Sunday, October 22

Mabaki ya ndege aina ya helikopta iliyoanguka Kenya haijapatikana

Majina ya watu waliokuwemo kwenye Ndege moja aina ya Helikopta ambayo ilihusika katika ajali Jumamosi asubuhi katika Ziwa Nakuru nchini Kenya, yametolewa. Kwa mjibu wa kanmshena wa kaunti ya Nakuru, Joshua Nkanatha, ndege hiyo ya Helikopta ilikuwa njiani kuelekea maeneo ya Narok ambapo Rais Uhuru Kenyatta alikuwa ahutubie mkutano wa kisiasa, siku chache kabla ya kufanyika uchaguzi mkuu wa Urais Oktoba 26, ajali hiyo ilipotokea.
Huyu ndiye Rubani Apollo Malowa wa ile ndege iliyoanguka Nakuru katika maeneo ya Bonde la Ufa nchini KenyaHaki miliki ya pichaTWITTER
Image captionHuyu ndiye Rubani Apollo Malowa wa ile ndege iliyoanguka Nakuru katika maeneo ya Bonde la Ufa nchini Kenya
Majina ya waliokuwemo kwenye Ndege hiyo imetolewa
Majina ya wahasiriwa ambao bado hawajapatikana ni Bwana Sam Gitau, John Mapozi, Anthony Kipyegon na mwanamke aliyetambuliwa tu kama Veronicah, pamoja na rubani wa ndege hiyo Bwana Apollo Malowa. Hadi sasa watano hao hawajulikani waliko.
Ramani ya Kenya
Image captionRamani ya Kenya
Ndege hiyo pia ilikuwa imepangiwa kuwabeba waandishi wa vyombo kadhaa vya habari nchini Kenya.
Taarifa ambazo bado hazijathibitishwa na wakuu nchini Kenya, zinasema kuwa abiria wa ndege hiyo pamoja na rubani walikuwa walevi- Kwani walikesha usiku kucha wakinywa vileo katika maeneo kadhaa ya burudani mjini Nakuru.
Ndege hiyo ya helikopta aina ya 5Y-NMJ ilianguka katika ziwa Nakuru nchini Kenya muda mfupi baada ya kuondoka katika hoteli moja mjini humo.
Afisa mkuu wa Polisi mjini Nakuru Joshua Omukata amethibitisha kutokea kwa ajali hiyo huku akikanusha taarifa kuwa ndege hiyo inamilikiwa na Rais Uhuru Kenyatta. Ndege hiyo inadaiwa kumilikiwa na kampuni ya Flex Air Charters, na kusimamiwa na Kapteni Bootsy Mutiso.
Aidha, amesema kuwa shughuli za kutafuta mabaki ya ndege hiyo na miili ya wahasiriwa zinaendelea.
Ripoti zinasema kuwa kulikuwa na watu watano katika ndege hiyo.
Seneta wa Nakuru Susan Kihika amesema kuwa watatu kati ya wale waliokuwa wameabiri ndege hiyo, walikuwa wanachama wa kitengo chake cha mawasiliano.
Kwa mjibu wa kanishena wa kaunti ya Nakuru, Joshua Nkanatha, ndege hiyo ya Helikopta ilikuwa njiani kuelekea maeneo ya Narok ambapo Rais Uhuru Kenyatta alikuwa ahutubie mkutano wa kisiasa, siku chache kabla ya kufanyika uchaguzi mkuu wa Urais Oktoba 26, ajali hiyo ilipotokea.
Marehemu Apollo Malowa na wengine wanne walifariki katika ajali hiyoHaki miliki ya pichaTWITTER
Image captionMarehemu Apollo Malowa na wengine wanne walifariki katika ajali hiyo
Ndege hiyo iliondoka katika hoteli ya Jarika County Lodge na duru zinasema kuwa ilikuwa ikipaa chini chini kabla ya kuanguka.
Ndege hiyo ilitarajiwa kusafrisha waandishi wa habari katika mkutano wa kampeni za Rais Uhuru Kenyatta.
Waokoaji walilazimika kusubiri boti kusafirishwa kutoka Ziwa Naivasha.
Mkurugenzi wa Idara ya kitaifa ya kukabiliana na majanga Pius Masai amesema kuwa ndege ya polisi imetumwa katika eneo hilo kusaidia katika uokoaji.

Sauti ya Lissu ilivyoibua gumzo siasa za wiki


Sauti iliyosikika kwa mara ya kwanza tangu mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu apigwe risasi Septemba 7, si tu kuwa iligusa hisia za watu wengi, lakini inaweza kuwa miongoni mwa habari zilizotikisa wiki inayofikia ukingoni leo.
Lissu, ambaye alipigwa risasi akiwa nyumbani kwake, Area D mjini Dodoma, anapata matibabu katika Hospitali ya Nairobi nchini Kenya na kwa mara ya kwanza picha na sauti aliyorekodiwa zilitolewa kwa umma, Jumatano.
Tangu alipopigwa risasi, Lissu ameibua mijadala mingi huku watu wakijiuliza ni nani hasa aliyehusika katika jaribio la kutaka kumuua na kwa maslahi gani. Hata hivyo, Jeshi la Polisi limesisitiza kwamba linaendelea kuchunguza tukio hilo.
Chadema inavituhumu vyombo vya ulinzi na usalama na kusisitiza kwamba kuna haja ya kuruhusu vyombo vya uchunguzi kutoka nje ili kubaini ukweli wa tukio hilo.
Siku za nyuma wafuasi wa Lissu walijitokeza kumwombea, lakini walidhibitiwa na polisi kwa madai kwamba wanahatarisha amani.
Mikusanyiko yote ya kumwombea Lissu ilipigwa marufuku na wafuasi hao kutakiwa kufanya hivyo kwenye nyumba za ibada.
Matibabu ya Lissu yanagharamiwa na michango ya wananchi na wafuasi wa chama hicho na tayari zaidi ya Sh400 milioni zimetumika.
Oktoba 17, mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe alitoa taarifa ya maendeleo ya matibabu ya mbunge huyo na kusema sasa ameimarika na muda wowote atasafirishwa kwenda nje ya Afrika kwa ajili ya awamu ya tatu ya matibabu yake.
Mbowe alibainisha kwamba mpaka kufikia Oktoba 10, matibabu ya Lissu yalikuwa yamegharimu Sh413 milioni.
Alisema sasa Lissu anakula mwenyewe na ameondolewa mashine za oksijeni zilizokuwa zikimsaidia kupumua.
Picha na sauti ya Lissu zilisambaa kwenye mitandao ya kijamii kiasi cha kuvutia watu kuziweka kwenye kurasa zao. Wanasiasa nao waliandika kwenye kurasa zao za mitandao ya Twitter na Facebook.
Mbunge wa Mtama, Nape Nnauye aliandika kwenye ukurasa wake wa Twitter: “Mjomba tunashukuru kwa tabasamu hili la matumaini! Nakuombea afya iimarike kabla hujasema mengi. Tulia mjomba upone kabisa kwanza.”
Mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto Kabwe aliandika waraka mrefu akifurahishwa na maendeleo ya afya ya Lissu. “Jana (Jumatano) nimefarijika kukusikia tena sauti yako tangu nikusikie nilipokuja kukusabahi hospitalini.”
“Sauti yako sasa imeboreka na kurudi sauti ileile uliyokuwa nayo kabla hujashambuliwa kwa risasi nyumbani kwako Dodoma. Watanzania wamefarijika sana kuwa bado uko hai na utaweza kuungana nasi tena kuendeleza mapambano ya kujenga demokrasia yetu.”
Si hao tu bali mbunge wa Chalinze, Ridhiwani Kikwete naye aliandika kwenye ukurasa wake wa Instagram: “Mungu hutenda wema siku zote. Ashukuriwe yeye kwa kazi ya kurejesha tabasamu katika sura yako na afya kwa wanaokuuguza.”
“Nimefurahi kukuona tena msomi, kiongozi wangu na mwanakamati mwenzangu wa Bunge ukitabasamu na mwenye afya njema. Mungu akulinde na akusimamie katika matibabu yako. Looking forward to see you back into your good shape (nataraji kukuona ukirudi tena ukiwa na siha njema).”
Mbali na wanasiasa hao, wananchi wa kawaida pia waliweka picha tofauti tofauti za Lissu alizopigwa akiwa kwenye kiti cha magurudumu na nyingine akiwa kitandani katika Hospitali ya Nairobi.
Mkazi wa Mwanza, Anthony Kasota aliandika katika ukurasa wake wa Facebook akiambatanisha na picha ya Lissu: “Hero, welcome back. Quick recovery (shujaa, karibu tena. Pona haraka).”
Akizungumzia suala la Lissu kuwa gumzo hasa wiki hii, katibu mkuu wa Chama cha Kijamii (CCK), Renatus Muabhi alisema linatokana na ushujaa wake na mazingira ya tukio lenyewe la kupigwa risasi.
Muabhi alisema watu wameungana kumwombea kwa sababu wanatambua kwamba kila binadamu ana haki ya kuishi lakini zaidi ni kutokana na ujasiri wake wa kupaza sauti kwa niaba ya wengi ambao hawawezi kusema.
“Uwepo wa uhai wake ni muujiza, kila mtu lazima aguswe. Mbowe alieleza kwamba haijawahi kutokea mgonjwa aliyeongezewa damu nyingi katika hospitali anayotibiwa katika kipindi cha miaka 20,” alisema Muabhi.
Mwanasiasa huyo aliongeza kuwa wapo watu wachache aina ya Lissu duniani na thamani zao huwa ni kubwa.
Muabhi alisema Lissu alijitoa muhanga kuikosoa Serikali waziwazi katika mambo mbalimbali.
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Mzumbe, Gideon Masika alisema sauti ya Lissu iliyosambazwa iliongeza matumaini mengi kwa wananchi kwa sababu kuambiwa tu anaendelea vizuri haitoshi mpaka waonyeshwe anaendeleaje.
Masika alisema tukio la mwanasiasa huyo kupigwa risasi na kunusurika kifo lilikuwa la kustaajabisha ndiyo maana kila mtu ana shauku ya kujua maendeleo yake.
Aliongeza kuwa Lissu anapata huruma ya umma kwa sababu alishajipambanua kama shujaa asiyeogopa.
“Nadhani akipona atakuwa na ushuhuda mkubwa wa kuieleza jamii, halikuwa tukio la kawaida. Matumaini ya Watanzania yanarejea baada ya kusikia sauti ya Mtanzania mwenzao na kuona anapata nafuu,” alisema mwanazuoni huyo.
Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Askofu Frederick Shoo akizungumza na Mwananchi juzi alisema alibubujikwa machozi baada ya kuisikia sauti hiyo ya mwanasheria wa Chadema.
“Nilijikuta natoka machozi niliposikia sauti ya Lissu,” alisema Dk Shoo, ambaye pia ni Askofu wa Dayosisi ya Kaskazini.
Dk Shoo alisema kupona kwa Lissu ni onyo kwa waliohusika katika tukio hilo.

Pacha walioungana wanavyoishi chuo kikuu wakipigania ndoto zao


Tofauti na wanafunzi wengine, Maria na Consolata Mwakikuti wanaishi kwenye nyumba mpya ya vyumba vinne ikiwa na sebule, jiko, chumba cha kulala chenye choo na kingine cha msaidizi wao.
Kwa ufadhili wa Serikali, Chuo Kikuu cha Ruaha (Rucu) kimeweka mazingira rafiki ya kujifunzia kwa mapacha hao walioungana ambao wamelazimika kuwahi kuwasili chuoni hapo ili waanze masomo ya kompyuta kabla ya kuungana na wenzao ambao bado wapo likizo.
Kabla ya wanafunzi hao kujiunga na chuo kikuu hicho, uongozi ulilazimika kuchukua hatua za haraka kuweka mambo sawa ili kuhakikisha mabinti hao wanafurahia safari yao ya kuwa walimu wenye shahada.
Makamu mkuu wa chuo hicho, fedha na utawala, Padri Kelvin Haule anasema walianza maandalizi ya nyumba watakayoishi kwa kipindi chote cha masomo yao na kuandaa mazingira na mahitaji yote muhimu kwa ajili yao.
“Fahari yetu ni kuona wanafurahi, tunapenda kuona wanatimiza ndoto zao,” alisema Padri Haule na kufafanua:
“Tulianza kuandaa sebule. Hapa ndipo wanaposomea, kupokea wageni na kuna TV kwa ajili ya kupata habari mbalimbali. Sebule hiyo pia wanaitumia kwa ajili ya kusali.” Sebuleni kuna kochi kubwa kidogo lililotengenezwa maalumu kuwawezesha kukaa bila wasiwasi.
Chumbani kwao kuna kitanda kifupi na kipana. Kimetandikwa vizuri kana kwamba hakijawahi kulaliwa na mtu yeyote. Chumba hicho kina nafasi ya kutosha na kila kitu kimewekwa katika mpangilio mzuri.
Choo wanachotumia pacha hao kilijengwa ‘kimahesabu’ tofauti na vingine. Chao ni kifupi ili waweze kupanda na kukaa kwa urahisi. Mabomba ya maji na soketi za umeme pia vipo chini tofauti na ilivyozoeleka ili kuwarahisishia kuvitumia kutokana na maumbile yao.
“Wakitaka kuwasha au kuzima taa hawahitaji msaada wa mtu mwingine kwa kuwa miundombinu inawawezesha,” anasema.
Pamoja na maboresho hayo ya mazingira, hawakukuta kila kitu chuoni hapo, walihama na baadhi ya vifaa vya ndani kutoka Kilolo walikoishi na kusoma kuanzia kidato cha kwanza hadi cha sita.
Japokuwa ni muda mfupi umepita tangu wawasili chuoni hapo kuanza masomo yao ya elimu ya juu, pacha hao wana furaha na tabasamu la upendo wakati wote, hivyo kuwa rafiki wa kila mmoja.
Ukibahatika kupata nafasi ya kukaa na kuzungumza nao, hakika hutapenda kumaliza haraka. Kadri unavyozungumza nao ndivyo ungependa kuendelea. Ukarimu, ucheshi uliochanganyika na upole, hekima na upendo ni sifa za pekee zinazowafanya wapendwe zaidi.
Baada ya kuishangaza dunia walipofaulu kidato cha sita kutoka Sekondari ya Udzungwa iliyopo wilayani Kilolo, pacha hao wanaendelea kuthibitisha kuwa ulemavu si kukosa uwezo.
Maria na Consolata sasa ni wanafunzi wa chuo kikuu wakiishi kwenye nyumba maalumu iliyoandaliwa kwa ajili yao ndani ya chuo hicho.
Mwaka 2010 baada ya kuhitimu darasa la saba waliwahi kusema ndoto yao ni kufika chuo kikuu na sasa imetimia wakitarajia kuanza masomo ya shahada ya kwanza ya ualimu muhula mpya wa masomochuoni hapo utakapoanza hivi karibuni.
Consolata anasema haikuwa rahisi kwao kufika hapo na kwamba hilo limewezekana kwa neema za Mungu. “Tunafurahia maisha mapya, tunamshukuru Mungu kwa hatua hii hakika ni kwa neema tu wala si nguvu na uwezo wetu,” anasema.
Maria na Consolata wana malengo na wanajua wanachopenda kufanya baada ya kuhitimu masomo yao. “Tunapenda kuwa walimu wa Kingereza na Kiswahili,” wanasema.
Kufanikiwa kujiunga chuo kikuu kumewapa ari mpya na sasa wanafikiria kuendelea zaidi mpaka wapate shahada ya uzamivu (PhD).
Mshikamano
Unapozungumza nao unagundua ama mmoja wao huanza halafu mwingine hudakia baadaye au wanaanza na kumaliza sentensi pamoja.
Pacha hao huzungumza pamoja na hawawezi kuongea sentensi mbili au tatu bila kutamka baadhi ya maneno kwa pamoja.
‘Tunamshukuru Mungu’ ni neno lililotawala vinywa vyao. Kwao, Mungu ni wa kwanza. Wanaamini mafanikio yao ni kwa neema za Mungu na si kwa akili zao.
Mvuto wa Maria na Consolata ndani na nje ya nchi hautokani na kuungana kwao pekee, bali uwezo wa kitaaluma waliouonyesha katika shule walizosoma.
Siku chache kabla ya wenzao kufika chuoni hapo kuanza muhula mwingine, wao wamewahi ili wapate fursa ya kujifunza masomo ya kompyuta kwa miezi miwili kwa ajili ya kuendana na mahitaji ya ngazi waliyopo.
Padri Haule anasema wamefurahi kupata heshima kwa Maria na Consolata kuwa miongoni mwa wanafunzi wao. “Tunawapenda, tangu wafike wanaendelea vizuri,” anasema.
Mwandishi chuoni
Nilipowasili chuoni hapo, saa mbili asubuhi, ofisa habari wa Rucu, Mwadharau Matola alinipeleka kwenye nyumba wanayoishi mapacha hao tulikowakuta wameketi kwenye kochi wamejipumzisha baada ya kupata kifungua kinywa.
“Oooh dada Tuma, karibu sana,” walinikaribisha kwa furaha.
Kwa sababu safari yangu ilikuwa ya kikazi, walitaka kujiridhisha kama uongozi wa chuo una taarifa za ujio wangu.
“Father Kelvin anajua umekuja? Walimu wetu je? Father Mgimwa naye anajua?” waliniuliza kwa awamu. Mwadharau aliwaeleza chuo kimetoa baraka za kuongea nao. Tulianza mazungumzo.
Wanavyoishi
Siku walipowasili chuoni hapo, shughuli zilisimama kwa muda kwa kuwa kila mtu alikuwa na shauku ya kuwaona na kujua chochote kuhusu maisha yao.
Jambo la kufurahisha ni kuwa kila mmoja kwenye chuo hicho yupo tayari kuona mapacha hao wanatimiza ndoto zao. “Tulikusanyika kuwasubiri nje ya jengo la utawala na walipowasili tuliwapokea kwa shangwe kubwa,” anasema Padri Haule.
“Tulijiweka sawa kuona ni wenzetu tukistaajabia uumbaji wa Mungu.”
Kabla ya kuwasili kwao, chuo kilifanya maandalizi ya msingi. Padri Haule anasema taarifa za mapacha hao kuchaguliwa kujiunga chuoni hapo ziliwalazimu kujipanga jinsi ya kuwafanya wawe na maisha ya amani na furaha, hivyo walifunga safari kwenda Kilolo katika shule waliyoishi kabla ya kumaliza kidato cha sita ili kujifunza namna nzuri ya kuwalea.
“Kwa hiyo tulikwenda kujifunza ili nasi tunapowapokea tuhakikishe tuna miundombinu wezeshi kwao, wasione tofauti kubwa,” anasema.
Anasema walichozingatia zaidi ni muundo wa chumba cha kulala, bafu, sebule na choo pamoja na maisha yao ya kila siku. Walihakikisha wanajua wanachohitaji tangu wanapoamka hadi muda wa kulala.
Padri Haule anasema baada ya kupata ripoti ya mahitaji yao ya msingi walianza kuandaa mazingira kabla ya kuwapokea.
Anasema ili kufanikisha masomo yao chuoni hapo, Maria na Consolata wameandaliwa mhudumu wa nyumbani, muuguzi pamoja na dereva ambao wanalipwa na Serikali ili kuhakikisha wanahudumiwa kwa kila wanachohitaji.
RC, mhudumu wanavyozungumzia
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Halima Masenza anasema kuna fungu limetengwa kwa ajili ya Maria na Consolata na chuo kimefungua akaunti maalumu kwa ajili yao. “Wapo chini ya uangalizi wetu baada ya kuwapokea kutoka kwa masista, Serikali ndiyo iliyosimamia kuhakikisha wanapata mahitaji yote ya msingi. Chuo kina jukumu la usalama wao,” anasema.
Mhudumu anayewasaidia kazi mbalimbali nyumbani ikiwamo kuwapeleka darasani, Nuru Mfikwa anasema furaha yake imeongezeka tangu alipoanza kuwalea pacha hao. Baada ya vipindi vya darasani, marafiki zao au walimu huwa wanawasindikiza hadi nyumbani. “Najisikia mwenye furaha, nawapenda Maria na Consolata na nitajitahidi kuwahudumia kwa bidii,” anasema Nuru.
Kwenda, kutoka darasani
Katika kipindi hiki, wanachuo hao wapya hawaamki alfajiri sana, isipokuwa huamka saa moja, na kati ya saa tano hadi saba wanaingia darasani.
Wakiamka, huanza kwa kumshukuru Mungu kisha hutandika kitanda na kusafisha chumba chao.
Kwa siku moja niliyoshinda nao nilishuhudia wakichukua kompyuta yao kisha kupanda baiskeli na Nuru kuisukuma kuelekea darasani ambako kulikuwa na wahadhiri wawili; Robert Manase na Anthony Challu waliowapokea na kuwasaidia kukaa kwenye kiti chao ambacho pia ni maalumu.
Kiti hicho wanakitumika tangu wakiwa sekondari kwa kuwa watawa wa shirika la Maria Consolata waliokuwa wakiwalea awali waliwafungashia vifaa vyao muhimu walipokuwa wakijiandaa kujiunga na chuo hicho.
Katika kipindi cha takriban saa mbili, mwalimu Manase aliwafundishwa namna ya kutengeneza kadi kwa kutumia programu ya microsoft publisher. Kwa saa moja aliwaelekeza kabla hajawapa kadi ya harusi waitengeneze kama ilivyo.
Pia kwa muda mfupi waliitengeneza kadi hiyo na kuitoa kama ilivyokuwa. “Uwezo wao darasani ni mkubwa sana, ni wepesi wa kuelewa,” anasema Robert.
“Tumewatengenezea mouse mbili ingawa wanatumia kompyuta moja.”
Hata hivyo, wanayo kompyuta mpakato (laptop) wanayoitumia wakiwa nyumbani kwa vile hivi sasa wana kipindi kimoja kwa siku na hupewa kazi kwa ajili ya kuzifanya wakiwa kwenye makazi yao.
Kipindi kinapoisha, wanafunzi wenzao huwasaidia kupanda baiskeli na kuwasukuma kurejea kwao huku njiani wakipiga soga za hapa na pale. Wanafunzi chuoni hapo wanasema ni furaha kwao kuwa na Maria na Consolata.
Mmoja wa wanafunzi, Harrison Damas anasema ucheshi wa pacha hao umewafanya wawe marafiki wa kila mmoja wanayekutana naye.
“Ni wakarimu na wameifundisha jamii kwamba, unapowapa nafasi watu wenye ulemavu wanaweza kufanya maajabu ya kushangaza,” anasema.
Ingawa wanaye msaidizi ambaye huhakikisha mambo yako sawa, wakati mwingine wakifika kwenye nyumba yaohupenda kujishughulisha kwa kuandaa chakula cha mchana kisha kupumzika kidogo.
Kwenye ratiba yao ya kila siku upo muda ambao huutumia kusaidia kufanya kazi za nyumbani.
Padri Haule anasema awali hawakuwaandalia jiko wakijua watakuwa wanaandaliwa chakula na msaidizi wao.
Cha ajabu, anasema walipofika walitaka kuingia jikoni kupika. “Tulishangaa, ikabidi tuwaandalie jiko la gesi. Lakini ikashindikana kwa sababu gesi si nzuri kwao kutokana na harufu, waliomba jiko la mkaa,” anasema Padri Haule.
Kwa kawaida hawapendi kubweteka. Wanapenda kufanya kazi zote wanazoweza. “Tunaweza kufanya kazi zote isipokuwa kuanika nguo tu,” anasema Maria.
Wakiwa na muda huwa wanaondoka kwenda kutembea nje ya chuo hicho ili kubadilisha na kujifunza mazingira ya mji wa Iringa. Mara nyingi, kama eneo wanalokwenda wanaweza kufika, hufanya hivyo kwa kutumia baiskeli yao ingawa wanalo gari kwa ajili ya kuwapeleka popote wanapotaka. “Tumeshawahi kwenda sokoni na kurudi. Na tunaweza kwenda popote pale,” anasema Maria.
Padri Haule anasema awali alikuwa na wasiwasi, lakini kwa sababu pacha hao wapo simple na wasimamizi wao wanawalinda, huwaacha watembelee hasa maeneo yaliyopo jirani.
Serikali kutowakopesha
Ofisa elimu wa Mkoa wa Iringa, Majuto Nyaga anasema Serikali imetenga fungu maalumu kwa ajili yao ili pacha hao wasome bure. Anasema wameshawasiliana na Wizara ya Elimu pamoja na Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu (HESLB) kuhakikisha hawakopeshwi katika gharama za masomo yao.
“Hata wasaidizi akiwamo dereva na muuguzi watakaowahudumia kwa kipindi chote Serikali itagharamia,” anasema.
Anasema mkoa umegharamia mahitaji yote ya awali mpaka sasa huku wakisubiri hatua nyingine kutoka wizarani.
Hata hivyo, Mwadharau anasema Maria na Consolata wamejiunga na chuo hicho kikiwa na kitengo cha elimu maalumu. “Tunacho kitengo kwa ajili ya wenye mahitaji maalumu,” anasema.
Padri Haule anasema awali walipata shida kuhusu miundombinu ya madarasa walipowasili lakini tayari suluhisho limepatikana na mkakati wa chuo ni kuwa na mazingira rafiki zaidi kwa makundi yote. “Kwa hiyo mazingira yaliyopo wanaweza kuja kwa baiskeli yao kutoka nyumbani hadi darasani bila wasiwasi,” anasema.
Walivyomkosha RC
Maria na Consolata wanatoa somo kuhusu watu wenye ulemavu nchini.
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Masenza anasema wameonyesha kuwa inawezekana. “Licha ya kwamba ni walemavu wanaonyesha bidii, maana yake ni kwamba jamii isiwafungie watu wa aina hii ndani. Wawatoe na kuwapeleka shule wanaweza kufanya maajabu kama Maria na Consolata,” anasema.
Njia wanazopita kwenda kanisani
Chuo kinajua pacha hao wanapenda kuabudu, hivyo kimewaandalia mazingira yatakayowawezesha kwenda na kurudi kanisani.
“Kanisa lipo hapa chuoni lakini awali njia zilikuwa na ngazi ili kulifikia, kwa hiyo walikuwa wanapata shida, tukaamua kuandaa mazingira rafiki ili wakati wa ibada waende bila wasiwasi,” anasema Padri Haule.
Anasema waliandaa njia mbadala za wao kupita waendapo na kurudi kutoka kanisani bila wasiwasi. “Wanapita geti la kutokea chuo, wanaenda hadi ilipo benki ya NMB kisha wananyoosha hadi kwenye ATM ya CRDB, hapo tumejenga daraja dogo ambalo wanavuka na kuingia mlango utakaowapeleka moja kwa moja kanisani,” anasema.
Maria na Consolata wanaamini kusali ndiko kulikowafanya wafikie ndoto ya maisha yao.
Ni wajasiriamali
Maria na Consolata wanajua kutumia fursa. Pia wanaamini bidii pekee ndiyo inayoweza kuwafanikisha kwenye maisha yao. Wanafanya biashara ya vitenge na ukienda kuwatembelea watakuonyesha bidhaa zao ili uwaungishe.
“Tulikuwa na mtaji mdogo ila sasa umefika zaidi ya laki moja,” anasema Maria. Wanasema biashara hiyo haitawafanya washindwe kutimiza ndoto yao.
Mkuu wa Wilaya ya Iringa, Richard Kasesela anasema mapacha hao ni funzo kwa Watanzania wasiopenda kufanya kazi. “Nitawasaidia kwenye hii biashara yao kwa sababu wanaonyesha moyo wa kujituma licha ya uhakika wa Serikali na chuo kufanikisha kila kitu,” anasema.
Siyo vitenge tu, pacha hao wanapenda kufuma vitambaa huku mmoja akitumia mkono wa kushoto na mwingine wa kulia, wanaweza kushona vitambaa vizuri wanavyoviuza.

Msigwa aeleza anavyosuka mpango wa kumuondoa Spika


Mbunge wa Iringa Mjini (Chadema), Mchungaji Peter Msigwa ameelezea jinsi anavyosuka mpango wa kumng’oa Spika wa Bunge, Job Ndugai.
Msigwa ametangaza nia yake ya kupeleka hoja ya kumuondoa Spika Ndugai katika mkutano unaotarajiwa kuanza Novemba 7.
Msigwa ametangaza nia yake hiyo kupitia ukurasa wake wa Twitter akisema amezingatia kanuni ya 137 ya Kanuni za Kudumu za Bunge.
“Ninakusudia kupeleka hoja ya kumuondoa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano Tanzania Mhe. Job Ndungai, kwa kuzingatia Kanuni ya 137 ya Kanuni za Kudumu za Bunge ina complement Ibara ya 84 (7) (d) ya Katiba,” ameandika Msigwa katika ukurasa wake wa Twitter.
Akizungumza kwa simu na Mwananchi jana, Msigwa ambaye ni miongoni mwa wabunge wanaomlalamikia Ndugai wakidai anaendesha Bunge kwa shinikizo na upendeleo, alisema Spika huyo ameshindwa kuiongoza Tume ya Bunge na Bunge kwa ujumla. “Yeye ni kamishna wa Bunge amekuwa akipokea maelekezo kutoka kwenye mhimili wa utawala ili kuliongoza Bunge. Tume ya Bunge haiendeshwi ipasavyo,” alisema Msigwa.
Msigwa alimkosoa Spika Ndugai akidai amekuwa dhaifu kuliko maspika wote waliomtangulia na kwamba katika kipindi chake Bunge limekuwa dhaifu mbele ya Serikali.
Alipoulizwa kama ataungwa mkono katika hoja yake, Msigwa alisema hiyo haijalishi ilimradi tu hoja zake ni za msingi na ni za ukweli.
“Kupata support hilo ni jambo jingine, tutajenga daraja tutakapofika kwenye mto. Kitu cha msingi ni hoja ninazoeleza ni za msingi,” alisema.
Alipotafutwa kwa njia ya simu, Ndugai hakupokea licha ya simu yake kuita kwa muda mrefu. Hata hivyo aliwahi kujibu shutuma hizo siku za nyuma kupitia gazeti hili akisema Bunge linaongozwa na Tume ambamo Msigwa naye ni kamishna.
“Kitendo ambacho yeye anataka kuonyesha kuwa kiongozi mmojawapo ana upungufu, sioni kwa nini na yeye asiwe nao upungufu. Hilo ndilo jibu langu,” alisema Ndugai na kuongeza:
“Decision making yoyote za juu kuliko zote zinafanywa na tume na huyo ni mjumbe. Hapaswi kuwa mlalamikaji kama watu wengine.”
Kanuni za kumtoa Spika
Sehemu ya kwanza ya kifungu anachosimamia Msigwa kipo katika sehemu ya nne ya Kanuni za Bunge inayohusu kumuondoa Spika au naibu wake madarakani na kinasomeka:
“(1) Mbunge yeyote anayetaka kuwasilisha hoja ya kumuondoa Spika madarakani chini ya Ibara ya 84(7)(d) ya Katiba atawasilisha taarifa ya maandishi ya kusudio hilo kwa katibu (wa Bunge) akieleza sababu kamili ya kutaka kuleta hoja hiyo.”
Sehemu ya pili ya kifunmgu hicho inasema mara tu baada ya kupokea taarifa ya maandishi ya kusudio la kumuondoa Spika kwenye madaraka, katibu ataipeleka taarifa hiyo kwenye Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge kwa ajili ya kuijadili.
Inaendelea kusema, endapo Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge itaridhika kuwa zipo tuhuma mahsusi dhidi ya Spika zinazohusu uvunjaji wa masharti ya Ibara ya 84(7)(a), (b), (e), (f), (g) na (h) ya Katiba, Sheria au Kanuni zinazoongoza shughuli za Bunge, basi kamati hiyo itaidhinisha kuwa hoja hiyo ipelekwe Bungeni ili iamuliwe.
Kifungu hicho kinaendelea kufafanua kuwa, naibu Spika atakalia kiti cha Spika wakati wa kujadili hoja ya kutaka kumuondoa Spika madarakani na Spika atakuwa na haki ya kujitetea wakati wa mjadala.

Nkamia amfagilia JPM majadiliano na Barrick Gold


Mbunge wa Chemba (CCM), Juma Nkamia amesema Serikali inastahili pongezi kwa majadiliano yake na kampuni ya Barrick Gold yanayohusu uwekezaji kwenye madini.
Alhamisi iliyopita, Rais John Magufuli alipokea ripoti ya mazungumzo kati ya Serikali na kampuni mama ya Acacia, Barrick Gold iliyoeleza makubaliano yaliyoafikiwa ili kuendelea na uchimbaji wa dhahabu nchini, ikiwamo kulipa Dola 300 milioni za Marekani (zaidi ya Sh660 bilioni).
Lakini siku moja baada ya taarifa hiyo, ofisa mwandamizi wa fedha wa Acacia, Andrew Wray alisema kampuni hiyo haina uwezo wa kulipa kiasi hicho.
Kwa mujibu wa taarifa zilizoripotiwa na vyombo tofauti vya habari vya kimataifa, uongozi wa Acacia umesema hauna uwezo wa kulipa kiasi hicho cha fedha.
“Hatuna huo uwezo kuilipa Tanzania ili tumalizane kwenye mgogoro wa kodi uliopo,” alikaririwa ofisa mkuu wa fedha wa kampuni hiyo, Wray.
Pamoja na changamoto zilizopo, Nkamia alisema hatua hiyo bila kujali tofauti ya itikadi kutokana na vyama vilivyopo, Watanzania wanapaswa kumpongeza Rais Magufuli.
“Serikali imefanya kazi nzuri. Hata kama humpendi mtu, mpongeze akifanya vizuri,” alisema Nkamia.
Miongoni mwa makubaliano ya Serikali na Barrick Gold ni kwamba sasa pande hizo mbili zitakuwa zikigawana faida asilimia 50 kwa 50.

MGANGA MBARONI KWA KUNAJISI WATOTO 14

JESHI la Polisi mkoani Singida linamshikilia mganga wa kienyeji mkazi wa mtaa wa Minga, Daud Idd (74), kwa tuhuma ya kunajisi watoto 14 wenye umri kati ya miaka saba na 12 na kuwasababishia maumivu makali katika sehemu zao za siri.
Mgonga huyo maarufu kama Babu Karatu ameelezwa kuwa alikuwa akishirikiana kutenda vitendo hivyo na mtoto wa mdogo wake aitwaye Abdallah Yahaya (31).
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake leo Jumamosi, kaimu kamanda wa polisi mkoani hapa Isaya Mbughi amesema mtuhumiwa anadaiwa kutenda makosa hayo kwa nyakati tofauti kati ya Desemba mwaka jana, hadi Oktoba mwaka huu.
Amesema kuwa mwathirika mmoja mwenye umri wa miaka saba siku ya Oktoba 16 mwaka huu saa 11.45 jioni wakati akiogeshwa na mama yake alilalamika kuwa anasikia maumivu makali katika sehemu yake ya siri.
Amesema baada ya binti kuyo kulalamika kwa mama yake mama huyo aliweza kumchunguza kwenye sehemu zake za siri na kubaini kuwa michubuko inayotokana na kuingiliwa kimwili.
“Mama huyo baada ya kuona michubuko hiyo kwenye sehemu za siri za binti yake alimhoji mtoto wake na mtoto huyo aliweza kumtaja mganga wa kienyeji Karatu. Mwaathirika huyo alienda mbele zaidi na kumweleza mama yake kuwa si yeye pekee hufanyiwa vitendo hivyo, bali wapo watoto wengi wamefanyiwa.”
Kaimu kamanda huyo amesema baada ya hapo mama huyo alitoa taarifa kwa mwenyekiti wa mtaa wa Minga na kisha yeye na mwenyekiti wa mtaa waliweza kuongozana hadi kituo cha kati cha polisi mjini hapa.
“Jeshi la polisi liliweza kuwakamata watuhumiwa hao ambao wanaishi katika nyumba moja, kwa tuhuma ya ubakaji. Uchunguzi wa awali umebaini kuwa watoto waliofanyiwa unyama huo wanasoma katika Shule za Msingi Singidani, Nyerere na Mughanga,” amesema.
Mbughi amesema mbinu iliyokuwa inatumika kuwanasa watoto hao wa ni kuwarubuni na kisha kuwaonyesha video/movie, kwenye kompyuta mpakato.
“Wakati watoto hao wa kike wakiendelea kuangalia video sebuleni, mtuhumiwa huyo alikuwa akichomoa mmoja na kuingia naye chumbani na kumwingilia kimwili. Wachache alikuwa akiwachezea sehemu zao za siri. Baada kuingiliwa kimwili watoto hao walikuwa wakipewa zawadi ya shilingi mia mbili au shilingi 2,000,” amesema.

SOMA VICHWA VYA HABARI KATIKA MMAGAZETI YA LEO OKTOBA 22,2017