Thursday, September 5

Rais Kikwete na Paul Kagame wakutanishwa na Rais wa Uganda

Rais wa Uganda, Yoweri Museveni ameitisha mkutano wa dharura wa marais wa nchi za Maziwa Makuu (ICGLR), kujadili hali ya usalama Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. 

Rais Jakaya Kikwete ni miongoni mwa waalikwa kwenye mkutano huo ambao pia unatarajiwa kuhudhuriwa na Rais wa Rwanda, Paul Kagame.
 

Wakati hali ya usalama Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ikidhoofika, katika siku za karibuni, uhusiano wa Tanzania na Rwanda umekuwa wa shaka hasa baada ya Rais Kikwete kuishauri Serikali ya Rwanda kukaa na wapinzani ili kumaliza mzozo uliolikumba eneo la Maziwa Makuu.
 

Rais Kikwete alitoa ushauri huo wakati akiwa katika sherehe za maadhimisho ya miaka 50 ya Umoja wa Afrika (AU), zilizofanyika mjini Addis Ababa, Ethiopia. Mkutano wa leo utafanyika kwenye Ukumbi wa Commonwealth Resort, Munyonyo katikati ya Jiji la Kampala.
 

Kwa mujibu wa taarifa Rais Museveni ameitisha mkutano huo hasa kuzungumzia hatua ya Umoja wa Mataifa kupambana na Kundi la Waasi wa M23.
 

Mbali na viongozi hao wa Tanzania na Rwanda, viongozi wengine wanaotarajiwa kuhudhuria mkutano huo wanatoka Angola, Burundi, Jamhuri ya Afrika ya Kati, Jamhuri ya Kongo, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Kenya, Sudan, na Zambia.

Kesi ya waziri mkuu Mizengo Pinda kutajwa septemba 16 mwaka huu...DPP adai kuwa hiyo ni kesi FEKI

KESI ya kikatiba iliyofunguliwa dhidi ya Waziri Mkuu Mizengo Pinda kutokana na kauli yake ya kuruhusu wanaokaidi maagizo ya Dola wapigwe, itatajwa Septemba 16 mwaka huu katika Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam.

Kesi hiyo ilifunguliwa Agosti mosi mwaka huu na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), dhidi ya Waziri Pinda na Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), wakipinga kauli hiyo iliyotolewa bungeni.

Itasikilizwa na jopo la majaji watatu wa Mahakama Kuu, likiongozwa na Jaji Kiongozi Fakhi Jundu wengine ni Jaji Augustine Mwarija na Dk Fauz Twaib.

Inadaiwa Mei 20 mwaka huu, Pinda akiwa bungeni katika nafasi yake ya Waziri Mkuu, kinyume na Katiba ya Nchi alitoa kauli ya kuruhusu askari wa Jeshi la Polisi kuwapiga raia ambao hawatatii amri yao kunapokuwa na vurugu.

“Sasa kama wewe umekaidi, hutaki, unaona kwamba ni imara zaidi, wewe ndio jeuri zaidi watakupiga tuu na mimi nasema muwapige tu kwa sababu hakuna namna nyingine, eeh maana tumechoka sasa,” sehemu ya hati ya mashitaka iliyonukuu kauli ya Waziri Pinda.

Katika hati hiyo inadaiwa kwa mujibu wa utekelezaji wa Sheria za Jinai, kauli inayotolewa na kiongozi wa nafasi ya Waziri Mkuu, inaonekana kama amri inayopaswa kutekelezwa na vyombo vya Dola kama Polisi, hivyo itachukuliwa kama amri halali na kusababisha waendelee kuwatesa na kuwapiga wananchi wasio na hatia.

Aidha inadaiwa Pinda alivunja ibara ya 100 ya Katiba inayompa kinga mbunge anapotoa jambo lolote bungeni, kwa kuwa yeye hakuzungumza bungeni kama mbunge, bali alikuwa anatoa msimamo wa Serikali yake.

Akizungumza hivi karibuni, Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) alisema hakuna uhalali wa mashitaka hayo kwa sababu kauli ya Pinda kuwa pigeni haikuwa piga ua, alichosema ni kupiga wale wasiotaka kutekeleza amri halali na kuna sheria inayoruhusu wananchi kupigwa pindi wanapokaidi amri.

Katiba moto, Chadema, CUF watoka nje

Dodoma.Wabunge wa Kambi ya Upinzani Bungeni jana jioni walitoka ndani ya Ukumbi wa Bunge, baada ya kupuuzwa kwa mwongozo wao wa kutaka kuahirishwa kujadiliwa kwa Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, hadi hapo Zanzibar itakaposhirikishwa.
Wabunge waliotoka bungeni jana yapata saa 12.15 ni kutoka vyama vya Chadema, CUF na NCCR- Mageuzi huku Mbunge wa Vunjo na Mwenyekiti wa Taifa wa Tanzania Labour Party (TLP, Augustine Mrema akiendelea kubaki ukumbini.
Kitendo cha wabunge hao wa upinzani kilionekana kuwakera baadhi ya wabunge wa CCM, ambao walisikika wakiwakejeli kwa kupiga meza huku wakisema: “Kwendeni zenu, tumewazoea.”
Wakati wabunge hao wakiondoka, Naibu Spika wa Bunge, Job Ndugai, alikuwa akiwasisitiza wabunge wanaobakia wawe watulivu, maana kuna usalama wa kutosha ndani ya ukumbi huo.
“Mnaotoka nimewaona wote na mnanijua,” alisikika Naibu Spika Ndugai akiwatahadharisha wabunge wa upinzani waliosusa mjadala huo.
Wabunge wa CCM waliendeleza vituko ambapo baada ya wapinzani kutoka, wabunge Juma Nkamia (Kondoa Kusini), Hilary Aeshi ( Sumbawanga Mjini) na Murtaza Mangungu (Kilwa Kaskazini) walikwenda kukaa katika viti vya kambi ya upinzani.
Kabla ya kutoka kwa wabunge hao wabunge wawili kutoka CUF waliomba mwongozo wa Spika, wakitaka muswada huo kuondolewa ili kuwapa nafasi Wanzanzibar kutoa maoni yao.
Mbunge wa Mkanyageni, Habib Mohamed Mnyaa (CUF) aliomba mwongozo akitaka muswada huo uondolewe, hadi hapo Wazanzibar watakaposikilizwa.
Alisema kuwa kwa maoni ya Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala wamesikiliza maoni ya wadau wengi, lakini Zanzibar hawakwenda kuwasikiliza wadau wa eneo hilo.
“Na hili suala zima katika masuala ya katiba linahitaji usawa wa washirika, tunazungumza kitu kinachohusiana na Zanzibar na Tanzania Bara, ili kupata maoni ya nchi nzima kuna uhalali gani wa Bunge hili kuendelea na mjadala huu?” alihoji.
Hata hivyo, alikatizwa na kelele za Mbunge wa Viti Maalumu, Pindi Chana (CCM), ambaye alitoa taarifa kuwa Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala ilialika wajumbe mbalimbali ikiwamo Zanzibar.
“Miongoni wa wajumbe walioalikwa ni pamoja na Mkurugenzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi ya Zanzibar pamoja na wadau mbalimbali ambao walikuja mbele ya Katiba,” alisema Pindi ambaye pia ni Mwenyekiti wa kamati hiyo.
Mbunge wa Konde, Khatibu Said Alli (CUF), alitaka mwongozo wa Spika kuhusiana na ujumbe mfupi wa maneno ambao aliupokea ukimtisha, kutokana na kitendo chao cha kumuunga mkono Msemaji wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Tundu Lissu.
“Unashabikia mambo ya Tundu Lissu leo, endelea ila mtashughulikiwa,” aliunukuu ujumbe huo na kuongeza kuwa hafahamu umetoka kwa mbunge gani ila wahudumu wa Bunge ndio waliompelekea.
Akijibu mwongozo huo, Ndugai alisema kuwa ni miongoni mwa mambo ambayo anayachukua na kuyafanyia kazi ni suala hilo. Pia Ndugai aliomba ujumbe huo apelekewe.
“Hii ni demokrasia mara nyingi imeshatolewa miongozo, jibu linatolewa hapo hapo ama baadaye na kwa hoja zilizotolewa inakilazimu kiti kupata ushauri hapo baadaye,” alisema Ndugai.
Hata hivyo, baada ya Ndugai kutoa majibu hayo, wabunge wa upinzani waliamua kutoka ndani ya ukumbi huo.
Baada ya wabunge hao kutoka Naibu Spika Ndugai aliendelea na ratiba ya Bunge kwa kusema, jambo hilo halikupangwa kumalizika jana na kwamba litaendelea kujadiliwa hata ikibidi hadi keshokutwa.
Hata hivyo, Waziri wa Nchi katika Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi, alisimama kabla ya mjadala kuendelea na kutetea hoja kuwa makundi yote yalisikilizwa tofauti na inavyodaiwa na wapinzani.
“Hata katika marekebisho ya sheria mbili hizi, mimi na Mwanasheria Mkuu wa Serikali tumekutana na viongozi wengi na mawaziri na ndiyo maana tumeahirisha Muswada wa Sheria ya Kura ya Maoni,” alisema.
Alisema, yeye (Lukuvi) alikuwa Mwenyekiti wa ujumbe uliotumwa na Rais kuitisha makundi ya siasa ambayo yalijadili muswada huo. Lukuvi alisema kuwa, pande zote zimeshiriki kikamilifu katika kutoa maoni yao, “kama hizi ni sarakasi za kisiasa mimi sijui.”
Baada ya kutoka, wabunge wa vyama vya Chadema, CUF na NCCR-Mageuzi walifanya mkutano wa pamoja kwenye Ukumbi wa Pius Msekwa. Habari kutoka ndani ya kikao hicho zinaeleza kuwa, wabunge hao walikubaliana kufanya kila njia kuhakikisha wanazuia mjadala huo leo.
Pia wabunge wa CCM nao walikutana nao mara baada ya Ndugai kuahirisha kikao cha jioni.
Lissu achafua hali ya hewa
Hotuba ya Lissu ndiyo iliyochafua hali ya hewa baada ya kuituhumu Kamati ya Bunge ya Katiba, Sheria na Utawala kwa kutohoji watu wa Zanzibar wakati wakikusanya maoni kuhusu muswada huo.
Alisema licha ya kamati hiyo kukusanya maoni ya taasisi za kidini na za kiraia, taasisi za elimu ya juu na za kitaaluma, vyama vya siasa na asasi nyingine, lakini bado haikwenda Zanzibar kukusanya maoni ya watu wa huko.
“Wadau pekee walioshirikishwa kutoa maoni yao juu ya muswada huu ni Watanzania Bara tu. Wazanzibari hawakupatiwa fursa hiyo na hawakushirikishwa kabisa, licha ya sheria yenyewe kuwa na mambo mengi yanayoihusu Zanzibar,” alisema Lissu.
Pamoja na suala hilo, Lissu alitaka pia Rais wa Jamhuri ya Muungano aondolewe madaraka ya kuteua Wajumbe wa Bunge Maalumu wasiokuwa wabunge au wawakilishi kuwa inavuruga au kuondoa kabisa dhana ya uwakilishi wa wananchi na uhalali wa kisiasa katika mchakato wa Katiba Mpya.
Pia alipendekeza kuongezwa kwa idadi ya wajumbe ifikie 792, kwani Tanzania ina idadi ya watu milioni 45 kwa takwimu za Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2012.
Lissu pia alitaka wawakilishi wa Zanzibar waongezwe bungeni, kwa Zanzibar itakuwa na wajumbe 219 kwenye Bunge lenye wajumbe 604, sawa na takriban 36% ya wajumbe wote. Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inataka idadi iwe nusu kwa nusu kati ya pande mbili za Muungano.
Wajumbe 166
Kutakuwa na wajumbe 166 wasiotokana na Bunge na Baraza la Wawakilishi watateuliwa na Rais. Kutakuwa na Wabunge 357 na Wawakilishi 81 na kufanya Bunge Maalumu kuwa na jumla ya wajumbe 604.
Chikawe asoma muswada
Mapema akisoma muswada huo, Waziri wa Sheria na Katiba, Mathias Chikawe alisema Rais atakaribisha makundi mbalimbali kuwasilisha majina yasiyozidi matatu kila kundi ambao watateuliwa kama wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba. Alisema pia Kifungu cha 27 (2) kitatoa fursa kwa uhuru wa maoni katika mijadala ya Bunge Maalumu na maoni hayo hayatahojiwa mahakamani au sehemu yoyote nje ya Bunge Maalumu.
Chikawe alisema Bunge Maalumu la Katiba litakaa kwa siku 70 mfululizo jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kujadili rasimu hiyo. Hicho kitakuwa kikao kirefu zaidi cha Bunge kuwahi kukaa nchini Tanzania.
“Kutokana na unyeti wa suala lenyewe muswada huo unampa nguvu Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kuongeza siku 20 ili kujadili katiba,” aliongeza Chikawe.
Imeandikwa na Daniel Mjema na Sharon Sauwa - mwananchi 

Breaking news: Freeman Mbowe atimuliwa bungeni

Kiongozi wa kambi rasmi ya Upinzani Bungeni Mh Mbowe ametolewa nje ya Bunge, baada ya kukaidi amri ya Naibu spika Mh Ndugai alipomwamuru akae na Mh Mbowe kutokutii amri hiyo. 

Mh ngudai aliamuru askari wa Bunge kumtoa nje, hata hivyo baadaye wabunge karibu wote wa upinzani walitoka pia isipokuwa Mh. Augustin Mrema wa TLP. 

Upinzani Bungeni unadai muswada wa katiba 2013 unamapungufu.