nyawenga alisema CCM, yenye viongozi wenye hekima, busara, mapenzi na uadilifu mkubwa kwa wananchi, bado inaaminiwa na kukubalika miongoni mwa wananchi wengi wa Tanzania.
 Alisema wingi huo wa wanachama wake hautokani na wala haujaletwa na utajiri wa viongozi wake bali unatokana na uimara wa siasa, sera na itikadi yake.
 “Hasara ya kweli kwa CCM si kumpoteza tajiri mmoja anayetaka kubadili sera na itikadi ya CCM kwa maslahi yake binafsi na marafiki zake bali ni kuwapoteza mamilioni ya wanachama wake ambao wanachoshwa na viongozi walafi na wanafiki ndani ya CCM,” alisema.
 Alisema kwa kuzingatia ukweli huo, uamuzi wa Lowassa kujiondoa ndani ya CCM si jambo la kukishitua chama hicho, viongozi wake wala wanachama wake kwani CCM kamwe haiwezi kudhoofika wala kupasuka.
 “Hii si mara ya kwanza kwa CCM kuondokewa na kiongozi mwandamizi na kujiunga na upinzani. Mwaka 1989 CCM iliwafukuza uanachama jumla ya viongozi waandamizi 11 akiwemo waziri kiongozi wa zamani Maalim Seif Sharif Hamad akifuatiwa na Augustine Mrema ambaye alijiunga na NCCR Mageuzi,” alisema.
 Pia alisema mwaka 2014, CCM ilimfukuza mwakilishi wake na mweka hazina wa chama hicho, Mansoor Yussuf Himid na haijapoteza kitu kutokana na kitendo hicho.
“Kama mvuvi wa pweza tutakutana mwambani,” alisema.
 Aliwashangaa viongozi wa upinzani hasa vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), hususan viongozi wa Chadema kwa namna wanavyoendesha siasa alizoziita za ubabaishaji na ulaghai kwa Watanzania hata baada ya nchi kufikisha miaka 23 tangu kurejeshwa kwa siasa za ushindani.
Alisena tangu mwaka 1992, vyama vya upinzani vimeshindwa kuandaa wagombea wenye uwezo wa kuwaongoza Watanzania na kuishia kudaka mapumba yanayotoka CCM.
 “Mara nyingi tumewasikia wakijitoa kimasomaso kwa kukariri nusu nusu maneno ya Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere yanayosema ‘Watanzania wanahitaji mabadiliko na wasipoyapata ndani ya CCM, watayapata nje ya CCM’,” alisema.
“Kwa bahati mbaya sana wasia huu wa Baba wa Taifa unakaririwa nusu nusu. Naomba niwakumbushe viongozi wa Ukawa wasia huo unaendelea kutamka kwamba Rais wa Tanzania anaweza kutoka chama chochote kile lakini Rais bora wa nchi yetu atatoka CCM.”
Borafya Silima
Mwenyekiti wa CCM wa Mkoa wa Mjini, Borafya Silima ambaye alikuwa kinara wa kampeni za Lowassa na aliyewahi kutangaza kwamba anawakilisha wenyeviti wote wa mikoa mitano ya Zanzibar kumuunga mkono waziri huyo mkuu wa zamani, alisema wameachana na Lowassa kwa madai kuwa anataka madaraka zaidi.
Borafya, ambaye aliitisha mkutano huo wa jana na ambaye aliuongoza, alikiri kuwa walimpendekeza Lowassa kwa kuwa amefanya kazi nzuri katika chama, lakini wameachana naye baada ya kuona amekuwa anataka zaidi madaraka kama Maalim Seif.
 Borafya alianza kubabaika wakati akijibu maswali ya waandishi wa habari akitumia muda mwingi kujitetea na kumrushia lawama Maalim Seif Sharrif Hamad badala ya kujibu maswali.
“Kuna ishara kwamba labda huyu mtu anapenda ukubwa na madaraka kama Maalim Seif. Sisi chama chetu unatakiwa ukiambiwa nenda huku unaende, ukiambiwa fanya hivi, fanya” alisema Borafya.
“Chama chetu hakitaki mtu anayependa madaraka mkubwa kama Lowassa na kama Maalim Seif, mtu huyu anapenda madaraka makubwa sidhani kama wanachama wa CCM watamfuata Lowassa,” alisema Borafya.
 Borafya alisema alikuwa mtu wa kwanza kumuunga mkono Lowassa kwa sababu chama chake kilimteua na alifanya hivyo kwa dhati ya roho yake na mapenzi yake kwa Lowassa na ndio maana kila anapopita alimpigia debe akisema kwamba yeye ana mahaba naye.
Kuhusu tuhuma za rushwa dhidi ya Lowassa, alisema CCM haijawahi kumuhusisha mbunge huyo wa Monduli na suala hilo, bali upinzani.
Nahodha akana mizengwe
Wakati Borafya akitetea uamuzi wake wa awali wa kumpigia debe Lowassa, mjumbe wa Halmshauri Kuu wa CCM Zanzibar, Shamsi Vuai Nahodha alitumia muda mwingi kutetea utaratibu uliotumika kumpata mgombea wa urais wa chama hicho.
“Kazi ya Kamati Kuu si kuwaondoa wagombea bali ni kujadili wagombea kama walivyofanya mwaka 2005,” alisema na kutaja majina ya makada waliopitishwa mwaka huo kuwa ni Jakaya Kikwete, Salim Ahmed Salim, Frederick Sumaye, Abdallah Kigoda na Mark Mwandosya.
“Lowassa alikubaliana na utaratibu huo bila ya kuukosoa kwa kuwa ulikidhi haja na matakwa yake,” alisema Nahodha.
“Utaratibu huohuo ndio uliotumika mwaka huu wa kuwateua wagombea, lakini jambo la kushangaza ni kwamba kuna watu wanasema taratibu zimekiukwa wakati hakuna kilichobadilika.
“Utaratibu wetu sisi ni kuwajadili watu kwa sifa na mtu akiwa na sifa za msingi anateuliwa, lakini hizo hoja za kuwa mwenyekiti amekuja na majina yake mfukoni, ni hoja zisizo na msingi na ni hoja za kipuuzi.
 “Mimi inanisikitisha sana nikisikia mtu anasema taratibu zimekiukwa kwa sababu tu matakwa yake hayajatimizwa. Mimi kama mtu wa kulalamika, basi angesema Dk (Mohamed Gharib) Bilal kwa sababu yeye ni mtu wa pili baada ya Rais, lakini hatujamsikia kulalamika wala kusema lolote.”
Alisema CCM imefuata utaratibu uliopo ingawa wapo wanachama ambao wanataka utaratibu unaotumika hivi sasa ubadilike kulingana na wakati uliopo, lakini akasema hayo yatajadiliwa kwa wakati wake.
Nahodha alisema wapinzani waliomkumbatia Lowassa ndio waliokuwa wakimtuhumu Lowassa kwa kula rushwa na si kiongozi yeyote wa chama cha CCM wala si serikali.
 Alisema kwamba tatizo kubwa kwamba watu hawataki kukosolewa wala kuelezwa ukweli hivyo kama kuna watu wanaamini
 “Yule ambaye alimfuata Lowassa leo hayupo CCM na hatarudi tena, lakini yule ambaye alimfuata Lowassa kwa sababu aliamini huyu ni kada wa CCM na kila anachokifanya anafanya kwa CCM, basi CCM ipo na itadumu milele,” alisema Nahodha huku akishangiliwa.
Nahodha alisema sifa za mgombea wa urais wa CCM zinaeleweka na kwamba Dk John Pombe Magufuli aliyeteuliwa kupeperusha bendera ya chama hicho ana sifa zote.
Ramadhan Abdallah Shaaban
Waziri wa Maji Nishati na Ardhi, Ramadhan Abdallah Shaaban alisema katika kumteua mgombea kunafuatwa sheria na kanuni na kumtafuta mgombea kunatakiwa kumteua mtu asiye na shaka, lakini Lowassa alikuwa ametiliwa na shaka.
 “Wapinzani wao ndio walikuwa wamemtilia shaka kwa hivyo sisi CCM tumeona huyu ameshatiliwa shaka kwa hivyo ndio maana tukamkataa,” alisema Shaaban.
Ramadhan alisema Lowassa alitendewa haki kikamilifu na suala la kwamba kuna watu walimuunga mkono baadaye wakakataa kumuunga mkono ni kwa sababu ya yaliyotokea ndani ya kikao cha Kamati ya Maadili.
 “Unaweza kumuunga mkono mtu lakini ukasikia baadaye ana mambo yake, ukakataa kumuunga mkono…na Rais (wa awamu ya tatu, Benjamin) Mkapa aliwahi kusema kuwa ukikaa pale kwenye kiti unayajua mambo mengi kwa hivyo nasema Kamati Kuu haikukosea kumuengua Lowassa. Funika kombe mwanaharamu apite,” alisema Ramadhan.
Haji Omar Kheri
Kada mwingine aliyeweka msimamo wake kuhusu Lowassa kwenye mkutano huo ambao ukikatishwa mara kwa mara kwa vicheko na nyimbo, alikuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Vikosi Maalumu), Haji Omar Kheri ambaye alisema hakuna haja ya kumnyang’anya kadi ya CCM mgombea huyo wa urais wa Chadema, na badala yake wanafuta jina lake kwenye daftari la wanachama.

Kufa au kupona wagombea CCM


Dar es Salaam. Leo ni kufa au kupona kwa makada wa CCM wanaowania ubunge wakati wanachama wa chama hicho tawala watakapopiga kura wilayani kuchagua wagombea kwenye majimbo yao baada ya wiki kadhaa za vikumbo zilizojumuisha kurushiana ngumi, tuhuma za rushwa, malumbano na migomo.
Uchaguzi Mkuu umepangwa kufanyika Oktoba 25 mwaka huu.
Katika upigaji kura leo, wanachama watakuwa na kazi ngumu kuamua kuhusu makada waliogeukia ubunge baada ya kukosa urais, mawaziri katika Serikali ya Awamu ya Nne inayoondoka madarakani, waliotemwa mwaka 2010 wanaowania kurejea bungeni, wakuu wa wilaya ambao wameingia kwa wingi kwenye mbio hizo, na pia wabunge wanaomaliza muda wao ambao ama walikidhi mahitaji yao au kutofanya kazi ipasavyo.
Mchakato huo wa kura ya maoni unafanyika baada ya kumalizika kwa siku 10 za wagombea hao kujinadi kwa makada wenzao katika kata mbalimbali za majimbo wanayotaka kugombea, huku baadhi wakijitoa kutokana na kushindwa kulipa fedha kama mchango wao wa safari za kampeni. Mchakato wa kura za maoni, utafuatiwa na vikao vya kamati za siasa za wilaya na mikoa wakati kikao cha Halmashauri Kuu ya CCM kitafanyika kwa siku mbili kuanzia Agosti 11 kwa ajili ya uteuzi wa wagombea rasmi wa ubunge na udiwani wa CCM.
Gazeti hili linakuchambulia maeneo matano yatakayozua mjadala mkali mara baada ya matokeo ya kura ya maoni kutangazwa, pamoja na kilichojitokea wakati wa kampeni za wagombea hao.
Wagombea urais waliojitosa ubunge
Macho ya wana-CCM na wananchi wengine yatakuwa yakielekezwa kwa makada wa CCM walioanguka kwenye mbio za urais na ambao wamegeukia ubunge, ambao ni pamoja na Mwigulu Nchemba (Iramba Magharibi), Lazaro Nyalandu (Singida Kaskazini) na mwanasiasa mkongwe ambaye kwa sasa ni Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Steven Wasira.
Wengine ni aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo, ambaye alijiuzulu kutokana na kashfa ya escrow, lakini anataka kurejea bungeni kuwakilisha jimbo la Musoma Vijijini.
Pia yumo January Makamba wa Bumbuli mkoani Tanga, William Ngeleja (Sengerema), Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mathias Chikawe (Nachingwea), Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Dk Titus Kamani (Busega) na Waziri wa Afrika Mashariki, Dk Harrison Mwakyembe anayerudi Kyela mkoani Mbeya na Balozi Augustine Maiga anayewania Iringa Mjini.
Majimbo yenye mchuano mkali
Nzega Vijijini
Moja kati ya majimbo yenye upinzani mkali kwa sasa ni jimbo la Nzega Vijijini kutokana na uwepo wa makada wawili wa chama hicho, Lucas Selelii na Dk Hamisi Kigwangalla.
Katika uchaguzi uliopita wa 2010, makada hao walivaana lakini wote wakaangushwa na Hussein Bashe aliyeibuka wa kwanza akifuatiwa na Selelii, lakini Halmashauri Kuu ya CCM ikamchukua Dk Kigwangalla aliyekuwa mshindi wa tatu.
Mgawanyo wa majimbo uliofanywa hivi karibuni na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), umefanya mpambano huo uwe wa makada hao, baada ya kumwachia Bashe jimbo la Nzega Mjini.
Iringa Mjini
Jimbo jingine lenye mchuano mkali ni Iringa Mjini ambako Balozi Augustine Mahiga aliyekwama katika harakati za kuwania urais kupitia CCM, atapambana na makada wengine kuwania kupata tiketi ya kulikomboa jimbo hilo kutoka Chadema.
Makada wengine kati ya 12  wanaowania kiti hicho ni Mkuu wa Wilaya ya Wanging’ombe, Frederick Mwakalebela, mwenyekiti wa CCM wa mkoa, Jesca Msambatavangu na katibu mwenezi wa CCM mkoa wa Iringa, Dk  Yahya Msigwa.
Kundi lingine ambalo huenda likaleta upinzani katika uchaguzi huo linamjumuisha mjumbe wa NEC wa Iringa Mjini, Mahamoud Madenge, mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Mzumbe, Falles Kibassa na mwandishi wa habari, Frank Kibiki.
Wengine wanaowania Iringa Mjini ni Peter Mwanilwa, Frank Kibiki, Michael Mlowe, Nuru Hepautwa, Adestino Mwilinge na Adani Kiponda.
Jimbo la Mkalama
Jimbo la Mkalama linaongoza kwa kuombwa na makada 16 wakiongozwa na mwenyekiti wa mkoa wa Singida, Mgana Msindai, Profesa Shaaban Aman Mbogho, Nakey Samwel Sule, Orgenes Emmanuel, Joseph Mbasha na Allan Joseph Kiula.
Wengine wanaowania jimbo hilo ni Emmanuel Mkumbo, Dk Kissui Stephen Kissui, William Makali, Kyuza Kitundu, Dk Charles Mgana, Salome Mwambu, Francis Mtinga, Dk George Mkoma na Lameck Itungi.
Jimbo la Kalenga
Mchuano mkali pia upo, Kalenga linalowaniwa na mbunge wa sasa, Godfrey Mgimwa na Jackson
Kiswaga, na Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Abbas Kandoro na mbunge wa zamani wa jimbo hilo, George Mlawa.
Jimbo la Mwanga
Mshikemshike mwingine unatarajiwa kuibuka katika Jimbo la Mwanga ambako Waziri wa Maji, Profesa Jumanne Maghembe anapambana tena na hasimu wake mkubwa katika kiti hicho, Joseph Thadayo.
Maeneo yaliyotokea tafrani
Wakati baadhi wakikabiliana na upinzani mkali, makada wengine watakuwa wakihangaika kushawishi wapigakura baada ya kukumbana na hali ngumu kwenye kampeni.
Baadhi yao ni mbunge wa Muleba Kusini, Profesa Anna Tibaijuka, Harrison Mwakyembe (Kyela) na Assumpter Mshama (Nkenge).
Profesa Tibaijuka
Profesa Tibaijuka anayewania jimbo hilo kwa mara ya pili,  alishushwa jukwaani kwa kuzomewa na wananchi wake katika kata ya Nshamba wilayani Muleba na tafrani hiyo kudumu kwa dakika kadhaa na kusababisha wagombea wengine kulazimika kuondoka.
Kwa mara ya kwanza alizomewa Juni 8, wakati wa ziara ya katibu mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana kwenye kata hiyo hiyo kutokana na kutajwa kwenye kashfa ya escrow na kushindwa kutekeleza ahadi ya kuwajengea barabara ya lami.
Mwakyembe
Hasira za wananchi pia zilimkumba mbunge wa Kyela, Harrison Mwakyembe kwenye moja ya mikutano yake baada ya wananchi kupiga kelele kutotaka kumsikiliza.
Profesa Maghembe
Hali kama hiyo ilimkuta Profesa Maghembe kwenye jimbo lake la Mwanga wakati akijinadi katika mkutano wa kampeni uliofanyika Kisangara.
 “Kidumu Chama cha Mapinduzi. Kisangara saafii,” alisalimia Profesa Maghembe na kuitikiwa na sauti za “ondoka ondoka, tumekuchoka sasa, nenda kapumzike huna jipya, waachie wenzio”.
Profesa Maghembe alipoulizwa na gazeti hili jana kuhusu kadhia hiyo, alisema vijana waliomzomea walikodishwa na kupewa pombe katika baa ya jirani ili tu kujaribu kuchafua hali ya hewa.
Profesa Maghembe anachuana tena na mshindani wake wa 2010, Joseph Tadayo na wagombea wengine ambao ni Karia Magaro, Baraka Lolila, Ramadhani Mahuna, Japhar Mghamba na Miniel Kidali.
Naibu Spika Ndugai
Wakati Maghembe akikumbana na hasira za wananchi, Naibu Spika wa Bunge Job Ndugai alishindwa kuzuia hasira zake wakati maneno ya mgombea mwenzake yaliposababisha amvamie na kujikuta akihojiwa na polisi.
Ndugai alihojiwa na polisi kwa tuhuma za kumshambulia mgombea mwenzake, Dk Joseph Chilongani kwenye mkutano wa kampeni akimtuhumu kurekodi tukio la kutaka kumpiga mgombea mwingine aliyekuwa akijieleza na kuponda uongozi unaomaliza muda wake.
Hata kama atapita leo, suala lake linatarajiwa kuwa moja ya hoja kwenye kikao cha Halmashauri Kuu.
Mwigulu Nchemba
Hali kama hiyo ipo kwa mbunge wa Iramba Magharibi, Mwigulu Nchemba anayetetea jimbo lake akipambana vikali na katibu mkuu wa zamani wa Wizara ya Nishati na Madini, David Jairo, pamoja na Juma Hassan Kilimba anayerudi na Amon Gyuda.
Nchemba amekumbana na tafrani baada ya kuhojiwa na Takukuru kwa tuhuma za rushwa. Baadhi ya wagombea wanaowania pamoja naye walishtaki kuwa mwenzao anafanya vitendo ambavyo walivihusisha na rushwa na hivyo Takukuru kuchukua hatua.
Lusinde ‘Kibajaji’
Ushindani mkubwa katika jimbo la Mtera unaonekana kuwa baina ya mbunge anayemaliza muda wake, Livingstone Lusinde ‘Kibajaji’ na mtoto wa aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo, Samuel Malecela.
Lusinde pia amekuwa akikumbana na kadhia hiyo baada ya wananchi kumzomea wakati akieleza sera zake kwenye kijiji cha Nkwenda wilayani Chamwino.
Baada ya zomeazomea hiyo, mbunge huyo anadaiwa kuagiza kikundi cha vijana kuwashambulia wananchi ambao walikuwa wakimpiga kelele kumzomea.
Venance Mwamoto
Kada mwingine anayewania kurejea bungeni ni mwanasoka wa zamani, Venance Mwamoto ambaye amerejea Jimbo la Kilolo kupambana na mbunge wa sasa Profesa Peter Msolla.
Wanahabari wapambana
Wakati wanahabari wakikumbana na makada wa fani nyingine kwenye mbio hizo, Jimbo la Chemba linakutanisha wanahabari wawili, Naibu Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Juma Nkamia ambaye atavaana na mhariri kutoka gazeti la Mtanzania, Khamis Nkyota anayelitaka jimbo hilo kwa udi na uvumba.
Tayari Nkamia ameshalalamikia bungeni harakati za mwanahabari mwenzake kwenye jimbo hilo.
Manyoni Magharibi
Hali ushindani inayotokana na makada wengi kujitokeza pia ipo kwenye Jimbo la Manyoni Magharibi ambako John Lwanji, mbunge anayemaliza muda wake, anakabwa koo na binamu yake Eliphas Emmanuel Lwanji. Wengine ni Jamal Kuwingwa, Jane Likuda, Mohamed Makwaya, Yahaya Masare, Athumani Masasi, Yohana Msita, Moshi Mmanywa, Adimini Msokwa, Dk Mwanga Mkayagwa, Rashidi Saidi na Francis Shaaban.
Mbeya Mjini
Hali kama hiyo pia ipo Mbeya Mjini ambako Charles Mwakipesile aliyepambana na mbunge wa sasa Joseph Mbilinyi mwaka 2010, atakuwa akipambana na Stephen Mwakwenda, Nwaka Mwakisu, Aggrey Mwasanguti na  Mchungaji Jackson Numbi
Wengine ni Ibrahim Mbembela, Fatma Ismail , Shambwe Shitambala, Solomon Swila, James Mwampondele, Ulimboka Mwakilili, Samuel Mwaisume, Eliud Mwaiteleke, Michael Mbuza Aman Kajuna na  Shadrack Mwakombe.
Singida Kaskazini
Lazaro Nyalandu atakuwa na kazi ya kuzuia kazi ya Amos Makiya, Justin Monko, Michael Mpombo, Sabasaba Manase, Yahana Sinton, Mugwe na Aaron Mgogho.
Jimbo la Nanyumbu
Mgombea wa jimbo la Nanyumbu Dastani Mkapa yupo katika wakati mgumu kutokana na mgombea mpinzani wake William Dua kuonekana ana kasi ya kuchukua Jimbo hilo.
Jimbo la Ndanda
Mgombea wa jimbo jipya la Ndanda, Mariam Kasembe alijikuta akitoa machozi baada ya wananchi wa jumbo hilo kuuliza maswali kwa mgombea huyo na kushindwa kuyatolea majibu.
Jimbo la Newala
Mbunge wa jimbo hilo, George Mkuchika ana wakati mgumu kurudi katika nafasi hiyo kutokana na ushindani uliopo kuwa mkubwa ukilinganisha na uchanguzi wa 2010.

Nape afafanua sakata lake na Takukuru Lindi


Lindi. Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye amefafanua sakata lake la kuchukuliwa na askari wa Takukuru kwa mahojiano muda mfupi baada ya kuchukua fedha benki, akisema alikuwa akielekea kulipa mawakala.
Nape, anayewania ubunge wa Jimbo la Mtama, jana mchana aliamriwa na maofisa wa Takukuru kufika ofisi zao baada ya kutoka kuchukua fedha benki ya NMB eneo la Misonobarini mkoa Lindi.
“Ninadhani hawa jamaa walipotoshwa. Mimi nimekwenda zangu benki kuchukua fedha, lengo langu ni kuwalipa mawakala,” alisema Nape jana jioni alipopigiwa simu na Mwananchi kutoa ufafanuzi wa sakata hilo.
“Wakaja hawa jamaa, wakajitambulisha kuwa wanatoka Takukuru, wakaniuliza ‘mbona ninachukua fedha nyingi kipindi hiki?’ Nikawaambia ‘nakwenda kulipa mawakala, na fedha zenyewe ni hizi Sh3.6 milioni’.
“Basi, tukatoka taratibu tukaenda ofisini kwao, ni karibu tu na benki. Wakanihoji hata haikumalizika nusu saa, niliwaambia nataka kulipa mawakala wangu, tena fedha zenyewe hazitoshi, wako zaidi ya 100.”
Nape aliongeza kusema kuwa walimkamata na akawaambia kuwa yeye ni mwadilifu.
“Halafu ninyi, mnaacha marushwa makubwa makubwa huko, watu wanahonga halafu mnamvizia Nape masikini kwa Sh3mil?,” alisema.
Nape alielezea kufadhaishwa na tukio hilo akidai kuwa limetengenezwa kwa ajili ya kumchafua hasa kwa kuwa leo kuna kura za maoni, lakini akasema anaamini yeye ni msafi.
Kamanda wa Takukuru wa Mkoa wa Lindi, Stephen Chami alikiri kumhoji Nape, lakini akasema walijiridhisha kuwa fedha hizo ni kwa ajili ya kulipa mawakala.
“Unajua tuna watu wetu, kwenye maeneo mbalimbali hasa kipindi hiki cha uchaguzi, tumeweka watu wetu maeneo mengi, tunataka kukomesha rushwa,” alisema.
Kilango ageuka ‘mbogo’
Katika hatua nyingine, Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Anne Kilango Malecela juzi aligeuka mbogo baada ya kuzushiwa katika mitandao ya kijamii kuwa anashikiliwa na polisi.
Taarifa hizo zilizosambazwa jana, zilidai kuwa Kilango alikamatwa juzi saa 5:00 usiku katika eneo la Dimbi, kijiji cha Bagamoyo kwa tuhuma za kutoa rushwa, madai ambayo ameyakanusha.
Hata hivyo, Kilango alipoulizwa jana alisema tuhuma hizo ni uzushi uliotengenezwa na baadhi ya washindani wake wakiamini kwa kufanya hivyo watamvurugia katika kura ya maoni inayofanyika leo.
“Sijakamatwa na wala sijaona hata polisi mmoja nyumbani kwangu. Nimelala nyumbani kwangu jana (juzi) na leo (jana) nimeamka nyumbani kwangu na niko kwenye mikutano ya kuomba kura,” alisema.
Kilango aliongeza,”Sasa hivi nimetoka kuomba kura Mtii nilikuwa peke yangu wagombea wanzangu wameingia mitini. Niko Bombo sasa hivi (saa 9;00 alasiri) ndio wanakuja nishapiga bao.”
Kwa mujibu wa Kilango, baadhi ya wagombea wamekuwa wakifanya kampeni zisizo za kistaarabu kwa kuandaa vijana aliodai wamepewa pombe ili wamzomee katika baadhi ya maeneo aliyopita.