Thursday, September 21

TAASISI YA MOYO JAKAYA KIKWETE (JKCI) KWA KUSHIRIKIANA NA HOSPITALI YA BLK YA NCHINI INDIA YAFANYA UPASUAJI WA MOYO KWA WAGONJWA 64



MADAKTARI kutoka  Taasisi ya Moyo ya Jakaya kikwete kwa ushirikiana na wenzao wa Hospitali ya B.L.K ya nchini India wamewafanyia wagonjwa 64 upasuaji wa moyo  ambao ni wa kufungua na bila kufungua  kifua.

Kati ya hao wagonjwa nane walifanyiwa upasuaji wa kufungua kifua na 52 walifanyiwa upasuaji wa bila kufungua kifua (catheterization)  kwa kutumia mtambo wa Cathlab.

Pia madaktari hao wamepata mafunzo ya kufanya upasuaji wa milango miwili ya moyo  ambapo awali huduma hiyo ilikuwa haitolewi kwenye taasisi hiyo .Mafunzo hayo ya siku tano yaliyo ongozwa na wataalamu kutoka Hosipitali ya BLK ya Nchini India itasaidia serikali kuokoa zaidi ya milioni 30 ambazo zingetumika kwaajili ya matibabu ya mgonjwa wa moyo wenye uhitaji wa upasuaji wa  milango miwili  ambapo asilimia 25 ya wagonjwa wana uhitaji huo.

Akizungumza na Waandishi wa habari jana Dar es Salaam Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo  Peter kisenge alisema kupitia kambi ya siku tano ya  madaktari nane wanaotibu maradhi ya moyo ,Wataalamu wa usingizi ,Wataalamu wa kutoa damu kwenye mapafu ,kutoka Hosipitali ya BLK ya nchini India imesaidia kutoa mafunzo ya uwekaji na upasuaji wa milango miwili kwenye moyo kwa wagonjwa wenye matatizo hayo ambapo huduma hiyo itakuwa ya kwanza kutolewa hapa nchini.

Mbali na huduma hiyo Dk Kisenge alisema tayari madaktari watatu wa taasisi hiyo wanaweza kutoa huduma ya uwekaji wa milango miwili ya damu kwenye moyo  huku Daktari mmoja akipata mafunzo ya miaka miwili  nchini india.Kuanza kwa huduma hiyo alisema watasaidia watoto wadogo ambao milango yao imeziba ambapo awali walikuwa hawafanyiwi upasuaji kutokana kutokuwepo kwa ujuzi wa upasuaji wa milango hiyo.
Alisema kwa wagonjwa 64 waliofanyiwa upasuaji katika taasisi hiyo wangesafirishwa nchini india serikali ingepoteza zaidi ya bilioni 6 .

Kwa upande wake Daktari Bingwa Upasuaji wa moyo na mishipa ya damu kutoka Hosipitali ya BLK ya Nchini India Dk Ajal Kajul alisema wataendelea kutoa ushirikiano kwa madaktari hapa nchini ambapo baadhi ya madaktari walioambatana nao watabaki katika taasisi hiyo kwaajili ya kuendelea kutoa mafunzo zaidi.

 Dk. Kaul alisema wataendelea kuonyesha ushirikiano wa kutoa ujuzi kwa madaktari wa hapa nchini ambapo octoba mwaka huu watatoa mafunzo ya upandikizaji wa figo,na wagonjwa wenye matatizo ya mgongo katika Hosipitali ya Taifa ya Muhimbili. 
 Daktari Bingwa wa upasuaji wa Moyo na Mishipa ya damu kutoka Hospitali ya B.L.K ya nchini India Ajal Kajul akizungumza na waandishi wa habari kuhusu uhusiano wao na Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) ambapo kwa pamoja wameweza kuwafanyia upasuaji  wa kufungua na bila kufungua  kifua  wagonjwa 64. Kushoto ni Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo Peter Kisenge.
  Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Peter Kisenge akizungumza na waandishi wa habari kuhusu uhusiano wao na Hospitali ya B.L.K ya nchini India   ambapo kwa pamoja wameweza kuwafanyia upasuaji  wa kufungua na bila kufungua  kifua  wagonjwa 64. Kulia  ni Daktari Bingwa wa upasuaji wa Moyo na Mishipa ya damu kutoka Hospitali ya B.L.K ya nchini India Ajal Kajul.


Wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakimsikilliza Daktari Bingwa wa upasuaji wa Moyo na Mishipa ya damu kutoka Hospitali ya B.L.K ya nchini India (hayupo pichani) wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu uhusiano wao na Taasisi hiyo ambapo kwa pamoja wameweza kuwafanyia upasuaji  wa kufungua na kufungua kifua  wagonjwa 64. (Picha na JKCI)

WAKAZI WA ARUSHA WATAKIWA KUTOA USHIRIKIANO KWA MKANDARASI


 Mhandisi Mshauri kutoka Kampuni ya Cheil Engineering Bw. Shin Soo akimueleza Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (katikati) maendeleo ya ujenzi wa barabara ya mchepuo (Arusha bypass), inayojengwa kwa kiwango cha lami yenye urefu wa KM 42.4. Kushoto ni Meneja wa TANROADS mkoa wa Arusha Mhandisi Johnny Kalupale.
 Mafundi wa Kampuni ya M/S Hanil-Jiangsu J/V wakiendelea na ujenzi wa moja kati ya madaraja makubwa saba yanayojengwa katika barabara ya mchepuo (Arusha bypass), inayojengwa kwa kiwango cha lami yenye urefu wa KM 42.4.
 Meneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS), mkoa wa Arusha Mhandisi Johnny Kalupale (kulia) akimuonesha Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (wa kwanza kushoto) hatua mbalimbali za maendeleo ya ujenzi wa barabara ya mchepuo (Arusha bypass), wakati Waziri huyo alipoikagua, mkoani Arusha.
 Moja kati ya madaraja saba yanayojengwa katika barabara ya mchepuo (Arusha bypass), inayojengwa kwa kiwango cha lami yenye urefu wa KM 42.4, jijini Arusha.
 Tingatinga likiendelea na kazi ya ujenzi wa awali ya madaraja katika barabara ya mchepuo (Arusha bypass), inayojengwa kwa kiwango cha lami yenye urefu wa KM 42.4, jijini Arusha.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (kushoto) akitoa maelekezo kwa Mhandisi Mshauri kutoka Kampuni ya Cheil Engineering Bw. Shin Soo (katikati)alipokagua maendeleo ya ujenzi wa barabara ya mchepuo (Arusha bypass), inayojengwa kwa kiwango cha lami yenye urefu wa KM 42.4 jijini Arusha.Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa, ametoa wito kwa wakazi wa Arusha kutoa ushirikiano kwa Mkandarasi wa Kampuni ya M/S Hanil-Jiangsu J/V ili kuweza kukamilisha kwa wakati ujenzi wa barabara ya mchepuo (Arusha bypass), inayojengwa kwa kiwango cha lami yenye urefu wa KM 42.4.

Akikagua mradi wa ujenzi wa barabara hiyo mkoani humo, Profesa Mbarawa amesema kukamilika kwa barabara hiyo kutapunguza msongamano wa magari katikati ya jiji hilo na hivyo kuvutia watalii na kukuza uchumi wa mkoa.

"Kukamilika kwa barabara hii ya Arusha bypass kutapunguza kwa kiasi kikubwa msongamano kwani magari makubwa ya mizigo yatatumia mchepuo huu na kurahisisha huduma za usafirishaji jijini Arusha", amesema Waziri Mbarawa.Ameongeza kuwa Wizara yake itasimamia kwa ukaribu ujenzi wa barabara hiyo ili ikamilike kwa wakati uliopangwa na viwango vinavyostahili vilivyokubalika.

Aidha, Prof. Mbarawa ameupongeza Wakala wa Barabara (TANROADS), mkoani humo kwa usimamizi mzuri wa barabara ya Sakina-Tengeru KM 14.1 iliyokamilika kujengwa kwa kiwango cha lami na kusisitiza kuitunza barabara hiyo ili idumu kwa muda uliopangwa.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Barabara wa Wizara hiyo (Sekta ya Ujenzi), Eng. Ven Ndyamukama, amesema Wizara kwa kushirikiana na TANROADS itaendelea kuhakikisha barabara na madaraja yote nchini yanajengwa kwa viwango vilivyopo kwenye usanifu wa kina (Detail design), na thamani ya fedha inapatikana.

Naye, Meneja wa TANROADS mkoa wa Arusha Mhandisi Johnny Kalupale, amemhakikishia Waziri Prof. Mbarawa kuendelea kumsimamia mkandarasi huyo ili akamilishe mradi kwa wakati kama walivyokamilisha ujenzi wa barabara ya Sakina-Tengeru KM 14.1 na kwa ubora unaostahili.

Mhandisi Kalupale, ameeleza changamoto zinazoikabili barabara hiyo kuwa ni wingi wa  udongo wa tifutifu na  mfinyanzi na hivyo kulazimu Usanifu wa kina wa barabara hiyo kurudiwa upya.

Ujenzi wa Barabara ya Arusha bypass unatarajiwa kutumia zaidi ya shilingi Bilioni 67 ikiwa ni ushirikiano wa fedha za Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), na Serikali ya Jamhuri ya Tanzania na ujenzi wake utahusisha madaraja makubwa 7, maboksi kalvari 55 na madaraja ya bomba 55.
Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

TAASISI YA TACC YATOA MAFUNZO KWA VIJANA WAJASIRIAMALI WILAYANI KIABAHA YA KUWAJENGEA UWEZO KATIKA KUPAMBANA NA SOKO LA AJIRA


NA VICTOR MASANGU, KIBAHA .

VIJANA wajasiriamali zaidi ya 50 kutoka Wilayani Kibaha Mkoa Pwani wamepatiwa mafunzo kwa lengo la kuweza kujifunza stadi mbali mbali za maisha pamoja na namna ya kuweza kujiajiri wao wenyewe kupitia biashara ndogo ndogo wanazozifanya ili kuweza kupambana na wimbi la umasikini na  kujikwamua kiuchumi kwa lengo la kuweza kuleta mabadiliko chanya ya kimaendeleo.

Mafunzo hayo ya vijana ambayo yanafanyika mjini Kibaha kwa muda wa siku 14 yameandaliwa na Taasisi isiyokuwa ya kiserikali ya ushindani na biashara Tanzania  (TECC) kwa kushirikiana na wadau  mbali mbali wa maendeleo kwa lengo la kuweza kuwawezesha vijana hao  ili waweze kupambana na changamoto inayowakabili kwa sasa ya upatikanaji wa soko la  ajira.

Akizungumza katika uzinduzi wa programu  hiyo ya kuwasaidia vijana wajasiliamari Mkurugenzi mtendaji wa  Taasisi hiyo ya TECC Sosthenes Sambua amesema kwamba lengo lao kubwa ni kuhakikisha kwamba inawakomboa vijana hao kwa kuwajengea uwezo wa kuweza kujikwamua kimaisha.

Naye Meneja wa Shirika la kuhudumia viwanda vidogo vidogo (SIDO) Mkoa wa Pwani Agnes Yesaya amesema lengo lao kubwa ni kuhakikisha inatoa mafunzo zaidi kwa vijana waliopo katika vikundi mbali mbali pamoja na kuwapatia mikopo pamoja na kuwajengea uwezo kwa ajili ya kuanzisha viwanda vidogo ambayo itaweza kuwapa fursa ya kujiendeleza zaidi katika  kukuza mitaji yao.

“Sisi kama sido Mkoa wa Pwani lengo letu kubwa ni kuhakikisha kwamba tunawasaidia vijana katika kuwapatia mafunzo mbali mbali ya ujasiriamali pamoja na stadi za maisha kwa lengo la kuweza kupambana na ajira, hivyo tunatarajia baada ya mafunzo haya yataweza kuwasaidia kwa kiasi kikubwa vijana wetu ikiwemo kupambana na wimbi la umasikini.,”alisema Yesaya.

Kwa upande wake Afisa vijana  halmashauri ya mji Kibaha  Mwanaishamu Nassoro amebainisha kuwa mafunzo hayo ana imani yataweza kuwa ni mkombozi mkubwa kwa vijana hao kutokana na  hapo awali walikuwa wanakabiliwa na changamoto ya soko la upatikanaji wa  ajira hivyo kuwapa wakati mgumu katika kujikwamua kimaisha.

Kadhalika aliongeza kuwa mikakati waliyojiwekea halmashauri ya mji kibaha katika kuwasaidia vijana wajasiriamali ni kuhakikisha asilimia tano iliyotegwa kwa ajili yao inawanufaisha kwa kuwapatia mikopo mbali mbali ambayo itaweza kuwasaidia kujiendeleza zaidi katika kufanya biashara zao na kukuza mitaji yao.

Nao baadhi ya vijana ambao wameshiriki katika mafunzo hayo akiwemo Hussen Peter  na Eveline Ndunguru  walisema kuwa baaada ya mafunzo hayo wataweza kutumia ujuzi walioupata katika kujiajiri wao wenywe ili kuweza kujiendesha wenywe kimaisha bila ya kuwa tegemezi.

TAASISI hiyo ya TECC hadi sasa imeshatoa mafunzo mbali mbali ya kuwawezesha vijana wajasiliamali kutoka  baadhi ya mikoa mbali mbali hapa nchini  zaidi ya 1200 ambao wamefundisha mbinu mbali mbali ambazo zitaweza kuwasaidia katika kujiajiri wao wenyewe pamoja na kujenga viwanda vidogovidogo.

 Meneja wa shirika la kuhudumia viwanda vidogo vidogo (SIDO) Mkoa wa Pwani Agnes Yesaya akizungumza jambo mara baada ya uzinduzi wa progamu ya kuwasaidia mafunzo mbali mbali  vijana wajasiriamali zaidi ya 50  kutoka Wilayani Kibaha Mkoa wa Pwani (PICHA NA VICTOR MASANGU)
 Mkurugenzi mtendaji wa  Taasisi  ya TECC, Sosthenes Sambua ambao ndio waandaaji wa mafunzo hayo ya vijana akizungumzia kuhusina na mikakati ya kuwawezesha vijana hao  ili waweze kutimiza ndoto zao mara baada ya kupatiwa ujuzi katika mafunzo hayo.
 Baadhi ya washiriki katika mafunzo hayo wakiwa wametulia kwa ajili ya kusikiliza mafunzo ya ujasiliamali.


Mmoja wa vijana wajasiriamali akizungumza na baadhi ya wenzake katika mafunzo hayo kuhusina na jinsi alivyoweza kupata fursa ya kuweza kujiajiri yeye mwenyewe na kupitia mafunzo aliyoyapata hayo awali.(PICHA ZOTE NA VICTOR MASANGU)

Ecobank yazindua njia salama ya malipo kwa mtandao


Ecobank yaja na suluhisho la kufanya malipo salama kwa njia mtandao kupitia MASTERPASS na MVISA . 

Ecobank katika kuendeleza dhamira yake ya kutoa huduma bora na kuwa suluhisho kwenye sekta ya biashara ya huduma za kibenki hapa nchini leo imezindua applikesheni ya simu za mkononi itakayojulikana kama Ecobank Mobile App – MASTERPASS NA MVISA ili kusaidia wafanyabiashara na watoa huduma mbalimbali kufanya Malipo kwa njia rahisi na kwa usalama zaidi mahali popote.

Mtanzania yeyote ataweza kutumia teknolojia hii ya mpya ya MASTERPASS QR na MVISA kulipia gharama mbali mbali kwa kutumia simu zao za mkononi kwa kupitisha Quick Response (QR) kwa wauzaji mbalimbali wa bidhaa au watoa huduma ndani na nje ya nchi.

Akizungumza jijini Dar es Salaam leo wakati wa uzinduzi huo, Mkurugenzi Mtendaji wa Ecobank Tanzania Bi, Mwanahiba Mzee alisema “applikesheni ya Ecobank Mobile App ilizinduliwa Februari mwaka huu lakini kwa sasa imeboreshwa zaidi ili wateja wa Ecobank na wale wasio wateja wa bank hii waweze kutumia applikesheni hii duniani kote”.

‘Applikesheni ya Ecobank Mobile App ni njia rahisi ya kujipatia huduma za kibenki ndani ya nchi 33 ambazo Benki yetu inafanya biashara lakini pia unaweza kuitumia ukiwa kokote duniani. Wateja wanaweza kupakua applikesheni Ecobank Mobile App na papo hapo kujifungulia akaunti ya Ecobank kwa njia ya mtandao na kuanza kupata huduma za kibenki kama vile kufanya malipo au kuhamisha fedha bila kutembelea tawi lolote la Benki”, alisema Bi Mzee.

“Tunayo furaha kwamba applikesheni yetu ni sulushisho la huduma za haraka za kibenki kupitia mtandao wa simu za mkononi na bado inaendea kuboreshwa zaidi na zaidi na sasa tunatumia teknolojia ya Masterpass QR na Mvisa kwa kufanya malipo mbali mbali, aliongeza.

Bi Mzee aliongeza kuwa Masterpass QR na Mvisa ni njia za mtandao (kidigitali) ambazo humfanya mteja kulipa kwa kadi ya Benki au akaunti zake za benki ambazo pia zimeunganishwa katika mtandao huu kwa kugusisha na kufanya malipo. ‘Hii ni njia ya kutumia simu za mkononi ambapo mnunuzi ataweza kumlipa muuzaji au mtoa huduma yeyote na hivyo inakuwa ni suluhisho kwa wajasiriamli wadogo, wa kati na wakubwa’, aliongeza Bi Mzee.

Kwa upande wake Mkuu wa kitengo cha wateja binafsi Swere Ndabu alisema “Ili kutumia huduma hii wateja wa Ecobank na wasio wateja wa Ecobank wanatakiwa kupakua Applikesheni ya Ecobank Mobile App kwenye smartphone zao kisha wanajisajili kwa kutumia kadi ya Visa au Master , au kufungua akaunti ya Ecobank Xpress papo hapo na kuanza kufanya miamala ya malipo. Kwa wale ambao ni wateja wanatakiwa kupakua na kuanza kutumia applikesheni kwa kutumia debit card au Ecobank Retail internet banking.”

“Kwa kutumia applikesheni hii wakati wa kufanya Malipo, mteja atanufaika kwa kuokoa muda wake na kupunguza gharama za kutembelea tawi la Benki, ataweza pia kufanya Malipo kwa haraka na kwa usalama zaidi pamoja na kuongeza mauzo kwa vile njia hii itachochea matumizi au manunuzi salama. Vilevile itamsaidia muuzaji sana kwani ni njia rahisi ya kutunza kumbu kumbu za mauzo.” alisema Swere.

Swere aliongeza kuwa kwa kutumia applikesheni ya Ecobank Mobile App mteja anaweza akahamisha fedha kwenye akaunti yake ya Ecobank akiwa hapa nchini au nje ya Tanzania, pia ataweza kuhamisha fedha kwenda Benki nyingine hapa nchini au kwenda kwenye kadi za Visa duniani kote na pia kwenye mitandao ya simu za mkononi ya M-Pesa, Tigo Pesa na Airtel Money.
 
  Mkurugenzi  Mtendaji wa Benki ,Ecobank Tanzania, Mwanaiba Mzee, akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana wakati wa Uzinduzi  huduma ya Malipo kwa njia ya Mtandao, inayayojulikana kama MasterPass na MVISA .Kulia ni Mkuu wa Kitengo cha Biashara wa Benki  hiyo, Respige  Kimati  na Mkuu wa Kitengo cha wateja wa Reja reja, Ndabu Sware (kushoto).
 Mkuu wa Kitengo cha wateja wa Reja Reja wa Ecobank Ndabu Lilian Sware (kushoto) akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana wakati wa Uzinduzi  huduma ya Malipo kwa njia ya Mtandao, inayayojulikana kama MasterPass na MVISA. Kati kati Mkurugenzi  Mtendaji wa Benki hiyo Mwanaiba Mzee na kulia ni Mkuu wa Kitengo cha Biashara wa Benki  hiyo, Respige  Kimati.
Baadhi ya wafanyakazi wa Ecobank Tanzania wakifuatilia kwa umakini wa Uzinduzi  wa huduma ya Malipo kwa njia ya Mtandao, inayayojulikana kama MasterPass na MVISA. Ecobank Tanzania inakuwa Benki ya kwanza hapa Tanzania kuzindua huduma ya Mobile App ambayo inakuwa ni suluhisho kwa huduma za kifedha.

MAHAKAMA YA HAKIMU MKAZI KISUTU YAMUACHIA HURU MBUNGE WA BUKOBA MJINI, WILFED LWAKATARE

Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imemuachia huru mbunge wa Bukoba Mjini, Wilfed Lwakatare baada ya Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP). Kuwasilisha hati ya kuondoa shauli hilo kwa kuwa hana nia ya kuendelea na mashtaka dhidi yake.

Lwakatare ambaye kesi yake imedumu kwa zaidi miaka minne alikuwa akikabiliwa na tuhuma za kula njama kutenda kosa

Akiwasilisha hati hiyo mbele ya Hakimu Mkazi, Thomas Simba, wakili wa serikali mwandamizi, Mutalemwa Kishenyi ameeleza kuwa wanaomba kesi hiyo iondolewe chini ya kifungu cha 91(1) cha Mwenendo wa Makosa ya Jinai kilichofanyiwa marekebisho 2002 sababu (DPP) hana nia ya kuendelea na kesi hiyo.

Baada ya kueleza hayo, Hakimu Simba amesema ameifuta kesi hiyo na mshtakiwa(Lwakatare) yupo huru.Mapema, DPP aliondoa maombi yake dhidi ya Lwakatare, kuhusiana na shtaka la ugaidi katika Mahakama ya Rufaa.

Katika maombi hayo DPP aliomba kibali cha kufungua mapitio kuhusiana na uamuzi wa Mahakama Kuu kumfutia Lwakatare mashtaka ya ugaidi.

Katika kesi hiyo, Lwakatare na mwenzake Ludovick Rwezaura, walikuwa wakikabiliwa na jumla ya mashtaka manne likiwemo la kula njama za kufanya vitendo vya kigaidi kwa lengo la kumdhuru kwa sumu aliyekuwa Mhariri wa gazeti la Mwananchi, Denis Msacky.

MRISHO MPOTO KUTUMBUIZA TAMASHA LA UTALII NCHINI CHINA.


 Msanii wa muziki wa asili nchini, Mrisho Mpoto akiwa katika picha nchini China mara baada ya kuwasili kuiwakilisha Tanzania katika Tamasha la Utalii Duaniani. 
 Msanii wa muziki wa asili nchini, Mrisho Mpoto amewasili nchini China leo katika eneo ambalo litakuwa likionesha utalii ikiwa ameenda huko kwaajili ya kuwakilisha nchi katika tamasha la Utalii Duniani ambalo litafanyika kuanzia Leo Septemba 21,2017.
Msanii wa muziki wa asili nchini, Mrisho Mpoto akiwa na mwenyeji wake katika viwanja ambavyo Tamasha la Utalii linafanyika nchin China.

Msanii wa muziki wa asili nchini, Mrisho Mpoto amewasili nchini China Jumatano hii kwaajili ya kuiwakilisha Tanzania katika Tamasha la Utalii Duaniani. 

Muimbaji huyo ambaye anafanya vizuri na wimbo ‘Kitendawili’, aliondoka nchini Tanzania siku ya Jumatatu akiwa ameambatana na kikundi chache cha ngoma kikiwa na jumla ya watu sita pamoja na yeye mwenyewe.
Akiongea na mwandishi wetu akiwa nchini humo baada ya kuwasili katika eneo ambalo litafanyika tamasha hilo, Mpoto amesema Alhamisi hii wataanza kufanya maonyesha hayo katika tamasha hilo ambalo linayakutanisha mataifa mbalimbali duniani.

“Kama nilivyowaambia watanzania wakati naondoka Tanzania, tumekuja China kwaajili ya watanzania, tumekuja kuwawakilisha wao, tunatangaza utalii wa ndani, lugha zetu za makabila zaidi ya 120, lugha yetu hadhimu ya Kiswahili, mbuga zetu za wanyama kwahiyo sisi tutawaambia Tanzania ni nchi ambayo ina kila kitu kama ukiamua kuitembelea,” alisema Mpoto.

Aliongeza,“Tumejiandaa vizuri kufanya kile kitu tulichokipanga, watanzania wananijua mimi ni mtu gani kwenye hizo anga, Kiswahili ni lugha yangu kwahiyo naweza kusema tumejipanga kuuonyesha ulimwengu tuna kitu gani ambacho tumewaletea na bila shaka kila ambaye amekuja katika eneo hili atondoka na meseji ya Tanzania ni sehemu sahihi ya kuitembelea,”

Pia amewataka watanzania kuwaunga mkono wasanii ambao wanafanya jitihada mbalimbali za kuitangaza Tanzania katika nyanja mbalimbali za utalii kwa kuwa utalii ni moja kati vyanzo vizuri vya mapato nchini.

“Uwepo wangu mimi hapa sio kwaajili ya familia yangu, hiki ninachokifanya hapa ni kwaajili ya watanzania, yule mtalii ambaye atakuja Tanzania baada ya kusikia meseji yangu ile pesa anayolipa kwaajili ya kutalii ndio ile ambayo inajenga hospitali na kununua dawa. Kwahiyo mimi ningewataka watanzania kuwa wazalendo kwenye mambo ya msingi ambayo bila shaka yanaleta tija kwaajili ya watanzania wote," alisema Mpoto.
Muimbaji huyo amesema kila mtanzania anaweza kuitangaza nchini yake kwa mazuri hivyo wamewaka watanzania kuwa wazalendo na kudumisha amani iliyopo.

JAJI MKUU AZUNGUMZIA TAARIFA YA CHAMA CHA WANASHERIA WA UINGEREZA YA KUHUSIANA NA TUNDU LISSU.


Jaji Mkuu wa Serikali, Profesa Ibrahim Musa akijibu swali la Mwandishi wa habari wakati alipoulizwa kuhusiana na Taarifa iliyotumwa na Chama cha wanasheria Uingereza. Taarifa Kamili ya Chama hicho Soma hapa chini.


WATU WAWILI WASHIKILIWA NA JESHI LA POLISI MKOA WA PWANI BAADA YA KUKAMATWA NA GUNIA NANE ZA BHANGI


 JESHI la Polisi  Mkoa wa Pwani  wamewakamata watuhumiwa wawili  ambao wameshikwa  wakisafirisha  dawa za kulevya  aina ya Bhangi  magunia nane.
 Watuhumiwa hao walionaswa  na Jeshi la Polisi wamefahamika  kwa  mjina Abraham Michael  mwenye umri wa miaka  31 mkaazi wa Jijini Dar es Salaam na Godfrey  Malakasuka  mwenye umri wa miaka 21 mkaazi wa Kimara  waliokamatwa katika eneo la Ubena Zomozi wakitokea Mkoani Morogoro kuelekea Jijini Dar es Salamaa.
Akizungumza na  waandishi wa habari  Kamanda wa Mkoa wa Pwani ACP Jonathan Shanna  alisema kuwa watuhumiwa  wamekamatwa na vidhibiti  hivyo wanastahili  kupata adhabu kali pindi watakapofikishwa  mahakamani

MFUMO WA KIDIGITALI UTAKAOUNGANISHA MIFUMO YA TAARIFA YA SERIKALI NA BINAFSI NCHINI KATIKA UTOAJI HUDUMA KUANZISHWA


Kikao cha wataalamu wa masuala ya teknolojia ya Mawasiliano leo kimeendelea mjini Bagamoyo kwa kuhusisha Wadau wakuu katika masuala ya utoaji huduma nchini zikiwemo Wizara, Taasisi , Mashirika na Makampuni binafsi. 

Katika kikao cha leo wadau wanajadili mapendekezo ya timu ya wataalamu iliyokutana siku ya kwanza ya kikao hicho kuhusu kuundwa kwa timu ya pamoja ya wataalamu ambayo itapendekeza mfumo rafiki na rahisi utakaorahisisha utoaji huduma nchini na kuboresha maisha ya watanzania kwa kutumia mfumo wa Taifa wa Utambuzi na Usajili wa watu unaosimamiwa na Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA). 

Akichangia katika siku ya pili ya mkutano huo, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi Mhe. Balozi Hassan Yahya Simba amesema ubora wa huduma na maendeleo ya Taifa unategemea uwepo wa mfumo huu ambao ni kwa manufaa si tu ya Serikali lakini pia kwa Sekta binafsi.
Mwakilishi wa Benki ya Dunia (World Bank) Ndugu Robert Polacious akizungumza kwenye siku ya pili ya kikao cha wadau kuhusu kuundwa kwa mfumo wa kidigitali utakaoungalisha mifumo ya taarifa nchini kwa kutumia Mfumo Mama wa Utambuzi na Usajili wa Watu unaosimamiwa na Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NDIA) 
Dr. Elias Mturi mtaalamu katika teknolojia ya mawasiliano akiwasilisha mada wakati wa Warsha ya Wadau Bagamoyo. 

Amesema kwa sasa Serikali ina kila sababu ya kuwa na mfumo huu kutokana na mahitaji yaliyopo katika kuboresha huduma za Kijamii, kuwezesha wananchi kushiriki kupata huduma za kifedha na Kibenki, kuongeza wigo wa ukusanyaji mapato, uchaguzi na kuongeza fursa za uzalishaji katika kufikia maendeleo ya haraka. 

Washiriki wengine wanaoshiriki kuchangia kuundwa kwa mfumo huu ni Kampuni za simu Tanzania, Benki, Mashiriki ya Kimataifa yanayotoa huduma nchini, Mashirika yasiyo ya Kiserikali, Wataalamu wa ndani na nje katika masuala ya teknolojia na wakuu wa Taasisi wa nchi za Estonia na India ambazo tayari mfumo wa kuunganisha taarifa kidigitali (Digital ID ecosystem) imeshaanzishwa na kupata mafanikio makubwa. 

Warsha hii inategemewa kumalizika na maazimio ya pamoja ya namna mfumo huo utakavyoundwa nchini kwa kutumia teknolojia na kushiriki wadau wote muhimu. 
Wawakilishi wa Umoja wa Makampuni ya Simu Tanzania wakiwasilisha mada na maoni ya wadau katika kuundwa kwa mfumo wa Taifa wa kidigitali unaounganisha mifumo ya taarifa kupitia mfumo Mama wa Utambuzi na Usajili wa Watu unaomilikiwa na NIDA. Katikati ni ndugu Paul Bomani wa AIM Group akiwasilisha mada kwa niaba ya MOAT. 
Washiriki wa Warsha ya wataalamu na wadau wakijadiliana kwenye vikundi wakati warsha ya kuunda mfumo wa kidigitali wa mawasiliano Tanzania inayofanyika Bagamoyo.

WAFANYAKAZI WA KUJITOLEA WA PEACE CORPS WAPATAO 57 WAAPISHWA KUHUDUMU NCHINI KWA MIAKA MIWILI


 Kaimu Balozi wa Marekani nchini Tanzania Dk. Inmi Patterson aliwaapisha wafanyakazi wa kujitolea wa Peace Corps wapatao 57 kuhudumu nchini Tanzania katika kipindi cha miaka miwili katika hafla iliyofanyika katika ofisi za Peace Corps jijini Dar es Salaam. 

Wafanyakazi hawa wa kujitolea wa Kimarekani watakaofanya kazi katika sekta ya elimu watapangiwa kuhudumu katika wilaya za Iringa, Mufindi, Same, Kyela, Masasi, Maswa, Singida Vijijini, Lushoto, Chamwino, Hai, Rombo, Wete, Rungwe, Njombe, Iringa Vijijini, Sumbawanga, Kusini Unguja, Kaskazini Unguja, Hanang, Mbeya, Nachingwea, Hanang, Iramba, Kiomboi, Mbeya Rural, Shinyanga na Singida Mjini.
Mgeni rasmi katika hafla hii alikuwa ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Dk. Leonard D. Akwilapo. Hafla hii ilihudhuriwa pia na wafanyakazi wa kujitolea wa Peace Corps wanaoendelea kuhudumu na wale waliohudumu hapo zamani pamoja na maafisa kutoka mashirika mengine yanayojihusisha na wafanyakazi wa kujitolea. 

Akizungumza na wafanyakazi hao wa kujitolea Kaimu Balozi Patterson alisema: "Wakati ambapo kuna uwezekano kwamba mnaweza kuwa Wamarekani wa kwanza kuishi na wafanyakazi wenzenu au majirani wa Kitanzania, ni wazi kwamba kwa Watanzania hao nyinyi mtaendelea kuwa wawakilishi wa Watu wa Marekani."

Peace Corps ni taasisi ya Serikali ya Marekani iliyoanzishwa na Rais John F. Kennedy mwaka 1961 ambayo hivi sasa inahudumia zaidi ya wafanyakazi wa kujitolea zaidi ya 7,000 katika zaidi ya nchi 70 duniani. Kwa zaidi ya miaka 50, Peace Corps imekuwa taasisi inayoendesha shughuli za mabadilishano ya kiufundi na kitamaduni zisizoegemea mrengo wowote wa kisiasa na kidini. Peace Corps ina dhamira ya kukuza amani na urafiki duniani kwa kutekeleza malengo matatu yafuatayo:

• Kutoa wafanyakazi wa kujitolea wa Kimarekani watakaochangia kuleta maendeleo ya kijamii na kiuchumi katika nchi itakayohitaji wafanyakazi hao;
• Kukuza uelewa kuhusu Wamarekani miongoni mwa watu katika jamii zinazohudumiwa na Wafanyakazi wa kujitolea;
• Kuimarisha uelewa wa Wamarekani kuhusu dunia na watu wake.

Zaidi ya wafanyakazi wa kujitolewa wa Peace Corps 2,500 wamehudumu nchini Tanzania toka mwaka 1961.  Peace Corps hutoa wafanyakazi wa kujitolea wa Kimarekani wenye utaalamu katika nyanja mbalimbali ambao hupangiwa kufanyakazi katika jamii wakifundisha katika shule za sekondari (hisabati, sayansi na Kiingereza), wakitoa elimu ya afya na utunzaji wa mazingira.

ZAIDI YA MILIONI 400 KUTUMIKA MRADI MKUBWA WA MAJI KUTOKA ENEO LA PONGWE HADI MUHEZA

Mhandisi wa Mradi wa Maji kutoka eneo la Pongwe Jijini Tanga hadi wilayani Muheza kutoka kampuni ya Koberg Construction Co.Limited Mhandisi Stepheni Kingili kushoto akitoa maelekezo kwa Mbunge wa Jimbo la Muheza (CCM) Balozi Adadi Rajabu namna watakavyoanza kutekeleza mradi huo kuanzia kesho(leo) wakati wa halfa ya makabidhiano ya vifaa vya mradi huo yaliyofanyika ofisi ndogo za mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira Jijini Tanga (Tanga Uwasa) eneo la Pongwe
Mbunge wa Jimbo la Muheza (CCM) Balozi Adadi Rajabu akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kuwasili kwenye ofisi ndogo za mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Jijini Tanga (Tanga Uwasa) kushoto ni Mkurugenzi wa Tanga Uwasa,Mhandisi Joshua Mgeyekwa
Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Jijini Tanga (Tanga Uwasa) Mhandisi Joshua Mgeyekwa akiingia kwenye halfa hiyo
Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Jijini Tanga (Tanga Uwasa) Mhandisi Joshua Mgeyekwa akizungumza katika halfa hiyo kulia ni Mbunge wa Jimbo la Muheza (CCM) Balozi Adadi Rajabu 
Mbunge wa Jimbo la Muheza(CCM) Balozi Adadi Rajabu akizungumza wakati wa halfa hiyo 
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Muheza,Luiza Mlelwa akizungumza katika halfa hiyo 
Afisa Uhusiano wa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Jijini Tanga (Tanga Uwasa) Dorrah Killo akizungumza katika halfa hiyo 
Sehemu ya wagen kutoka maeneo mbalimbali waliojitokeza kushuhudia makabidhiaano haayo 
Sehemu ya wadau waliohudhuria makabidhiano hayo eneo la Pongwe Jijini Tanga
Mbunge wa Jimbo la Muheza (CCM) Balozi Adadi Rajaabu wa pili kutoka kulia akiongozana na baadhi ya viongozi kukagua mabomba yatakayotumikaa kwenye mradi huo kushoto ni Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Jijini Tanga (Tanga Uwasa) Mhandisi Joshua Mgeyekwa kulia ni Mkurugenzi wa Halmashauri ya Muheza Luiza Mlelwa na kushoto ni Mhandisi wa Mradi huo ambao utatoa maji Pongwe Jijini Tanga Hadi wilayani Muheza
Moja kati ya vifaa mbalimbali vitakayotumika kwenye mradi huo.
Sehemu ya Mabomba ambayo yatatumika kwenye mradi huo mkubwa utakaogharimu zaidi ya milioni 400 kwa ajili ya kutoa maji eneo la Pongwe Jijini Tanga Hadi wilayani Muheza


WANANCHI wa wilaya ya Muheza mkoani Tanga wataondokana na adha ya huduma ya maji baada ya Serikali kutenga fedha zaidi ya milioni 400 kwa ajili mradi mkubwa wa kutoa maji kutoka eneo la Pongwe Jijini Tanga hadi wilayani Muheza.

Hatua hiyo ina lenga kuondoa changamoto ya uhaba wa maji wilayani Muheza ambayo ilikuwa kikwazo cha maendeleo kwa wananchi kutokana na kutumia muda mwingi kusaka
huduma hiyo badala ya kufanya shughuli za kujiingizia kipato.

Akizungumza jwakati wa kukabidhi mabomba yatakayotumika kwa mkandarasi wa mradi huo katika eneo la Pongwe Jijini Tanga, Mbunge wa Jimbo la Muheza (CCM) Balozi Adadi Rajabu alisema mradi huo utakuwa ndio mkombozi mkubwa kwa wananchi.

Alisema mradi huo ambao ni mkubwa ni moja kati ya ahadi za Rais John Magufuli alipofanya ziara mkoani Tanga ambapo alihaidi kuhakikisha wakazi wa mji huo wanaondokana na changamoto ya uhaba wa maji.

"Kwanza nimshukuru mh Rais kwa kutekeleza ahadi yake mapema jambo ambalo limetupa faraja kubwa sisi wakazi wa Muheza na vitongoji vyake lakini niwaambie katika mradi huu nitakuwa mkali sana na nitafuatilia kila mwezi kuhakikisha unajengwa kwa viwango kutokana na thamani ya fedha"Alisema.

Aidha alimsisitizia mkandarasi wa ujenzi wa mradi huo kuhakikisha ajira zitakazotolewa ziwalenge vijana waliopo katika maeneo hayo ili kuweza kupunguza ukali na ugumu wa maisha kwao na jamii zinawazunguka.

Awali akizungumza katika makabidhiano hayo,Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Jijini Tanga (Tanga Uwasa) Mhandisi Joshua Mgeyekwa alisema mradi huo ni miongoni mwa miradi ya maji inayotarajiwa kutekelezwa wilayani Muheza ili kumaliza tatizo la maji wilayani humo.

Alisema katika mradi huo mamlaka hiyo imetumia zaidi ya milioni 30 katika bajeti zake kufanya tathimini ya mradi huo huku serikali itokea fedha zote ambazo zitatumika katika mradi huo ambao utakwenda sanjari na ujenzi wa tanki la kuhufadhia maji eneo la Kilapura litakalokuwa na ujazo wa lita laki saba.

"Lengo la mamlaka ya maji na serikali ya wilaya ya Muheza pamoja na Mbunge wa Jimbo hilo kuhakikisha wananchi wanaondokana na adha ya huduma ya maji ambayo ndio kilio chao kikubwa kwa wilaya hiyo "Alisema.

Akizungumzia suala la utunzaji wa mradi huo,Mhandisi Mgeyekwa alisema mradi huo ni mali ya wananchi hivyo lazima wahakikishe wanakuwa mabalozi wazuri wa kulinda miundombinu ya maji ili iweze kuwasaidia wao na vizazi vijavyo.

Naye kwa upande wake,Mkandarasi wa Mradi huo kutoka Kampuni ya Koberg Construction Limited,Mhandisi Stephen Kingili alisema mradi huo utatekelezwa kwa wakati ili kuweza kutoa fursa kwa wananchi wa wilaya ya Muheza kuweza kunufuika na huduma hiyo.

Alisema utekelezaji wa mradi huo utaanza kutekelezwa kesho (Septemba 21) ambao utakamilika Mei 19 mwakani ukichukua miezi 8 ili kuweza kukamilika na hivyo wananchi kuweza kuutumia.

Aidha alisema mradi huo utakuwa na urefu wa km 16.9 kutoka eneo la Pongwe Jijini Tanga mpaka Muheza mjini ambao utakwenda sambamba na maungio ya kuchepusha maji katika vijiji vyote utakaopita ili kuwarahisishia wananchi kuweza kujiunganishia huduma hiyo pindi wanapokuwa wakihitaji.

Habari kwa hisani ya Blog ya Kijamii ya Tanga Raha