Friday, March 16

Mwili wa tajiri wa mabasi wakutwa kwenye kiroba


Wiki mbili tangu mmiliki wa kampuni ya mabasi ya Super Sami, Samson Josia kutoweka, mwili wake umepatikana katika Mto Ndabaka ukiwa umefungwa kwenye kiroba.
Mwili huo ulipatikana juzi ikiwa ni siku tano baada ya gari lake aina ya Toyota Land Cruiser kukutwa limeteketezwa kwa moto ndani ya eneo la Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, Ijumaa iliyopita.
Habari kutoka eneo la tukio zinasema kuwa mwili huo uliokotwa na wavuvi waliokuwa wakiendelea na shughuli zao ndani ya mto huo unaotenganisha Bunda na Busega.
Mfanyabiashara huyo, ambaye mabasi yake yanasafiri kati ya mikoa ya Mwanza, Dar es Salaam, Dodoma, Iringa na Kagera alikuwa akiishi Wilaya ya Magu mkoani Mwanza na alitoweka tangu Februari 27 ambayo ilikuwa siku ya mwisho kuwasiliana na familia yake.
Polisi wazungumza
Akizungumza kwa simu jana, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mara, Jaffari Mohammed alisema mwili uliookotwa umethibitika kuwa ni wa mfanyabiashara huyo.
Alisema mwili huo ulikutwa ukiwa umefungwa ndani ya mfuko wa ‘salfeti’ na kutupwa ndani ya Mto Ndabaka wilayani Bunda.
Kamanda Mohamed alisema jeshi hilo linawashikilia watu wanne kwa mahojiano kuhusiana na mauaji hayo huku likiendelea kuwasaka wengine ambao hakutaja idadi yao wanaohusishwa na kifo hicho.
“Tukio hili limejaa mambo mengi yenye utata, tunawashikilia watu wanne kwa mahojiano na tunaendelea na uchunguzi wa kina kuwanasa wote waliohusika,” alisema Kamanda Mohammed.
Aliwataka wananchi wenye taarifa zitakazosaidia kupatikana kwa waliohusika na kifo hicho wajitokeze kutoa taarifa kusaidia uchunguzi wa polisi.
Kikao kabla ya kupotea
Akizungumzia tukio hilo, ofisa habari wa Chama cha Wamiliki wa Mabasi Tanzania (Taboa), Mustapher Mwalongo alisema tukio la mwisho aliloshiriki mfanyabiashara huyo katika chama hicho ni cha kamati ndogo ya Taboa Mkoa wa Mwanza kilichofanyika Februari 26, siku moja kabla hajapotea.
“Ni tukio la kusikitisha na kuogofya, tunaviomba vyombo vya dola kufanya uchunguzi na kuwanasa wote waliohusika ili hatua za kisheria zichukuliwe dhidi yao,” alisema Mwalongo.
Mabasi yabeba waombolezaji
Mabasi zaidi ya 10 yanayomilikiwa na mfanyabiashara huyo jana yalikuwa yakisomba waombolezaji kutoka jijini Mwanza kwenda nyumbani kwake wilayani Magu.
Mmoja wa mawakala wa tiketi katika Kituo Kikuu cha Mabasi cha Nyegezi, Leonard Joseph alisema kifo hicho kimepokewa kwa mshtuko na wafanyakazi, wafanyabiashara na wadau wa sekta ya usafirishaji jijini Mwanza kutokana na mazingira yake na ukaribu wa marehemu na watu waliomzunguka.
“Kesho (leo), wote tutaenda kwenye mazishi Magu. Kuna mabasi zaidi ya matano yatabeba watu bure kwenda na kurudi msibani. Hata leo (jana), kuna mabasi yanapelekea waombolezaji kutokea Buzuruga,” alisema Joseph
Joseph aliliomba Jeshi la Polisi kufanya uchunguzi wa kina kuwanasa wahusika wa tukio hilo.
Watu kupotea, miili kuokotwa
Tukio hilo limetokea kukiwa na taarifa za matukio mengi ya watu kupotea katika mazingira ya kutatanisha katika miaka za hivi karibuni na miili ya watu kuokotwa ikiwa imefungwa kwenye viroba.
Tukio la kwanza lilibainika Desemba 6, 2016 katika Mto Ruvu eneo la Bagamoyo, Mkoa wa Pwani wakati miili zaidi ya 15 ilipopatikana ikiwa imefungwa kwenye viroba. Baadaye miili mingine iliokotwa kwa nyakati tofauti katika maeneo mbalimbali hasa fukwe za Bahari ya Hindi.
Baadhi ya watu waliotoweka na hawajapatikana ni pamoja na Ben Saanane ambaye alikuwa msaidizi wa mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, aliyetoweka Novemba 2016 na mwandishi wa habari wa kujitegemea wa Kampuni ya Mwananchi Communications Ltd (MCL), Azory Gwanda aliyetoweka zaidi ya siku 100 zilizopita.

Sumatra yagawanywa, chombo kipya cha kusimamia meli, bandari chaanzishwa

Dar es Salaam. Mamlaka ya Udhibiti, Usafiri wa Majini na Nchi Kavu (Sumatra) imegawanywa na kuanzishwa chombo kipya kitakachoshughulikia masuala ya meli na bandari.
Sheria namba 14 ya mwaka 2017 iliyopitishwa na Bunge iliridhia kuanzishwa kwa Shirika la Wakala wa Meli (Tasac) ambalo lilitajwa kuanza kazi, Februari 2018.
Kaimu mkurugenzi mkuu wa Tasac, Japhet Loisimaye alisema hayo alipokutana na wadau wanaotoa huduma za bandari na meli wakati wa kupitia kanuni mpya zilizoundwa.
Alisema chombo hicho kimeanzishwa ili kuleta ufanisi zaidi kwenye masuala ya bandari na usafiri wa majini ili kama kuna yaliyosahaulika au kuwekwa tofauti yashughulikiwe.
“Tumekutana ili kupitia kanuni kabla chombo hiki hakijaanza kazi rasmi, kama kuna lililowekwa tofauti liweze kurekebishwa na kama kuna lililosahaulika liweze kuingizwa,” alisema Loisimaye.
Alifafanua kuwa uamuzi huo umefikiwa ili kuboresha huduma na kupunguza muda wa mteja kukaa na kusubiri mizigo pamoja na kuboresha huduma za bandari na meli.
Loisimaye alisema kitaanzishwa chombo ambacho kitashughulikia masuala ya barabara hivyo kwa sasa wataendelea kutumia kanuni zilizopo na jina la Sumatra.
Wakala wa Forodha wa Kampuni ya Fly Shipping, Edward Urio akizungumzia sheria mpya za Sumatra, alisema wao wakiwa wadau hawapingi sheria zilizoletwa ila wanamuongezea Mtanzania ugumu wa kuendesha huduma kutokana na adhabu zilizowekwa.
Alisema wanapoanzisha kampuni ya kutoa huduma mtaji wake ni Sh50 milioni lakini kwa mzigo wa mteja utakaopotea watatozwa faini ya Sh40 milioni na kwa kosa litakalofanyika ni Sh60 milioni.
“Tunamuomba Rais atutengenezee mazingira mazuri ya kufanya biashara kwani adhabu iliyowekwa ni kubwa” alisema Urio.
Alisema sheria mpya zinawabana kuagiza baadhi ya bidhaa ikiwamo mashine kubwa za migodi hivyo wameomba ifanyiwe marekebisho waruhusiwe kuagiza.
Hawa Ally, mwakilishi kutoka TCCA alisema wakala wadogo kwenye sheria mpya wameongezewa malipo ya ukataji leseni na itakuwa vigumu kupata leseni mpya inapoisha muda wake.
“Changamoto yetu kubwa ni kuongezwa kwa malipo ya kukata leseni sisi wakala wadogo tutapata ugumu wa kupata leseni mpya” alisema Hawa.

Maswali matano yaibuka kutekwa mwanafunzi UDSM

Wanasheria na wanaharakati wameibua maswali matano kuhusu sakata la mwenyekiti wa Mtandao wa Wanafunzi Tanzania (TSNP), Abdul Nondo, anayeshikiliwa na Jeshi la Polisi kwa siku 10 sasa kwa madai ya kudanganya kuwa alitekwa.
Wanasema maelezo yaliyotolewa na polisi hayajaweka wazi baadhi ya mambo hivyo kuibua maswali zaidi kuhusu kutoweka kwa mwanafunzi huyo anayeshikiliwa na Kanda Maalumu ya Kipolisi Dar es Salaam.
Nondo, ambaye ni mwanafunzi wa mwaka wa tatu wa Chuo Kikuu Dar es Salaam (UDSM), alidaiwa kutoweka usiku wa kuamkia Machi 6 na kupatikana usiku wa Machi 7 huko Mafinga, Iringa baada ya kudaiwa kujisalimisha polisi.
Swali la kwanza linaloibuka ni kwa nini polisi hawamuweki wazi mpenzi wa Nondo na kumhoji kama walivyoeleza awali kuwa walifuatilia mawasiliano ya mwanafunzi huyo na kubaini alikwenda Mafinga kwa mpenzi wake.
Pia wamehoji sababu za Jeshi la Polisi Iringa na Dar es Salaam kutoa kauli zinazokinzana kuhusu tukio hilo.
Tatu, ni suala la mwanafunzi huyo kutopewa dhamana wala kufikishwa mahakamani; nne, sababu zilizotolewa na polisi kwamba hakutekwa kwa kuwa hakuwa na jeraha lolote wala mchubuko na tano ni taarifa za uchunguzi kwa watu mbalimbali waliotekwa kutowekwa wazi.
Kupewa dhamana
Wakili wa mwanafunzi huyo, Jebra Kambole alisema mteja wao anashikiliwa na polisi kinyume cha sheria kwa maelezo kuwa tangu akamatwe zimeshapita saa 24 ambazo zinairuhusu polisi kuwa naye kwa mujibu wa kifungu cha 20 cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai namba 32 (1).
Kambole alisema wanashangaa kuona Nondo anashikiliwa zaidi ya wiki sasa, huku ikionekana hakuna dalili za kupewa dhamana wakati kosa lake lina dhamana.
“Tumewasiliana na polisi mara kadhaa ili watukutanishe na mteja wetu lakini wametukatalia wakitueleza kwamba wamemshikilia kama mwathirika na sio mtuhumiwa, hivyo watatuita pale watakapokuwa wanamuhoji kama mtuhumiwa,” alisema Kombole.
“Kwa hali ilivyo tumeamua kufungua kesi Mahakama Kuu ili iweze kutusaidia kuamuru polisi wamfikishe mahakamani ambapo tutajua anashikiliwa kwa makosa gani kwa sababu Mahakama ina mamlaka kwa mujibu wa sheria,” alisema.
Madai ya kwenda kwa mpenzi wake
Kombole alisema taarifa ambayo inatolewa na polisi kuwa Nondo alikwenda kwa mpenzi wake Mafinga, haipaswi kuaminiwa kwa sasa kwa kuwa mteja wao hakupewa nafasi ya kuzungumza na mawakili wake kubainisha nini kilichomkuta, kwamba mpaka sasa bado hawajazungumza naye jambo lolote.
Kauli polisi Iringa, Dar kupishana
Machi 8, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Iringa, Juma Bwire alisema Nondo alijisalimisha polisi na kudai alitekwa na watu ambao walimtelekeza, kwamba wamefungua jalada la uchunguzi ili kubaini iwapo alitekwa au alitoa taarifa za uongo kwa lengo la kuhamamisha wanafunzi kuvuruga amani.
Wakati Bwire akieleza hayo, Kamanda wa Polisi Kanda Maalum Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa alisema mwanafunzi huyo alionekana Mafinga akiendelea na shughuli zake na wala hakuripoti tukio la kutekwa kituo chochote cha polisi na kwamba ndio sababu ya kuendelea kumshikilia.
Akizungumzia kupishana kwa kauli hizo Profesa wa Chuo Kikuu cha Ruaha, Gaudence Mpangala alisema kauli zilizotolewa na makamanda hao zinapishana huku zikionyesha kulenga kuunga mkono viongozi wa Serikali aliodai kuwa kabla ya uchunguzi wa polisi kukamilika, waliibuka na kudai kuwa Nondo amejiteka, anapaswa kuchukuliwa hatua kali.
“Kauli zao zinawaumbua inaonyesha wanafanya kazi ili kuunga mkono kauli za baadhi ya viongozi waliozungumzia tukio hilo hata kabla uchunguzi kukamilika,” alisema Profesa.
Profesa Mpangala alisema matukio ya baadhi ya watu kutekwa, kuteswa na kuuawa yapo, hivyo Polisi kuunganisha tuhuma za mwanafunzi huyo kujiteka huku wakiahidi kuendelea na uchunguzi ni mambo yanayoshangaza.
Kutokutwa na majeraha
Wakili Faraji Mangula alisema kwa mujibu wa sheria si lazima mtu aliyetekwa awe amejeruhiwa, anaweza asiwe na vyote hivyo lakini akatambuliwa kwa kuathirika kisaikolojia.
Mangula ametoa kauli hiyo baada ya Mambosasa kusema Nondo alikuwa na afya njema, hakupewa dawa yoyote ya kumlevya na hakuwa na majeraha.
Katika ufafanuzi wake Mangula alisema mtu aliyetekwa anaweza kutambulika kwa vitu vingi ikiwamo makovu yanaonyesha alipata kipigo au majeraha mabichi au kuathirika kisaikolojia.
Taarifa za uchunguzi
Mangula aligusia taarifa za uchunguzi wa matukio ya utekaji kutoanikwa hadharani, “Sheria ina upungufu kwenye masuala ya uchunguzi, ikilinganishwa na nchi nyingine ambazo taasisi au watu binafsi huchunguza. Hapa kwetu polisi pekee ndiyo wanachunguza, hata kama wenyewe ndiyo watuhumiwa.”
Alibainisha kuwa anayepaswa kuwahoji polisi kwa utendaji wao ni Mkuu wa Jeshi la Polisi au Tume ya Haki za Binadamu na Utawala bora ambayo ilianzishwa kwa lengo hilo.
Alisema taasisi hizo mbili zinapochelewa kushughulikia mambo hayo, ndipo jamii inashuhudia taasisi hiyo ikishikilia watu kinyume cha sheria, au kuchunguza baadhi ya matukio katika hali ambayo inaacha maswali mengi kwa jamii.
Kwa nini polisi wanatamka kwamba amesingizia kutekwa wakati yeye mwenyewe hajawahi kutamka kwamba ametekwa ila aliandika kwenye kupitia simu yake kwamba , “I am at high risk.”

Jinsi ya kutengeneza mtandao bora wa kiajira au kibiashara


Shughuli nyingi duniani zinafanikiwa kwa kutegemeana. Hauwezi kufanikiwa kwa kuamua kufanya kila kitu peke yako pasipo kuwashirikisha au kujifunza kutoka kwa wengine.
Hii inatulazimu kuhakikisha tunatengeneza mitandao ya watu watakao kuwa na tija kwenye mafanikio ya shughuli zetu.
Kila siku kuna jambo jipya la kujifunza linaloweza kukusogeza hatua moja mbele katika mafanikio ya kile unachofanya.
Njia nzuri ya kujifunza ni kuwa karibu na wale waliofanikiwa tayari.
Lengo la kutengeneza mtandao wa kiajira au biashara siyo kujifunza pekee, bali kupata fursa mbalimbali zinazoweza kuwa matokeo ya kuwa karibu na wale wanaoweza kuwa msaada katika kukupa fursa mbalimbali ikiwamo taarifa.
Wewe kama ni mfanyabiashara, kuna wafanyabiashara wengine ambao wanaweza kusadia biashara yako kwa namna moja ama nyingine.
Hawa ni watu wa kuwaweka karibu sana. Kama unatarajia kufanya kazi kwenye kampuni fulani hapo baadaye, ni vyema kutafuta mtu au watu wanaoweza kuwa msaada kufikia lengo hilo.
Mtandao wa kiajira au kibiashara ni jumla ya watu wako wa karibu unaowasiliana nao mara kwa mara huku uhusiano wenu ukiwa umejengwa kwa lengo la wewe kunufaika au kunufaishana katika shughuli mnazofanya au mnazotarajia kuzifanya.
Je, ni nani wa kumuweka kwenye mtandao wako?
Sio kila mtu anastahili kuwa kwenye matandao wako. Kuna mambo kadhaa ya kuzingatia unapoamua kumuingiza mtu kwenye aina hii ya mtandao.
Lakini kigezo kikubwa ni mtu anayaweza kukupa fursa au mwenye uwezo wa kukuunganisha na fursa au watu wengine wenye fursa au yeye mwenyewe ni fursa katika mafanikio ya shughuli zako.
Usimuweke mtu kwenye mtandao wako ambaye si msaada na wala hatakuwa msaada katika shughuli zako, sababu mwisho wa siku anaweza kuwa mzigo pia.Ukiwa unatamani kuwa mshereheshaji (MC) mwenye mafanikio, ni vyema kuanza kufanya utafiti ili kujua ni watu gani wamefanikiwa katika eneo hili na kuwaweka karibu. Wakati mwingine itakubidi kuwaomba ufanye nao kazi hata bila malipo ili uweze kujifunza na kuunganishwa na watu wengine wanaoweza kuwa msaada kwako.
Mbinu hii inawafaa sana wale walio kwenye mchakato wa kutafuta ajira. Ni vyema kuwa karibu na wale wanaoweza kuwa ngazi ya mafanikio yako kama siyo sasa basi ni ya baadaye.
Unawezaje kuwapata watu sahihi wa kuwaweka kwenye mtandao?
Kile unachokifanya au unataka kukifanya mara nyingi kinakuwa tayari kimeshafanywa na watu wengine na wameshafanikiwa kwa kiasi kikubwa. Ukitaka kuanzisha biashara ya kuafirisha nafaka kutoka mkoa mmoja kwenda mkoa mwingine wapo watu wamekuwa wakiifanya biashara hii kwa miaka mingi na wana uzowefu.
Tafuta wawasilino yao na omba kuonana nao ana kwa ana kama inawezekana.
Kama ni ngumu kuonana nao zungumza nao kwa simu au barua pepe ukieleza lengo la wewe kutaka kujifunza kutoka kwao.
Inawezekana wapo wanaoweza wasipende wazo hili lakini pia wapo wanaoweza kuonesha moyo wa kusaidia.
Katika masuala ya biashara wateja wako wa sasa na wateja wako watarajiwa ni watu muhimu sana kuwaweka karibu ili wawe msaada kwenye biashara yako.
Wapo wafanyabiashara waliojiwekea utaratibu wa kuwajulia hali wateja wao na kufanya ufuatiliaji wa mrejesho wa huduma au bidhaa wanayo uza.
Kumbuka ni vyema kuwa mtu wa kujichanganya na kujitambulisha kwa watu tofauti ili wajue unafanya shughuli gani na kama ni mtafuta ajira wajue sifa ulizo nazo. Umeenda kwenye kongamano na umekutana na watu mbali mbali, wasalimie, ongea nao ili ujue shughuli waazofanya na mwisho ubadilishane nao mwasiliano na ukumbuke kuwasiliana nao muda mfupi baada ya kuachana nao.
Jinsi ya kuimarisha mtandao wako
Unapoamua kuanzisha mtandao au kumuweka mtu kwenye mtandao wako ni vyema kuzingatia kuwa ili mtandao uwe na tija ni lazima uimarishwe.
Njia kuu ya kuimarisha mtandao wa aina hii ni mawasilinao ya mara kwa mara.
Mawasiliano haya yanaweza kuwa kwa njia ya simu, barua pepe na njia nyingine za mawasilinao lakini kukutana ana kwa ana pale inapowezekana.
Wasiliana na wadau wako hasa wateja.
Unaweza jiuliza, kama nina wateja wengi sana huo muda wa kumjulia hali mmoja mmoja au kujua kama wamelidhika na huduma ua bidhaa yangu nitautoa wapi? Si lazima ufanye wewe lakini pia teknolojia imerahisisha mawasilino kwani waweza tuma barua pepe moja kwa mamia ya wateja wako au kwa kuwatumia ujumbe mfupi wote kwa pamoja.
Kwa wale wadau wako wakuu au wa karibu sana ni vyema kufanya mawasilino ya moja kwa moja na ikiwezekana kukutana nao mara kwa mara.
Suala jingine ni kuhakikisha kuwa unakuwa mwaminifu. Si vyema kutoa taarifa za uongo na ahadi usizowezo kuzitekeleza.
Mambo haya yana athari kubwa sana katika mtandao na yanaweza kukuharibia sifa njema na kuondoa imani kutoka wadau mbali mbali.
Angalizo
Kwa kuzingatia kuwa mawasiliano ndiyo msingi wa mtandao bora ni vyema kuhakikisha kuwa mawasiliano yanafanywa kwa uangalifu.
Watu hututathamini kwa namna tunavyowasiliana nao.
Hakikisha kuwa mawasilino yako hayawi kero au usumbufu kwa watu kwenye mtandao wako.
Ni vyema kuzingatia muda wa kufanya mawasilino; si kila wakati ni muda muafaka wa kufanya mawasilino.
Wapo ambao hawapendi kufanya mawasiliano usiku wanapokuwa na familia zao na hupenda kufanya hivyo muda wa kazi pekee.
Mtandao bora ni ule ambao ni kutegemeana na siyo wa kunufuisha upande mmoja hivyo ni vyema kuhakikisha unajitahidi kuangalia mtandao wako utawanufaishaje watu kwenye mtandao wako.
Inawezekana hauwezi kutoa ajira lakini unaweza kutoa taarifa zinazoweza kuwa msaada kwa watu wengine kwenye mtandao wako.

DTB yaahidi neema


Benki ya Diamond Trust (DTB) imewaahidi wajasiriamali wadogo na kati kuwapatia mkopo Sh500 milioni ndani ya siku tano.
Ahadi hiyo imetolewa na meneja wa benki hiyo, Viju Cherian kwa wajasiriamali hao kwenye warsha iliyofanyika mjini Morogoro jana.
“Kutokana na mchango wao kwenye uchumi, wajasiriamali wadogo na kati wanahitaji kuungwa mkono kwenye shughuli zao. Kwa miaka miwili iliyopita, tumekopesha zaidi ya Sh285 bilioni. Kwa sasa, mteja anaweza kupata mpaka Sh500 milioni ndani ya siku tano tu,” alisema Cherian kwenye warsha hiyo ya kuwajengea uwezo wajasiriamali.
Kwa kushirikiana Kampuni ya Ushauri wa Kodi ya PFK Associates, wajasiriamali walifundishwa namna ya kutunza vitabu vya kumbukumbu za biashara, Sheria ya Kodi na utaratibu wa kulipa, Sheria ya Fedha ya mwaka 2017 pamoja na Sheria ya Ajira.
Fursa hiyo pia, ilitumika kuwapa uelewa wa bidhaa mbalimbali zinazotolewa na benki hiyo pamoja na taasisi nyingine za fedha kama udhamini wa benki kwenye miradi mikubwa, udhamini wa bima na uhamishaji wa fedha.
Cherian alisema wafanyabiashara hao wanahitaji kuboresha mazingira yao hasa kuzingatia sheria na kanuni za nchi ili kusonga mbele zaidi.

Viongozi watano Chadema washindwa kufika polisi


Viongozi wawili wa Chadema leo Machi 16 wamewasili kituo kikuu cha polisi na wengine watano kushindwa kufika.
Viongozi waliowasili ni Mwenyekiti wa Chadema Taifa Freeman Mboe na Naibu katibu Mkuu Zanzibar Salum Mwalimu.
Machi 13 Katibu Mkuu, Dk Vicenti Mashinji na Naibu Salum Mwalimu walifika wakati viongozi wengine watano ambao ni wabunge walishindwa kufika kutokana na kuwapo Dodoma kwenye vikao vya kamati za kudumu za bunge.
Wakili Alex Massaba amesema viongozi walioshindwa kufika ni wabunge na Katibu Mkuu  ni kiongozi wa chama.
"Tumekuja kuripoti kama tulivyoambiwa ila kama mnavyojua kamati zinaendele na vikao waliobaki ni wabunge na katibu mkuu yuko kwenye majukumu mengine," amesema Massaba.
Ameongeza kuwa tarehe 26 itakuwa ni mara ya mwisho kufika kituoni hapo kwani viongozi wote walishahojiwa na kama mashtaka yao yanafaa kuwafikisha mahakamani ni vyema wangepelekwa.
Mbali na katibu mkuu Mashinji wengine ambao hawakufika ni naibu katibu mkuu bara John Mnyika, mwenyekiti wa wanawake Halima Mdee, mwenyekiti wa kanda ya Serengeti, John Heche na mweka hazina wa kanda hiyo Ester Matiko.
Viongozi hao wametakiwa kufika tena kituoni hapo siku ya Alhamisi Machi 22 saa mbili asubuhi.
Viongozi hao walipokea wito Februari 20 na jeshi la polisi likiwataka kufika kituoni hapo baada ya maandamano ya Februari 16 walipokuwa wakielekea kudai viapo kwenye ofisi ya msimamizi wa uchaguzi ambapo Mwanafunzi wa Chuo cha Usafirishaji (NIT) Akwilina Akwilini alifariki dunia akiwa kwenye daladala kwa kupigwa risasi eneo la Mkwajuni, Dar es Salaam.

Mabasi yabeba waombolezaji bila malipo


Magu. Vilio, simanzi na majonzi vimetawala kwa  waombolezaji kutoka jijini Mwanza na maeneo jirani wanaendelea na ibada ya mazishi ya mfanyabiashara Samson Josia yanayofanyika nyumbani kwake mtaa wa majengo mapya wilaya ya Magu mkoani Mwanza.
Mwili wa mfanyabiashara huyo uliokutwa ukiwa umefungwa kwenye viroba ukielea ndani ya Mto Ndabaka mpakani mwa wilaya za Bunda mkoa wa Mara na Busega mkoani Simiyu umewasili asubuhi ya leo Machi 16 ukitokea Hospitali ya Rufaa Mara ulikohifadhiwa kwa ajili ya uchunguzi tangu juzi.
Tangu asubuhi, mamia ya waombolezaji kutoka jijini Mwanza na maeneo jirani wamekuwa wakimiminika nyumbani kwa marehemu wakitumia mabasi ya kampuni aliyokuwa akimiliki.
Mabasi ya kampuni nyingine pia yanatumika kusafirisha waombolezaji kutoka jijini Mwanza bila malipo.
Marehemu Josia aliyezaliwa mwaka 1968 alipotea tangu Februari 27 kabla ya gari lake kukutwa likiwa limeteketezwa kwa moto ndani ya eneo  la hifadhi ya Taifa ya Serengeti mkoani Mara Machi 9.
Ibada ya mazishi inaongozwa na Mchungaji Jackson Meza kutoka Kanisa la African Inland Church of Tanzania (AICT) huku kwaya ya kanisa ambayo marehemu alikuwa mfadhili wake ikiimba nyimbo za maombolezo.
Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi mkoa wa Mara, Jaffari Mohamed, watu wanne wanashikiliwa na jeshi hilo kwa mahojiano kuhusiana na kifo hicho kilichoibua hofu na maswali yasiyo na majibu miongoni mwa ndugu, jamaa, marafiki na wakazi wa jiji la Mwanza ambako marehemu alikuwa akiendesha shughuli zake za kibiashara.

Kampuni ya TCCIA yaorodheshwa DSE

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango,
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango, Amina Shaaban 
Kampuni ya Uwekezaji ya Chama cha Wafanyabiashara Wenye Viwanda na Wakulima (TCCIA investment) imesajiliwa Soko la Hisa Dar es Salaam (DSE).
Kampuni hiyo ya 27 kuorodheshwa DSE, imekamilisha mchakato huo baada ya kufanikiwa kuuza hisa milioni 112.5 kwa Sh400 kila moja.
Akizindua uorodheshaji huo, leo Machi 16, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango, Amina Shaaban ameipongeza kampuni hiyo kwa uwezo wake wa kusimamia michango ya wanachama walioianzisha mpaka kufikisha mtaji wa Sh30 bilioni.
"Mtaji wenu umeongezeka kutoka Sh1.97 bilioni mpaka Sh30 bilioni mwaka jana. Mmefika hapo bila kukopa wala kupata msaada kutoka taasisi yoyote," amesema Amina.
Kuongeza ushiriki wa Watanzania kwenye biashara ya hisa, Amina amewataka wadau kutoa elimu kwa wananchi ili kuwapunguzia mashaka waliyonayo.
Kampuni hiyo ilianza kuuza hisa zake za awali (IPO) Februari Mosi mchakato uliokamilika Machi 14 na ilitarajiwa kuorodheshwa Aprili 24 mwaka jana. Hata hivyo, kutokana na kutokamilisha utaratibu wa DSE unaotumika hivi sasa, ililazimika kusubiri mpaka leo.
Ofisa mtendaji mkuu wa TCCIA Investment, Donald Kamori amesema mapungufu ya taarifa za wanahisa wa awali wa kampuni hiyo iliyoanzishwa mwaka 1999 ndiyo yaliyochangia ucheleweshaji huo.

"Sasa hivi kila mwanahisa ni lazima awasilishe akaunti ya benki, namba ya simu, nakala ya kitambulisho, majina yake matatu na anuani yake miongoni mwa taarifa muhimu zinazohitajika. Zamani haikuwa hivyo...muda wote huu tulikuwa tunakusanya taarifa hizo," amesema Kamori.

Adaiwa kukutwa na mihuri ya Serikali


Dar es salaam. Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam linamshikilia mkazi wa Yombo Kilakala kwa tuhuma za kukutwa na nyaraka mbalimbali ikiwamo mihuri na vyeti vya taasisi za Serikali.
Akizungumza leo Machi 16 Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalum Lazaro Mambosasa amesema Machi 13 saa 10:30 jioni baada ya kupata taarifa walikwenda kufanya upekuzi kwenye nyumba ya mtuhumiwa huyo kwa kushirikiana na uongozi wa Serikali ya mtaa na kufanikiwa kumkamata mtuhumiwa na nyaraka hizo.
“Baada ya kufanya upekuzi tulikamata mihuri ya Baraza la Mitihani (Necta), muhuri wa Veta (Mamlaka ya Elimu ya Ufundi Stadi Tanzania), Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Chuo cha Sokoine (Sua), Chuo cha Bandari na Chuo cha Usafirishaji (NIT),” amesema Mambosasa.
Alitaja vitu vingine alivyokuta navyo kuwa ni mihuri ya Mahakama ya Kisutu, Mkuu wa Shule ya Marangu, Mkurugenzi wa Jiji la Estern London pamoja na nyaraka nyingine za shule za msingi na sekondari.

Watanzania wakamatwa na dawa za kulevya Kenya


Dar es Salaam. Watanzania watatu wamekamatwa Kenya wakidaiwa kukutwa na dawa za kulevya aina ya heroin zenye thamani ya Sh1.9 bilioni.
Watuhumiwa hao ambao majina yao hayakutajwa walinaswa wakiwa katika hoteli moja mjini Mombasa huku dawa hizo zikiwa zimefichwa katika nguo zilizowekwa kwenye mabegi.
Kwa mujibu wa gazeti dada la Mwananchi, Daily Nation la Kenya, polisi walikuwa wakijiandaa kuwafikisha mahakamani. Waliingia nchini humo kwa usafiri wa basi wakitumia mpaka wa Lunga Lunga.
Dawa hizo zinadaiwa kuwa na uzito wa kilogramu 30.
Katika miaka ya hivi karibuni Kenya imekuwa ikichukua mkondo wa mataifa mengine duniani kukabiliana na mitandao inayosafirisha dawa za kulevya.
Mapema mwaka uliopita vyombo vya usalama vya Taifa hilo viliwakamata washukiwa 13 wa ulanguzi wa dawa za kulevya mjini Mombasa.

‘Wakazi wa Dar maji yapo, msilalamike’


Dar es Salaam. Wakazi wa Dar es Salaam wametakiwa kuacha kulalamikia uhaba wa maji kwa kuwa huduma hiyo inapatikana kwa wingi katika sehemu kubwa ya jiji.
Ofisa Mtendaji Mkuu wa Shirika la Majisafi na Majitaka (Dawasco), Mhandisi Cyprian Luhemeja amesema hayo leo wakati wa maadhimisho ya wiki ya maji.
Amesema kuna changamoto kubwa ya watu kutoomba maji licha ya kuwa maji ya Dawasco yanapatikana katika maeneo yao.
Mhandisi Luhemeja amesema kwa sasa Dawasco inazalisha lita milioni 502 kwa siku ambayo ni sawa na asilimia 92 ya maji yanayohitajika. 
"Maji yapo tena mengi sana na tunaendelea na juhudi kuhakikisha tunayafikia maeneo yote, nichukue fursa hii kuwaambia wakazi  Dar na Pwani, maji yapo waje waombe," amesema  Mhandisi Luhemeja na kuwataka viongozi wa Serikali za mitaa kuwawezeshe wananchi kuzifikia huduma za shirika hilo.
"Viongozi wa mitaa wawakusanye wananchi wanaotaka maji, waje kwetu hatulipishi gharama zozote mwanzoni, utapigiwa hesabu kisha utaunganishiwa maji halafu utalipa taratibu," amesema. 
Katika hatua nyingine, Mhandisi Luhemeja amesema shirika hilo linatambua ufinyu wa mtandao wa maji taka na liko mbioni kutatua changamoto hiyo.
Amesema tayari Sh26 bilioni na kazi ya upanuzi wa mtandao huo itaanza. 
"Lengo ni kuwasaidia wananchi hasa katika maeneo yanayokumbwa na magonjwa ya kipindupindu kama Tandale, Mwananyamala Kisiwani na Makumbusho," amesema.
Dawasco pia, imejipanga kuongeza mtandao wa usambazaji maji kwa mwaka wa fedha 2018/19 na kwamba Sh62 bilioni zimetengwa kwa ajili ya kazi hiyo.
Mhandisi Luhemeja amesema upanuzi huo umelenga kuyafikia maeneo ya Tabata,Temeke, Kigamboni, Kimara na kwenye viwanda wilayani Kibaha.

Waandishi watakiwa kuwa na umoja

Rais wa Baraza la Habari Tanzania (MCT), Jaji mstaafu Thomas Mihayo amewataka waandishi wa habari kuwa na umoja na kuaminiana na Serikali iliyopo madarakani ili kufikia lengo la kuwatumikia wananchi kwa pamoja.
Akizungumza Machi 15, 2018 katika hafla ya kuiaga na kuikaribisha Bodi mpya ya MCT jijini Dar esSalaam, Jaji Mihayo amesema tasnia ya habari inapita katika mawimbi makubwa ili kuyashinda inahitajika ushirikiano wa pamoja wa wadau wote.
Akizindua bodi hiyo, mgeni rasmi katika hafla hiyo, Mwandishi nguri, Hamza Kasongo amesema MCT imesaidia nchi kadhaa kushawishi kuanzishwa kwa Baraza la Habari.
Kasongo amesema kwa miaka miwili kuna vyombo vya habari vimefungiwa, kufutwa na vingine kutozwa faini kwa madai ya kutangaza habari ambazo hazikuwa na mizania.
Naye Mhariri Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Mwananchi Communications Limited (MCL), Bakari Machumu ambaye ni mmoja wa wajumbe wa bodi ya MCT amesema vyombo vya habari na Serikali, Bunge au Mahakama wanapaswa kuwa wadau wanaotegemeana kutokana na umuhimu wake kwenye jamii.
Amesema vyama mbalimbali vya habari na waandishi mmoja mmoja wanapaswa kutambua jukumu kubwa walilonalo la kuihudumia jamii.

RC Makonda amsifu Meya wa Chadema


Dar es Salaam. Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Paul Makonda amesifia utendaji kazi wa meya wa jiji Isaya Mwita kwa kile alichodai hayumbishwi na misimamo ya vyama.
Akizungumza leo Machi 16, Makonda alisema Mwita ambaye ni diwani wa Chadema hana tabia kama za wenzake na muda mwingi anafikiria maendeleo.
Akiwa katika uzinduzi wa wiki ya maji baada ya Mwita kumkaribisha kuzungumza, Makonda alianza kwa kumtania,
"Meya nilijua utazungumzia maandamano ila niseme wazi namkubali sana Isaya, ni miongoni mwa watu ambao unaweza kukaa nao mkazungumzia maendeleo."
"Hii ndiyo aina ya maandamano inayotakiwa. Tunataka kuandamana kwa kujadili na kutafuta ufumbuzi wa changamoto kwa wananchi tunaowaongoza.
"Wangekuwa wale wengine wangejiweka huko lakini huyu anapenda maendeleo.
"Wengine wanasubiri wawaingize watoto wa watu barabarani waandamane wavunjwe miguu halafu wawatafute watu wa Ulaya wawape hela," amesema Makonda.

Mtoto aliyezuia kuuzwa shamba ataka ualimu

Mwanafunzi wa darasa la kwanza aliyemzuia baba yake kuuza shamba kwa kumtishia kumpeleka polisi, amesema ndoto yake ni kuwa mwalimu.
Mwanafunzi huyo, Anthony Petro (10) anayesoma katika Shule ya Msingi Ngunduzi wilayani Ngara Mkoa wa Kagera, amesema akiwa mwalimu atawasaidia watoto wengi kuelimika.
Anthony amesema kutokana na ndoto yake hiyo ameamua kusoma kwa bidii kwa kuwa anajiamini ana uwezo wa kufanya vizuri.

Mwandishi aliyekimbilia Finland aijibu Serikali


Dar es Salaam. Mwandishi wa habari Ansbert Ngurumo ameijibu Serikali huku akisisitiza kupata vitisho, ikiwamo kutishiwa maisha kutokana na namna alivyowakosoa viongozi.
Majibu ya Ngurumo yametokana na maelezo ya Serikali kwamba madai ya mwandishi huyo si ya kweli na yamejaa usanii.
Ngurumo ambaye kwa sasa amepewa hifadhi nchini Finland, amedai kwamba Serikali haina rekodi nzuri juu ya watu wanaofuatiliwa na kutekwa ndiyo maana haijui hata Azory Gwanda na Ben Saanane waliko.
Amehoji kama maelezo yake ni usanii wanaotenda maovu ya kuteka na kutesa watu ndani ya nchi, inakuwaje Serikali isijue ni akina nani?
Ngurumo amesema wasamaria ndiyo waliomsaidia kutoroka na kuzijua mbinu za watu waliokuwa wakitaka kumdhulu, hasa katika mikoa ya Mwanza, Kagera na Dar es Salaam ikiwamo kuyatambua magari waliyokuwa wakiyatumia kumfuatilia.
Amesema mbali na kutoa taarifa kupitia mtandao wa kijamii wa Twitter Oktoba 3, 2017, hakutaka tena kupiga kelele na badala yake aliendelea kupambana kimyakimya, kujilinda na kumulika wabaya wake akiwa mbali.

Tanzania na Burundi miongoni mwa nchi ambazo raia hawana furaha duniani kwa mujibu wa UN 2018

Mwanamke mwenye huzuniHaki miliki ya pichaAFP
Tanzania, Burundi na Rwanda zimeorodheshwa kuwa kati ya nchi zenye watu wasio na furaha duniani katika orodha ya kila mwaka ya Umoja wa Mataifa kuhusu viwango vya furaha duniani.
Burundi ndilo taifa ambalo wakazi wake hawana furaha zaidi duniani katika nafasi ya 156 ambapo imechukua nafasi hiyo kutoka kwa Jamhuri ya Afrika ya Kati (CAR) iliyokuwa inashikilia nafasi hiyo mwaka jana.
CAR ndiyo inayoifuata Burundi katika orodha ya mwaka huu.
Tanzania imeshika nafasi ya 153 sawa na mwaka jana huku Rwanda pia ikishikilia nafasi ya 151 sawa na mwaka jana kati ya mataifa 156.
Orodha ya mwaka jana hata hivyo ilishirikisha mataifa 155.
Taifa linaloongoza kwa furaha duniani mwaka huu ni Finland, kwa mujibu wa ripoti hiyo ya UN ambapo nchi hiyo imechukua nafasi hiyo kutoka kwa Norway.
Ripoti hiyo huangazia furaha waliyo nayo watu wa taifa furahi na chanzo cha furaha hiyo.
People enjoy a sunny day on the Esplanade in Helsinki, Finland, in May 2017Haki miliki ya pichaREUTERS
Image captionMataifa ya Ulaya Kaskazini yanashikilia nafasi tano za juu katika orodha hiyo, Finland wakiongoza
Mataifa ya Ulaya Kaskazini yanashikilia nafasi tano za juu kwa kuwa na viwango vya juu vya raia walioridhika, huku nchi zilizoathiriwa na vita vya muda mrefu pamoja na nchi kadha za Afrika Kusini mwa Sahara zikiendelea kwa mara nyingine kushikilia nafasi tano za chini.
Burundi, taifa ambalo raia hawana furaha zaidi, lilitumbukia kwenye mzozo wa kisiasa baada ya Rais Pierre Nkurunziza kuamua kuwania tena urais kwa muhula wa tatu mwaka 2015. Mwaka huo kulitokea pia jaribio la mapinduzi ya serikali.
Nchi zenye watu walio na furaha na wasio na furaha Duniani mwaka 2018
Nchi zenye watu walio na furaha DunianiNchi zenye watu wasio na furaha Duniani
1. Finland147. Malawi
2. Norway148. Haiti
3. Denmark149. Liberia
4. Iceland150. Syria
5. Switzerland151. Rwanda
6. Netherlands152. Yemen
7. Canada153. Tanzania
8. New Zealand154. South Sudan
9. Sweden155. Central African Republic
10. Australia156. Burundi
Orodha hiyo huaandaliwa kwa kuangazia pato la mtu kwa kila mwaka, miaka ambayo mtu anatarajiwa kuishi, kuwa na mtu wa kutegemea kwa usaidizi, dhana ya kuwepo uhuru wa kufanya maamuzi maishani, uhuru kutoka kwa ufisadi, na ukarimu miongoni mwa mengine.
Imetayarishwa na shirika la maendeleo endelevu, Sustainable Development Solutions Network (SDSN), ambalo lilianzishwa na Umoja wa Mataifa.
Mwaka 2017, hali ilikuwa hivi:
Nchi zenye watu walio na furaha na wasio na furaha Duniani mwaka 2017
Nchi zenye watu walio na furaha DunianiNchi zenye watu wasio na furaha Duniani
1. Norway146. Yemen
2. Denmark147. Sudan Kusini
3. Iceland148. Liberia
4. Uswizi149. Guinea
5. Finland150. Togo
6. Uholanzi151. Rwanda
7. Canada152. Syria
8. New Zealand153. Tanzania
9. Australia154. Burundi
10. Sweden155. Jamhuri ya Afrika ya Kati
Maoni ya Watanzania kuhusu ripoti hii
tanzania
Image captionWageni waliokuja kutembea Tanzania hawawezi kujua maisha yetu
tz
Image captionTanzania imekuwa na amani miaka yote
tanzania
Image captionMusa anatamani kupata ufafanuzi zaidi maana alijiuliza sana
Mwaka huu, ripoti hiyo iliangazia pia takwimu kuhusu furaha ya wahamiaji katika mataifa wanamoishi ambapo Finland iliibuka kuwa nchi bora zaidi kwa wahamiaji kuishi.

Finland hufahamika sana kutokana na nini?
  • Raia wa Finland hupenda sana bafu ya mvuke, pengine kutokana na baridi kali nchini mwao. Taifa hilo bafu za mvuke 3.3 milioni za kutumiwa na raia 5.5 milioni.
  • Ndiyo nchi iliyo na bendi nyingi zaidi za muziki aina ya 'metal'. Bendi zao maarufu ni kama vile HIM, Nightwish na Children of Bodom
  • Kutoka Lapland, unaweza kuwaona kulungu wa nchi za baridi, Mwanga wa Kaskazin na iwapo una bahati utamuona Santa Claus
  • Taifa hilo ni maarufu duniani kwa vibonzo kama vile Moomins na app ya kuchezwa kwenye simu ya Angry Birds
"Nafikiri kila kitu hapa kimepangwa kuwawezesha watu wanafanikiwa, kuanzia kwa vyuo vikuu na mifumo ya uchukuzi ambayo hufanya kazi vyema sana," mwalimu Mmarekani Brianna Owens, anayeishi jiji la pili kwa ukubwa Finland, Espoo, aliambia Reuters.

Shirika hilo la UN liliorodheshwa nchi 156 kwa viwango vya furaha na 117 kwa furaha ya wahamiaji.
Norway, Denmark, Iceland na Uswizi ndizo nchi hizo nyingine zinazoshikilia nafasi tano za kwanza kwa furaha.
Uingereza na Marekani zinashikilia nafasi za 19 na 18 mtawalia.
Togo imeimarika zaidi mwaka huu kwa kupanda nafasi 17, nayo Venezuela ikashika zaidi - nafasi 20 - hadi 102.
'Wahamiaji wenye furaha'
Utafiti huo ulibaini kuwa mataifa 10 yenye furaha zaidi pia yanaongoza kwa wahamiaji wao kuridhika.
Finland, taifa la watu 5.5 milioni, lilikuwa na wahamiaji 300,000 mwaka 2016.
Ripoti hiyo ya UN huandaliwa pia kwa kuwahoji watu zaidi ya 1,000 katika zaidi ya nchi 150.
Ripoti hiyo hata hivyo huwa haielezi ni kwa nini nchi moja ina furaha zaidi kushinda nyingine.