Friday, October 20

NAIBU WAZIRI KWANDIKWA AWATAKA WAFANYAKAZI MIZANI KUACHA RUSHWA.

Wafanyakazi wa mizani nchini wametakiwa kufanya kazi kwa weledi, uadilifu na kuachana na vitendo vya rushwa ili kuleta tija na ufanisi wa kazi zao 
katika usimamiaji na ulinzi wa barabara ambazo Serikali imekuwa ikitumia gharama kubwa katika ujenzi wake.
Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Mheshimiwa Elias Kwandikwa, leo mkoani Shinyanga, alipokuwa akikagua  mzani wa Tinde (Shinyanga), na Mwendakulima (Kahama),  ambapo amesisitiza ushirikiano kati ya wafanyakazi hao na madereva ili kutatua changamoto zinazojitokeza katika  vituo vya mizani.

"Watumishi na madereva shirikianeni kutokomeza vitendo vya rushwa, kamwe msijihusishe kutoa wala kupokea rushwa ili kupata huduma za haraka, tukikubaini tutakuchukulia hatua kali za kisheria", amesema Naibu Waziri Kwandikwa.
Aidha, ametoa wito kwa madereva wa magari ya mizigo wanaotakiwa kuwa na stika maalum za usafirishaji wa mizigo yao kufuata utaratibu wa kuchukua stika hizo mahali husika ili kuepusha usumbufu na msongamano wa magari katika vituo vya mizani.
Akiwa katika eneo la sehemu ya maegesho na kulaza magari mjini Kahama Naibu Waziri Kwandikwa, ametoa wito kwa viongozi wa Halmashauri hiyo kuchukua hatua kali kwa madereva wanaopaki nje ya eneo hilo, ili kudhibiti uchafuzi wa mazingira unaoweza kufanywa na baadhi ya madereva hao.
Ameshauri kwa uongozi wa Halmashauri hiyo kuona namna ya kujenga maegesho mengine kama hayo ili kupata chanzo cha mapato na kusaidia kuujenga mji kuwa na Taswira nzuri.
Kwa upande wake, Meneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS), mkoani Shinyanga, Mhandisi Mibala Ndilindi, amethibitisha kuwepo kwa vitendo vya rushwa kwa baadhi ya wafanyakazi wa mizani nchini ambapo amefafanua katika kupambana na suala hilo kwa watumishi wa mkoa wake tayari mwezi uliopita amewachukulia hatua za kinidhamu watumishi watatu wa mzani wa Mwendakulima.
Naye, Msimamizi wa shughuli za mzani wa Mwendakulima kutoka TANROADS Shinyanga, Bi Herieth Monjesa, amesema kuwa changamoto za msongamano wa magari katika mizani zinasabaishwa na baadhi ya madereva wa magari ya mizigo wanaotakiwa kuwa na stika maalum za usafirishaji wa mizigo yao kushindwa kufuata utaratibu, hivyo kupelekea usumbufu kwa wahudumu na watumiaji wengine wa mizani.  

Katika hatua nyingine, Naibu Waziri Kwandikwa, amekagua barabara ya Uyovu-  Bwanga (KM 45), ambapo ujenzi wake kwa sasa umefika asilimia 98 na mkandarasi amebakisha kazi za ujenzi wa mifereji na uwekaji wa alama za barabarani.

Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.
 Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Mheshimiwa Elias Kwandikwa (Mwenye suti), akiangalia namna shughuli za upimaji wa magari zinavyoendeshwa katika mzani wa Tinde, mkoani Shinyanga. Kushoto kwake ni Meneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS), wa mkoa huo, Mhandisi Mibala Ndilindi.
 Msimamizi wa shughuli za mzani wa Tinde kutoka Wakala wa Barabara (TANROADS), mkoani Shinyanga, Bw. Lugembe Vicent (kushoto), akitoa taarifa ya kiutendaji ya mzani huo kwa Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Mheshimiwa Elias Kwandikwa. Mzani huo unapima magari 300 kwa siku.
 Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Mheshimiwa Elias Kwandikwa, akiangalia namna watumishi wa mzani wa Tinde, mkoani Shinyanga wanavyopima na kurekodi taarifa za magari yanaoingia kupima uzito kwenye mzani huo.
 Magari yakiwa katika foleni kusubiri huduma za upimaji uzito ili kuendelea na safari kwenye mzani wa Tinde, mkoani Shinyanga. 
Muonekano wa barabara ya Uyovu- Bwanga (KM 45) kwa kiwango cha lami iliyopo mkoani Geita, ikiwa imekamilika kwa asilimia 98.

RAIS DKT MAGUFULI AENDESHA KIKAO CHA BARAZA LA MAWAZIRI IKULU JIJINI DAR ES SALAAM LEO

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiongoza kikao cha kawaida cha Baraza la Mawaziri Ikulu jijini Dar es Salaam leo Oktoba 20, 2017. PICHA NA IKULU

PROF. KABUDI ATOA UFAFANUZI KUHUSU MAKUBALIANO KATI YA TANZANIA NA KAMPUNI YA MADINI YA BARRICK

Waziri wa Katiba na Sheria Prof. Palamagamba Kabudi ambaye ni Kiongozi wa Timu ya Tanzania katika majadiliano kati ya Serikali na Kampuni ya Barrick kuhusu biashara ya madini ya Dhahabu nchini, atoa ufafanuzi zaidi kuhusu yale yaliyofikiwa baada ya kuwepo sintofahamu kwa baadhi ya watu kuhusu muafaka wa ripoti iliyotolewa jana tarehe 19 Oct 2017, kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli.

USAJILI WILAYA YA MOSHI WASHIKA KASI; WANANCHI WAHAMASISHANA KUJITOKEZA KWA WINGI KUSAJILIWA VITAMBULISHO VYA TAIFA


Wakazi wa Kata ya Rau Mitaa ya Kariwa Chini, Kalikacha na Sabasaba wakipata huduma ya kujaziwa fomu za maombi ya Vitambulisho vya Taifa. Zoezi katika Kata hiyo linafanyika katika shule ya msingi Rau Wilaya ya Moshi – Kilimanjaro.

Wananchi katika Kata ya Ng’ambo Mitaa ya Mnazi, Lombeta na Ng’ambo wakiwa katika harakati za kukamilisha fomu zao, kuhakikiwa na Idara ya Uhamiaji na  kugongewa mihuri na watendaji kwenye mitaa yao kabla ya kuingia kwenye chumba maalumu kupigwa picha na kuchukuliwa alama za vidole na saini .
………………..
Wananchi katika Kata za Ng’ambo, Rau na Mfumuni wameendelea kujitokeza kwa wingi kusajiliwa Vitambulisho vya Taifa katika zoezi linaloendelea kwa sasa katika mkoa wa Kilimanjaro huku wananchi wakihimizana na kuhamasishana kwa njia ya ujumbe mfupi sms na simu.
Diwani wa Kaya ya Ng’ambo Mhe. Genesis Seth Kiwelu (Chadema) amesema wananchi wa Kata ya Ng’ambo wamebuni utaratibu mzuri wa kuhakikisha wanapeana taarifa ya kuwepo kwenye vituo vya usajili kwa siku ambazo zimepangwa; na kutoa kipaumbele kwa wazee na wasio jiweza pindi wanapofika kusajiliwa.
“ Kata ya Ng’ambo ina wananchi wengi na tunafanya jitihada za kuhakikisha wananchi wote wenye miaka 18 wanasajiliwa na tumebuni mbinu ya wananchi kuhamasishana kwa njia mbalimbali” alisema
Zoezi la Usajili kwa Wilaya ya Moshi kwa Kata za Ng’ambo, Rau na Mfumuni linamalizika Ijumaa 20/10/2017 na litaendelea kwa Kata za Msaranga, Miembeni na Majengo.
Afisa Usajili Mkoa wa Kilimanjaro Bw. Brighton Mtugani amewataka wananchi katika Kata zinazofuata kuanza kuandaa nyaraka zao muhimu zitakazowatambulisha  ili zoezi hilo kwenye kwa haraka na kwa muda uliopangwa. Viambatisho ambavyo mwananchi anatakiwa kuwa navyo ni pamoja na Cheti cha kuzaliwa, Vyeti vya Shule, Pasi ya kusafiria(Passport), Kati ya Kupigia Kura, Leseni ya Udereva, Nambari ya Utambulisho ya Mlipa Kodi (TIN),Kitambulisho vya Mzanzibari Mkaazi, Kadi ya  Bima ya Afya na Kadi ya  Mfuko wa Hifadhi ya Jamii.
Wilaya zingine zinazoendelea na zoezi hilo kwa Mkoa wa Kilimanjaro ni Same Kata za Same, Kisima na Njoro, Mwanga Kata za Mwanga, Kileo na Lembeni. Wilaya zingine ni Rombo, Siha na Hai

ZELOTE: RAIS NDIYE ATAKAYENIONDOA MADARAKANI

MKUU wa Mkoa wa Rukwa, Zelote Steven amewaambia wafugaji mkoani humo mwenye uwezo wakumuondoa ni Rais pekee, kwani ndiye aliyempangia akafanye kazi na wala sio wao.
Akizungumza wakati wa kikao cha bodi ya barabara kilichofanyika hivi karibuni, alisema wapo baadhi ya wafugaji wanaomchukia kiasi cha kutaka aondoke kwakua amekuwa akiwakamata pindi wanapo kiuka utaratibu wakusafirisha mifugo yao kwani wengine huipitisha kwenye barabara za lami.
Alisema mara nyingi amekuwa akiwazuia wafugaji kuingiza mifugo yao mkoani humo na wakati mwingine kuwakamata yeye mwenyewe kitendo kinachowaudhi nakuona Kama anawanyanyasa.
“Baadhi ya wafugaji nimekuwa nikiwakamata mwenyewe na kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria, wanakiuka utaratibu unaowataka kusafirisha mifugo yao kwa kutumia malori, wamekuwa wakikaidi na ninapo wakamata wanaweka chuki kiasi kwamba wanauliza nitaondoka lini”alisema
Alisema hakuna mwenye uwezo wa kumuhamisha Mkoa wa Rukwa ama kutengua nafasi hiyo labda Rais  Dk. John Magufuli, lakini wao wasahau wanachopaswa kufanya ni kutiisheria kwani hawezi kuwavumilia kwakuwaacha wapitishe mifugo katika barabara za lami zilizojengwa kwa gharama kubwa.
Naye  Mbunge wa Kwela,  Ignas Malocha (CCM),  aliutaka uongozi wa mkoa huo kukabiliana na ma wakala  wa pembejeo za kilimo ambao wamekuwa na tabia ya kuwauzia wakulima pembejeo za bandia.
Alisema baadhi ya wakulima wamekuwa wakipata hasara kwa kununua pembejeo za bandia na hivyo kuzidi kuwatia umasikini.
“Hivi sasa karibu tunaanza msimu wa kilimo, ni vizuri serikali ya mkoa ikaanza kujipanga kuwadhibiti mawakala hao ili kuwalinda wakulima wasipate hasara,”alisema.
Aliwasihi wakulima kuendelea kujituma katika kilimo licha ya malalamiko ya bei ya mazao kuwa ya chini kwani itafika wakati watanufaika na kilimo cha muhimu ni kuto kukata tamaa.

Waziri Jafo adai Polisi wanasababisha foleni ya magari hayo


Dar es Salaam. Serikali imesema ni wakati mwafaka mabasi yaendayo haraka (Mwendokasi) kutumia mfumo wa  taa zilizopo katika barabara zake badala ya kuongozwa na askari wa barabarani.
Hatua hiyo hiyo itasasidia mabasi hayo kufika kituoni kwa wakati kuliko hivi sasa yanachelewa njia kutokana na kuongozwa na askari wa barabarani.
Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Tamisemi), Seleman Jafo baada ya kufanya ziara ya kutembelea mradi wa mabasi hayo kuanzia eneo la Morocco hadi Kivukoni.
Kutokana na hatua hiyo, Jafo amewagiza Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Mabasi Yaendayo Haraka, Mhandisi Ronald Lwakatare   kuwasiliana na uongozi wa Jeshi la Polisi Kikosi cha Usalama Barabarani kuangalia uwezekano wa polisi kuacha kuyaongoza magari hayo.
Amesema taa za kuongozea magari zilizopo kwenye mfumo wa barabara za mabasi hayo ziachwe zifanye kazi ya kuongezea magari  badala ya askari.
 “Kuna umuhimu mkubwa wa mabasi haya yakatumia taa za barabarani kuliko kuongozwa na askari ili yaweze kukidhi mahitaji na malengo yaliyokusudiwa,’’ amesema Jafo.
Kuhusu mabasi ya  ‘Express’ yaliyotengwa maalumu kwa ajili ya  kutoa huduma ya moja kwa moja kutoka kituo kikuu cha Kivukoni  hadi  Kimara  na kutochukua abiria pindi yanaposhusha  yanaposhusha wasafiri  Kivukoni, hatua hiyo imekuwa  kero kwa  wanaotumia usafari huo hasa wanaotaka kwenda Kimara.
“Unaweza kukuta mabasi yanashusha abiria Kivukoni na kuna kundi la abiria wanaohitaji kwenda moja kwa moja Kimara, lakini hayachukui abiria, jambo hili linapaswa kurekebishwa kwani linasababisha kero kwa abiria,” amesema
Mbali na hilo,  amewataka madereva wa bodaboda  kutokukatisha katika  barabara za mfumo na  mabasi hayo  na kwamba kufanya hivyo ni  kuhatarisha usalama wao na abiria wanaotumia mfumo wa mabasi.

Aliyeshika nafasi ya kwanza darasa la saba hakutarajia ufaulu kiwango hicho

Mwanafunzi kutoka shule ya msingi Sir
Mwanafunzi kutoka shule ya msingi Sir John,Hadija Aziz Ali akiwa na mama yake mzazi aitwaye Jane Kihiyo mara baada ya kusikia taarifa za kuongoza mtihani wa kitaifa wa darasa la saba. 
Tanga. “Niliamini kwamba nitafaulu mtihani wa darasa la saba lakini sikutarajia kupata ufaulu wa kiwango hiki, namshukuru Mungu, wazazi wangu, walimu na wanafunzi wenzangu kwa ushirikiano walionipa.”
Ni kauli ya Hadija Aziz Ali, baada ya kusikia taarifa kwamba ameongoza mtihani wa darasa la saba kitaifa.
Hadija ni miongoni mwa wanafunzi 41 wa Shule ya Msingi Sir John ya jijini Tanga waliofanya mtihani wa kitaifa wa darasa la saba mwaka huu.
Kwa matokeo yaliyotolewa leo Ijumaa Oktoba 20,2017 na Baraza la Mitihani la Tanzania (Necta), Hadija ameongoza kitaifa na kuiwezesha shule yake kushika nafasi ya nne kitaifa na kuongoza katika wilaya na Mkoa wa Tanga.
Hadija amesema aliingia chumba cha mtihani akiwa na nia ya kutimiza ndoto zake za kufaulu ili apate nafasi ya kusoma masomo ya juu na hatimaye awe daktari bingwa wa magonjwa ya watoto baadaye.
Akizungumza akiwa nyumbani kwao mtaa wa Donge jijini Tanga, Hadija amesema siri ya kufanya vizuri ilitokana na juhudi za walimu wake, ushirikiano baina ya wanafunzi na wazazi ambao walikuwa kila siku wakimpa moyo.
“Nawashukuru wanafunzi wenzangu Florence Julius, Saada Ahmed na Lina John, nitawakumbuka siku zote kwa sababu tulikuwa tukipeana moyo tukiwa
darasani,” amesema Hadija.
Mama yake amwaga chozi
Jane Kihiyo (48), mama mzazi wa Hadija akizungumza huku akilia kwa kutoamini matokeo hayo, amesema mwanaye  alitambua kwamba atafaulu kwa sababu alikataa kufanya mitihani ya kujiunga na kidato cha kwanza katika shule za binafsi.
“Mwanangu alikataa kabisa kufanya interview kwenye shule za sekondari za binafsi, mimi na baba yake tulihangaika kutafuta shule nzuri lakini alikataa katakata,” Kihiyo ambaye ni muuguzi katika
kituo cha afya cha Besha jijini Tanga.

Finland ,Tanzania kushirikiana kuitunza


Dar es Salaam. Balozi wa Finland nchini, Pekka Hukka amesema Serikali yake itaendelea kushirikiana na Tanzania katika utunzaji wa misitu na mazingira kwa kuwezesha miradi mbalimbali inayohusiana na sekta hiyo.
Balozi Hukka ameyasema hayo leo jijini Dar es Salaam, muda mfupi baada ya kupanda mti kuadhimisha miaka 100 ya uhuru wa Finland na miaka 50 ya nchi hiyo kujihusisha na sekta ya misitu.
Balozi Hukka amesema nchi yake inaamini miti na misitu ina thamani kubwa kwa uchumi na maisha ya watu hivyo ina wajibu wa kuitunza.
Kupitia program na miradi mbalimbali ya mazingira na maliasili nchi hiyo imekuwa ikitoa fedha kuhakikisha miti na misitu inaendelea kuwepo na kuoteshwa kwa wingi.
Amesema kwa sasa tayari nchi yake imetenga Euro 10 milioni ambazo ni zaidi ya Sh26 bilioni kwa ajili ya mradi utakaoviwezesha vijiji kushiriki katika utunzaji na uhifadhi wa misitu.
“Tumeshazungumza na kukubaliana na Wizara ya Maliasili na Utalii kuhusu huu mradi kila kitu kipo sawa tunasubiri maelekezo madogo kutoka wizara ya fedha ili utekelezaji uanze,”amesema Hukka
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Jumuiko la Maliasili Tanzania (TNRF), Dk Suma Kaare ameiomba serikali kuendelea kushirikiana na wadau kuweka mikakati mbalimbali itakayohakikisha misitu inawanufaisha wananchi.
Amesema hilo likizingatiwa wananchi nao watashiriki kikamilifu katika utunzaji na usimamizi wa misitu hiyo.
“Wenzetu wa Finland wamekuwa wakitufadhili kwa muda mrefu katika masuala ya misitu, tuna kila sababu ya kushukuru kwa hilo. Kwa upande wa serikali tunaona ni muhimu kwa wananchi kuendelea kushirikishwa na wakajiona ni sehemu ya maliasili hii,”amesema
Amesema ni muhimu kuwa na mipango ya uvunaji endelevu wa misitu kwa kila halmashauri ambayo pia itahusisha wananchi wa eneo husika.

Dkt. Kigwangalla - Tanzania na Oman kushirikiana kwenye Utalii wa Kihistoria na Utamaduni

Waziri wa Maliasili na Utalii, Mh. Dkt.Hamisi Kigwangalla amesema  Tanzania na Nchi ya Oman zimefanya mazungumzo katika kuimalisha sekta ya Utalii hasa kwenye Utalii wa kukuza Utamaduni na ule wa Kihistoria uliokuwepo miaka mingi kwa Mataifa hayo.

Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt. Kigwangalla amebainisha hayo jioni ya jana Oktoba 18,2017, wakati alipokuwa mgeni rasmi kwenye maonyesho ya nyimbo na ngoma za Taifa la Oman yaliyofanyika kwenye viwanja vya Mnazi Mmoja Jijini Dar es Salaam ambapo pia tukio lilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wakiwemo Mawaziri na viongozi wa Taifa hilo la Oman ambao wapo Nchini kwa ziara ya kusambaza Ujumbe wa Amani na Upendo kupitia meli ya kifahari ya Mfalme wa Oman Mhe. Qaboos bin Said ‘Fulk Al Salamah’.
Akizungumza mara baada ya kushuhudia maonyesho ya ngoma na nyimbo hizo za Taifa la Oman, Dkt. Kigwangalla amebainisha kuwa, Watanzania wameweza kujifunza na kufurahia utamaduni wa Oman hasa kupitia nyimbo, ngoma na mashahiri ambapo amebainisha kuwa Serikali itaendeleza ushirikiano mwema hususani wa Kiutaduni na kukuza Utamaduni.
“Watanzania na watu wa Taifa la Oman ni ndugu. Hivyo kupitia ngoma  na nyimbo hizi walizoonesha hapa zinafanana sana za zile za Visiwa vya Zanzibar na ukanda wetu huu wa Pwani wa Tanzania.
Pia hata baadhi ya viongozi waliokuja na msafara huu wanazungumza vizuri lugha ya Kiswahili bila kuchanganya na lugha nyingine huku wengine kama mulivyowaona wana asili ya Tanzania ikiwemo Visiwa hivyo vya Zanzibar ambapo walizaliwa huko.” Ameeleza Dkt. Kigwangalla.
Aidha, ameeleza kuwa, kwa sasa wanakusudia kutengeneza chanzo kipya cha Utalii ambacho kitakuwa ni cha Kihistoria na Kiutamaduni baina ya Mataifa hayo mawili  na kufafanua kuwa, Histoia ya Tanzania hasa Lugha ya Kiswahili huwezi kukitenganisha Bara la Arab hususani watu wa Oman.
“Kuna wengine wasomi wa Historia na utamaduni wa Uislamu wamebainisha kwenye taarifa za kisayansi, kuwa pengine hata dini ya kiisilamu ilianza kufika ukanda wa Pwani wa Afrika Mashariki kabla ya hata haijafika baadhi ya Nchi ya Mashariki ya Kati.
Hii ni pamoja na makaburi ya kale kule Bagamoyo, Pemba na sehemu nyingine za Tanzania ambapo kwa pamoja yanaonesha uwepo wa Waislamu na mashekhe wa kiisilamu waliofika kuanzia mwaka 1200 mpaka hadi 2000, miaka mingi iliyopita.” Alibainisha Dkt. Kigwangalla.
Ameongeza kuwa: “Wao wakitangaza vivutio vyao, watavitangaza na vivutio vyetu vya Tanzania. Lakini pia sisi tutatumia fursa vivutio tulivyonavyo ambavyo wao hawana kama Mbuga za Wanyama kuwaalika watu wa Omani kuja kutalii Tanzania, kipindi cha Mwezi Juni, Julai hata Agosti wao ni kipindi cha joto kali kwani wakati mwingine  msimu huo kule wao wanakuwa na utaratibu wa kutoa rikizo ama mapumziko ya muda wa zaidi ya siku 30 hadi 40 hivyo tutatumia  fursa ya kipindi hicho na hata wale wanaowapokea Oman waweze kuja Tanzania kutalii” alieleza.
Pia alimalizia kwamba,  ushirikiano huo, utaongeza soko kubwa la kiutalii.
Msafara huo wa viongozi wa Oman wakiwemo Mawaziri na wafanyakazi wa Meli hiyo ya Mfalme wa Taifa hilo unajumuisha watu zaidi ya 300 ambapo leo Oktoba 19,2017, umetembelea Wilaya ya Bagamoyo kujinea fursa za kiuwekezaji na uchumi katika ukanda huo wa Pwani huku Meli hiyo kesho Oktoba 20,2017 ikitarajiwa kuondoka kuelekea Mombasa Nchini Kenya.

 Waziri wa Maliasili na Utalii, Mh. Dkt.Hamisi Kigwangalla akisalimiana na Waziri wa Mafuta na Gesi wa Oman Dkt. Mohamed Hamad Al Rumhy alipokuwa akiwasili kwenye tukio la Ngoma na nyimbo za Taifa la Oman, Jijini Dar es salaam
 Waziri wa Maliasili na Utalii, Mh. Dkt.Hamisi Kigwangalla akisalimiana na Waziri wa Uwekezaji wa Oman Mhe. Salem Ben Nasser Al Ismaily, Kulia ni Waziri wa Mafuta na Gesi wa Oman Dkt. Mohamed Hamad Al Rumhy alipokuwa akiwasili kwenye tukio la Ngoma na nyimbo za Taifa la Oman, Jijini Dar es salaam
 Waziri wa Maliasili na Utalii, Mh. Dkt.Hamisi Kigwangalla akifurahia jambo pamoja na Waziri wa Uwekezaji wa Oman Mhe. Salem Ben Nasser Al Ismaily, alipokuwa akiwasili kwenye tukio la Ngoma na nyimbo za Taifa la Oman, Jijini Dar es salaam
 Waziri wa Maliasili na Utalii, Mh. Dkt.Hamisi Kigwangalla akiteta jambo pamoja na Waziri wa Uwekezaji wa Oman Mhe. Salem Ben Nasser Al Ismaily, wakati akishuhudia tukio la Ngoma na nyimbo za Taifa la Oman, Jijini Dar es salaam
  Waziri wa Maliasili na Utalii, Mh. Dkt.Hamisi Kigwangalla akiongea  na Waziri wa Uwekezaji wa Oman Mhe. Salem Ben Nasser Al Ismaily, wakati akishuhudia tukio la Ngoma na nyimbo za Taifa la Oman, Jijini Dar es salaam
 Bendi ya Jeshi la Taifa la Oman wakipiga nyimbo za Taifa hilo zinazofanyika wakati wa vita na ukombozi
 Baadhi ya wananchi wakiwa na bendera za Taifa la Oman na Tanzania wakishuhudia tukio hilo
 Baadhi ya Askari wa kikosi Maji cha Oman wakiwa katika tukio hilo.

 Dkt. Kigwangalla akizungumza na wanahabari 
 Dkt. Kigwangalla akizungumza na wanahabari 
 Dkt. Kigwangalla akizungumza na wanahabari 
 Kikundi cha utamaduni  cha Oman wakionesha ngoma za Utamaduni wa Taifa hilo.
 Kikundi cha utamaduni  cha Oman wakionesha ngoma za Utamaduni wa Taifa hilo.
 Kikundi cha utamaduni  cha Oman wakionesha ngoma za Utamaduni wa Taifa hilo.
Kikundi cha utamaduni  cha Oman wakionesha ngoma za Utamaduni wa Taifa hilo.

MAKAMU WA RAIS,SAMIA SULUHU AMKABIDHI CHETI CHA PONGEZI AFANDE IBRAHIM SAMWIX

 Makamu wa Rais, Samia Hassan Suhuhu akimpa Mkono, Mkuu wa Kituo cha Ukaguzi wa Mabasi cha Ubungo, Ibrahim Samwix  katika wiki usalama barabarani iliyofanyika mkoani Kilimanjaro.Ikiwa ni pongezi kwa kusimamia vizuri sheria za usalama barabarani.

Waziri wa mambo ya ndani ya nchi, Mwigulu Lameck Nchemba akimpa mkono Mkuu wa Ukaguzi wa Kituo cha Mabasi cha Ubungo, Ibrahim  Samwix  katika  Wiki Usalama Barabarani  iliyofanyika mkoani Kilimanjaro, Mkuu kituo cha mabasi ubungo alitunukiwa cheti cha  usimamizi wa sheria za usalama barabarani .

SHEIKH SHARIFF MAJINI KUFANYA KONGAMANO KUBWA IRINGA JUMAMOSI NA JUMAPILI HII

Sheikh Shariff Majini kutoka katika kituo cha Dua na Maombi Mabibo Mwisho jijini Dar es salaam, mwishoni mwa Mwezi Oktoba Jumamosi tarehe 28 na Jumapili tarehe 29 anataraji kufanya Kongamano kubwa pamoja na Dua katika Mkoa wa Iringa.
Kongamano linatarajiwa kufanyika katika ukumbi wa OLUFEA uliopo KITANZINI Manispaa ya Iringa Mjini. Kongamano litafanyika kuanzia saa saba mchana mpaka saa kumi naa mbili jioni.
Sheikh amelazimika kufanya kongamano Iringa kufuatia kila siku kupigiwa simu na waumini wa Iringa ili afike kwa ajili ya kuwasikiliza shida zao mbalimbali.

Polisi kuendelea kudhibiti "mtandao" wa mashoga Tanzania

Maandamano nchini Malawi yakupinga kifungo kilichotolewa kwa mtu aliyekuwa anadaiwa kujihusisha na ushoga nchini Malawi, 2010.
Watu 12, wakiwemo wananchi wawili wa Afrika Kusini na mwananchi wa Uganda wamekamatwa na polisi wakidaiwa kuwa ni mashoga, ikiwa ni sehemu ya kampeni ya serikali ya Tanzania katika kupambana na ushoga.
“Tumewakamata wahalifu hawa katika hoteli ya Peacock—wakiwa wanaufagilia ushoga. Wawili kati yao ni wananchi wa Afrika Kusini, mmoja ni Mganda na tisa ni Watanzania,” mkuu wa polisi Dar es Salaam Lazaro Mambosasa amesema.
Vyanzo vya habari nchini Tanzania vimesema Kamanda huyo amesema kuwa wengine 12 bado wanahojiwa kabla ya kufikishwa mahakamani na hakusema ni lini walikamatwa.
“Sheria za Tanzania zinakataza kitendo cha mapenzi kati ya watu wa jinsia moja na ni uvunjifu wa sheria za nchi,” amesema Mambosasa.
Ameongeza kuwa meneja wa hoteli hiyo ni miongoni mwa watu waliokamatwa “kwa kuwapa chumba” watu hao.
Mombasa amewahimiza watu kutoa taarifa kwa vyombo vya umma iwapo watakuwa wameshuhudia harakati kama hizo "ilituweze kuchukua hatua mara moja".
Polisi pia wamewakamata watu 20 kati yao wanane ni wanaume na 12 wanawake kwa makosa ya ushoga katika kisiwa cha Zanzibar mwezi uliopita.
Kwa mujibu wa polisi, zoezi la kuwakamata lilifanyika katika hoteli ambako kikundi hicho kilikuwa kinapewa mafunzo na Asasi ya kiraia ya kimataifa iliyokuwa imesajiliwa rasmi, inayojihusisha na elimu juu ya ukimwi.
Mwezi Februari, Tanzania ilikosolewa na Marekani baada ya kutangaza kufunga vituo vya afya kadhaa vinavyoshughulikia kuelimisha watu kujilinda na Ukimwi, ikidai kuwa vilikuwa ni vituo vya kuhamasisha ushoga.
Serikali Dar es Salaam iliahidi kuwaondoa nchini raia wa kigeni wote wanaofanya kampeni kutaka mashoga wapewe haki zao.
Ushoga kwa kukutana kimwili wanaume unaadhibiwa kwa kifungo kati ya miaka 30 hadi maisha katika Sheria za Tanzania. Hakuna katazo kama hilo kwa kosa la mapenzi baina ya wanawake.
Kwa mujibu wa Shirika la Haki za Binadamu Amesty International, ushoga ni kinyume cha sheria katika nchi 38 kati ya nchi za Kiafrika 54 na adhabu yake ni kifo huko Mauritania, Somalia na Sudan.
Uganda in 2014 tried to impose the death penalty on those found guilty of being homosexual, however the controversial law was later repealed.
Uganda mwaka 2014 ilijaribu kuweka adhabu ya kifo kwa wale watakao kutinakana na kosa la kujihusisha na ushoga , lakini sheria hiyo tata iliondolewa kabisa siku za usoni.

Kenyatta akutana ana kwa ana na jaji mkuu David Maraga

Uhuru akutana na Maraga Oct 20, 2017.
Kwa mara ya kwanza tangu mahakama ya juu ya Kenya kubatilisha uchaguzi wa tarehe nane mwezi Agosti, Ijumaa rais Uhuru Kenyatta alikutana ana kwa ana na jaji mkuu David Maraga wakati wa hafla ya sherehe za kuadhimisha Mashujaa Day kwenye bustani za Uhuru Park mjini Nairobi.
Rais Kenyatta alionekana kumpa mkono jaji huyo na wawili hao wakafanya mazungumzo kwa muda mfupi.
Punde tu baada ya uamuzi huo wa mahakama, Kenyatta, akionekana mwenye gadhabu, alimkosoa Maraga na wenzake huku akitumia maneno ambayo wakosoaji wake waliyataja kama yasiyofaa.
Tume ya IEBC inajitayarisha kwa uchaguzi wa marudio siku ya Alhamisi licha ya muungano wa upinzani Nasa kusema kuwa mgombea wao pamoja na wafuasi wake hawatashiriki kwenye zoezi hilo.

Itikadi za Xi Jinping zapongezwa

China imepongeza itikadi ya kisiasa ya Rais Xi Jinping iliyozinduliwa jana katika mkutano mkuu wa chama cha Kikomunisti ishara kwamba huenda ikaingizwa katika katiba ya chama hicho na kuimarisha nguvu za kiongozi huyo.

China Peking Kommunistischer Parteitag Xi Jinping (Reuters/A. Song)
Maafisa wa chama tawala cha Kikomunisti nchini China walishangilia kwa kuimba na kucheza huku wengine wakibubujikwa na machozi wakati wakipongeza itikadi hizo, siku moja baada ya kuufungua mkutano ambao unafanyika kila baada ya miaka mitano na kuahidi kujenga ''mafanikio ya kisasa ya kijamaa'' kwa ajili ya ''zama mpya''. 
Kwa mujibu wa shirika la habari la China, Xinhua, wajumbe watatu wanaomaliza muda wao katika kamati kuu ya watu saba ambayo Xi anaiongoza, wamesema wanayaheshimu mawazo ya kiongozi huyo kuhusu ujamaa na China mpya. Wachambuzi wanasema kauli kama hizo zinaonyesha Xi ataimarishia nguvu katika madaraka yake kwa kutumia kaulimbiu yake mpya na kuingizwa katika katiba ya chama.
China Peking Kommunistischer Parteitag (picture-alliance/ZumaPress/Lan Hongguang)
Wajumbe wa mkutano wa chama cha Kikomunisti China
Hakuna kiongozi mwingine ambaye itikadi yake iliingizwa katika katiba wakati akiwa mdarakani, tangu utawala wa Mao Zedong, mwanzilishi wa China ya sasa. Huenda wiki ijayo Xi akachaguliwa tena kukiongoza chama hicho kwa kipindi cha miaka mitano mingine ijayo.
Maafisa wa chama hicho wamempongeza Xi kama kiongozi mwenye hekima na busara, heshima ambayo walipewa viongozi wawili tu, akiwemo Mao Zedong na mrithi wake Hua Guofeng.
Gazeti la kila siku la Beijing limeripoti kuwa Katibu Mkuu wa chama cha Kikomunisti mjini Beijing, Cai Qi, anasema Xi amepewa mapenzi na heshima ndani ya chama hicho, jeshi na watu wote kwa ujumla na anastahili kuitwa kiongozi mwenye hekima. Qi ni mmoja wa washirika wa karibu wa Xi.
Wachambuzi wanasema, kitendo cha maafisa kumsifu na kumpongeza kiongozi wa juu wa chama katika mkutano mkuu sio cha ajabu, lakini kitendo cha kuonyesha hisia au mapenzi binafsi sio kitu cha kawaida.
Xi amekiimarisha chama
Xi mwenye umri wa miaka 64 amekiimarisha chama hicho tangu alipochukua madaraka mwaka 2012, na kuziba mianya yote ya rushwa, kudhibiti vikali mashirika ya kiraia na kuipandisha nafasi ya China katika ngazi ya kimataifa.
China Shenzhen Statue Mao Zedong (imago/China Foto Press)
Sanamu ya Mao Zedong
Itikadi iliyopewa jina la Xi kuiongoza China na chama, itaongeza mamlaka yake, anasema Ryan Manuel, mtaalamu wa masuala ya siasa za China katika Chuo Kikuu cha Hong Kong. Watangulizi wa Xi, Hu Jintao na Jiang Zemin, walikuwa na dhana zao za itikadi ambazo zilitajwa katika katiba, lakini sio majina yao.
Mwaka uliopita, chama hicho kilimpa Xi cheo cha ''Kiongozi Imara'', hali iliyomuimarishia nafasi yake kabla ya mkutano huo mkuu. Na kulingana na uvumi, Xi anaweza kubakia madarakani zaidi ya muda wa kawaida wa vipindi viwili na hata kukumbushia cheo cha mwenyekiti wa zamani wa chama hicho, Mao Zedong.