Friday, October 27

PITIA VICHWA VYA HABARI KATIKA MAGAZETI YA LEO OKTOBA 27,2017

Tigo Kukabidhi Nyenzo za Kidigitali shule ya sekondari wasichana Machame


Mkuu wa Wilaya ya Hai, Gelacius Byakanwa akikata utepe kuzindua rasmi maabara yenye nyenzo za elimu ya kidigitali ya Tigo eSchools kwa shule ya sekondari  wasichana Machame jana. Kulia ni Kaimu Mkurugenzi wa Tigo kanda ya kaskazini, Henry Kinabo.

Mkuu wa wilaya ya Hai, Gelacius Byakanwa (aliyekaa kulia)akipata maelezo ya matumizi ya kujisomea vitabu kwa njia ya mtandao kupitia Tigo eSchools toka kwa mwanafunzi wa shule ya sekondari wasichana Machame, Delynes Laurian mara baada ya kampuni ya Tigo kukabidhi huduma hiyo shuleni hapo jana.

Mtaalam wa tovuti toka Shule Direct, Emmanuel George akielezea jambo kwa mkuu wa wilaya ya Hai mkoani Kilimanjaro, Gelacius Byakanwa wakati wa uzinduzi wa Tigo eSchools shule ya wasichana Machame leo. Wengine nyuma kushoto Kaimu Mkurugenzi wa Tigo kanda kaskazini, Henry Kinabo, mwalimu mkuu wa shule ya Machame, Asteria Massawe

Umati wa wanafunzi wa  shule ya wasichana Machame Machame wakiwa wanashuhudia uzinduzi wa Tigo eSchoolsl mapema jana.

SERIKALI YAELEZA INAVYOTUMIA FEDHA ZA MIKOPO


SERIKALI imesema kuwa inatumia mikopo inayoipata kutoka kwa wadau wa maendeleo kwenye miradi ya uzalishaji na miundombinu ili iweze kuwa na tija kwa jamii.
Hayo yamesemwa jana Dar es Salaam na Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Philip Mpango, alipokutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Sweden nchini, Katarina Rangnitt.
Alisema Serikali imejipanga kulipa madeni kwa wadau mbalimbali baada ya kuhakikiwa.
Hata hivyo, alisema kuwa hatua za kukopa zitaangaliwa kwa umakini mkubwa ili kuzuia kuwa na madeni ambayo hayana tija kwa wananchi na Serikali.
“Katika kuhakikisha Serikali inaendelea kuwahudumia wananchi ipasavyo, kumekuwa na mikakati ya kuwaongezea watumishi ujuzi ili kuendana na kasi ya maendeleo, kuelekea uchumi wa kati kwa kuwa tuna uhaba wa watu wenye ujuzi wa kutosha, hivyo ni vyema wadau wa maendeleo wakalitazama hilo ili kusaidia katika kuharakisha ukuaji wa uchumi.
“Siwezi kuwa Waziri wa Fedha ikiwa sitakuwa na wafanyabiashara, kwa kuwa wao ndio wanaolipa kodi zinazosaidia kuendesha nchi,” alisema Dk. Mpango.
Akizungumzia kuhusu utekelezaji wa demokrasia na haki za binadamu, alisema kuwa mambo hayo yapo katika katiba, hivyo Serikali inaifuata na kuiheshimu, na kwamba haki za binadamu zinafuatwa kwa mujibu wa sheria.
Hata hivyo, alieleza kuwa ni vema tamaduni za Mtanzania zikaendelea kuheshimiwa wakati wa utekelezaji wa makubaliano ya ushirikiano wa maendeleo.
Alitoa wito kwa jamii kuendelea kutangaza mazuri yanayojitokeza nchini, yakiwamo ya kukua kwa uchumi kwa kuwa Tanzania itajengwa na Watanzania.
“Inashangaza kuona baadhi ya watu wakieleza mabaya tu ilihali kuna mafanikio mengi yaliyopatikana, tunakaribisha ukosoaji, lakini wenye tija,” alisema Dk. Mpango.
Alisema Serikali inafanya jitihada za dhati kuhakikisha kuna mazingira bora ya biashara na ili kufikia huko, kumekuwa na majadiliano ya mara kwa mara na wafanyabiashara nchini na kwamba kero zao nyingi zimetatuliwa ikiwamo kupungua kwa wingi wa kodi.
Kwa upande wake Balozi Rangnitt alisema kuwa nchi yake ina nia ya kusaidia kukuza sekta ya nishati na tayari mazungumzo na wizara husika yameanza.
Alisema kuna umuhimu wa sekta binafsi katika kukuza uchumi wa nchi.
Balozi huyo alisema nchini mwake wafanyabiashara wanachangia pato la ndani kwa asilimia 50 kwa kuwa kuna biashara huria.

KAMATI YA BUNGE YA BAJETI YAKUTANA MJINI DODOMA LEO


Wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Bajeti wakiwa katika kikao cha Kamati hiyo Mjini Dodoma ambapo walikuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Bajeti, Mheshimiwa Hawa Ghasia akiongoza kikao cha Kamati hiyo kilichofanyika Mjini Dodoma ambapo leo imekutana na Taasisi ya Sekta Binafsi kujadili kuhusu vyanzo vya mapato ya Serikali na mapendekezo ya hatua za kupunguza utegemezi wa kibajeti kwa mwaka 2018/19
Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Bajeti, Mheshimiwa Hawa Ghasia akiongoza kikao cha Kamati hiyo kilichofanyika Mjini Dodoma ambapo leo imekutana na Taasisi ya Sekta Binafsi kujadili kuhusu vyanzo vya mapato ya Serikali na mapendekezo ya hatua za kupunguza utegemezi wa kibajeti kwa mwaka 2018/19
Mjumbe wa Kamati ya Bajeti, Mheshimiwa Janeth Mbene akichangia jambo katika kikao cha Kamati hiyo kilichofanyika Mjini Dodoma, Kamati Bajeti 3 ambapo leo imekutana na Taasisi ya Sekta Binafsi kujadili kuhusu vyanzo vya mapato ya Serikali na mapendekezo ya hatua za kupunguza utegemezi wa kibajeti kwa mwaka 2018/19.

KUKATIKA KWA UMEME NCHI NZIMA: DKT. KALEMANI AWAOMBA RADHI WANANCHI


NA K-VIS BLOG/Khalfan Said
WAZIRI wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani, (pichani juu), amewaomba radhi wananchi kufuatia kukatika kwa umeme nchi nzima Oktoba 25 na 26, 2017 kulikosababishwa na hitilafu kwenye mfumo wa Gridi ya Taifa.
Dkt. Kalemani amabye alikuwa mjini Dodoma akishiriki vikao vya kamati za bunge, alilazimika kusafiri mapema leo asubuhi Oktoba 26, 2017 kuja jijini Dar es Salaam ili kufuatilia juhudi za kurekebisha tatizo hilo.

"Ndugu wananchi hali ilivyotokea sisi kama Shirika la TANESCO na Serikali tunawataka radhi wananchi kwa matatizo yaliyotokea lakini niseme tu kwamba kuna hatua madhubuti zinazochukuliwa hivi sasa kurekebisha hali hiyo ili wananchi muendelee kupata umeme wa uhakika." Alisema Dkt. Kalemani katika taarifa yake kwa wananchi aliyoitoa makao makuu ya Wizara jijini Dar es Salaam baada ya ziara yake ya kutembelea kituo cha udhibiti cha Gridi ya Taifa, (GCC), kilichoko Ubungo na kituo cha kufua umeme wa gesi cha Kinyerezi1 jijini  Dar es Salaam.

Taarifa za awali zilieleza kuwa kukatika kwa umeme kulisababishwa na "Gridi kuchomoka" Oktoba 25, 2017 majira ya saa 10;08 alfajiri na kurejea saa 12:09 asubuhi ambapo umeme ulirejea mikoa yote isipokuwa Zanzibar, ingawa juhudi za mafundi wa TANESCO ziliwezesha umeme kurejea Zanzibar majira ya saa 1 asubuhi.

Hata hivyo tatizo hilo lilirejea tena majira ya saa 12:30 jioni siku hiyo hiyo ya Oktoba 25, 2017, ambapo takriban mikoa yote iliathirika. Umeme ulirejea tena majira ya saa 3 usiku lakiji ilipofika Oktoba 26, 2017 majira ya saa 12:03 tatizo hilo likajirudia tena na kuathiri takriban mikoa yote ikwiemo Zanzibvar.

"Nimekuja kutoka Dodoma ili kuona nini kimetokea, nini kimesababisha na hatua gani za haraka zichukuliwe ili kuondoa tatizo hilo hii ndio hasa dhamira ya safari yangu." Alisema Dkt. Kalemani baada ya kufika kwenye kituo cha udhibiti Gridi ya Taifa, Ubunmgo.

Lakini niwapongeze TANESCO kwa kutoa taarifa mapema kwa wananchi kuwajulisha kuhusu tatizo hilo, alisema. Akifafanua zaidi Dkt. Kalemani alisema, chanzo cha tatizo ni pamoja na mfumo wenyewe (GCC) na bado unafanywiwa marekebisho na taratibu zinaendelea, na kule Kinyerezi kuna mashine moja haifanyi kazi nayo inafanyiwa marekebishiom ikiwa ni pamoja na valvu moja iliyoharibika nayo pia inafabnyiwa kazi.

"Gridi ya taifa imerejea tangu jana usiku (Oktoba 25), na umeme unapatikana nchi nzima lakini hata hivyo yapo maeneo machache ambayo hayapati umeme wa kutosha kwa sababu mtambo mmoja wa Ubungo namba mbili wenye jumla ya megawati 129 haujaanza kufanya kazi na nimeelekeza wataalamu wafanye kazi usiku na mchana na wamenihakikishia kufikia saa 5 asubuhi kesho  (Oktoka 27), mtambo huo utaanza kufanya kazi na umeme utarejea katika hali yake ya kawaida." Alibainisha.

Dkt. Kalemani akiwa kwenye kituo cha udhibiti wa Gridi ya Taifa (GCC), Ubungo jijini Dar es Salaam.
 
Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, anayeshughulikia uzalishaji (Generation), Mhandisi Abdallah Ikwasa, (kushoto), akimpatia maelezo Waziri Dkt. Kalemani alipotembelea mitambo ya kufua umeme ya Kinyerezi 1 jijini Oktoba 26, 2017. Wakzanza kulia ni Naibu Katibu Mkuu Nishati, Dkt. Juliana Palagyo.
 
Meneja Mwandamizi wa TANESCO, anayeshughulikia uzalishaji, Mhandisi Costa Rubagumya akifafanua jambo. 
 
Meneja wa udhibiti ifumo ya Gridi ya Taifa (Protection), Mhandisi Izahaki Mosha, akimfafanulia Waziri Dkt. Kalemani (kushoto). 
 
Dkt. Kalemani (kushoto), akiwa kwenye chumba cha udhibiti cha Kinyerezi 1 akifafanua jambo.

Uhuru Kenyatta apiga kura akijivunia demokrasia


Dar es Salaam. Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya, amepiga kura ya marudio ya urais  akisema Taifa hilo limeonyesha mfano wa kidemokrasia barani Afrika. 
“Ujumbe wangu ni kwamba Kenya inaimarika kidemokrasia. Kenya imethibitisha kuwa inaweza kwenda kwenye uchaguzi wa urais, ukafutwa na ikakubalika na kisha Wakenya wakapata nafasi ya kurudi,” amesema Rais Uhuru leo Alhamisi Oktoba 26,2017 alipojibu maswali ya waandishi wa habari baada ya kupiga kura.
“Tunatakiwa wote twende mbele. Sisi Wakenya tunakwenda mbele baada ya Wakenya kutumia haki yao kidemokrasia,” amesema.
Amewataka Wakenya kutowabughudhi maofisa wa Tume ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC), kwa sababu wameruhusiwa kusimamia uchaguzi ambao kila Mkenya ana haki ya kushiriki.
Rais Uhuru amepiga kura katika kaunti ya Kiambu eneo la Gatundu akisindikizwa na mkewe, Margaret Gakuo.

Mvua yasimamisha shughuli


Dar es Salaam. Mvua zinazoendelea kunyesha jijini Dar es Salaam zimesababisha baadhi ya nyumba na vituo vya mafuta eneo la Tegeta Nyaishozi kufunikwa na maji.
Pia, zimesababisha mali za wakazi wa maeneo hayo kusombwa na maji usiku wa kuamkia leo Alhamisi Oktoba 26,2017.
Mvua bado inaendelea kunyesha na imesababisha mitaro na barabara katika maeneo mengi kujaa maji.
Katika eneo la Tegeta Nyaishozi wananchi wamekuwa wakihangaika kutoa maji katika nyumba zao na barabara hazipitiki kutokana na kujaa maji. Mbali na hayo, hakuna  huduma za kijamii  zinazopatikana.
Akizungumza na Mwananchi mkazi wa Tegeta Nyaishozi, Abuu Magessa amesema mvua imesababisha maafa na hawajui cha kufanya.
"Tumekaa tu, maji yameingia hadi ndani magari yanaelea," amesema.
Mkazi mwingine wa eneo hilo, Said Juma amesema eneo la Ushenzini halipitiki. "Vitu vimelowa vikiwa ndani wananchi wameshindwa kuvitoa, wamebaki wanaviangalia," amesema.
Hayo yakitokea Tegeta, katika daraja la Mbezi Mwisho maji yamejaa hivyo kusababisha magari kushindwa kupita. Madereva wanalazimika kutumia njia ya Goba.
Kutokana na nguvu ya maji, gari la abiria linalofanya safari kati ya Mbezi Mwisho - Makumbusho limesombwa.
Hata hivyo, imeelezwa hakuna mtu aliyedhurika kwa kuwa wote wametoka kwa kupitia madirishani.

UCHAMBUZI: Kwa tabia hii ya uchomaji moto nguzo tusitarajie umeme wa uhakika nchini



Lilian Timbuka 
Lilian Timbuka  
Hivi karibuni kuna taarifa zilizotolewa na Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) kwamba kuna baadhi ya watu wasiojulikana wanachoma moto misitu na kuharibu miundombinu ya umeme inayojengwa na shirika hilo nchini.
Uharibifu huo umeripotiwa katika mikoa ya Njombe, Ruvuma, Lindi na Mtwara.
Lakini pia, uharibifu huo umebainika kufanyika mkoani Rukwa katika Msitu wa Kirando wilayani Nkasi.
Kaimu Meneja Uhusiano wa Tanesco, Leila Muhaji, anasema uharibifu huo mkubwa wa miundombinu unaathiri upatikanaji wa umeme kwa wateja wa mikoa hiyo wanaopata huduma ya umeme ya njia ya msongo mkubwa.
Mbali ya kukosa huduma, Leila anasema miundombinu hususan nguzo nyingi zinateketea na kusababisha hasara kubwa.
Binafsi nadhani ifike mahali sasa wananchi wote waishio kwenye maeneo hayo wazionee uchungu fedha zao za kodi ambazo zinatumika pia kujenga miundombinu hiyo ya umeme pamoja na kuiokoa kwa manufaa yao na ya Taifa.
Tanesco nao wavitumie ipasavyo vyombo vya ulinzi na usalama vya mikoa kuwabaini wahusika ili wachukuliwe hatua stahiki kwa mujibu wa sheria.
Kwani kuharibiwa kwa miundombinu hiyo ambayo mingine ni mipya kama ile ya Mradi wa Makambako Songea ni kurudisha nyuma maendeleo ya nchi.
Kwa mfano katika mikoa ya Njombe na Ruvuma, moto unaounguza nguzo hizo unadaiwa kusababishwa na shughuli za kibinadamu za kuandaa mashamba. Nadhani wataalamu wa kilimo nao waanze sasa kutoa elimu ya uandaaji bora wa mashamba badala ya wakulima kutumia njia ya uchomaji moto, watumie njia nyingine mbadala.
Hivi karibuni, baadhi ya wahariri wa vyombo vya habari waliotembelea Mradi wa Umeme wa Makambako Songea walishuhudia nguzo takribani 19 zikiwa zimeunguzwa huku baadhi zikiwa zimebakia nyaya tu ziking’inia kando ya Barabara ya Songea-Mbinga kwenye Kijiji cha Lipokela.
Sasa vitendo kama hivi vinasikitisha na kutia uchungu. Umefika wakati kwa wananchi kuacha tabia hiyo kwani miradi hii ya umeme inayojengwa kwa kutumia gharama kubwa, inalenga kubadilisha maisha ya wananchi na Taifa kiuchumi.
Kwani kufanya uharibifu huo ni sawa na kuhujumu jitihada za Shirika la Tanesco linalofanya kazi kwa niaba ya Serikali kutatua changamoto ya upatikanaji wa umeme wa uhakika nchini.
Utamaduni huu wa wananchi mkoani Ruvuma na Njombe wa kuchoma moto nyasi na misitu kwa nia ya kutayarisha maeneo ya kilimo haina tija na ni bora wakaiacha kabisa.
Nilifurahi hivi karibuni nilipomsikia Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Dk Binilith Mahenge alizungumzia vitendo hivyo na kuwaagiza viongozi wa serikali kwenye kata na vijiji kuwaelimisha wananchi kuhusu madhara ya vitendo hivyo.
Litakuwa jambo la busara kama viongozi wote wa mikoa wakaweka utaratibu wa kulinda miundombinu hiyo badala ya kulalamika mara umeme unapokatika kwenye maeneo yao bila kujua chanzo cha ukatikaji huo. Hivi karibuni pia ilielezwa kuwa nguzo 101 za umeme ziliteketezwa na kusababisha hasara ya Sh. milioni 121, kutokana na kuwapo kwa vitendo vya uchomaji moto ovyo, vinavyofanywa na baadhi ya wananchi, katika maeneo mbalimbali mkoani Kagera.
Ofisa Mazingira wa Mkoa wa Kagera, Haji Kiselu, alisema jana kuwa nguzo zote hizo zimechomwa moto mwaka huu. Anasema uchomaji huo wa moto unatokana na kutosimamiwa vyema kwa sheria ya mazingira namba 20 ya mwaka 2004, ambayo inaelekeza uundwaji wa kamati kuanzia ngazi za vijiji.

Dawa za kulevya za Sh5 bilioni zakamatwa kwenye jahazi Dar


Mwanza. Maofisa wa Mamlaka ya Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) wakishirikiana na vyombo vingine vya ulinzi na usalama usiku wa kuamkia juzi walikamata zaidi ya kilo 100 za mihadarati aina ya heroin zilizokuwa zikisafirishwa kwenye jahazi kutoka Unguja kwenda Dar es Salaam.
Maofisa hao wa nchini wakishirikiana na vyombo vingine vya kimataifa walilitilia shaka na kuamua kulizuia jahazi hilo lililokuwa na raia kumi wa Iran na Wazanzibari wawili.
Kamishna wa sheria wa DCEA, Edwin Kakolaki amesema baada ya upekuzi wa awali walifanikiwa kukamata paketi 104 za dawa wanazoshuku kuwa ni heroin ambazo watazipeleka ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali kwa vipimo.
“Tunaendelea na ukaguzi wa jahazi na sasa tumepeleka mbwa kusaidia kazi hiyo,” alisema Kakolaki.
Hadi jana jioni maofisa wa DCEA walikuwa wakifanya upekuzi kwa kusaidiwa na mbwa wanusaji kuona kama kuna mizigo zaidi.
Habari zaidi zinasema baada ya kuona wamezungukwa, raia hao wa Iran walijaribu kubadili mwelekeo, lakini walizidiwa nguvu na kuanza kutupa baadhi ya mizigo kwenye maji ya Bahari ya Hindi.
Kamishna Mkuu wa DCEA, Rodgers Siyanga amesema kiwango hicho cha dawa kingekuwa kikubwa zaidi isingekuwa kitendo cha watu hao kutupa kiasi kingine baharini.
“Nasema vyombo vya dola viko imara kupambana na usafirishaji wa dawa za kulevya na hatutaacha kuyadhibiti magenge na mitandao yao. Kwa hiyo mtu yeyote anayepanga kuingiza dawa za kulevya ni vema ajiulize mara mbili na aache, tutampata tu,” alisema Siyanga.
Meli iliyotumika katika operesheni hiyo ya usiku wa manane ilitumika pia kulivuta jahazi hilo na kulifikisha Bandari ya Dar es Salaam juzi saa nne usiku.
Ofisa mwingine aliyeshiriki operesheni hiyo alisema baada ya kukamatwa raia hao wa Iran walijitetea kuwa wao ni wavuvi. “Tulipowabana wakadai wanakwenda nchini Somalia kusaka chombo cha wenzao walichodai kutaarifiwa kimeharibika huko.”
Imeelezwa pia kuwa Wazanzibari wawili waliokutwa kwenye meli hiyo walijitetea kuwa wao walitumwa tu kupeleka chakula katika jahazi hilo.
Raisi John Magufuli aliwahi kusema Serikali yake haitakuwa na huruma na watu wanaojihusisha na biashara ya dawa za kulevya ambazo zimeharibu nguvu kazi ya Taifa kwa kiasi kikubwa.
Akiamuapisha Siyanga mwezi Aprili, Rais Magufuli alisema, ‘isingekuwa sheria imesema, yeye mwenyewe angekuwa mwenyekiti badala ya waziri mkuu’, huku akimtaka Kamishna Siyanga kufanya kazi bila woga.

Chadema kuitumia Mahakama kumtoa mkurugenzi wake mahabusu


Dar es Salaam. Baada ya Polisi kuendelea kumshikilia Mkurugenzi wa Chadema wa Operesheni na Mafunzo, Kigaila Benson chama hicho kimesema kimekwenda Mahakama Kuu kuiomba itoe amri kwa jeshi hilo kumfikisha kortini.
Wakati Chadema ikisema hayo, Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa akizungumza na Mwananchi leo Alhamisi Oktoba 26,2017 amesema, “Upelelezi unaendelea na huenda kesho akafikishwa mahakamani.”
Kigaila anashikiliwa na polisi tangu Jumatatu Oktoba 23,2017 aliporipoti Kituo Kikuu cha Polisi cha kanda hiyo kuitikia wito wa jeshi hilo.
Taarifa ya Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano ya Chadema, Tumaini Makene iliyotolewa leo Oktoba 26,2017 imesema baada ya kumaliza mahojiano, askari kutoka Ofisi ya Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai Kanda Maalumu ya Dar es Salaam (ZCO), waliokuwa wakimhoji Kigaila walisema hawana mamlaka ya kumwachia kwa dhamana.
Makene amesema sababu waliyoitoa ni kwamba wakubwa na wenye mamlaka ya kuruhusu dhamana au kutoa dhamana hawakuwepo ofisini.
“Juhudi za mawakili waliokuwepo polisi kumpatia Kigaila msaada wa kisheria, kueleza kuwa dhamana ni haki yake kwa mujibu wa sheria, huku wakihoji ni kwa nini kusifanyike mawasiliano ili hao wakubwa watoe ruhusa hiyo hata kama wako nje ya ofisi, hazikufua dafu!” amesema Makene.
Amesema tuhuma alizohojiwa Kigaila zilihusu kauli za uchochezi anazodaiwa kuzitoa Septemba 12,2017 siku chama hicho kilipotoa tamko la maazimio ya kikao cha dharura cha Kamati Kuu iliyoketi kujadili tukio la kushambuliwa na kujeruhiwa  mwanasheria wa Chadema, Tundu Lissu.
Makene amesema kwa kuitikia wito wa Jeshi la Polisi na kwenda mwenyewe kituoni, ni sababu inayojitosheleza kuonyesha kuwa Kigaila ni mwaminifu na anatoa ushirikiano kwa sheria za nchi.
“Bila kumfikisha mahakamani au kumwachia huru, tafsiri yake ni kwamba Kigaila anashikiliwa na jeshi hilo kinyume cha sheria za nchi,” amesema.
Amesema Chadema imeagiza Kurugenzi ya Katiba na Sheria kuratibu na kusimamia hatua za kisheria ili kuhakikisha Kigaila anapata haki zake za msingi kwa mujibu wa sheria za nchi.