Wednesday, April 4

DPP Zanzibar alia uhaba wa mawakili kukwamisha kesi


Zanzibar. Mkurugenzi wa Mashtaka Zanzibar (DPP), Ibrahim Mzee Ibrahim amesema kuchelewa kwa utolewaji wa uamuzi katika kesi mbalimbali visiwani humu kunatokana na uhaba wa mawakili uliopo katika ofisi hiyo ya Serikali.
Mzee alisema hivi sasa Zanzibar nzima kuna mawakili 57 tu ambao wanashughulikia kesi zote za Unguja na Pemba, kiwango ambacho ni kidogo ikilinganisha na idadi ya kesi zinazofunguliwa.
Hata hivyo, Mzee hakutaja kiwango cha mawakili wanaowahitaji ili kufikia malengo yao.
Alisema malalamiko ya baadhi ya kesi hizo kuchelewa kutolewa uamuzi, linaweza kumalizika jitihada za kuongeza mawakili hao zitakapofanikiwa.
“Tunaomba sekta husika kuliangalia suala hili kwa kutuongezea idadi ya mawakili katika ofisi yetu ili ofisi yetu ifanye kazi zake kwa umakini,” alisema Mzee.
Alisema licha ya uhaba huo wa mawakili, wana mpango wa kuwaendeleza kitaaluma mawakili waliopo ili wawe wabobezi katika kesi maalumu, hatua ambayo alieleza inaweza kuzaa matunda ya kuwa na mawakili weledi kwa kila aina ya kesi. Mkurugenzi huyo alitaja baadhi ya faida ambazo ofisi yake imepata kuwa ni kushiriki kufanya mapitio ya sheria yaliyosababisha utayarishwaji wa miswada ya sheria, ikiwamo sheria ya adhabu ya mwaka 2018 na sheria ya mwenendo wa makosa ya jinai mwaka 2018.
Faida nyingine ni uendeshaji kesi za udhalilishaji, dawa za kulevya kwa njia ya operesheni na kuamsha ari ya jamii katika kupambana na vitendo vya uhalifu na utoaji elimu kwa umma.
Mwenyekiti wa Tume ya Kurekebisha Sheria Zanzibar, Jaji Mshibe Bakar alisema tume yao ina jukumu kubwa la kuona sheria zilizopo zinatekelezwa ipasavyo.
Jaji Mshibe aliahidi kusimamia vyema majukumu yao ili kuona kila mmoja anakuwa chini ya sheria.
Naye mkurugenzi Mamlaka ya Kuzuia Rushwa na Uhujumu Uchumi Zanzibar, Mussa Haji alisema kila jambo linahitaji umoja na ushirikiano, hivyo kuzitaka taasisi mbalimbali za kisheria kuungana na jitihada za ofisi yake ili kufikia malengo yanayotakiwa na SMZ.

Waziri Hamad ahimiza wanawake kujitokeza chanjo ya saratani



Waziri wa Afya Zanzibar, Hamad Rashid Mohamed
Waziri wa Afya Zanzibar, Hamad Rashid Mohamed 
Zanzibar. Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) imewataka wanawake kujitokeza kupatiwa chanjo, ili kujikinga na ugonjwa wa saratani ya mlango wa kizazi.
Waziri wa Afya Zanzibar, Hamad Rashid Mohamed alitoa wito huo wakati akizindua mkutano wa uhamasishaji uliowahusisha wakuu wa wilaya na mikoa.
Alisema saratani ya kizazi ni hatari zaidi hivyo wanawake wanatakiwa kujitokeza kupata kinga ambayo inatolewa bure.
Hamad alisema takwimu zinaonyesha aina hiyo ya saratani inayoongoza Tanzania, ikiwamo Zanzibar kwani wanawake 51 kati ya 100,000 wanaathirika na ugonjwa huo.
Pia, alisema wanawake 38 kati ya 100,000 hufariki dunia kila mwaka kutokana na ugonjwa huo na inakadiriwa wastani wa wanawake 466,000 wanagundulika kuwa na saratani hiyo kila mwaka kwa nchi zinazoendelea.
Baadhi ya washiriki wa mkutano huo walisema upo umuhimu wa kusambaza elimu waliyoipata.

Miezi mitatu ya mjadala Bunge la bajeti Dodoma


Dar es Salaam. Kuanzia leo, wabunge wanatarajia kutumia takriban miezi mitatu kujadili Bajeti ya Taifa kwa mwaka ujao wa fedha.
Katika bajeti iliyopita, moja ya mambo ambayo yaliwavutia wengi ilikuwa ni kufutwa kwa tozo ya barabara (road license) na kuondoa ushuru wa mazao chini ya tani moja yanayosafirishwa kutoka sehemu moja kwenda nyingine.
Kingine kilichopendezesha mjadala wa Bunge la Bajeti lililopita ni mabadiliko ya sheria tatu za madini ambazo zilikuwa na michango iliyokinzana kutoka kwa wawakilishi hao 364 wa wananchi.
Baada ya bajeti hiyo ya 2018/19, itabaki nyingine moja ya 2019/2020 kuhitimisha awamu ya kwanza ya miaka mitano ya Rais John Magufuli kumalizika.
Wakati wadau wa Serikali za Mitaa wakiendelea kukuna vichwa kutafuta vyanzo mbadala, vya kudumu kuziba pengo lililoachwa baada ya kodi ya majengo kuhamishwa, vipaumbele vipya vinatarajiwa kubainishwa kwenye mjadala huu.
Majibu yanayosubiriwa
Wakati wananchi wakisubiri kufahamu vipaumbele vya mwaka ujao wa fedha, yapo maeneo yaliyopendekezwa kufanyiwa kazi kwenye bajeti inayoendelea kutekelezwa ambayo bado hayajaonyesha mafanikio.
Baadhi ya changamoto za utekelezaji wa bajeti zimekuwa zikijirudia mara nyingi hivyo kero zake kuendelea kuwasumbua wananchi na wabunge wanatarajiwa kuzijadili na kutafuta suluhu kuanzia leo, vikao hivyo vinapoanza.
Kilimo
Kwa muda mrefu, tangu kupitishwa kwa Azimio la Maputo mwaka 2003 linalozitaka Serikali kuelekeza asilimia 10 ya bajeti nzima kwenye kilimo, Tanzania haijawahi kufanya hivyo. Kwenye bajeti ya mwaka 2017/18, ni Sh267.86 bilioni pekee kati ya Sh31.7 trilioni zilitengwa kwa ajili ya Wizara ya Kilimo sawa na asilimia 4.8.
Waziri wa Kilimo, Dk Charles Tizeba alisema kila nchi ina mfumo tofauti wa kusimamia sekta zake na kwamba suala lililopewa uzito katika bajeti ya 2017/18 ni upatikanaji pembejeo.
“Azimio la Maputo halizungumzii mifumo ya nchi mbalimbali. Kwa mfano, sisi mfumo wetu wa kilimo unashikiliwa na wizara nyingi siyo ya kilimo tu. Kwa hiyo, ukijumlisha mchango wa wizara zote zinaweza kufikia hiyo asilimia 10,” alisema Dk Tizeba.
Katiba na Sheria
Miongoni mwa vipaumbele vya Bajeti ya Wizara ya Katiba na Sheria mwaka 2017/18 ilikuwa kukuza na kutetea haki za binadamu hususan makundi yenye mahitaji maalumu ikiwa ni sehemu ya kuimarisha Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora.
Hata hivyo, wizara hiyo itapaswa kuandaa majibu ya kutosha kuhusiana na madai ya kutokuwapo kwa uhuru wa kujieleza. Katika suala la utoaji haki za binadamu, wakili wa kujitegemea, Harold Sungusia anasema Tanzania imerudi nyuma.
“Taifa tumerudi nyuma, hata simung’unyi maneno. Uhuru wa kujieleza umepotea kabisa. Hata haki ya kupata habari za Bunge imeminywa tofauti na zamani ambapo watu waliangalia Bunge moja kwa moja ‘live’. Hata kwenye mitandao ya jamii watu hawako huru kutoa maoni yao,” alisema.
Sungusia alitoa mfano wa uvunjaji wa nyumba zilizojengwa kwenye hifadhi ya barabara uliofanyika katika Wilaya ya Ubungo, Dar es Salaam kwamba wapo baadhi ya waathirika ambao walikuwa na zuio la Mahakama, lakini nyumba zao zilivunjwa.
Mhadhiri wa Sheria wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dk Jesse James alisema: “Hakuna fedha ilitengwa kwa ajili ya mabadiliko ya Katiba jambo linalomaanisha hakutakuwa na mchakato huo. Hata Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora haipati bajeti ya kutosha, kwa hiyo usitegemee ufanisi mkubwa.”
Viwanda
Tangu mwishoni mwa mwaka jana, kumekuwa na changamoto ya sukari ya viwandani ambayo ni muhimu kwa uzalishaji wa bidhaa zao.
Mbali ya changamoto hiyo, mkuu kitengo cha ununuzi wa kampuni ya dawa ya Shelys Pharmaceuticals, James John alisema hata ulipaji wa kodi za aina mbalimbali unapaswa kutazamwa upya.
“Tunaambiwa tulipe VAT (Kodi ya Ongezeko la Thamani) kwenye vifungashio pamoja na malighafi ingawa zina msamaha. Hutukuchukua zaidi ya wiki kufuatilia suala hilo hivyo kulazimika kulipa gharama za kutunza mzigo bandarini kwani Mamlaka ya Bandari hutoa siku saba tu mhusika awe amekamilisha utaratibu wote na kuondoka na mzigo wake” alisema.
Maeneo mengine ambayo sekta binafsi inapenda yafanyiwe marekebisho ni kodi ya kampuni, malipo ya makandarasi na waliotoa huduma serikalini, fidia ya asilimia 15 ya uagizaji wa sukari ya viwandani.
Mwenyekiti wa Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF), Reginald Mengi alisema endapo mfumo wa kodi utaangaliwa na kufanyiwa marekebisho muhimu, “Tutashuhudia ongezeko kubwa la biashara hivyo kuimarisha mzunguko wa fedha.”
Mazingira bora pia ni kilio cha wasanii wa muziki na sinema. Baada ya nyimbo kadhaa kufungiwa baadhi walilalamika kutoungwa mkono na Serikali. Bunge litalazimika kutafuta majibu ya namna ya kuwawezesha wasanii hao pamoja na wanamichezo.
Elimu
Ukiacha changamoto za muda mrefu kama vile miundombinu ya madarasa na madawati yasiyokidhi mahitaji pamoja na upungufu wa walimu, yapo maeneo mengine yanayotarajiwa kujadiliwa.
Hayo ni pamoja na ruzuku inayotolewa kufanikisha elimu bure kwenye shule zote za umma, muundo wa elimu wa kuishia darasa la sita unaotajwa kuanza kutumika badala ya miaka saba ya sasa na mfumo wa elimu kwa ujumla.
Hivi karibuni, Rais mstaafu, Benjamin Mkapa alisema kuna janga katika elimu nchini na kushauri kuitishwa kwa mdahalo wa wazi, utakaoshirikisha makundi yote ya jamii kutafuta suluhu ya kudumu.
Alisema hayo kutokana na shule za Serikali kuendelea kufanya vibaya kwenye matokeo ya mitihani ya kitaifa.
Madini
Yapo mambo mengi kwenye sekta ya madini ambayo wananchi watapenda kupata mrejesho baada ya kutofanyiwa kazi kama ilivyoahidiwa kwenye Bunge lililopita.
Akisoma bajeti ya iliyokuwa Wizara ya Nishati na Madini mwaka jana, Charles Mwijage alisema: “Wizara ilipanga kukusanya Sh370.68 bilioni mwaka 2016/17 ikilinganishwa na Sh286.66 bilioni za 2015/16. Mwaka 2017/18, wizara inatarajia kukusanya Sh727.5 bilioni sawa na ongezeko la asilimia 96.3.”
Mwaka jana, Serikali iliahidi kuanza kuweka akiba ya dhahabu na madini mengine ya vito, kuanzisha kampuni ya kusimamia uchimbaji madini, kuendeleza utafutaji wa helium, kuwarasimisha wachimbaji wadogo na kufanikisha uchenjuaji wa madini nchini.
Kuongeza ushiriki wa Watanzania, Serikali iliahidi kusimamia usajili wa kampuni za madini kwenye Soko la Hisa Dar es Salaam (DSE) na uuzaji wa hatifungani za Williamson Diamonds, Dangote, TanzaniteOne, Mgodi wa Geita (GGM), Shirika la Madini la Taifa (Stamico) na Mgodi wa Luika.
Afya
Msisitizo mkubwa sasa umeelekezwa kujenga uchumi wa viwanda utakaosaidia kuifanya Tanzania kuwa na kipato cha kati ifikapo mwaka 2025.
Kufanikisha lengo hilo, afya za wananchi watakaotoa nguvukazi hiyo ni muhimu. Kuzikabili changamoto za sekta ya afya zinazojumuisha ujenzi na uendelezaji wa viwanda vya dawa, utoaji wa bima ya afya kwa wote na mfumo wa rufaa nchini ni miongoni mwa mambo yatakayojadiliwa kwa kina.

Charles: Iko siku ndege hii itaruka


Soma anachoeleza mhitimu wa darasa la saba kuhusu kinachosababisha ndege aina ya helikopta kupaa na isidondoke.
‘’ Hapo unadhibiti tu mvutano wa hewa kwa kuwa na upanga yaani kata upepo katikati na nyuma. Huu upanga wa katikati ni kwa ajili ya kudhibiti kani mvutano na ule wa nyuma ni kwa ajili ya kuzuia ndege isiyumbe. Vitu hivyo ni muhimu na vikikosena vyote au kimoja kati ya hivyo, ndege itadondoka chini.”
Huyu ni kijana mtundu aitwaye Deogratius Charles, mkazi wa kijiji cha Bunga kilichopo mkoani Pwani, ambaye ana ndoto kuu ya kutengeneza mfano wa ndege na kuirusha.
Tangu akiwa mtoto, fikra zake hazikuwahi kutoka nje ya anachosema kutengeneza ndege na hatimaye kuirusha.
Sasa akiwa na miaka 26 amefanikiwa kutengeneza kifaa mithili ya helikopta anayosema amebakiza vifaa vichache iruke angani. Tena vifaa hivyo anasema havihitaji kiwango kikubwa cha fedha, akipata sh 1.2 milioni Charles ataanza kuirusha angani.
Anasema ndege hiyo inayotumia mafuta ya petroli na injini ya pikipiki kubwa za Kijapan, itakuwa na uwezo wa kukaa angani kwa saa tatu.
Ndege hiyo ameitengeneza kwa vifaa mbalimbali vikiwemo vyuma vya aluminiamu. Anasema ili iweze kuruka inahitaji mashine, mota pamoja na taa ambavyo kwa pamoja gharama zake zinafikia Sh 1.2milioni.
Alivyoanza ubunifu wake
Akiwa na umri wa miaka mitano, Charles anasema alipenda kuchora michoro mbalimbali wakati akicheza na wenzake hasa michoro ya ndege.
“Nilipenda kujifunza vitu mbalimbali kwa kuangalia, mathalani nikiona picha hata ya mnyama nachora kama ilivyo na wenzangu waliniita bwana chorachora,”anasema na kuongeza kuwa:
“Nilikuwa na rafiki yangu ana kitabu cha picha, nilipendelea kuangalia picha za helikopta nilivutiwa na picha zile kuanzia siku hiyo nikaweka ahadi ya kuwa mtengenezaji wa ndege,”anaeleza.
Kutokana na umri wake kuwa mdogo kwa kipindi hicho alitengeneza ndege ndogo kwa ajili ya kuchezea ambazo alitengeneza kwa kuangalia picha hizo za kwenye kitabu.
“Nilianza kutengeneza kwa kutumia maboksi, naangalia mchoro halafu naunda ya kwangu. Hapo ndipo nilipoanzia hadi kufikia hii kubwa ambayo naamnini ipo siku itapaa angani,” anasema.
Kwa kuwa ni kitu ambacho alipenda kutengeneza tangu akiwa mdogo, hakutaka kupoteza ubunifu wake kwani anasema utengenezaji wa chombo hicho utampa fursa ya kupata ajira katika kampuni za usafirishaji wa anga
“Lakini pia nilijaribu kuangalia kitu ambacho kitakuwa cha tofauti na wengine. Unajua hivi sasa ukiangalia wabunifu wengi wanatengeneza vitu vya kufanana, mimi chaguo langu limeangukia hapa,”anasema
Matarajio yake
Charles ana matarajio ya kurusha ndege yake siku moja ili hatimaye ajivunie ubunifu wake na kujitangaza kimataifa.
Mbali na hilo anatarajia kuwa mhandisi atakayeungana na wengine waliopo kutatua changamoto za usafiri wa anga nchini.
“Sipendi kuishia hapa nilipo, ndoto yangu siku moja niwe fundi bora kwa kutengeneza ndege mbalimbali zitakazosafiri ndani na nje ya nchi yetu,”anaeleza.
Anasema endapo atawezeshwa, atatengeneza ndege nyingi. Amefanikiwa kutengeneza ndege hiyo moja kutokana na kuwa na kipato kidogo.
Lengo la Charles ni kusaidia vijana wenzake kutoka katika wimbi la kuwa tegemezi, kwani anasema mradi wake ukiwa mkubwa kipaumbele cha kwanza kitakuwa ku fundisha vijana wenzake.
Changamoto
Haikuwa kazi ndogo kwake kufika alipo, kwa kuwa amepitia vikwazo kadhaa anavyosema alifanikiwa kuvivuka kwa sababu ya kuwa mvumilivu.
Anasema mara nyingi ndugu na jamaa walimkatisha tamaa, kwani wanafikiri kuwa anachokifanya ni sawa na kupoteza muda na fedha.
‘’ Niwe tu mkweli, kwa kipindi cha mwanzo, ndugu walinikatisha tamaa kwa kutoonyesha ushirikiano na kutaka fedha ninazotumia kununua vifaa bora, nizifanyie vitu vingine ikiwamo kujenga,”anaeleza.
Anasema kwa sasa ndugu hao wakiwamo wazazi wake wameanza kuelewa anachokifanya.
“Mwanzoni wakati naanza kuunda, waliona kama utani sasa hivi wakiona hatua niliyofikia wanafurahi na mimi napata faraja,”
Changamoto nyingine ni kutokuwa na fedha ya kutosha kwa ajili ya kununulia vifaa…. “Isingekuwa tatizo la fedha, nina imani hii ndege ingeshakamilika.’’
Anasema changamoto hizo zote na nyingine ndizo zinazosababisha ndege hiyo kuchelewa kuruka. Hata hivyo, anaamini kuchelewa huko sio sababu yeye kurudi nyuma kwa kuwa imani yake ni kuwa; ‘ipo siku itaruka’.
Wito wake kwa Serikali
Anatoa rai kwa Serikali kuunga mkono ubunifu wake kwa kumtembelea na ikiwezekana kukutanishwa na wabunifu wengine.
“Mimi naomba viongozi serikalini waje waone hiki chombo, pengine wanaweza kunishauri mengi ambayo yatanijenga zaidi katika safari yangu hii ya ubunifu wa ndege,”anaeleza.
Kwa kuwa changamoto yake kubwa ni fedha kwa ajili ya kununua vifaa, anasema kwa sasa kilio chake ni kupata Sh 1.2 milioni kwa ajili ya vifaa ili aweze kukamilisha matengenezo yaliyosimama kwa muda.
“Kipato changu ni kidogo, pea ninayopata katika kazi yangu ya ufundi magari na pikipiki inatosha kwa ajili ya kujikimu, lakini wakati mwingine najitahidi hivyo hivyo kujibana kuweka fedha kidogo kwa ajili ya vifaa,” anaongeza kusema.
Kwa kuwa aliishia elimu ya msingi, Charles anahitaji kupatiwa elimu ili kukuza ujuzi na maarifa aliyonayo.
“Nikipata nafasi ya kwenda chuo cha ufundi nitafurahi, nikiwa na elimu itajenga uaminifu katika kampuni mbalimbali za usafiri wa anga zitakapotaka kunichukua,” anasema.
Anasema Serikali itoe kipaumbele kwa wabunifu kwani kulingana na ukuaji wa sayansi na teknolojia, utakuwa na fursa nyingi za ajira na kupunguza wimbi la vijana wasiokuwa na kazi.
“Mimi naamini kama tutapatikana vijana 20 kama wabunifu tuna uwezo wa kutengeneza ndege zetu wenyewe zikafanya safari za ndani kuliko kununua kutoka nje,”.
Anasema wapo vijana wanaobuni vitu vingi lakini Serikali inashindwa kuwatambua kutokana na kutokuwa na utaratibu wa kuwatembelea hasa wale waliopo maeneo ya vijijini.
Kwa sasa Charles, anaendesha maisha yake kwa kutengeneza pikipiki na magari, hata hivyo anasema ndoto yake haipo huko. Anahitaji msaada wa ujuzi zaidi ili atimize ndoto yake ya kuwa mhandisi wa ndege.
Kauli ya Mamlaka ya Usafiri wa Anga
Charles anafanya haya yote akiwa kwa hajui lolote kuhusu taratibu za urushaji wa ndege, kama zinavyoainishwa na mamlaka husika.
“Sijui kama kuna taratibu zozote za kurusha ndege na nitakapokamilisha hivyo vifaa, natamani nionane nao ili wanipe mwongozo,” anasema.
Ofisa habari Mamlaka ya Usafiri wa Anga (TCAA) Bestina Magutu anasema utaratibu uliopo ni kwamba ndege kabla haijaruka angani, mhusika anatakuwa kuwasiliana na mamlaka hiyo.
“Ni jambo zuri ila cha msingi kama anataka kuendelea mbele na ubunifu wake awasiliane na TCAA ili kujua ni jinsi gani anaweza kusaidiwa, lakini pia anavyoweza kupewa ushirikiano zaidi,”anaeleza.
Costech yamkaribisha
Hata Tume ya Sayansi na Teknolojia (Costech), haitambui ubunifu wa Charles, licha ya ukweli kuwa tume hy imekuwa ikiwasaidia wabunifu na wagunduzi wanaojitokeza nchini
Huyo kijana hatumtambui lakini anaweza akaja katika ofisi zetu tukamshauri mambo mbalimbali. Inavyoonekana huyu kijana ni mtundu kwa kuwa ameweza kutengeneza bodi ya helikopta,’’ anasema mtafiti mwandamizi wa Costech Dk Georges Shemdoe.
Anasema tayari Tume imeanzisha kambi za ubunifu katika mikoa mbalimbali, kwa lengo la kuwasaidia wabunifu.

Radi zinavyozitikisa shule Kagera



Tangu tukio la mwaka 2005 lililosababisha vifo vya wanafunzi wawili na majeruhi, radi imetikisa tena shule ya msingi Kyakailabwa iliyopo Manispaa ya Bukoba mkoani Kagera.
Katika tukio hilo la miaka 12 iliyopita lililoshuhudiwa na walimu na wanafunzi, pia mwanamke mmoja alifariki na maajabu makubwa zaidi siku hiyo ni jinsi mtoto wake mchanga alivyonusurika.
Aliyekuwa mwalimu mkuu wa shule hiyo wakati huo Jacob Kaijage, anasema alishuhudia matukio hayo na jinsi mamia ya wananchi walivyokusanyika kushuhudia janga hilo.
Radi iliyojirudia Machi 22,haikuleta madhara makubwa japo wanafunzi 61 pamoja na walimu wao wawili walipata mshtuko mkubwa na kulazimika kulazwa katika hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Kagera.
Katibu wa hospitali hiyo Kilwanila Kiiza alisema pamoja na baadhi yao kupata michubuko na mshituko, hawakuwa kwenye hatari kubwa na waliruhusiwa kwa awamu kurudi nyumbani.
Radi shule za Kagera
Pamoja na kuwa radi haizoeleki, lakini limekuwa jambo linalojirudia mara kwa mara katika shule tofauti za Mkoa wa Kagera na mara kadhaa huacha madhara.
Kwa mfano, moto wa radi ndio uliochukua uhai wa Angelika Frolian mwaka 2014 aliyekuwa mwanafunzi wa shule ya sekondari Iluhya iliyopo Wilaya ya Bukoba aliyekuwa amejikinga mvua kwenye ukuta wa darasa.
Tukio la shule ya msingi Kyakailabwa pia linarejesha kumbukumbu ya vifo vya wanafunzi wawili wa shule ya sekondari Kamuli Wilayani Kyerwa waliopigwa na radi na kupoteza maisha mwaka 2014.
Ushuhuda walimu na wazazi
Mwalimu Kaijage ambaye sasa anafundisha Shule ya Msingi Bilele Manispaa ya Bukoba, wakati wa tukio lililoua wanafunzi wawili wa shule ya Kyakailabwa ndiye aliyekuwa mwalimu mkuu.
Pamoja na kuwa shule anayosimamia sasa haina historia ya matukio hayo, anasema hofu yao sio kubwa kwa kuwa ni majirani na uwanja wa ndege wa Bukoba wenye mitambo kwa majanga kama hayo.
‘’Radi inaogopesha na kujenga hofu nilishuhudia nikiwa Kyakailabwa walimu na wanafunzi walivyotaharuki baada ya kuua wanafunzi wawili na mama aliyekuwa na mtoto mchanga’’anasema.
Majanga mengine shuleni
Shule za Mkoa wa Kagera zimeandamwa na majanga kwa nyakati tofauti ikiwa ni pamoja na tukio la wanafunzi wanne wa shule ya msingi Tumaini ya mjini Bukoba kuuawa kwa bomu August,31 mwaka 1994.
Shule hiyo ambayo imehamishiwa eneo jingine baada ya kiwanja cha ndege kurefushwa, alama pekee iliyobaki ni mnara wenye majina ya wanafunzi wanne waliofariki siku ya tukio.
Pia tukio la karibuni zaidi ni wanafunzi watano wa darasa la kwanza wa Shule ya Msingi Kihinga Wilayani Ngara, kufariki baada ya kulipukiwa na bomu walilokuwa wanamiliki baada ya kuliokota.
Hali sio nzuri Kagera na Kigoma
Matukio ya radi yanakuwa mengi mkoani Kagera hasa mjini Bukoba baada ya kupakana na Ziwa Victoria, kama ulivyo Mkoa wa Kigoma unaopakana na Ziwa Tanganyika.
Tafiti za hali ya hewa zilizofanyika kwenye Ziwa Victoria zinathibitisha kuwa mawingu yenye chaji hatari zinazotengeneza radi yako upande wa Magharibi na Mashariki.
Malundo anasema kuwa matukio hayo hayakwepeki kwenye miji ya Bukoba,Tarime na Kisumu nchini Kenya.
‘’Zile chaji haziwezi kukaa angani lazima ziingie ardhini; matukio haya yanatokea wakati wa asubuhi na jioni upande wa Kaskazini na Kusini. Tatizo sio kubwa kama pande nyingine za Ziwa Victoria,’’anabainisha Malundo.
Chukua tahadhari
Kitu kilichounguzwa na radi inashauriwa kisiguswe haraka au hatua hiyo ifanyike kwa tahadhari, kwa kuwa huwa bado kimezungukwa na chaji ambazo bado zinaelekea ardhini.
Inashauriwa kutumia kipande kikavu cha mti ambacho hakina maji maji yanayoweza kutumika, kama mkondo wa kusafirisha maji na kukufikia kwa urahisi.
Ni hatari zaidi kuwa chini ya mti wakati wa mvua kwa kuwa maeneo yenye vitu virefu ikiwemo miti hutumika kusafirisha chaji za radi kwenda ardhini.
Pia hakuna usalama ukitembea kwenye eneo la wazi wakati wa mvua, kwa kuwa linaweza kutumika kama kifaa cha kusafirisha chaji kwenda ardhini na kupoteza maisha.

Tuzo za Sziff zilivyosimamisha nchi kwa saa tano

Baadhi ya washiriki wa filamu ya Safari ya
Baadhi ya washiriki wa filamu ya Safari ya Gwalu, wakiwa katika picha ya pamoja baada ya kukabidhiwa tuzo. 
Macho na masikio ya Watanzania katika usiku wa Aprili 1, mwaka huu yalielekea Ukumbi wa Mlimani City, zilipokuwa zikitolewa tuzo za filamu zinazofahamika kwa jina la ‘Sinema Zetu International Film Festival Award (SZIFF)’.
Macho na masikio ya Watanzania katika usiku wa Aprili 1, mwaka huu yalielekea Ukumbi wa Mlimani City, zilipokuwa zikitolewa tuzo za filamu zinazofahamika kwa jina la ‘Sinema Zetu International Film Festival Award (SZIFF)’.
Tuzo hizo ziliandaliwa na kutolewa na kituo cha Televisheni cha Azam kupitia chaneli yake ya Sinema Zetu kwa lengo la kutambua kazi za wasanii wa tasnia hiyo.
Mazungumzo katika majukwaa yote yalitawaliwa na utoaji wa tuzo hizo tangu hafla ya utoaji tuzo hizo ilipoanza saa 2:00 usiku mpaka 7:00 usiku.
Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali akiwemo Rais Mstaafu wa awamu ya nne, J
Macho na masikio ya Watanzania katika usiku wa Aprili 1, mwaka huu yalielekea Ukumbi wa Mlimani City, zilipokuwa zikitolewa tuzo za filamu zinazofahamika kwa jina la ‘Sinema Zetu International Film Festival Award (SZIFF)’.
Tuzo hizo ziliandaliwa na kutolewa na kituo cha Televisheni cha Azam kupitia chaneli yake ya Sinema Zetu kwa lengo la kutambua kazi za wasanii wa tasnia hiyo.
Mazungumzo katika majukwaa yote yalitawaliwa na utoaji wa tuzo hizo tangu hafla ya utoaji tuzo hizo ilipoanza saa 2:00 usiku mpaka 7:00 usiku.
Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali akiwemo Rais Mstaafu wa awamu ya nne, Jakaya Kikwete ambaye alikuwa mgeni rasmi, Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Juliana Shonza, Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni Ali Hapi na Katibu Mtendaji wa Bodi ya Filamu, Joyce Fisoo.
Mbali ya viongozi, pia walikuwepo wasanii wa filamu kutoka Kenya, Rwanda, Zambia na India akiwamo mwanadada anayeigiza katika tamthiliya ya Beintih, Preetika Rao, jina la usanii Aliyah.
Katika tuzo hizo jumla ya vipengele 19 vilishindaniwa, ambapo katika washindi wapo waliondoka na kitita cha Sh5 milioni na Sh2 milioni kwa msanii bora wa kike, wa kiume na muongozaji bora wa filamu.
Mratibu wa tuzo hizo ambaye pia ni msimamizi wa chaneli ya Sinema Zetu, Zamaradi Nzowa alisema Sh41 milioni ziliandaliwa kwa ajili ya zawadi.
Katika upande wa mwigizaji bora wa kike, tuzo hiyo ilienda kwa mrembo Wema Sepetu na mwigizaji bora wa kiume aliinyakua mwigizaji Salim Ahmed maarufu Gabo huku muongozaji bora ikienda kwa Daniel Manege aliyeongoza filamu ya Safari ya Gwalu.
Vitu gani vilivutia katika tukio zima
Katika tukio hilo la utoaji tuzo kulikuwa na mambo mbalimbali yaliyovutia lakini kivutio kilikuwa mwanamuziki Diamond Platnumz kuungana na mwanamitindo Hamisa Mobeto katika kukabidhi tuzo.
Wawili hawa wamekuwa kivutio kutokana na hivi karibuni kuingia katika mgogoro wa matunzo ya mtoto wao aitwaye Dyllan, mpaka kufikia hatua ya kufikishana mahakamani kutafuta suluhu ya jambo hilo.
Hata hivyo, juzi katika utoaji wa tuzo hizo, Diamond ambaye alikuwa wa kwanza kuitwa jukwaani kwa ajili ya kukabidhi na baadaye mshehereshaji kumuita Mobeto katika kuungana na msanii huyo.
Alipofika kwenye ngazi, mshereheshaji wa kike aliyetambulika kwa jina moja la Sofia, alimsaidia kumshika mkono wakati anapanda ngazi na kumkabidhi kwa Diamond ambaye naye alimkumbatia kwa kumshika kiuno na kuibua kelele ukumbini.
Baada ya hapo Diamond alisema amefurahishwa na tuzo hizo kwani zimemuwezesha kukutana na mzazi mwenzie, jambo ambalo lilisababisha tena ukumbi kulipuka kwa shangwe.
Diamond ambaye alikuwa amevalia suruali ya maua maua iliyochanganyika na rangi nyeupe na koti jeupe juu lililotanguliwa na fulana nyeupe, hakuishia hapo kwani alimsifia Mobeto kwa namna alivyopendeza na kueleza kuwa anaamini uwepo wao hapo hata mtoto wao huko alipo kama anawaona atakuwa amefurahi zaidi.
Alipomaliza hapo alimuonyesha karatasi Mobeto ili aweze kumsoma mshindi na ndio hapo akaitaja filamu ya ‘Safari ya Gwalu’ kuwa ndio imeshinda kipengele cha ‘Best Original Music’.
Baada ya kumaliza kufanya hivyo, Diamond alimshika Mobeto na kushuka naye jukwaani na kurudi alipokuwa amekaa na yeye kwenda kumsalimia Rais Mstaafu Jakaya Kikwete.
Alipotakiwa kutoa maoni yake kuhusu tukio hilo, Wema Sepetu, ambaye chupuchupu tuzo hiyo iende kwake kupitia filamu ya ‘Heaven Sent’, kutokana na kuwa moja ya filamu iliyoingia kwenye kipengele hicho.
Wema ambaye aliwahi kuwa mpenzi wa Diamond miaka kadhaa iliyopita na hivi karibuni kuelezwa kwamba wamerudiana, amesema kitendo hicho kwake amekichukulia kawaida kwa kuwa Mobeto na Diamond ni mtu na mzazi mwenzake.
“Wee ulitaka nichukuliaje labda, Mobeto na Diamond hawa ni wazazi jamani, ulitaka nikasirike au halafu isitoshe mimi sina mahusiano ya kimapenzi na Diamond bali ni washkaji tu na si kama watu wanavyosema,” alisema Wema akizungumzia tukio hilo ambalo pia lilikua gumzo usiku kucha kwenye mitandao ya kijamii.
Kuhusu hatua yake ya kupata tuzo mbili ya msanii bora wa kike na chaguo la watu (People’s Choice Award) kupitia filamu yake ya ‘Heaven Sent’, Wema alisema amefurahi kuona majaji wameweza kuona kipaji alichonacho.
Pia aliahidi kuendelea kuwapa mashabiki wake kazi nzuri na kuwaondoa hofu wadau wa filamu waliokuwa wanasema kuwa Bongo Movie imekufa kuwa si kweli bali ilikuwa imelala tu. Hata hivyo, hakusita kutoa shukrani kwa mashabiki zake ambao amesema ni kati ya watu ambao walishiriki zoezi la kumpigia kura kwa wingi hadi kuhakikisha anapata ushindi huo.
Diamond aingia na kutoka kama upepo
Wakati macho na masikio yalikuwa kwa Diamond usiku wa tuzo hizo, katika hali isiyo ya kawaida Diamond aliingia ukumbini bila ya waandishi kushtukia mpaka pale walipomuona akiwa amekaa ukumbini hapo.
Hata hivyo, wakati wa kuondoka nako hali ilikuwa hivyo hivyo kwani baada ya kukabidhi tuzo hiyo alitokomea pasipo kujulikana na paparazi waliokuwa wakimvizia kufanya naye mahojiano hawakufanikiwa katika hilo.
JK awananga wanaowazodoa Bongo Movie
Katika hatua nyingine, Rais Mstaafu wa awamu ya nne, Jakaya Kikwete alionyesha kukerwa na namna watu wanavyokosoa Bongo Movie na kueleza kuwa walikotokea na walipo kuna utofauti.
Alikiri kwamba suala la vifaa, usambazaji wa kazi zao, mitaji vimekuwa kikwazo cha wao kutofikia ubora wa filamu za nchi nyingine kama zilivyo za Bollywood na Nollywood na kuomba Watanzania kuwaunga mkono kwa kununua kazi zilizo halisi ili waweze kufaidika na jasho lao.
Washindi waliopata tuzo nyingi
Katika tuzo hizo filamu aliyoigiza msanii Gabo imeongoza kwa kuzoa tuzo nyingi ambapo katika kipengele cha filamu ndefu, imetoa muigizaji bora wa kiume, muongozaji bora, filamu bora, best screen play na best original music.
Wakati kwa upande wa filamu fupi, filamu ya Binti Musa iliyoigizwa na wasanii kutoka visiwani Zanzibar ilizoa tuzo tatu ikiwemo filamu bora, best screen play na best original music. Wakati makala iliyodhaminiwa na Mfuko wa Waandishi wa Habari Tanzania (TMF), ikipata tuzo mbili za kipengele cha filamu bora na muongozaji bora.
Wasanii kuchelewa, upigaji picha, matumizi ya lugha
Mojawapo ya mambo ambayo hayakuvutia katika tuzo hizo ni pamoja na wasanii kuchelewa kufika ukumbini hadi mgeni rasmi kuwatangulia.
Mbaya zaidi wasanii hao ni wale waliokuwa wateule akiwemo Wema Sepetu ambaye aliingia ukumbini saa moja baada ya mgeni rasmi kuketi.
Jingine ni majina ya vipengele kuorodheshwa kwa lugha ya Kiingereza wakati tukio hilo kubwa lingekuwa fursa ya kukitangaza Kiswahili.
Pia, hakukuwa na utaratibu mzuri wa kuwawezesha wanahabari kushiriki upigaji picha kwa nafasi kutokana na kituo hicho kurusha moja kwa moja matangazo yake.
Katika hili kwa kuwa walikuwa na vyombo vya kisasa wangeweza kupandisha hata mitambo yao juu na kuwaacha wapiga picha wa vyombo vingine nao kupata picha za tukio hilo vizuri.
Wasanii kuwa ‘busy’ kupiga picha za kuuzia sura nje wakati matukio yakiwa yanaendelea ndani ikiwemo kupewa nasaha za namna ya kuboresha kazi zao zilizokuwa zinatolewa na viongozi mbalimbali ni miongoni mwa mambo yaliyojitokeza.
Pia ilishuhudiwa baadhi ya wasanii ambao tangu wamefika wamekaa kwenye zulia jekundu kwa ajili ya kuchukua picha mbalimbali na hata ungewauliza nini kilitokea ndani wasingeweza kukujibu.
Jingine ni filamu za kutoka nchini Kenya kushinda, wakati tuzo hizo tuliambiwa ni kwa ajili ya filamu za hapa nchini, katika hili ingependeza wakati mwingine waongeze kipengele cha filamu za Afrika Mashariki, kwani watakuwa hawajawatendea haki wasanii wa hapa Bongo.

Diamond, Samatta watakiwa nchini Marekani kutunukiwa tuzo


Moshi. Watanzania watatu na raia wa Marekani, wameteuliwa kutunukiwa tuzo katika tamasha lililoandaliwa na Watanzania waishio ughaibuni (Diaspora) litakalofanyika Dallas nchini Marekani.
Miongoni mwa watakaopewa tuzo ni Dk Steve Meyer ambaye ni daktari bingwa katika Hospitali ya Mercy iliyopo jiji la Sioux, Marekani aliyewatibu manusura wa ajali ya wanafunzi wa Lucky Vincent.
Katika ajali hiyo iliyotokea Mei 2017 eneo la mlima Rhotia wilayani Karatu mkoani Arusha, wanafunzi 32, walimu wawili na dereva walipoteza maisha katika ajali hiyo.
Mei 14, 2017, shirika la Samaritan Purse liliwapeleka manusura wa ajali hiyo, Doreen Mshana, Saidia Awadhi na Wilson Tarimo nchini Marekani na kurejea nchini Agosti 17 baada ya matibabu.
Akizungumza na gazeti hili kutoka Dallas jana, mratibu wa tamasha hilo, Ben Kazora alisema wanampa tuzo daktari huyo kwa kutambua mchango wake katika kuokoa maisha ya watoto hao.
“Sote tunatambua namna ajali ilivyokuwa mbaya na ilivyopoteza wapendwa wetu wengi. Dk Meyer na timu yake walifanya kila njia kuokoa maisha ya watoto wale watatu walionusurika,” alisema.
Kazora anayeishi Dallas, Texas aliwataja wengine walioteuliwa kupewa tuzo hiyo ni mwanamuziki wa kizazi kipya, Nassib Abdul maarufu Diamond Plutnumz na mwanasoka wa kimataifa, Mbwana Samatta.
“Tunampa Diamond zaidi kwa kutumia kipaji chake cha muziki kuitangaza nchi kitaifa na kimataifa, vivyo hivyo Samatta kwa kutumia kipaji chake cha kusakata kabumbu kuitangaza Tanzania,” alisema.
Kwa mujibu wa Kazora, mwingine ni mwanariadha John Akhwari ambaye mwaka 1968, alimaliza mbio katika michezo ya Olympic iliyofanyika Mexico City licha ya kuumia mguu.
Naye meya wa Dallas Texas nchini Marekani, Mike Rawlings aliwakaribisha Watanzania hao kushiriki tamasha la Tanzania Day, litakalofanyika jijini humo kwa lengo la kutangaza fursa za biashara na utalii.
Akizungumza kwa simu na gazeti hili, Rawlings alisema kwamba tamasha hilo linafahamika kwa jina la “Tanzania Day”, litafanyika Dallas na kuwakutanisha Watanzania na Wamarekani kwa ajili ya kubadilishana fursa za uchumi.

JPM amteua Dk Mafumiko kuwa Mkemia Mkuu wa Serikali


Dar es Salaam. Rais John Magufuli amemteua Dk Fidelice Mafumiko  kuwa Mkemia Mkuu wa Serikali.
Uteuzi huo wa Dk Mafumiko umeanza leo Jumanne Aprili 3, 2018.
Taarifa iliyotolewa leo na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu,  Gerson Msigwa imeeleza kuwa kabla ya uteuzi huo, Dk Mafumiko alikuwa Mkurugenzi wa Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima (TEWW).
Dk Mafumiko anachukua nafasi ya Profesa Samuel Manyele ambaye amemaliza muda wake.

JPM aitaka Tanesco kufikiria kupunguza bei ya umeme


Dar es Salaam. Rais John Magufuli amelitaka Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) kuanza kufikiria kupunguza bei ya umeme kwani nchi inatarajia kuwa na umeme mwingi.
Rais ameyasema hayo leo Aprili 3, wakati wa uzinduzi wa kituo cha kuzalisha umeme cha Kinyerezi awamu ya pili.
Amesema miradi yote ya umeme ukijumlisha na wa Stiegler Gauge itafikia megawati 5000 hivyo wataibana  Wizara ya Nishati ianze kufikiria kupunguza bei ya umeme.
“Muanze kufikiria namna ya kushusha bei ya umeme, mmeanza vizuri muendelee na utaratibu huo.
“Nchi ina vyanzo vingi vya kuzalisha umeme, maji , jua, upepo, makaa ya mawe, hata nyuklia, kwa sababu tunayo madini ya uranium yanayoweza kuzalisha umeme kwa nyuklia, kwa umeme wote huo hakuna haja ya kuwa na bei ya juu, ”amesema Magufuli.
Amefafanua kuwa anayetaka kuwekeza bila kukomoa aje, lakini siyo wawekezaji wababaishaji.
Ameeleza kuwa nchi itakuwa na umeme wa kutosha,  wa uhakika na kwa gharama nafuu.
Magufuli pia alizitaja sababu za bei ya nishati hiyo kuwa ya juu ni kutokana na umeme mwingi kuzalishwa kwa kutumia mafuta (dizeli), huku baadhi ya mikataba kuwa mibovu na ya ovyo.
Ameeleza takwimu zilizofanywa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) mwaka 2015/16 zinaonyesha asilimia 36.6 ya Watanzania ndiyo wameunganishiwa umeme.

Spika Ndugai arejea nchini


Dar es Salaam. Spika wa Bunge, Job Ndugai amerejea leo Aprili 3, 2018 akitokea nchini India alikokwenda kwa ajili ya kupata matibabu miezi miwili.
Akizungumza na Mwananchi leo Aprili 3, 2018, Katibu wa Bunge, Stephen Kagaigai amesema, “Mimi sijaonana naye, ila ninazo taarifa za Spika Ndugai amerejea leo na bado yuko Dar es Salaam hajaja Dodoma.”
Katika picha inayosambaa mitandaoni inamwonyesha Spika Ndugai akisalimiana na Mke wa Rais mstaafu, Jakaya Kikwete, Mama Salma Kikwete pamoja na wabunge wengine wakiwa na nyuso za tabasamu.

Tuzo ya Wema Sepetu ‘yawatoa povu’ Bongo Movie


Dar es Salaam, Tuzo ya mwigizaji bora wa filamu wa kike nchini ya SZIFF aliyoipata Wema Sepetu juzi, imeonekana kuwagawa mastaa wa Bongo Movie wengine wakimbeza na baadhi wakimpongeza.
Mpasuko huo umekuja kufuatia kuwepo baadhi ya mastaa wanaoona Wema amestahili tuzo hiyo huku wengine wakiamini amepewa kwa upendeleo.
Maneno yalianza kwenye mitandao muda mfupi baada ya Wema kutangazwa mshindi wa tuzo hiyo aliyokuwa akiwania na Riyama Ally na wasanii wengine wa kike chipukizi.
Kupitia ukurasa wake wa Instagram, mwigizaji Irene Uwoya aliweka picha ya Gabo na kuandika, "Hapa hawajapepesa umestahili."
Mwigizaji Youbnesh maarufu Batuli akaweka picha hiyo hiyo na kuandika," Ukisikia mtu kutenda haki na kutendewa haki ndio hii. Gabo wangu Mwenyezi Mungu aendelee kukunyanyua juu Inshallah, endelea kutunza heshima na tamaduni zetu, keep working hard baba hongera sana."
Kauli hizo zimeonekana kuwakera mashabiki wengi wa Wema na kujikuta wakiwashambulia mastaa hao kwamba kumpongeza Gabo peke yake kunaashiria kuwa hawakubaliani na ushindi wa mwigizaji huyo wa kike aliyewahi kuwa Miss Tanzania 2006.
Pamona na mashabiki kuja juu, mwigizaji  Eshe Buheti alikuwa na maoni tofauti na wenzake akionyesha kuamini kuwa Wema alistahili tuzo hiyo.
Hakuishia hapo Eshe aliwatupia lawama mastaa wa Bongo Movie kwa kudharau walipotakiwa kuwasilisha filamu ili zishindanishwe kwenye tuzo hizo.
"Mlitegemea nini wakati tulipoambiwa tupeleke filamu tulilegeza kamba, wenzetu wakatumia fursa. Hili ni funzo tumelipata nadhani mwakani kila mtu ataamka alipolala. Tuache maneno jamani, tupongezane kwa waliostahili.”
Mwingine aliyemtetea Wema ni mwigizaji Faiza Ally akisema waigizaji wana roho mbaya kwamba hawapendi kuona mwenzao akifanikiwa.

Mbunge CUF aibuka na Nondo bungeni

Dodoma. Mbunge wa Mgogoni (CUF) Dk Suleiman Ally Yussuf amehoji bungeni leo Jumatatu Aprili 3, 2018 sababu za Mwenyekiti wa Mtandao wa Wanafunzi Tanzania (TSNP), Abdul Nondo kuhoji sababu za kutopelekwa mahakamani kwa muda mrefu.
Nondo anayetuhumiwa kwa makosa mawili kwa sasa yupo nje ya dhamana. Kosa la kwanza ni kuchapisha taarifa za uongo mtandaoni Machi 7, 2018 akiwa Ubungo na kusambaza kwa kutumia mtandao wa WhatsApp kuwa yupo hatarini.
Shtaka la pili ni kutoa taarifa za uongo kwa watumishi wa umma mjini Mafinga alipokuwa akitoa taarifa katika kituo cha Polisi Mafinga kuwa alitekwa na watu wasiojulikana jijini Dar es Salaam na kupelekwa Kiwanda cha Pareti cha Mafinga.
Alikamatwa Machi 7 na kufikishwa Mahakama ya Wilaya ya Iringa  Machi 26.
Katika swali lake la  nyongeza Suleiman alitaka kujua ni kwa nini Nondo aliwekwa kwa muda mrefu katika kituo cha polisi bila ya kupelekwa mahakamani.
“Sheria gani inatumiwa na polisi kuwaweka mahabusu kwa muda mrefu na watu wanaotuhumiwa kuwa na makosa kama ilivyofanyika kwa kiongozi wa mtandao wa wanafunzi Abdul Nondo,” amehoji Suleiman.
Katika swali la msingi mbunge huyo amehoji ni kwa nini polisi wameshindwa kufanya kazi kwa weledi na kukamata watu pasipokuwa na ushahidi  kwa lengo la kukomoa tu.
Alitaka kujua iwapo kama Serikali haioni haja ya kuwawajibisha watendaji ambao wana tabia ya kuwakomoa wananchi kwa kuwakamata bila kuwa na ushahidi huku akidai anao ushahidi wa waliobambikiziwa kesi ambao ukihitajika anaweza kuwasilisha.
Akijibu maswali hayo kwa pamoja, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mwigulu Nchemba amesema polisi ni chombo kilichoundwa kwa mujibu wa katiba na sheria na linatekeleza majukumu yake kwa mujibu w akatiba.
Amesema polisi wana mamlaka kisheria kutuhumu, kukamata, kuhoji na kuweka watuhumia mahabusu kwa muda ulioruhusiwa kisheria endapo itabainika kuwa kuna viashiria au taarifa ya kuhusika katika kutenda kosa la jinai.
“Kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu za utendaji zinazoongoza jeshi la polisi inapobanika askari amebambika kesi kwa sababu zozote zile huchukuliwa hatua mbalimbali za kinidhamu ikiwmeo kufukuzwa,” amesema.
Hata hivyo, Mwigulu hakujibu chochote kuhusu Nondo lakini akasema suala la makosa makubwa na ya jinai uchunguzi wake huweza kuchukua muda mrefu zaidi na kuwa kesi zake huwa hazifutwi polisi au mahakamani kwa urahisi.