Tuesday, March 6

UPELELEZI KESI YA MAUAJI MKURUGENZI WA PALMS BADO HAUJAKAMILIKA



MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu imeelezwa, upelelezi wa kesi ya mauji ya Mkurugenzi na Mwanzilishi mwenza wa Shirika lisilo la kiserikali la Palms Foundation, Wayne Lotter inayowakabili watuhumiwa nane bado haujakamilika.

Wakili wa Serikali, Adolf Mkini ameeleza hayo leo mapema mbele Hakimu Mkazi Mkuu Wilbard Mashauri wakati kesi hiyo ilipokuja kwa kutajwa. Upelelezi bado haujakamilika

Aidha Mahakama ilielezwa na mshtakiwa Rahma Almas  kuwa mshtakiwa Mohammed Maganga anaumwa na yuko gerezani.

Kutokana na taarifa hizo, kesi imeahirishwa hadi Machi 21, mwaka huu kwa ajili ya kutajwa na kujua kama upelelezi utakuwa umekamilika ama la.

Washtakiwa katika kesi hiyo ni, raia wa Burundi, Nduimana Jonas maarufu Mchungaji (40) Mkazi wa Kamenge Burundi, Godfrey Salamba (42) Mkazi wa Kinondoni Msisiri A. Innocent Kimaro (23) Mkazi wa Temeke Mikoroshini, Chambie Ally(32) Mkazi wa Kia/Boma na Ofisa wa Benki ya NBC, Robert Mwaipyana (31) Mkazi wa Temeke Mikoroshini.

Wengine ni  Meneja wa Benki ya Baclays Khalid Mwinyi (33) Mkazi wa Mikocheni B, Mfanyabiashara Rahma Almas (37) Mkazi wa Mbagala B na Mohammed   Maganga (61) mchimba makaburi.

Washtakiwa hao wanakabiliwa na mashtaka mawili ambapo katika shtaka la kwanza wanadaiwa kuwa kati ya Julai Mosi na Agosti 16,mwaka 2017 wakiwa ndani ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania washtakiwa hao walikula njama ya kufanya mauaji ya Wayne Lotter.

Katika shtaka la pili, washtakiwa wanadaiwa Agosti 16, mwaka jana katika makutano ya barabara za Chole na Haile Selasie Kinondoni Dar es Salaam,  walimuua Lotter.

Kwa mujibu wa upande wa mashtaka, upelelezi katika kesi hiyo bado haujakamilika

MLINZI SUMA JKT AUAWA KWA KUKATWA MAPANGA


Na Ripota Wetu, Mbeya
JESHI la Polisi Mkoa wa Mbeya limesema watu wasiojulikana wamemvamia mlinzi wa SUMA JKT Chewe Wilson(34) na kumsababisha kifo baada ya kumkata mapanga sehemu za kichwani na mguu na kisha kupora silaha yake akiwa lindoni.


Akizungumza jana, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya Mohamed Mpinga amesema kuwa jeshi hilo limeendelea na jitihada zake za kukabiliana na matukio ya uhalifu ambapo kwa siku kadhaa sasa limekuwa likiendelea kufanya msako kwenye maeneo mbalimbali.

Kamanda Mpinga amesema kwa kushirikiana na wananchi na wadau wengine wa usalama, jeshi hilo limepata mafanikio makubwa katika kudhibiti wahalifu na matukio ya uhalifu mkoani Mbeya.

"Tumefanikiwa kupata mafanikio makubwa ikiwa ni pamoja na kukamata watuhumiwa mbalimbali wa uhalifu, silaha na vifaa mbalimbali vya kutengenezea silaha,"amesema.

MLINZI SUMA JKT AUAWA KIKATILI

Kamanda Mpinga amesema usiku wa kuamikia Februari 26 mwaka huu huko maeneo ya Kituo cha mafuta kiitwacho Manyanya kilichopo Uyole jijini Mbeya watu wasiofahamika majina walimvamia mlinzi wa SUMA JKT aitwaye Chewe Wilson mkazi wa Iduda.

"Mlinzi huyo akiwa lindoni katika kituo hicho alivamiwa na kisha kukatwa mapanga na silaha aliyokuwa nayo ikaporwa na watu hao na baada ya hapo wakatoroka nayo,"amesema Kamanda Mpinga.

Amefafanua mlinzi huyo alifariki dunia wakati akipatiwa matibabu katika Hospitali ya Rufaa Mbeya kutokana na majeraha aliyoyapata sehemu za kichwani.

Kamanda Mpinga amesema kutokana na tukio hilo Polisi walifanya msako mkali na kufanikiwa kuwakamata watuhumiwa watano ambao baada ya kuhojiwa wamekiri kuhusika na tukio hilo.

"Watuhumiwa watafikishwa Mahakamani kwa hatua zaidi za kisheria mara baada ya upelelezi kukamilika,"amesema.

WADAKWA WAKIWA NA  GOBORE

Kamanda Mpinga amesema wamefanya msako katika Kitongoji cha Kibaoni wilayani Chunya na kuwakamata watu wawili wakiwa na bunduki aina ya Shortgun iliyotengenezwa kienyeji na vifaa mbalimbali vinavyotumika kutengenezea bunduki.

Amewataja watuhumiwa hao ni Fadhili Mayega(60), na Mashaka Samuel(38), wote wakazi wa  Kambikatoto

Ameongeza baada ya watuhumiwa kupekuliwa walikutwa na bunduki hiyo na vifaa mbalimbali vinavyotumika kutengenezea bunduki aina ya shortgun za kienyeji ambavyo ni mMkono wa kuwekea risasi kwenye bunduki,  unga wa baruti wenye uzito wa gramu moja.

Pia mafuta ya kusafishia bunduki, risasi 25 zilizotengenezwa kienyeji, tupa 10, chuma kimoja cha kukatia risasi, tindo za kukatia mawe, vipande vya vyuma viwili, visu vitano, nyundo kubwa mbili, bisibisi moja, mguu wa Pedal ya baiskeli na triger mbili.

"Watuhumiwa watafikishwa mahakamani kwa hatua zaidi za kisheria mara tu baada ya upelelezi kukamilika,"amesema Kamanda Mpinga.

Ametoa mwito kwa vijana na jamii kwa ujumla kuacha tamaa ya kupata mali kwa njia zisizo halali kwa kujihusisha na vitendo vya uhalifu kwani ni kinyume cha sheria na badala yake wajishughulishe na kazi halali kwa ajili ya kujipatia kipato.

WATU 225 HUAMBUKIZWA VVU KWA SIKU


Takwimu zinaonesha kuwa Watanzania 225 huambukizwa Virusi vya Ukimwi kwa siku.
Hali hiyo inamaanisha kwamba kwa mwezi watu 6,750 huambukizwa VVU na kwa mwaka ni 81,000.
Takwimu hizo zimetolewa na Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Kudhibiti Ukimwi (TACAIDS), Dk. Leonard Maboko, leo Jumanne Machi 6, wakati akifungua mafunzo kwa waandishi wa habari kuhusu uandaaji wa programu bora za Virusi vya Ukimwi (VVU) na Ukimwi.
Amesema hali hiyo ni mbaya zaidi kwa vijana wenye umri kati ya miaka 15 hadi 24.
“Asilimia 40 ya maambukizo mapya hutokea kwa vijana wenye umri Kati ya miaka 15 hadi 24 na kati yao wengi ni wanawake.
“Hii inamaanisha kwamba katika hiyo asilimia 40 ya vijana waliopata maambukizi mapya, asilimia 80 ni wanawake,” amesema Dk. Maboko.

‘WANAWAKE WANAOUGUA MAGONJWA YA FIGO HUSHINDWA KUSHIKA MIMBA’



Wanawake wanaougua magonjwa ya figo hukabiliana na matatizo ya uzazi hasa kushindwa kushika mimba na hata kuharibika kwa mimba.
Kutokana na hali madaktari hulazimika kuwasaidia kukomaza mtoto iwapo mjamzito amekaribia kipindi cha kujifungua lakini pia kwa hali hiyo husababisha wengi huzaa mtoto njiti.
Daktari Bingwa wa Magonjwa wa Wanawake katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Dk. Vincent Tarimo amesema hayo jana alipozungumza na Mtanzania Digital katika mahojiano maalumu.
“Magonjwa ya figo kwa wanawake yanaweza kuwekwa katika makundi makubwa mawili, kuna yanayohusiana na ujauzito na yasiyohusiana na ujauzito ambayo yote huweza kuua,” amesema.
Amesema katika yale yanayohusiana na ujauzito tatizo la shinikizo la juu la damu ndilo ambalo huchochea zaidi figo kuathirika na kufa.

MASHEIKH WALIOPOTEA ZANZIBAR WAPATIKANA


MASHEIKH watano waliotekwa na watu wasiojulikana katika mazingira ya kutatanisha visiwani hapa, hatimaye wamepatikana.
Kiongozi wa Jumuiya ya Maimamu Zanzibar, Amir Haji Khamis Haji na wenzake wanne waliotoweka Februari 9, mwaka huu, waliachiwa juzi na kuungana na familia zao.
Akizungumza baada ya kuachiwa na watu hao, Amir Haji, alisema baada ya kukamatwa na watu hao, alifungwa kitambaa usoni na kupelekwa asikokujua na watu hao wasiojulikana.
“Binafsi siwajui hata waliofanya hivyo, lakini hadi leo hii (juzi) kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu milango ya asubuhi saa tano na nusu, naona nimeachiwa huru bila kuwa na madhara yoyote ikiwemo kuuawa.
“Na sasa niko nyumbani ni mzima, sikupata athari ya kupigwa na kitu chochote, kwahiyo nawaomba Waislamu wote waridhike na hilo, tuwe pamoja na waniombee dua mzee wao, hakuna kilichoharibika.
“Tuendelee na tuko pamoja na tuhifadhi mambo ya baadaye Inshallah. Sikuulizwa maswali yoyote, naona wao walikuwa wakifanya kazi yao, nasi kwa upande wa dini tunafanya pia.
“Kitu muhimu ni kuangalia masilahi ya baadaye na kuweka amani na hawa waliofanya haya nafikiri walikuwa wakifanya haya kwa ajili ya kuweka amani,” alisema Amir Haji.

Ripoti: Mapato ya mafuta Sudani Kusini yafadhili vita

Mashirika mawili ya uchunguzi yamedai kwamba kampuni ya mafuta inayomilikiwa na serikali nchini Sudan Kusini imekuwa ikitumika kufadhili vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini humo.

Südsudan - Kindersoldat (Getty Images/AFP/C. A. Lomodong)
Mashirika mawili ya uchunguzi yamedai kwamba kampuni ya mafuta inayomilikiwa na serikali nchini Sudan Kusini imekuwa ikitumika kufadhili vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini humo, ikiwa ni pamoja na wanamgambo wanaoegemea upande wa serikali ambao wanatuhumiwa kwa vitendo vya ukiukwaji wa haki za binaadamu. 
Katika ripoti iliyochapishwa hii leo, shirika la kimataifa la uchunguzi la Global Witness limesema ni mwaka wa tano sasa, mamilioni ya dola yatokanayo na kodi ya mafuta kuhamishwa kutoka katika shirika la mafuta la Nile Petrolium na kuingizwa katika kitengo cha usalama wa taifa cha Sudan Kusini, kwa lengo la kufadhili vita.
Shirika jingine la uchunguzi la Sentry, lililoanzishwa kwa ushirikiano na mcheza filamu wa Marekani George Clooney, limedai kwamba wanasiasa, wanajeshi, taasisi za serikali na makampuni yanayomilikiwa na wanasiasa na wanafamilia wa wanasiasa hao walilipwa zaidi ya dola milioni 80. 
Erdölförderung in Sudan (picture alliance/Tong jiang/Imaginechina)
Sudani Kusini ni taifa la tatu kuwa na hifadhi kubwa ya mafuta Afrika
Kampuni hiyo ya Nile Petrolium imekanusha  kufadhili shughuli yoyote ya kivita na kusema fedha zilizokuwa zikitolewa zimekuwa zikielekezwa kwenye miradi ya kijamii kama barabara, shule na hospitali. 
Mkurugenzi wa mahusiano wa kampuni hiyo ya mafuta Yiey Puoch Lur amenukuliwa akisema hawawezi kufadhili wanamgambo kwa kuwa hiyo si sehemu ya majukumu yao. Alisema, shirika la Global Witness lilighushi nyaraka hizo.
Ni wiki moja tu imepita tangu kamisheni ya Umoja wa Mataifa inaoyangazia haki za binadamu iliitaja Sudani Kusini kuwa miongoni mwa mataifa yanayokiuka haki za binadamu. Kwenye ripoti yake, mjumbe wa kamisheni hiyo nchini humo, Andrew Clapham alisema mzozo ulioanza mwaka 2013, umechangia kuongezeka kwa visa vya ukiukwaji, ambavyo ni pamoja na mauaji ya kikabila.
Marekani yaeleza kusikitishwa na ufichuzi huo.
Marekani imeuelezea ufichuzi huo kuwa ni wa kusikitisha sana.  
Afisa mahusiano wa ubalozi wa Marekani, Mark Weinberg aliliambia shirika la habari la Associate Press kwamba mapato yatokanayo na mafuta yanatakiwa kutumika kwa lengo la kuchochea uchumi wa nchi na si kutumika kinyume kwa kununua silaha ili kuiharibu zaidi nchi. Alisema, rasilimali ya Sudani Kusini zinatakiwa kutumika kwa ajili ya maslahi ya watu wake na viongozi wana wajibu wa kutanguliza kwanza maslahi ya watu wao.
Äthiopien Addis Abeba Salva Kiir Mayardit und Hailemariam Desalegn (Getty Images/AFP/Z. Abubeker)
Rais wa Sudani Kusini Salva Kiir anadhibiti kampuni hiyo ya mafuta inayotuhumiwa.

Kampuni ya mafuta ya Nile Petrolium inadhibitiwa moja kwa moja na rais wa Sudani Kusini Salva Kiir pamoja na mtandao wake wa karibu, hii ikiwa ni kulingana na ripoti ya Global Witness, iliyozingatia nyaraka za siri na ushahidi wa watu waliohusika.
Ripoti hiyo imesema, mkuu wa idara ya usalama wa ndani na mjumbe wa bodi ya wakurugenzi ya kampuni hiyo ya mafuta Akol Koor, amekuwa akiwasambazia wapiganaji silaha zilizonunuliwa kwa fedha kutoka kampuni hiyo. 
Sudani Kusini ni taifa la tatu kwa kuwa na hifadhi kubwa ya mafuta barani Afrika, kwa wastani wa mapipa bilioni 3.5. hata hivyo, baada ya miaka mitano ya vita vya wenyewe kwa wenyewe iliyosababisha vifo vya makumi kwa maelfu ya raia na wengine mamilioni kukimbia, taifa hilo limejikuta katika mzozo wa kiuchumi. Wabunge kwa muda mrefu wamewatuhumu maafisa wa serikali kwa kutumia fedha za mafuta kwa manufaa yao wenyewe, badala ya kuwasaidia raia.
Mbunge ambaye hakutaka kujitambulisha kwa hofu ya usalama wake alinukuliwa akilalama kuwa fedha hazitunzwi nchini humo, bali maafisa wa serikali wamekuwa wakizitumia kinyume cha utaratibu kwa kuzihifadhi kwenye mabenki ya nje.
Kulingana na shirika la Sentry, Marekani na Umoja wa Ulaya pamoja na jamii ya kimataifa wanatakiwa kuikabili Sudani Kusini kwa kutumia wizi kufadhili machafuko kwa kuwachunguza maafisa wa juu na kuwawekea vikwazo vya kimtandao. 

Hollywood: Filamu 'The Shape of Water' yanyakuwa tuzo nne za Oscars


Lupita Nyong'o, Winston Duke na Danai Gurira (kuanzia kushoto) wakiwasili katika maonyesho ya tuzo za Oscars huko Hollywood, jimbo la California., Machi 4, 2018.
Filamu ya kufikirika inayoitwa The Shape of Water (maumbile ya maji) imepata zawadi nne za Oscars wakati wa kutolewa tuzo za Academy siku ya Jumapili jioni, ikiwemo katika kundi la picha bora.
Filamu hiyo imempa nafasi mkurugenzi mwenye asili ya Mexico Guillermo del Toro kupata zawadi ya mkurugenzi wa filamu bora na pia kupata heshima kwa tathmini ya awali na uzalishaji wenye ubunifu.
Mwandishi wa VOA ameripoti kutoka mji wa Los Angeles ambapo onyesho hilo la Oscar lilifanyika maudhui ya usawa kwa wote yametawalia tuzo katika mwaka ambao wengi huko Hollywood wameungana kuwatetea wanawake.
Frances McDormand alitajwa kuwa muigizaji bora wa kike katika nafasi yake kama mama ambaye katika filamu hiyo alikuwa tayari kumumbua mkuu wa polisi katika juhudi zake za kutaka kumbainisha mtu aliyehusika na muuaji wa mtoto wake wa kike katika filamu maarufu Three Billboards Outside Ebbing, Missouri.
Swali ambalo wapenzi wengi wa filamu walikuwa wanajiuliza iwapo yoyote katika washindi wa tuzo ya Oscar mwaka 2018, jana Jumapili huko Hollywood, California, atatumia hotuba yake ya kupokea tuzo hiyo kuendeleza ajenda ya kisiasa, mtu pekee wa kumshukuru - au kumlaumu – Marlon Brando.
Wakati akipokea tuzo hiyo ya Oscar jana Jumapili, McDormand aliwaomba wanawake wenzie wasimame akiwemo mwigizaji mwanamke Meryl Streep.
“Waigizaji –Meryl, ukisimama, wengine wote watasimama, haya basi fanyeni hivyo – waongozaji wa filamu, wazalishaji wa filamu, wakurugenzi, waandishi wa filamu, Wakurugenzi wa picha, watengenezaji wa nyimbo, wandishi wa nyimbo, wabunifu.”
Amesema kuwa kila moja kati ya wanawake hao anajambo la kusimulia na mradi ambao unahitaji ufadhili.
Historia inaonyesha kuwa muigizaji wa Vito Corleone mwaka 1972 katika filamu The Godfather bado ni mashuhuri sana na mwenye kukonga nyoyo za wengi katika tasnia ya filamu.
Lakini kitendo chake cha kuingiza siasa mwaka 1973 wakati wa kupokea tuzo ya Academy Awards kilibadilisha mwenendo mzima wa Oscar.
Utamaduni uliokuwepo wakati huo ni washindi wa Oscar walipokea tuzo zao na kutoa hotuba wakiishukuru taasisi hiyo na sekta ya filamu.
Lakini Brando alileta mabadiliko. Yeye hata hakuhudhuria tafrija hiyo ya Oscar. Alimtuma mwigizaji Sacheen Littlefeather kumwakilisha. Alizungumza kupinga namna Hollywood ilivyokuwa inawafanyia watu ambao ni Wazawa wa Marekani (Native Americans).
Siasa zilijitokeza kuonyesha kuwepo athari za Brando katika sherehe za tasnia hiyo.
Maudhui yaliyojikariri wakati wa hafla hiyo jioni: madai ya unyanyasaji wa ngono na hoja dhidi ya kuongezeka idadi ya wanaume Hollywood. Pia tajiri katika ulimwengu wa filamu Harvey Weinstein, ambaye amekuwa akikabiliwa na tuhuma lukuki, amezuiwa kushiriki katika kinyang’anyiro cha maonyesho ya academy yaliyofanyika Oktoba.
Wengi waliohudhuria maonyesho hayo walivaa nguo nyeusi na beji nyeupe zenye ujumbe Time’s Up movement, ambayo ni umoja wa wanaharakati wanaotoa msaada wa kisheria kwa wanawake waliokuwa wamenyanyaswa kijinsia katika maeneo ya kazi.
Wengine walikuwa wamevaa riboni za rangi ya machungwa na beji zinazotaka hatua zichukuliwe dhidi ya matumizi mabaya ya silaha katika uvunjifu wa amani, kufuatia vifo vya watu 17 katika shule ya sekondari jimbo la Florida.
Maudhui nyingine katika maonyesho hayo jioni: Nguvu ya filamu katika kuleta mabadiliko katika jamii. Wakati akipokea tuzo ya Oscar kwa kuwa muongozaji wa filamu bora, del Toro amesema filamu zinaondoa vizuizi kati ya jamii.

Olympic yafungua mazungumzo kati ya Seoul, Pyongyang



Ujumbe maalum wa Korea Kusini wakati ukiwa uwanja wa ndege tayari kwa safari ya Pyongyang, Korea Kaskazini
Ujumbe maalum kutoka kwa Rais wa Korea Kaskazini Moon Jae-in umeripotiwa kukutana na kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong Un Jumatatu.
Ripoti za vyombo vya habari zimesema kuwa Kim aliandaa chakula cha usiku kwa heshima ya ugeni huo kutoka Korea Kusini.
Ujumbe huo wa watu 10 ambao umeongozwa na mshauri wa juu wa usalama wa taifa wa Moon, Chung Eui-Yong, uliwasili Pyongyang baada ya usafiri wa nadra wa ndege kufanyika kutoka Seoul.
Mkurugenzi huyo wa usalama wa taifa wa Korea Kusini amesema: ili kuendeleza wimbi la maelewano kupitia mazungumzo ya pamoja na mahusiano yaliopo hivi sasa kufuatia michezo ya kipindi cha baridi ya Olympic iliofanyika Pyeongchang, bila shaka tutafikisha ujumbe kutoka kwa Rais Moon kuwa ana nia ya dhati na utayari wa kuondosha silaha za nyuklia kutoka katika Rasi ya Korea na kufikia amani ya kweli na ya kudumu.
Chung amesema kuwa ataendeleza juhudi za kuwepo mazungumzo “ya kina” ili kutafuta njia ya kufanya matayarisho ya kuanza mazungumzo kati ya Pyongyang na Washington.
Harakati hizo zinaweza kukabiliwa na ugumu wa aina fulani kwa kuwepo mazoezi ya kijeshi yaliokwisha pangwa, lakini, kwa mujibu wa maoni yaliyochapishwa na Shirika la habari la Korea Kaskazini rasmi KCNA limetahadharisha kuwa Pyongyang “itakabiliana na Marekani” iwapo watafanya mazoezi ya kivita na Korea Kusini mwezi wa April.
Baada ya ziara hiyo ya siku mbili nchini Korea Kaskazini, ujumbe maalum kutoka Korea Kusini utasafiri kwenda Marekani ili kuwapa muhtasari maafisa wa serikali ya Marekani juu ya mazungumzo yaliojiri huko Pyongyang.
Hatua hiyo ya kupeleka ujumbe maalum Pyongyang, Moon alikuwa anarejesha ukarimu uliofanywa na Kim Jong Un katika uamuzi wake wa kupeleka ujumbe wa ngazi ya juu, akiwemo dada yake, Kim Yo Jong kuhudhuria michezo ya Olympics huko Pyeongchang.
Maafisa hao wa Korea Kaskazini walimwambia Moon kuwa wako tayari kuanza mazungumzo na Marekani, lakini Rais Donald Trump alijibu wito huo kwa kusema kuwa mazungumzo yatafanyika tu “katika hali inayoridhisha.”

Uganda: Kufukuzwa IGP, Waziri wa Ulinzi kwaibua hisia mchanganyiko

Rais Yoweri Museveni
Habari za kufukuzwa kazi Jenerali Kale Kayihura katika nafasi ya Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP) na Luteni Jenerali HenryTumukunde kama waziri wa ulinzi zimepokelewa kwa hisia tofauti na wasomaji wa mitandao nchini Uganda.
Wengi wa wachangiaji katika mitandao ya jamii wamemkosoa Rais Museveni katika hatua yake ya kuwafukuza viongozi hao na wengine wamewafurahia na kusema ilikuwa ikitegemewa kuwa hilo litatokea na pengine hatua hiyo imechelewa sana kuchukuliwa.
Wananchi wengine wa Uganda wanasema mabadiliko yalikuwa yanahitajika, hasa ukizingatia kiwango cha uhalifu kilivyokuwa kinaongezeka nchini Uganda, na ukweli wa kuwa majenerali hao walikuwa wameripotiwa kutokuwa na maelewano. Badala ya kukaa pamoja na kutafuta njia za kutatua tatizo lililokuwa linaongezeka la ukosefu wa amani wao walikuwa wako katika mivutano.
Kwa upande wa wale waliokuwa na sikitiko juu ya kufukuzwa majenerali hao wawili kupitia mitandao ya jamii wamesema kuwa pengine walikuwa wanafanya bidii kabisa kwa kadiri wawezavyo kuondoa uhalifu pamoja na kukabiliwa na changamoto mbalimbali kama vile ukosefu wa fedha na mahitaji mengine ambayo yako nje ya uwezo wao.
Museveni alimuondoa Jenerali Kayihura na kumweka badala yake Martin Okoth Ochola ambaye amekuwa naibu wake.
Kamanda wa jeshi la polisi mstaafu Brig Sabiiti Muzeei ni IGP mpya hivi sasa. Pia Museveni amemfukuza Luteni Jenerali Henry Tumukunde kama Waziri wa Ulinzi na kumweka Jenerali Elly Tumwine.

Akatwa mapanga kwa kumshika mbuzi wa tambiko


Moshi. Mtu mmoja aliyetajwa kwa jina la James Mallya amejeruhiwa baada ya kukatwa mapanga na kiongozi wa tambiko baada ya kumshika mbuzi wa tambiko katika msiba kwenye Kata ya Kibosho wilayani Moshi mkoani Kilimanjaro.
Akizungumza leo Machi 6, 2018 Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Hamis Issah amesema Mallya amekatwa mapanga Machi 5, 2018 baada ya kumshika mbuzi huyo aliyeandaliwa kwa ajili ya msiba na amelazwa katika Hospitali ya Rufaa ya KCMC, mjini Moshi.
Amesema alikatwa mapanga baada ya kiongozi wa tambiko kuchukizwa na jinsi alivyokuwa akimshika mbuzi wa tambiko, kwa kuwa kitendo hicho kiliharibu utaratibu wa mila.
“Mallya ni mkazi wa Dar es Salaam alifika kwa ajili ya kushiriki msiba, akiwa msibani alikwenda kumshika mbuzi aliyekuwa amefungwa jirani ambaye alikuwa ni kwa ajili ya tambiko kwenye msiba huo,” amesema Issah.
“Alipomshika mbuzi ndipo kiongozi wa tambiko hilo jina tumelihifadhi alipomsogelea na kuanza kumkata kwa panga kichwani.”
Kamanda huyo amesema kiongozi huyo wa tambiko alipoulizwa sababu za kufanya hivyo, amesema amechukua uamuzi huo kwa sababu Mallya aliharibu utaratibu wa tambiko, kwamba kwa mujibu wa mila zao hairuhusiwi kumshika mbuzi wa tambiko.
Katika tukio jingine, mtu mmoja aliyefahamika kwa jina moja la Rama amekutwa amefariki dunia na mwili wake kutupwa katika shimo la maji machafu jirani na nyumba aliyokuwa akiishi kwenye kijiji cha Oria Kata ya Kahe Magharibi wilayani Moshi.

Afya ya Mbowe yazidi kuimarika


Moshi. Afya ya mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe aliyeruhusiwa jana kutoka Hospitali ya Rufaa ya KCMC baada ya kulazwa kwa saa 24 inazidi kuimarika.
Akizungumza leo Jumanne Machi 6, 2018 katibu wa Chadema Mkoa wa Kilimanjaro, Basil Lema amesema Mbowe ambaye pia ni mbunge wa Hai kwa sasa anaendelea vizuri na yuko kwenye mapumziko.
"Tunamshukuru Mungu mwenyekiti anaendelea vizuri sana kwa kweli. Kwa sasa yupo katika mapumziko,” amesema Lema.
Mbowe, ambaye jana Machi 5, 2018 alipaswa kuripoti Kituo Kikuu cha Polisi jijini Dar es Salaam, aliugua ghafla juzi usiku akiwa anapata chakula na viongozi wengine katika hoteli ya Keys mjini Moshi kabla ya kuwahishwa KCMC kwa matibabu.

Madiwani Chadema kujiunga CCM kwaibua utata

Serengeti. Wakati madiwani wawili wa Chadema kutoka halmashauri ya wilaya ya Serengeti wakitangaza kujivua uanachama na nyadhifa zao kuunga mkono kazi inayofanywa na Serikali, uongozi wa halmashauri hiyo inayoongozwa na chama hicho umesema haujapokea taarifa rasmi kuhusu uamuzi huo.
Madiwani waliotangaza kuondoka Chadema na kujivua nyadhifa zao kupitia taarifa zinazosambaa kupitia mitandao ya kijamii ni Michael Kunani wa kata ya Ikoma na John Mongita ambaye ni diwani wa kata ya Manchira.
Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri Dk Tito Kagize alisema hajapata taarifa  rasmi zaidi ya kusoma kwenye mitandao
Wakizungumza kwa nyakati tofauti kwa ya simu leo Machi 6, Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Serengeti Juma Porini na Kaimu Mkurugenzi wa halmashauri hiyo, Dk Tito Kagize wamesema nao wamesikia, kusoma na kuona taarifa za madiwani kutangaza kujiuzulu kupitia mitandao ya kijamii.
“Tunajua wako mkoani Arusha kwa muda mrefu wakijadiliana na viongozi wa CCM wa Kitaifa wanaofanya ziara mkoani humo kuhusu wao kujivua uanachama na kujiuzulu udiwani; tunasubiri taarifa yao rasmi,” amesema Porini.
Hata hivyo, mwenyekiti huyo wa halmashauri ya wilaya inayoongozwa na Chadema amesema ni hiari na haki ya kikatiba na kisheria kwa kila mtu kujiunga na chama chochote cha siasa na kuongeza kuwa wakipokea taarifa rasmi chama kitaheshimu uamuzi wa madiwani hao.
“Taarifa za wao kuondoka Chadema na kuhamia CCM zilisikika hata wakati wa ziara ya Waziri Mkuu Serengeti mwezi uliopita; nadhani walikuwa hawajafikia makubaliano ndio maana hawakufanya hivyo wakati ule,” amesema Porini.
Amesema kwa muda sasa, madiwani hao hawahudhurii vikao kikiwemo kile cha kujadili na kupitisha bajeti cha wiki iliyopita.
Halmashauri ya wilaya ya Serengeti yenye jumla ya madiwani 43, inaongozwa na Chadema yenye madiwani 25 na wabunge wawili inayofanya idadi yao kufikia 27 huku CCM ikiwa na madiwani 16.

Kesi za kikatiba kuanza kusikilizwa Ijumaa



Dk Makongoro Mahanga 
Dk Makongoro Mahanga  
Dar es Salaam. Mashauri mawili ya kikatiba yaliyofunguliwa na umoja wa wanaharakati wa kudai  demokrasia Tanzania yataanza kusikilizwa Ijumaa Machi 9, 2018 Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam.
Mashauri hayo ya kikatiba  yalifunguliwa katika mahakama hiyo na umoja huo kwa kushirikiana na wanasheria kupinga namna demokrasia ya vyama vingi, uhuru wa kujieleza na kukusanyika unavyokiukwa hapa nchini.
Pia mashauri hayo yalilenga kuhoji namna utendaji wa vyombo vilivyoundwa kwa mamlaka ya kikatiba vinavyoikiuka katiba hiyo.
Mratibu wa Umoja huo Dk Makongoro Mahanga amesema kesi hizo zitatajwa Ijumaa mahakamani hapo, kuanzia saa tatu asubuhi.
Amesema shauri namba 6/218 lililofunguliwa na Bob Chacha Wangwe, akisimamiwa na Wakili Fatuma Karume kuhusu Sheria ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi litatajwa mbele ya jopo la majaji watatu wa Mahakama Kuu.
Dk Mahanga amewataja majaji hao kuwa ni Jaji Wambali JK, Jaji Mwandambo J na Jaji Teemba J.
Amesema shauri namba 4/2018 lililofunguliwa na Francis Garatwa, Baraka Mwango na Allan Bujo ambao wanatetewa na Wakili Jebra Kambole kuhusu Sheria ya Jeshi la Polisi na Sheria ya vyama vya siasa litatajwa mbele ya jopo la majaji watatu ambao ni Jaji Wambali JK, Jaji Sameji R na Jaji Teemba J.
“Wananchi wapenda demokrasia ya kweli ni vema na busara kuhudhuria na kufuatilia mashauri haya yatakayokuwa yakiendelea kunguruma Mahakama Kuu, ”amesema Dk Mahanga.

VIDEO-DC apiga marufuku kondomu shuleni

Serikali imetoa onyo kwa taasisi zisizo za Serikali kuacha kupandikiza vitanzi na kuwagawia kondomu wanafunzi shuleni kwani wanahamasisha ngono kwa umri mdogo.
Kauli hiyo imetolewa leo Machi 6 na Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana, Mery Tesha wakati wa maonyesho ya siku mbili ya wanawake katika viwanja vya Ghandh All.
Tesha amesema Serikali imebaini baadhi ya mashirika na taasisi zisizo za Serikali zinazunguka na kutoa huduma hizo shuleni.
“Wanafunzi hawa tuwalee katika maadili mema yanayostahili badala ya kuwapatia kondomu na vitu vingine vinavyohamasisha kufanya ngono, jambo hili halikubaliki hata kidogo,” amesema Tesha.
Mwananfunzi anayetarajia kujiunga kidato cha tano Sada Jabiri ameiomba Serikali kuifuta sheria ya mwaka 1971 ambayo inamruhusu mtoto kuolewa akiwa na miaka kuanzia 15.
“Ili kumjengea mtoto haki ya kujitambua na kutoa uamuzi sahihi ni vyema sheria ingesema hata ianzie miaka 21 ambapo mtoto anakuwa ana ufahamu mkubwa,” amesema Sada.
Mwenyekiti wa baraza la watoto Mkoa wa Mwanza, Neema Theonest alisema katika hali hii ya kuelekea uchumi wa viwanda ifikapo 2025 ni vyema kuimarisha usawa wa kijinsia na uwezeshaji wanawake vijijini.
Neema amewataka wanawake waache kubweteka badala yake wajitume kufanya kazi ili kupandisha uchumi kuanzia ngazi ya familia na kutokomeza umasikini.
Akisoma risala kwa niaba ya wanawake wa Nyamagana, Grace Saiti aliiomba Serikali iendelee kutoa fursa nyingi za ajira kwa wanawake na kuwapatia nyadhifa mbalimbali kwani wanawake wana uwezo wa kuongoza na kusimamia shughuli mbalimbali za maendeleo kiuchumi, kisiasa na kijamii.
Pia amesema  elimu ya masuala ya uzalishaji na uanzishaji wa viwanda ifanyike zaidi kwenye maeneo yote ili mwanamke hata wa kijijini afikiwe na aweze kujiendeleza.

Wafanyabiashara waeleza hasara kuteketea soko Mbagala


Dar es Salaam. Soko la Kampochea lililopo Mbagala Rangi Tatu jijini Dar es Salaam limeteketea kwa moto alfajiri ya leo Jumanne Machi 6, 2018 na kusababisha hasara kwa wafanyabiashara wa eneo hilo.
Imeelezwa moto huo ulianza kuteketeza mabanda ya soko hilo saa 12 alfajiri huku uongozi ukitaja kuwa chanzo ni hitilafu ya umeme.
Mwenyekiti wa soko hilo, Mohamedy Njiwa amesema limekuwa likikumbwa na hitilafu za mara kwa mara licha ya kuripoti kwa mamlaka husika.
"Wiki mbili zilizopita hapa kulikuwa na hitilafu ya umeme, ulikuwa unakuja na kukata. Tanesco walikuja kufanya ukaguzi wakaeleza kuwa kuna hitilafu kwenye transfoma,"amesema.
Amesema mabanda yote 673 yaliyokuwapo eneo hilo yameungua kwa moto na kwamba, hasara ni kubwa.
Mmoja wa wafanyabiashara sokoni hapo, Chacha Mwang'wene amesema hajafanikiwa kuokoa chochote zaidi ya taarifa zake za biashara.
Msemaji wa Zimamoto Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Peter Mwambene amesema jeshi hilo lilijitahidi kudhibiti moto huo, lakini tatizo kubwa ni aina ya bidhaa zilizokuwamo.
"Soko hili lina mali ambazo zinachangia kusambaza moto kwa kasi sana kama mitumba ambayo ni rahisi kuteketea kwa moto,"amesema.
Pia, amesisitiza kuwapo kwa vifaa vya awali vya kuzimia moto ili kunusuru mali kwenye masoko mengine jijini hapa.
Hatahivyo, wafanyabiashara hao wameeleza nia yao ya kuendelea kulitumia soko hilo licha ya agizo la mkuu wa Wilaya ya Temeke kuwataka kuhamia masoko mengine.

TWB kunadi mali za wadaiwa sugu


Dar es Salaam. Benki ya Wanawake Tanzania (TWB) imetangaza kuzipiga mnada mali za wadaiwa sugu 7,065 watakaoshindwa kulipa madeni yao ndani ya siku saba kuanzia leo.
Mwenyekiti wa bodi wa benki hiyo, Beng’i Issa amesema leo Machi 6 kwamba  uamuzi huo ni sehemu ya kukabiliana na ongezeko la mikopo chechefu au isiyolipika iliayo.
“Mpaka sasa mikopo isiyolipika imefia Sh7.9 bilioni hivyo kuongeza ugumu kidogo katika kuhakikisha tunapata mtaji wa kutosha,” amesema Issa.
Ndani ya muda walioutoa, alisema wateja wanaodaiwa wanapaswa kulipa madeni yao ambayo ni ya muda mrefu.
“Wengi wameshapitiliza siku 90 za kutorejesha madeni yao kinyume na utaratibu na makubaliano na benki,” amesema
Kwa watakaoshindwa kulipa fedha hizo ndani ya muda uliotolewa wa benki kuchukua hatua za kisheria kabla ya kunadisha dhamana zao, amesema wenye dhamira ya kulipa waende kwenye tawi lolote la benki hiyo wakiwa na mpango mahususi wa jinsi watakavyofanikisha malipo yao.
Januari 4, wakati Benki Kuu Tanzania (BoT) inatangaza kufuta leseni za baadhi ya benki nchini, TWB ilipewa agizo la kuongeza mtaji ndani ya miezi sita ili kukidhi mahitaji ya ukwasi unaohitajika.
Kulingana na masharti ya taasisi za fedha na benki za biashara nchini, kila moja inatakiwa kuwa na mtaji na ukwasi wa kutosha kukidhi mahitaji ya kila siku.
Wakati TWB ikipewa onyo hilo, benki za Covenant, Efatha, Benki ya Wananchi Njombe, Kagera Farmer’s Cooperative Bank na Benki ya Wananchi Meru zilifutiwa leseni.
Mkurugenzi mtendaji wa Benki ya Wanawake Tanzania, Japhet Justine amesema  sheria inawaruhusu kuuza mali au dhamana za wateja walizoweka endapo watashindwa kurejesha mkopo kwa wakati waliokubaliana.
“Mbali na kupiga mnada mali zao, taarifa zao tutazipeleka Benki Kuu ya Tanzania wasiweze kupata mkopo katika benki nyingine yoyote nchini,” amesema Justine.
Amesema tangu kutolewa kwa taarifa ya awali kuwa benki ipo katika hali mbaya, wamekusanya zaidi ya Sh2 bilioni kutoka kwa wadaiwa walionao, hatua ambayo alisema ni nzuri.
Kwa sasa, alisema wapo katika maongezi na wadau mbalimbali kuwawezesha kupata mtaji waliowekewa na Benki Kuu na kwamba mwelekeo unaonekana kuwa mzuri.
“Baada ya benki yetu kupewa maagizo ya kuongeza mtaji na Benki Kuu tunapokea wateja na wageni wengi wanaohitaji ufafanuzi kuhusu fedha zao lakini wote wanaelewa,” ameongeza.