Friday, October 20

USAJILI WILAYA YA MOSHI WASHIKA KASI; WANANCHI WAHAMASISHANA KUJITOKEZA KWA WINGI KUSAJILIWA VITAMBULISHO VYA TAIFA


Wakazi wa Kata ya Rau Mitaa ya Kariwa Chini, Kalikacha na Sabasaba wakipata huduma ya kujaziwa fomu za maombi ya Vitambulisho vya Taifa. Zoezi katika Kata hiyo linafanyika katika shule ya msingi Rau Wilaya ya Moshi – Kilimanjaro.

Wananchi katika Kata ya Ng’ambo Mitaa ya Mnazi, Lombeta na Ng’ambo wakiwa katika harakati za kukamilisha fomu zao, kuhakikiwa na Idara ya Uhamiaji na  kugongewa mihuri na watendaji kwenye mitaa yao kabla ya kuingia kwenye chumba maalumu kupigwa picha na kuchukuliwa alama za vidole na saini .
………………..
Wananchi katika Kata za Ng’ambo, Rau na Mfumuni wameendelea kujitokeza kwa wingi kusajiliwa Vitambulisho vya Taifa katika zoezi linaloendelea kwa sasa katika mkoa wa Kilimanjaro huku wananchi wakihimizana na kuhamasishana kwa njia ya ujumbe mfupi sms na simu.
Diwani wa Kaya ya Ng’ambo Mhe. Genesis Seth Kiwelu (Chadema) amesema wananchi wa Kata ya Ng’ambo wamebuni utaratibu mzuri wa kuhakikisha wanapeana taarifa ya kuwepo kwenye vituo vya usajili kwa siku ambazo zimepangwa; na kutoa kipaumbele kwa wazee na wasio jiweza pindi wanapofika kusajiliwa.
“ Kata ya Ng’ambo ina wananchi wengi na tunafanya jitihada za kuhakikisha wananchi wote wenye miaka 18 wanasajiliwa na tumebuni mbinu ya wananchi kuhamasishana kwa njia mbalimbali” alisema
Zoezi la Usajili kwa Wilaya ya Moshi kwa Kata za Ng’ambo, Rau na Mfumuni linamalizika Ijumaa 20/10/2017 na litaendelea kwa Kata za Msaranga, Miembeni na Majengo.
Afisa Usajili Mkoa wa Kilimanjaro Bw. Brighton Mtugani amewataka wananchi katika Kata zinazofuata kuanza kuandaa nyaraka zao muhimu zitakazowatambulisha  ili zoezi hilo kwenye kwa haraka na kwa muda uliopangwa. Viambatisho ambavyo mwananchi anatakiwa kuwa navyo ni pamoja na Cheti cha kuzaliwa, Vyeti vya Shule, Pasi ya kusafiria(Passport), Kati ya Kupigia Kura, Leseni ya Udereva, Nambari ya Utambulisho ya Mlipa Kodi (TIN),Kitambulisho vya Mzanzibari Mkaazi, Kadi ya  Bima ya Afya na Kadi ya  Mfuko wa Hifadhi ya Jamii.
Wilaya zingine zinazoendelea na zoezi hilo kwa Mkoa wa Kilimanjaro ni Same Kata za Same, Kisima na Njoro, Mwanga Kata za Mwanga, Kileo na Lembeni. Wilaya zingine ni Rombo, Siha na Hai

No comments:

Post a Comment