Thursday, September 5

Kesi ya waziri mkuu Mizengo Pinda kutajwa septemba 16 mwaka huu...DPP adai kuwa hiyo ni kesi FEKI

KESI ya kikatiba iliyofunguliwa dhidi ya Waziri Mkuu Mizengo Pinda kutokana na kauli yake ya kuruhusu wanaokaidi maagizo ya Dola wapigwe, itatajwa Septemba 16 mwaka huu katika Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam.

Kesi hiyo ilifunguliwa Agosti mosi mwaka huu na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), dhidi ya Waziri Pinda na Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), wakipinga kauli hiyo iliyotolewa bungeni.

Itasikilizwa na jopo la majaji watatu wa Mahakama Kuu, likiongozwa na Jaji Kiongozi Fakhi Jundu wengine ni Jaji Augustine Mwarija na Dk Fauz Twaib.

Inadaiwa Mei 20 mwaka huu, Pinda akiwa bungeni katika nafasi yake ya Waziri Mkuu, kinyume na Katiba ya Nchi alitoa kauli ya kuruhusu askari wa Jeshi la Polisi kuwapiga raia ambao hawatatii amri yao kunapokuwa na vurugu.

“Sasa kama wewe umekaidi, hutaki, unaona kwamba ni imara zaidi, wewe ndio jeuri zaidi watakupiga tuu na mimi nasema muwapige tu kwa sababu hakuna namna nyingine, eeh maana tumechoka sasa,” sehemu ya hati ya mashitaka iliyonukuu kauli ya Waziri Pinda.

Katika hati hiyo inadaiwa kwa mujibu wa utekelezaji wa Sheria za Jinai, kauli inayotolewa na kiongozi wa nafasi ya Waziri Mkuu, inaonekana kama amri inayopaswa kutekelezwa na vyombo vya Dola kama Polisi, hivyo itachukuliwa kama amri halali na kusababisha waendelee kuwatesa na kuwapiga wananchi wasio na hatia.

Aidha inadaiwa Pinda alivunja ibara ya 100 ya Katiba inayompa kinga mbunge anapotoa jambo lolote bungeni, kwa kuwa yeye hakuzungumza bungeni kama mbunge, bali alikuwa anatoa msimamo wa Serikali yake.

Akizungumza hivi karibuni, Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) alisema hakuna uhalali wa mashitaka hayo kwa sababu kauli ya Pinda kuwa pigeni haikuwa piga ua, alichosema ni kupiga wale wasiotaka kutekeleza amri halali na kuna sheria inayoruhusu wananchi kupigwa pindi wanapokaidi amri.

No comments:

Post a Comment