Wednesday, December 6

WAZIRI MKUU AKAGUA MAKAZI YA MAKAMU WA RAIS

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amekagua matengenezo ya makazi ya muda yanayotarajiwa kutumiwa Makamu wa Rais, Mhe. Samia Suluhu Hassan pindi atakapohamia Dodoma.
Waziri Mkuu amefanya ukaguzi huo leo mchana (Jumatano, Desemba 6, 2017) katika eneo la Kilimani, mjini Dodoma ambako yalikuwa makazi ya Mkuu wa Mkoa huo.
Akitoa taarifa ya ujenzi huo, Waziri wa Nchi (OWM) anayeshughulikia Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Ajira, Wenye Ulemavu na Vijana, Bibi Jenista Mhagama alisema Kikosi kazi cha kuratibu zoezi la Serikali kuhamia Dodoma kilibaini kuwa mahali alipokuwa akiishi awali siyo sahihi kwa ajili ya makazi ya kudumu ya Mhe. Makamu wa Rais.
“Pale palikuwa panafaa kwa ajili ya ziara za kikazi alipokuwa akija Dodoma, kwa hiyo tumeamua tufanye ukarabati hapa, ili aweze kuishi kwa viwango vinavyostahili.”
Alisema kazi ya matengenezo kwenye makazi yake itagharimu sh. bilioni 1.5 wakati kazi ya kutenganisha ofisi za watumishi na wasaidizi wa Makamu wa Rais itagharimu sh. milioni 680.
Waziri Mkuu pia alikagua matengenezo ya Ofisi inayotarajiwa kutumiwa na Makamu wa Rais ambayo itakuwa eneo la Ndejengwa.
Wakati huohuo, Kaimu Meneja wa TBA Mkoa wa Dodoma, Bw. Steven Simba ambaye anasimamia ujenzi huo, alimweleza Waziri Mkuu wanataraji kuwa kazi hiyo itakamilika kabla ya Desemba 30, mwaka huu.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akipokea maelezo ya ujenzi kutoka kwa Msanifu Majengo, Edward Kayombo (kulia) wakati alipoenda kukagua ofisi na makazi ya Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan mjini Dodoma Desemba 6, 2017 wa pili kulia ni Kaimu Meneja wa TBA-Dodoma, Steven Simba (kushoto) ni Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Bi. Maimuna Tarishi, na wapili kushoto ni Waziri wa Nchi Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Walemavu Jenista Mhagama.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akipewa maelezo ya mpangilio wa Ofisi ya Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan kutoka kwa Msanifu Majengo, Edward Kayombo (kulia) wakati alipokwenda kukagua ofisi hiyo mjini Dodoma Desemba 6, 2017 (katikati) ni Waziri wa Nchi Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Walemavu, Jenista Mhagama. 


Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akikagua ukarabati wa makazi ya Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan mjini Dodoma Desemba 6, 2017.

RAIS DKT. MAGUFULI AFANYA UTEUZI WA WENYEVITI WA BODI SITA

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli amefanya uteuzi wa wenyeviti wa bodi sita za taasisi za Serikali baada ya wenyeviti waliokuwepo kumaliza muda wao.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo tarehe 06 Desemba, 2017 na Katibu Mkuu Kiongozi Balozi John Kijazi, Kwanza Mhe. Rais Magufuli amemteua Bi. Monica Ngenzi Mbega kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Mazao Mchanganyiko kuanzia tarehe 30 Novemba, 2017.

Pili, Mhe. Rais Magufuli amemteua Prof. Egid Beatus Mubofu kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Kampuni ya Mbolea Tanzania (TFC) kuanzia tarehe 01 Desemba, 2017.

Tatu, Mhe. Rais Magufuli amemteua Prof. Abiud Kaswamila kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro kuanzia tarehe 01 Desemba, 2017.

Nne, Mhe. Rais Magufuli amemteua Prof. Esther Hellen Jason kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali kuanzia tarehe 01 Desemba, 2017.

Tano, Mhe. Rais Magufuli amemteua Dkt. Kenneth Mdadila kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya taasisi ya kifedha ya Self Microfinance Fund Limited kuanzia tarehe 01 Desemba, 2017. 

Sita, Mhe. Rais Magufuli amemteua Dkt. Titus Mlengeya Dismas Kamani kuwa Mwenyekiti wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania kuanzia tarehe 06 Desemba, 2017.

Gerson Msigwa
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Dar es Salaam
06 Desemba, 2017

Chama cha wanasheria kutofutwa


Mtwara. Naibu katibu Mkuu, Wizara ya Katiba na Sheria, Amon Mpanju amesema Serikali haina mpango wa kukifuta Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS), badala yake itashirikiana na viongozi wa taasisi hiyo kuboresha upungufu uliopo ili kukidhi mahitaji.
Mpanju amesema hayo leo Jumatano Desemba 6,2017 wakati wa maadhimisho ya wiki ya sheria katika kanda ya kusini mkoani Mtwara yanayofanyika kwenye viwanja vya Mashujaa vilivyopo Manispaa ya Mtwara Mikindani.
Amesema sheria iliyopo imepitwa na wakati kutokana na kuwepo ongezeko la mawakili, hivyo inatakiwa kufanyiwa marekebisho kukidhi mahitaji yaliyopo na kutengeneza mazingira mazuri katika tasnia hiyo.
“Serikali haina wazo la kufuta chama cha wanasheria kwa sababu ndicho chombo kinachowaunganisha na kutoa msaada wa kisheria. Tunachotaka kufanya ni kuweka mazingira mazuri kwa lengo la kuboresha ili kukidhi mahitaji,” amesema Mpanju.
Mwenyekiti wa chama cha wanasheria kanda ya kusini, Stephen Lekeya amesema walikuwa na hofu ya kufutwa TLS kwa kuwa walishapewa bango kitita kwa ajili ya kutoa maoni.
“Tulikuwa na hofu baada ya aliyekuwa Waziri wa Katiba na Sheria kutoa kauli juu ya kufutwa kwa chama chetu si kwa maneno bali tulishapewa bango kitita kwa ajili ya kutoa maoni ya kuwepo bodi itakayosimamia chama hiki na kitakuwa chini ya Serikali,” amesema Lekeya.
Amesema katika maadhimisho hayo mwitikio wa wananchi wa kupata huduma ya msaada wa kisheria umekuwa mdogo.
Lekeya amesema wamepata idadi ndogo ya wananchi wanaohitaji huduma ya msaada wa kisheria kwa sababu ama hawaelewi dhana ya msaada wa kisheria, watu hawana matatizo ya kisheria au wameogopa kwamba watatozwa fedha kwa kuwa mawakili wapo.

Upelelezi wa mfanyabiashara aliyekamatwa Z’bar bado


Imeelezwa kuwa mfanyabiashara aliyekamatwa kwa tuhuma za kukutwa na vito vya dhahabu na mamilioni ya fedha ya nchi 15 ataendelea kuwa chini ya ulinzi hadi uchunguzi dhidi yake utakapomilika.
Naibu Mkurungezi wa Makosa ya Jinai Zanzibar, Ramadhani Ng’anzi alisema juhudi za ukamilisha uchunguzi dhidi ya tukio hilo zinaendelea.
“Hatuwezi kusema wapi tumefikia hadi pale tutakapokamilisha kazi yetu ya uchunguzi, ila tunaendelea kumshikilikia kwa mujibu wa taratibu zetu,” alisema Ng’anzi.
Kaimu Kamishna wa Polisi Zanzibar, Juma Yussuf Ali alisema mfanyabiashara huyo alikamatwa baada ya kutiliwa shaka wakati akitaka kusafiri nje ya nchi.
Ali alisema kwa mujibu wa taratibu za kipolisi na kiusalama ililazimika kumzuia mfanyabiashara huyo kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi wa mali alizotaka kuondoka nazo nje ya nchi.
Msemaji wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Zanzibar, Makame Abdalla alisema kukamatwa kwa mfanyabiashara huyo uwanjani hapo ni tukio kubwa la kwanza kutokea.

Wabunge tisa wa Ukawa watajwa kuhamia CCM


Joto la wanasiasa wa upinzani, hasa kutoka vyama vilivyounda Ukawa, kuhamia CCM likiendelea kuongezeka, majina ya baadhi ya wabunge yamekuwa yakihusishwa na wimbi hilo.
Lakini walipotafutwa na Mwananchi, baadhi hawakuwa tayari kutoa msimamo wao kuhusu uvumi huo, wengine walisema watatoa taarifa rasmi leo na baadhi yao walikanusha vikali.
Kwa kauli ya “kuunga mkono jitihada za Rais John Magufuli”, madiwani walianzisha joto hilo kwa kujivua nyadhifa zao na kutangaza kuhamia CCM, lakini Lazaro Nyalandu alibadilisha upepo alipojivua ubunge na kukihama chama hicho tawala, akisema anaungana na wapinzani kupigania Katiba, haki za binadamu na demokrasia.
Sasa wimbi hilo limehamia kwa wabunge baada ya Maulid Mtulia kujivua uanachama wa CUF na ubunge wa Kinondoni mwishoni mwa wiki. Uamuzi wake umefuatiwa na ubashiri kuwa kuna wabunge wengine kadhaa walio safarini.
Habari hizo zimesambaa kwenye mitandao ya kijamii, zikiwakariri baadhi ya wabunge wakiwatuliza wanachama na wafuasi wao wasishangae watakaposikia wenzao wametangaza kuhama upinzani.
Taarifa hizo zinawataja baadhi ya wabunge kutoka Chadema na CUF kwamba wako kwenye mazungumzo ya kuhitimisha safari yao ya kuhamia CCM kwa madai ya “kuunga mkono jitihada za kuleta maendeleo nchini zinazofanywa na Rais Magufuli”.
Baadhi ya wabunge wa Chadema ambao wanatajwa ni Saed Kubenea (Ubungo), James Millya (Simanjiro), Anthony Komu (Moshi Vijijini), John Mnyika (Kibamba), Japhary Michael (Moshi Mjini) na Cecil Mwambe wa Ndanda.
Kwa upande wa CUF ni Zubery Kuchauka (Liwale), Magdalena Sakaya (Kaliua) na Maftaha Nachuma wa Mtwara Mjini.
Taarifa za wabunge hao kuhama zilichagizwa na kauli ya mbunge wa Arusha Mjini (Chadema), Godbless Lema aliyeandika katika akaunti yake ya Twitter kwamba leo (Jumatano) au Ijumaa kuna wabunge wa upinzani watatangaza kuhama.
Lema alibashiri kuwa mbunge wa zamani wa Kigoma Kusini, David Kafulila aliyekuwa NCCR-Mageuzi na baadaye Chadema, angehamia CCM, akimuelezea kama “mwanasiasa kijana aliyekuwa machachari 2010-2015”.
Katika ujumbe wa juzi, Lema, ambaye ni mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema, aliandika: “Kati ya Jumatano (leo) wiki hii na Ijumaa, pesa itakuwa na thamani kwa maisha ya mvulana mmoja ambaye ni mbunge kutoka Chadema.”
Kauli hiyo ya Lema iliamsha mjadala huku anayezungumzwa zaidi kuhama akiwa ni Kubenea ambaye inaelezwa kwamba atahamia CCM, lakini alipoulizwa jana hakuweka bayana.
“Siwezi kuzungumza na chombo kimoja kimoja cha habari. Kesho au keshokutwa nitazungumza. Nipo katika maandalizi na nitaeleza hicho kinachoelezwa,” alisema Kubenea.
Jibu kama hilo lilitolewa na Ole Millya, ambaye alihamia Chadema 2015 wakati wa ‘mafuriko’ ya aliyekuwa Waziri Mkuu, Edward Lowasa.
“Kwa sasa nisijibu chochote, wakati ni dawa,” alisema.
Alipoulizwa kuhusu hali ya sintofahamu kwa wananchi waliomchagua, alijibu: “Wananchi wangu, najua jinsi ya kudeal nao mimi.”
Baadaye Ole Millya alisema heshima aliyopewa na wana Simanjiro ni kubwa na anatambua hilo, hivyo wapuuze yanayoandikwa kwenye mitandao ya kijamii.
Alisema ana njozi ya Simanjiro mpya na aliweka msimamo asizungumze chochote hadi Ijumaa, ila kwa heshima ya wana Simanjiro ameamua kukanusha hilo.
“Nimesema niwajulishe kwa sababu ninyi ndiyo marafiki, mabosi wangu. Nami nataka muwe na ukweli kutoka kwa mbunge wenu. Wacha wapige ramli, waendelee kupiga ramli zao,” alisema Ole Millya.
Kauli ya Ole Millya inalingana na ya Kuchauka ambaye alisema akiwa upinzani anaweza kuisimamia Serikali vilivyo kuliko akiwa CCM.
“Kwanza hawawezi kuja na wakija, unatakiwa uwe umeonyesha mwelekeo huo na mimi ninaamini nikiwa upinzani naweza kuisimamia Serikali na kuisema ila ukiwa CCM unafungwa mdomo na huwezi kuisimamia au kuikosoa,” alisema Kuchauka.
Kauli kama hiyo ilitolewa na Sakaya. “Hao wanaonitaja ni propaganda tu. Mimi ni mtu wa misimamo na sijawahi kuyumbishwa na wala sitegemei kushikiwa akili,” alisema kaimu katibu mkuu huyo wa CUF upande wa Profesa Ibrahim Lipumba.
“Mimi ni mbunge, nimekuwa napongeza inapobidi na kukosoa inaponilazimu. Hao wanaoondoka kuwa wanamuunga mkono Rais sijui wamekwenda shule? Kwani ukiwa upinzani huwezi? Wananchi wamekuamini halafu. Nafikiri kuna ajenda na yawezekana wananunuliwa kwa fedha nyingi ambazo mimi siwezi kukubali.”
Mnyika alipotafutwa na Mwananchi alijibu kwa kifupi tu; “sio kweli, ni habari za uongo.”
Hali haikuwa rahisi kwa Mwananchi kumpata Komu, Mwambe na Jafary.
Lakini juzi, meya wa Ubungo Boniface Jacob aliandika ujumbe katika akaunti yake ya Instagram kuwahakikishia wanachama na wafuasi kuwa kuna jaribio la kumng’oa Mnyika.
“Mwambieni... aache kupiga simu ovyo. Tumemrekodi na tutaendelea kumrekodi tumuaibishee. Any time atume sms au apige tena aone,” ameandika katika akaunti hiyo na kuonya kuwa Mnyika si mtu wa kuahidiwa cheo na madaraka ya kuhongwa.
Akizungumza na Mwananchi jana, Meya Jacob alisema walikuwa wakimsumbua Mnyika.
“Niliamua kutoa ufafanuzi huo kwa kuwa tulikuwa na Mnyika halafu wanampigiapigia simu hao (anawataja majina). Ndio maana nikaamua kuandika hivyo kuwa Mnyika hawezi kuhama na kesho (leo) tutakuwa na Kamati Kuu,” alisema.   

Uchafu wa mazingira waisababishia hasara Serikali

Dodoma. Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu amesema Tanzania inapoteza zaidi ya Sh340 bilioni kila mwaka kutokana na uchafu wa mazingira.
Amesema hali hiyo inasababishwa na uzembe wa maofisa afya ambao hawatekelezi majukumu yao ipasavyo.
Ummy amesema hayo leo Jumatano Desemba 6,2017 alipozungumza na wananchi wa Kijiji cha Humekwa wilayani Chamwino mkoani Dodoma, kuelekea uzinduzi wa awamu ya pili ya kampeni ya kitaifa ya usafi wa mazingira kesho Desemba 7,2017.
Ametoa agizo kwa maofisa afya kuzingatia usafi wa mazingira kwa kuwa Tanzania haiwezi kuwa nchi yenye uchumi wa kati ikiwa usafi hautazingatiwa.
"Tunazungumzia kuokoa fedha za Serikali na kuzielekeza kwa jamii kwenye mambo yanayogusa wananchi moja kwa moja. Kwa uchambuzi wa Benki ya Dunia tunapoteza Sh340 bilioni kila mwaka kutokana na kukosekana hali ya usafi," amesema Ummy.
Amesema litakuwa kosa la jinai kwa kaya isiyokuwa na choo bora baada ya sheria kubadilishwa.

Madabida na wenzake wapanda kizimbani kwa uhujumu uchumi


Dar es Salaam. Aliyekuwa Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Dar es Salaam, Ramadhani Madabida na wenzake watano leo Jumatano wamepanda kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na mashtaka sita ya uhujumu uchumi ikiwamo kusambaza dawa bandia za kufubaza virusi vya Ukimwi ' ARV’s ' na kusababisha hasara ya Sh 148 milioni.
Kabla ya kusomewa mashtaka ya kesi hiyo mpya ya uhujumu uchumi namba 80 ya 2017, mahakama ilimfutia kesi iliyokuwa na mashtaka matano yanayofanana na hiyo iliyofunguliwa mwaka 2014.
Kesi hiyo imefutwa na Hakimu Mkazi Mwandamizi, Victoria Nongwa baada ya Wakili wa Serikali, Shedrack Kimaro kuomba iondolewe kwa kuwa Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) hana nia ya kuendeleza mashtaka dhidi yao.
Kesi hiyo ilikuwa katika hatua ya usikilizwaji wa ushahidi wa mashahidi wa upande wa mashtaka na mashadi tisa walikuwa wamekwishatoa ushahidi wao na washtakiwa walikuwa nje kwa dhamana.
Baada ya kesi hiyo kufutwa, Madabida ambaye ni ofisa mtendaji mkuu wa kiwanda hicho na wenzake walikamatwa tena na kufunguliwa kesi hiyo mpya ya uhujumu uchumi.
Mbali na Madabida wengine wanaokabiliwa na kesi hiyo ni 
Seif Shamte ambaye ni mkurugenzi wa uendeshaji,  
Simon Msoffe (meneja masoko) na  Fatma Shango (mhasibu msaidizi) wa Tanzania Pharmaceutical Industries Ltd.
Pamoja na Sadick Materu na Evans Mwemezi ambao ni maofisa wa Bohari Kuu ya Dawa.  
Baada ya kusomewa mashtaka washtakiwa hao hawakurusiwa kuongea chochote kwa sababu mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu haina mamlaka ya kuisikiliza kesi hiyo hadi Mahakama Kuu.
Wakili wa Serikali, Pius Hilla alisema upelelezi wa kesi hiyo umekamilika lakini DPP bado hajafanya maamuzi kama isikilizwe Kisutu ama Mahakama Kuu.
Washtakiwa hao wanatetewa na Mawakili Denis Msafiri, Makaki Masatu na Nehemiah Nkoko.
Wakili Msafiri alisema Mahakama ya Kisutu inayo mamlaka ya kuisikiliza hiyo kwa sababu kiwango chake cha fedha kipo chini ya Sh 1 bilioni  ambayo ndiyo inapaswa kusikilizwa Mahakama Kuu.
Kutokana na hoja hiyo Wakili Hilla aliomba wapewe muda hadi kesho Alhamisi ndiyo wajibu hoja ya upande wa utetezi.
Hakimu Nongwa aliiahirisha kesi hiyo hadi kesho Alhamisi kutokana na ombi hilo na kuamuru washtakiwa wapelekwe polisi hadi kesho Alhamisi itakaposikilizwa hoja kama mahakama hiyo ina mamlaka ya kuisikiliza kesi hiyo ama la.

Rais Magufuli atuma rambirambi kifo cha Bendera


Dar es Salaam. Rais John Magufuli ameomboleza kifo cha mkuu wa mkoa mstaafu, Joel Bendera kilichotokea katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH). 
“Jioni hii nimepokea kwa mshtuko na huzuni kubwa taarifa za kifo cha Mkuu wa Mkoa mstaafu Dk Joel Nkaya Bendera, natoa pole kwa familia yake na wote walioguswa na msiba huu, pia naungana nao katika kipindi hiki cha majonzi,” amesema Rais Magufuli katika taarifa iliyotolewa na Ikulu leo Jumatano Desemba 6,2017.
Bendera amefariki dunia jioni ya leo katika Hospitali ya Muhimbili alikofikishwa kwa ajili ya kupata matibabu.
Rais Magufuli amesema Bendera atakumbukwa kwa mchango alioutoa kwa Taifa akiwa kiongozi katika nyadhifa mbalimbali zikiwemo ukuu wa mkoa, naibu waziri na mbunge. Pia, katika maendeleo ya michezo.
“Alikuwa kiongozi shupavu, mahiri na mchapakazi, alipenda kufanya kazi kwa ushirikiano na daima alitamani kupata mafanikio makubwa katika majukumu aliyokuwa nayo, hakika tutamkumbuka,” amesema Rais Magufuli.
Pia, amewapa pole wananchi wa mikoa ya Manyara alikokuwa mkuu wa mkoa Oktoba 26,2017 na mkoani Tanga alikokuwa mbunge.
Rais Magufuli ametoa pole kwa wanachama wa Chama cha Mapinduzi (CCM), wanamichezo na wote walioguswa na msiba huo.

Polisi waua watuhumiwa kwa kuwapiga risasi

Wakazi wa Manispaa ya Moshi mkoani Kilimanjaro
Wakazi wa Manispaa ya Moshi mkoani Kilimanjaro wakiitambua miili ya watu waliouawa wakituhumiwa kuwa majambazi katika chumba cha kuhifadhia maiti cha Hospitali ya Mawenzi. Waliuawa jana usiku eneo la Njoro. Picha na Diones Nyato. 
Moshi. Watu watatu wanaodaiwa kuwa majambazi wameuawa kwa kupigwa risasi na polisi mkoani Kilimanjaro.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Hamis Issah amesema watu hao waliuawa jana Jumanne Desemba 5,2017 jioni katika msitu wa Njoro wakati wa majibizano ya risasi na polisi.
Amesema watuhumiwa hao wa ujambazi walikuwa wakiishi chumba kimoja eneo la Njoro ambako polisi walipofika hawakuwakuta na walipata taarifa kuwa wamejificha msituni.
Kamanda Issah amesema kwa kushirikiana na wananchi walikwenda ndani ya msitu huo ambako walisikia milio ya risasi ndipo askari walipofyatua risasi na kusababisha vifo vyao.
Amewataja waliouawa kuwa ni Yusufu Juma Mdoe aliyekuwa akikabiliwa na kesi ya mauaji mwaka 2015; Francis Hamis Kinyaia ‘Wakudata’ ambaye amesema alikuwa akikabiliwa na kesi ya mauaji mwaka 2013.
Kamanda Issah amemtaja mwingine kuwa ni Valerian Joackim ‘Mdoe’ aliyekuwa na kesi ya mauaji ya mwaka 2013.
Amesema uchunguzi wa polisi umebaini watuhumiwa hao walihusika katika tukio la kufungwa miguu, mikono na kuzibwa mdomo mlinzi lililotokea Novemba 24,2017 eneo la Uru Shimbwe. Katika tukio hilo, bunduki mbili aina ya shotgun ziliporwa. 
Kamanda Issah amesema katika msitu wa Njoro walikuta bunduki moja aina ya shotgun iliyokatwa mtutu na kitako, huku namba zikiwa zimefutwa, risasi tatu, maganda matatu ya risasi, mapanga mawili, mkasi unaotumika kukata makufuli, kirungu cha polisi, tindo na misokoto miwili ya bangi.
Ameema miili ya watuhumiwa  imehifadhiwa katika Hospitali ya Mkoa wa Kilimanjaro ya Mawenzi.

CWT yataka upandishaji madaraja, vyeo uanze Juni, 2016


Dar es Salaam. Chama cha Walimu Tanzania (CWT) kimetaka Serikali kuanza kuhesabu madaraja na vyeo walivyopewa walimu kuanzia Juni, 2016 badala ya Novemba, 2017 kama ilivyotangazwa.
Kazi ya upandishaji madaraja ilitarajiwa kufanyika miezi 19 iliyopita kabla ya kuzuiwa kupisha uhakiki wa watumishi hewa na wenye vyeti feki.
Kaimu Rais wa CWT, Leah Ulaya amesema leo Jumatano Desemba 6,2017 kuwa matarajio yao yalikuwa ni kuona baada ya uhakiki kukamilika madaraja yaendelee kama kawaida kuanzia pale kazi ilipositishwa.
“Tunabaki na swali la kujiuliza, wale walimu waliopandishwa madaraja kati ya Februari na Aprili, 2016 mapunjo na hatima yao ikoje na hasa baada ya agizo hili la madaraja kuanza Novemba Mosi,2017,” amesema Ulaya.
Amesema kuna baadhi ya walimu walioachishwa kazi wakati uhakiki ukiendelea na baadhi wakiwa wameshapata barua za kupandishwa madaraja, hivyo Serikali inatakiwa kuangalia namna ya kuwasaidia.
Ulaya amesema Serikali inapaswa kutoa ufafanuzi wa kutosha kwa walimu ili watambue barua na madaraja waliyopewa awali kama yana maana yoyote.
Amesema kwa kuzingatia hilo, wamepanga kufikisha kilio chao kwa Rais John Magufuli katika kikao kitakachofanyika Desemba 14 na Desemba 15,2017 mjini Dodoma.

Maandalizi sherehe ya miaka 56 ya Uhuru yaiva


Maandalizi ya maadhimisho ya miaka 56 ya Uhuru yamefikia hatua za mwisho huku Serikali ikieleza kuwa sherehe hiyo itapambwa na gwaride la mkoloni litakalofanywa na Jeshi la Polisi.
Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Dk Binilith Mahenge alisema
itakuwa ni mara ya kwanza kwa gwaride hilo la mkoloni kufanyika katika sherehe hiyo ambayo mgeni rasmi atakuwa Rais John Magufuli.
“Maandalizi muhimu ikiwa ni pamoja na marekebisho ya uwanja na mahitaji mengine muhimu yapo katika hatua za mwisho,” alisema DK Mahenge.
Alifafanua kuwa maonyesho hayo yatakayofanyika Desemba 9 yatajumuisha gwaride maalumu la heshima lililoandaliwa na vikosi vya ulinzi na usalama nchini na onyesho la makomandoo.
Nyinginie ni kwata ya kimya kimya iliyoandaliwa na Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), Onyesho la Jeshi la mkoloni kutoka Jeshi la Polisi.
“Watoto 225 kutoka shule za sekondari watashiriki katika gwaride hilo,” alisema.
Alisema lengo la Serikali kuwashirikisha ni kuwafundisha na kuwaridhisha tunu ya uhuru, uzalendo, umoja, mshikamano na utaifa.
Pia, kutakuwa na vikundi vya ngoma za asili kutoka Ruvuma, Kigoma, Zanzibar pamoja na kwaya kutoka Chunya mkoani Mbeya.
DK Mahenge aliwasihi Watanzania kumuunga mkono Rais Magufuli kupiga vita rushwa na kufanya kazi kwa bidiii kwa ajili ya kujiletea maendeleo.
Pia, aliwataka wananchi kujitokeza kwa wingi katika maadhimisho hayo na kutoogopa mizinga itakayopigwa katika sherehe hizo kwasababu haina madhara.

Gharama iliyojificha kwa wanaohama vyama


Si jambo jipya tena kwa sasa kusikia mwanasiasa amehama kutoka chama kimoja cha siasa kwenda chama kingine. Kuhama imekuwa sehemu ya siasa za Tanzania.
Huwezi kusikia matukio makubwa ya kisiasa sasa kama mikutano mikubwa au midahalo ya kutafuta suluhu za matatizo ya nchi. Habari zote ni fulani kahama pale kahamia hapa.
Baadhi ya wanasiasa ambao walihama vyama vyao vya awali miaka miwili iliyopita ndiyo waliorudia safari hii.
Maulid Mtulia aliyekuwa Mbunge wa Kinondoni wiki mbili zilizopita hayupo tena CUF sasa ni kada wa chama tawala na ubunge wake umetoweka. Lazaro Nyalandu moja ya makada maarufu wa CCM na aliyekuwa Waziri wa Maliasili na Utalii wa Serikali ya awamu iliyopita naye ameshahamia Chadema.
Wakati unatafakari ni kiongozi gani wa chama au wa kuchaguliwa kutoka ngazi ya tawi hadi Taifa atakayehama kesho, zipo fununu kuwa kuna wabunge wengine watavitema vyama vyao hivi karibuni kwenda kwingine.
Hata hivyo, tofauti na miaka ya nyuma aina ya kuhama kwa sasa kuna nyanja nyingi za kutazama ili kupata mustakabali wa siasa na ukuaji wa demokrasia na maendeleo ya nchi. Baadhi ya mambo ya awali kuyaangazia ni sababu za kuhama, aina ya watu wanaohama na athari wanazoziacha kwa Taifa.
Kipindi wanachohama
Kulikuwa na utamaduni wa miaka ya hivi karibuni kwa watu kuhama vyama baada ya kutokea msigano ndani ya chama ama baada ya majina yao kukatwa katika kuwania nafasi fulani. Kama siyo hivyo basi mwanasiasa huyo ameng’olewa kwa tuhuma mbalimbali kama usaliti.
Pia kuna aina ya kuhama tuliishuhudia mwaka 2015 wakati wa Uchaguzi Mkuu baada ya vigogo kuhama vyama. Kumbukumbu kubwa ni uamuzi mawaziri wakuu wastaafu Edward Lowassa na Frederick Sumaye kuhamia Chadema.
Sehemu kubwa hawa walionekana wazi kuumizwa na mchakato wa uchaguzi. Kulikuwa na watu wengi wa aina hii waliohama vyama vyao au kuachana navyo bila kuhamia sehemu nyingine kama ilivyokuwa kwa Dk Willibrod Slaa aliyetangaza kuachana kabisa na siasa.
Lakini, safari hii wanasiasa wanahama katikati ya safari ikiwa ni miaka miwili baada ya uchaguzi.
Mbaya zaidi wapo wanaohama wakiwa na vyeo vyao vya kuchaguliwa, jambo linalofanya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kuitisha uchaguzi mdogo.
Sababu za kuhama
Ukiwasikiliza wengi waliokuwa wanahama CCM wakati huo ilikuwa ni kwamba kulikuwa na ufisadi uliokithiri na kwamba kwa mfumo uliokuwapo wasingeweza kufanya mabadiliko wakiwa ndani. Ilikuwa ndiyo sababu kuu ambayo hadi sasa imebaki.
Wachache waliokuwa wakiondoka vyama vya upinzani walijitetea kutokuwepo mfumo imara wa kiuongozi ndani ya vyama.
Hata hivyo, ukichambua kwa kina kwa sasa wanaohamia CCM kutoka upinzani wana sababu zinazofanana kana kwamba kuna mtu kaandika barua ya mfano ambayo wote wanapaswa kuifuata.
Sehemu kubwa ya wanaobwaga manyanga kutoka vyama vya upinzani wamevutiwa zaidi na utendaji wa Serikali ya Rais John Magufuli.
“Nimebaini kuwa Serikali ya CCM inafanya kazi kubwa ya kutekeleza Ilani na imefanya vizuri katika mambo mengi ambayo sisi upinzani tuliahidi kuyatekeleza,” alisema Mtulia wakati wa kujiuzulu.
Athari kwa Taifa
Moja ya maswali mengi ambayo huenda wengi wanajiuliza ni iwapo kuhamahama kuna faida kwa Taifa.
Jambo la msingi hapa la kufahamu katika suala hili ni kwamba kuhama kupo kikatiba. Ibara ya 20 (1) ya Katiba ya mwaka 1977 inaeleza uhuru wa “mtu kukutana na watu wengine kwa hiari yake na kwa amani, kuchanganyika, kushirikiana na watu wengine na kwa ajili hiyo kutoa mawazo yake hadharani na kuanzisha na kujiunga na vyama au mashirika yaliyoanzishwa kwa madhumuni ya kuhifadhi au kuendeleza imani au masilahi yake au mengineyo.”
Kwa muktadha huo kuhama chama si dhambi na wala si kosa kwa kuwa ni uhuru wa mtu kujiunga na chama anachotaka.
Suala la msingi ni iwapo kuhama huko kutakuwa na tija katika kujenga msingi wa demokrasia hususan ndani ya chama na iwapo kutahusisha gharama ambazo zitafanya Serikali itumie fedha za walipakodi.
Je, kasi ya watu kuhama vyama vya siasa ina tija kwa mustakabali wa siasa nchini? Hili ni swali linalohitaji mjadala. Hata hivyo, kuna haja ya kufanya utafiti wa kina kuona kama vyama vinanufaika na watu hao wanaohamia.
Ukiachana na sifa za kisiasa ambazo vyama vinavyowapokea watu huzipata, kuna maswali ya msingi yanayoweza kusaidia utafiti huo.
Mosi, watu wote waliohama vyama baada ya kuhamia kwenye vyama vipya walifanya nini? Ni wangapi wamesaidia mabadiliko na wangapi waliendelea kuwa mizigo?
Je, wote wana sifa kama za Zitto aliyeanzisha ACT na kuwaletea kiti cha kwanza cha ubunge au enzi za John Shibuda ambaye alipata ubunge baada ya kuhamia Chadema akitoka CCM?
Mbali na mchango wa ndani ya chama, walifanya nini katika kukuza demokrasia na maendeleo ya nchi baada ya kuingia kwenye chama kipya.
Mchango wa David Kafulila akiwa mwanachama na mbunge wa NCCR-Mageuzi wa kuchochea uwajibikaji katika sakata la Akaunti ya Tegeta Escrow, ulifanana na alipokuwa Chadema? Ndani ya chama chake kipya—CCM Kafulila ataweza kuibua au kuchochea uwajibikaji?
Vipi kuhusu Nyalandu kuingia Chadema. Kama alishindwa kushawishi mabadiliko akiwa moja ya vigogo ndani ya chama tawala, ataweza kuchochea mabadiliko ya kitaifa akiwa upinzani ambao kwa sasa wanasubiri mikutano ya uchaguzi mdogo au mikutano na wanahabari kupaza sauti zao?
Kujadili mwenendo wa wanaohama vyama kwa sasa bila kujibu sehemu ya maswali kama hayo ni kujifanya tunaona wakati tupo gizani. Tusipokuwa makini huenda ikawa chachu ya kuua vyama na demokrasia siku zijazo iwapo utafiti wa kina hautafanyika.
Ukiachana na manufaa ya wanaohama kwa chama na Taifa, kuna gharama za ziada ambazo walipa kodi tunaziingia ili kutimiza matakwa ya watu tulioamini wanaweza kutuongoza.
Kwa bahati mbaya sheria zinatutaka tuwachague wakitokea kwenye vyama na hii ni kwa sababu Katiba hairuhusu mgombea binafsi. Hii ina maana kuwa kiongozi wa kuchaguliwa aliyepoteza sifa za uanachama wake basi na yale madaraka tuliyomuamini nayo yametoweka.
Vyama vimekuwa na nguvu kuamua hatma ya wale tuliyowachagua. Matokeo yake Taifa limekuwa likiingia kwenye uchaguzi mdogo kwa sababu tu kiongozi fulani aliondolewa kwa hila na chama chake au kaamua kubwaga manyanga.
Kuna kila dalili kwa sasa, sababu hii inatumika kuwashawishi wanasiasa kuachana na vyama vyao ili kushawishi uchaguzi mdogo kwa kuwa ndiyo kipimo kipya cha vyama vya siasa.
Mwenendo huu umesababisha madiwani wengi kuhama kutoka Chadema wakiwamo watano kutoka Wilaya ya Meru na Monduli mkoani Arusha.
Wakazi wa Meru wamepoteza madiwani wengi nchini kwa mfumo huo wa kuhama chama katikati ya safari. Kumekuwapo na tuhuma za kununuliwa ambazo Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) inachunguza.
Lakini, ukiachana na viongozi wanaofariki au kushindwa kuendelea na majukumu kutokana na ugonjwa, wanaohama vyama wanawanyonya walipakodi bila sababu ya msingi.
Serikali inaingia gharama kubwa za uchaguzi mdogo kwa sababu yao. Katika uchaguzi mdogo wa madiwani uliofanyika katika kata 43 hivi karibuni, NEC ilibainisha kuwa ilitumia Sh2.5 bilioni kuukamilisha.
Kwa mujibu wa Mkurugenzi wa NEC, Kailima Ramadhani ni kwamba msingi wa bajeti huo unatokana na vituo vya kupigia kura na idadi ya wapiga kura waliojiandikisha.
Katika uchaguzi huo, ulioisha kwa rabsha katika baadhi ya maeneo nchini kwa baadhi ya watu kujeruhiwa katika vurugu, kulikuwa na vituo vya kupigia kura 884 na wapiga kura 333,309.
Kama uchaguzi mdogo wa udiwani wa kata 43, Serikali ilitumia Sh2.5 bilioni je ni fedha kiasi gani zitatumika kugharamia uchaguzi mdogo katika majimbo ya Kinondoni, Singida Kaskazini na mengineyo ambayo kuna fununu wabunge wake watahama vyama?
Sh2.5 bilioni ni nyingi kwa hali ya sasa ya kiuchumi na hazitakiwi kufujwa bila sababu za msingi. Ni busara kufanya uchaguzi mdogo kwa matukio makubwa kama ya kifo au ugonjwa ambayo hayawezi kuzuilika.
Fedha hizo zingesaidia kununua dawa katika vituo vya afya au kujenga visima katika maeneo yenye uhaba mkubwa wa maji kama Nachingwea mkoani Lindi.
Gharama hizo siyo tu kwa walipakodi bali hata vyama na wagombea wenyewe. Fedha ambazo zingetumika kufanya maendeleo ndani ya chama na kwa wagombea wenyewe zinaishia kugharamia chaguzi za mara kwa mara ambazo msingi wake huenda ni wa kutimiza matakwa ya kisiasa zaidi kuliko kujenga mustakabali wa nchi.
Kuna baadhi watasema demokrasia ni gharama. Ndiyo ni gharama lakini siyo gharama zinazosababishwa kizembe kama za diwani kuchaguliwa leo na kuondoka kesho kwa kutoa sababu za kizembe.
Vyama vyenyewe vinaumia kwa aina hii ya siasa kama ambavyo CUF imeonyesha.
“CUF haikutarajia kuingia katika uchaguzi mdogo hasa jimbo la Kinondoni kabla ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020 labda kingetokea kifo. Tunawaomba radhi wakazi wa Kinondoni,” Mkurugenzi wa Habari, Uenezi na Mawasiliano ya Umma wa CUF, Abdul Kambaya aliwaambia wanahabari baada ya Mtulia kujiondoa katika chama chao.
Kama hakutakuwa na uchunguzi wa kina kwa wanaohama, huenda Taifa likajikuta kila baada ya miezi mitatu linafanya uchaguzi mdogo kwa kuwa ndiyo itakuwa kipimo kipya cha umaarufu wa kisiasa.
Hata hivyo, kuna njia za kutokomeza tabia hii ya watu kuhamahama kila siku hasa viongozi wanaoongeza gharama kwa Serikali.
Mosi, tumalizie mchakato wa Katiba Mpya. Katiba mpya inaweza kupunguza gharama hizi za kuitisha uchaguzi kwa kuwa mtu kajitoa kwenye chama iwapo itaruhusu mgombea binafsi na kuweka masharti rafiki ya watu kutopoteza nafasi zao hata baada ya kuhama vyama.
Jambo jingine ni kuacha fikra za siasa ya kubomoana na kukomoana. Siasa za kuchekelea kuwa tumeng’oa ‘injini’ muhimu huku mkiwaumiza wananchi, siyo rafiki na hazifai kuwepo kwenye Taifa la wastaarabu kama Tanzania.
Sehemu kubwa wanaohama inaonekana kama ni matokeo ya kwamba tuwakomoe wapunguze viti vya udiwani au ubunge.
Matokeo yake hata huo uchaguzi mdogo uliofanyika hivi karibuni haujawa na matokeo mazuri kwa demokrasia kutokana na kuwa na mwitikio mdogo na vurugu zilizojitokeza ikiwemo baadhi ya watu kukatana mapanga.
CCM au upinzani wanaweza wakawa wamepata viti vya udiwani katika uchaguzi huo uliopita lakini makovu na majeraha walioyapata Watanzania hao hayafutiki kirahisi na huenda yamezigharimu familia zao. Siasa za namna hii ni mbaya na hazifai kwa kushabikiwa hata kidogo.
Tanzania inaweza kusonga mbele katika siasa ya maendeleo iwapo siasa itafanywa kwa kufuata misingi imara ya demokrasia.

Benki ya Kilimo lawamani kwa kutokopesha wakulima


Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage amelaumu uongozi wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) kwa kutunza fedha badala ya kuwakopesha wakulima.
Akifungua mkutano wa wadau wa kilimo leo Jumatano Desemba 6,2017, Mwijage amesema benki hiyo ina mabilioni ya fedha lakini kasi ya kuwakopesha wakulima ni ndogo.
“Rais John Magufuli ameuliza wakati nikiwepo ni kwa nini mabilioni ya fedha hayakopeshwi kwa wakulima,” amesema Mwijage.
Amesema Serikali imekuwa ikikopa kwa riba kwa ajili ya kuwekeza katika benki hiyo lakini yenyewe inakaa na fedha.
“Benki imekuwa mtunzaji wa fedha badala ya kuwa mkopeshaji,” amesema Mwijage.
Waziri amesema benki hiyo imekuwa ikisema ina hofu kwamba wakopaji hawawezi kurejesha mikopo.
Amesema hayo baada ya Mwenyekiti wa Baraza la Kilimo Tanzania (ACT), Dk Yusuph Sinare kumwomba Mwijage kufikisha kilio cha wakulima kwa Serikali kutaka benki hiyo iongezewe uwezo wa kukopesha.
Mwijage amesema mpango wa Serikali wa ujenzi wa viwanda utasaidia wakulima kupata masoko ya mazao yao.
Amesema wakulima wanatakiwa kuungana kujenga viwanda vidogo vya kusindika mazao ili kuyaongeza thamani.
“Kiwanda cha kusindika nyanya kinagharimu Sh200 milioni, hivi wakulima tunashindwa kuungana na kuanzisha viwanda vya namna hii,” amehoji Mwijage.
Amewataka kuachana na dhana iliyojengeka kwamba, wakulima kazi yao itaishia katika kilimo tu bali wanaweza pia kujenga viwanda.
Mwijage amezitaka mamlaka za Serikali kuacha kufanya kazi kipolisi bali zielimishe wawekezaji na si kuwatisha. “Kuna mwekezaji alitishwa na watu wa mazingira kwamba asipofuata sheria ya mazingira atafungwa jela miaka saba.”
Mwenyekiti wa ACT, Dk Sinare amesema wakulima hawawezi kuwa na nguvu kama hawana benki imara. “Tunaiomba Serikali iiongezee nguvu benki ya wakulima iweze kutoa mikopo kwa wakulima.”
Kuhusu masoko ya mazao, amesema wakati umefika kwa Serikali kuhifadhi chakula cha kutosha na wakulima kuruhusiwa kutafuta masoko ya mazao popote pale duniani.
Mwenyekiti mstaafu wa bodi ya ACT, Salum Shamte amewataka wakulima kutokuwa wazalishaji wa malighafi bali wabadilike na kuyaonge