Friday, September 6

‘Marekebisho yanazungumzika bungeni’




Dodoma. Waziri Mkuu, Mizengo Pinda amesema Serikali haitauondoa Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba kwa sababu mambo ambayo Kambi ya Upinzani Bungeni inayadai, yanazungumzika na yanaweza kubadilishwa kwa mamlaka ya wabunge.
Pinda alikuwa akijibu swali la nyongeza la Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe katika kipindi cha Maswali ya Kwa Waziri Mkuu Bungeni, Dodoma jana.
Mbowe ambaye pia ni Mbunge wa Hai (Chadema), alisema yapo matukio ya kibabe, kejeli, matusi na ya dharau ambayo yamekuwa yakifanya kuchelewa kwa utaratibu mzima wa utungaji wa sheria... “Pamoja na rai mliyoiondoa, sisi tunasema yapo maeneo mengi yasiyo na tija ambayo yanafanya msingi wa marekebisho ya sheria mlioleta jana (juzi), kuwa hayana tija kwa mchakato huu.”
Akijibu swali hilo, Pinda alisema: “Hivi kweli Mbowe una ngoja hadi muswada unafika ngazi ya Bunge, ndipo unakuja na hoja hiyo wakati tulikuwa na fursa kubwa?”
Alisema kwa mambo ambayo alielezwa kuwa ndiyo yaliyosababisha wabunge wa kambi ya upinzani kutoka nje ya Ukumbi wa Bunge juzi, hakuna atakayeona umuhimu wa kuondoa muswada huo.
“Kwa sababu ni vitu ambavyo ndani ya Bunge hili vinazungumzika na vinaweza kubadilishwa kulingana na mamlaka mliyopewa,” alisema.
Katika swali la msingi, Mbowe alisema mchakato wa Katiba Mpya unahitaji ustahimilivu, ushirikiano, uwazi, dhamira njema na kwamba wabunge wanapaswa kutambua kuwa wapo wadau nje ya Bunge wanahitaji ushirikiano.
Pinda alisema: “Mategemeo ni wabunge tulio ndani tutaujadili muswada huu kikamilifu na maeneo yote ambayo yanadhaniwa yanaweza yasiwe na tija, neema kwa nchi yetu, ni jukumu letu kujadili kwa uwazi, uaminifu na kiukweli.
Mbunge wa Kuteuliwa, James Mbatia (NCCR –Mageuzi), alihoji kama Serikali haioni ni busara mazungumzo ya kisiasa kufanyika kwanza kisha yakafuatiwa na sheria ambayo itasaidia kuunda dhana ya dola. Alisema kumekuwa na ukiukwaji mkubwa wa Katiba kwa kuruhusu mabadiliko ya Katiba ya Zanzibar.
Kuhusu hilo, Pinda alisema kulikuwa na mashauriano makubwa kati ya vyama, taasisi na pande mbili za Muungano kabla muswada huo kufikishwa bungeni na kwamba Katiba Mpya itameza yote yaliyomo katika katiba hiyo ya zamani na kuja na mawazo mapya ambayo itaongoza Taifa.

Mheshimiwa SUGU anasakwa na polisi kwa kosa la kuwakashifu walinzi wa Bunge

Taarifa kutoka Dodoma zinadai kuwa kuna Askari mmoja ambaye ni miongoni mwa walinzi wa Bunge ameenda kufungua faili Polisi Dodoma na kusema kuwa ametishiwa kupigwa na Mbunge Sugu...
Baada ya kufungua Jalada hilo polisi wamechukua Difenda 6 na wameingia mitaani kumtafuta ili awekwe ndani mpaka kesho ndio afikishwe mahakamani asubuhi.

"Mbowe ni Mjinga na Mpuuzi"...Hii ni kauli ya Kigwangalla bungeni

Mbunge wa Nzega Dr. Kigwangalla, ametumia muda wake karibu wote wa kuchangia Muswada wa Katiba kwa kumshambulia Mwenyekiti wa CHADEMA, Mhe. Mbowe kuwa ni Mjinga, Mpuuzi, ametia aibu aibu 
Kigwangalla  amempongeza  Naibu  Spika  kwa  kumtimua  Mbowe  bungeni  na  kusema  kuwa  kitendo  hicho  kimemshikisha  adabu...
Aidha, mbunge  huyo  wa  Nzega amedai kuwa Mbowe sio Mchaga bali ni mhuni fulani  aliyejivika  sura  ya  Uchaga  kwa  masilahi  yake  binafsi !.
Kigwangalla  alihitimisha  mchango wake  kwa  kudai  kuwa wapinzani wana akili za shetani  zisizovumilika!

Wananchi walilaani Bunge la Tanzania kutokana na vurugu zinazoendelea

Baada ya kuibuka mvutano mkali bungeni jana, kati ya Naibu Spika, Job Ndugai na wabunge wa Kambi ya Upinzani, wasomi, wanaharakati, Chama cha Madaktari Tanzania (Mat), Chama cha Walimu Tanzania (CWT) na Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (Tucta), vimesema kinachoendelea sasa ndani ya Bunge ni masilahi ya vyama vya siasa siyo taifa.
 

Walitoa kauli hiyo muda mfupi baada ya Naibu Spika, Job Ndugai kuwataka askari kumtoa nje ya Ukumbi wa Bunge, Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe.
 

Mbowe aligoma kukaa chini na kuungwa mkono na wabunge wa upinzani, akishinikiza kuahirishwa kujadiliwa kwa Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, hadi hapo Zanzibar itakaposhirikishwa, muda mfupi baada ya wabunge kupiga kura na 156 kutaka ujadiliwe na 56 wakitaka uondolewe.
 

Wabunge hao wa upinzani kutoka vyama vya Chadema, CUF na NCCR- Mageuzi, juzi walitoka nje ya Ukumbi wa Bunge wakishinikiza kuahirishwa kujadiliwa kwa muswada huo. 
Wakizungumza kwa nyakati tofauti, Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Bashiru Ally alisema mvutano huo umejaa masilahi ya wanasiasa kwa kila upande kujaribu kuvutia kwake.
 

“Mvutano ule hauzungumzi kabisa mwafaka wa Bunge la Katiba, binafsi nadhani Bunge la Katiba linatakiwa kuwa na wabunge wapya kabisa na wasiotoka katika chama chochote cha siasa,” alisema
 

Katibu Mkuu wa Tucta, Nicolaus Mgaya alisema: “Marekebisho hayo yanafanyika kwa ajili ya mustakabali wa Muungano wetu, kama Zanzibar hawakushirikishwa, uwekwe utaratibu wa jambo hilo kufanyika ili kipatikane kitu bora, siyo bora Katiba.”
 

Alisema nchi zilizoendelea zimepata mafanikio kwa kuwa zina Katiba nzuri ambazo zinaweza kudumu kwa miaka 100 kabla ya kufanyiwa marekebisho..

Ripoti maalumu ya gazeti la MWANANCHI kuhusu vurugu zilizotokea jana bungeni


Jana, Bingwa wa Dunia wa uzani wa kati (super middle), unaotambuliwa na Shirikisho la Ngumi Duniani (WBF), Francis Cheka alitembelea Bunge baada ya kutwaa taji hilo karibuni na jana hiyohiyo, Bunge hilo lilishuhudia ngumi kavukavu katika vurugu kubwa pengine kuliko zote zilizowahi kutokea katika ukumbi wake. 

Katika masumbwi hayo yasiyo rasmi, Mbunge wa Mbeya Mjini (Chadema), Joseph Mbilinyi ‘Sugu’ anadaiwa kumpiga kichwa Askari wa Bunge na kumchania sare na kung’oa kipaza sauti.
 

Mbilinyi jana alisema alikuwa anatafutwa na polisi huku akisema hilo limemshangaza akidai kwamba yeye ndiye aliyeshambuliwa na askari huyo.
 

Vurugu hizo zilitokea baada ya Naibu Spika, Job Ndugai kuamuru kutolewa nje kwa Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe.
 

Katika vurugu hizo Mbilinyi alibebwa juujuu na polisi hadi nje ya ukumbi huku akiwa hana viatu.
 

Pamoja na tafrani hiyo, Ndugai alisema wakati akihitimisha kikao cha Bunge kipindi cha asubuhi kuwa amewasamehe wabunge wote waliohusika na kosa hilo la utovu wa nidhamu na kuwaruhusu kurejea kipindi cha jioni kuendelea na Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba. 

Hata hivyo, wabunge wote CUF, NCCR-Mageuzi na Chadema ambao baada ya tukio hilo walitoka nje ya ukumbi, hawakurejea na baadaye walitoa msimamo wa pamoja wakisema hawatashiriki katika mjadala huo.
 

Msimamo huo ulitolewa na Mbowe ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chadema, Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia na Mbunge wa CUF, Habib Mnyaa.
 

Mbowe alisema wameamua kususia majadiliano hayo kuonyesha msimamo wao wa kupinga kupitisha mambo yasiyo na masilahi kwa nchi.
  
“Hatuko tayari kushiriki katika uchakachuaji wa Katiba... Matumizi ya nguvu ya polisi kamwe hayatatupatia Katiba nzuri,” alisema. Alisema kambi rasmi ya upinzani inalaani vikali kitendo cha Ndugai kuruhusu Bunge kunajisiwa kwa kuruhusu polisi kuingia ndani kinyume na kanuni.
 

Mnyaa alisema kitendo cha wadau wa Zanzibar kutoshirikishwa katika kutoa maoni yao katika muswada huo wa marekebisho ni dharau kubwa.
 

Mbatia alisema Tanzania haiwezi kuingia Uchaguzi Mkuu wa 2015 kwa kutumia Katiba ya sasa kwa sababu tayari kuna mgongano wa kikatiba kati ya Zanzibar na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
 

Mnadhimu wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Tundu Lissu alimtaka Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Kuu, (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi kutoa ushahidi kama Rais aliteua wajumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba kulingana na mapendekezo ya taasisi zao.

Kuanza kwa tafrani
Sakata hilo lilianza saa 6:45 mchana muda mfupi baada ya kukamilika kwa kura kuamua kama Bunge liahirishwe au la kutokana na hoja iliyotolewa na Mbunge wa Mkoani (CUF), Ali Hamisi Seif (CUF). Waliotaka liahirishwe walipata kura 59 na waliokataa 159.

Baada ya Ndugai kutangaza matokeo hayo na kutaka shughuli za Bunge ziendelee, Mbowe aliposimama na kusema ana hoja Naibu Spika alimwamuru akae chini.

Baada ya Mbowe kusisitiza ana hoja na kumwomba Spika amsikilize ndipo Ndugai alipomwamuru atoke nje na alipokaidi alisema:” Naomba askari wote waliopo katika mazingira haya (ya Bunge) waingie ndani ya ukumbi wa Bunge”.

Baada ya kitambo kifupi, Mbowe akiwa bado amesimama alitoa maagizo atolewe nje: “Kiongozi wa upinzani atolewe nje.”

Polisi waliingia ndani ya Ukumbi wa Bunge lakini Wabunge wa Kambi ya Upinzani kwa umoja wao, walimzinga Mbowe asifikiwe na askari hao.

Baada ya kuona polisi wanaelekea kushindwa, Ndugai alitoa maagizo mengine: “Askari hamjaletwa humu ndani kufanya majadiliano mnatakiwa kuhakikisha kiongozi wa upinzani anatolewa nje”.

Alisema yeye ndiye anayeendesha kikao hicho hivyo lazima Mbowe atolewe nje.

Hapo ndipo wabunge hao wa upinzani walipoanza kuimba: “Hatutaki kuburuzwa hatutaki kuburuzwa… hatutaki kuonewa,” huku wakiendelea kumzinga Mbowe.

“Askari wote mliopo humu ndani naomba mnisikilize… Sasa naagiza kwa mara ya mwisho... nasema kiongozi wa upinzani atolewe nje.”

Ngumi zarushwa
Baada ya kauli hiyo ya Ndugai, ndipo polisi walipotumia nguvu hasa kwa Mbilinyi na Mbunge wa Maswa Mashariki (Chadema), Silvester Kasulumbai.

Katika patashika hiyo, inadaiwa kwamba Mbunge wa Kasulu Mjini (NCCR-Mageuzi), Moses Machali alipigwa ngumi ambayo ilimfanya apepesuke hadi sakafuni.

Kilichomponza Mbilinyi ni hatua yake ya kusogelea Siwa. Polisi waliokuwa karibu, walimbeba juujuu hadi nje ya ukumbi.

Wakati akitolewa nje ya ukumbi, alijaribu kujizuia kwa kushika kipaza sauti kinachotumiwa na upande wa upinzani hadi kikang’oka.

Mbunge wa Viti Maalumu (CUF), Mozza Abeid, alivuliwa hijabu katika vurumai hizo wakati polisi walipokuwa wakitumia nguvu ili kumfikia Mbowe.

Baada ya kuona hali inazidi kuwa mbaya, Mbowe aliamua kutoka nje huku akisindikizwa na polisi pamoja na wabunge wa vyama hivyo na alipofika nje ya ukumbi alipokewa na polisi wa kawaida waliomweka chini ya ulinzi kabla ya kumwachia baada ya ombi la Mbunge wa Rombo (Chadema), Joseph Selasini.

Kutokana na hali ya mambo kuwa tete, askari wa Bunge waliwaondoa wageni waliokuwa wamekaa katika kumbi za wageni wakiwamo wanafunzi wa shule mbalimbali za sekondari huku baadhi ya wabunge wa CCM waliokuwa na simu za kisasa za mkononi na kompyuta mpakato (Ipad) wakichukua picha za tukio zima.

Inadaiwa kwamba baada ya kutoka nje ya ukumbi, Mbilinyi alimtwanga ngumi mmoja wa askari waliomtoa kwa nguvu kabla ya kuamuliwa na wabunge na polisi.
Wakati wote huo, wafanyakazi wa Bunge na wageni walionekana wakiwa wamejikusanya katika makundi wakitafakari na kushangaa yaliyokuwa yakitokea.

Balaa lilivyoanza
Akitumia Kanuni ya 69(1), Mbunge wa Mkoani (CUF), Ali Hamisi Seif, alitaka kuahirishwa kwa mjadala wa Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba wa mwaka 2013 kutokana na ukweli kuwa Kamati ya Sheria, Katiba na Utawala ya Bunge ilipaswa kukusanya maoni ya wadau mbalimbali nchini ikiwamo upande wa Zanzibar jambo ambalo halikufanyika wakati wa maandalizi ya muswada huo.

“Ilipaswa sheria hii inapotaka kufanyiwa marekebisho iende tena kulekule Zanzibar lakini jambo la kusikitisha kamati inayohusika na masuala ya Katiba haikwenda. Mimi ni mjumbe wa kamati na tuliitwa Dar lakini ratiba waliyotupa haikuonyesha kama tungekwenda Zanzibar,” alisema. 

Mkosamali naye aliomba mwongozo kwa Spika, akisema kwa kuzingatia matakwa ya kiapo cha Spika au Naibu alipaswa kuendesha Bunge kwa haki bila upendeleo.

“Kanuni inasema Spika ama Naibu Spika ama Mwenyekiti ataendesha shughuli za Bunge kwa haki, uadilifu, bila chuki wala upendeleo wowote kwa kuongozwa na Katiba ya nchi,” alisema na kuongeza: “Kwa kuwa sisi tumekuweka hapo ili uendeshe Bunge kwa uadilifu, usiburuzwe na chama chako na uzingatie miongozo yote kwa wakati. Kwa nini usitumie mamlaka yako kuondoa muswada huu”?

Mbunge wa Peramiho (CCM), Jenister Mhagama aliomba mwongozo kwamba kwa kuwa bado kuna malalamiko basi waipe Serikali nafasi ya kuthibitisha kwamba majadiliano ya kamati yalikamilika.

Lissu katika kuomba mwongozo wake, alisema Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Sheria, Katiba na Utawala, Pindi Chana alilidanganya Bunge alipowasilisha maoni ya kamati kwamba wadau wa muswada huo walishirikishwa jambo ambalo alisema si kweli.

Lissu alisema hakuna Mzanzibari aliyefika mbele ya kamati hiyo kutoa maoni kuhusu muswada wowote.

Hata hivyo, Chana alijibu akisema wadau wa Zanzibar walitoa maoni yao na kukabidhi nyaraka mbalimbali kwa Spika kuthibitisha kauli yake hiyo. Alivitaja vyama vya Jahazi Asilia na ADC kuwa vilihojiwa.

Kwa upande wake, Lukuvi alimshambulia Lissu kwa kauli yake ya juzi kwamba uteuzi wa Wajumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba uliofanywa na Rais Jakaya Kikwete ulikuwa na walakini. “Lissu alisema jana (juzi) kwamba wapo wadau ambao walisema ijapokuwa waliandikiwa barua ya kuwasilisha majina matatu kila moja ili Rais ateue mmoja lakini hakuna mjumbe aliyeteuliwa”.

Alitaja majina ya walioteuliwa kuwa ni Maria Kashonda (Tec), Jesca Mkuchu (CCT), Humphrey Polepole (Civil Society) na Profesa Palamagamba Kabudi (Kundi la Wasomi).

Lukuvi aliwataja wengine waliopendekezwa na taasisi zao na Rais kuwateua kuwa ni Mwamtumu Malale (Bakwata) na Dk Sengondo Mvungi (NCCR) na Profesa Mwesiga Baregu wa Chadema.

Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Fredrick Werema alisema katika mchakato wa muswada huo, Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) iliwasilisha maoni yake mbele ya kamati.

Alisema Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi aliwasilisha kwa kamati mapendekezo ya SMZ, Mei mwaka huu na mapendekezo hayo ikiwamo uteuzi wa wajumbe 166 yalizingatiwa.


Waacha muswada, wapiga vijembe
Baada ya kurejea katika kikao cha Bunge cha jioni jana, wabunge wa CCM waliopewa fursa ya kuchangia mjadala wa muswada huo walitumia muda mwingi kuwajadili wabunge wa kambi ya upinzani.