Sunday, November 12

POLISI WAKAMATA WAHALIFU 760 DAWA ZA KULEVYA, UWINDAJI HARAMU

WAHALIFU zaidi ya 760 wamekamatwa na Jeshi la Polisi mkoani Morogoro katika msako wa kipindi cha mwezi mmoja, wakiwamo 25 wanaojihusisha na dawa ya kulevya na uwindaji haramu, ambapo pembe za ndovu zenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 100 zimekamatwa.
Akizungumza jana na waandishi wa habari, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Ulrich Matei, alisema kati ya wahalifu hao, 25 wanajihusisha na uwindaji haramu, dawa ya kulevya na 22 ambao walisalimisha silaha zao aina ya gobore zinazotumia baruti na marisao (gololi).
Kamanda Matei alisema jumla ya silaha 26 zikiwamo pisto 1, gobore 25, risasi za shortgun 4 pamoja na vipande 5 vya pembe za ndovu na pembe  za ndovu mbili nzima zenye thamani  zaidi ya shilingi milioni 100 zimekamatwa.
Alisema Oktoba 12 saa saba mchana katika maeneo ya Mtakuja Kata ya Dakawa wilayani Mvomero, walikamatwa watuhumiwa 5 wote wanaume wakiwa na pistol moja aina ya revolver 32 S&W long yenye namba R.374973 .
Aidha, alisema silaha nyingine aina ya gobore 1 inayoweza kutumia risasi 2 za shortgun, iliyokuwa imehifadhiwa katika mfuko wa salfeti iliokotwa na askari polisi waliokuwa doria Oktoba 19 mwaka huu saa 8 mchana katika Kijiji cha Madato wilayani Kilosa.
Pia alisema wananchi wa Kijiji cha Mlunga Wilaya ya kipolisi Ruhembe na wa Kitongoji cha Ibanda Kata ya Uleling’ombe Tarafa ya Mikumi, walisalimisha jumla ya magobore 22 kufuatia agizo la Kamanda wa Polisi
Mkoa wa Morogoro la kusalimisha silaha zote zinazomilikiwa na wananchi kinyume cha sheria.
Matei alisema watuhumiwa wengine watatu walikamatwa mmoja akiwa na magobore 2 yenye namba 9916 na 539 na wengine wawili waliokuwa na risasi 2 za silaha aina ya shortgun bila kibali.
Alisema mtu mmoja aitwaye Nehemia Nashoni, alikamatwa Novemba 8 katika maeneo ya Nanenane Hoteli ya B-Z na baada ya kupekuliwa alikutwa na pembe za ndovu vipande vitano na pembe za ndovu nzima 2 alivyokuwa amevihifadhi kwenye begi jeusi vyenye thamani zaidi ya shilingi milioni 100 na hatua za kumfikisha mahakamani zinaendelea.
Hata hivyo, Kamanda Matei, amewapongeza wananchi kwa kushirikiana vyema na Jeshi la Polisi katika kuwafichua wahalifu na kuzitaka halmashauri kuacha kutoa vibali vya umiliki wa silaha kiholela.

DIWANI, MWENYEKITI KORTINI KWA KUCHOMA MALI ZA MWEKEZAJI


DIWANI wa Kata ya Mabuki, Nicodemas Ihano (CCM) na Mwenyekiti wa Kijiji cha Mwanangwa kilichopo wilayani Misungwi Mkoa wa Mwanza, Faustine Malago (CCM), wamefikishwa mahakamani kwa tuhuma za kuvunja  nyumba, kuiba na kuchoma  moto mali za mwekezaji.
Ihano ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri  ya Wilaya ya Misungwi na wenzake watatu, wamefikishwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mfawidhi wa wilaya hiyo na kusomewa hati za mashtaka matatu ambapo walikana mashtaka yanayowakabili na wote wako nje kwa dhamana.
Akisoma mashtaka hayo mbele ya Hakimu Mfawidhi, Russy Mkisi, Mwendesha Mashtaka wa polisi, Ramsoney Salehe, aliiambia Mahakama hiyo kuwa watuhumiwa hao kwa  pamoja Oktoba 24, mwaka huu saa 7.00 mchana kwenye Kijiji cha Mwanangwa  eneo la machimbo ya madini ya almasi, walikula njama na kuvunja  nyumba na kuiba vitu mbalimbali vyenye thamani  ya Sh milioni 2.8.
Salehe alisema tuhuma nyingine zinazowakabili washtakiwa hao ni kuchoma moto nyumba na magari mawili vyote vikiwa na thamani ya Sh milioni 170.8 mali ya Badar Sudi mkazi wa Shinyanga ambaye ni mwekezaji  na mchimbaji wa kati wa madini ya almasi katika Kijiji cha Mwanangwa.
Watuhumiwa wote walikana mashtaka yanayowakabili ambapo walikidhi masharti ya dhamana iliyowataka kila mmoja kuwa na wadhamini wawili wenye mali isiyohamishika na wote wako nje kwa dhamana ya Sh milioni 5 kila mmoja.
Washtakiwa wengine katika kesi hiyo ni Stephano Bengwe (32) na  Herddius Gwido (40), wote wakazi  wa Kijiji  cha  Mabuki, ambapo Hakimu Mkazi Mfawidhi, Russy Mkisi, aliahirisha kesi hiyo ambapo itatajwa tena Novemba 14, mwaka huu.

MAAJABU YA ‘TAJIRI’ ALIYETAKA KUNUNUA MAHEKALU YA LUGUMI

ALIYESHINDA mnada wa nyumba tatu za kifahari zinazomilikiwa na mfanyabiashara maarufu, Said Lugumi, zenye thamani ya Sh bilioni 2.3, Dk. Louis Shika, anaishi kwenye chumba kimoja katika nyumba ya kupanga, MTANZANIA  Jumapili linaripoti kwa uhakika.
Dk. Shika, ambaye anashikiliwa na  Jeshi la Polisi kwa siku ya tatu sasa kwa tuhuma za kuvuruga mnada, alijitokeza kununua nyumba mbili zilizopo Mbweni JKT  na moja iliyopo Upanga, katika mnada  uliokuwa ukifanywa na Kampuni ya Udalali ya Yono kwa amri  ya Mamlaka ya Mapato nchini (TRA).
Jeshi la Polisi linamshikilia Dk. Shika kutokana na kushindwa kulipa asilimia 25 ya manunuzi ya nyumba hizo kama masharti ya mnada yanavyoelekeza.
Gazeti hili  jana lilifika nyumbani kwa Dk. Shika, eneo la Tabata Mawenzi, Mtaa wa Chonde, kwa msaada wa Ofisa wa Ofisi ya Serikali ya Mtaa ya Darajani, baada ya kupatafuta kwa zaidi  saa tatu.
Baada ya kufika katika nyumba hiyo yenye geti la rangi nyeusi na maua meupe, mwandishi aligonga na kisha alitoka kijana wa kiume ambaye hakutaka kutaja jina lake  anayekadiriwa kuwa na umri  kati ya miaka 15-17, ambaye alishindwa kujibu kama daktari huyo yupo au la,  kwakuwa alishindwa kutambua jina.
Mwandishi wa habari hizi alilazimika kumwonyesha kijana huyo picha ya Dk. Shika kupitia simu yake ya mkononi na baada ya kumtambua, alikiri kuwa ni mmoja wa wapangaji wa nyumba, lakini alisema kwa wakati huo hakuwapo na kwamba ana zaidi ya siku mbili haonekani.
“Humu ndani wote ni wapangaji na hawapo, kila mtu anakwenda kwenye shughuli zake anarudi jioni, nipo mimi hapa na si mwenyeji, huwa nakuja mara moja moja, lakini huyu mzee namfahamu huwa namkuta hapa nikija kwa ndugu yangu anakaa chumba hiki hapa (anaonyesha kijana huyo chumba ambacho kilikuwa kinaning’inia kufuli ndogo)”.
Kwa mujibu wa kijana huyo, nyumba hiyo yenye  uzio na geti jeusi ina wapangaji watano na kila mmoja anakaa kwenye chumba chenye choo ndani,  isipokuwa cha   Dk. Shika kipo tofauti, kwakuwa anatumia choo cha nje.
Baada ya maelezo hayo, mwandishi alijaribu kuangalia chumba hicho kwa upande wa dirishani na kukuta hakina pazia, tofauti na vyumba vingine.
MPANGAJI MWENZAKE
Gazeti hili lilielezwa kuwa, mmoja wa wapangaji wa nyumba hiyo aitwaye Amina, ambaye anaweza kueleza kwa uhakika Dk. Shika ni nani, ofisi yake ipo hatua chache kutoka mahali ilipo nyumba hiyo.
Kutokana na hali hiyo, gazeti hili lililazimika kumfuata Amina, ambaye anauza duka la nguo maarufu kama ‘madela’, ambaye alisema Dk. Shika akiwa peke yake alifika kuishi katika nyumba hiyo baada ya kupelekwa na  mwenye nyumba aitwaye Leonard Ntakamulenga, ambaye anaishi eneo tofauti na hapo.
“Dada mimi siwezi kuongea sana kwa sababu huwa simfuatilii, sema ninachojua aliletwa na mwenye nyumba wetu na alituambia kuwa ni mpangaji kama tulivyo sisi, sasa sijawahi kumfuatilia anafanya nini, maana muda mwingine mimi huwa nawahi kutoka na ninarudi usiku,” alisema Amina.
Amina alisema aliwahi kusikia kuwa Dk. Shika huwa anatumiwa fedha za kujikimu na mmiliki wa nyumba hiyo, ingawa alikiri kutofahamu uhusiano wao.
MWENYE NYUMBA
Gazeti hili liliwasiliana kwa njia ya simu na mmiliki wa nyumba hiyo, Ntakamulenga, ambaye kwa sasa yupo Dodoma kikazi na kukiri kumfahamu Dk. Shika.
Akieleza alivyomfahamu, Ntakamulenga alisema aliletewa na madalali kama mpangaji na alijitambulisha kwake kama daktari wa binadamu katika hospitali ya Songea.
“Alikuja miezi sita iliyopita na alilipa kodi ya mwezi mmoja shilingi 50, na tangu wakati huo hajawahi kulipa tena, aliniambia nisubiri ana fedha nyingi nje ya nchi, lakini aliniambia anakaa hapo ili aweka mambo yake vizuri katika kituo chake cha kazi Songea,” alisema Ntakamulenga.
Ntakamulenga alisema kadiri siku zilipokuwa zinayoyoma alipokuwa akimkumbusha habari za kodi yake, Dk. Shika alikuwa akisisitiza kuwa hana fedha.
“Nilipomchunguza niligundua kuwa si tu kodi, bali alikuwa anakosa hata fedha ya kula, sasa kwa sababu mimi ni Mkristo nikaamua kumuacha iwe kama sehemu ya sadaka,” alisema baba huyo mwenye nyumba ambaye alikiri kusikia kwamba Dk. Shika amekamatwa.
Alipoulizwa kwamba aliwahi kumchunguza kufahamu kama kweli Dk. Shika ni daktari wa binadamu, Ntakamulenga alisema kuwa, hakuwahi kufanya hivyo, kwa kuwa si jambo rahisi kwa sababu yeye anaishi mbali na nyumba hiyo.
MAJIRANI
Gazeti hili  lilifika lilipo duka ambalo linatumiwa na wenyeji wa mtaa huo, ikiwamo nyumba anayoishi Dk. Shika.
Mmiliki wa duka hilo, ambalo lipo nyumba ya tatu kutoka anapoishi Dk. Shika, Hashim Said, alisema  taarifa za  daktari huyo kununua nyumba zilimshtua, kwakuwa kwa jinsi alivyokuwa anamfahamu si mtu wa kuwa na kiasi kile cha fedha kilichotajwa.
“Huyu mzee mimi namfahamu anakuja hapa dukani kwangu, nilivyoona kwenye mitandao  anataka kununua nyumba za Lugumi nilishangaa, maana mtu mwenyewe tangu nilipomuona siku ya kwanza sijawahi kumuelewa,” alisema Hashim.
Alisema alianza kupata wasiwasi na Dk. Shika baada ya siku moja kumuagiza bidhaa ambazo dukani kwake hazikuwapo zenye thamani ya Sh 30,000, lakini alipozileta alimwambia amhifadhie, huku akimuagiza nyingine.
“Siku ile ile niliyoleta vile vitu, akaniagiza vingine ambavyo dukani havikuwapo, tena vyenye thamani hiyo hiyo ya Sh 30,000 na nilikwenda kumchukulia kwa kuwa aliniahidi kuvichukua, cha kushangaza akaniambia   hawezi kuvichukua hivyo niviache watanunua wengine,” alisema Hashim.
Alisema hata siku ya mnada alipata wasiwasi na kwamba alidhani kuwa anaahidi kulipa Sh milioni 300, aliposikiliza kwa makini akasikia ni Sh bilioni tatu, jambo ambalo lilimshtua.
Akiuelezea mwonekano wa Dk. Shika, mmiliki huyo wa duka alisema siku zote amekuwa akionekana msafi na kwamba kutokana na umaridadi wake aliwahi kufikiri hata nyumba anayoishi huenda kuwa ni yake na anaishi na familia yake.
Alisema mbali na hulka yake ya utanashati, Dk. Shika pia anao utaratibu wa  kila siku kwenda kusoma magazeti katika kituo cha mabasi cha Kimanga.
“Yaani huyu mzee huu mnada itakuwa aliusoma kwenye magazeti, maana ana ratiba yake huwa anapita asubuhi hapa anakwenda barabarani kusoma magazeti na muda mwingine huwa ananunua,” alisema Hashim.
Alisema  mara nyingi anapokaa mahali huongelea habari za fedha, japokuwa  hajawahi kusikika akisema atazipata wapi.
“Kwa mazungumzo yake anaonekana kipindi cha nyuma alikuwa akishika fedha nyingi, lakini kwa sasa anaonekana hana ndiyo maana akikaa kama anawaweweseka mambo ya fedha,” alisema Hashim.
Hashimu alisema mara ya mwisho  walimuona Dk. Shika juzi akishuka katika gari la polisi  huku akiongozana na polisi watatu ambao walikwenda naye moja kwa moja hadi katika chumba chake.
Alisema baadaye walimuona Dk. Shika na polisi hao wakitoka nje na kumwingiza tena kwenye gari na kuondoka naye.
Naye mmoja wa  jirani ambaye ni mama wa makamo ambaye alihofia kutaja jina, alisema alianza kumuona Dk. Shika katika kipindi cha miezi kadhaa na kwa mujibu wa taarifa alizokuwa akizipata kutoka kwa wapangaji wenzake ni kwamba, ni rafiki wa mwenye nyumba.
“Huyu mtu inasemekana ni rafiki wa mwenye nyumba amemuweka hapa akae kwa muda sasa, lakini huwa hafanyi kazi yoyote, mara nyingi anatoka amevaa vizuri anakwenda mpaka Mawenzi pale kituoni baada ya muda anarudi, sijawahi kumuona katoka akarudi jioni,” alisema mama huyo.
Alisema alishawahi kulalamikiwa na baadhi ya wapangaji wenzake kuwa Dk. Shika anaweza akalala na njaa hata siku mbili na wakati mwingine wamekuwa wakimsaidia chakula.
Alisema kwa maisha anayoishi Dk. Shika, hawezi kununua nyumba za gharama kama zinazoonyeshwa mitandaoni.
Naye Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Kimanga Darajani, Chacha Mwenge, alisema alianza kusikia taarifa za Dk. Shika kupitia mitandaoni, lakini baada ya kuandikwa magazetini akajua ni mmoja wa wananchi wake.
“Mimi huyu mtu nilikuwa simjui, nilivyosikia anaishi mtaani kwangu nilijaribu kuulizia kwa watu wanaomjua kupitia simu, wengine walisema hawamfahamu, wapo waliokuwa wanasema huwa wanamuona tu anapita barabarani, nadhani ni mgeni huku,” alisema Mwenge.
Alisema baada ya gazeti hili kufika ofisini kwake alilazimika kufanya juhudi, ndipo alipogundua kuwa Dk. Shika anakaa Mtaa wa Chonde.
Dk. Shika, ambaye kwa sasa yupo katika kituo cha polisi kwa uchunguzi, siku ya  mnada alijitambulisha kwa waandishi wa habari kama Rais wa kampuni ya kimataifa inayojishughulisha na kemikali za viwandani iitwayo Ralcefort, iliyopo nchini Urusi na aliahidi kutoa fedha hizo kutoka nchini huko ndani ya saa 48.

Wabunge 40 Uingereza hawana imani na May

Jumla ya wabunge 40 wa chama tawala nchini Uingereza cha Conservative wamekubaliana kusaini barua ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu Theresa May.

Theresa May London (Reuters/T.Melville)
Taarifa hizo zimeripotiwa leo Jumapili (12.11.2017) na Gazeti la Sunday Times, na kwamba idadi hiyo ni ndogo ikilinganishwa na ile ya wabunge 48 ambao wanahitajika kushinikiza kufanyika uchaguzi mpya, ambao huenda ukamuondoa May madarakani.
May amekuwa katika shinikizo kutoka ndani ya chama chake cha Conservative kutokana na uchaguzi mkuu wa mapema uliofanyika Juni 8, ambapo chama hicho bila kutarajia kilipoteza wingi wa kura bungeni. Utawala wa May pia umekosolewa jinsi unavyoyashughulikia mazungumzo ya Uingereza kujionda kwenye Umoja wa Ulaya, mchakato unaojulikana kama Brexit.
Wakosoaji wamesema kuwa awamu sita za mazungumzo ya Brexit kati ya Uingereza na Umoja wa Ulaya, yamepiga hatua kidogo sana na hayana uwazi wa kutosha kuhusu mchakato mzima wa kujiondoa kwenye umoja huo pamoja na ratiba kamili.
Barua ya siri kwa May yagundulika
Wakati huo huo, taarifa nyingine iliyochapishwa leo na gazeti la Jumapili la Mail, imegundua barua ya siri kutoka kwa Waziri wa Mambo ya Nje wa Uingereza, Boris Johnson na Waziri wa Mazingira, Michael Gove, inayomtaka May kushinikiza mipango migumu ya Brexit.
Boris Johnson Michael Gove London (Getty Images/C.J.Ratcliffe)
Boris Johnson na Michael Gove
''Ikiwa tunataka kukabiliana na wale wanaotaka kuuharibu mchakato huo, kuna njia za kusisitiza kuhusu namna ya kulitatua hilo,'' wamesema mawaziri hao. Mawaziri hao wamewambia May ''afafanue mawazo'' ya mawaziri walioko katika baraza lake la mawaziri ambao wanaunga mkono mipango myepesi katika mchakato wa Brexit na
Kwa mujibu wa gazeti la Mail, Johnson na Gove wametaka mipangilio ya kipindi cha mpito kwa ajili ya nchi hiyo kujiondoa katika Umoja wa Ulaya ikamilike Juni 20, mwaka 2021.
Mawaziri hao wa mambo ya nje na mazingira, walipiga kampeni kuunga mkono Uingereza kujiondoa katika Umoja wa Ulaya katika kura ya maoni ya 2016, huku May akiunga mkono kambi ya waliokuwa wanataka nchi hiyo ibakie kwenye umoja huo.
Aidha, akizungumza katika kipindi cha Andrew Marr kinachoroshwa na Shirika la Utangazaji la BBC, Waziri Gove amesema hatomzuia May iwapo ataamua kuongeza kiwango cha fedha anazotakiwa kilipa katika mchakato wa kujiondoa kwenye Umoja wa Ulaya. Amesema hawezi Kumzuia May kufanya kile ambacho anakiona kuwa ni sahihi.
Amesema haamini kama ni muda muafaka wa kujiondoa katika mazungumzo ambayo yanasuasua kutokana na kiwango cha fedha ambacho Uingereza inapaswa kuchangia kabla ya kujiondoa kwenye Umoja wa Ulaya. Uingereza ambayo imekuwa mwanachama wa Umoja wa Ulaya tangu 1973, imekuwa ni nchi ya kwanza kuanzisha mchakato wa kujiondoa katika umoja huo.

Mwanariadha aliyefungiwa hajui kama alitumia dawa za kusisimua misuli


Arusha. Shirikisho la Riadha nchini (RT) wiki iliyopita liliwafungia wanariadha Elia Sidame na Msenduki Ikoki bada ya kugundulika kutumia dawa aina moja ya Norandrostorene kwa nyakati tofauti katika mashindano waliyoshiriki mwaka jana na mwaka huu nchini China na Brazil walipokuwa kwenye mialiko yao binafsi.
Sidame alishiriki mashindano mawili nchini Brazil katika Jiji la Rio de Janeiro, Meia Maratona International Oktoba 16 na Circuito da Longividade Novemba 13 mwaka huo huo na kumaliza nafasi ya tano katika mashindano yote mawili na vipimo vya mashindano yote alipatikana na kosa la kutumia Norandrostorene.
Mwanariadha Msenduki yeye alishiriki mbio za CXD Xiamen International Marathon januari 2 mwaka huu na kumaliza nafasi ya nne huko Nchini China naye alikutwa na hatia ya kutumia dawa hizo hizo.
Hata hivyo, Sidame amesema kuwa hakutegemea kama angeweza kupata kifungo hicho kwa kuwa hajui ni kwa namna gani alitumia dawa hizo katika mbio za mialiko yake ambayo yalifanyika kwa wakati tofauti sio Tanzania tu.

Hospitali yaelemewa wagonjwa


Ukosefu wa hospitali ya wilaya inayotoa huduma za upasuaji, kumesababisha msongamano wa wagonjwa katika Hospitali ya Mkoa wa Ruvuma huku wakilala wawili kitanda kimoja na wengine chini.
Kutokana na adha hiyo, Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Pololet Mgema aliwaomba Watanzania, wafanyabiashara na wadau wenye nia njema kuchanga Sh19 bilioni zitakazotumika kujenga Hospitali ya Wilaya ya Namtumbo.
Mgema ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Songea alisema kukamilika kwa hospitali hiyo ya Namtumbo kutaokoa maisha ya watu ambao hufariki dunia wakiwa njiani kufuata huduma mkoani.
Alisema hospitali hiyo ikikamilika itawasaidia watu 200,000 wa Wilaya ya Namtumbo na za jirani.
Mgema alisema tayari pazia la uchangiaji limefunguliwa na kwa awamu ya kwanza kupitia mbio za Namtumbo wanatarajia kukusanya Sh1.2 bilioni kwa ajili ya ujenzi wa chumba cha upasuaji na wodi ya wazazi.
“Tukifanikisha kujenga wodi ya wazazi na chumba cha upasuaji, tutapunguza vifo wakati wa kujifungua na itasaidia pia kuipunguzia mzigo hospitali ya mkoa.
“Huduma za upasuaji nazo ni muhimu, katika mkoa mzima hatuna hospitali kubwa ya wilaya inayotoa huduma hizo ingawa tumeanza kidogo kule Madaba na Manispaa ya Songea,” alisema Mgema.
Mkuu wa Wilaya ya Namtumbo, Luckness Amlima alisema kutokana na umuhimu wa a hospitali hiyo amekuwa akitafuta njia mbalimbali kuhakikisha ujenzi wake unafanikiwa.
“Lengo la kujenga hii hospitali lipo muda mrefu nikaona nitafute namna tunayoweza kuwahamasisha watu wengine waweze kutusaidia ndipo wazo la marathon likaja,” alisema 

Watoto 270 hufariki dunia kila siku nchini


Watoto 270 walio chini ya miaka mitano hufariki dunia nchini kila siku kutokana na sababu mbalimbali, imeelezwa.
Idadi hiyo imepungua ikilinganishwa na takwimu za mwaka 2015 zinazoonyesha kuwa watoto waliokuwa wakipoteza maisha kila siku ni 2,015.
Akizungumza katika mafunzo ya kuandika habari za watoto yanayoendeshwa na Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), mtaalamu wa masuala ya kuzuia maambukizo ya Virusi vya Ukimwi (VVU) kutoka kwa mama kwenda kwa Mtoto, Hafsa Khalfani alisema malaria na magonjwa yatokanayo na lishe duni yanachangia vifo hivyo.
Khalfani ambaye ni mtaalamu kutoka Shirika la Afya Duniani (Unicef), alisema asilimia 34 ya watoto nchini wana utapiamlo, 20 hawapati mlo kamili, 40 hawapati haki zao za msingi wakati asilimia 75 wameshafanyiwa ukatili.
Alisema changamoto zinazowahusu watoto zinaweza kutatuliwa ikiwa kila mmoja atashiriki kuzitatua.
Mwenyekiti wa TEF, Theophil Makunga alisema mafunzo hayo yanafanyika ili kuwanoa waandishi kuhusu habari za watoto kutokana na umuhimu wa kuandika kiweledi.
Ofisa Habari wa Unicef, Usia Nkoma alisema wazazi wana jukumu la kuhakikisha watoto wanakwenda shule na kurejea nyumbani wakiwa salama.
Alisema wazazi na walezi wamekumbushwa wajibu wao wa kuwalinda watoto baada ya baadhi ya tafiti kuonyesha moja ya maeneo wanayofanyiwa ukatili wa ngono ni kwenye mabasi ya shule.
Nkoma alisema mtoto wa kwanza kuingia kwenye gari la shule na wa mwisho kushuka wapo hatarini kufanyiwa ukatili huo, ikiwa usafiri huo utabaki kwa watumishi bila usimamizi wa walimu au walezi.
“Hata kama mzazi umebanwa na kazi bado una jukumu la kuhakikisha mtoto kama yupo salama, mfano tu kwenye masuala ya usafiri, ikiwa basi hilo halina muhudumu mwingine au mwalimu ni hatari kwa hiyo, wanafanyiwa ukatili wa kingono,” alisema Nkoma.
Akifundisha masuala ya sheria za watoto, Jesse Kwayu alisema chanzo kikubwa cha uhalifu ni malezi hafifu.
“Hivi mmewahi kujiuliza mtoto wa mtaani anapokuwa mtu mzima anakwenda wapi? Jambo hili kila mmoja anapaswa kutafakari kwa sababu vinginevyo kila mmoja ataathirika,” alisema.

Mike Tyson azuiliwa kuingia nchini Chile

Mike Tyson akiandamana na maafisa wa polisi wa idara ya uhamiaji katika uwanja wa ndege wa SantiagoHaki miliki ya pichaCHILE INVESTIGATIVE POLICE UNIT
Image captionMike Tyson akiandamana na maafisa wa polisi wa idara ya uhamiaji katika uwanja wa ndege wa Santiago
Bingwa wa uzani mzito duniani Mike Tyson amezuiliwa kuhudhuria sherehe ya kupeana tuzo mjini Santiago, Chile.
Lakini raia huyo wa Marekani mwenye umri wa miaka 51 ambaye aliwahi wakati mmoja kuhudumia kifungo jela kwa ubakaji, unyanyasaji na umiliki wa dawa za kulevya alirudishwa nyumbani na maafisa wa polisi wa idara ya uhamiaji.
Maafisa wa polisi katika uwanja wa Santiago walisema kuwa Tyson alirudishwa nyumbani kwa kufeli kuafikia sheria za uhamiaji.
Tyson alizuiliwa kuingia nchini Uingereza 2013 kutokana na matatizo yaliomkubw wakati wa nyuma.
''Baada ya kutathmini rekodi yake kulingana na sheria za uhamiaji ,wageni wote ambao walihukumiwa kwa kutekeleza uhalifu wowote hawaruhusiwi kuingia nchini humu'', polisi walisema.
Bingwa huyo mara mbili alihudumia miaka mitata jela katika kifungo cha miaka sita 1992 kwa kumbaka mgombea wa shindano la malkia wa urembo nchini humo.
Alikuwa bingwa wa uzani mzito mwenye umri mdogo katika historia ya uzani huo wakati alipomshinda Trevor Berbick 1986.

Mshukiwa awazuia polisi kwa kujamba Kansas, Marekani

Sean Sykes Jnr mug shotHaki miliki ya pichaJACKSON COUNTY DETENTION CENTER
Image captionSean Sykes Jnr, 24, alifanya mambo kuwa magumu kwa makachero
Mahojiano ya polisi na mshukiwa katika mji wa Kansas, Missouri nchini Marekani yalisitishwa ghafla baada ya mshukiwa huyo kujibu maswali ya polisi kwa kutoa ushuzi kwenye tupu yake ya nyuma.
Taarifa katika vyombo vya habari huko zinasema Sean Sykes Jnr alikuwa anakabiliwa na makosa ya kumiliki bunduki kinyume cha sheria na pia kuwa na dawa za kulevya.
Alikuwa amesimamishwa na polisi akiendesha gari mara mbili mjini Kansas.
Aliachiliwa awali Septemba lakini akazuiliwa tena mwezi huu.
Maelezo sasa yametolewa kuhusu jinsi mahojiano ya mwanzo ya Sykes na polisi yalivyositishwa ghafla Septemba.
Kwa mujibu wa gazeti la Kansas City, ripoti ya kachero aliyekuwa akimhoji inasema Sykes "aliinama upande mmoja wa kiti na kujamba kwa nguvu" alipoulizwa na polisi anwani yake wakati wa mahojiano Septemba.
"Sykes aliendelea kushuta na hivyo tukasitisha mahojiano," kachero huyo aliandika, baada ya kupata nafuu.
Hakuna mashtaka yoyote yaliyokuwa yamewasilishwa dhidi ya Bw Sykes baada yake kukanusha kwua na ufahamu wowote kuhusu vitu alivyodaiwa kukamatwa navyo.
Lakini mwanamume huyo wa miaka 24 alisimamishwa tena na polisi mwezi huu. Ameshtakiwa kuwa na bunduki iliyokuwa imeibiwa na kuwa na nia ya kuuza kokeni.
Ripoti hiyo ya kachero ilifichuliwa mshukiwa alipofikishwa kortini Jumatatu.

Diamond Platinumz azungumza na Salim Kikeke


Kila mtu ana ndoto zake maishani. Kwa msanii wa muziki nchini Tanzania Nasibu Abdul maarufu kama Diamond Platinumz ndoto yake yeye ni kuuweka muziki wa nchi yake katika ramani ya dunia.
Lakini pia kunayo kuhusu maisha yake ambayo yamezungumziwa sana.
Amebainisha hayo wakati akizungumza na Salim Kikeke mjini London

MHANDISI MTIGUMWE ATEMBELEA KITUO CHA UKAGUZI WA MAZAO MPAKA WA HOLILI NA TARAKEA

Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo Mhandisi Mathew John Mtigumwe Leo Novemba 11, 2017 ametembelea Vituo vya ukaguzi wa mazao vilivyopo Wilaya ya Rombo Mkoani Kilimanjaro ili kujionea ufanisi wa utendaji kazi sambamba na kubaini Changamoto zinazowakabili ili kuongeza tija katika ukusanyaji wa ushuru.

Katika ziara hiyo ya kikazi Mhandisi Mtigumwe ametembelea Kituo cha HOLILI na TARAKEA ambavyo vipo upande wa Tanzania ikiwa ni mpakani mwa Tanzania na Kenya.HOLILI ni moja ya mpaka kati ya Tanzania na Kenya ambalo upo umbali wa takribani Kilomita 25 Kutokea Himo Njiapanda huku Mpaka wa TARAKEA ukiwa umbali wa Takribani Kilomita 58 kutokea Himo Njiapanda.

Miongoni mwa Changamoto alizozibaini katika ziara hiyo kwenye Vituo vya ukaguzi wa Kilimo kwenye hivyo mipaka miwili ni pamoja na uduni wa vifaa vya kufanya kazi za Kiofisi, Kutokuwa na vifaa vya kufanya kazi ya kupimia Sampuli ya mazao katika Maabara ya Holili.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo Mhandisi Mtigumwe amewataka watumishi wanaosimamia ukaguzi wa mazao kutojihusisha na vitendo vya upokeaji Rushwa kwani kwa mtumishi atakayebainika kufanya hivyo sheria zitachukuliwa haraka dhidi yake ikiwemo kufukuzwa kazi na kufikishwa katika vyombo vya sheria.

Mpaka huo wa TARAKEA una jumla ya Njia za panya 250 kutokea Mpaka wa Hororiri mpaka kufikia mpaka wa Namanga.Aidha, Alisema serikali inaendelea na juhudi mbalimbali za kuzikabili Njia za panya zote ili kubaini kila aina ya uhalifu unaofanywa ikiwemo magendo yanayopitishwa kinyemela.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo Mhandisi Mathew John Mtigumwe akiwasili katika Kituo cha Ukaguzi wa Mazao cha TARAKEA kilichopo Katika Wilaya ya Rombo Mkoani Kilimanjaro Mpakani Mwa Tanzania na Kenya.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo Mhandisi Mathew John Mtigumwe akiwasili katika Kituo cha Ukaguzi wa Mazao cha HOLILI kilichopo Katika Wilaya ya Rombo Mkoani Kilimanjaro Mpakani Mwa Tanzania na Kenya.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo Mhandisi Mathew John Mtigumwe akisikiliza maelezo ya utendaji kazi katika Kituo cha Ukaguzi wa Mazao cha HOLILI kilichopo Katika Wilaya ya Rombo Mkoani Kilimanjaro Mpakani Mwa Tanzania na Kenya.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo Mhandisi Mathew John Mtigumwe akikagua maabara ya upimaji wa mazao katika Kituo cha Ukaguzi wa Mazao cha HOLILI kilichopo Katika Wilaya ya Rombo Mkoani Kilimanjaro Mpakani Mwa Tanzania na Kenya.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo Mhandisi Mathew John Mtigumwe akifungua bomba ili kuona kama maji yanatoka wakati akikagua maabara ya upimaji wa mazao katika Kituo cha Ukaguzi wa Mazao cha HOLILI kilichopo Katika Wilaya ya Rombo Mkoani Kilimanjaro Mpakani Mwa Tanzania na Kenya.
Picha ya pamoja kati ya wafanyakazi wa Kituo cha Ukaguzi wa Mazao cha HOLILI kilichopo Katika Wilaya ya Rombo Mkoani Kilimanjaro Mpakani Mwa Tanzania na Kenya na Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo Mhandisi Mathew John Mtigumwe.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo Mhandisi Mathew John Mtigumwe akisaini kitabu cha wageni Ofisi za Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) mara baada ya kuwasili katika Kituo cha Ukaguzi wa Mazao cha TARAKEA.

ZAIDI YA WANAFUNZI 3000 WA VYUO VIKUU KUNUFAIKA NA MRADI WA ”MOBILE FOR CHANGE”


Meneja Ruzuku na Mawasiliano wa Vodacom Tanzania Foundation, Sandra Oswald (katikati) akizungumza na waandishi wa habari jijini Mwanza mwishoni mwa wiki, wakati wa uzinduzi wa mpango wa kuwajengea uwezo wanavyuo katika nyanja za Uongozi, kibiashara, maisha ya kawaida na masuala ya kifedha kwa njia ya mtandao”Banking on Mobile for Change in Universities Project”, kushoto ni Mkurugenzi wa Taasisi ya Green Hope itakayosimamia mafunzo na Katibu Mkuu wa Serikali ya Wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustino(SAUT) Thomas Yohana.

Zaidi ya wanafunzi 3000 wa vyuo vikuu wataanza kunufaika na mradi wa”Mobile banking for change”kupitia taasisi ya maendeleo ya jamii ya Vodacom Tanzania Foundation ikishirikiana na shirika la Green hope.

Akizungumza na waandishi wa habari mapema jana wakati wa uzinduzi wa program hiyo,Meneja ruzuku na Mawasiliano wa Vodacom Tanzania Foundation, Sandra Oswald alisema mradi wao utatumika kuwajengea wanafunzi uwezo katika ujuzi wa nidhamu ya fedha,stadi za maisha na uongozi bora.

Sandra alisema wanafunzi watakaofaidika ni takriban 3000 kutoka vyuo vya mtakatifu Agustino (SAUT), Chuo kikuu cha Dodoma (UDOM) na Chuo kikuu cha Dar-es-salaam(UDSM).
Katibu Mkuu wa Serikali ya Wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustino(SAUT) Thomas Yohana akielezea manufaa watakayo yapata wanafunzi kupitia mpango wa kuwajengea uwezo wanavyuo katika nyanja za Uongozi, kibiashara, maisha ya kawaida na masuala ya kifedha kwa njia ya mtandao”Banking on Mobile for Change in Universities Project”, uliozinduliwa jijini Mwanza mwishoni mwa wiki na Vodacom Tanzania Foundation, kushoto ni Meneja Ruzuku na Mawasiliano wa Vodacom Tanzania Foundation, Sandra Oswald na Meneja Mauzo na Usambazaji wa Vodacom Tanzania mkoani Mwanza Victoria Chale.

“Mafunzo yetu yanalenga kunufaisha wanawake 2,100 sawa na asilimia 70 huku wanaume 900 sawa na asilimia 30 ambao watakaopatikana katika vyuo husika,” Sandra alisema.

Hata hivyo, meneja huyo alisema mafunzo hayo yataanza mwezi huu na kuisha April 2018 na yatafundishwa kwa njia ya semina pamoja na midahalo.

Sandra alisema baada ya mafunzo hayo wanafunzi watakuwa na uelewa wa kutosha kuhusiana na  stadi za maisha,ongezeko la kudhibiti matumizi ya fedha zao pamoja na kujiwekea akiba.

Kwa upande wake mkurugenzi wa shirika la Green Hope ambao ndiyo wasimamizi wa mradi huo,Martin Lusenga alisema baada ya mafunzo hayo wanafunzi watakuwa na uhakika wa kuweza kujitunzia kipato chao.

“Lengo letu sisi ni kuhakikisha kwamba kizazi hiki kinapata fursa ya kupanua wigo ya masuala mbali mbali ikiwemo kujiajiri hata baada ya masomo,” alisema.

Mmoja ya washiriki kutoka chuo cha SAUT, Thomas Yohana alisema anawaomba wanafunzi wenzake wahakikishe wanashiriki mafunzo hayo kwa wingi ili kujifunza maswala mbali mbali kwa manufaa yao ya baadaye.

“Ni mara chache sana kupatikana kwa fursa kama hii, hivyo basi niwashauri wanafunzi wenzangu kujitokeza mara tu nafasi kama hizi zinapokuwa zimetoka,” alisema Yohana.
Wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustino(SAUT) ,wakimsikiliza Meneja Ruzuku na Mawasiliano wa Vodacom Tanzania Foundation, Sandra Oswald mwishoni mwa wiki baada ya kuzindua mpango wa kuwajengea uwezo wanavyuo katika nyanja za Uongozi, kibiashara, maisha ya kawaida na masuala ya kifedha kwa njia ya mtandao”Banking on Mobile for Change in Universities Project”.

Waandamanaji Manila wapinga ziara ya Trump

Waandamanaji mjini Manila wakiwa wanaelekea Ubalozi wa Marekani kupinga ziara ya Rais Trump nchini Ufilipino alipowasili kuhudhuria mikutano ya viongozi wa Bara la Asia na Marekani.
Rais wa Marekani Donald Trump amewasili Jijini Manila Jumapili kuhudhuria mikutano ya viongozi wa Bara la Asia na Marekani akiwa na shauku kubwa.
Ndege ya Trump ya Air Force One iliwasili Manila muda mfupi kabla ya saa kumi na mbili jioni, majira ya nchi hiyo, baada ya takriban waandamanaji wa Ufilipino 3,500 kufanya jaribio la kuandamana kwenda Ubalozi wa Marekani.
Waandamanaji hao walipiga kelele wakimtaka Trump kuondoka nchini humo na kuishutumu serikali ya Marekani, mkoloni aliyeikandamiza Ufilipino kwa kiasi cha miaka 50, ikianzisha vita nje ya nchi yake.
“Tunajua kuwa Marekani imekuwa ikianzisha vita duniani kote, na wanajaribu kuvamia nchi zote za ulimwengu wa tatu,” amesema mwanadamanaji Kristine Cabardo, 23. Amedai kuwa ubeberu wa Marekani kitu cha kwanza unaleta vita tu na maangamizi.
Maelfu ya askari wa kuzuia fujo nchini Ufilipino waliwazuia waandamanaji hao, ambao walikuwa wamehamasishwa na chama cha kisiasa cha mrengo wa kushoto.
Waandamanaji hao walidhamiria kufika katika ubalozi wa Marekani au eneo lolote ambalo Trump alikuwa amepangiwa kwenda kuhudhuria mikutano iliyokuwa imeandaliwa na Jumuiya ya Nchi za Kusini-Mashariki mwa Bara la Asia unaoendelea hadi Jumanne.
“Ukweli ni kuwa serikali ya Ufilipino haishughulikii maslahi ya watu wake,” Cabardo amesema.
“Hata wanajeshi na jeshi la polisi hawako kwa ajili ya kulinda na kuwahudumia wananchi. Wao wanatumikia na kuwalinda wale walioko kwenye madaraka, Utawala wa Marekani na Duterte, utawala wa kibaraka wa serikali hii,” alisema mwandamanaji huyo.

Makaburi ya halaiki yapatikana Hawija Iraq

Iraqi forces inspect a mass grave near Hawija, 11 Nov 2017Haki miliki ya pichaAFP/GETTY IMAGES
Image captionMakaburi yahalaiki yapatikana Hawija Iraq
Afisa mmoja mkuu nchini Iraq, amesema, makaburi kadhaa ya halaiki, yanayokisiwa kuwa na zaidi ya maiti 400, yamepatikana karibu na mji wa Hawija, mahali ambapo kundi la wanamgambo wa kiislamu wa Islamic State, walifurushwa mwezi uliopita.
Gavana wa jimbo hilo la Kirkuk, amesema kuwa, makaburi hayo yaligunduliwa karibu na uwanja mmoja wa ndege, Kaskazini mwa Iraq.
Anasema kuwa baadhi ya maiti hizo zilikuwa zimevalishwa magwanda ya wafungwa, ambayo kundi la IS, huwavalisha wale ambao wamehukumiwa kifo, huku baadhi ya wengine walikuwa wamevalia mavazi ya kiraia.
Bw Said alisema kuwa ji ulikuwa umegeuzwa na kuwa eneo la kiwanyonga watu
Vikosi vya Iraq vimefundua makaburi maeneo ambayo wakati mmoja yalikuwa chini ya udhibiti wa Isamic Sate.
Mwaka uliopita shirika la AP lilichapisha takwimu za makaburi ya jumla ya sehemu 72.
Makaburi hayo yanaweza kuwa na miili ya kuanzia 5,200 hadi zaidi ya miili 15,000.
Map of Iraq showing Hawija and Baghdad
Image captionMakaburi ya halaiki yapatikana Hawija Iraq