Friday, October 6

Wabunge kupewa fedha kuomba ushauri ukomo umri wa rais


Kampala, Uganda. Kila mbunge anatarajiwa kupewa kiasi fulani cha fedha zitakazomsaidia kupata ushauri kwa wapigakura jimboni kwake kuhusu Muswada wa Marekebisho ya Sheria wa 2017 unaolenga kuondoa ukomo wa umri kwa wagombea urais.
Baada ya muswada huo kusomwa kwa mara ya kwanza na Raphael Magyezi, mbunge wa Igara Magharibi kutoka chama tawala cha NRM, kisha kupelekwa katika Kamati ya Kudumu ya Sheria na Huduma za Bunge, Jumanne Spika Rebecca Kadaga aliwataka wabunge kwenda kushauriana na wapigakura wao.
Baada ya uamuzi huo wa Spika, mnadhimu mkuu bungeni Ruth Nankabirwa amesema Tume ya Bunge inafikiria kutenga bajeti maalumu kwa ajili ya kuwarahisishia wabunge.
“Tume ya Bunge inajiandaa kutengeneza bajeti kwa sababu ni Bunge ambalo litaturahisishia sisi sote …Tutaelezwa ni kiasi gani na namna gani kila mbunge atapata na kwenda kushauriana kwa sababu tunahitaji usafiri,” Nankabirwa ameviambia vyombo vya habari.
Nankabirwa hakuweka wazi undani wa bajeti hiyo akisema tu kwamba Tume ya Bunge ndiyo itapanga na kubainisha kiasi kinachohitajika. Lakini mbunge wa Kakumiro kutoka NRM, Robinah Nabbanja ambaye ni mjumbe wa Tume ya Bunge alisema mgawo huo utakuwa kwa wabunge wote bila kujali vyama vyao.
“Tutakutana haraka na kukubaliana. Sitaweza kukutajia kiwango kwa sasa kwa sababu bado hatujakubaliana. Huwezi kuwatuma wabunge (kupata ushauri) bila kuwawezesha kiasi,” amesema Nabbanja.
Kuhusu suala la wapi fedha hizo zitatoka hasa ikizingatiwa hazijatengwa katika bajeti ya sasa, Nabbanja amesema watapunguza kutoka kasma ya safari za nje.
“Jambo lolote linapokuwa la dharura, kwa kawaida huwa tunagusa fedha za usafiri wan je, tunaweza kuhamisha vifungu ndani ya bajeti,” amesema.
Mnadhimu wa kambi ya upinzani Ibrahim Ssemujju amepuuza uwezeshaji huo akiuelezea kuwa ni jaribio la “kusafisha rushwa kwa wabunge”.

HABARI ZA UKIMWI, KODI ZAONDOLEWA TUZO ZA EJAT

Habari za Ukimwi na Virusi vya Ukimwi (VVU), kodi na manunuzi ya umma, habari za uchambuzi na matukio na kundi la Afya ya Uzazi kwa Vijana, zimeondolewa katika makundi yatakayowania Tuzo za Umahiri wa Uandishi wa Habari(EJAT) kutokana na sababu mbalimbali ikiwamo rasilimali fedha.
Tuzo hizo zimezinduliwa rasmi leo ambapo makundi makundi matano kati ya 19, yamepunguzwa kutokana na sababu hizo.
Mwenyekiti wa maandalizi ya tuzo hizo zinazosimamiwa na Baraza la Habari nchini (MCT), Kajubi Mukajanga amesema mwaka huu kutakuwa na ushindani wa umahiri wa habari katika makundi 14 kati ya 19 yaliyokuwa yakishindaniwa mwaka jana.
Amevitaja vipengele vilivyobaki katika tuzo hizo ni habari za afya, habari za michezo na utamaduni, habari za uchumi, biashara na fedha, na uandishi wa habari za biashara, kilimo, elimu, utalii na uhifadhi, uchunguzi, data, haki za binadamu na utawala bora, mpiga picha bora wa magazeti na runinga, mchoraji katuni bora, habari za jinsia, wazee na watoto na kundi la wazi.
“Kazi zitakazoshindanishwa ni zile zilizochapishwa na kutangazwa kati ya Januari Mosi hadi Desemba 31 mwaka huu, na mwisho wa kuwasilisha kazi zao ni Februari 16, mwakani na tuzo hizi zitatolewa Aprili 27, mwakani,” amesema.

MBARONI KWA KUKUTWA NA MIRUNGI

JESHI la Polisi mkoani Morogoro, linawashikilia watu watatu   kwa tuhuma mbalimbali, ikiwamo  kukamatwa na dawa za kulevya aina ya bangi na mirungi.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Leonce Rwegasira, alisema tukio la kwanza lilitokea Septemba 26, mwaka huu  saa 9 usiku eneo la Mikese Mizani wilayani Morogoro Vijijini.
Aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Iddi Juma (42) ambaye ni  dereva na Mkazi wa Tabata-Segerea, Dar es Salaam na Aniset Ferdinand (30) mkazi wa Tabata-Chang’ombe.
Alisema watuhumiwa hao walikamatwa na kupekuliwa na askari waliokuwa doria na kukutwa na bangi viroba 6 inayokadiriwa kuwa na uzito wa kilo 80 wakiisafirisha kwenda Dar es Salaam, ikiwa kwenye gari lenye namba za usajili T438 ARN aina ya Toyota Corsa.
Alisema watuhumiwa pamoja na gari wanashikiliwa na Kituo cha Polisi Mikese.
Katika tukio jingine, Ally Daudi anashikiliwa na jeshi hilo kwa tuhuma za kukamatwa na vichane 27 vya mirungi akiwa amevihifadhi kwenye mfuko wa sandarusi.
Alisema mtuhumiwa alikamatwa Septemba 27, mwaka huu saa 10 jioni eneo  la Vibandani Manispaa ya Morogoro.

DIAMOND, ZARI MWISHO WANUKIA

Na JESSCA NANGAWE


UHUSIANO wa mwanamuziki maarufu wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’ na mjasiriamali Mganda, Zarina Hassan ‘Zari The Boss Lady’, unawaka moto na huenda wasiwe na mwisho mzuri, MTANZANIA linaripoti.
Penzi la wawili hao ambao wamejaaliwa watoto wawili; Tiffah na Nillan, limeonekana kupoteza afya tangu wakati na baada ya Diamond kukiri kwenye redio moja jijini Dar es Salaam, kuzaa na mwanamitindo Hamisa Mobetto.
Katika maelezo yake, wakati akithibitisha madai hayo ya muda mrefu, Diamond aliomba radhi kwa mzazi mwenzake Zari, lakini inaelezwa kuwa Zari hakuridhika na kurudisha moyo wa kumsamehe mpenzi wake.
Baada ya tukio la kuomba radhi, Diamond alionekana kwa mara ya kwanza akiwa pamoja na Zari kwenye sherehe ya kuzaliwa ya mzazi mwenzake huyo iliyofanyika nchini Afrika Kusini.
Aidha, Diamond kupitia ukurasa wake wa Instagram aliandikia ujumbe mzuri wa kumpongeza Zari kwa kumbukumbu yake ya kuzaliwa, huku akionyesha kujutia kwa kuchepuka na Hamisa.
Kinyume na matarajio ya wengi, wakati Diamond naye akiadhimisha siku yake ya kuzaliwa Oktoba 2, Zari hakuandika chochote kama walivyozoea kufanya wapendanao, badala yake zikaanza ‘vurugu za mitandao’ zilizoonyesha wazi penzi lao kwa sasa lipo kwenye wingu zito.
Tukio la hivi karibuni linaloonyesha kuwa ‘picha limeanza’ ni lile la Zari kufuta picha zote za Diamond kwenye ukurasa wake katika Mtandao wa Kijamii wa Instagram na kuacha picha tatu tu ambazo wamepiga na familia ya Diamond.
Baada ya Zari kufanya hivyo, Diamond naye alijibu mapigo kwa kufuta picha zote za mwaka huu za mrembo huyo isipokuwa picha mbili tu; moja ikiwa ya sherehe ya siku ya kuzaliwa ya Zari.
Zari alikwenda mbali zaidi kwa kuandika ‘maneno yenye ukakasi’ kupitia ukurasa wake kwenye Mtandao wa Kijamii wa Snapchat ambapo aliandika: “Hakuna tena uthibitisho wa wanaume kwenye mitandao ya kijamii na kukufanya kuonekana mjinga.”
Kituo cha Runinga cha NTV nchini Kenya katika taarifa yake ya habari ya juzi, kiliripoti taarifa za wawili hawa kuonekana kutengana.
Hatua hiyo imeendelea kuwaacha watu bila majibu ya uhakika, huku kila mmoja akiamini huo unaweza kuwa mwanzo wa mwisho wa penzi lao licha ya wenyewe kutoweka wazi kinachoendelea kati yao.
Wakati huohuo, mwanamitindo Hamisa Mobetto, mzazi mwenzake na Diamond amemburuza mahakamani msanii huyo kwa madai ya matunzo ya mtoto wao, Daylan ‘Abdulatiff’.
Habari zilizopatikana Dar es Salaam jana, zinasema kuwa kesi imefunguliwa katika Mahakama ya Watoto.
Katika madai yake Hamisa kupitia mawakili wake, Abdullah Lyana na Walter Godluck wa Kampuni ya Uwakili ya Century Attorneys, anaomba Diamond amuombe radhi kwa umma kwa kumsababishia madhara yaliyoishtua familia yake na pia amkubali mtoto huyo kuwa wake kwa masharti ya wazi.
Msanii huyo alitumiwa wito Septemba 14, mwaka huu akitakiwa mahakamani hapo kwa ajili ya mwafaka wa madai yaliyofunguliwa dhidi yake ambapo hakujibu. Kutokana na hali hiyo, Hamisa kupitia mawakili wake hao akafungua kesi kwa mujibu wa Sheria ya Watoto Namba 42, 43 na 98 ya mwaka 2009.
Anadai Diamond amlipe Sh milioni tano kwa mwezi kwa ajili ya matunzo yake na mtoto au zaidi kama mahakama itakavyoamua kutokana na hali yake kutotengemaa tangu amejifungua ambapo amekuwa akijihudumia mwenyewe.
Hamisa anadai alipwe Dola za Marekani 15,000 ambazo ni zaidi ya Sh milioni 30 kama gharama za mtoto hadi sasa.
Katika madai hayo, Hamisa pia anadai maombi hayo yakishindwa kutimizwa ndani ya siku saba baada ya mlalamikiwa kupokea wito huo, watafungua madai mapya dhidi yake ambayo yanajumuisha uamuzi wa baba wa mtoto.
Aidha, katika madai hayo atalazimika kudai fidia kutokana na matusi na maneno yasiyofaa dhidi yake yaliyotolewa na Diamond na mpenzi wake Zari ambayo yamemsababishia maumivu.
Aidha, Hamisa amekubali kuwa alikuwa na uhusiano wa kimapenzi na Diamond, ambapo walikubaliana uwe wa siri uliomsababishia kupata mimba na kufanikiwa kupata mtoto wa kiume.
“Kutokana na ujauzito huo, alikubali kuachana na kazi yake ya uanamitindo ili kupata nafasi kubeba kitu ambacho ulikuwa unakihitaji sana (mtoto) kwa mujibu wa maneno yako mwenyewe, ambapo alijitolea kwa ajili ya kujiandaa kuwa mama.
“Katika uhusiano wenu mara baada ya kujifungua Agosti 8, mwaka huu ndipo maigizo yalipoanza baada ya wewe kuamua kuchagua hospitali ya yeye kujifungulia na daktari wa kumhudumia, lakini hukufanya malipo yoyote, hatua iliyosababisha mteja wetu na mama yake kuhangaika na kulipa gharama zote peke yao.
“Mwisho wa siku uliacha kabisa kumhudumia mteja wetu pamoja na mtoto wake, ambapo ilimlazimu mama yake kumhudumia yeye na mjukuu wake hasa ukizingatia mteja wetu amejifungua kwa njia ya upasuaji, ambapo anahitaji zaidi uangalizi wa karibu, maziwa, nguo na fedha za matumizi kutoka kwako ukiwa baba mtoto wake lakini aliambulia matusi, kudhalilishwa na maneno machafu kutoka kwa timu yako,” anadai Hamisa katika madai yaliyoandikwa na wakili wake.
Pamoja na mambo mengine, Hamisa anadai Diamond ameendeleza vitimbi kwa kumdhalilisha kwenye vyombo vya habari pamoja na mtoto wake, hali inayomuumiza  pamoja na familia na mashabiki wake.
“Pamoja na hayo, mteja wetu hakuwahi kujibu chochote hata pale uliposema mimba si yako katika mahojiano mbalimbali uliyofanya na vyombo vya habari.
“Mteja wetu amekuwa mvumilivu ambapo ulitumia udhaifu wake huo wewe na mpenzi wako, Zarina Hassan kwa kumtishia maisha, kumtukana na kumdhalilisha yeye na mtoto wake kwa kumtumia ujumbe mfupi wa maandishi na katika mitandao ya kijamii ikiwamo Instagram, Facebook na mingineyo,” maelezo hayo yamesema yakimnukuu Hamisa.

AJINYONGA BAADA YA KUUA MKE WAKE

Na Mohamed Hamad-Kiteto

MKAZI wa Kijiji cha Banyibanyi mkoani Dodoma, Mussa Chisimilo (37), amejinyonga kwa shuka hadi kufa, baada ya kudaiwa  kumuua mke wake, Edna Chisimilo (26) kwa kumkata na jembe kichwani.
Tukio hilo lilitokea Kitongoji cha Mbeli wilayani Kiteto mkoani Manyara, kutokana na ugomvi wa kifamilia ambao unadaiwa kusababishwa na wivu wa mapenzi
Mwenyekiti wa Kijiji cha Kimana, Willison Ngolanya, aliliambia MTANZANIA kuwa tukio hilo lilitokea Agosti 4, mwaka huu.
Alisema mtuhumiwa alitekeleza mauaji usiku na kutoweka, lakini alfajiri  majirani zake walikuta  mke akiwa amefariki.
Baada ya taarifa kutolewa kwa uongozi ndipo zikapatikana tena  taarifa zingine kuwa naye amejinyonga juu ya mti kwa kutumia shuka yake.
Taarifa kutoka kwa familia zinasema marehemu wameacha watoto watatu wadogo ambao wanahitaji malezi ya karibu.
Walisema mwanamume atazikwa Kitongoji cha Mbeli ya Kiteto na mwanamke alisafirishwa kwenda Kijiji cha Dongo Kiteto.
Jeshi la Polisi mkoani Manyara limethibitisha kutokea tukio hilo na kudai uchunguzi unafanyika.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Manyara, Francis Massawe, alisema mwanamume huyo alimuua mke wake kwa kumkata kwa jembe kichwani.

IGP SIMON SIRRO ATEMBELEA NJOMBE, AWATAKA WANASIASA KUTOLIINGILIA JESHI LA POLISI ILI LIENDELEE NA KAZI ZAKE

 Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini (IGP) Simon Sirro, akiwasili uwanja wa ndege wa Njombe, kwa ziara ya kikazi ya siku moja akitokea mkoani Ruvuma, ili kuzungumza na maafisa na askari wa Jeshi hilo pamoja na kuona changamoto wanazokutana nazo wanapotekeleza majukumu yao na namna ya kuwasaidia. 

 Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini (IGP) Simon Sirro, akikagua gwaride maalumu lililoandaliwa kwa ajili yake alipowasili mkoa Njombe, kwa ziara ya kiazi ya siku moja 
Wajumbe wa kamati ya Ulinzi na Usalama ya mkoa wa Njombe, wakimsikiliza Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini (IGP) Simon Sirro, ambaye yupo mkoani humo kwa ziara ya kikazi ya siku moja yenye lengo la kuzungumza na maafisa na askari wa Jeshi hilo na kuona changamoto wanazokutananazo wanapotekeleza majukumu yao na namna ya kuwasaidia. 
Picha na Jeshi la Polisi.

Mahakama kuwahoji Odinga na Musyoka

Mwendesha mashitaka Kenya ameagiza viongozi wa muunganao wa upinzani NASA, Raila Odinga na Kalonzo Musyoka, wahojiwe kuhusiana na kauli zao walizotoa kuwa uchaguzi mpya wa Oktoba 26 hautafanyika.

 
Sikiliza sauti03:07

Mahojiano na Herman Manyora

Mahakama ya Juu iliamuru uchaguzi mkuu urudiwe baada ya kufuta matokeo ya awali ya uchaguzi wa August 8, ambapo rais Uhuru Kenyatta alishinda. DW imezungumza na mmoja wa wachambuzi nchini humo, Herman Manyora ambaye anatoa maoni yake kuhusiana na hatua hiyo.

Mjadala wa udhibiti wa umiliki bunduki washika kasi Marekani

Chama kinachotetea umiliki wa bunduki nchini Marekani NRA chataka shirika la udhibiti wa bunduki na zana za milipuko ATF kutafakari kubadilisha sheria kuhusu vifaa vinavyoongezea bunduki uwezo zaidi.

Bump Stock Waffe USA (Getty Images/G.Frey)
Wabunge wa Marekani hapo Alhamisi waliimarisha  juhudi zao za kupiga marufuku vifaa vilivyotumiwa na mshambuliaji wa Las Vegas vilivyowezesha bunduki yake kufyatua risasi kwa haraka. Kadhalika chama cha kitaifa cha wamiliki bunduki kimewahimiza maafisa wa shirikisho kuujadili uhalali wa kisheria wa vifaa hivyo.
Bila ya kutarajiwa, Chama kinachotetea umiliki wa bunduki nchini Marekani NRA kilivunja utamaduni wake wa tangu zamani wa kuzipinga juhudi zozote za kudhibiti umiliki wa bunduki, pale kilipolitaka shirika la udhibiti wa bunduki na zana za milipuko  ATF kutafakari kubadilisha sheria .
Kwenye taarifa yake, NRA inaamini kuwa vifaa vinavyowezesha bunduki ndogo kufanya kazi kwa nguvu kubwa sawa na bunduki zenye uwezo mkubwa zinapaswa kuwekewa sheria zaidi.
Kifaa kinachounganishwa na bunduki kuipa uwezo mkubwa kufyatua risasi
Kifaa kinachounganishwa na bunduki kuipa uwezo mkubwa kufyatua risasi
White House ipo tayari kwa mjadala wa kudhibiti umiliki wa bunduki
Huku maafisa wa polisi wakichunguza kilichomsababisha Stephen Paddock kuwaua watu 58 na kuwajeruhi 500 katika tamasha la muziki mjini Las Vegas mapema wiki hii, Ikulu ya White House pia ilitangaza kuwa ipo tayari kwa mazungumzo zaidi kuhusu vifaa hivyo. Juhudi za mtangulizi wa trump, Brack  Obama kutaka udhibiti wa bunduki hazikuzaa matunda.
Hata hivyo baadhi ya Wademocrats sasa wanasema ipo haja kubwa kudhibiti umilikaji huo. Seneta wa jimbo la California Dianne Feinstein asema: "Lazima tuseme yanatosha . Lazima tuseme hakuna haja ya kuibadilisha bunduki ndogo kuwa ysawa na silaha kamili  maangamizi makubwa ya vitani."
 Wakati Bunge la Marekani likionekana kujiandaa kujadili uwezekano wa kudhibiti umiliki wa bunduki kwa mara ya kwanza, imebainika kuwa huenda Paddock alipanga kufanya mashambulizi kama hayo katika miji mingine mikuu.

Ghala la matairi la Superdoll lawaka moto


Dar es Salaam. Ghala la matairi ya magari la kampuni ya Superdoll lililopo Barabara ya Nyerere limeugua kwa moto.
Ghala hilo lililopo jirani na jengo la Quality Center limeungua leo Ijumaa mchana.


Jeshi la Zimamoto na Uokoaji limefika eneo hilo la tukio na uokoaji wa mali umefanyika.

Mpinzani wa Kagame Diane Rwigara afikishwa mahakamani Rwanda

Rwigara alifikishwa mahakamani akiwa amefungwa pingu
Mwanasiasa wa upinzani nchini Rwanda Diane Rwigara, mamake na dadake wamdefikishwa mahakamani mjini Kigali kwa mara ya kwanza wiki mbili baada ya kuzuiliwa na polisi.
Watatu hao wameshitakiwa kuchochea uasi nchini, mashtaka wanayokanusha wakisema yana misingi ya kisiasa.
Diane Rwigara alizuiwa kugombea kiti cha urais katika uchaguzi uliofanyika mwezi wa 8 mwaka huu ambapo Rais Paul Kagame alishinda kwa asilimia 98 ya kura.
Mwandishi wa BBC Yves Bucyana mjini Kigali anasema chumba cha mahakama kilikuwa kimejaa watu wengi miongoni mwao wanadiplomasia wa baadhi ya nchi za Magharibi na Marekani.
Ulinzi ukiwa umeimarishwa, watuhumiwa hao watatu waliingizwa mmoja baada ya mwingine katika chumba cha mahakama huku wakifungwa pingu.
Jaji alifungua kikao kwa kusikiliza hoja ya watuhumiwa, Diane Rwigara na Mamake Adeline Rwigara wamesema wana tatizo la kuwasiliana na mawakili wao.
Rwigara
Wamesema wameweza kuwasiliana mara moja tu kabla ya mawakili kukataliwa kuwaona tena huku Dadake Anne Rwigara yeye akisema kuwa hajapa wakili.
Wote wameomba kesi kuahirishwa ili kupata muda zaidi wa kutayarisha kesi dhidi yao.
Hoja hiyo imekubaliwa kwa kesi kuahirishwa hadi Jumatatu wiki ijayo.
Mashitaka yanayowakabili yalikuwa tayari yamewekwa hadharani na mwendeshamashtaka kabla ya wao kufikishwa mahakamani leo.Wote watatu wameshitakiwa kuchochea uasi miongoni mwa wananchi.
Zaidi ya hayo, Diane Rwigara ameshtakiwa kughushi nyaraka huku Mamake Adeilne Rwigara akishtakiwa pia kosa la kugawa wananchi kwa misingi ya kikabila.
Awali walipokuwa katika ngazi ya upelelezi wa mwanzo walishitakiwa makosa ya kutaka kuiangusha serikali na ulaghai wa kukwepa kulipa kodi, lakini makosa hayo yalifutwa.
Wote wanapinga mashitaka dhidi yao wakisema yana misingi ya kisiasa.Diane Rwigara mwenye umri wa miaka 35 alizuiliwa kugombea kiti cha urais uliofanyika mwezi wa 8 mwaka huu.
Tume ya uchaguzi ya Rwanda ilisema kwamba alifanya ulaghai katika kutafuta saini za wafuasi wake ili kutimiza matakwa ya tume hiyo.
Tangu ulipoanza mchakato huo wa kutaka kuingia ikulu,Diane Rwigara amejitokeza kama mpinzani na mkosoaji mkuu wa chama tawala RPF.
Na baada ya kukataliwa kugomea urais alianzisha vugugugu alilotaja kuwa na lengo la kupinga uonevu na kupigania haki miongoni mwa wananchi.

Godbless Lema aweka wazi anavyofatiliwa na wasiojulikana


Mbunge wa Arusha Mjini kupitia CHADEMA Godbless Lema leo amesimama mbele ya Waandishi wa habari Dar es salaam na kueleza jinsi anavyofatiliwa na watu wasiojulikana kutishiwa maisha yake.
Lema amesema “Mimi niko kwenye target na wameshindwa kuelewa kwanini wananishindwa maana wamenitafuta sana, kila mtu ametishwa, Nassari ametishwa…. mimi pia walinifatilia usiku saa sita na gari nikakimbiza sana gari, nikaacha usukani nikamuacha mke wangu nikakimbia machakani
Unaweza kumtazama Godbless Lema na viongozi wengine wa CHADEMA wakiongea kwa urefu kwenye hii video hapa chini.

Mipango ya kumpeleka Tundu Lissu Marekani yasimamishwa


Siku 14 sasa zimepita tangu Mbunge wa Singida Mashariki Tundu Lissu apigwe risasi na watu wasiojulikana akiwa nyumbani kwake Dodoma kisha kupelekwa kwenye matibabu katika Hospitali ya Nairobi Kenya huku watu wa jamii mbalimbali wamekuwa wakihamasishwa kuchangia huduma za matibabu yake.
Watu mbalimbali wameendelea kumtembelea Lissu Hospitali kumjulia hali na miongoni mwao ni Mbunge wa Singida Kaskazini Lazaro Nyalandu ambaye kupitia account zake za Twitter na Facebook ameeleza kuwa wanasubiri ripoti ya Madaktari kujua mwenendo wa matibabu ili kuwapatia madaktari bingwa wa Marekani.
Tumekuwa #NairobiHospital tukisubiri MADAKTARI watoe RIPOTI ya mwenendo wa MATIBABU ya Mh #TunduLissu kwa minajili ya kuwapatia MADAKTARI BINGWA wa Marekani na kuona uwezekano wa Mh #TunduLissu kupatiwa RUFAA kwa matibabu zaidi NJE., LAKINI bado KALAMU zao ni nzito kuandika RIPOTI hii siku ya tatu tangu tuahidiwe.
Binafsi, nimerudi NAIROBI tangu JANA kushiriki maandalizi ya uwezekano wa kumhamishia Mh #TunduLissu Marekani kwa ajili ya huduma yenye ubora zaidi, endapo MADAKTARI wa #NairobiHospital wangeridhia. Kesho asubuhi nitarejea hospitalini kusikiliza kauli ya mwisho ya MADAKTARI kuhusu 

YALIYOJIRI KORTINI KUHUSU KESI YA VIONGOZI WA SIMBA

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu imeahirisha kesi ya utakatishaji fedha na kugushi inayowakabili Rais wa Simba, Evans Aveva na Makamu wake, Geofrey Nyange ‘Kaburu’ hadi October 11, 2017 kwa sababu upelelezi haujakamilika.
Mwendesha Mashtaka wa TAKUKURU, Leornad Swai amemueleza Hakimu Mkazi Mkuu, Godfrey Mwambapa kuwa shauri hilo limeitishwa kwa ajili ya kutajwa na upelelezi haujakamilika, hivyo anaomba ipangiwe tarehe nyingine ambapo baada ya kueleza hayo Hakimu Mwambapa aliahirisha kesi hiyo hadi October 11, 2017.
Evans Aveva na Makamu wake, Geofrey wanakabiliwa na mashtaka matano ya kughushi, kuwasilisha nyaraka ya uongo na kutakatisha Dola za kimarekani 300,000.
Katika shtaka la kwanza, washtakiwa hao wanadaiwa kuwa walikula njama ya kughushi fomu ya maombi ya kuhamisha fedha ya March 15, 2016 wakionesha Klabu ya Simba inalipa mkopo wa Dola za kimarekani 300,000 kwa Evans Aveva wakati si kweli.
Katika shtaka la pili alidai kuwa March 15, 2016 katika benki ya CRDB tawi la Azikiwe Ilala, Aveva akijua alitoa nyaraka ya uongo ambayo ni fomu ya maombi ya kuhamisha fedha ya March 15, 2016 wakati akijua ni kosa.
Katika la tatu la kutakatisha fedha, Aveva na Nyange wanadaiwa kuwa kati ya March 15 na June 29, 2016 Dar es Salaam  kwa pamoja walikula njama ya kutakatisha fedha kwa kupata Dola za kimarekani 300,000 wakati wakijua ni zao la uhalifu.
Kwa upande wa shtaka la nne la kutakatisha fedha, Aveva anadaiwa kuwa kati ya March 15, 2016 katika benki ya Barclays Mikocheni alijipatia Dola za kimarekani 300,000 wakati akijua zimetokana na kughushi.
Katika shtaka la tano la kutakatisha fedha, mshtakiwa Nyange anadaiwa kuwa March 15, 2016 katika benki ya Barclays tawi la Mikocheni alimsaidia Aveva kujipatia Dola za kimarekani 300,000 wakati akijua fedha hizo zimetokana na kughushi.
Washtakiwa wapo rumande kwa sababu shtaka la kutakatisha fedha linalowakabili halina dhamana.

Tanzania: Nchi Wanachama Jumuiya ya Afrika Mashariki Zitunge Sheria Zinazolingana Katika Udhibiti wa Dawa

Image result for east africa community

Tanzania imetoa wito kwa nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki kutunga sheria zinazolingana ili kuwezesha udhibiti wa pamoja wa dawa na vifaa tiba zinazoingia katika nchi wanachama.
Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dk. Mpoki ametoa wito huo leo wakati akifungua Kikao cha Siku Mbili cha Kamati ya Maandalizi ya Mpango Ulinganishaji wa Kanuni za Usimamizi wa Dawa kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki unaofanyika katika Hoteli ya New Africa jijiji Dar es Salaam.
“Juhudi za kweli hazina budi kuchukuliwa kudhibiti utengenezaji na uingizaji wa dawa zisizokidhi viwango ambazo mwishowe huwafikia watumiaji na matokeo yake ni wananchi kuathirika kwa kupata madhara makubwa kiafya”Dk. Mpoki alieleza.
Alisisitiza kuwa “magonjwa hayajui mpaka” hivyo uwepo wa dawa zenye ubora unaofanana katika nchi wanachama kunarahisisha matibabu kwa wagonjwa na kunaepusha matumizi ya dawa hafifu katika nchi moja ambako kunakoweza kusababisha usugu wa vidudu vya maradhi.
Dk. Mpoki alieleza wajumbe wa Kamati hiyo ambao ni wawakilishi wa mamlaka za udhibiti wa dawa za nchi wanachama kuwa jukumu na wajibu wa kuhifadhi na kuinua afya ya jamii katika jumuiya lazima zitambuliwe na ziungwe mkono na nchi wanachama  kupitia wizara zinazosimamia sekta ya afya.
“Mamlaka hizi zimekuwa kama mlango unaolinda mfumo wa utoaji huduma za afya dhidi ya vifaa tiba na dawa zenye viwango duni, zisizo salama na zisizofanyakazi vyema kuingia katika masoko yetu“Dk. Mpoki alieleza.
Alibainisha kuwa Tanzania ndio iliyopewa jukumu la kusimamia suala la kanuni hivyo kupitia ufadhili wa washirika mbali mbali wa maendeleo, watalaamu wanaohusika na usalama na dawa na vifaa tiba hukutana mara kwa mara kufanya tathmini kuangalia hatua iliyofikiwa.
“Lengo la Jumuiya ni kuhakikisha kuwa ikifika mwisho wa mwaka huu dawa au kifaa tiba kikiingia katika moja katika nchi zetu kinakuwa na ubora ulio sawa” Dk. Mpoki.
Katibu Mkuu huyo alieleza pia maazimio ya mkutano huo yatapelekwa, kupitia kwa makatibu wakuu, kwenye Kikao cha Mawaziri wa sekta husika kitakachofanyika nchini Uganda tarehe 23-25 Oktoba mwaka huu.
Mkutano huu ulitanguliwa na mafunzo ya wiki mbili kwa wataalamu wa udhibiti na ukaguzi wa dawa kutoka nchi wanachama ambayo yalikuwa yakiendeshwa kwa pamoja kati ya TFDA na Shule ya Famasi ya Chuo Kikuu cha Tiba na Sayansi ya Afya Muhimbili.
Akimkaribisha, Mgeni Rasmi, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Chakula na Dawa nchini (TFDA) Bwana Hiiti Sillo aliwashukuru washirika mbalimbali wa Maendeleo ambao wamekuwa wakisaidia programu hiyo ya ulinganishaji kanuni za udhibiti na ukaguzi wa dawa.