Monday, September 9

CUF: Ndugai anahujumu

Dar es Salaam. Chama cha Wananchi (Cuf), kimesema kitendo cha Naibu Spika wa Bunge, Job Ndugai kukataa kumpa nafasi Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe na kuamuru askari wa Bunge wamtoe nje ya ukumbi huo ni kumhujumu Rais Kikwete kwenye azma yake ya kupata Katiba Mpya.
Pia, chama hicho kimesema kinafanya juhudi za kuwasiliana na viongozi wa vyama vingine ili kuweka mkakati wa pamoja wa kukabiliana na hujuma dhidi ya mchakato wa kupata Katiba Mpya na kuimarisha umoja wa kitaifa  kwenye kipindi hiki cha kukabiliana na changamoto za nchi jirani.
Akizungumza Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa chama hicho, Profesa Ibrahimu Lipumba alisema, Cuf inalaani vitendo vya kuwanyanyasa na kuwadhalilisha wabunge wa upinzani akiwamo Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni na kudai kuwa inaonyesha wazi CCM wanampango wa kutengeneza katiba ya upande mmoja.
“Kwa mfumo wa mabunge ya Jumuiya ya Madola, kwa Tanzania Waziri Mkuu na kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni ndiyo wanawakilisha pande mbili ndani ya Bunge, hivyo kumnyima Mbowe fursa ya kuzungumza ni unyanyasaji na udhalilishaji na kwamba kitendo hicho hakikubaliki,” alisema.
Profesa Lipumba alisisitiza muswada uliokuwa unajadiliwa  ulikuwa na utata, Serikali imeubadili kwa nguvu na kuondoa maoni muhimu ya wadau.


Tutatumia nguvu ya umma kukwamisha Katiba

Dodoma. Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimesema kitatumia nguvu ya umma kuikataa Katiba Mpya endapo CCM na Serikali yake: “vitaendeleza hila na ubabe katika mchakato unaoendelea.”
Pia chama hicho kikuu cha upinzani nchini, kimeitaka Serikali kuboresha Daftari la Kudumu la Wapigakura kabla ya upigaji wa kura ya maoni ya Katiba Mpya huku kikisema kinyume chake suala hilo litaibua mgogoro mkubwa.
Kauli hizo zimetolewa kwa nyakati tofauti na Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na Mkurugenzi wa Mawasiliano wa chama hicho, John Mnyika katika mahojiano yaliyofanyika Mjini Dodoma mwishoni mwa wiki.
Mnyika alisema baada ya CCM kuhodhi muswada wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba na hivyo kulifanya Bunge la Katiba liwe ni hodhi ya chama hicho tawala karata pekee waliyobakiwa nayo ni kura ya maoni... “Rais Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM, ndiye atakayeteua wajumbe 166 kutoka taasisi na makundi na kufanya Bunge zima la Katiba kuwa na wajumbe zaidi ya 600.”
Alisema kwa sasa, Tanzania Bara hakuna utaratibu wa kikatiba wa namna ya kuendesha kura ya maoni na kuongeza.
“Wenzetu Zanzibar katika Katiba yao wanao mfumo wa kura ya maoni, sisi haupo ni lazima tutengeneze sheria ya kura ya maoni ya Katiba Mpya na Sheria ya kura ya maoni ya Muungano,” alisema Mnyika.
Mnyika alisema Kamati ya Bunge la Katiba, Sheria na Utawala inapaswa kuanza kukutana kwa dharura kupata maoni ya wadau kuhusu kura ya maoni na ianze na Zanzibar ambayo haikushirikishwa.
“Kamati ianze sasa, isisubiri Bunge la Oktoba 29 maana kati ya mambo yaliyoifanya Serikali kuondoa muswada wa Sheria ya Kura ya Maoni ni mgongano wa kikatiba kati ya Zanzibar na Muungano,” alisema.
Alisema pia Tanzania inahitaji kuwa na Katiba ya mpito ambayo itaweka chombo huru kitakachosimamia upigaji wa kura ya maoni badala ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC).
Mbowe alisema Serikali ya CCM inatumia hila na ubabe kuhakikisha inapatikana Katiba Mpya itakayobeba masilahi ya chama hicho kwa gharama yoyote.
 “Endapo CCM itaendelea na hila zake hizi niwaambie Chadema tumejipanga… Tutatumia teknolojia ya kisasa kuwafikia Watanzania hata ikibidi kutumia helikopta nne ili waikatae wakati wa kupiga kura ya maoni,” alisema Mbowe na kuongeza: “Hila yoyote itakayotokea kwenye Katiba tutahamasisha Watanzania kuikataa, wasifikiri wanachokifanya ni salama kwao… Wanageuza mchakato kuwa wa kichama badala wa wananchi.”
Alisema msimamo wa CCM kukataa mapendekezo ya muundo wa Serikali tatu si wa wanachama wake wa kawaida, bali matakwa ya viongozi wake wa juu.

“Tunapozungumzia kumdhibiti Rais, wao (CCM) wanafikiri tunamzungumzia Rais Kikwete (Jakaya)… Tunataka kudhibiti madaraka ya Rais yeyote ajaye awe wa  Chadema, CCM au NCCR”.
Alisema mapendekezo ya wananchi kuhusu Serikali tatu yalianzia wakati wa Rais wa Zanzibar, Aboud Jumbe mwaka 1984 na baadaye mwaka 1991 wakati wa Tume ya Jaji Mkuu Francis Nyalali.
Alisema pamoja na kutotekelezwa kwa mapendekezo hayo ya wananchi, bado wabunge wa G55 walianzisha vuguvugu hilo lakini likazimwa kwa kutumia nguvu kubwa.
“Tume ya Jaji Robert Kisanga nayo ilikuja na mapendekezo hayohayo na sasa Tume ya Jaji Joseph Warioba na bado CCM haitaki kuamini ni ya wananchi,” alisema.
Mbowe alisema ndiyo maana Chadema sasa kimeamua kujitoa mhanga kuwahamasisha hadi wanachama wa CCM kuikataa Katiba Mpya endapo itapatikana nje ya matakwa ya Watanzania... “ Nia tunayo, sababu tunayo na uwezo tunao.”
Alisema matumizi ya polisi hayatalipatia taifa Katiba Mpya na nzuri. “Wajue kuwa wako Watanzania wenye busara kwa mamilioni walioko nje ya Bunge ambao wana sauti katika Katiba yao na CCM wasifikiri wao ni alfa na omega (mwanzo na mwisho),” alisema Mbowe.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia amesema hata kama Tanzania haitapata Katiba Mpya hadi ifikapo 2015, bado ya sasa haitafaa kutumika.
“Hata kama tutashindwa kupata Katiba Mpya hatuwezi kwenda kwenye uchaguzi na katiba hii ya sasa kwa sababu katiba mpya ya Zanzibar imejiingiza katika mgogoro na Katiba ya Muungano,” alisema.
Alisema kama dalili za kutopatikana kwa Katiba Mpya zimeanza kuonekana, ni vyema ikatumika busara na hekima katika kuvuka kikwazo hicho na njia pekee ni meza ya mazungumzo.
“Sisi siyo tutakaoifanya Tanzania isitawalike, bali CCM…  Tunafanya haya kwa nia njema kabisa, hatutaki damu ya Watanzania imwagike kwa jambo linaloepukika,” alisema.