Monday, September 4

MKURUGENZI MKUU WA FAO KUZURU TANZANIA, KUFANYA MAQZUNGUMZO NA VIONGOZI WAANDAMIZI WA SERIKALI, WADAU


Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa, (FAO), José Graziano da Silva(pichani), Jumanne wiki hii ataanza ziara rasmi nchini Tanzania ambapo anategemewa kufanya mikutano na mazungumzo na maofisa waandamizi wa serikali na wadau.
Bw. Graziano da Silva anategemewa kukutana na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli na Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Dkt. Ali Mohamed Shein.
Mkurugenzi Mkuu wa FAO amepanga kufanya mikutano na Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi (Tanzania Bara), Dkt. Charles Tizeba, na Waziri wa Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi wa Zanzibar, Hamad Rashid Mohamed.
Ziara hii ya Mkurugenzi Mkuu inakuta wakati FAO ikiadhimisha miaka 40 toka kuanza shughuli zake hapa Tanzania. Wakati wa ziara hii, Bw. Graziano da Silva atakutana na uongozi na wafanyakazi wa FAO hapa Tanzania kabla ya kuhudhuria hafla maalum hapa Dar es Salaam kusherehekea maadimisho hayo. Hafla hiyo itahudhuriwa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Bi. Samia Suluhu Hassan.
Mwakilishi Mkazi wa FAO hapa nchini, Bw. Fred Kafeero, amethibitisha kuwa Bw.  Graziano da Silva atakuwa hapa nchini kufuatia mwaliko wa Serikali ya Tanzania. “Mkurugenzi Mkuu wa FAO atabadilishana mawazo na Serikali ya Muungano wa Tanzania kwenye masuala makuu yanayohusiana na uhakika wa chakula na maendeleo ya kilimo, ikijumuisha juhudi za FAO kitaifa na kikanda,” alisema. Bw. Graziano da Silva pia atajadili mambo mengine yanayohusiana na ushirikiano kati ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na FAO, pia masuala mengine ya umuhimu kati ya pande hizo mbili, aliongeza. Mbali ya Maafisa wa Serikali, Mkurugenzi Mkuu atakutana na wadau wengine wa FAO hapa nchini wakiwa ni pamoja na asasi za kiraia, taasisi za elimu, na taasisi za utafiti.
Baadae Mkurugenzi Mkuu ataenda Zanzibar ambapo, miongoni mwa mambo mengine, anategemewa kuweka jiwe la msingi katika jingo la Mradi wa Kuzalisha vifaranga vya samaki unaofadhiliwa na Serikali ya Jamhuri ya Korea kupitia Shirika lake la Maendeleo ya Kimataifa KOICA.  Pia Bw. Graziano da Silva atapata fursa ya kutembelea mradi wa kilimo cha mwani na pia kuona maonesho ya bidhaa mbali mbali zilizotengenezwa na wanawake wanaojihusisha na kilimo cha mwani.

Tanzania ilijiunga na FAO mwaka 1962, na mwaka 1977 FAO ilifungua ofisi zake hapa Tanzania. Katika miaka 40 ya uwepo wake, FAO imeisadia Serikali ya Tanzania katika kupanga na kutekeleza sera, mikakati na mipango ya kilimo hapa nchini. Kazi ya FAO imejikita katika kuboresha usalama wa chakula na lishe pamoja na maisha ya wakulima wadogo na hivyo kuwa chachu ya kukua kwa uchumi kupitia sekta ya kilimo. 

Marekani kuipiga Korea Kaskazini ikimgusa mshirika wake

Trump amesema Korea Kaskazini inajitafutia matatizo
Image captionTrump amesema Korea Kaskazini inajitafutia matatizo
Waziri wa masuala ya ulinzi wa marekani James Mattis amesema kuwa tishio lolote kutoka korea kaskazini kwa Marekani ama washirika wake litajibiwa vikali na jeshi.
Mattis amezungumza hayo baada ya mkutano wake na Rais Trump juu ya masuala ya usalama wa nchi kufuatia jaribio la nyuklia huko Pyongyang.
Trump ameonya kuwa Marekani inaweza kusimamisha kufanya biashara na nchi yoyote inayoshiriki biashara na Korea Kaskazini.
China ndio mshirika mkuu wa baishara na Pyongyang, ameongeza kuwa korea kaskazini imekua tishio na imeleta fedheha kwa Beijing.
Alivyoulizwa na waandishi wa habari kama Marekani itashambuliwa na korea kaskazini, rais trump alisema kuwa tutaona''
Nayo korea kusini imesema kuwa imefanya majaribio matano kama majibu ya jaribio la nyuklia la korea kaskazini.
Image captionRais wa Korea Kaskazini Kim Jong-un, (katikati) akipokea maelekezo ya namna bomu hilo linavyofanya kazi
Rais wa Urusi na Raisi wa china wote wamesisitiza juu ya umuhimu wa kuondokana mzozo wa Korea.
Nao Japan wamesema kuwa jaribio hilo si la kusamehewa.
Jaribio hilo ni la sita kufanywa na kore kaskazini katika kipindi cha miaka 10.
Limesababisha tetemeko la ardhi lenye ukubwa wa 6.3 lilifika katika mkoa wa china uliokaribu na Korea Kaskazini.

Njiwa aliyetumiwa kusafirisha mihadarati hadi gerezani Argentina

Pigeon found carrying drugs in KuwaitHaki miliki ya pichaAL-RAI
Image captionMaafisa waligundua kuwa ndege huyo alikuwa amefungiwa mfuko mdogo kwenye mgongo wake uliokuwa na tembe za madawa ya kulevya
Polisi nchini Argentina walimpiga risasi njiwa ambaye alitumiwa kusafirisha mihadarati kwenda gereza moja, kwa mujibu wa mamlaka za gereza.
Njiwa huyo alionekana akiruka hadi uwanja wa gereza lililo mji wa Santa Rosa.
Maafisa waligundua kuwa ndege huyo alikuwa amefungiwa mfuko mdogo kwenye mgongo wake uliokuwa na vidonge vya madawa ya kulevya.
Njia hiyo ya kusafirisha madawa ilikuwa imegunduliwa na ilikuwa ikifanyiwa uchunguzi.
Gazeti la Clarin lilichapisha picha ya njiwa huyo akiwa na mfuko mweupe uliokuwa na tembe 44 za madawa ya kulevya.
Magereza nchini Argentina yalionya mwaka 2013 kuwa walanguzi wa madawa ya kulevya walikuwa wakitumia njiwa waliokuwa wakifanya safari mara 10 hadi 15 kwa siku.
Watu watatu walikamatwa na njiwa 15 kupatwa baada ya uchunguzi wa mwaka 2013.
Mapema mwaka huu njiwa ambaye alikuwa na mfuko uliokuwa na tembe 178 za dawa ya kulevya alishikwa nchini Kuwait karibu na mpaka na Iraq.

Kamera ya kupiga picha ndani ya mwili wa binadamu yagunduliwa

Kamera mpya inavyofanya kazi ya kubaini photons ndani ya mwili wa binadamuHaki miliki ya pichaGETTY IMAGES
Image captionKamera mpya inavyofanya kazi ya kubaini photons ndani ya mwili wa binadamu
Wanasayansi wamebuni kamera yenye uwezo ya kupiga picha viungo vya ndani ya mwili wa binadamu.
Kifaa hicho kimeundwa kuwasaidia madaktari kusaka vifaa vya madaktari, vinavyofahamika kama endoscopes, amvayo huenda vinaweza kusalia ndani ya viungo vya binadamu wakati wa upasuaji.
Hadi sasa, matabibu wamekuwa wakitegemea uchunguzi unaogharibu fedha nyingi, kama vile picha za X-ray, ili kufuatilia mafanikio yao.
Kamera hiyo mpya, itafanya kazi ya kubaini mwanzo wa mwangaza ndani ya mwili wa binadamu, kama vile sehemu ya ncha ya mwisho ya kifaa cha upasuaji cha tube ya endoscope.
Kifaa kihi kimeundwa kumsaidia madaktari kusaka vifaa vya kimatibabu vinavyojulikana kama endoscopes mwilini mwa binadamuHaki miliki ya pichaGETTY IMAGES
Image captionKifaa kihi kimeundwa kumsaidia madaktari kusaka vifaa vya kimatibabu vinavyojulikana kama endoscopes mwilini mwa binadamu
Profesa Kev Dhaliwal, wa Chuo Kikuu cha Edinburgh, anasema: "Ina uwezo mkubwa wa kutumika katika hali tofauti tofauti, kama vile inavyoelezwa ikiwa kazini. "Uwezo wa kuona iliko kifaa kilichosahaulika ndani ya mwili wa binadamu hasa katika sekta mbalimbali ya kitengo cha kiafya, huku tukisonga mbele kupunguza hali na mbinu ya kila aina ya kutibu maradhi mbalimbali."
'tishu na viungo'
Majaribio ya awali, inaonyesha kifaa cha prototype, kinaweza kubaini na kufuatilia mwangaza kupitia eneo la mshipa wa sentimita 20, katika hali tu ya kawaida.
Miali ya mwangaza kutoka kwa endoscope, inaweza kupenyeza ndani ya mwili, lakini mara nyingi hutawanyika au kuangazia nje ya mshipa na viungo, badala ya kupernyesa moja kwa moja mwilini.
Hali hii inatatiza hali ya kupata picha halisi ya iliko kifaa kilichoachwa mwilini.

Korea Kusini yafanya majaribio ya makombora kujibu majaribio ya Korea Kaskazini

This handout photo taken on 4 September 2017 and provided by South Korean Defence Ministry in Seoul shows South Korea's missile system firing Hyunmu-2 missile into the East Sea from an undisclosed location on South Korea's east coast during a live-fire exercise simulating an attack on North Korea's nuclear site.Haki miliki ya pichaAFP/GETTY IMAGES
Image captionKorea Kusini yafanya majaribio ya makombora kujibu majaribio ya Korea Kaskazini
Korea Kusini imefanya mazoezi ya makombora yake kuashiria shambulizi dhidi ya Korea Kaskazini, kujibu jaribio la sita la nyuklia lililofanywa na Korea Kaskazini.
Mazoezi hayo yalihusu kurushwa kwa makombora ya masafa marefu kutoka kwa ndege za kivita na ardhini.
Hii ni baada ya waziri wa ulinzi wa Marekani James Mattis kuonya kuwa tisho lolote kwa Marekani au washirika wake kutoka Korea Kaskazini litajibiwa vikali kijeshi.
Korea Kaskazini ilisema kwa ilifanyia jaribio bomu la haidrojeni linaloweza kuwekwa kwa kombora la masafa marefu.
This handout photo taken on 4 September 2017 and provided by South Korean Defence Ministry in Seoul shows South Korea's missile system firing Hyunmu-2 missile into the East Sea from an undisclosed location on South Korea's east coast during a live-fire exercise simulating an attack on North Korea's nuclear site.Haki miliki ya pichaAFP/GETTY IMAGES
Image captionKorea Kusini yafanya majaribio ya makombora kujibu majaribio ya Korea Kaskazini
Korea mara kwa mara imekiuka vikwazo vya Umoja wa Mataifa na shinikzo za kimataiafa ya kuitaka iachane na mpango wake wa zana za nyuklia.
Ndani ya miezi mwili iliyopita, Korea Kaskazini imefanya majaribio ya makombra ya masafa marefu na hata kurusha kombora kupitia juu ya anga ya Japan hadi bahari ya Pacific.
Baraza la ulinzi la Umoja wa Mataifa litafanya mkutano wa dharura leo kujadili jibu la hatua hiyo ya Korea Kaskazini.
North Korean leader Kim Jong-un in this undated photo released by North Korea's Korean Central News Agency (KCNA) in Pyongyang September 3, 2017.Haki miliki ya pichaREUTERS/KCNA
Image captionKorea Kaskazini ilisema kwa ilifanyia jaribio bomu la haidrojeni linaloweza kuwekwa kwa kombora la masafa marefu

Venezuela yatoa dola milioni 5 kuisaidia Marekani kukabili kimbunga Harvey

Helikopta ikipita baadhi ya sehemu zilizoathirika vibaya kusaidia uokoaji
Image captionHelikopta ikipita baadhi ya sehemu zilizoathirika vibaya kusaidia uokoaji
Serikali ya Venezuela imesema itachangia dola milioni tano kama msaada kwa wahanga wa kimbunga Hurricane Harvey kilichoipiga Texas mwishoni mwa mwezi uliopita.
Waziri wa mambo ya nje wa Venezuela Jorge Arreazza amesema msaada huo utatoka katika sehemu ya mapato ya kampuni kubwa ya mafuta ya Citgo.
Arreazza amesema kwa kuzingatia ubinaadam, nchi yake imeamua kuweka kando tofauti za kisiasa na kusaidia watu.
Citgo iliwekewa vikwazo vya kiuchumi mwezi uliopita kwa sababu kwamba Rais wa Venezuela Nicolas Maduro anakiuka haki za kibinaaman na kukandamiza demokrasia.

Somalia yaonya mpango wa Alshabab kusambaza uranium Iran

Wapiganaji hao wamekua wakichimba madini ya uranium katika mkoa wanaoushikilia
Image captionWapiganaji hao wamekua wakichimba madini ya uranium katika mkoa wanaoushikilia
Serikali nchini Somalia imeonya kuwa wapiganaji wa Alshabab wana mpango wa kusambaza uranium huko Iran wakipata msaada kutoka Marekani.
Waziri wa mambo ya nje wa Somalia Yusuf Garaad amesema kuwa wapiganaji hao wamekua wakichimba madini ya uranium katika mkoa wanaoushikilia.
Mwandishi BBC wa masuala ya usalama Afrika amesema kuwa madai hayo hayajaeleza ni jinsi gani Alshabab wanachimba ama kusambaza madini hayo.
Idara ya ulinzi ya Marekani haijatoa maelezo yoyote.

Merkel asema Uturuki haiwezi kuingia Umoja wa Ulaya

Baada ya mdahalo huu, Merkel ameonekana kumpita wazi Schulz
Image captionBaada ya mdahalo huu, Merkel ameonekana kumpita wazi Schulz
Kansela wa Ujerumani Angela Merkel amesema kuwa anaamini kuwa Uturuki haiwezi kuingia kwenye umoja wa ulaya na kusema kuwa atahakikisha anasisitiza kutokuwepo kwa mazungumzo ya kukubaliwa Uturuki kujiunga na Umoja wa Ulaya.
Markel ambae anawania kushinda muhula wa nne katika uchaguzi utakaofanyika mwezi huu amezungumza hayo katika mdahalo na mpinzani wake Martin Schulz ulioonyeshwa kwenye televisheni.
Mahusiano kati ya Berlin na Ankara yameingia mashakani baada ya raia wa ujerumani kuwekwa kizuizini nchini Uturuki.
Mdahalo huo ulikijita katika suala la maelfu ya wahamiaji waliongia ujreumani.
Merkel alionekana kuungwa mkono na wengi alipowasili kwenye mdahalo
Image captionMerkel alionekana kuungwa mkono na wengi alipowasili kwenye mdahalo
Markel alikubali kuwa kuna mafunzo aliyoyapata.
Schulz alimshutumu markel kwa kushindwa kutafutu suluhu.
Kura za maoni zinaonesha kuwa Schulz hawezi kuchukua nafasi ya Markel.

Matukio saba yaliyotikisa miezi sita


Matukio hutokea na kupita, baadhi yakiacha maswali pasipokuwa na majibu. Kati ya Februari na Agosti, kuna matukio takriban saba yaliyoibua mjadala mpana na hasa kwenye mitandao ya kijamii ambayo yamepita na kuacha mtikisiko.
Matukio hayo ni kutangazwa kwa majina ya vigogo waliohusishwa na dawa za kulevya; aliyekuwa waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Nnauye kunyooshewa bastola hadharani; uvamizi wa kituo cha Clouds Media; kutekwa kwa msanii wa muziki Roma Mkatoliki; mauaji ya Kibiti; kuzuiwa kwa makontena 275 ya makinikia na utata wa mlipuko katika kampuni ya mawakili ya Imma jijini Dar es Salaam.
Kila tukio kati ya hayo lilichukua wastani wa ama wiki au mwezi mmoja kujadiliwa katika mitandao na makundi mbalimbali ya kijamii.
Wakizungumzia kutikisa kwa matukio hayo, wachambuzi wa mambo ya kijamii na kisiasa wamelieleza gazeti hili kuwa, kulitokana na ugeni wa jamii katika mabadiliko ya mfumo wa Serikali iliyopo madarakani.
“Hatukuwa tumezoea kuona Serikali inayotoa maagizo, inafuatilia na kufanya tathmini lakini kwa bahati mbaya kuna Watanzania wamekuwa wakianzisha makundi mitandaoni kusifia wasichokifahamu na wengine kukosoa au kulalamika bila kuwa na mawazo mbadala,” alisema Profesa Haji Semboja kutoka Idara ya Uchumi, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM).
“Watu wanapoteza muda bure badala ya kufanya kazi au kujadili masuala ya kisera na kimkakati kuhusu ajenda iliyopo.”
Profesa Semboja alisema baadhi ya wananchi kwa bahati mbaya pia hupokea habari zilizoandaliwa na vyombo visivyotekeleza majukumu yake kwa weledi, hivyo kuiathiri jamii.
Alisema sababu nyingine ni wananchi kutumia haki yao ya msingi kuhoji jambo na kutafakari kupitia mfumo wa habari licha ya changamoto zinazojitokeza katika mijadala husika.
Mhadhiri mwandamizi kutoka Idara ya Sayansi ya Siasa na Utawala Bora, UDSM, Richard Mbunda alisema kila tukio hugusa hisia za mtu kwa namna tofauti, hivyo kuibua mijadala.
“Miaka ya nyuma watu walitumia vijiwe na maskani kukutana kujadili matukio yanayojitokeza katika jamii au serikalini, hata Ulaya ilikuwa hivyo lakini sasa teknolojia imerahisisha, mijadala imeongezeka kwa sababu ya uwazi na urahisi wa kupata habari,” alisema.
Februari 2, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda alianzisha mjadala wa dawa za kulevya baada ya kutaja majina ya askari zaidi ya 10 na wasanii saba waliodaiwa kujihusisha na biashara hiyo na baada ya siku kadhaa akawataja wengine wakiwamo wafanyabiashara, viongozi wa dini na wanasiasa.
Makonda katika awamu ya pili alikabidhi ripoti ya majina 97 ambayo hakuyataja kwa kamishna mkuu wa Mamlaka ya Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya, Rogers Sianga katika mkutano maalumu wa kutoa tathmini ya kampeni ya kutokomeza biashara haramu ya dawa za kulevya.
Uamuzi wa kutaja majina hadharani ulipingwa na wanaharakati na wasomi kabla ya Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa kupiga marufuku kutaja majina hadharani.
Nape kuonyeshwa bastola
Machi 23, mbunge wa Mtama, Nape Nnauye alitishwa kwa bastola nje ya hoteli ya Protea baada ya mkutano wake na wanahabari kuzuiwa na polisi wa Kinondoni.
Tukio hilo lilitokea siku moja tangu Rais John Magufuli alipotengua uteuzi wake wa uwaziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kutokana na mvutano wa sakata la uvamizi wa kituo cha Clouds.
Uvamizi wa Clouds
Machi 28, asasi za kiraia 33 barani Afrika zililaani kitendo cha kuvamiwa studio za Clouds na kulazimisha maudhui yasiyostahili yarushwe hewani. Tamko la asasi hizo lilitolewa siku chache baada ya Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB), Jukwaa la Wahariri (TEF) na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) kulaani kitendo hicho.
Kutekwa kwa Roma
Aprili 6, msanii wa muziki wa hip hop, Ibrahim Mussa maarufu Roma Mkatoliki akiwa na wenzake wawili walitekwa na watu wasiojulikana katika studio za Tongwe Records zilizopo Masaki jijini Dar es Salaam. Tukio hilo lilitanguliwa na kukamatwa kwa msanii mwingine, Emmanuel Elibariki maarufu Ney wa Mitego baada ya kutoa wimbo wa Wapo.
Mauaji ya Pwani
Wilaya za Mkoa wa Pwani za Rufiji, Kibiti na Mkuranga zilikumbwa na mauaji dhidi ya viongozi wa vijiji na vitongoji tangu Mei, 2016 na watu zaidi ya 32 wakiwamo polisi waliuawa.
Sakata la makinikia
Juni 12, kamati ya pili iliyoundwa na Rais John Magufuli kuchunguza masuala ya kiuchumi na kisheria kwenye makinikia ilitoa ripoti iliyoonyesha upungufu kwenye mikataba ya madini. Ripoti hiyo ilijadiliwa sana mitandaoni.
Sakata la Immma
Agosti 26, kwa kutumia milipuko iliyotengenezwa kienyeji, ofisi za kampuni ya uwakili ya Immma zilizopo mtaa wa Charambe, Upanga jijini Dar es Salaam zililipuliwa na tukio hilo likasababisha Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) kutangaza mgomo wa mawakili kwa siku mbili.   

Uwekezaji Morogoro wawaweka matatani raia watatu wa China


Siku moja baada ya agizo la Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa kutoa agizo kwa uongozi wa Mkoa wa Morogoro kufuatilia utendaji wa kampuni ya Zhong Fenq, umeviagiza vyombo vya ulinzi kuwakamata raia watatu wa China wanaodaiwa kuendesha shughuli za uwekezaji kinyume cha sheria.
Juzi, Waziri Mkuu Majaliwa alimuagiza mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Dk Stephen Kebwe na kamati ya ulinzi na usalama ya mkoa kwenda katika kijiji cha Maseyu kufuatilia utendaji wa kampuni hiyo kama inafuata sheria, kanuni na utaratibu.
Dk Kebwe jana alitoa agizo kwa vyombo vya ulinzi kuwakamata raia hao na kuamuru warudishwe kwao mara moja baada ya kugundulika kujihusisha na uchimbaji wa madini ya kutengeneza marumaru bila kufuata utaratibu, kanuni na sheria za nchi.
Waziri mkuu alitoa agizo hilo kutokana na malalamiko ya mbunge wa Morogoro Kusini Mashariki, Omary Mgumba kuwa wawekezaji hao kutoka China wanaendesha shughuli za uchimbaji bila ya kuwa na kibali.
Mgumba alisema tangu mwaka 2011 wawekezaji hao wameendesha shughuli zao bila kulipa kodi za Serikali na tozo za halmashauri, hivyo kuikosesha Serikali mapato.
Mbunge huyo ambaye machimbo hayo yako jimboni kwake, alisema licha ya uongozi wa mkoa kwenda eneo hilo na kuizuia kampuni kuendelea na uchimbaji hadi itakapopata vibali ilikaidi na kuendelea na shughuli zake.
Majaliwa alisema iwapo wahusika watabainika kuwa hawajafuata sheria, kanuni na utaratibu hatua zichukuliwe dhidi yao ikiwa ni pamoja na kuwaondoa katika eneo hilo chini ya ulinzi na kuwasiliana na ubalozi wa China nchini.
Akitoa agizo jana, Dk Kebwe alimtaka kamanda wa polisi Mkoa wa Morogoro na kamanda wa Uhamiaji wa mkoa kuhakikisha wanawakamata na kuwasafirisha raia hao wa China hadi jijini Dar es Salaam na utaratibu wa kuwaondoa nchini ufanyike mara moja. “Nawaagiza kuhakikisha mnaorodhesha vifaa na vitu vyote vilivyopo katika mgodi huo,” alisema Dk Kebwe.
Raia hao wa China kwa sasa wanashikiliwa na polisi wakisubiri kukamilishwa kwa utaratibu wa kuwarudisha kwao, huku mali za mgodi huo zikiwa chini ya uangalizi wa jeshi hilo.
Katika hatua nyingine, Dk Kebwe aliagiza polisi kuwakamata mhasibu wa halmashauri ya Wilaya ya Morogoro, ofisa biashara, mtendaji wa kata ya Maseyu na mtendaji wa kijiji hicho kwa kushindwa kutoa taarifa za raia hao wa kigeni kuendelea na uchimbaji huo.
Pia, Dk Kebwe alisema waliendelea kuwatoza kodi ya huduma hadi Juni mwaka huu licha ya kujua kuwa hawana kibali.
Akizungumzia kuchelewa kuondoka kwa Wachina hao, ofisa madini mkazi Mkoa wa Morogoro, Bertha Luzabiko alisema mamlaka ya Wizara ya Nishati na Madini ndiyo ilikuwa ikishughulikia suala lao.
Mkuu wa uhamiaji Mkoa wa Morogoro, Safina Muhindi alisema mpaka sasa hajaona pasipoti wala vibali vya kufanya kazi nchini vya rais hao, hivyo ufuatiliaji unaendelea.
Kamanda wa polisi Mkoa wa Morogoro, Ulrich Matei alisema walichofanya ni kutekeleza agizo la mkuu wa mkoa la kuwakamata
Mwaka 2016 mgodi huo ulizuiwa kufanya shughuli za uchimbaji wa madini na uzalishaji wa marumaru baada ya kubainika kuwa wawekezaji hao hawana vibali, huku bidhaa zilizokuwa zikizalishwa na kampuni hiyo zimekuwa zikiandikwa kuwa zinatengenezwa China. Imeelezwa uongozi wa mgodi ulisitisha shughuli kwa muda na baadaye ulirejea kuendelea na uzalishaji.   

Mtekaji asimulia alivyowachukua watoto Arusha


Matukio ya utekaji watoto mjini Arusha yameanza kupata mwelekeo wa ufumbuzi baada ya kijana wa miaka 18 kukiri kuwateka watoto wanne alipokamatwa katika mji wa Katoro wilayani Geita alikofanya tukio jingine la utekaji.
Akizungumza mbele ya waandishi wa habari akiwa chini ya ulinzi wa polisi jana, kijana huyo aliyejitambulisha kwa jina la Samson Petro alisema watoto wawili aliwarudisha kwa wazazi wao baada ya kupewa Sh300,000.
Alisema wengine wawili aliwatelekeza mtaani baada ya wazazi wao kutotoa kiasi cha fedha walichotakiwa kumpa.
Samson alisema alianza ‘shughuli’ hiyo ya utekaji watoto kutokana na mahitaji ya fedha na kwamba, aliacha shule akiwa kidato cha tatu katika Shule ya Sekondari Lutozo iliyopo Katoro.
“Naishi na wazazi wangu, lakini nao ni masikini, nilifanya hivi ili nipate fedha na nilikuwa nikimchukua mtoto naandika ujumbe kwenye karatasi, naandika na namba ya simu napeleka karibu na familia ili wanitafute,” alisema Samson.
Awali, kamanda wa polisi Mkoa wa Geita, Mponjoli Mwabulambo alisema walimkamata kijana huyo katika nyumba ya kulala wageni ya Shitungulu iliyopo mjini Katoro juzi saa mbili usiku.
Mwabulambo alisema polisi mkoani Geita kwa kushirikiana na wenzao wa Arusha walifanya uchunguzi na kubaini mtuhumiwa alikuwa Katoro.
Alisema walipata taarifa za kutekwa Justin Ombeni (2) Septemba Mosi nyumbani kwao katika eneo la Shilabela ambako mtuhumiwa alikwenda na kuwakuta watoto wanne wakicheza nyuma ya nyumba. Alisema aliwagawia pipi na kuondoka na Justin.
Kamanda huyo alisema polisi ilipata taarifa kuwa kijana huyo yupo chumba namba 103 katika nyumba hiyo ya wageni ambako waliweka ulinzi kuizunguka.
Alisema walipoingia katika chumba hicho walimkuta akiwa na mtoto huyo.
Mwabulambo alisema mtuhumiwa atafikishwa mahakamani baada ya uchunguzi kukamilika.
Ombeni Mshana ambaye ni baba wa Justin alisema mtekaji huyo alimpatia ujumbe mtoto wa jirani uliomtaka kutuma Sh4 milioni na walipokuwa wakiwasiliana na mtuhumiwa alishusha kiwango hadi Sh1 milioni. Alisema polisi walimtahadharisha kwamba asitume fedha hizo.
Kamanda Mwabulambo alisema tukio la kutekwa Justin ni la pili katika kipindi cha miezi minne baada ya mwingine kutekwa. Kesi kuhusu tukio hilo la kwanza inaendelea mahakamani baada ya mtoto kupatikana.
Katika hatua nyingine, kikosi kilichoundwa na wananchi mkoani Arusha kikiongozwa na mwenyekiti wa Mtaa wa Olkerian, Kata ya Olasiti, Daudi Safari na familia za watoto wawili waliotekwa kimewakamata watuhumiwa wawili na kuwafikisha polisi.
Watoto hao ambao bado hawajapatikana ni Moureen David (6) anayesoma darasa la kwanza shule ya msingi Lucky Vincent na Ikram Salim (3).
Wakizungumza jana nje ya kituo kikuu cha polisi Arusha baada ya kuwafikisha kituoni watuhumiwa hao, Safari na wazazi wa watoto hao, David Njau na Salim Kassim walisema kwa nyakati tofauti wameanzisha msako baada ya kuona siku zinakwenda bila watoto kupatikana.
Moureen alitekwa Agosti 21 saa 11 jioni akiwa anacheza nyumbani kwao eneo la Olasiti, wakati Ikram alitekwa Agosti 26 saa 12 jioni akiwa anacheza na watoto wenzake nyumbani kwao, Burka - Olasiti.
Safari alisema wamemkamata mtu mmoja (jina linahifadhiwa) ambaye simu yake ilitumiwa na watekaji kuomba fedha kwa mzazi wa Ikram Salim.
Alisema pia wamemkamata wakala wa fedha wa kampuni moja ya simu (jina tunaihifadhi) aliyetoa Sh300,000 kwa watekaji baada ya fedha kutumwa na mzazi wa Ikram. Imeelezwa kuwa wakala huyo amekamatwa kwa kuwa fedha hizo zilitolewa pasipo kuorodheshwa popote na mpokeaji hakuonyesha kitambulisho chochote.
Akizungumzia operesheni hiyo, Njau alisema hawatapumzika mpaka watoto wao wapatikane.
Alisema ufuatiliaji walioufanya kupitia minara ya kampuni za simu unaonyesha wahusika walikuwa eneo la Kwa Mrombo jijini Arusha walipopiga kuomba Sh4.5 milioni ili wamwachie Doreen na kiasi kingine kama hicho kwa ajili ya Ikram.
Watekaji hao kupitia ujumbe waliotuma nyumbani kwa Njau walidai kama wasipopewa fedha wangempoteza mtoto huyo japokuwa hawana nia hiyo.
Kassim Salim ambaye ni babu wa Ikram alisema, “tunaendelea kuomba msaada zaidi kwa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) na vyombo vya dola watusaidie tuwapate watoto wetu.”
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Charles Mkumbo alisema juzi kuwa watu watatu wanashikiliwa wakihusishwa na tukio hilo akiwapo dereva wa bodaboda mkazi wa Olasiti aliyetumwa kuwarejesha watoto wawili waliokuwa wametekwa.
Matukio ya utekaji yalianza kuibuka Agosti 21 baada ya kutekwa watoto wanne. Watoto wawili Ayoub Fred na Bakati Selemani wakazi wa eneo la FFU, kata ya Murieti jirani na kata ya Olasiti walirejeshwa.  

Hukumu ya Kenya yaendelea kutikisa nchini


Hukumu iliyoweka historia ya aina yake nchini Kenya kwa Mahakama ya Juu kubatilisha ushindi wa Rais Uhuru Kenyatta na kuamuru uchaguzi mwingine ufanywe ndani ya siku 60, imeendelea kutikisa hapa nchini.
Uamuzi huo wa Ijumaa iliyopita uliifanya Kenya kuwa Taifa la kwanza barani Afrika na la nne duniani kwa mahakama kubatilisha matokeo ya urais.
Nchi nyingine zilizowahi kufanya hivyo ni Ukraine, Austria na visiwa vya Maldives.
Baadhi ya wasomi na wanasiasa nchini wameendelea kutoa maoni yao, na jana hawakuwa tofauti na siku nyingine tangu kutolewa kwa hukumu hiyo saa 60 zilizopita.
Waliotoa maoni yao jana, walisema kuna haja ya kuhitimisha mchakato wa kupata Katiba mpya ili kuwezesha matokeo ya urais nchini kupingwa mahakamani, lakini wakaongeza na mbadala wake.
Iwapo hilo halitawezekana, wameshauri yafanyike mabadiliko ya sheria ya uchaguzi kwa kuweka kipengele cha kuruhusu matokeo ya urais kupingwa mahakamani.
Maoni hayo yametolewa siku moja baada ya juzi, spika wa zamani wa Bunge la Jamhuri ya Muungano, Pius Msekwa kusema wakati wa kupinga matokeo ya uchaguzi wa urais mahakamani umeshafika na kilichobaki ni kupitisha rasimu ya Katiba ambayo ina ibara inayotoa haki hiyo.
Kwa mujibu wa ibara ya 41(7) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1997, iwapo mgombea (urais) ametangazwa na Tume ya Uchaguzi kwamba amechaguliwa kuwa Rais kwa mujibu wa ibara hii, basi hakuna mahakama yoyote itakayokuwa na mamlaka ya kuchunguza kuchaguliwa kwake.
Hata hivyo, Msekwa, ambaye pia aliwahi kuwa makamu mwenyekiti wa CCM-Bara alitoa kauli hiyo wakati akizungumza kwa simu na gazeti hili kuhusu hatua ya mahakama nchini Kenya kubatilisha uchaguzi wa Rais wa nchi hiyo uliofanyika Agosti 8 baada ya mgombea wa Muungano wa Nasa, Raila Odinga kufungua kesi akidai kulikuwa na ukiukwaji wa sheria.
Akizungumza na gazeti hili jana, Profesa Benson Bana wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) aliunga mkono kauli ya Msekwa akisema kupinga matokeo mahakamani kutaondoa ‘figisufigisu’ ambazo zinaweza kusababisha machafuko wakati wa Uchaguzi Mkuu.
Alishauri Tanzania isipitwe na wakati, bali iwe na kipengele hicho kwenye Katiba kwa kuwa matokeo ya uchaguzi wa madiwani na wabunge yamekuwa yakipingwa mahakamani.
“Uchaguzi ndiyo kitovu cha siasa katika nchi, watu wanafanya siasa ili kugombea madaraka. Kuna umuhimu wa chombo cha mahakama kusimamia haki hii,” alisema. Akitoa mfano wa Kenya, alisema kama kusingekuwa na kipengele cha kupinga matokeo mahakamani, walioshindwa wangeweza kuanzisha vurugu, lakini walikuwa na imani na chombo hicho.
“Muungano wa Nasa hawakuridhika na matokeo ya urais, tegemeo lao likawa mahakamani na wameshinda. Uamuzi wa kurudia uchaguzi umetolewa,” alisema.
Profesa Bana alisema kuwapo kwa Katiba inayoruhusu kupinga matokeo mahakamani kutaepusha vurugu hasa katika nchi za Afrika.
Kwa mtazamo wake, kiongozi wa chama cha ACT -Wazalendo, Zitto Kabwe alisema mapendekezo ya kupinga matokeo ya urais mahakamani ni sehemu ndogo ya mabadiliko yanayohitajika katika mfumo wa demokrasia unaohitajika kwa Watanzania.
Zitto alisema hata mabadiliko ya kuhamia mfumo wa vyama vingi vya siasa yalihitaji kuboreshwa katika demokrasia iliyokuwa ikisimamiwa na CCM.
“Imefika wakati Watanzania tuamue aina gani ya demokrasia tunayoitaka, kwa sasa CCM ndiyo inayoamua aina gani ya demokrasia ituongoze, tuseme hapana. Tangu mwaka 1965 hadi mabadiliko ya mfumo wa vyama vingi 1992, CCM iliamua aina ya demokrasia,” alisema.
“Hata baada ya 1992 bado CCM inatuamulia aina ya demokrasia, kwa sasa inatuandalia sheria nyingine ya vyama, sasa Msekwa amesema imefika wakati lakini naomba Watanzania ndiyo tuseme hapana na tuamue aina ya demokrasia tunayoitaka.”
Naibu katibu mkuu wa CCM (Bara), Rodrick Mpogolo alisema mapendekezo ya Msekwa yanagusa masuala ya kisera, hivyo asingependa kutoa maoni.
“Ningependa nisizungumze lolote hata kutoa maoni yangu. Kama ni maoni ya chama ungemtafuta msemaji (Humphrey Polepole) au ungezungumza na Serikali ambayo inahusika kwa ukaribu zaidi na masuala ya kisera,” alisema Mpogolo.
Profesa wa Chuo Kikuu Katoliki cha Ruaha (Rucu), Gaudence Mpangala alisema kauli ya Msekwa inaonyesha namna suala hilo lilivyo muhimu katika ujenzi wa demokrasia.
Alisema mwanasiasa huyo mkongwe alishiriki kikamilifu katika uandaaji wa Katiba ya Tanzania ya mwaka 1977 lakini ameona kwa sasa upo umuhimu wa kupinga matokeo ya urais mahakamani.
Profesa Mpangala alisema hata kama mchakato wa kupata Katiba mpya utachelewa, basi ifanyiwe marekebisho sheria ya uchaguzi ili kubadilisha kipengele ambacho kitaruhusu kupinga matokeo ya urais mahakamani.
“Matokeo ya udiwani yanapingwa mahakamani, matokeo ya ubunge yanapingwa mahakamani, isiwe dhambi matokeo ya urais Tanzania yakapingwa mahakamani,” alisema Profesa Mpangala.
Kwa mtazamo wake, Profesa wa Chuo Kikuu cha Mzumbe mkoani Morogoro, George Shumbusho alisema mchakato wa Katiba mpya ni lazima uendelee ili matokeo ya urais yaweze kupingwa mahakamani kama ilivyo kwa Kenya.
“Katika Katiba Inayopendekezwa kuna kipengele kinachoelekeza matokeo ya urais yakishatangazwa na Tume ya Uchaguzi yanaweza kupingwa kwenye Mahakama ya Juu,” alisema Profesa Shumbusho.
Alisema uamuzi wa kurudia uchaguzi kwa amri ya mahakama nchini Kenya umetoa fundisho la demokrasia kwa nchi za Kiafrika ambazo matokeo ya uchaguzi wa Rais huambatana na vurugu.
Aliongeza kuwa ingawa Tanzania imeendelea kuwa nchi ya amani hata yanapotangazwa matokeo ya urais, wakati umefika wa kuwa na chombo cha kuwasikiliza wanaolalamikia matokeo.
Wakati ibara ya 140 ya Katiba ya Kenya inaruhusu mtu yeyote kupinga matokeo ya uchaguzi wa Rais mahakamani ndani ya siku saba tangu kutangazwa kwa mshindi, Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inakataza.
Ibara ya 74(12) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inasema hakuna mahakama yoyote nchini itakayokuwa na mamlaka ya kuchunguza jambo lolote lililotendwa na Tume ya Uchaguzi (NEC) katika kutekeleza madaraka yake kwa mujibu wa masharti ya Katiba.
Hilo ni jambo ambalo limekuwa likijadiliwa tangu kubatilishwa kwa uchaguzi wa Rais wa Kenya, lakini alipoulizwa kuhusu suala hilo juzi, Msekwa alisema muda umefika. “Tunaweza kufikia hatua hiyo na tumeshaifikia. Katiba mpya iliyopitishwa na Bunge mwaka 2014 inasema matokeo ya urais yanaweza kupingwa mahakamani. Katiba ya sasa hairuhusu, lakini Katiba Inayopendekezwa imeruhusu. Tunachosubiri ni referendum (kura ya maoni) tu,” alisema Msekwa.
Mchakato wa kubadili Katiba ulianzishwa na Rais wa Serikali ya Awamu ya Nne, Jakaya Kikwete mwishoni mwa mwaka 2011 lakini ukakwama mwaka 2014 ukiwa katika hatua ya kura ya maoni baada ya NEC kueleza kuwa haikuwa na muda wa kutosha .
Hata hivyo, mchakato huo uliingiwa na dosari baada ya baadhi ya wajumbe wa Bunge la Katiba, hasa kutoka vyama vya Chadema, NCCR-Mageuzi, CUF na NLD kuususia wakidai kuwa chombo hicho kiliacha Rasimu ya Katiba iliyoandaliwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba na kuingiza ajenda za chama tawala.
Kususia kwa vyama hivyo vinne ndiyo kulikuwa mwanzo wa kuundwa kwa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).
Licha ya hilo, wajumbe waliosalia bungeni waliendelea na mchakato na kupitisha Katiba Inayopendekezwa. Hata hivyo, Rais John Magufuli ameshasema kuwa Katiba mpya siyo kipaumbele chake kwa kuwa kwa sasa anataka “kuinyoosha nchi”.
Katika hukumu iliyoweka historia nchini Kenya, Mahakama ya Juu ilisema Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) ina hatia ya kukiuka sheria katika upokeaji na utangazaji wa matokeo ya kura.
Mgombea wa Nasa, Odinga alifungua kesi kupinga matokeo ya uchaguzi uliofanyika Agosti 8, akisema ulitawaliwa na udanganyifu ikiwamo kuchezewa kwa mifumo ya kujumlishia matokeo.
Katika uamuzi wake, mahakama hiyo ilisema uchaguzi huo ulikuwa na dosari nyingi, hivyo kukiuka misingi ya uchaguzi huru na wa haki kama ilivyoelekezwa katika Katiba ya nchi hiyo.
Katika uchaguzi wa mwaka 2013, Odinga alikwenda mahakamani kupinga matokeo lakini mahakama hiyo ilitupilia mbali hoja zake na kuridhia matokeo yaliyompa ushindi Rais Kenyatta.
Katika uchaguzi wa Agosti 8, Kenyatta alitangazwa mshindi kwa kupata kura 8,203,290 (sawa na asilimia 54.27), huku mpinzani wake Odinga akipata kura 6,762,224 (sawa na asilimia 44.74).