Friday, September 6

‘Marekebisho yanazungumzika bungeni’




Dodoma. Waziri Mkuu, Mizengo Pinda amesema Serikali haitauondoa Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba kwa sababu mambo ambayo Kambi ya Upinzani Bungeni inayadai, yanazungumzika na yanaweza kubadilishwa kwa mamlaka ya wabunge.
Pinda alikuwa akijibu swali la nyongeza la Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe katika kipindi cha Maswali ya Kwa Waziri Mkuu Bungeni, Dodoma jana.
Mbowe ambaye pia ni Mbunge wa Hai (Chadema), alisema yapo matukio ya kibabe, kejeli, matusi na ya dharau ambayo yamekuwa yakifanya kuchelewa kwa utaratibu mzima wa utungaji wa sheria... “Pamoja na rai mliyoiondoa, sisi tunasema yapo maeneo mengi yasiyo na tija ambayo yanafanya msingi wa marekebisho ya sheria mlioleta jana (juzi), kuwa hayana tija kwa mchakato huu.”
Akijibu swali hilo, Pinda alisema: “Hivi kweli Mbowe una ngoja hadi muswada unafika ngazi ya Bunge, ndipo unakuja na hoja hiyo wakati tulikuwa na fursa kubwa?”
Alisema kwa mambo ambayo alielezwa kuwa ndiyo yaliyosababisha wabunge wa kambi ya upinzani kutoka nje ya Ukumbi wa Bunge juzi, hakuna atakayeona umuhimu wa kuondoa muswada huo.
“Kwa sababu ni vitu ambavyo ndani ya Bunge hili vinazungumzika na vinaweza kubadilishwa kulingana na mamlaka mliyopewa,” alisema.
Katika swali la msingi, Mbowe alisema mchakato wa Katiba Mpya unahitaji ustahimilivu, ushirikiano, uwazi, dhamira njema na kwamba wabunge wanapaswa kutambua kuwa wapo wadau nje ya Bunge wanahitaji ushirikiano.
Pinda alisema: “Mategemeo ni wabunge tulio ndani tutaujadili muswada huu kikamilifu na maeneo yote ambayo yanadhaniwa yanaweza yasiwe na tija, neema kwa nchi yetu, ni jukumu letu kujadili kwa uwazi, uaminifu na kiukweli.
Mbunge wa Kuteuliwa, James Mbatia (NCCR –Mageuzi), alihoji kama Serikali haioni ni busara mazungumzo ya kisiasa kufanyika kwanza kisha yakafuatiwa na sheria ambayo itasaidia kuunda dhana ya dola. Alisema kumekuwa na ukiukwaji mkubwa wa Katiba kwa kuruhusu mabadiliko ya Katiba ya Zanzibar.
Kuhusu hilo, Pinda alisema kulikuwa na mashauriano makubwa kati ya vyama, taasisi na pande mbili za Muungano kabla muswada huo kufikishwa bungeni na kwamba Katiba Mpya itameza yote yaliyomo katika katiba hiyo ya zamani na kuja na mawazo mapya ambayo itaongoza Taifa.

No comments:

Post a Comment